‘Mwanangu safari yangu ya kwenda kutibiwa India ilinijia kwenye
ndoto, siku ile nilipokuwa nimezirai sijitambui, na kila hatua ilijionyesha
wazi ndani ya ndoto, na kama ningekuwa najua kuwa ni kweli ningeliwaambia kuwa
msiwe na wasiwasi, lakini sikuwa na uhakika nini tafsiri ya ile ndoto, kwani
nilikuwa nusu mfu.
‘Mama hata siamini...nisamehe mama nilikusahau kabisa....’nikasema
huku tukiwa tumekaa ndani na muda huo yule docta aliaga akasema anaondoka kuwajibika
ila atarudi tena kuona kama kila kitu kipo shwari…
‘Najua mna hamu sana ya kuongea mengi , kwa ratiba yangu mimi hapa tumemalizana mimi nahitajika kazini, kwahiyo sijui mama
unasemaje…najua dereva wako atajua jinsi gani ya kukurudisha nyumbani kwako... au bado unanihitajia, maana uliniogopesha...?’ akauliza docta
‘Mhh, ilimradi nimemuona mwanangu , sina shaka tena...dereva wangu atajua jinsi gani ya kunirudisha nyumbani kiliniki kwangu..’akasema mama
‘Kilini kwako, ina maana mama bado unatibiwa...?’ nikauliza kwa mshangao
‘Mama yako kaniambia ana kliniki yake ya kuwahudumia wagonjwa wanaosumbuliwa na maumivi ya kichwa, kuumwa na kichwa kusikosikia dawa, unakunywa dawa kinatulia, bado kinarudia tena..au kuna watu wanasema wana changanyikiwa kama mashetani, mama yako kwa mkono wake anaombea kinapona...kiufupi mama yako ana utaalmu fulani anaufahamu yeye mwenyewe..'akasema docta
Nikaguka kumuangalia mama na jinsi alivyovaa, nikajaribu kukumbuka vile alivyokuwa akijifunika, ..japokuwa kiukweli alifunika kichwa, ila sasa hivi hajajifunika usoni, na docta akazidi kuongea;
'Na nimefurahi sana, maana mama yako kaniambia ana nyumba yake ambapo ndipo anapoishi
kwa sasa....ila nimemwambia sikuchukua maana upo
kwa mtu ambaye alichukua dhamana na wewe inabidi umsubirie huyo mtu kwanza ili muongee
naye. Ili kujua kama kuna madai yoyote, huo ndio ubinadamu na ndivyo tulivyokubaliana...au sio mama....’akasema
‘Kuna madeni!?, …mmm sasa nitatoa wapi pesa za kumlipia maana wao
walinichukua sijijui, nilikuwa sikumbuki kitu mama, lakini hakuwahi kuniambia kuwa nadaiwa, au ananitibu kwa mkopo….’nikasema
‘Usijali mwanangu kama kuna madeni yatalipwa..mimi mama yako nipo
kwa uwezo wa muumba kila kitu kitakwenda vyema…’akasema mama, huku
nikimuangalia mama bila kummaliza, hivi ni yule mama aliyekuwa omba omba….siamini
‘Sasa mlijuaje kuwa mimi nipo hapa...?’ nikauliza kwa mshangao na
docta akasimama na kusema
‘Yote atakusimulia mama yakom maana kanitoa kazini kwangu kama vile nadaiwa,... ngoja mimi niwaache..’akasema docta
na kuondoka.
‘Nashukuru sana docta nisamehe, lakini sikuwa na jinsi nyingine..'akasema mama, na docta akaaga na kuondoka, tukabakia na mama, na mama aksema
'Mwanagu tulihangaika sana kukutafuta unajau nilirudi sasa ni nina miezi mitatu, tumehangaika mpaka nimeenda kijijini, nikarudi, tukatfuta kila sehemu, hata wenzangu wakafikia kusema umeshakufa, nikawaambia mwanangu hajafa yupo hai, ila sijui wapi ulipo na hilo limfanyika kwa matakwa ya mungu...'akasema mama
'Poleni sana, ni kwasababu mimi nimekuwa mtu wa ndani,..nilikuwa siwezi kutembea, ila leo uliponiombea naweza...sijui kama nitashindwa, si umeona pale nimeweza kusimama kidogo...na mwili uliokuwa hauna nguvu sasa una nguvu, ...miguu sasa naweza kunyosha si unaona...
