Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, June 18, 2015

RADHI YA WAZAZI-6


 Kaka wa profesa alikuwa ndio keshafika mlangoni na muda huo kijana naye alikuwa ameshaingia akiwa katokea kwenye masomo ya ziada, au kama ijulikanavyo `tuition’ na alipofika tu haraka haraka akawa anaelekea kwenye jokofu, na ndipo wakakutana na baba na mtoto, na wote wakasimama, wakiangaliana.

Baba hakuamini jinsi mtoto wake alivyovaa, na masikioni kaweka vitufe vya kusikilizia mziki, kutoka kwenye simu, na jinsi alivyovaa huwezi kufikiria ni mwanafunzi,...

‘Ni nini hiki....’akasema baba mtu, na kijana akatoa zile waya masikioni akamwangalia huyo mtu aliyesimama mbele yake, kwa muda ule kwanza hakufahamu ni nani, ndipo akauliza

Who are you....?’ akauliza japo sasa alishamkumbuka

‘Hiyo ndio salamu yako kijana kwa baba yako,...hiyo ndio adabu uliyofundishwa na baba yako mdogo, au ndiye amekuharibu kiasi hiki..., hebu angalia ulivyovaa, ni kama muhuni gani sijui,....hivi kweli huyu ni mwanafunzi au ni mtu gani, wewe bwana mdogo ni nini kavaa huyu mtoto,...?’ akauliza kaka mtu

‘Bro....huo ni utandawazi bro, ni wakati wa huo..., sasa hivi wapo likizo, sio lazima kuvaa sare za shule, wanajifurahisha vijana,...’ilikuwa sauti ya profesa akija, akijua asipofika hap kunaweza kutokea sintofahamu.

‘Sasa ndio hata salamu hakuna wakiwa likizo hawasalimii, ndivyo walivyofundishwa huk shuleni kwao...?’ akauliza

‘Wewe kijana,...hamfundishwi kusalamia wakubwa....?’ akauliza

‘How are you sir....?’ akasema

‘Sema shikamoo baba...hawayuu, hawayuu..wewe ni mtanzania unatakiwa usalimie kwa lugha yako yenye kuonyesha adabu....’akasema na kijana akasimama akiwa anataka kupita.

‘Hutaki kusalamia sio, nikufundishe kusalamia.....?’ akamuuliza

‘But, nimeshakusalamia, unataka zaidi...’akasema kijana

‘Mimi ni nani kwako?’ akauliza

‘Sijui....sikujui....’akasema

‘Hujaambiwa kuwa mimi ni baba yako...?’ akaulizwa

‘Kiukweli, ...hata kama nimeambiwa, lakini huwezi kunilazimisha kuwa wewe ni baba yangu...mimi hadi nimefikia umri huu, najua kuwa mimi ni mtoto yatima, sina baba wala mama...’akasema

‘Lakini sasa umeshaambiwa kuwa una baba na mama yako, na mimi ndio baba yako,..’akasema

‘Siwezi kuwa na baba kama wewe...’akasema

‘Eti nini....?’ akauliza kwa hasira, na kijana akageuka kutaka kuondoka, na baba yake akawa anamjia kutaka kumshika

Dad, is this man again, I told you before...’akaanza kuongea kijana sasa akimpita baba yake akielekea kule aliposimama profesa bila kujali..., lakini hakuweza kumpita baba yake, baba yake akamdaka na kumshika mkono.

‘Wewe mtoto, ujue mimi ni baba yako, na kama hujafundishwa adabu leo mimi nitakufundisha adabu, ...’akasema sasa akimvuta tayari kumzaba kibao, na isingelikuwa profesa kuja kuwahi kuwatengenisha, kijana angelishaonja kibao kipigo.

What....unataka kunipigia nini,.... I am not your son, sikutaki...sikujui,...wewe sio mzazi wangu,  kwanini unanifuatilia maisha yangu....’kijana akasema sasa akiwa huru pembeni kwa profesa.

