Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, June 12, 2015

RADHI YA WAZAZI-2



‘Mimi niliwahi kusoma, enzi hizo,...usinione hivi,  nikafika hadi nje, watu wakiniona natangaza madawa ya kienyeji basi wanafikiria mimi ni mwenzao,.. na hilo ndilo lililonifanya niwe karibu sana na huyu kijana, namuita kijana msomi mwenye mazarau,alifikia hata kunizarau hata mimi, nikamwambia wee, wee ...kumbuka ulipotoka...lakini bwana sikio la kufa halisikii dawa...’akasema

‘Kwahiyo wewe ni mtoto wake kivipi?’ akaulizwa

‘Huyu ...chizi, eeeh ni mtoto wangu, baba yake na baba yangu wamezaliwa tumbo moja, ...unasikia japokuwa kulitokea namna yao, wakaachana, lakini ni damu yetu .....’akaanza kutuelezea.

‘Huyu ni mtoto pekee kwa mama yake, mama yake alichika mapema tu, na kipindi hicho alikuwa na ujazito wa huyu kijana,...unasikia sana...sasa hebu tulieni, nahisi mnata kujua hasa ilianzaanzaje ili msije mkapoteza muda wenu bure.....’akatulia, halafu ndio akaanza kuhadithia kisa hicho kwa marefu akiturudisha miaka 32 iliyopita...

*****
‘Huyu si mama Totoo...?’ mama mmoja akiwa na mwenzake akasema na mwezake akasema

‘Ndio yeye, jamani kadondekea mtoni, hebu njoo tumsaidie kumtoa ...’akasema huyo mama akitangulia bondoni kwenye eneo wanapochotea maji,...na mwenzake kwanza alisita, akiogopa kuwa huenda huyo mama ni maiti, lakini alipoona mwenzake akielekea hapo alipolala huyo mama bila kuogopa na yeye akamfuata nyuma, na wote wawili walipofika hapo mtoni, wakaaza kazi  ya kumtoa huyo mama hapo mtoni na bahati nzuri sehemu ya kichwa ilikuwa nje ya maji japo ilikuwa ni kwenye matope.

‘Mhh, bado anahema,....jamani huu ugojwa sio wa kumuachia mwenyewe, kwanini wanafanya hivi hawa watu...bahati hakuyanywa maji, maana angekuwa maiti....’ akasema huyo mama

‘Lakini ni bahati mbaya tu, kwani walijua itamtokea....., maana hiyo hali haitokei  mara kwa mara, wakati wote, mbona anaweza hata kukaa miezi bila kusikia tukio kama hili....’akasema mama mwenzake.

‘Mhh, lakini ni hatari, halafu hebu angalia, mbona  yaonekana kama alikuwa kabeba kitu nyuma huoni hii hicho kitenge aliyojifunga nyuma, hakuwa amebeba kitu kama mtoto....’akasema mwenzake

‘Mtoto ! Haiwezekani, kama angelikuwa kabeba mtoto tungelimuona, ...na hiki kisima nilisikia wakisema kina chatu na mamba, mungu wangu, kama alibeba mtoto mmmh,..... hebu tutoe taarifa nyumbani kwao haraka...’wakasema na mmoja akabakia na mgonjwa, huku mwingine akipanda juu huku akipiga yowe la kuomba msaada.

Kwanza akafika mzee mmoja, na kabla hajamchunguza huyo mama, ambaye wakati huo alikuwa akibabaika, hajajijua vyema na mara ndugu wa huyo mama wakafika, na wakati huo huyo mama akawa sasa keshazindukana, na akawa anaulizia,;

‘Mtoto wangu yupo wapi...mtoto wangu yupo wapi jamani....?’ akawa anauliza akijishika huku na kule

‘Ulikuja mtoni na mtoto...?’ akauliza yule mama aliyemsaidia

‘Jamani mtoto wangu yupo wapi...nani kamchukua mtoto wangu?’ akauliza na ndugu sasa wakawa wanaangalia huku na kule kama kuna dalili yoyote ya mtoto.