'Pole sana mwanangu, kukupata wewe ni baada ya kufika hapo muhimbili, na
kukutana na huyo dakitari ….’akasema
‘Mlikuwa na nani….?’ Nikauliza
‘Na wafanyakazi wangu , na docta mwingine ambaye alinisaidia
kipindi kile cha mwanzo, lakini badaye akakkata tamaa, na ila alipokuja jana akasema tujaribu kuulizia Muhimbili, hatukuwa na wazo hilo kabla, limekuja tu na kumbe ndio ikawa sababu ya kukupata wewe, tuliwahi kufika kipindi cha mwanzo hapo muhimbili tukauliza , huyo tuliyemuuliza alisema hakuna taarifa yoyote ya mtu kama wewe, nahisi hakutaka kutusaidia, lakini safari hii docta akakutana na madocta wenzake, akawaelezea, na ndipo akatokea huyo docta akasema anakumbuka kumuhudmia mtu kama huyo... ..’akasema mama
‘Mwanangu nilishaota ndoto kuwa nisipokupata leo nitakukuta maiti….kwahiyo
nilikuwa kama nimechanganyikiwa, na hata nilipofika hapo Muhimbili nikamkuta
huyu docta akiwa na kazi zake, aliponiambia tu kuwa kuna mtu kama huyo aliwahi
kulazwa hapo, akamuhudumia yeye , nikamwambia;
‘Naomba unipeleke nikamuonea haraka…’nikasema
‘Lakini mama mimi nipo kazini ziwezi kutoka hapa labda nikupe
mawasialiano ya mtu ambaye ninamfahamu ambaye alimchukua na akasema atakuwa
naye ..huyo mtu ana kiliniki yake ya ‘physiotherapy’, …ni rahisi kufika kwake’akasema mama
‘Nataka wewe unipeleke mguu kwa mguu na usipofanya hivyo kama mtoto wangu akifa na wewe utakufa…’nilimwambia hivyo na akaogopa, akasema;
‘Haya mama ngoja niage wenzangu,...' na kweli akawaaga wenzake na akawasiliana na huyo
mtu aliyekufadhili, yeye yupo safarini lakini alisema kuna mdada anakusaidia
hapo tunaweza kumkuta lakini kama huyo mdada hayupo, maana huyo mdada ana kazi zake nyingine, anafika hapo kusaidia tu, wafanyakazi wengine wapo watatuelekeza wapi ulipo, …’akasema
mama
‘Ina maana kumbe nipo kwenye kiliniki,…mmh nilijua nipo nyumbani
kwangu….na huyu mdada hapa ni mfanyakazi wa humu ...leo kachelewa sana kufika sijui kuna nini...’nikasema
‘Mdada….?’ Akauliza mama.
‘Yupo mdada huwa ndiye ananihudumia kwa kuninyosha viungo na
chakula…..’nikasema
‘Mimi sijamuona, labda upande wa pili, maana wewe upo huku nyuma,
hujawekwa sehemu ya wagonjwa...na ngoja tuagize chakula maana mimi nina njaa’akasema mama akatoka na mimi nilibakiwa nikiwaza mengi, haikuchukua muda mama akarudi akiwa na chakula.
'Mama utafikiri wewe ni mwenyeji, mimi bado najiona mdhaifu..'nikasema
'Umeshapona, kinachohitajika ni mazoezi machache na kuondoa ile hofu, ...'akasema mama
‘Oh, akili ilikuwa haipo mama, …sikuweza kukumbuka kitu, nilikuwa kama mfungwa wa akili….sasa mama ikawaje..?’ nikamuuliza
‘Mwanangu kabla nilishamuomba mungu kuwa niwe nawe hadi mwisho wa
maisha yangu, na nilishakuota kwenye ndoto ambayo ilinielekeza mengi kuhusu
wewe lakini ilifungwa kujua wapi ulipo , pamoja na karama alizonijali mungu,
lakini hazikuweza kujua wapi ulipo....’akasema na kunyosha mikono juu
‘Karama gani mungu kakujalia mama....?’ nikamuuliza
‘Mungu ni mkubwa mwanangu, wanadamu tunazarauliana sana na
kunyanyasana, lakini huwezi kujua huyo unayemnyanyasa mungu kamjalia nini..unakumbuka
niliwahi kukuhadithia kuwa niliwahi kuitwa mama mwenye mkono wa baraka…?’
akaniuliza…’akasema
‘Mhh mama, sijakuelewa…uliwahi kunihadithia ….oh, yah, nimekumbuka
na kweli kuna mambo nahitajia kujau kutoka kwako, ….nimekumbuka kuleee
ulipokuwa kijijini, ukaunguzwa na moto…’nikasema
‘Ni kweli mimi nina karama hiyo ila nilikuwa sijijui, …namshukuru
sana mungu, niligundua hilo zaidi nikiwa huko India, wakati nasubiria
kurekebishwa sura yangu,...unajua huko nilikwenda kwa ajili ya upasuaji wa
uvimbe kichwani sio swala la kurekebisha sura yangu iliyokuwa imeharibika…unaikumbuka
sura yangu ilivyokuwa awali…?’ akaniuliza
‘Mama hapana….nakumbuka utundu wa utoto tulijaribu kukufunua,
lakini mimi sikupenda, nilijali sana ulivyonifundisha, …kuwa na adabu kwa
wazazi…sikumbuki mama…’nikasema
‘Sasa una uhakika gani kuwa mimi ni mama yako..?’ akaniuliza
‘Hahaha, mama…siwezi kukusahau ,…macho yako na yangu naona
yanafanana…nakumbuka kuna picha nilikuwa nayo nikiwa mdogo, …macho yangu yapo
hivyo hivyo, ila sasa yameanza kubadilika sio kama nnilivyokuwa mdogo…mimi nina uhakika wewe ni mama yangu , japo
hujanionyesha ushahidi…kwanza hebu nambie ilikuwaje huko India ulifikaje…? Nikauliza
‘Tutaongea hayo tukiwa na muda , yapo mengi ya kuongea, ..’akasema
mama
‘Ehe…..’nikasema
‘Kwahiyo baada ya upasuaji kwa ajili ya uvimbe kwenye ubongo
kufanikiwa nikawa nasuburiwa kurudi nyumbani, hakukuwa na pesa hiyo ya
kurekebisha sura yangu, kwani mfadhili aliyefika huko aliulizwa kama kuna pesa
kwa ajili tatizo hilo akasema yeye hakupewa hilo fungu, kwahiyo nirudi nyumbani
kama itapatikana hiyo pesa basi nitarudishwa tena huko India.
