Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, July 2, 2015

RADHI YA WAZAZI-14



 Wanasema kawaida mwizi huwa hatoki ,mbali, kwahiyo mimi nikajenga ukaribu na hiyo familia, nikichunguza nyendo, tabia....na nilipohakikisha nimefanikiwa, nikaanza kazi 


Tuendelee na kisa chetu

                                             ************
Jamaa huyo alikuwa na familia, ya mke na watoto wawili,  binti mkubwa  akisoma kidato cha sita, na kijana wa kiume akiwa kidato cha nne, na mke alikuwa akifanya kazi mbali tofauti na mume wake.

Mume yeye  alikuwa akifanya kazi karibu sana na nyumbani wanaposihi, ukilinganisha na mkewe , lakini mke alikuwa wakati wote wa kwanza kufika nyumbani.

Mume alikuwa na tabia  ya kupitia kwenye bar moja na kupata kinywaji, na alikuwa na muda wake maalumu wa kuondoka, huwa haupitlizi....ukishafika muda huo wa kuondoka, haraka analipia bili yake na kuelekea kwenye gari lake , na akifika kwenye gari lake huchukua muda kidogo, haijulikani anafanya nini kwenye gari, baadaye huondoka.

 Basi mimi nilipohakikisha nimekusanya zile habari muhimu nilizozihitajia ndani ya hiyo familia, nikaona sasa niingie hatua nyingine,..hatua hiyo ilihitajia msaidizi, na nilishajua ni nani atanifaa ili kuweza kukamilisha hiyo kazi ya pesa nyingi.

Kwahiyo nilikwenda kwenye hiyo bar,ambayo huyo jamaa huwa anakwenda kupata kinywaji, sio mbali na hapo nyumbani kwao, ni mtaa wa pili yake, nilishapata habari za juu kwa juu kutoka kwa mtaalamu, kuwa huyo jamaa huwa halewi sana, anakunywa kiasi, kwahiyo isingelikuwa ni rahisi sana kupitiliza na kupoteza utashi wa kujichunga.

‘Kwa namna hiyo ni lazima upate binti mcheshi anayejua kumpagawisha mwanaume, ahakikisha anamzoea , halafu ahakikishe anamfanya amuone tofauti, na ikibidi uongeze makali kwenye kinywaji chake....’alikumbuka alivyoelekezwa na mtaalamu.

‘Mhh, hilo la kuongeza makali, ni hatari...naliogopa sana, sitaki kufanya kosa hilo tena...’akasema profesa

‘Siseme umuwekee madawa, usininakili.... hapana, siku hizi kinywaji kinaweza kuongezwa makali kutokana na mnywaji mwenyewe, niongezee sijui gongo, au nini,....au sio...wauzaji wanalifahamu hilo..’akasema

‘Inabidi kujihami, maana ni lazima akija kuzindukana atajua kuna kitu kilifanyika na kama ni mjanja anaweza kwenda kupima, akigundua aliwekewa kitu, unahisi itakuwaje, binti aliyehusika atakuwa matatani, na binti akiingia matatani,mini sitaaminika tena,...mimi naona nikumweka sawa huyo binti yeye atajua ni nini cha kufanya, wao ni wazoefu wa hizo kazi, sizani kama atashindwa....’akasema profesa

‘Hiyo ni kazi yako, muhimu ni kucheza na muda,...tunataka tuliwahi tui, likiwa bado...ok, mimi siwezi kukuingilia huko, muhimu uwe makini na huyo binti utakayemchagua..., awe kweli anaweza kumpagawisha huyu mtu, ..na msiri...kazi hii pamoja na yote inahitajia usiri...'akasema mtaalamu

'Huyu jamaa bado hajafahamu mazingira na tabia za hapa kwetu, na anavyoonekana, kahamanika na vimwana wa hapa, anafikiri vyote ving'aavyo ni dhahabu, anaonekana ana kihoro, ana pupa, na nahisi mkewe sio mlishaji mnzuri, ...na watu kama hawa wakipata mwanya...si unajua ...’akasema mtaalamu akitikisa kichwa na tabasamu mdomoni.

