Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, May 28, 2015

NANI KAMA MAMA-83



Siku ya pili mama alifika akamalizana na mfadhili wangu na hatukuruhusiwa kuondoka moja kwa moja, mfadhili alikuwa na hamu ya kusikia mengi kutoka kwa mama wapi alitokea, na mama akasema;

‘Mengi ya maisha yangu ni ya kawaida japokuwa yamejaa mitihani mingi, na maisha yangu mengine nisingelipenda kuyaongea kwa kila mtu, ila kwa vile mtoto wangu kaniuliza swali akitaka kujua pale nilipoishia wakati nilipomhadithia kuhusu maisha yangu…nitaongea kidogo kabla hatujaondoka…’akasema mama na kutulia akijinyosha kwenye kiti.

‘Kiukweli historia za maisha yangu,  zilizopita zinaweza kufufua vidonda vilivyoanza kupona, lakini wakati mwingine ni ibra , ni  taswira ya kukuonyesha wapi ulipotoka, na wapi unapokwenda…kiukweli maisha yangu ya nyuma yamejaa sana simanzi , na ukiyawaza sana mwishowe unakaribisha hasira za visasi, mwanangu unaonaje tukiyasahau yaliyopita tukaganga yajayo…?’Mama akasema

‘Ni kweli mama, lakini mimi natamani niyasikie, kwani ulishanianzishia maelezo na ukafika sehemu ambayo ulishindwa kuendelea pale ulipo-poteza fahamu, naomba mama uendelee tu kuanzia pale kama hutojali..’

nikamsisitizia mama. Na mama akaniangalia tena , halafu akaanza kunihadithia pale tulipoishia.

 Tuendelee na kisa chetu…

***********

‘Mwanangu, siku ile nesi na dada yake walijikuta wakifurahia ujauzito  ambao kwao ulikuwa kama mgumba kupata mtoto, kiasi kwamba walijikuta wanasahau kile  kilichokuwa kimewaleta pale, na docta bosi wa nesi alipoangalia saa, akashituka na kusema;

‘Mhh, muda umekwenda, mimi natakiwa kurudi mjini….’akasema

‘Docta, kwanini usilale ukaondoka kesho….’akaambiwa na mama mwenye nyumba

‘Hapana, ni lazima niondoke, ila nesi anaweza kubakia na mtoto, na anaweza kukaa hapa akarudi kazini jumatatu, kwa vile leo ni Ijumaa..’akasema docta.

‘Mhh, nashukuru sana docta, maana furaha niliyo nayo sitaki kuondoka hapa haraka..’akasema nesi

‘Lakini sasa wasiwasi wangu ni huyo mama, anaweza kufika hapa naomba akifika hapa msimkabidhi huyo mtoto kwanza, tunahitajia mambo yaende kisheria, mtoto atakabidhiwa kwake, baada ya kuhakiki mambo yote muhimu, na hilo litafanyika kule kule hospitalini..’akasema docta.
‘Mhh, jamani ina maana bado kang’ang’ania kwanini sije tukaongea, mtoto tukaishi naye hadi hapo atakapokuwa mkubwa, na mimi mbona sijamini kuwa mtoto huyu ni wake..’akasema mama mwenye nyumba.
‘Ni wa kwake bwana…’akasema baba mwenye nyumba kwa sauti kali.

‘Una uhakika gani…?’ akauliza mkewe

‘Nimeshakuambia hivyo na unielewe hivyo, huyu mtoto arudishwe kwa wazazi wake, ..’akasema baba mwenye nyuma kwa ukali.

‘Haya jamani mimi naondoka ila kama nilivyowaambia, muhakikishe huyo mtoto anakuwa salama na anarudi kule kwa ajili ya taratibu za kisheria, mengine tutaongea huko na huyo mama, kama atakubali, basi tutaona jinsi gani ya kufanya..’akasema docta

‘Mtajua wenyewe la kufanya, ila mimi kama nilivyowaambia sitaki kujiingiza na maswala ya hao watu, kwangu hapa wapaone kituo cha polisi, …’akasema baba mwenye nyumba na nesi akabakia akimuangalia kwa mshangao, docta kwa vile walishaongea na mtu huyo hakuonyesha kusangaa sana.