‘Tulikuambia ukija mtoni usije na mtoto, sasa unaona.....mtoto yupo wapi...?’alikuwa mama yake

‘Huu sio muda wa kulaumiana, cha muhimu ni kutafuta mtoto yupo wapi....’akasema baba mtu, na watu wakaitwa na kuanza msako, lakini hakukuwa na dalili ya mtoto.

‘Tatizo mto huu una mamba na kenge na chatu..., lakini hapa hakuna dalili ya kuonyesha mtoto kachukuliwa na hao wadudu wabaya..., tungeliona damu au alama yoyote...’akasema mzee mmoja anayefahamu sana tabia za hao wanyama

‘Sasa mtoto atauwa kaenda wapi...au alipoona mama yake kapoteza fahamu alianza kutembea ovyo...?’ ndugu wakaulizana bila jibu. Baadaye, taarifa zikafika kwa vyombo vya usalama, lakini hakukuonekana cha mtoto wala dalili ya mtoto.

Mama wa mtoto akawa analia, hakubali kuondoka eneo hilo la tukio, akasema hawezi kuondoka hapo mpaka mtoto wake apatikane, na baadaye watu wa usalama wakafika na kuanza kumhoji huyo mama;

Kwani ulipojisikia vibaya mtoto alikuwa wapi...?’ akauliza

‘Nilimbeba mgongoni na kitenge, sikutaka kumuachia ...’akasema mama yake

‘Ehe, hebu tueleze ikawaje, ...’akaambiwa

‘Mimi nilifika kuchota maji, mara nikasikia kitu kama mchakato, nikawa naogopa, nikajua ni wanyama wabaya...nikatulia hadi mchakato huo ukaisha nikachota maji, mara nikaanza kuhisi vibaya, nikaanza kuvutwa kama inavyotokea, na sikukumbuka kitu hadi nilipozindukana na kumuona huyu mama akiwa pembeni yangu...’akasema

‘Ulianzaje kujisikia vibaya...?’ akaulizwa

‘Mhh, ni .....nahisi kama harufu, ...sia uhakika, nilichokumbuka ni kuwa nilianza kutikisika, na mwili ukawa unavutwa.....pumzi ikaniishia na....’akatulia, na yule mtu wa usalama akamgeukia huyo mama aliyeambiwa alikuwepo wakati huyo mgonjwa alipozidukana.

‘Mhh na wewe mama ulimkutaje huyu mama....?’ akaulizwa huyo mama na yeye akaelezea ilivyotokea na huyo mama aliyekuwa naye akatoa ushahidi kuwa walikuwa wanapita ndio wakamuona huyo mama akiwa kalala kwenye tope nusu ya mwili ukiwa majini, lakini kichwa kilikuwa nje ya maji, wakasaidiana na kumtoa nje

‘Je wakati mnamtoa mliona nini mwilini kwake...?’ akauliza mtu wa usalama

‘Tuliona hicho kitenge kikionekana kuwa alikuwa kabeba kitu mgongoni, ndio tukahisi alikuwa kabeba kitu, lakini sisi hatukuwa na mawazo ya mtoto, maana tujuavyo familia yake isingelikubalii huyu mama aje huku kisimani na mtoto wakijua kuwa ana matatizo..’akasema huyo mama.

‘Ana matatizo!, matatizo gani?’ akaulizwa na huyo mama akawageukia wazazi wa huyo mama mgonjwa, ili wao wajielezee, lakini kabla hawajasema kitu huyo mama mgonjwa akaaza kulia tena akisema;

‘Mtoto wangu jamani....nirudishieni mtoto wangu...’akasema huyo mama

‘Unahisi ni nani anaweza kumchukua mtoto wako?’ akaulizwa huyo mama

‘Mimi sijui jamani,...na kwanini wamchukue mtoto wangu,nimewakosea nini...hivi hawanionei huruma, pamoja na mitihani huu wa ugonjwa, nimeachika kwasababu ya huu ugonjwa, mungu kanijalia mtoto bado tu binadamu hawanitaki, basi na mimi waniue...’akawa analalamika.

‘Hebu tuambieni mume wa huyu mama yupo wapi?’ mtu wa usalama akamgeukia mzazi wa huyo mama na kumuuliza maswali

‘Aliachika...’akasema baba mtu

‘Kwanini aliachika, waligombana au kulikuwa na tatizo gani...?’ akaulizwa

‘Ni kutokana na matatizo aliyokuwa nayo mwanangu,...’akasema mama wa binti

‘Matatizo gani?’ akaulizwa

‘Ana tatizo la kudondoka, dondoka, na kupoteza fahamu...’akasema mama akioyesha kusita

‘Ana tatizo la kifafa...’akaongezea baba wa mtoto alipoona mkewe anasita kufafanua

‘Ina maana wakati aanolewa haikujulikana kuwa ana tatizo hilo?’ akauliza mtu mwingine

‘Mwanangu hakuwa na tatizo hilo kabisa, tatizo hilo limetokea huko huko kwa mwanaume, wamampachika mtoto wangu gonjwa, halafu wakampa talaka, ...’akasema mama wa binti

‘Kwahiyo aliachika akiwa na mimba...?’ akaulizwa

‘Wakati wanamuacha hawakujua kuwa ana mimba, mimba hii tumeigundua wakati tupo naye, ...’akasema mama

‘Je baba yake anafahamu kuwa mtaliki wake ana mtoto...?’ akauliza

‘Ndio waafahamu, ,...kumekuwa na mvutano sana kuhusu huyo mtoto, kwanza huyo baba yake alikataa kuwa sio mimba yake tulipomweleza mwanzoi..., lakini mtoto alipozaliwa akaonekana ni dume, na anafanana na huyo mwanaume, basi wakabadilika, na kuanza kuja kudai mtoto...’akasema baba wa binti

‘Mkaelewana au ilikuwaje?’ wakaulizwa

‘Kuna cha kuelewana hapo, hebu fikiria mwenyewe, walimuacha, kwa dharau kuwa eti mtoto wetu aa huo ugonjwa, ataharibu familia yao, tukasema sawa, kama hawamtaki basi binti yetu ana kwao, hatua shida, baadaye tukagundua kuwa binti ana mimba, na binti akasema ni mimba ya huyo mwanaume aliyemuacha,..ikabidi twende huko kutoa taarifa, wakakana kuwa mimba hiyo sio ya mtoto wao, na mtoto wao akakana mbele yetu...’akatulia

‘Sasa kazaliwa dume...na sura sawa kabisa na baba mtu...wakaanza kueleta vurugu, nikawaambia wasisogee kabisa kwenye eneo langu, la sivyo tutatafutana ubaya, ....wakaenda kushitaki, lakini sheria ikawabana, kwani kauli ya kukataa mimba ilitolewa mbele ya wazee wenye hekima zao...’akatulia

‘Kwahiyo wakakubali kushindwa..?’ wakaulizwa

‘Sasa wangefanyaje...?’ naye akawa kama anauliza

‘Je kwa hali hiyo mnaweza kuhisi kuwa huenda wao ndio wamemchukua huyo mtoto?’ wakaulizwa

‘Hilo hatuna uhakika nalo, kwasababu hao watu wanaishi kijiji cha mbali, na kama wangelionekana huku tungelipata taarifa....’akasema mzee mmoja.

‘Wanaweza kutuma mtu kuja kuifanya hiyo kazi...’akasema mzee mwingine

‘Haiwezekani, maana mimi nalima hapo jirani, sikuwahi kuona mtu yoyote akipita eneo hili, na unaona pale shambani kwangu kulivyo ni juu, mtu akija eneo hili namuona kabisa...’akasema mzee mmoja

‘Je huyu mama wakati anapita kuja kisimani wewe ulimuona?’ akaulizwa huyo mzee, na huyo mzee bila kusita akasema;

‘Ndio nilimuona kwani alisimama tukasalimiana, ...’akasema huyo mzee

‘Na alikuwa na mtoto mgongoni...?’ akaulizwa

‘Ndio alikuwa na mtoto mgongoni...’akasema huyo mzee

‘Na kama ulivyosema mtu akija au kutoka kisimani, unamuona ina maana huyo mtoto kama alimtoroka mama yake akiwa kazimia, ungelimuona, au sio...?’ akaulizwa

‘Ndio ningelimuona...huyo mtoto hajatoka humu, ....sizani, angelipita wapi...’akasema huyo mzee

‘Je wakati hawa akina mama wanapiga ukelele wa msaada uliwasikia?’ akaulizwa

‘Ndio niliwasikia, na nilikuwa wa kwanza kuja eneo hili la tukio, ndio nikamkuta huyu mama akiwa na huyo mama mwenye mtoto, na wakati huo alikuwa hajajitambua vyema, na baadaye ndugu zake wakafika....’akasema huyo mzee

‘Sasa kiutaratbu wa kuisaidia polisi, nyie mama wawili na wewe mzee uliyemuona huyo mama tutaongozana hadi kituo cha polisi mkaandikishe maelezo yenu, na tutawahoji kidogo, ili kupata ukweli,...’akasema huyo mtu wa usalama

‘Lakini sisi tulikuwa tunapita tu...’wakalalamika hao akina mama wawili

‘Na mimi nilikuwa nalima tu....’akasema huyo mzee

‘Ni utaratibu, tunataka kupata uhakika, na sio hawa tu, tutawahoji watu wote tutakaowahisi, maana hatuna uhakika bado...kama huyo mtoto apotea kivipi, na tumewaita watu wa wanyama pori wajaribu kutafiti eneo lote ili tuwe na uhakika zaidi...’akasema huyo mtu wa usalama

‘Kwahiyo mnaweza kutawanyika, na sisi tutaendelea kufanya uchunguzi...’wakasema watu wa usalama

‘Mimi siondoki, mpaka nimpate mtoto wangu...’mama wa mtoto akagoma kuondoka

***********

‘Hivyo ndivyo ilivyotokea awali....’akasema huyo mzee na kutulia, na tulipoona haendelei, tukaanza kumuuliza maswali

‘Ina maana huyo mama alikuwa na ugojwa wa kifafa...?’ nikauliza

‘Ndio huyo mama yake alikuwa na tatizo la kifafa...unajua tatizo hili enzi za mababu zetu ukionekana nalo, kama ni mwanamke aghalabu kuolewa, basi mama yake alipogundulikana ana tatizo hilo, baba yake akaamua kumuacha...’akasema

‘Kwanini walikuwa wakifanya hivyo....?’ akauliza mwenzangu

‘Sijui, ila mimi kama mganga wa kienyeji, nina tiba za kusaidia, ila ukichunguza sana, kwa vile ilishafikia hali wanaona ugonjwa huo hauna tiba hasa ikiwa tatizo hilo limetokana na kurithiwa, ina maana ukiwa nao unaweza kuzaa watoto wenye matatizo hayo,....’akatulia

‘Hivi ndivyo ilivyo, ina maana kifafa hakina dawa...?’ mwenzangu mmoja akauliza

‘Dawa ni za kutuliza tu, mababu zetu wao waliona Ili kukwepa kuuendeleza hilo tatizo, wakaamua kuwa kama mke ana hilo tatizo haolewi na akiolewa na akagundulikana anao anaachika...’akasema huyo mzee

‘Na kama mwanaume ndiye mwenye tatizo hilo, ina maana haoii...?’ nikauliza

‘Wazazi wa mke wakigundua hilo, hawatamruhusu binti yao kuolewa huko....japokuwa kwa kujitetea wanasema ugonjwa huo ukitokea kwa mama ndio unaendelea lakini kama ni kwa baba, unakuwa hauna nguvu sana ya kuendelea...hilo ni kwa wazee wetu...’akasema

‘Mhh, huo sio ubinadamu...’akasema mwenzangu.

‘Ndio hivyo hayo ni ya kizamani na wao walikuwa na mfumo wao, na kwa vile utaalamu ulikuwa haujakwenda mbali zaidi, basi ilibidi wafanye hivyo, huwezi kuwalaumu,....’akasema huyo mzee

‘Lakini kwa umri wa huyu mwenzetu sio zamani kihivyo, eti....madawa yapo, tiba zipo, ...na unyanyasaji tu..’akalalamika mwenzangu

‘Hivi unajua kuna sehemu bado watu wanafuata mila za zamani kabisa, kwa karne hii...wengine hata dawa za hospitalini hawaziamini...nchi hii kubwa,...’akasema mwigine na yule mzee, akakohoa kama atalazimisha tunyamaze akaendelea kusema;

‘Sasa mama yake huyu alikuwa na tatizo hilo, na aliweza kudondoka popote na hata akiwa 
jikoni anaweza kudondoka hata kuungua...kwahiyo ni ugonjwa fulani unaotesa, na unamuadhiri sana muathirika, mtu una...hamjana mtu mwenye tatizo hilo anavyokuwa, ....ni hatari kidogo...’akasema huyo mzee

‘Kwahiyo watu wenye tatizo hilo hawana haki ya kuoana..si ndivyo hivyo?’ akauliza mwenzagu

‘Mimi sijasema hivyo, maana mimi nina tiba zake, ....unasikia sana...ila wao, walifikia maamuzi hayo,....mimi muda huo nilikuwa sipo ningelikuwepo ningewashauri vinginevyo....’akasema

‘Baba yake huyo kuona hivyo akaamua kumuacha kutokana na ushauri wa familia yao, wakiogopa kuwa akizaa mtoto atakuwa na huo ugonjwa, na kizazi hicho kitaendeleza huo ugonjwa ...na hawakutaka kizazi au familia hiyo iwe na tatizo kama hilo...’akasema huyo mzee

‘Kwahiyo huyo mama na mume wake hawakukaa wakajadili na kufikia makubaliano , maana nijuavyo mimi, wawili hao walioana wakiwa wanapendana, hawakulazimishiwa kuoana..au sio?.’akauliza mwenzangu.

‘Unajua, pamoja na mapenzi waliyokuwa nayo, lakini ilifika waati mume akashauriwa na wanandugu, si unafahamu wanadugu walivyo, ikabidi akubali, na kusimamia upande wa ndugu, hakumjali tena mkewe, na hakutaka hata kukaa na mkewe kushauriana lolote..,japokuwa walipendana, hata kuoana kwao, kulikuwa ni kwa ubishi, ...hayo nikipata muda nitawasimulia...ila mjue tu kuwa walioana bila kufuata ushauri wa wazazi wao, na ilipotokea hili, wakamwambia unaonaeeh, usemi wenu hua....basi kukawa hakuna jinsi.’akasema

‘Mzee hebu tueleze maisha hayo ya wanandoa hao ili tujue chimbuko la huyu , huyu eeh, jina lake nani, nimesikia wakimuita Kejeli miondoko,...na hivi kweli mzee ugonjwa, ndio usababishe watu kuachana , waliopendana wakatiliana kiapo cha shida na raha,  mimi naona kama ni uonevu fulani...?’ akauliza mwenzangu na huyo mzee akakaa kimia, na haikuonyesha dalili kuwa anaendelea na simulizi hilo, na mimi nikamuuliza...

‘Sasa baaadaye ikawaje...?’ nikamuuliza huyo mzee, na huyo mzee akaoyesha ishara kuwa koo limekauka...

NB, Tukutane sehemu ijayo...


WAZO LA LEO: Mnapofikia hatua mbaya ya mfarakano,kati ya wanandoa, ni muhimu mkakaa na kutafuta njia sahihi za kusuluhisha hilo tatizo lenu, na kama itafikia hatua mbaya ya kuachana, ni vyema mkajadiliana msitakabali wa watoto, ...mjue matatizo yenu yatawaathiri sana watoto, kwahiyo kunahitajika hekima ya hali ya juu kuhakikisha kuwa watoto hawaumii au kuteseka.

Ni mimi: emu-three

No comments :