‘Mimi sio mzazi wako,...? ‘akauliza jamaa kwa hasira sasa akimfuata kijana kutaka kumshika, na kijana akakimbia

‘Bro, kwanini unataka kulazimisha mambo, nimeshakuambia huyu kijana bado hajaelewa, ndio ni mkubwa, miaka kumi na sita ni miezi kadhaa, lakini kwa vile hakuwahi kuishi na nyie, bado hajawaelewa, na ....ni kutokana na ile hali ya kusoma na kuambiwa kuwa yeye ni mtoto yatima....’akasema profesa

‘Sasa hilo ni kosa la nani...wewe ndiye umefanya haya yote, ...kwahiyo lawama zote zitakuendea wewe...na ole wako, ....nakuambia hii sio mara yangu ya mwisho kuja hapa, nikija safari nyingine namchukua huyo kijana, sitaki aende popote, nataka nikaishi naye kijijini, unanielewa, nikitoka hapa kurudi kijijini nitahakikisha shera zote zinafuatwa,..sitaki nije kueleweka vibaya...’akasema kaka mtu.

‘Aaaah kaka, tulishaongea hilo, kwanini utake kuharibu,....unataka kuniharibia na mimi, huyu ana wafadhili, na kila mwezi kuna pesa tunapata kwa ajili ya kumlea, kwa vile ni yatima, hana baba wala mama, ukifanya hivyo misaada yote itakatika, na huenda nikaingia matatani....’akasema.

‘Ohooo, kumbeee,ndio maana, ina maana utajiri wote huo unapata kwa kupitia mgongo wa mwanangu, unapata mipesa, na sisi wazazi wake hatujui,....sasa hilo nitahakikisha nimelikomesha...mimi naondoka, na nikirudi tena hapa nakuja na watu wa usalama, waliokuwa wakimtafuta...’akasema.

‘Kaka ukija kufanya hivyo, udugu utakufa,.....nikuambie ukweli, unajua jinsi gani nilivyohangaika a huyu mtoto, ndio shukurani yenu hiyo....nenda kashitaki, na hapo hutampata tena huyu mtoto...’akasema na kaka mtu akageuka akamuangalia kwa makini halafu akasema.

‘Kama mimi sio kaka yako tutaona, si unataka kushindana na mimi, kwa vile unajiona umesoma, kumbe kusoma kwenyewe ni kwa utapeli, wizi na ulaghai,...sasaa wewe utaishia kifungoni...sijali cha udugu...’akasema na kuondoka.

*********

‘Kwanini umefanya hivyo...?’ profesa alimuendea kijana akiwa kajiinamia pale alipokaa kitandani kwake.

I told you before dad, mimi simtaki huyo mtu...unaona alivyotaka kunipiga, kama ingelikuwa ulaya ningemshitaki....na kesho nakwenda polisi kumshitaki, ...’akasema

‘Sikiliza hapa sio sawa na ulaya, ..hapa kuna utaartibu wake, ..mtoto anatakiwa kumtii baba yake na baba ana weza kukuchapa ukikosea,...na alichotaka kukuelekeza ni kuwa wewe umuheshimu kama baba yake, ...’akasema profesa

‘Lakini yeye sio baba yangu...’akasema kijana

‘Sasa baba yako ni nani...?’ akauliza profesa

‘Baba yangu ni nani, kila kitu kipo kwenye maandishi mimi ni mtoto yatima, sina baba wala mama, ...’akasema

‘Tulishaongea hilo , kwanini hutaki kunielewa, tatiz lako umerithi ubishi wa baba yako, yeye akiamua kitu hataki kurudi nyuma,..sasa sikiliza, kwa hali inavyokwenda, mimi naweza kukamatwa kwa kosa la kukuchukua kutoka kwa wazazi wako...na sitaki hilo litokee...’akasema

‘Kukamatwa kwa kosa gani....?’akauliza

‘Hukusikia yule kaka yangua alivyosema anakwenda kuchukua polisi, na polisi wakiambiwa kila kitu kitaharibika, ...kwahiyo sasa tujiandae, hapa tunaondoka,...nataka ikiwezekana kesh tuwe safarini, tutapitia Kenya,...kule Kenya nina jamaa yangu, ...na tukitoka huko unarudi shuleni kwako...’akasema

That’s is a god news dad, ..ndio maana nakupeda Dad, wewe ndiye baba yangu, ...hao sijui baba, sijui mama, ...halafu yule mama,...mmh,sitaki kabisa kuwa naye karibu, anaumwa nini....?’ akaulizwa

‘Yule ni mama yako, chunga ulimi wako...utakuja haribikiwa,....nilishakuambia chezea baba yako, lakini usije kuchezea mama yako,....utaiona dunia ngumu....’akasema

I don’t care...unasikia dad, mimi ni yatima, simjui baba au mama....kama wewe wawataka sawa, lakini mimi msimamo wangu ndio huo..siwezi kabisa kuishi na mama kama yule,...’akasema  na profesa akatulia kwa muda, akiwaza kichwani alikuwa hataki hiyo kauli ya huyo mtoto, lakini alishindwa asema nini kwa muda huo.