‘Mhh, hilo nitalijua nikiongea na huyo binti, wapo wanajua hiyo kazi muhimu ni pesa tu...na kama anakunywa mahali hapo....ameingia mkenge....’akakumbuka alivyomwambia mtaalamu.

 Basi mimi baada ya kuifahamu hiyo familia na udhaifu wa huyo jamaa hatua ya pili ikawa sasa kumtafuta mwenza, ambaye atacheza picha na jamaa,huyu ni muhimu sana, na anatakiwa mtu unayemfahamu vinginevyo anaweza kukuuza,ukainga hatiani, au akakusaliti na ukajikuta mnanyang’anyana tonge.

Nilishakuwa mtaalamu wa mambo hayo, kwahiyo nilijua nimuendee nani, na muda gani,siku hiyo nilimaliza kazi zangu mapema za vibarua vya hapa na pale nikapata pesa ya kukaa kiti kirefu,....sina shida, utafikiri ninazo,kumbe nanuka ukata...

Nikafika kwenye hiyo bar, muda ambao najua huyo jamaa anakuwa bado hajafika, nikaagiza kinywaji rahisi, na wakati nakata kiu, nikamuita dada mmoja ninayemfahamu, aliponiona tu akajua kuna jambo.

‘Mhh,nambie maana weweukija hapa najua kuna jambo,na sizani kamaumekuja kunilipa pesa yangu....’akasema

‘Una muda kidogo nataka tuongee dili...’nikasema

‘Si unaona mwenyewe,...muda kama huu wateja bado kabisa, wewe nambie....’akasema

‘Nikaongea naye moja kwa moja bila kuficha maana ni mdada tunayefahamiana, na alishakuwa karibu nami sana,na kutokana na maelezo  ya mtaalamu,huyo mdada alishakuwa na ukaribu na huyo jamaa,binti huyo nilishamzoea kabla,na kuna kazi nyingine nilishawahi kufanya naye.

Sikupoteza muda nikamwambia lengo langu, ...

‘Mhh,tatizo lako wewe unaniona nina maana pale ukinipa kazi zako, lakini ukishazishika pesa mkononi waniona sina maana tena...,unanipa shida kuzifuatilia pesa zangu, sasa sitaki tena kazi zako,kwanza zinaniweka kwenye wakati mgumu, naishi kwa mashaka mashaka wakati mshahara wangu unanitosha...’akasema

‘Lakini wewe wahitajia kutoka, kujijenga, na hutegemei kupata pesa nyingi kama hizi za safari hii, safari hii kuna kazi nzuri yenye masilahi zaidi ukizipata unaweza kufanya jambo la maana,...’akasema

‘Nimekuambia sitaki,kazi zako,...kwanza nilipe lile deni langu, usifikiri nimesahau, ...’akasema.

‘Sikiliza kazi hii ndio itanifanya nikulipe deni lako,....ni kazi rahisi sana,lakini ina pesa nyingi ajabu..wewe hutaki pesa nyingi...?.’profesa akasema na huyo binti ukimtajia pesa nyingi,uso unameta meta kwa furaha

‘Unajua,mimi sikuamini,..ila kama kuna pesa nyingi kama ulivyodai,nataka ukipata kwanza unilipe deni langu, na nakuonya, safari hii,nahitajia pesa yangu mapema,la sivyo,nitakuumbua...’akasema huyo binti.

‘Wewe usijali, ...kama unataka tuandikishane,hakuna shida,nina uhakika wa pesa nyingi...’profesa akasema.

‘Inamuhusu nani,na isije ikawa kama zile kazi nyingine ambazo zitanifanya nikimbizane na polisi, sitaki matatizo na polisi....’akasema binti

‘Hiyo kazi rahisi sana,...nina uhakika  polisi hawatahusika kamwe....’akasema profesa

‘Mhh, ngoja nifikirie...’akasema

‘Hakuna muda wa kufikiria, tukichelewa, itakuwa vigumu kuzipata hizo pesa...’akasema profesa

‘Ina muhusu nani,au unataka mimi nifanya nini...?’ akauliza binti

‘Kuna yule jamaa mmoja anakuja hapa na akija hupenda kukaa pale pembeni na wewe ndiye unayemuhudumia sana....anakuja muda wa jioni....,ni mgeni mgeni sana...’profesa akasema.

‘Nilijua tu,....nyie watu,...mhh, ehe wataka nifanya nini na yule mbaba...?’akasema na kuuliza.

‘Ni lazima hawa wau tuwakaribishe mjini,...,si umemuona jamaa mwenyewe alivyo lakini...nimgeni kweli,na kuku mgeni hakosi nini,...kamba au sio,umeona kamba yake  ilivyoning’inia mguuni...haijifichi...sasa kazi zaidi nitakuelezea....’profesa akasema

‘Mhh,hapana,..unajua nyie mnamuangalia mtu kwa nje,mimi nilishamuona na nilifikiria hivyo , nikajua hata mimi mwenyewe naweza kumtoa pesa, lakini ni mumu, bakhili..sijawahi kuoana...’akasema.

‘Huyu ni rahisi sana...tumeshamchunguza kila kona,...tunachohitajia, ni wewe kucheza naye, afike kitandani....sio lazima ufikie hatua ya.....tunahitajia picha zile za kumfanya mkewe, azimie...najua hilo unalifahamu...’akasema.

‘Mhhh,.hapo pagumu, unajua halewi sana...na anajua kutumia muda, ukifika muda wake wa kuondoka, haraka anasimama, hata kama mlishafikia mazungumzo gani, hataki tena kuendelea kuongea, utafikiri kafinywa...sasa sijui...’akasema mdada.

‘Tafuta mbinu, wewe hujawahi kushindwa jambo, wewe unawajulia wanaume, sizani kama huyo atakushindwa, hata ikibidi,...tunahitaji alewe , apitilize, asijitambue, sizani kama akilewa anaweza kujimudu, hakuna anayeweza kuzitawala hisia zake kipindi kama hicho, ...’akasema

‘Si mpaka alewe, umenielewa hapo,maana siwezi kumnunulia pombe, pombe ananunua mwenyewe,...siwezi kumgharamia mimi,...nikifanya hivyo atanishitukia,...’akasema mdada.

‘Hiyo hiyo anayonunua yeye,...badala ya kuchanganya kipimo anachotaka yeye, ongeza ukali, lakini usije kuweka madawa ambayo yakipimwa, inaweza kuleta matatizo,...kwani ni lazima tuchukue tahadhari zote....najua hilo unalielewa,...na mhh,kwani hawezi kwenda kunywea vyumba maalumu vya juu, ...huwezi kufanya mpango huo...?’ akaulizwa

‘Hilo linawezekana, lakini si pesa ya mtu bhana..., jamaa huyo ni bakahili pesa yake anaitolea kwapani,wewe ukimuona akitoa pesa yake utacheka...hahaha....lakini sijui...nahitajia muda wa kumjaribisha...’akasema

‘Hatuhitaji muda wa kupoteza, sikiza, ...tayarisha pombe yake mapema, ongeza makali kabla hajafika,...akija tu, usipoteze,muda,....ongea naye, kimapenzi, nilimsikia akilalamika,lalamika ..kuna kitu wanasigishana na mkewe, na hapo ndipo pa kupenyeza sumu,...halafu unamualika juu kuwa unamuhitaji akupe company, na siku hizi za mwezi si huwa mnafanya vijisherehe vyenu, hakuna anayesherehekea siku ya kuzaliwa, sasa hapo hapo unaweza kuchezea karata yako...’akasema

‘Mhh nakuelewa sana, hayo yote lishayafikiria, ....si unajua zangu, natafuta pesa, kwa mbinu ....najua huyu jamaa ana pesa, natafuta sana jinsi ya kumtoa, lakini sikutaka kuingia kwenye mambomabaya....’akasema.