‘Basi siku hiyo wakati nasubiria vipimo vingine kuhakikisha kuwa
nimeshapona, akaja dakitari huyo bingwa wa upasuaji wa kurekebisha sura, alifika
kujua kama anaweza kufanya hiyo kazi, yeye anfanyia hapo hapo hospitalini, lakini
alikuwa katuzoea sana, alikuwa kila mara anakuja kunisalimia, na siku hiyo alipofika
akawa analalamika kuwa anaumwa kichwa
‘Kichwa changu kinauma sana,....’akawa analalamika alikuwa
akiongea kiingereza huku akiwa ameshika kichwa, ilionyesha anaumwa kweli mpaka
machozi yanamtoka, na unajua mganga hajigangi, pamoja na utaalamu wake lakini alitumia
dawa zote anazozifahamu yeye lakini hakuweza kupona kabisa huwa kinarudia mara
kwa mara. Basi hata sijui kwanini ...mimi nikamwambia mfadhili wangu amwambie huyo
docta nimuombee huenda kitapona
‘Wewe mama mwenyewe ulishindwa kujiombea, mpaka ukaletwa huku,
....achana na hao watu wewe tusubiri hivyo vipimo tuondoke zetu....’akaniambia
huyo mfadhili wangu
‘Mganga hajigangi, wewe mwambie hivyo hisia zinanituma kuwa
nikimombea huyo dakitari kichwa chake atapona kabisa....’nikamwambia na yeye
hakukutaa akaenda kumwambia hivyo huyo dakitari wakati huo kakaa chini kainama
kichwa kinamuuma kweli, ya mungu mengi ...akakubali. akasema niende pale
alipokaa maana alikuwa hawezi hata kusimama na ubingwa wake wote wa udakitari
Nikaenda hadi pale alipokaa nikanyosha mkono wangu na kuuweka
kichwani kwake, nikamuombea,.....akapona......’akasema mama
‘Mama ulimuombejae....?’ nikamuuliza mama kwa bashasha
‘Nani kama mama mwanagu, ....mungu muweza uliyejalia uzima, na
kumjalia mama kupata mtoto kwa njia ya mateso, akiwa na imani thabiti
akamtegemea mungu dua yake haina kipangamizi mwanagu,… maneno ya kumuombea huja
hapo hapo, siwezi kukumbuka ni maneno gani kwa hivi sasa... kwani maneno yangu
ya karama hutokea kutegeemeana na tatizo la mtu, na hunijia tu nikianza kuomba
.....’akasema
‘Mhh mama, kwahiyo hata mimi kupona kwangu uliniombea au ilikuwaje
maana mama ulipokuja hapa sikuwa nakumbuka chochote, na nilipokuona tu kichwa
kikaanza kuuma, nikawa kama nachanganyikiwa, akili ilikuwa kama sio yangu,
nikaanza kuona vitu vya ajabu kichwani, kichwa kikawa kinauma karibu kupasuka,
lakini ulivyoweka mkono wako kichwani, mama ikawa ni ajabu kabisa ....’nikasema
‘Mama ikawa kama vile umenimwagia maji ya baridi yakipooza hayo
maumivi ndani kwa ndani, na cha ajabu maji hayo yana hisia, ikapooza maumivu na
hapo hapo ikawa inasisimua ubongo na mwili uliopooza, .....ajabu kabisa mama....ulifanyaje
mama?’ nikauliza, na mama akawa kimia nikasema;
‘Mama hebu fikiria mwili ambao ulikuwa hauwezi kufanya kitu,
nilikuwa natembelea hicho kigari hapo, mwili ulikuwa umepooza, siwezi kusimama,
nifanya kujikokota kwa shida, kuna muda
najaribu kusimama lakini miguu inakuwa haina nguvu, na hicho kigari cha
kusukuma, ndio miguu yangu…lakini sasa mama naweza kusimama.
‘Mama nimepona, si unaoana...nikasimama nikayumba kidogo, lakini
nikajitahidi na kuanza kutembea huku na kule, nikaruka kwa raha,...