*******

Siku ya pili yake, alihakikisha kijana ametangulia kuondoka, akiwa kaongozana na jamaa yake anayefahamiana naye wakiekea Kenya kama walivyopanga, yeye alibakia nyuma akihakikisha shughuli zake zipo salama, na wakati anataka kuondoka mara gari la watu wa usalama likasimama nje ya nyumba yake...

‘Niwasaidie nini....?’ akauliza akiwa keshajipanga kuongea nao, hakuonyesha wasiwasi.

‘Sisi ni watu wa usalama,....’wakaonyesha vitambulisho vyao,

‘Tumekuja hapa kwako.., kuna malalamiko kuwa wewe unaishi na mtoto ambaye sio mtoto wako....’akaambiwa

‘Ni nani kawaambia hivyo?’ akauliza akijifanya kushangaa, anajua jinsi gani ya kuigiza kihali hiyo.

‘Ni mama wa huyo mtoto...’akaambiwa

‘Mama wa huyo mtoto, ina maana ni mke wangu, mlionana naye wapi, maana mke wangu tuliachana naye muda sasa...imekuwaje amuache mume wake aje kudai tena huyu mtoto, niwaulize kitu, yeye huyo mke wangu ana uhakika gani kuwa huyo mtoto anayemdai ni mtoto wake....?’ akauliza

‘Yeye sio mke wako bwana....ila yeye ni mama wa huy mtoto, kwahiyo kama ni maam wa huyo mtoto, atakuwa na uhakika huo, kwa vile yeye ndiye aliyemzaa huyo mtoto...’wakasema

‘Ndugu zanguni, nyie ni watu wa usalama...si ndio, mimi hapa nilikuwa naishi na kijana wangu, mtoto wangu niliyezaa na mke ambaye tuliishi naye tu, hatukuwahi kufunga ndoa, ..na ikawa bahati mbaya, akaolewa, na tulikaa tukakubaliana kuwa mtoto huyo nimlee mwenyewe, huo ndio ukweli wenyewe....’akasema

‘Sasa kama ni yeye kanigauka tena, akaja kwenu kudai huyo mtoto, basi kamwambieni aje tuongee, ...’akasema

‘Tumekuambia kuwa huyo anayedai mtoto sio mke wako, ni mama mwingine tu, naye alikuwa na mume wakaachana,....’akasema

‘Ohooo, umenikumbusha kitu, siku moja, nilikutana na mama mmoja anaumwa hivi, unajua lile tatizo la kifafa, linaweza kumharibu mtu akili,.....mimi ni profesa, na ni mtaalamu sana wa matatizo hayo...sasa nilikwenda kumtibia huyo mama, nikiwa na huyo kijana wangu, huyo mama sijui kwanini, ...mara akaonyesha dalili za kusema huyo mtoto wangu ni mtoto wake...niliona ajabu kabisa, hata mtoto wangu akaogopa na kukimbia...’akasema

‘Hayo yote tumeambiwa,....lakini huyo mama anadai kuwa huyo mtoto ni wa kwake.....kwahiyo tulikuwa tunahitajia tumuone huyo mtoto...’akasema

‘Nyie ni watu wa usalama, najua mnatimiza wajibu wenu siwakatazi,..ila huyo mama anashuku tu,...hivi huyo mama ana akili nzuri, mumemchunguza vyema...hebu wekeni akili, mtu aje akute mtu ana mtoto wake, halafu aanza kudai kuwa ni mtoto wake....mbona haiji akilini...je mumefanya utafiti gai hadi mkaona kuwa hayo madai ya huyo mama yana ukweli?’ akauliza

‘Kwanini unasema hivyo?’ akaulizwa

‘Mliwahi kumuuliza huyo mtoto anayemdai alikuwa wapi...ana umri gani, maana kijana aliyenikuta naye ni kijana wangu mkubwa tu....’akasema

‘Yupo wapi huyo kijana....tunataka tumuone?’ akauliza huyo askari

‘Kijana wangu kesharudi shuleni...shule zimeshafunguliwa, kwahiyo nimempeleka mtoto wangu shuleni....’akasema

‘Kwahiyo ni mtoto wako..?’ akauliza askari sasa akiwa anakagua kwa macho hiyo nyumba na vilivyomo humo ndani

