Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, May 22, 2015

NANI KAMA MAMA-81


 ‘Hivi kweli mimi nina mke, mke wangu yupoje, anafananaje, je ananipenda…naona atafurahi sana akiniona nimepona, au…oh nahis huenda tulikuwa na furaha sana,’ yalikuwa maswali mengi kichwani, na sijui kwanini nilikuwa nikiwaza hili la mke sana,  kuliko mambo mengine.

Nilifikia kuwaza jinsi tulivyokutana tukapendana,….tukafikia kuoana..nikajenga taswira nyingi za huyo mwanamke kuwa ni mrembo sana….nikajaribu kufikiria sura nzuri zaidi,…na mimi mwenyewe kujiona kijana mtanashati…yaani mawazo mawazo….

‘Sijui sasa mke wangu atakuwaje…kakonda, hapana, ni ….mmmh….’nikajikuta naongea peke yangu.

 Nikawa nasubiri kuwaona hao jamaa zangu ambao niliambiwa wanakuja kila siku, nakumbuka kuna watu huwa wanakuja, tunasalimiana na wanandoka, lakini sijui ni akina nani, labda ndio hao jamaa zangu sikuwa na uhakika kwa kweli.

Siku hiyo niliwaza sana, nikiwa na matumaini ya kuwaona hao ndugu zangu, nikiwa na matumaini ya kwenda kupaona hapo nyumbani kwangu, sikuwa najua ni wapi, na kama nina nyumba au nimepanga,…

Wakati nawaza haya nikashikwa na usingizi, na ndani ya usingizi nikamuona mwanamke mmoja akiwa, kavaa nguo zinazomeremeta, alikuwa kakaa kwenye kiti, halafu anakunywa kinywaji kweny gilasi, alikuwa mwanamke mrembo wa kuvutia, na alionekana hataki kuguswa na takataka, kwani kila mara alikuwa akijiangalia na kila akiona kitu tofauti anakifuta,…alikuwa anameta meta

Baadaye nikaona hali inabdilika, ile sura yake ikawa inabadilika taratibu, na ilna akawa anaingiwa na madoa ya uchafu , na kila kiona hivyo anahangaika kuyaondoa hayo madoa lakini yakwa yanamjia kwa aksi, akawa anabadilika hata sura, na baadaye ile rangi ikawa sura ya kutisha ajabu, mdomoni akawa anatoa uchafu, ….ulikuwa unatoa harufu mbaya ajabu. Na alipofunua meno yake yakawa ya kutisha kama ya shetani…

Nikawa sitaki kumtizama yule mwanamke, naye anakazania nimtizame kile anachotoa mdomoni, na mara akatokea mwanamke mwingine akiwa kajifunika usoni, alikuwa akimtizama yule mwanamke kwa macho ya huruma, halafu akanitizama mimi, na akawa kama ananionya kuwa huyo mwanamke atanilisha uchafu wake nisogee pembeni, nikawa najaribu kusogea lakini sikuweza kuinua hata mkono.

Yule mwanamke anayetoa uchafu mdomoni, akacheka kicheko cha dharau, huyo mwanamke mwingine ambaye kajifunika, akatikisa kichwa na kunyosha mkono wake kuniweka kichwani, lakini kila akijaribu kunisogelea yule mwanamke anayetoa uchafu anamzuia, ikawa kama wanashindana, na mimi siwezi kuinuka, wala kufanya lolote….

Na katika juhudi hizo ,yule mwanamke aliyejifunika uso, akaweza kunifikia na mkono wake akanifikia kichwani,  ilikuwa kama ubaridi fulani, au kitu ambacho huamusha hisia mwilini, …kwani nilihisi mwili ambao ulikuwa joto unapoa, mwili ambao ulikuwa hauna hisia unahisi kitu fulani.

Mara yule mwanamke anayetoa uchafu akaanza kubadilika sura, na kama vile anaoza, na kuanza kumomonyoka, na baadaye akawa anapotoea kidogokidogo huku anapiga ukulele. Huyu mwanamke aliyenishika kichwani akawa ananitizama usoni, lakini nilikuwa simuoni vyema sura yake kwani alikuwa amejifunika usoni kwa nguo.

Baadaye yule mwanamke aliyebadilika akapotoea kabisa nikabakia na huyo mwanamke aliyejifunika usoni, akaniuliza,. ..

‘Unajisikiaje kwa sasa,….?’ Akaniuliza nikajaribu kupanua mdomo niongee sikuweza, basi nikawa namjibu kwa hisia

‘Naona nimepona…’nikasema kwa hisia, halafu akaniuliza;

‘Unajua mimi ni nani?’ akauliza yeye alikuwa anatoa sauti, mimi nikamjibu kwa hisia tu.

‘Nitajuaje we ni nani wakati umejifunika uso wako….’ Na nikijibu kwa hisia anaelewa, nikaongezea kumuuliza kwa hisia;

‘Naomba ujifunue uso wako maana naona wewe ni mtu mwema sana ….kwani wewe unanifahamu kuwa mimi ni nani….?’ Akanitizama, alitoa sauti kama ya kicheko, halafu akasema;

‘Mimi nakufahamu sana, hata kama wewe ungejifunika kama mimi ningekufahamu pia,…’akasema

‘Kwa vipi, kwani wewe ni nani mpaka unifahamu kihivyo,..?’ nikauliza kwa hisia nikionyesha mshangao

‘Mimi nakujua ,a kukufahamu hata kabla wewe hujajiua wewe ni nani…’akasema

‘Mhh, basi wewe sio binadamu wa kawaida…naomba nikufahamu wewe ni nani…kwani kuna ubaya….naomba pia nikuone sura yako….’nikasema kwa hisia

‘Ipo siku utaniona vyema kwani kwasasa siwezi kutizimika,….nilivyo watu, hata wewe hutatamani kunitizama, ….’akasema

‘Kwanini huwezi kutizamika, kwani sura yako ipoje, inatisha, au imefanyaje au wewe sio binadamu wa kawaida? …mimi kwa vyovyote uwavyo nitafurahi kukuona sura yako…’nikasema kwa hisia, na yeye akasema.

‘Yote ni mapenzi ya mungu, na yote yametokea ili mapenzi ya kweli ya mama na mtoto wake yaonekane…’akasema

‘Mama na mtoto wake…?’ nikauliza

‘Nikuulize wewe je unamfahamu mama yako ni nani, mama yako wa kweli, aliyekuzaa, akakulea, …?’

Nikijaribu kufunua mdomo ili nitamke neno mama, lakini haukuweza, nikasema kwa hisa ile ile,

‘Mama, mama yangu, yupo wapi…mimi simjui mama yangu….’nikasema

‘Unaona..wewe humjui mama, je kweli mtoto anaweza kuzaliwa bila mama yake..?’ akaniuliza

‘Hapana….najua kuwa nina mama, lakini sijawahi kumuona..’nikasema kwa hisia

‘Lakini mama yako anakujua na anajua ana mtoto kama wewe hata kama kumbukumbu zake hazipo, …unajua ni kwanini?’ akauliza
‘Mhh…sijui…’nikasema hivyo hivyo kwa hisia, nikashngaa kwanini kaniuliz vile, na kabla sijasema neno kwa hisia akasema ,

`Nikuonyesha kuwa hakuna kama mama, kwani mama anakujua wewe kabla hujajiua, alikuhisi ukiwa tumboni mwake, ukacheza huko ndani ukampiga mateke, akakuzaa kwa shida, wewe hujui na wala hujijui, je atawezaje kukusahau baada ya kukuzaa…’akasema.

‘Lakini ….wewe ni nani, basi niambie mama yangu ni nani na yupo wapi…’ nikauliza swali na akasema

‘Usiwe na haraka, utamfahamu kwa wakati muafaka…kwani ukimfahamu sasa hivi huenda, kwa hali ya kibinadamu ukaweza kuingiwa na huzuni, na hata kuchukia, na mwisho wake utakosa radhi,,,vuta subira kwani kila jambop la heri huja kwa amani na kwa wakati muafaka...’huyo mama akasema na akawa kama anapotoea

‘Mama…mama yangu yupo wapi…’sasa kilichotamka ni mdomo, na nilipoweza kutamka hivyo, mara nikazindukana kutoka kwenye ile ndoto.

 Nilipogundua kuwa ilikuwa ndoto nikapapasa macho na kutizam huku na kule, nilijikuta nimezungukwa na baadhi ya watu akiwemo dakitari na wanaume wawili na mwanamke mmoja…akili ilianza kufanya kazi kuwa hawa watu sio mara ya kwanza kuwaona, nikajaribu kukumbuka wapi niliwaona lakini ikawa vigumu.

‘Hawa ndio jamaa zako niliokuambia, …inaonekana ulikuwa kwenye ndoto kali , na hatukutaka kukuamusha maana ilionekana ni ndoto njema, mwanzoni uliweweseka na kupiga ukelele, lakini baadaye ukaonyesha furaha, unaweza kutuambia ulikuwa unaota nini..?’ docta akauliza.

‘Mhh, hata sikumbuki…mmh, ngoja nikumbuke, nilikuwa naongea na mtu, na wanawake wawili, na wote wamepotoea, .’ nikasema

‘Hukuweza kuwakumbuka sura zao, na je unawafahamu ni akina nani..?’ akauliza dakitari.

‘Kwa kweli siwajui, ila mmoja anatisha, sitaki hata kukumbuka alikuwa anatoa harufu mbaya mdomoni na kila neno analoongea linanuka…aah, sijui ni kwanini…’nikasema

‘Na huyo mwingine…?’ akauliza docta

‘Mhh huyu wa mwisho alikuwa mwema sana, alinishika kichwani, nikajiona nimepona, aliniambia maneno matamu ambayo nilitamani kuyasikiliza wakati wote, ila aliniuliza swali moja kabla sijamjibu akawa mumeniamusha, ….huyu mwanamke amejifunika uso mzima, …sijui kwanini…’ nikawaangalia kama vile walikuwepo kwenye ndoto , na wao wakabakia kushangaa.

‘Hebu tuambie sasa unajisikiaje sasa, maana umesharuhusiwa, na hawa ndio jamaa zako….’akasema docta na wale watu wakanisogelea

‘Haya inuka tuondoke…maana umesharuhusiwa , docta kasema huhitajiki kuendelea kukaa hapa kwani hali yako inaendelea vyema, ni swala la kurudisha kumbukumbu tu ndilo limebakia…na tumekuja na kigari utakuwa unakitumia hadi hapo utakapoweza kutembea vyema’ akasema mwanaume mmojawapo na yule mwanamke alikuwa akikusanya vitu nilivyokuwa nikitumia, nikajiuliza ndio mke wangu nini, mbona ni mkarimu sana kwangu.

Nilikiangalia kile kigari nikawa najissikia vibaya, kwani kutokuweza kutembea vyema ndio tatizo jingine lililokuwa likinikera docta alisema hayo yanatokana na tatizo kwenye ubongo, kumbukumbu zikikaa vyema na hata kutembea kutarudi,…

‘Inaoenekana unawaza sana, hujakumbuka lolote..?’ aliyeuliza hivyo alikuwa ni yule dakitari wangu wa kila siku.

‘Kukumbuka, …hapana, nakumbuka ulisema mke wangu yupo, ndio yupi, nilitarajia angekuja kuniona leo, au…’ nikamgeukia yule mwanamke aliyekuwa akikusanya vitu , yeye hakuwa akituskiliza kwani alikuwa akihangaika kukusanya vitu, na alipogeuka akakuta ninamtizama, akashangaa na kutuangalia.

‘Vipi mbona wote mnanitizama mimi..’ akauliza huyo mwanamke

‘Mgonjwa anahisi wewe ni mkewe…’ akasema mwanaume mmoja

‘Hahaha kweli….unafikiria hivyo, …basi usiwe na wasiwasi mimi ni mke mwema sana, nikipata bahati ya kuwa na wewe hutapata shida, utapona kabisa..’ akasema huku anaweka vifaa kwenye kapu.

Na mimi nikawa nashangaa, kuwa mbona kanijibu kama vila utani, mimi nilizania kuwa yeye ndiye mke wangu halafu anajibu kinyume na matarajio yangu.

Tuliondoka hapo hospitalini hadi kwenye nyumba moja nzuri, hapo nikaambiwa kuwa patakuwa nyumbani kwangu,…nikashangaa kwa akuli hiyo

 `Patakuwa nyumbani kwangu, kwani kwangu ni wapi..nikajiuliza lakini sikutaka kuuliza sana, nikawa mara nyingi namwangalia yule mwanamke kwa kujiiba, na alikuwa mkarimu kwangu kupita kiasi, wakati mwingine ananikanda akisema kufanya vile kunasaidia kurudisha hisia za mwilini na kunipa mazoezi hasa ya miguu ili iweze kuwa na nguvu ya kutembea.

Hali yangu ilikuwa ikirudi kidogokidogo sana, mwili ukaanza kuingiwa na nguvu, na kuongezeka kidogo kidogo, maana nilikonda sana,…na nilionekana kama mzee, lakini sasa sura ikaanza kutakaka, lakini tatizo likawa ni  kumbukumbu na kuweza kutembea vyema, nikawa natumia kigari cha kukaa…..ilinikera sana hiyo hali.

Miezi ikapita mingi tu na mwaka sasa unaingia….sijaweza kukumbuka au kuweza kutembea bila kutumia kigari, san asana nikisimama natumia fimbo, na napaat shida na husihia kudondoka chini.

 Siku moja tulibakia mimi na huyo mwanamke, akawa nanifanyia `masaji’ na alipomaliza nilihisi  msisimuko mwilini, msisimuko ambao sikuwahi kuuhisi kabla, kwani mara nyingi mwili wangu ulikuwa kama una ganzi fulani, lakini kila mara alipokuwa akinishika huyu mwanamke, nilikuwa nahisi kuwa kweli ananishika tofauti na awali.

‘Nahisi msisimuko, leo umenipaka nini mwilini..?’ nikauliza, na yule mwanamke akacheka na kutabasamu, akasema ni mafuta yale, yale ya kawaida. Nilimtizama machoni mpaka akaona aibu, akaniuliza kuwa nawaza nini, nikamwambia nahisi kuwa yeye ni mke wangu,

Nilipoatamka hivyo akacheka sana ,hakusema kitu akamaliza kazi zake na baaadaye akaja akakaa karibu name, akaniuliza

‘Kwanini unahisi kuwa mimi ni mke wako..?’ akaniuliza

‘Maana docta aliniambia yupo mke wangu, na tangu nifike hapa sijamuona nakuona wewe, sasa kwanini nisikubali kuwa wewe ni mke wangu.

‘Unamfahamu vyema huyo mke wangu..?’ nikamuuliza.

‘Mhh,..si unajua tatizo langu, sina kumbukumbu za nyuma, sikumbuki kitu, simkumbuki hata nikimuona..hata sura siikumbuki…’nikasema

‘Mhh, sasa kwanini unifikirie kuwa mimi ni mkeo ….?’ Akaniuliza

‘Ni kama nilivyokuambia, wewe ndiye upo karibu nami, na kama kweli nina mke kwanini hajafika kuniona..zaidi yako wewe….au wewe unamfahamu mke wangu…?’nikasema na kumuuliza

‘Nitamjua wapi wako, wakati tangu tuanze kukuuguza , ukatoka hospitalini, tumekuleta hapa tumekaa wote, tumeulizia jamaa zako, lakini hakuna aliyejitokeza, kwa kweli hatujawahi kumuona ndugu yako yoyote aliyewahi kuja kukuona….! ..’akasema na hapo nikahisi mwili ukinyong’onyea, ina maana kumbe hawa sio ndugu zangu ni wasamaria wema tu.

‘Mhh, ina maana nyie sio ndugu zangu…?’ nikauliza
‘Kiukweli sisi sio ndugu zako, tunasubiri upone labda utatuambia ndugu zako ni nani, maana hatuna njia nyingine ya kuwajua, tumejitahdi tuwezavyo, tumefikia hatua tumekata tamaa..’ akasema yule mwanamke.

‘Wewe umeolewa…?’ nikamuuliza, na yule mwanamke akacheka sana.

‘Hahaha…swali gani hilo mpendwa, kama sijaolewa unataka kunioa wewe…utaniweza lakini?’ akaniuliza

‘Kwanini nisikuweze, niambia ukweli kama hujaolewa….’nikasema

‘Mimi ndio nimeolewa….sasa nikuambia ukweli’akasema na hapo mwili ukazidi kuisha nguvu sijui ni wivu sijui ni-nini

‘Umeolewa na nani…nilijua tu ni huyo mwanamue unayekuja naye mara kwa mara…na siku hizi simuoni tena, yupo wapi, ndiye mume wako…, lakini mbona sijasikia mkiitana mke wangu, mume wangu…sioni dalili kama hiyo..?’ nikauliza na yeye akanitizama usoni, akasema,

‘Ndio…si umateka nikuambie ukweli,  mimi- nimeolewa- na –wewe, umefurahi sasa… hebu kumbuka vyema , yaani wewe unamsahau hata mke wako, mmh wewe ni mume gani , ….’ akasema na kunitizama usoni, alinitizama hivyo kwa muda mpaka nikawa anjiuliza kwanini alikuwa akinitizama hivyo, nami nilihisi kitu fulani moyoni, nilimuona kama mwanamke mwema, mrembo , na nilitamani awe kweli ni mke wangu.

‘Mhh, sasa hapo unanichanganya,…mwanzoni ulisema wewe sio mke wangu,…sasa tena unasema wewe ni mke wangu, hebu niambie ukweli ili nisichanganyikiwe zaidi..’nikasema

‘Kwani wewe ulitakaje..hebu nambie ukweli wako, wewe ulitaka iwe vipi?’ akaniuliza

‘Mimi eeh, ..nataka hivi kama hujaolewa…eeh, unajua nikuambie ukweli wewe ni mwanamke mwema sana, wanaume wanatafuta mke kama wewe, wewe unaonekana ni mke mwema sana…na kama kweli sina mke …au mke wangu hanitaki,…maana naanza kuamini kuwa wewe kweli sio mke wangu, ..’nikatulia kidogo na yeye alipoona nimetulia akaniangalia akasema

‘Kwanini sasa uaamini hivyo, kuwa mimi sio mke wako…?’ akaniuliza

‘Mhh, kama wewe kweli ni mke wangu, mbona hujawahi kuja kulala na mimi..’nikasema na yeye akasimama, maana muda wote alikuwa kaka karibu yangu , alianza kukusanya vitu, akawa kimia kwa muda.

‘Kama kweli nina mke kwanini huyo mke wangu haji kuniona, unajua siamini,…siamini kama kweli nina mke…., sizani, mimi nahisi sina mke, eti hata wewe huwezi kuliona hilo….! Kusema ukweli natamani wewe uwe mke wangu…’ nikasema nay eye akageuka kuniangalia huku akitabasamu akasema.

‘Usijali, najua ukipona utabadili mawazo, …hiyo ni kawaida kwasababu nipo karibu nawe muda wote, kwahiyo unahisi kuwa mimi ni wa pekee sana, akili ikichanganya na kuwaona wanawake wengine, au akija mke wako, utagundua kuwa mimi si chochote mbele yao….’ Akasema huku ananimiminia gilasi ya juice ya matunda.

Nilipomaliza kunywa huyo mwanamke akaondoka, nikabakia peke yangu, nami niliendelea kutawaliwa na hisia ambazo sio za kawaida, hisia hizi zilinitawala akilini, na akili ikawa kama inawanga vile…na ingawaje yule mwanamke alishaondoka, lakini nilikuwa bado namuwaza yeye, nikawa natamani kumuita arudi lakini alishaondoka na akiondoka kurudi kwake hapo ni muda wa chakula cha mchana.

Siku zikaenda na hali ilikuwa ni ile ile…na siku moja nikiwa nimepumzika, nikitafakari dunia ilivyo, nilishajiona mwenye mapungufu mwili, maana kama siwezi kutembea vyema mpaka kutumia kigari, na kama siwezi kukumbuka vyema basi mimi ni nani..

Niliwaza sana na kitu kikanijia kichwani, kikiniambia mimi ni bora nife tu, nitafute sumu nijiue,…sijui kwanini wazo hilo lilinijia muda kaam huo, kujiua, kwanini nijiue, kwasababu sina faida, kwasababu mimi ni mtu wa kuhudumiwa tu, sina ndugu, sina thamani yoyote duniani

Wazo lilianza kama mzaha, nikajikuta natafuta njia za kujiua, kwa sumu au kwa kujinyonga…nikawa nawazia kila njia, akili sasa ikaganda kwenye hilo wazo, nikaenda mlangoni nikaufunga kwa ndani, sikutaka watu waje kunikatiza nilitaka nife kimia kimia…

Na wakati napanga njia rahisi ya kutenda tendo hilo, mara nikasikia hodi mlangoni…

Kwa muda huo nilikuwa nimekaa kwenye hicho kigari cha kukokotwa na kusukumwa kwa mikono, nilikuwa najaribu kuangalia njia ya kutenda hilo wazo lililonijia akilini, hodi ndio iliyolipoteza hilo wazo..nikageuka kuangalia mlangoni, sikutarajia hodi kwa muda huo..nikawa najiuliza ni nani huyo..

Sikupoteza muda nikasukuma magudumu ya kile kigari change cha kusukuma hadi mlangoni.. nilikuwa nimefunga mlango kwa ndani,…ili nikifanya nikaufungua

Aliyekuwa kasimama mlangoni alikuwa alikuwa ni mwanamke mmoja akiwa kashika begi dogo, na nyuma yake yupo docta. Nilipomuangalai yule mwanamke nikajikuta kama nashikwa na kitu kama kizunguzungu na mara sura nyingi zikawa zinakua kichwani, na sauti nyingi sana, ilikuwa kama mtu kawekwa kwenye chumba cha giza ambacho kinakuja mwanga wa sura za watu, halafu makelele mengi…

Hi ile ikanitesa sana na kichwa kikawa kinauma kweli, nikashika kichwa na kuhangaika  nikawa kama nachanganyikiwa, nikashika kichwa na kuanza kulalamika kichwa changu , kichwa changu, huku nahangaika sana , na docta akaja karibu yangu na kuniambia nimeze dawa ya maumivu ya kichwa, lakini sikumuuelewa. Na sikutaka kumsikiliza..kwani sauti yake ilikuwa kama kero fulani inapaa kama mwangi, nikawa nimeshikilia kichwa nalia…

Yule mwanamke aliyeshika begi mkononi akawa anashangaa na kunionea huruma, akanisogelea, na kumuomba docta asogee pembeni, akanitizama usoni, na nikaona machozi yakimtoka …akatikisa kichwa na mara akainua mkono wake, na kunishika kichwani.

Ajabu ilioje, nilihisi ubaridi ukiniingia mwilini, nilihisi kitu fulani kikisafaisha yale mahangaiko na makelele kwenye ubongo wangu , maumivu yote yakapotea…na mwili ukawa kama unaingiwa na ubaridi na hisia kutoka kichwani taratbu ukashuka hadi miguuni..

Ilikuwa ni maajabu, nikainua kichwa kumtizama yule mwanamke na mkono wake ukiwa bado kichwani mwangu…na mara kumbukumbu zikaanza kunijia kwa  mbali, nikawa nakumbuka kitu,…nikawa nayaona maisha yaliyopita kama vile mtu anajitizama kitu kwenye runinga….

NB: Mhh, kidole kinauma tusihie hapa kwa leo

WAZO LA LEO: Ugumu wa maisha ,mawazo,  matatizo, shida fedheha, vinaweza kumtuma mtu kufanya jambo ambalo hata hakulikusudia,…wengine hukimbilia kulewa, lakini je itasaidia,…. muhimu ukijiona upo kwenye hali hii mkumbuke mola wako, kumbuka kuwa kuna watu walipata matatizo zaidi yako kumbuke wale waliopo chini yako,…kuna watu wasio na uwezo kabisa,..lakini bado wanaishi, wana furaha, na wanafanya hayo kwa sababu gani,kwasababu wamemuweka mungu mbele wakijua kuwa mungu ndiye mjuzi wa hayo yote,kwake yeye yote yanawezekana.


Ni mimi: emu-three

No comments :