Basi docta na mlinzi wake wakaondoka kurudi mjini, wakitarajia kuwa watakutana na huyo mama huyo hospitalini, na walipanga wakikikutana naye watamshauri afanye subira ili taratibu za kisheria zifanyike ikiwemo vipimo vingine, na hata watu wa sheria wawepo ili kulimaliza hilo tatizo kabisa.

Huku nyuma nesi akabakia na ndugu zake wakifurahi na mtoto naye akifurahia kuwaona wazazi wake wa kufikia yeye alijua hao ndio wazazi wake.

***********

Docta wakafika mjini hospitalini, na walipofika hospitali wakakuta taarifa kuwa yule mama alirudi hapo hospitalini, na alipofika hakuonyesha ule ukali aliokuwa nao mwanzoni, alikuwa mpole na mstaarabu sana, akauliza mtoto wake yupo wapi, jibu alilopewa ndilo lilimbadili hiyo hali na kuanza kucharuka tena

‘Na nesi na mwenzake wapo wapi?’ akauliza kwa hasira

‘Wamekwenda huko kijijini kwao…’akaambiwa

‘Na mtoto wangu sio…wanataak kumrudisha huko, sikubali…’akasema na hakuna aliyetaka kuongea naye sana, yeye akageuka kutaka kuondoka, na docta aliyekutana naye akamwambia

‘Mama unajua hujaruhusiwa kuondoka, hujapona, …..’akaambiwa

‘Hivi mnafikiri kama ingelikuwa ni nyie, mngefurahia hili mnalonifanyia mimi, au kwa vile ni mimi, au kwa vile mnaniona nimechanganyikiwa, …’akasema

‘Sio hivyo mama..’akasema docta

‘Hivi kweli mnapenda mama atengane na mtoto wake hivihivi, kirahisi tu…sikubali, nitampata mtoto wangu mpende msipende…subirini…mtaona kitakachotokea, sitaki ubaya na mtu, na sitaki mtu aumie tena,….’ Akasema na kuanza kuondoka, na docta hakutaak kusumbuka na huyo mama tena, na jinsi alivyoondoka, wengi walijua anaelekea tena huko kijijini.

‘Kwahiyo mkamuacha akaondoka..?’ akauliza docta huyu aliyetokea kijijini

‘Ndio tungefanyaje…unajua huyo mama keshapona, keshajijua, na hali aliyo nayo, sio ya kumlazimisha, ni bora tumuache tuone anachotaka kukifanya ni nini..’akasema docta mwenzake.

‘Ok, sawa kwa vile nilishaongea na nesi na ndugu zake, sizani kama akifika huko kijijini ataleta fujo, muhimu n kuwaatarifu tu wajiandae kwa ujio huo…’akasema docta

 Siku ya Jumamosi kukawa na mawasiliano kati ya docta bosi na nesi, akitaka kujua kama huyo mama kawasili huko kijijini, na nini kinaendelea huko ! Cha kushangaza taarifa zilizofika ni kuwa yule mama hajaonekana huko kijijini, na wao walijua labda huyo mama amekubali kusubiri huko hospitali …!

Taarifa hiyo ikawaacha mdomo wazi madocta na watendaji wa hiyo hospitalini, na  kuwaacha kwenye mashaka wakijiuliza huyo mama atakuwa kaenda wapi maana bado alikuwa ni mgonjwa wao!

‘Au kagundua kuwa sio yeye na mtoto sio wa kwake, na kaamua kuishia!..mimi bado nina mashaka sana na huyo mama , mimi simuamini bado…?’ akasema nesi

‘Lakini dalili na vielelezo vyote kama alivyotupa docta kijana vinaendana na yeye, sasa sidhani kama kuna mama mwingine zaidi yake labda…kama yupo mama mwingine mwenye sura kama hiyo…labda, …mimi naona tungoje, kama ndio yeye lazima atarudi tu, kama sio yeye basi tutakuwa na kazi ya ziada, maana tumemuachia mgonjwa kuondoka bila ruhusa na pili ni kumtafuta huyo mama halali wa mtoto, vinginevyo, inabidi uwaombe ndugu zako waendelee kumkubali huyo mtoto kama mtoto wao..’ akasema docta bosi wa nesi.

‘Hilo la ndugu zangu kumchukua huyu mtoto kama wao, sidhani kama litawezekana kwasababu shemeji yangu anasema akimwangali huyo mtoto anamkumbuka mbaya wake, kwsababau wanafanana sana..si unaona hiyo nimejaribu kuongea naye kwa marafu na mapana, kiukweli shemeji yangu hataki kusikia lolote kuhusu huyo mwanamke na familia yake’ akasema nesi.

‘Sasa kwa vile shemeji yako anamjua baba wa huyo mtoto na kijiji kwao, kwanini asifanye mipango ili baba halali wa mtoto akapatikana..tuje hapo na watu wa uslama mgu kwa mguu hadi kwa huyo baba halali?’akauliza docta.

‘Docta hawa watu wawili hawawezi kuelewana abadani, na kama kuna kitu ambacho shemeji yangu hakitaki, ni kukutana na huyo mwanaume,….anasema huenda wakikutana kutazuka fujo ambayo haijawahi kutokea,…tumeongea naye na amaesema ili kuwe na amani, basi tusiongee maswala ya hao watu…kiufupi hilo la huyu mtoto kubakia hapa halitawezekana aliniambia alishakuelezea msimao wake…’ akaseme nesi.

‘Aliniambia lakini mimi naona ni jaziba tu, kama tutamkalisha chini na busara zikatumika, yeye anaweza kuwa msaada mkubwa kwetu, hasa kuipata familia ya huyo mama, mume wake….’akasema docta

‘Je huyo mama ameshamkumbuka mume wake?’ akauliza nesi

‘Hajataka kutuambia, …na nahisi hataki kuliongelea hilo, japo anadai hakumbuki…’akasema docta

‘Anadai mna uhakika kuwa sasa amaeshakumbuka kila kitu..?’ akauliza nesi

‘Kwa hali aliyofikia tunahisi hivyo, ila hatuwezi kumlazimisha, sisi tulitaka kwanza tulimalize hili la mtoto, yeye akutane na mtoto wake tuone athari zake, …..ni lazima kutakuwa na mabadiliko makubwa watu wawili hawa wakikutana mama na mtoto wake..’akasema docta

‘Basi mimi nitajaribu kuongea tena na shemeji na dada tuone watasaidiaje kabla sijarudi huko, lakini nijuavyo msimamo wa shemeji hauwezi kubadilika…’akasema nesi
‘Ongea nao kwanza tuone, na jingine ni jinsi ya kumtoa mtoto hapo nyumbani yeye anafahamu kuwa hao ndio wazazi wake, ni muhimu umueleze shemeji yake atumie hekima, asija akaonyesha chuki za wazi kwa huyo mtoto,…natumai ataelewa..’akasema docta

‘Haya baadaye…kama huyo mama ataonekana nitakupigia…’akasema nesi na kukata simu

**************

Mazungumzo ya docta na nesi kwenye simu yaliishia bila kupata ufumbuzi wa maana, iliyobakia ni kusubiri tu nini kitatokea , kama huyo mama atatokea tena au kuna mama mwingine atakuja kujitambulisha yote kwao itakuwa heri, lakini lazima utaratibu ufuatwe ili, isije ikaleta mgongano baadaye…!

Siku ya Jumamosi ikapita, na siku ya Jumapili ikaingia.

Ilikuwa siku ambayo wanafamilia walipanga kukutana  na siku hiyo waliipangia kuwa iwe siku muhimu sana kwao, waliamua kufanya tafrija ndogo ambayo walikuwa wameipanga awali wakawa wanaiahirisha kwasababu hizi na zile, na hata kuna muda waliona labda tafrija hiyo ifanyike baada ya kujifungua, lakini wakaona siku hiyo ya Jumapili inafaa kwao kwa vile wanafamilia wamekamilika, basi wakaitayarisha kwa harakaharaka.

Pamoja na hayo, waliona ni muhimu kama wanafamilia kukutana na kubadilishana mawazo, wakaitana wanafamilia wote waliopo karibu, na bahati nzuri , wanafamilia wengi walikuja , na ikaandaliwa tafrija fupi ya kumshukuru mungu kwa mama aliyekuwa hakutarajiwa kupata mtoto , sasa ni mja mzito, na mambo mengine ya kifamilia yakafanyiak kutoka na taratibu na mila zao, na nesi akawa anawaza kichwani, hapo ni mimba tu, jei siku akizaliwa huyo mtoto sijui itakuwaje…

Pilika pilika zikaanza,  majirani wengine wakajumuika na muongeaji mkuu akaelezea ni nini hasa dhumuni la ile tafrija fupi, hakuelezea kwa undani zaidi , alisema ni tafrijaya kumshukuru mungu kwa kumwezesha mwanafamilia kupata kile alichokiomba kwa muda mrefu, na pia ni tafrija ya kuwakumbuka waliotangulia, na zaidi ya hayo ni kukutana kama wanafamilia kujadili mambo yao…

‘Lakini mbona hawajatuweka wazi , kuwa walichokitaka wamekipata ni kitu gani au ni uja uzito wa huyo mama, lakini mbona huyo mama ana mtoto tayari kwanini waseme walikuwa wakitafuta na wamepata, …’watu wakaanza kunong’ona

‘Labda aliataka mtoto wa pili…’mwingine akasema

‘Lakini kuna kitu mimi nilisikia…’akasema mwingine

‘Mumesikia nini…?’ wakaulizana

‘Kuwa huyo mtoto sio wao, na mama yake huenda ni yule mama aliyekuja kudai mtoto …’wakasema

‘Una maana yule mama aliyechanganyikiwa,….’wakasema

‘Ndio yeye….yawezekana kweli..’wakazidi kuongea

‘Lakini yule mama alikuwa akidai kwa wengi kuwa mtoto huyu mara yule ni wake…’wakasema

‘Sijui kwanini tusiwaulize wenyewe….’wakasema lakini hakuna aliyekuwa na sababu za kwenda kuuliza, wakawa wanaendelea na shereeh na kile aliyeulizwa hakuwa na jibu zaidi ya wahusika wenyewe ambao ni mume na mke na nesi.

Wakati watu wamejimwaga na vyakula vinaliwa, hakuna aliyekuwa na wazo lolote zaidi ya ile sherehe, dada wa nesi na nesi walikuwa wamevalia sare, na mume mtu alikuwa kavalia suri yake safi wakawa wamekaa pale mbele kama wahusika wakuu, picha za kumbukumbu zikapigwa.

‘Mwiteni mtoto wetu  naye apate picha ya kumbukumbu…’ akasema dada wa nesi, akiwa na dada yake na hata nesi akasema hivyo. Hoja hii aliipingwa na shemeji mtu, na shemeji mtu alipoona wenzake wanasisistiza, akaona isiwe taabu yeye akaondoka pale walipokuwa wamekaa na kujitenga.

‘Mnaona niliwaambia… huyo mtoto sio wa hiyo familia kwanini yulebaba hataki kupiga picha pamoja na yule mtoto, mtoto kaitwa yeye kajitenga..’watetesi wakazidi kuongea

Kiukweli katika hizo siku tatu baba wa hiyo familia alikuwa na wakati mgumu, hakupenda kabisa kushinda humo nyumbani, akawa anarudi usiku sana akiwa na uhakika yule mtoto kalala, na yule mtoto alikuwa akilala na nesi na ikitokea wakakutana na huyo mtoto hutafuta visingizio vya kumtoroka, licha ya kuwa mtoto kila mara alikuwa akimlilia na kumuita `baba, baba…’

Siku hiyo ya jumapili hakuweza kumkwepa huyo mtoto, na alipoona mtoto anamtaka sana wakae pamoja  moyo wa huruma ulimuingia, basi kwa kujibaragua akamchukua mtoto na kujifanya anamjali,…lakini alipomtizama usoni ,…mmh, alijikuta akimweka chini …na akatafuta mwanya wa kutoka hapo nyumbani , na kwenda zake nje kukutana na marafiki zake.

Mkewe alimshauri sana kuwa anachofanya siyo jambo la kiungwana, kwani yule mtoto hana kosa kabisa, yeye kama mtoto hajui kabisa nini kilitokea…mumewe anamjibu kuwa yeye hajui machungu gani aliyoyapitia , na mtoto huyo humtonesha donda ambalo lilishaanza kupona! Na mazungumzo hayo hayaishii vyema, mume mtu anaamua kundoka na kutembea tembea akisubiria muda huo wa sherehe.

Basi mtoto akaambiwa aitwe ili picha ya pamoja ipigwe

‘Mtoto haonekani…’ akasema dada mmoja ambaye alitumwa kwenda kumchukua huyo mtoto nje alipokuwa akicheza.

‘Umemwangalia huko alikokuwa akicheza na wenzake..’ akauliza nesi

‘Kote nimeangalia na nimewauliza wenzake wanasema hawajui wapi ameenda..’akasema

‘Atakuwa kaenda wapi naye hata tabia ya kutembea mbali na hapa nyumbani..’akasema mama wa kufikia alipopewa hiyo taarifa.

‘Alisema anakuja kunywa maji, na alipoondoka hajarudi…’akasema mtoto mwingine.

‘Mimi nilimuona akiangalia ng’ombe aliokuwa wakipigana kule..’akasema mtoto mwingine …’ ilimradi kila mtoto alisema lake. Ikawa shughuli kumtafuta mtoto kaenda wapi. Mtoto hakuonekana, shughuli ikaingia mtafaruku.
.
‘Sasa tutafanyaje maana hii sasa ni kesi akija mama wa mtoto tutamwambia nini…na wakuu wangu walishanikabidhi hili jukumu, si ndio kufukuzwa kazi, ..hili ni balaa gani tena…’ akaanza kulalamika nesi.

‘Bwanae, naona unataka kutuharibia tafrija yetu, niliwaambia huyo mtoto sio damu yetu atatuletea mabalaa hamtaki kusikia, angalieni sasa,  mimi hili nilishaliona kabla, tangu huyo mtoto aletewe hapa, kila mara linazuka jambo la utata..mnaona sasa..’akasema baba mtu
‘Usiseme hivyo baba mtarajiwa, hapa cha muhimu ni kuhakikisha huyo mtoto anapatikana hiyo ni dhamana tulikabidhiwa, …’akasema mke wake.

‘Mimi simo kabisa, na wala msinishirikishe, maana huyo mwanamke balaa akija hapa atanizukia mimi na kuniletea mambo nisiyo yataka…’ akasema shemeji mtu.

‘Hili ni letu sote kwasababu mtoto huyu aliachwa hapa kwenye nyumba yako, huwezi kulikwepa cha muhimu ni kusaidiana jinsi ya kumtafuta , na bora tuwape taarifa polisi…’ akasema mke mtu.

‘Nani aende polisi, yaani nipoteze muda wangu kwa ajili ya…mtoto ambaye katelekezwa kwangu wakati wazazi wapo…hivi mnamjua baba yake, ni tajiri wa ng’ombe….’ Aksema mume mtu na kabla hajamaliza simu ikaiita, na nesi alipoitizama simu yake akakuta anayeiita ni docta, akasogea pembeni huku akiwa na wasiwasi atamwambiaje huyo docta bosi wake ambaye alishachukua dhamana ya usalama wa huyo mtoto!

NB: Kwa leo naishia hapa maana nahangaika kutafuta wadhamini wa kuweka matangazo ili tuweze kwenda sawa


WAZO LA LEO: Ulimi ni kitu cha kuchunga sana, kauli tunazozitoa kwa watu tujaribu kuwa makini nazo, sio kwa vile unajiweza , au wewe ni kiongozi bosi, unaona sawa vyovyote utakavyoongea, hapana ukubwa wako , utajiri wako, ubosi wako hauna maana kama utakuwa na kauli chafu, roho mbaya na dharau.Tukumbuke kuwa hekima busara ndiyo inamjenga mtu aoanekana wa maana mbele ya wengine. 

Ni mimi: emu-three

No comments :