‘Mama nimepona,.....nakushukuru sana mama yangu....’nikasema na
kumsogelea, kumkumbatia mama akasema;
‘Mshukuru mungu....unasikia nyosha mikono juu umshukuru mungu
wako, na kawaida mtu akipona yeye ndiye anataja kiwango gani cha kunilipa mimi,
kwahiyo taja unataka unilipe nini....’ mama akasema
‘Mwanagu karama za mungu ni nyingi, na ukiwa nazo hata wewe
mwenyewe huwezi kuzisema tu, kwani unafanya hivyo sio kama wewe, ni mungu
mwenyewe anashusha nguvu zake na kuzijaza mdomoni mwako, sio wewe ....kwahiyo
siwezi nikasema mimi ndiye natenda hizo karama, hapana, sio mimi mponyaji au
mtoa baraka ni mungu mwenyewe kwa kupitia mkono alionijalia na pumzi alionijali
na mdomo, ulimi wa kusema alionijalia, sio mimi mwanagu mimi ni njia tu..’akasema
mama
‘Mama.....mmh, na umasikini wangu huu, mama nitakununulia eeh,
gari zuri saan la kutembelea....’nikajikuta nimesema hivyo wakati mimi sina
kitu , hohe hahe
‘Sawa mwanangu, wewe ni mtoto wangu, japokuwa sihitaji hilo gari
maana mimi ninalo gari langu, lakini ndio masharti ya karama hii ukipona ni
wewe mwenyewe unataja gharama kutokana na uwezo wako, na mara nyingi kauli hiyo
huja kwa uwezo wa muumba,....’akasema
‘lakini mama ukifanya hivyo watu si watakudhulumu, wengine
hawatataja kutokana na uwezo wao, wenye mioyo ya dhuluma,,,,,’ nikamwambia mama
, na mama akatabasamu na kucheka, akasema
‘Nikiwa India alikuja tajiri mmoja, tajiri huyo licha ya utajiri
wake, lakini alikuwa akisumbuliwa sana na maumivu ya kichwa, kichwa ambacho alikihangaikia
sana akatafuta madakitari wa kila namna lakini hakupona, na tajiri huyo alkuwa
na tatizo kubwa la ubahili, roho mbaya.....dhuluma, na hakujua kuwa kichwa
hicho kinamuuma kwasababu ya dhuluma, na tabia yake hiyo...’akasema mama
‘Ikawaje…’ nikatulia kusikiliza
‘Basi alipokuja nikamuombea, akapona kichwa chake, kama kawaida
akaniuliza ushuru, nikamwambia yeye ataje atanilipa nini…akasema dola elifu
moja, watu waliokuwepo hapo wakashangaa maana ni tajiri kweli pesa hiyo
aliyotaja kwake ni pesa ndogo sana
‘Sawa ..’mimi nikamwambia na akatoa akaondoka, na kwa muda huo huo
akafika mtu mmoja yeye ni masikini , wanamjua sana watu wa huko, alikuwa na
tatizo hilo hilo, nilipomuomba nikasema ataje kiwango, akasema dola laki moja…watu
wakacheka, mimi nikamwambia ‘sawa’
‘Nenda kazilete….’nikamwambia maana nilijua hana, lakini kauli
hiyo sio yake, ni kauli imetoka kwa mungu,…akaondoka, haikupita siku hiyo akaja
na hiyo pesa…’akasema mama
‘Aliipata wapi,…?’ nikauliza
‘Kutoka kwa yule tajiri wa mwanzo,..’akasema mama
‘Kwa vipi..?’ nikauliza kwa hamasa
‘Yule masikini alipotoka hapo, alikwenda masikani kwake, ….unajua
maswala ya haja, haja ndogo tu, yanaweza kumpata mtu popote pale ukashindwa
kuvumilia, kule kuna sehemu kuna sheria hutakiw kukojoa ovyo..