‘Ndio hivyo waheshimiwa,...nashangaa mnakuja kudai kuwa ninaishi na mtoto asiye wa mtoto wangu, nimewauliza je mliwahi kufanya uchunguzi gani, au mnakuja kuvamia nyumba za watu tu,hebu fuateni utaratibu wa kazi zenu...’akasema

‘Una ushahidi gani kuwa huyo mtoto unayeishi nawe ni mtoto wako....?’ akaulizwa

‘Hahaha....hivi nyie niwaulize na huyo mama ana ushahidi gani kuwa huyo mtoto anayedai kuwa ni mtotowake ni mtoto wake kweli, anao ushahidi wowote....?’ akauliza

‘Tusitake kusumbuana, ...sisi ni askari polisi, na huyo mama miaka kumi sita iliyopita alipotelewa na mtoto wake, kuna kumbukumbu za hayo madai,.....kwahiyo alivyomuona huyo mtoto akamtambua....’akasema

‘Miaka kumi na sita nyuma..leo hii mnakuja kudai mtoto..huyo mama hebu mkamchunguze vyema,...mimi nahisi ana matatizo ya akili...kama ni yule niliyemtibia, nahisi yale matatiz yamemletea athari akilini, lakini zile dawa nilizompa zitamsaidia sana...yupo wapi huyo mama...?’ akasema na kuuliza

‘Wewe ndio unasema hivyo, lakini sisi tunajua huyo mama ana akili sawasawa,...usitake kugeuza geuza maneno.’akasema huyo askari mwingine aliyeonyesha kuwa na uhakika lakini mwenzake alionekana ameshakurizika kuwa huyo mtoto sio wa huyo mama.

‘Sasa tusipotezeane muda, mimi nina ushahidi kuwa huyo ni mtoto wangu, nataka na nyie mnipe huo ushahid kuwa huyo ni mtoto wa huyo mama....’akasema akifungua mkoba wake na kutoa cheti cha kuzaliwa
Polisi wakaangaliana, na mmojawapo akataka kukiona hicho cheti, na profesa,akasema;

‘Aaah, ...nionyesheni na nyie ushahidi wenu, vinginevyo hili swala tutalifikisha mahakamani, kwani mnanivunjia heshima yangu..maana nyie badala ya kufanya kazi zenu kwa sahihi, mnaingilia nyumba za watu na kuleta madai yasiyosahihi,..huko ni kukiuka haki za raia,.....’akasema,

‘Tunataka tuone huo ushahidi wako,.....’akasema yule askari na profesa akaona isiwe shida, akachukua kile cheti cha kuzaliwa cha mtoto akamkabidhi huyo askari, na yule askari akakifungua na kuanza kukisoma....

*********

Siku iliyofuata waliokuja hapo nyumbani kwa profesa ni kaka mtu, akiwa  kaongozana na wale watu wa usalama, na walipofika wakitarajia kuwa watamkuta,  lakini walipofika waliambiwa profesa hayupo

‘Hayupo kaenda wapi ?’ akauliza kaka mtu kwa hasira

‘Amesafiri ...’akaambiwa,

Kasafiri kwenda wapi, na mtoto je , kwanini hajaniaga, siku zote akisafiri huwa ananiaga,...ananipigia simu kuwa anasafari ?’ akauliza akionyesha kutokuamini

‘Kwakweli sisi hatujui,..yeye jana aliondoka na ndege ya usiku, kwenda ulaya..na mtoto aliondoka mapema tu kurudi shuleni huko alipokuwa akisoma.....’akaambiwa

‘Haiwezekani..huyu bwana mdogo anataka kunipanda kichwa,..kwaninis asioe akazaa mtoto wake mwenyewe, kwanini anataka kuharibu watoto wa wenzake...’akasema kaka mtu kwa hasira

‘Ina maana huyo mdogo wako hana mke?’ akauliza mtu wa usalama

‘Hana mke yule, ...hajawahi kuoa, na ataishi na mke yule....mtu hajatulia, tulimshauri siku nyingi aoe, lakini anasema wake yupo, na ni huyo huyo...mara akasema huyo mchumba wake kaolewa, na kama kaolewa, yeye hataoa tena....ni muhuni fulani hivi....’akasema kaka mtu kwa hasira

‘Lakini katuonyesha cheti halali cha kuzaliwa cha mtoto, inaonyesha kweli yeye ni baba wa huyo mtoto kisheria...na alisema alikuwa na mwanamke aliyezaa naye huyo mtoto, japokuwa hawakuwahi kufunga naye ndoa...’akasema huyo mtu wa usalama

‘Mhh,....muongo, ndio zake hizo, anaweza akatunga uwongo, mpaka wote mkaamini,.... huyu mdogo wangu ananitafuta ubaya...bora ningekiona hicho cheti,na nikaonana na yeye mwenyewe,mbona hakuwahi kunionyesha hichoo cheti,...kitakuwa ni cheti ni cha bandia ili kufanikisha mambo yake...lakini yeye sio kweli kuwa ni baba wa huyo mtoto, ..’akasema

‘Kwanini afanye hivyo....?’ akauliza mtu wa usalama, hapo kaka mtu hakuwa tayari kuongea kila kitu, akasema;

‘Sijui, yule ndivyo maisha yale yalivyo, kujifanya mjanja mjanja, kamuharibu hata mtoto wangu,...ila ninachowaambia  yule mtoto ni mtoto wangu nilizaa na mke niliyeachana naye....na angekuwepo hapa angesema ukweli wote, lakini kwa vile kuna mambo yake anataka yafanikiwe kwanza ndio maana akawaambia hivyo....’akasema

‘Sawa lakini kisheria anaweza kuwashinda, je nyie mnacho cheti cha huyo mtoto cha kuzaliwa kinachoonyesha kuwa nyie ni wazazi wake halali, ...?’ akauliza huyo mtu wa usalama

‘Cheti ..cha nini...sawa, kwa ajili ya mtoto sio, ...unajua huyo mtoto alikuwa mikononi mwa mama yake,...sasa huko kwa mama yake, sina uhakika kama walifuatilia hicho cheti,.., labda nikifuatilie mimi mwenyewe,...hata hivyo, unajua mimi kama baba yake, sihitaji kuthibitisha hilo,...kwanini nithibitishe, wakati kweli nafahamu kuwa mimi ni baba yake halali...’akasema

‘Lakini kama mtoto keshasema yule ni baba yake, na huyo baba yake ana cheti cha kuthibitisha hilo, mtakuwa hamna haki ya kumdai kuwa ni mtoto huyo ni wa kwenu....’akasema mtu wa sheria

‘Huyu mtoto kajazwa ujinga na huyo mdogo wangu, ...yeye bado mdogo, ...siwezi kumlaumu sana, ila kama ataendelea hivyo, wakati keshaujua ukweli, akaja kunikataa, oooh,...sijui...unajua mzazi ni mzazi tu,..hata aweje ukimkataa, oh, sijui, dunia itamfunzam na mwenyewe atakuja kunitafuta, kama bado nipo hai...akisubiria nikifa atapata shida....’akasema

‘Mhh, hapo mwenzenu kawazidi ujanja...na kweli kuna anachokitafuta sio bure tu...huwezi kung’ang’ania mtoto wa mtu hivi hivi...na kwa vile anasoma huko ulaya, basi atarudi....ila ni nani anamdhamini kusomea huko, ni huyo baba yake mdogo ndiye anayemlipia gharama, au...?.’akauliza mtu wa usalama

‘Unasema kanizid ujanja, hahaha, ujanja  gani huo, damu ya mtu hata siku moja haiibiwi bwana,..sema tatizo ni kuwa anamuharibia mtoto maisha yake, ....na sijui ni nani anaye mlipia hizo gharama, ...’akasema kaka mtu akijaribu kuficha ukweli.

‘Na....vipi huyo mama yake, maana hali yake kwa sasa sio nzuri, anataka ampate mtoto wake, ...na anasema ni njama zetu watu wa familia yenu, mlimuiba mtoto ni kweli mlifaya hivyo?’ akaulizwa

‘Mimi nigefaya hivyo ningehangaika hivi....huyu bwana mdogo, sijui alimpataje.. wale wananinyoshea kidole bure, najua ni kwasababu ya yaliyopita, kuwa tumeachaa...lakini hayo yalishapita, ....’akasema

‘Ulimuacha eti kwa vile alikuwa anaumwa, ana matatizo kama hayo ya kudondoka dondoka...?’ akauliza mtu wa usalama

‘Hayo yalishapita....., na ni kati yangu mimi na yeye, hayana mahusiano na mtoto,...na mimi ninawalaumu sana wao..., kwanini hawakuwa makini na kumlea huyo mtoto, alifikaje kwa huyu bwana mdogo,...wao ndio wa kulaumiwa, sio mimi kumuacha yeye..., na kama kweli wangelikuwa makini na ulezi kwanini mtoto anawakana, mtoto hataki hata kumuona mama yake..kwanini ....’akawa kama kauliza

‘Nasikia huyo mama alidondoka na kupoteza fahamu, alipoambiwa huyo mtoto hamtambui yeye kama mama yake,...mmmh,huyo kijana hajui kiasi gani anavyomuumiza huyo mama...lakini je ni kosa lake...na kwanini ilifikia hapo, nahisi kuna tatizo....na wewe ulikuwa unawasiliana na huyo mtoto?’akauliza huyo mtu wa usalama.

‘Kuwasiliana kwa vipi...? Usiniuliza swali la ujanja ujanja, la kunitega...nimeshakuambia mimi sijui huyu bwana mdogo alimpataje huyu mtoto, nilikuja kugundua siku za hivi karibuni, ndio nikaja kuongea na nyie,...na..na nikaona kwa vile hili swala lilikuwa mikononi mwa sheria, basi ngoja niwaone nyie ...sikujali kuwa huyo ni ndugu yangu,...si mnajua mimi ni mjumbe, najua sheria, ...ndio nikawaambia....’akasema

‘Basi hilo tuachieni, tutapambana na huyu mtu,  huyu ni tapeli tutana mwisho wake ni wapi,...na mtoto mwenyewe atafikia umri wa kujua baya na zuri, sasa hivi hatuwezi kumlaumu sana huyo mtoto na nyie kama wazazi mnatakiwa kutumia hekima, mbaya ni huyo mdogo wako,...’akasema mtu wa usalama.

‘Sawa hata huyo mtoto akifikia umri wa kujua ukweli na bado akaendelea kuleta hiyo tabia, akaendelea kuwakana wazazi wake,...ataiona dunia chungu..mimi si nipo hapa, mtakuja kuniambia, ..’akasema

‘Usiseme hivyo mzazi.....’akasema mtu wa usalama

‘Aaaah, mimi sina tatizo, maana nina watoto wengine, tatizo ni kwa huyo mama yake...si mumeona hali aliyo nayo...’akasema na kutikisha kichwa akionyesha huzuni.

‘Ila sisi sasa tutapambana na na huyo anayejifanya ni profesa wa ulaghai, wenzake wanaumiza vichwa madarasani kuupata huo uprofesa, yeye wa kwake anaupatia mitaani kwa kulaghai watu, watu kama hao wapo mpaka maofisini, wenzao wameumiza vichwa kusomea fani fulani, wao wanatumia ujanja kujifanya wanajua...’akasema jamaa mwingine aliyekuwepo

‘Hata maofisini pia,..mmh, mimi huko sijui maana sijawahi kuajiriwa,...lakini ni ujinga tu..kwanini wasitafute chao, kama ni kusoma , wakasomee hiyo fani, ni ujinga na sio ujanja..hata kama atapata utajiri, lakini utajiri huo utakuwa unanuka dhuluma....’akasema

‘Ok tutaona nani zaidi, uprofesa wake wa ulaghai au sheria...tutampata tu...’akasema mtu wa usalama, huku akiandika kumbukumbu kwenye makabrasha yao..

Profesa akawa keshaondoka nchini, na hakuonekana mpaka miaka kumi na kitu mingine,...na alirejea akiwa mikononi mwa polisi, akiwa na hali mbaya kweli, kakonda, yupo kama mgonjwa, na isitoshe zaidi alikuwa anadaiwa, na alipofika tu nyumba yake ikapigwa mnada kulipia madeni,...

‘Kwanini...?’ tukauliza tulipoona msimuliaji akitulia,..


WAZO LA LEO: Binadamu huwa tunakosea, na wengi tunafahamu kuwa tumekosea, tumemkosea huyu na yule kwasababu hii na ile, ubora wa imani thabiti, ni kutubu, na kukirini moyoni kuwa nimekosa, na muhimu kumuendea yule uliyemkosea na kumuomba msamaha, au kumrejeshea kile ulichomdhulumu, hapo utafanikiwa kuwa na imani thabiti, katika maisha yako ya hapa duniani na kesho ahera. Tutubu toba ya kweli, kwani mwezi mtukufu, mwezi wa toba, na kusamehewa umeshafika,  RAMADHANI KAREEM.


Ni mimi: emu-three

No comments :