‘Haya sio mambo mabaya, ni yeye mwenyewe atajiingiza huko...yeye mwenyewe ndiye atajilengesha...’akasema.

‘Ndio maana nakuambia nahitajia mazoezi, huwezi ukamchukua mtu kwa haraka hivyo, hilo niachie nitalifanyia kazi, na kama kuna pesa nzuri una uhakika huo, haitachukua siku mbili,mimi nitatimiza nafasii yangu ...mambo mengine ni juu yako,...’akasema.

‘Haya ya juu yangu usijali, nimeshajiandaa kabisa...’akasema profesa.

‘Lakini mbaba wa watu namuonea huruma sana...nilishamuona, anajionyesha kama ananipenda sana, na wengi humu wameshaniambia mbaba, yupo hoi juu yako, hajui kuwa anapenda nyoka mwenye sumu,....hahaha, ...kiukweli,...ila simuamini...’akasema

‘Kwa vipi?’ akauliza profesa akionyesha mashaka

‘Ipo siku mkewe aliwahi kufika, alikuja kumtafuta,...sijui kwanini, haijatokea... akanikuta nipo naye, aliniangalia kwa jicho la chuki, akamshika mumewe mkono,wakaondoka naye....’akasema.

‘Kama waliondoka naye kuna ubaya gani, wewe si muhudumu tu...’akasema profesa

‘Ni wakati wanaondoka naye,...yule mkewe akawa akigeuka kunitizama mara mbili tatu,sikupenda,alihisi kitu...keshaijua sura yangu kwahiyo naogopa sana kuja kufanya makosa....sitaki uhasama na wake za watu....’akasema

‘Mkewe huna haja ya kukutana naye...eti hutaki uhasama na waume za watu, wewe, mbele ya pesa, hoo, umwambie mwingine sio mimi,..'akasema profesa na huyo binti akacheka tu

'Sikiliza, sisi tunachohitajia ni kuhakikisha muda wa tendo, unakuwa sio wewe, kisura ....hutakuwa ni wewe...si unajua zile zako, tayarisha vifaa, , ....sina haja ya kukufundisha, maana unatakiwa hiyo pesa uifanyie kazi...pesa nzuri lazima ina gharama zake....’akasema profesa

‘Kujiweka tofauti, ni gharama, vifaa hivyo ni vya kukodi, kwahiyo hapo uanifanya nitumie pesa yangu , hata sijapata hiyo pesa, je isipopatikana, ...’akasema

‘Hiyo ni gharama yako...kwenye mahesabu yako, sihitaji kulipia mimi, unajua utaratibu ulivyo...kama vipi nikate kwenye mahesabu yako’akasema profesa

‘Sawa, ...hahaha, umeshanitamanisha...kiukweli kama kuna pesa nyingi, mimi siwezi kuipotezea...utaona vumbi langu, ila nahitaji pesa zangu za nyuma kwanza, hilo utaniona mbaya, siwezi kutumiwa kama malaya, wakati mimi sio malaya...’akasema binti.

‘Umeshaanza,..pesa yako nitakulipa,...pesa itakuja kwa kazi hiyo,nilikabanwa kidogo,na yule bosi wangu, lakini sasa nimeachana naye,...’akasema

‘Sasa unaishije,...?’ akauliza

‘Ndio hivyo,mtoto wa mji mimi,...nalala siku moja na njaa, siku ya pili akili inafanya kazi, ukinipa leo kidogo ya kula sio mbaya, tutakatana mbele kwa mbele...,'akasema

'Eti nini...hahaha, usiongee kitu kama hicho,kwangu hupati hata senti moja.....'akasema mdada

'Sikiliza, wewe fuata nitakavyo kuambia...sasa ni saa eeh,...’nikaangalia saa kwa mbwembwe, nilishajiona tajiri hapo