Huyu masikini ana simu yake ya kuchukua picha aliiokota tu, sasa
alipofika masikani kwake, yule tajiri alikuwa akipita na gari lake, alishikwa
na haja, hakujua eneo hilo kuna mtu anaishi, akazarau akijua ni uchochoroni tu,
yule tajiri akawa anajisaidia, ni uchochoro, lakini ni eneo lenye sheria hizo,
alishikwa na haja hakuweza kuvumilia, yule masikini akatoa kamera yake haraka
akamchukua picha ya video jamaa hajui..kamaliza haja yake, anataka kuondoka
masikini yule akamkabili
‘Umevunja sheria…’akasema na walinzi wakamsogelea wakita
kuhakikisha bosi wao hazuriki, akawaambia walinzi wamuache tu, maana yeye
anamfahamu huyo masikini akamuuliza nimevunja sheria gani
‘Umekojoa eneo lisiloruhusiwa..’akasema na huyo tajiri akashituka
hakujua kabisa kuwa kaonekana, akamuuliza
‘Una ushahidi gani..?’ akauliza
‘Utaujualia mahakamani..’akasema masikini, na yule tajiri kwanza
alitaka kutumia nguvu lakini akashituka akaujua ni lazima huyo masikini atakuwa
na kitu cha kuweza kumsaidia, akasema
‘Unataka nikupe nini, ili usinishitaki….?’ Akauliza
‘Dola laki moja na nusu…’akasema
‘Nini…wewe unaota nini…’akasema
‘Na huo ushahidi nimeshauhifadhi kwenye mtandao huwezi kuuondoa, mpaka mwenyewe nikubali..’akasema,
na yule tajiri akasema;
‘Haya twende nyumba ni nikakupe..akijua akifika huko atamfanyia
vituko, lakini masikini yule alikuwa mjanja, alikuwa na akili japokuwa nakama
zilimuandama, akasema
‘Mpaka awepo mwanasheria wangu..’akasema na walinzi wakacheka, na
hakujali kicheko chake akampigia wakili mmoja anayejulikana sana, wakili ambaye
sifa yake kubwa ni kuwasaidia wasiojiweza , anajitolea ..hakuipita muda akafika
huyo wakili, yule tajiri akaona sasa anaumbuka.
‘Kwani wewe una ushahidi gani…?’ aakmuuliza
‘Yule masikini akatoa simu yake akampa yule wakili na yule wakili
akaliona hilo tendo, na wakili sasa akawa anaongea na huyo tajiri, yule
masikini akakaa pembeni.
‘mteja wangu aantaka dola laki mbili pamoja na gharama zangu,,….’akasema
wakili
‘Eti nini…?’ akasema huyo tajiri
‘Kama hutoi tutakuita mahakamani, na ujue vyombo vya habari
viatakuwepo…’akasema, na kwanini huyo tajiri asitoe hizo pesa, na yule masikini
kwa haraka akaja kunipa hizo pesa na nyingine akampa yule wakili ushuru wake,
na akabakiwa na haki yake…’akasema mama
‘Mama ni hadithi au ni kweli…’nikamuuliza mama
‘Mwanagu kutokana na matatizo haya, kutokana na karama hii
nimekutana na mambo mengi ya ajabu, na ukitaka nikusimulie yaliyonikuta
tutakesha, ila wewe elewa kuwa mungu ndiye mtoa riziki, na hata uwe tajiri vipi
kama mungu kapanga kuwa riziki uliyo nayo itakwenda kwa mtu mwingine kamwe
hutaweza kuzuia,..’akasema mama
‘Sawa mama turudi kwa huyo dakitari bingwa ikawaje kwake..?’
nikamuuliza
‘Kutokana na lile tendo, maana wakati namuombea walifika
madakitari wengine wa hapo wakawa wanataka kushuhudia, mama muafrika anawezaje
kumtibu huyo dakitari bingwa, ilienea kwa hara ka sana.
