Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, June 19, 2015

RADHI YA WAZAZI-7


Baada ya kama miaka kumi na miwili hivi mingine wakati watu wameshaanza kusahau, na hata watu wa usalama wakawa wamekata tamaa kufuatilia hiyo kesi, mara siku moja ikaja taarifa kuwa Profesa karudi, na yupo kituo cha polisi, na karudi akiwa kasindikizwa na watu wa usalama wa kimataifa...

Aliyepewa taarifa hiyo alikuwa kaka mtu, akaambiwa ndugu yake yupo polisi anatakiwa kwenda kumdhamini la sivyo ataishia jela

‘Mimi siwezi kupoteza muda wangu na mtu kama huyo...’akasema kaka mtu akiwa kajichokea, na mkewe akamwambia;

‘Usifanye hivyo huyo ni ndugu yako, na huenda kaja na mtoto wako....’mkewe akamwambia

‘Na hata kama kaja na huyo mtoto, mimi atanisaidia, ...?’ akauliza

‘Swala sio la wewe kusaidiwa, lakini ni muhimu kama baba kwenda kujua ukweli, na ikibidi utoe msaada...’akaambiwa

‘Mimi nitatoa msaada gani, maisha yetu tunajua wenyewe, niharibu nauli yagu hadi huko, haya nikifika huko nikatakiwa kudhamini, au kuna kitu cha kulipa nitapatia wapi hizo pesa, ....’akasema akiwa hataki hata kusikiliza

‘Lakini fanya juhudi, hata ikibid kuuza mbuzi, ..’akaambiwa

‘Hivi wewe hujakutana na hao watu, eeh,..mfani haya nikienda huko, nikakutana na huyo mtoto,na huyo mtoto akija kunikana mbele za watu nitasema nimekwenda kutafuta nini, si kwenda kujisononesha na kujiletea magonjwa ya moyo kwa hasira, niache, waache kama wapo jela, dunia iwafunze....’akasema

‘Lakini ujue hapo labda yupo mtoto wako, na huyo ni ndugu yako ni muhimu uende tu ukajue ni nini kinachoendelea, unafikiri ukiamua kuchukulia hasira dunia itakuwaelewaje...mfano wazazi wako wangelikuwa hai ungelifanya hivyo, ujue huko walipo wanakuona..na wewe ndiye kaka yao mkubwa ....’akaambiwa

Baada ya ubishani wa muda, kaka mtu akakubali kufunga safari kwenda hadi kituo alichoshikiliwa ndugu yake, alipofika, akakutana na wahusika ndipo akaanza kupewa taarifa kamili.

‘Huyu ndugu yako karudishwa kutoka huko alipokuwa anaishi....’akaambiwa

‘Najua alikuwa huko Ulaya sio, kwanini sasa arudishwe yeye si alishaukana utaifa wake, na huyo mtoto naye yupo wapi...?’ akauliza

‘Sisi tumempokea ndugu yako kwa taarifa ndefu ya makosa yake, kwanza huko alipokuwa akiishi kibali chake kilishaisha muda wake, akawa anaishi kwa kujiiba iba...hata hivyo, pamoja na hayo, aligeuka kuwa tapeli, na muuza madawa yasiyokubalika...na makosa meng mengi.....’akaambiwa

‘Nilijua tu mwisho wake utakuwa huo, huwezi kuishi kwa maisha ya kuhadaa, sasa ikawaje..kwanini mnamshikilia....hapa nchini aliondoka akiwa kaacha nyumba yake,...na pia alikuwa na biashara zake, kwanini asiende kwenye nyumba yake, na biashara zake?’ akaulizwa

‘Huko alipokuwa akiishi, ilifikia muda hana kazi, si unajua maisha ya huko, kuna kulipia kodi ya serikali, pia kulipia pango alipokuwa amepanga, ...watu wakaja kumgundua kuwa ni tapeli wa dawa zake..., na muda huo alikuwa na madeni mengi ya watu, ...akashitakiwa, na kuswekwa, ndani, huku akitakiwa kulipa madeni ya watu....’akaambiwa

‘Kifungo cha utapeli kilipoisha, akatakiwa kulipa madeni ya watu, akawa hana pesa, kwahiyo alitakiwa kuendelea kufungwa, ...lakini akawa ameahidi kuwa huku nyumbani ana nyumba na miradi ambayo inaweza kulipa hilo deni....akadhaminiwa na watu wanaomfahamu....’.

‘Basi ndio akarejeshwa huku, akiwa kaambatana na watu wa usalama, na hao walimdhamini, na wakaja huku kupiga mnada hiyo nyumba, na duka lake la dawa, ...kwahiyo amerudi hapa akiwa hana mbele wala nyuma, ukizingatia kuwa huko katokea kifungoni kwa makosa ya utapeli, na wizi wa hadaa....’

‘Sasa hivi haruhisiwi kusafiri nchi yoyote, atakuwa hapa hapa nchini kwa kifungo cha nje...na tulihitajia mtu wa kumdhamini, kama wewe ni kaka yake basi ubebe hilo jukumu...’akaambiwa kaka mtu,na kama mtu kwanza alikataa, lakini alipoambiwa kama hakuna mdhamini ndugu yake anakwenda kufungwa jela ya ndani, udugu ukamjia, akakumbuka kuwa wazazi wake walimuachia majukumu ya kulea ndugu zake, akasema;

‘Na mtoto aliyekuwa naye?’ akauliza

‘Hana cha mtoto, tumemuuliza,anasema mtoto alimkana, na kwa vile mtoto alikuwa na cheti cha kuonyesha kuwa yeye ni yatima, na ndivyo alivyoandikishwa huko, ikawa haina nguvu,....sisi tumempokea yeye, mengine yatafuta baadaye, kama waliomshitakia watafufua kesi iendelee haya....’akaambiwa

‘Kwahiyo hata yeye kakanwa na mtoto, kuwa yeye sio baba yake, si mlisema alikuwa na cheti cha kuonyesha kuwa yeye ni baba yake...?’ akauliza

‘Tulimuuliza, lakini huko nje cheti hiko hakikutambulikana, hakuweza hata kukionyesha, na hakutaka hata kukitoa, anasema vitu vyake vyote viliibiwa, kwahiyo hajui wapi kilipo, hata hivyo, mtoto mwenyewe hamtambui....’akasema mtu wa usalama

‘Basi naomba niongee naye kwanza kabla sijakubali hiyo dhamana, maana anaweza kunikana, ....’akasema kaka mtu

‘Kwa hali aliyo nayo hawezi kufaya hivyo, alishakutaja kuwa wewe ndiye ndugu unayeweza kumsaidia,....sasa kama wewe utakataa, kubeba hiyo dhamana, sis hatuna jinsi inabidi tukamfunge jela ya ndani...’akaambiwa

Basi kaka mtu ikabidi akaongee na mdogo wake, na alimkuta mdogo wake kalazwa kwenye kitanda cha wagonjwa, kwa hali aliyomkuta nayo, alivyoisha, kakonda, mgonjwa, na kawa mzee hata kuliko yeye, akajikuta machozi yanamlenga lenga, ...na mdogo mtu alipomuona kaka yake, akaishia kupiga magoti huku akilia

‘Kaka nisamehe sana..najua nimewakosea, lakini nilichofanya wakati huo ilitakiwa kiwe hivyo, nikiwa na nia ya kumsaidia mtoto, ..japokuwa pia niliona ndio nafasi yangu ya kujipatia maisha mazuri...’akasema

‘Kwa kupitia mtoto wa watu, utapeli na dhuluma au sio, ukamuharibu huyo mtoto, ili asiwatambue wazazi wake....si ndio hivyo?’ akaulizwa

‘Mimi sikumuharibu kihivyo, sikuwahi kumuambia asiwatambue wazazi wake, siku zote nimekuwa nikimsihi kuwa mimi sio baba yake hasa, nilimwambia wazazi wake wapo, ndio maana kipindi kile nilikuja naye, lakini hakukubali...’akatulia

‘Huko Ulaya aliandikishwa kama yatima ili aweze kusoma, na nilifanya hivyo ili apate hiyo nafasi,....na kiukweli nilijitahidi sana ili awatambue wazazi, wake..hasa tukiwa huku, lakini mtoto mwenyewe ndiye alikataa,ningefanya nini, na mimi pia nilihitajia hiyo misaada, ili maisha yaendelee..hilo nawathibitishia..kuna mengi mengi sana....’akasema

‘Lakini chanzo cha kuharibika mtoto ni wewe, kama usingelifanya hayo yote haya yasingelitokea...ukajifanya unajua zaidi, ukitaka kuchuma kwa kutumia migongo ya wenzenu...’akaambiwa

‘Ndio hivyo..hil nakiri kuwa nimefanya kosa, naombeni mnisamehe..maana hapa naumwa, sijui mbele wala nyuma, kila nilichokuwa nacho kimechukuliwa, na huko ulaya nadaiwa, hayo madeni ni baadhi tu, kuna watu walishaapa kuwa wakiniona wataniua kwahayo niliyowafanyia, najuta kabisa...na sizani kama nina muda mrefu wa kuishi....nisamehe kaka yangu...’akasema

‘Leo umefikia hivyo, kujiamini kote kumeishia hapa, siamini, wewe tulikuwa tukifika kwako unatuona kama wachafu, watu wa kijijini, tusiojua maisha,...hahaha, kweli ishi uone...sasa hali yetu unaifahamu mimi nitakusaidia nini...?’ akauliza kaka mtu

‘Yaani hapa nilipo, japo maisha nayatamani, lakini sina halii ni bora ya mfu, nimeshakuwa zaidi ya masikini...kaka wewe ni dhamini tu nisiende jela, najua kabisa nikienda huko sitaishi, nitakufa tu....’akawa analalamika

‘Hiyo ndio adhabu ya mtu kama wewe, mali yote uliipata kwa ujanja ujanja, kuwatapeli watu,ukajiona umesoma sana, unajua kila kitu sheria wewe, kila kitu wewe, sisi wazee wako ukatuona hatuna maana ...na adhabu za watu kama nyie zinaanzia hapa hapa duniani...sasa sijui kama utaweza kuishi maisha ya huko kwetu kijijini....’akaambiwa

‘Na ukumbuke kuwa huko bado una kesi, unatafutwa kwa kuiba mtoto wa watu,, ukamtumia kwa mambo yako...kule nilipokuwa nimeoa, wameahidi kuwa ukionekana tu kesi ipo pale pale....umefanya mama wa watu hajitambui....’akaambiwa

‘Lakini mimi sikumuiba huyo mtoto, nilimuokoa na ushahidi nilikuwa nao, ukienda kwenye mtandao utaona...hilo ni kweli kabisa.., na kama wenyewe mnamuhitaji, huyo mtoto muende huko alipo, mkamchukue, mimi kazi yangu ya kumsomesha, ilishakwisha,  kwanza sasa hivi sio mtoto ataweza kujieleza mwenyewe, ...’akasema

‘Sasa kwanini hukurudi naye...?’ akaulizwa

‘Aaah, mimi sitaki hata kuonana naye tena, kaniharibia kila kitu, kanikana kuwa hanijui, wakati mimi ndiye niliyemfikisha hapo alipo...’akalalamika

‘Ina maana hata wewe amekukana...kuwa wewe sio baba yake, wewe si ulikuwa na cheti cha kuzaliwa cha huyo mtoto...ukadai kuwa wewe ndiye baba yake halali....?’ kaka mtu akamuuliza

‘Nimeshawaambia vitu vyote niliibiwa, ..cheti cha kuzaliwa kilinisaidia hapa nchini tu, huko ulaya hakikutakiwa kuonekana kabisa....na ilifika mahali sikuwa na cha kujitetea, na ambaye angeniokoa kwenye hilo tatizo na huyo mtoto, lakini akajifanya hanitambui, baada ya kuambiwa nina madeni mengi, na hasa alipotajiwa kuwa nina kesi inayonikabili....’akasema

‘Ulikuwa na kesi gani?’ akaulizwa

‘Aaah, kesi ya ...tuyaache hayo, ilibidi nianza maisha hayo, sikuwa na ujanja ningeliishije huko ulaya. Ujue kazi ya wafadhili kwa walishamaliza na ikafikia kijana ana kazi yao, na kuweza kujimudu, nikawa sipati kitu tena...nilitegemea yeye atanitetea, anisaidie lakini ndio hivyo...kanikana...kuna mambo ya ajabu sana alinifanyia huko,sikuamini,....’akawa anaonyesha huzuni

‘Sasa huyo mtoto yupo wapi, maana sasa sio mtoto tena si umesema ana kazi au sio ana kazi gani sijui, ...au ndio kaandikishwa uraia wa huko nje...tunajua sasa sio mtoto ana maisha yake, na hatutaki kumuingilia, keshakuwa mkubwa msomi au sio..lakini sisi bado tunataka kujua yupo wapi na huko anafanya nini...na muhimu ni mama yake ambaye hajiwezi, haachi kumtaja mtotowake hadi hii leo...?’ akaulizwa

‘Nitawaambia kila kitu ili watu wajifunze, ..lakini kwanza kaka naomba unitoe humu, nikapate dawa...kuna dawa zangu nikizipata najua tatizo hili litakwisha, na dawa hizo zipo huko kijijini.....’akasema, na kaka mtu akacheka, kichwani alikuwa keshakata tamaa, alijua huyo mtu anapeleka maiti, kwa hali aliyo nayo alijua hatamaliza mwezi..

‘Kaka nina mengi ya kuwahadithia ili watu wajifunze...maisha ya ulaya mmh, hapana...ni bora huku kwetu kijijini...’akasema

‘Leo unaona kijijini ni bora ehe....haya ukawahadithie wenzako huko kijijini, ili wakuelewe...wenzako wanasema heri wakafungwe huko ulaya kuliko maisha wanayoishi nayo sasa ...’akasema kaka mtu akigeuka kuondoka

‘Hawajui tu....nitawasimulia ...kule hakuna ujanja, kama huna kazi, umekwisha, kama huna kibali cha kuishi huko...kaka nitoe humu...tafdahali nipo kwenye miguu yako...’akawa anaendelea kupiga magoti

NB: Tutaona hayo kwenye sehemu ijayo


WAZO LA LEO: Mwisho wa dhuluma, ni fedheha tu, mungu atakuachia utambe, ujione unacho, ujione wewe mjanja, ujione wewe umefika ...lakini muda utafika, utabakia kujuta, na majuto ni mjukuu huja baadaye, ukiwa huna mbele wala nyuma. Acha dhuluma, tafuta riziki ya halali, hata kama ni kwa shida, kwani riziki ya halali ina baraka.

Ni mimi: emu-three

No comments :