‘Muda wake wa kufika bado kabisa.....’akasema mdada

‘Hebu kwanza nikuuliza wewe na yeye mlishafikia wapi...mumekwenda mbali kiasi gani, alishawahi kukuomba urafiki, upenzi,kuacha yale ya utani,...maana nijue wapi pa kuanzia...?’ akauliza

‘Sana sana ni porojo tu na miadi ya hapa na pale, kutongoza ndio zake, na ahadi kibao,ukifikia kwenye kutoa pochi, anashikwa na kiguumizi...akitoka ananiachia kiasi kidogo tu, ni bahili kweli...si unanijua nilivyo na mimi, wanaume bakhili ni takataka kwangu, sina muda nao kabisa, lakini huyu mmh, nilishahisi kuna pesa inakuja...’akasema

‘Nakufahamu unajua kunusa pesa...sasa tufanye kazi....nataka wewe uache umalaya kabisa, ukipata pesa hiyo unafungua salooni yako, au sio...’akasema

‘Nafahamu wanaume wengi mnanifikiria hivyo kuwa mimi ni malaya, kumbe ni maneno tu,mwisho wa siku wanakung’uta mifuko yao,mimi huyooo..lakini huyu kiukweli nina usongo naye, maana sijawahi kuachiwa pesa ndogo kiasi hicho...ananishushia hadhi yangu, nilitaka nimtumpie usoni, siku ya kwanza, lakini ....’akakunja uso kwa hasira

‘Mteja ni mfalme au sio....usisahau kunipa pesa ya kula leo,...pesa inakuja usijali kabisa....’akasema profesa

‘Usinichefue...tuongee kuhusu huyo jamaa,mimi huyo jamaa nimemlia chachandu...nitamuhangaikia,nitamfanya ajisikie yupo nyumbani, na ataingia kwenye anga zangu, atamsahau mkewe, atajikuta anafungua pochi lake hadharani....’akasema na kutoa kicheko chake cha mahaba.

‘Nakuaminia mdada,sio pochi tu...atahudhuria ATM yake na account yake kama inamdai,...wewe utaona tu...kila kitu kimeshawekwa sawa,ni wewe tu...’akasema profesa

‘Hahahaha, ni mimi tu eeh, acha wee...mimi eeh, wewe utaona mshindwe nyie...mimi ukiongelea pesa,ushaniloga,naweza kufanya lisilofanyika,..ila ....ohoo...’akasema na kuendelea kujichekesha, ...

Huyu binti akicheka, na kutabasamu, utafikiria ni mrembo wa kutoka mlimbwende wa kimataifa ni mnzuri, sio utani, tatizo ni hiyo tabia aliyo nayo, tamaa na kupenda sana pesa

‘Ulishawahi kuwa na urafiki naye wa kimpenzi...?’ kaka mtu akauliza akimuangalia ndugu yake kama anaangalia mtoto mpotevu

‘Bro, ...dau lake kubwa, simuwezi, urafiki wetu sana sana ni wa kikazi tu alishaniambia mimi ananijali kwa vile najua mbinu za kupata pesa, vinginevyo, hana habari na mimi kabisa....’akasema

‘Nilipomuona mara ya kwanza nilijiuliza kwanini mrembo kamahuyu haolewi,akawa na mume wake  wakatulia..maana ni mrembo kweli,lakini ukimgusia maswala ya kuolewa,anakuambia,hawezi kuwa mtumwa wa ndoa, na akihitajia kuolewa,ataolewa na tajiri wa kiukweli huko kwao...

‘We jiendekeze tu,uzuri wenu mungu kaujalia,lakini una muda maalumu, ni kama ua linavyochanua kwenye kikonyo, haliwezi kuchanua milele,linafikia muda linanyauka na uzuri unapotea...sasa wewe jipotezee muda wako tu...’nikamwambia

‘Kwahiyo unataka unioe wewe, kapuku, usiye na mbele wala nyuma....sitembeagi na mtu asiye na pesa....hata siku moja,ni nuksi kwangu...’akasema

‘Sio lazima mimi, nakushauri kama dada yangu, unajua nimekuzoea sana ni mtu ambaye tunafanya kazi pamoja nikipata dili, tunalindana, nikikwama unaniinua,japo kwa masimango...’akasema profesa

‘Usijali,hata mimi najijua,...najua lini na wakati gani nifanye nini,sasa hivi ni muda wa kutumia...muda wa kutulia na kupata mume ukifika hutaamini...’akaniambia siku nilipoanza kuzoeana naye

‘Basi,tuongee biashara...’nikamwambia,na kweli kila nikihitajia pesa za haraka kwa kumtumia huyo binti sizikosi, ila tatizo langu kama anavyosema,mimi nikishika pesa ni zangu, kuzitoa ....mmh,labda nikununulie kinywaji, nikiwa kwenye matumizi, natanua kweli, nanunulia watu najitangaza, ...lakini sio kutoa pesa taslimu, pesa ikiwa mkoni mwangu ni yangu...

‘Kwahiyo tuanze lini...?’ akauliza binti

‘Leo, leo hii akija wewe muanze, na hata kama leo ataingia kwenye kingi, ..mimi nipo tayari, kila kitu nimeshatayarisha, si unajua siku hizi, simu inakuwa na kila kitu...ni wewe tu, unajua zile ishara zetu...sichezi mbali...’akasema profesa

‘Sawa, muhimu tu, tusije kuonana wabaya,...ngoja namalizie hizi kazi ili nije tukae unipe mikakati yote, na kiasi changu kitakuwa shilingi ngapi....na nataka kwa maandishi...’akasema binti

‘Maandishi, ya nini , unataka kuharibu sasa...’akasema profesa

‘Na safari hii kaka yangu atakuwepo, kuhakikisha hunidhulumu...’akasema

‘Aaah, kaka wako wa nini...’akasema profesa

‘Yeye hatashiriki, na wala hatajua,  ila hatacheza mbali, nilishamwambia ikifika jioni aje, awe bodyguard , siku hizi hana kazi,...namlipa kitu kidogo, kwa siku ili asilale njaaa, sasa wewe ukinidhulumu tu, nitampa ishara na yatakayotokea mimi sipo...’akasema binti

‘Hapana hilo siwezi kukubaliana nalo...sihitaji mtu mwingine hususani kaka yako, kaka yako mimi simuamini  kabisa, ni mshari, na anapenda uchimbi, simuamini kabisa...’akasema profesa

‘Nimekuambia yeye hatashiriki, yeye anakuwa nje, kunisubiria wakati wanguu wa kuondoka, ni mimi na yeye, siwezi kumuambia leo usije wakatii tumeshapangana hivyo,....’akasema

‘Yule ananusa..anajua hapa kuna jambo, simuamini kabisa,....’akasema

‘Kama hutaki basi mimi hata hiyo kazi yako siitaki,sio lazima niifanye mimi , tafuta mtu mwingine...nimeshakuambia safari hii sitaki kudhulumiwa, nimeshafanya kazi zako nyingi, na mwisho wa siku naishia kudhulumiwa, ....sasa uamuzi ni wako...’akasema binti

NB: Habari ndio hiyo, lakini usiige, ni hatari,ni mbaya..utaona mwisho wake...

WAZO LA LEO: Penye dhuluma, hakuna kuaminiana kila mmoja anataka zaidi, kwani mwenye tabia ya kudhuluma huwa hatosheki, kajawa na roho mbaya, na kwa vile ni dhuluma, mwisho wake watu haohao walioshiriki kwenye kudhulumu wenzio huja kuumbuana wenyewe kwa wenyewe.

Dhuluma ni mbaya, dhuluma ni laana, na kama usipojirekebisha mapema, dhuluma hiyo hutafuna baraka ya riziki kama kansa inavyotafuna uhai wa mtu, kama asipowahiwa haraka kutibiwa. Tuache dhuluma, na tutosheke na riziki ya halali ya jasho letu.
Ni mimi: emu-three

No comments :