Mimi nilipomaliza kufanya yale maombi nilishangaa nimezungukwa,
madakitari manesi wa hapo wamakuja kushuhudia,….’akasema mama
‘Nilipomaliza nikageuka kwa mfadhili wangu nikamwambia;
‘Nimemaliza, atapona tu hicho kichwa chake, kwa uwezo wa mungu…’hata
huyo mfadhili wangu hakuamini, maana yule dakitari alisimama akaniangalai sana
akasema
‘Nitakufanyia huo upasuaji kwa gharama zangu mwenyewe…, nahis
kichwa kimepona, …its like a magic….’akasema
‘Kweli mama, ikawa hivyo…?’ nikauliza
‘Ndio hivyo nikafanyiwa huo upasuaji na sura yangu ikarekebishwa,
japokuwa niliandamwa na ugonjwa wa ngozi nahis ni aleji, nikawa natokwa na vipele,..lakini vilikuja kuisha ndio maana
unaniona hivi…. na baada ya hapo wakataka kuniajiri niwe mfanyakazi wao…nikakataa,
nikasema ninaweza kukaa hapo kuwasaidia watu, kwa muda, lakini sio kwa
kuajiriwa…
‘Basi wakanikubalia, lakini kwa sharti kuwa ni lazima kuwe na
malipo, ili niweze kuwalipia kodi na hapo hospitalini, wao wakataka kupanga
kiwango nikawaambia mimi karama yangu haina kiwango, kiwango kinatokana na
uwezo wa mtu kama wanataka sawa, kama hawataki narudi kwetu..wakakubali…’akasema
mama
‘Basi kwa kupitia huyo dakitari nikajulikana, …unajua kuna watu
wengi wana matatizo ya kichwa, kichwa kinauma sana, na wengine hufikia hadi
kuchanganyikiwa, na kutokana na karama hii nimeweza kuwasaidia watu wengi,…watoto
wanaolia lia, matatizo ya kupoooza viungo kutokana na maumivi ya kichwa..’akasema
mama
‘Kwahiyo mama ukawa tajiri…?’ nikamuuliza mama
‘Kwa uwezo wa mungu na karama zake sasa hivi mwanagu hatuna shida
tena, walitaka nikae huko India lakini sikukubali, baada ya miezi kadhaa
nikawaambia narudi nyumbani, nakwenda kumtafuta mwanangu najua mwaanngu yupo
matatizoni.
‘Waliniomba sana, nikawaambia nitarudi, hapo nitakapohakikisha
nimemuokoa mwanangu..na ndio nikarudi nikakuta nyumba imeshajengwa, na ipo kliniki
imeshajengwa, kutokana na ahadi za wale nilioaombea na gari hilo hapo nje....kwahiyo
mwanangu tuna nyumba yetu nzuri tu, kiliniki , na gari..na p[esa nyingi tu…’akasema
mama
‘Nyumba yetu....?’ nikauliza
‘Ndio ni yetu mimi na wewe...sina mtoto mwingine zaidi
yako,.....na kama nisingelikupata basi sijui.....ingekuwa haina maana
kwangu....’akasema mama
‘Oh mama...ina maana…,’nikasema
‘Mwanangu ukiwa na shida ukiwa na matatizo usikate tamaa, shida
hiyo ni mithani ya mungu kukuelekeza kwenye jambo la heri...shida hiyo ni mitihani
ili msimamo wako kwa muumbako ujulikane...ukitulia , ukatuliza mawazo
ukaelekeza uso wako kwa mungu...utafanikiwa tu mwanangu...’akasema mama
‘Mwanagu kuna ile ndoto niliyoota, unakumbuka nilikuahadithia
kuhusu ile ndoto...Niligundua ukweli wa ile ndoto nilipokuwa nasubiri
urekebishwaji wa sura yangu.
Nawashukuru sana wafadhili waliojitolea kuhakikisha naondolewa huo
uvimbe na sura yangu kurejea hapa ilipo…hata mimi sikuamini pale nilipoambiwa
nijitizame kwenye kiyoo, ilikuwa kama najiona wakati nipo msichana…’ aliongea
mama huku namtizama usoni
Nilijaribu kumuwazia alivyouwa awali, bila kufanikiwa, kwa maelezo
yake sura yake iliharibia sana, hata haitizamiki, ilifikia hata yeye mwenyewe
alijichukia, na kutokana na jinsi alivyouwa wengi waliamua hata kumuita mwanga kwa ajili
ya michirizi na kuchanikachanika usoni, na sura kuwa ya kutisha, na ukichanganya
na macho yake yaliyouwa na utofauti fulani, basi ilikuwa kama kisingizo.... leo
hii ni mwanamama mwenye sura ya kipekee…
Ni ajabu iliyoje yale macho ukiwa na sura kama ile ya utisha alionekana
wa ajabu, na kuonekana ni mwanga, mchawi…lakini sasa akiwa na sura nzuri, macho
hayo yalimfanya mama aonekane mrembo,…nilijikuta nikitabasamu na kusema moyoni,
ama kweli mama alijaliwa uzuri
‘Mungu ni mkubwa mama, siamini hadi sasa naona kama namtizama
ndugu yako, kwani sikumbuki kuiona sura yako ukiwa katika hali nzuri kama
hii..’nikasema
‘Nitakuonyesha picha zote nilizopiga nikiwa huko kabla na baada ya
huo upasuaji, ili ujue kuwa dunia hii kuna wataalamu, tuwashukuru sana
madakitari ambao fani yao kwakweli ni ya kujali uhai wa mwanadamu…’ akasema
mama
Mama akaongezea kusema, `Kumbuka nilikimbiwa, niliitwa mchawi,
nikadharauliwa sababu ya sura ile, ambayo sikupenda kabisa iwe vile, ila
ni kwasababu ya watu wenye roho mbaya…’akasema mama .
‘Mwanangu ndani ya ndoto yangu niliota kuwa upo katika hali mbaya,
na yale yaliyomtokea mama yako akimbiwe kuwa ni mchawi, yamekuandama kwa
namna nyingine, watu wanakukimbia na kunynyapaa kwa hali uliyo nayo, kukonda
kwako kumekuwa ni sababu ya kuonekana si mwanadamu….yote hayo niliyaona
kwenye ndoto kwa namna ya fumbo, lakini usijali mwanangu kwani yote hayo ni
mitihani ya kimaisha, ikija unatakiwa uwe na subira, na usimamie katika haki…’
mama akanishika kichwa.
‘Kwahiyo mama unataka kuondoka..?’ nikamuuliza
‘Nakwenda kuwawahi wateja , wataje ni wafalme, nitapitia hapo
kuangalia gharama zako, nijue nikiasi gani halafu nitakuja kulipia, tutaondoka
sote….’akasema mama
‘Sawa mama, lakini kabla
hujaondoka … unakumbuka uliwahi kunihadithia maisha yako ulipopitia na
nakumbuka ulikatisha siku ile ulipozidiwa ukashindwa kunimalizia kuwa
ilikuwaje , je yule mama kule hospitalini alikuwa wewe au nani na siku
ile alipoondoka kule nyumbani kwa dada yake nesi alikwenda wapi na je
alimpataje mtoto wake, na huyo mtoto ndio mimi au alikuwa mwingine…?’ nikamuuliza maswali mengi kwa pamoja.
Mama alimwangalia mwanae kwa muda, halafu akatabasamu na kusema,
‘hivi mwanangu bado una hamu na vidonda vinavyoonza kupona, huoni ukiyawaza
hayo , ukayahadithia , yanatia simanzi , na mwishowe unakaribisha hasira za
visasi, mimi naona tusahau hayo tugange yajayo…’Mama akasema akiinuka
kuondoka.
NB: Je mnahitaji kujua hayo, yaliyokuwa yamebakia huko kijijini,
je unahitajia kujua jinsi mama alivyokwenda India, …kama mnapenda, tuelezane,
vnginevyo, kisa kinaweza kuishia hapa, iliyobakia ni hitimisho tu…
WAZO LA LEO: Dunia tulivyo, mnaweza mkahangaika
pamoja, kutafuta pamoja, lakini pale mnapopata tabia hubadilika, uchu, uchoyo
ubinafsi huteka nyoyo zetu, tunaweza kusahau kabisa jinsi gani tulivyohangaika
pamoja, na huenda hata katika kuhangaika mmoja au wachache ndio waliokuwa
wakitumika zaidi, lakini wale wategaji, wajanja-wajanja, waongeaji sana bila
vitendo, ndio wanaweza kudai masilahi
zaidi ya wengine…huo sio uungwa, huo sio upendo, huo sio uadilifu, ili kweli
tuwe wachamungu wa kweli, wepenzi wa kweli, ni pale kila mmoja atakapokuwa
tayari kutoa , au hata kuacha ili mwenzake apate, kuoneana huruma, hata kama ni
kidogo uwe radhi mwenzako apate wewe ukose, je kuna upendo kama huo,. Je watu
kama hao wapo kwenye hii dunia?
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment