Profesa
alichukuliwa na kaka yake hadi kijijini, huko akagiza dawa anazojua yeye
mwenyewe aletewe maana hata kutembea hadi huko maporini ilikuwa ni shida,
kiukweli mtu huyu alishakuwa mtaalamu wa dawa za mitishamba, lakini kilichokuwa
kikimuharibu ni tamaa, na tamaa yake hiyo ikampelekea kuwa muwongo, akawa sasa
anaongeza chumvi, ili kupata zaidi.
‘Kaka naomba
ukanitafutie huu mti, na mizizi yake,...na huu mti na majani yake, ukinieletea
nitatengeneza dawa yangu mwenyewe ...sihitaji kwenda kutibiwa
hospitalini....’akasema
‘Kwanini
usiende kupimwa kwanza ukajulikana unaumwa nini?’ akashauriwa.
‘Najua
watakuja kutaja maradhi makubwa..na nyie mtakata tamaa...mimi najua dawa za
maradhi haya, dawa hizi huongeza CD4, mnajua CD4 nyie...hamjui kwahiyo
niachieni mwenyewe,..’akasema
‘Hali uliyo
ayo si yakuuguliwa nyumbani, ....’akazidi kuambiwa
‘Nyie
msijali, najua nina maradhi makubwa, lakini nitapambana nayo, nyie nileteeni,
hivyo nilivyowaagiza, nikitengeneza hizo dawa , nitapata nguvu na huenda maradhi hayo
mengine hayatakuwa na nguvu sana....’akasema huku akijaribu kujiinua kwa shida
‘Kwahiyo
wewe unafahamu unaumwa maradhi gani, kwanini hutuambii,....?’ akaulizwa
‘Kaka nyie
fanyeni hivyo....ili nisje kuwakatisha tamaa,mnavyozidi kuniuliza mnapoteza
muda,au mnataka nife....’akasema na kaka yake akafanya hivyo, akaenda
kumtafutia hiyo miti shamba
Na kweli
dawa alizotengeneza alipozitumia, akaanza kubadilika, afya iliyozorota, ikaanza
kutengamana, akaanza kuingiwa na siha, na mwili wake ukarejea katika hali
inayorizisha, japokuwa sio kama awali, ila akaweza kuanza maisha ya kijijini,
na kuanza shughuli zake za madawa, japokuwa baadhi ya watu walishaanza
kutokumuamini
‘Huyu ndugi
yako katumia dawa gani maana ulisema sio mtu wa kuishi, ...?’ watu wakaanza
kuhoji
‘Mhh, mungu
mwenyewe ndiye anajua, si mlishasikia ni mtaalamu wa miti shamba,
kajitengenezea mwenyewe, .....’akasema na hilo likasaidia kuwavuta watu kuja
kununua dawa kwake.
Siku moja
akiwa katulia, kaka yake akamjia na kumuuliza maswali
‘Je
unakumbuka ahadi yako?’ akaulizwa
‘Ahadi gani
tena kaka yangu, maana niliyoahidi kwa watu ni mengi, na niliyowahi kutelekeza
ni machache, na hilo linaniuma sana....nilikuwa mtu wa kuahidi hata
yasiyotekelezeka,...ili tu niweze kupata chochote....’akasema huku akitikisa
kichwa kwa masikitiko.
‘Kwanini
ulifanya hivyo, hukujua kuwa ahadi ni deni?’ akaulizwa
‘Nilijua
hilo, lakini tamaa ya kupata, hata kama najua ni ulaghai ilikuwa mbele yangu,
nilikuwa kama mafundi ambao hupenda kupokea kazi mpya kila siku, bila kujali
ahadi ya kazi za awali, ambazo hajazitekelezeka, na ndio maana mafundi wengi
sio waaminifu, hata sisi waganga, hasa wakienyeji tunafanya hivyo, wengi wetu
ni waongo...’akasema
‘Na wewe
ulikuwa fundii wa hadaa, fundi wa kuwarubuni watu, ukitumia ulimi wako na
taaluma ndogo aliyokuruzuku mungu ya ulimi, ukautumia ulimi kwa masilahi yako
binafsi,hujui ulimi unaweza kukuingiza motoni ...’akasema kaka mtu
‘Nimekuelewa
kaka, na najitahidi kujirekebisha, ila najua unalo jambo, ulitaka kunikumbusha
ahadi gani niliyowahi kuiahidi...?’ akauliza huku akijikuna kichwa kwa mashaka
akihisi labda kuna deni anadaiwa.
‘Ulisema
utatuhadithia, maisha yako ya huko Ulaya, na kijana wetu ili watu wapate
kuelemika, hebu tuambie ilikuwaje hadi ukaingia jela,.je kijana wetu huko
yupoje, na atarudi lini...?’ akaulizwa
Tuendelee na
kisa chetu
**************
‘Kaka wengi
wetu tunaamini kuwa ulaya na marekani ni kama sehemu yenye asali na maziwa, kuwa
ukifika huko utachota na kunywa,...kiukweli maisha ya huko ni magumu, hasa
ukiwa huna kipato cha kuaminika....hata wale wenye kipato huishi kwa kubana
matumizi kweli kweli...wanaishi kwa bajeti...’akatulia.
‘Kwanza ujue
kama nchi, kama eneo husika, kuna namna ya kuhakikisha kila mtu analipa
kodi,...’akashika simu yake na kuiinua juu
‘Wenzetu
wana mitandao ya kukusanya kodi, hii simu usiione ivi unatumia tu, lakini kule
inakuwa kielelezo cha kukujua wewe upo, wapi..na kwa vile umeshajiandikisha
kama raia, au mgeni, popote utakapokuwep utajulikana tu.....’akawa anafunga
funga dawa zake
‘Kwahiyo
wewe kama raia huna ujanja wa kukwepa kodi, ...kule hakuna muda wa kupoteza,
kila mmoja yupo mbio mbio, kutafuta pato la siku maana usipolipata ujue una
deni la kodi ya serikali, una deni la sehemu unapoishi, na wewe unatakiwa ule,
na kule hakuna mjomba au shangazi kuwa utakwenda kudowea, kwake kuwa usibiri
kiive ule huko hakuna ukikuta mwenye anakula ujue utameza mate tu..hata
akibakisha hakupi, anakwenda kutupa, maana sio bajeti yako....’akasema
‘Hata ukiwa
umekwama, huna hela ya kula, huwezi kwenda kuomba...kwa jirani, au kwa ndugu
labda ukakope tena kwa riba, kwasababu gani yeye keshapanga bajeti yake ya
siku, kutokana na kipato chake anachopata...’akatulia
‘Mimi
nilipofika awali, dawa zangu zilipendwa,..unajua tena kipya kinyemi, zikawa
zinasaidia watu, laikini siku zilivyokwenda wenye dawa kama hizo wakawa wengi,
ukawa ni ushindani tena wa biashara, na mimi nikaanza kuyumba,...’akatulia
‘Na
kilichonisaidia sana awali, ambachoo kilinidanganya ni zile pesa za misaada
niliyokuwa nikipata kwa ajili ya kuwa mlezi wa huyo kijana, niliaminika kama
mlezi wake, kwahiyo nikapewa dhamana ya kupokea pesa zake, lakini hilo lilikuwa
na mwisho wake, maana yule kijana naye alifikia umri wa kufanya kazi, na kweli
akapata kazi na kuanza kujitegemea..hapo ule mrija wa ruzuku
ukaziba,...’akatulia
‘Hao
wadhamini ni wale ambao wanazalisha kwa wingi, wapo watu wa namna hiyo wenye
ubiandamu, lakini sio wote...’akatulia kidogo
‘Bashara ya
dawa ikawa haina mauzo..., siku inaweza kupita bila kuuza chochote, na njaa
ikaanza kuninyemelea, nikaona sasa naumbuka, mwanzoni, ikabidi nimuendee
kijana, nimuombe msaada, na yeye kama walivyo wengine wa daraja hilo, alikuwa
na bajeti yake ya maisha,..mwanzoni alinisaidia,kidogo,lakini alipoona nazidi
kuja kumuomba, akaanza kunikatalia
‘Kijana,
unajua mimi ni baba yako..?’ nikamwambia
‘Ni baba
mlezi ndio natambua hilo, lakini maisha kama unavyoona, siwezi kukubeba
zaidi,.....’akasema
‘Hicho unachopata
tugawane, la sivyo nitakuja kusema wewe hukuwa yatima..unakumbuka ulipotoka,
bila mimi usingelikuwepo hapo ulipo....’ikafikia muda nikamtishia hivyo
‘Hahaha, dad,
...usinitishe kwa hilo, na kwa vile umelitamka hilo, kuanzia sasa ujua maisha
yako mwenyewe, na kama unataka kunipakazia, hivyo, nenda kasema,....mimi
siogopi...’akasema kwa hasira, na toka siku hiyo akawa hataki hata kuniona
‘Basi siku
ya siku, nikaibiwa vitu vyangu vyote, nikamuhisi kuwa ni yeye kijana alifanya njama hizo kwa kutuma watu
kuiba vitu vyangu ili akipate hicho cheti cha kuzaliwa, nilichokuwa nikimtishia
nacho kuwa nitakionyesha na itajulikana kuwa yeye hakuwa ni mtoto
yatima....’akasema
‘Na kweli
ulipanga kufanya hivyo kwa kijana wako mwenyewe kama hakukusaidia...?’
akaulizwa
‘Maisha ya
Ulaya ni ushindani, na kila nafasi unatakiwa uitumie, kwa jinsi alivyonifanyia,
...sijui, hata wewe huoni mbona mimi hajanionea huruma, mimi nilimpenda sana
kama mtoto wangu lakini yeye hakunijali...’akasema
‘Sasa
kwanini ulipoona hali ni mbaya kwanini usingelirejea nyumbani kwenu mapema, una
nyumba yako, una biashara zako na ulishajenga jina huku...ungalifanya hivyo mapema
yote haya yasingekupata...?’ akaulizwa
‘Ukionja
asali, huwezi kuonja mara moja,akili ilikuwa na hamu ...nilijua ninaweza
kufanikiwa,tamaa ilikuwa mbele, na pia aibu, si unajua tena ...hata hivyo
ningeondakaje kirahisi hivyo, sina nauli, nadaiwa....’ akasema huku akitabasamu
kwa aibu.
‘Balaa
halikuishia hapo, mimi kwa kukosa soko, nikawa nafanya biashara zingine haramu,
huku nauza dawa, huku nauza madawa ya kulevya, nikaja kugundulikana,
nikashitakiwa, nikafungwa, ...’hapo akatulia kidogo kama anakumbuka jambo.
‘Japokuwa kifungu
hicho cha mwanzo kilikuwa ni kidogo tu, kwasababu hakukuwa na ushahidi wa moja
kwa moja, nilitakiwa kulipa faini, na sikuwa na pesa,...niliomba wamuone kijana
wangu ili anilipie, lakini hakupatikana, nahisi alikataa, japokuwa sikuweza
kuonana naye kwa kesi hiyo, basi ikabidi
nifungwe tu..nikaja kuachiwa, hata kabla muda haujaisha.
Nikaendelea
na biashara zangu, lakini hakukuwa na masilahi, siku moja wakaja watu wa vibali
vya kuishi huko, nikakamatwa tena, kwani waligundua kuwa hata kibali changu cha
kuishi huko kilikuwa kimekwisha, ...’akatulia
‘Ikabidi
nifanya mipango ya kuongeza muda,...ilihitajika pesa tu, tatizo sikuwa na pesa,
nikaona sasa nitarudi nyumbani, lakini nitarudije na mimi sina kitu.. nikakopa
kopa pesa kwa washikaji..., nikafanyiwa mipango nikapata hicho kibali cha muda,
lakini kibali hicho kilikuwa na masharti,...aina za biashara na kazi..kwahiyo
hapo nikawa nafanya kazi zile za muda muda tu, hutaamini nilifikia kufanya kazi
za kufagia barabarani, kuomba kazi hata za kusafisha vyoo kwa wazungu,....’akatulia
‘Nikakutana
na matepeli wa huko, wakaniingiza kwenye biashara nyingine haramu,..mbaya hata
siwezi kuzihadithia,...hizo zikanifanya niwe mbaya wa watu, maana nikajikuta
nafitinisha watu kwa kutafuta machafu yao na kuyauza ili watoe pesa...maisha
magumu ajabu...ilikuwa nikipewa kazi ya kusafisha vyoo, au kazi yoyote ndani
naweka vifaa vingine kuchunguza watu wanavyoishi, na kuwafanyia
utapeli,..nikaja kugundulikana...
‘Haikupita
muda, kukatokea mauaji, na ikaonekana mimi nami kwa namna moja au nyingine
nilihusika,..lakini haiuwa ni kweli, lakini sikuwa na jinsi ya kujitetea,
wakiangalia kumbukumbu zangu za nyuma, nikaonekena na mimi nilikuwa ni chanzo,
..na kesi hii ikawa ni mbaya kwangu, wenzangu wakaniruka, nikabakia peke yangu,
na hukumu ikatolewa kufungwa miaka mingi tu...’akatulia
‘Ilitakiwa
nipate wadhamini ili nitoke kwa dhamana, kwani nilikata rufaa, lakini nani
atanidhamini, nikaomba aitwe kijana wetu aje kunidhamini, kijana akakana kuwa
hanijui,....niliomba angalau aje tuongee, na siku alipokuja akanipa makavu
makavu, kuwa yeye hana baba tapeli, mwizi, muuza madawa ya kelevya, hanijui na
wala nisimjue,....’
‘Kijana
naomba unidhamini, maana kesi hii nimebambikiwa tu, nitashinda, nikishinda
nitakulipa gharama zako...?’ nikamuomba hadi kumpigia magoti, lakini aliondoka
huku akisema;
‘Its too
much, nimekukopesha pesa nyingi tu ambazo hata huwezi kunilipa ..siwezi kabisa
kukubeba tena, na kwa jinsi ulivyo utanifanya hata mimi niingie kwenye
matatizo...., siwezi...sikujui na usinijue...’akasema na kuondoka, nililia sana
siku hiyo maana ndani ya jela nilikuwa
na maadui wengi, na walishapanga kunifanyia ubaya
‘Kiukweli
jela niliyofungwa kipindi hiki cha mwisho ilikuwa ile ya watu wabaya,..huko
nikageuzwa mtumwa wa machafu...sijawahi kuteseka kama nilivyoteseka hapo,
nikaanza kuumwa...na hukoo kuumwa ndiko kuliniokoa, kwani nililazwa
hospitalini, ikabidi niombe niendelee kuumwa....’ akasema
‘Ina maana jela
huko ni kubaya sana, mbona kuna vijana wanataka wafike huko hata kama ni
kufungwa wafungwe, wanavyodai huko jela, ni bora kuliko maisha wanayoishi huku, ..ndivyo wanavyodai
wao...?’ akaulizwa
‘Asikudanganye
mtu, ukumbuke jela, kuna watukutu, wengine ni wabaya kweli,...wasiotosheka,
wenye tabia mbovu,...hata kama wangepewa nini bado kuna ubabe,...kuna dhuluma,
kuna tabia chafu...huna uhuru,...jela ni jela tu hata kama
kungekuwaje,...hakuna jela nzuri...sijawahi kufungwa hapa nchini, lakini
usiombe kwenda jela...sipendi kuwaficha, jela ni mateso,...’akasema
‘Wakati
nafungwa nilikuwa na madeni mengi, ya kodi za serikali, ya watu, na wengine
nilikutaa nao huko jela, wakanigeukia....kwahiyo sikuwa na amani, nilijua hata
nikitoka bado nitajikuta kwenye maisha magumu, ...ndipo nikakumbuka kuwa
nyumbani ni nyumba yenye thamani kubwa, nikatafuta wakili, akanisaidia, nikiwa
nimemuahidi kumlipa kutokana na mauzo hayo ya nyumba..
‘Kwa vile
ile kesi niliyofungwa ilikuwa ya kutengenezwa, ili maadui zangu wanikomoe,
wakili wangu akaenda kuongea na hao watu, kuwa nitawalipa kiasi fulani, na wao wakaona hakitaharibika kitu.., basi mambo
yakawekwa sawa, ikakubalika hivyo...
‘Huyu wakili
ulimpataje na wewe huna pesa...?’ akaulizwa
‘Yupo jamaa
anatokea huku ananifahamu, na anajua kuwa kweli nina nyumba yenye thamani kubwa,
huyo ndiye aliyefanikisha hilo.....akijua kuwa kweli ikiuzwa atarejesha gharama
zake pia, maisha ya sasa ni ushindani, ukiona sehemu ina masilahi unabahatisha,
na huyo wakili ndio maisha yake, akabahatisha hivyo, na kweli kafanikiwa....’akasema
‘Mhh,
...kwahiyo kesi ikaisha tu kihivyo...ina maana hata huko rushwa ipo?’akaulizwa
‘Hakuna
sehemu kusipokuwa na rushwa, hata hivyo yangu haikuwa ni rushwa, ni kitu kipo
moja kwa moja, walionishitakia walihitaji fidia kubwa ili esi hiyo ifutwe...,
mimi nikawa sina na kiukweli sikupatikana moja kwa moja kama muuaji, basi tu ,
ni kutokana na tabia yangu, na jinsi nilivyokuwa nikichukua machafu ya watu na
kuyatumia kuwatishia, wasiponipa pesa nawatangaza, nikaonekana mimi ni mchochezi,
unaona hapo....’akasema
‘Hutaamini,
...nikaachiwa hivyo kuwa nirejeshwe nyumbani na mali yangu iuzwe madeni ya watu
yalipwe, na nisionekane tena huko ulaya..na hiyo ikawa ndio salama yangu...na
kwa muda huo nilikuwa naumwa kweli, hali yangu ilikuwa mbaya sana... waliniona
kama mzigo tu wakaona bora nirejeshwe nchini kwangu....’akatulia
‘Ndio
nikasaidiwa hivyo,na huyo wakili akafanya taratibu zote, nikarejeshwa nyumbani
na mali zangu zikapigwa mnada,wakili akachukua kilich chake nyingine zikalipia
madeni ya watu ....na ikawa mwisho wa maisha yangu , sasa sina kitu nipo nipo
tu....’akasema
‘Pole
sana..lakini vipi maisha ya kijana wako, maana sitaki hata kumuita kijana
wangu, huyo ni kijana wako uliyemtengeneza wewe mwenyewe maana kaharibikia
mikononi mwako, hebu tuambie,unasema
ameshaoa mwanamke, tena mwanamke wa
kizungu..., je maisha yake yapoje...na vipi anatarajia kurudi huku kwao tena..?’
akaulizwa
‘Mhh...maisha
yake ni ya kawaida tu, kwa vile ana kazi, na aliyemuoa ni binti anayetoka
kwenye familia ya kawaida tu,japo, haikuwa rahisi hivyo kumpata ...unajua huyo
binti nilimfanyia mimi mipango,.. ..lakini yeye hilo halikumbuki, keshasahau...’akasema
‘Ulimfanyia wewe mipango kwa vipi....?’ akaulizwa
NB,
Tutaliona hilo sehemu ijayo.
WAZO LA LEO: Unapoamua kubeba majukumu, ujue
kuwa mzigo huo ni wako, na utawajibika nao, na unatakiwa kuufikisha sehemu
husika salama. Unapoamua kulea mtoto wa mwenzako ujue huyo ni mtoto wako
umtendee vyema, kwa kumlea vyema, kama vile ambavyo ungelimtendea, au kumlea
mtoto wako, na ujua akiharibika wewe ndiye mwenye kulaumiwa, kwani ilivyo kila
mmoja atakuja kuulizwa kila kilichokuwa mikononi mwake, jinsi gani
alivyowajibika nacho.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment