Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, May 21, 2015

NANI KAMA MAMA-80


Kwa hali niliyoiona kwa wale wafadhili wangu nikajua nikiendelea kukaa nao nitawazidshia mzigo, na isitoshe nimezembea na kufanya vibaya kwenye mitihani ya kidato cha nne, nikaona aibu na hata waliponisisitizia kuwa niendelee kukaa nao sikuweza kukubali kusema;

‘Hapana nitazidi kuwapa mzigo..mimi niacheni, nitajua cha kufanya….’ nilikataa na kuingia mitaani kutafuta maisha.

*******

Maisha ya mitaani ndio jadi yangu, sikuchagua kazi, lakini nilishajijua kuwa fani yangu ni ya ufundi, kwahiyo moja kwa moja nikaenda kwa jamaa, niliowafahamu nikawaomba nijifunze ufundi wa kutengeza magari, wakanikubalia, …

Kwasababu nilikuwa na kipaji cha ufundi, haikuchukua muda sana kujua mambo mengi na jamaa yangu akaniamini sana, akajitahidi kunifundisha kadri alivyoweza, hata hivyo sikubwetekea na fani hiyo peke yake, nikawa najichanganya kwenye kila shughuli ilimradi iniingizie kipato cha siku

Mwanzoni nilikuwa narudi kwa wale wafadhili wangu kulala, lakini baadaye nikaona nitafuta sehemu ya kuishi peke yangu ili niweze kupambana na maisha kivyangu, nikatafuta chumba na bahati nikapata chumba cha banda la uani kwa bei nafuu. Kutokana na ufundi magari nikajifunza kuendesha magari ya kila aina, nikaamua nipate leseni kabisa ya udreva.

Kwa vile kiingereza kilikuwa kinapanda, japokuwa nilifeli kidato cha nne, nikaona kwanini nisitafute kazi ya kuajiriwa, nikajaribu, ..unajua waajiri wengi wanababaika na lugha, basi nilipoitwa kwenye usahili,…oh, jamaa wakanikubali, nikapata kazi kwenye kampuni moja, ambayo nilifanya kazi hadi siku ile nilipoona jina langu kuwa mimi ni miongoni mwa waliopunguzwa kazi.

***

Hayo yote yalikuwa ni mawazo, na mawazo hayo yalikuwa kichwani, wakati natembea, sikujua kuwa nimefika kati kati ya barabara..muda huo ukumbuke nilikuwa natokea hospitalini, naelekea kuchukua majibu ya vipimo vyangu, akili ilikuwa sio yangu tena hapo…, kumbe nimeshafika kati kati ya mataa ya trafiki, sikujali kuangalia kuwa tumerhusiwa watembea kwa miguu, sijui, sijijui.

Kumbe wakati huo magari yalisharuhusiwa, muda wa watembea kwa miguu umepita mimi nikawa nimeshaingia barabarani, magari kutoka upande wa pili yanakuja kwa kasi, …mara ya pili inanitokea hivyo.

Nilishituka magari haya yapo mbele yangu,…nikatoka kwenye njozi ya kuwaza na kuiona hali halisi,…siunajua unapokuwa kati kati ya magari, magari yanakuja, unajikuta unababaika  nikaanza kubabaika, mara niende mbele au nirudi nyuma, na kabla sijafanya lolote nikajikuta naelea hewani na kabla sijatua chini nikajikuta nimedondokea kwenye kiyoo cha mbele cha gari..

Ilikuwa ni ajali mbali, maana watu waliokuwepo hapo, waliniambia walikuwa kimia kila mmoja akishikilia kichwa,akijua mimi ni maiti….gari lilinigonga na kunirusha juu nikaja kudondokea kwenye kiyoo, halafu nikaserereka na kudondokea mbele ya hilo gari-chini mbele ya lile gari lilonigonga,na bahati nzuri lile gari likafunga breki haraka, vinginevyo ningelikuwa chapati kwani magurudumu yalikuwa yanakuja kichwani mwangu.

‘Yallah,… mnaniua ili nisimsaidie mama yangu…..’ nikajikuta nasema maneno haya na sikukumbuka kilichofuata baadaye.

‘Docta huyu mtu …anaonekana kabisa anaumwa…na ajali hii imetokana na athari za huko kuumwa,…na huenda ni mmoja wa watu tunaowahitajia…, mnaona jinsi alivyo, nahisi anaweza kuwa ni miongoni mwa waathirika na huu ugonjwa tunaojaribu kupambana nao …’nilisikia sauti ya mtu akiongea kwa sauti yenye mawimbi,masikio yangu yalikuwa kama mtu aliyezama kwenye maji.

‘Mhh, kwanza tulikuwa tunahangaikia majereha na kuona kama hajavunjika mahali, tumechukua x-ray, na pia tutachukua vipimo vya damu, lakini cha muhimu kwa sasa ni vipimo vya x-ray…hilo jingine linafuatiliwa baadaye, …’sauti ikasema

‘Mhh, maana kwa uzoefu wangu …watu kama hawa, huwa wanakuwa kama wamechanganyikiwa hasa kama hawajapata ushauri nasaha,…wakipitia sehemu za ushauri nasaha wanabadilika, maana wengi hawajajua kuwa ugonjwa huu ni sawa na ugonjwa mwingine, muhimu ni masharti tu….’sauti ikasema

‘Ni kweli…’sauti nyingine ikasema

‘Na huyu mtu amekonda sana, ….mmh docta tumesikitika kuwa tumemgonga, lakini sio kusudio letu, unamuonaje docta, nahisi atakuwa na hilo tatizo au sio docta?…’ nikasikia sauti ile ya kwanza ikisema, na wakawa kimya, halafu nikasikia sautii nyingine, ikikohoa, ilikuwa karibu yangu sana

‘Mhh tusubiri vipimo tu….siwezi kusema lolote kwa sasa, sisi kazi yetu ni kushughulikia ajali, tuone kama kuna atahri kwenye mifupa nk..sasa ikifikia huko kwenye tiba nyingine mtaongea na docta muhusika….’sauti ikasema na kukawa na ukimia fulani, nikajaribu kufungua macho, lakini yalikuwa mazito sana, na baadaye kwa mbali nilimuona huyu aliyepo karibu nami akiwa na mavazi meupe, akinikagua kagua akafunua macho yangu, mimi nilikuwa nimeyafumba, sikutaka wajue kuwa nasikia wanachokiongea

Huyu aliyekuwa karibu yangu nikagunduaa kuwa ni dakitari.Kulikuwa na ukimia, na nikasikia wale watu wakiongea lakini kwa sauti ndogo, nahisi walikuwa wakiongea wenyewe wakati dakitari ananikagua na kuona nipoje.

Baadaye nikasikia watu wakisalimiana na maongezi yakaendelea

‘Aheri umekuja docta, maana huyu mtu akitoka hapa atakuwa mgonjwa wako..’sauti ikasema

‘Kwani vipi ana matatizo gani zaidi..?’ sauti ikauliza

‘Nahisi atakuwa na matatizo mengine nah ii ajali huenda imetokana na matatizo hayo,kama unavyomuona amekonda sana..na mwili wake ni mzaifu, sasa ngoja tumalize shughuli yetu, halafu,…’akakatisha

‘Ok, hamna shida, naweza kumkagua kidogo…’sauti ikauliza

‘Endelea tu docta, ….tupo pamoja…’sauti ikasema na kukapita muda, nilihis huyo docta mwingine akinikagua na kunishiak shika,akafunua mboni za macho yangu, nilijitahidi kuyafumba, ….baadaye akasema;

‘Nahisi keshazindukana , lakini hajakuwa sawa..’sauti ikasema

‘Ok, kwahiyo umemuonaje…?’ sauti ikauliza

‘Nahisi huyu mtu nimeshawahi kukutana naye, sijawa na uhakika kabisa..’akasema

‘Wapi..?’ sauti ikauliza

‘Mhh  nimeshamkumbuka huyu jamaa na hii itakuwa mara ya pili kukutaa naye, alikuja kule Lugalo, akiomba apimwe vipimo vyote kikiwemo kipimo cha kujua kuwa kaathirika na ugonjwa wa ukimwi au vipi, na tulimpima tukawambia arudi kesho yake, …hakutokea siku hiyo na tukajua kaamua kutokurudi.

‘Alikuja mwenyewe akitaka kupimwa ukimwi..?’ akaulizwa

‘Mhh ndio, nilikutana naye hospitali ya lugalo, huwa nakwenda kule mara kwa mara kutokana na kazi yangu hii,…na akaja akitaka kupimwa….’ huyu dakitari akawa anaongea.

‘Kuna kitu muelewe, kukonda sana sio lazima uwe ni muathirika, inawezekana kukawa an sababu nyingine, …na ili kujua hilo anahitajika kupitia vipimo vingi, …na vipimo peke yake ndivyo vinaweza kuthibitisha kuwa ana…eeh tatizo gani...’akasema docta mwingine.

‘Ndivyo nilivyowaambia hawa jamaa maana wao wanatokea kwenye shirika la wafadhili wa walioathirika….na bahati mbaya wakamgonga kwa bahati mbaya, akiwa katikati ya barabara….na kwa jinsi walivyomuona wakahisi ni miongoni mwa waathirika wa huo ugonjwa…’akasema

‘Unajua kule Lugalo nakwenda kwa matatizo kama haya ya kupima walioathirika na kutoa ushauri nasaha…na huyo jamaa nimemkumbuka alikuja nikakutana naye,… alipofika, alishakata tamaa, nikajaribu kuongea naye, lakini alikuwa yupo kama hayupo, nilihitajia muda wa kuongea naye zaidi….lakini muda niliokuwa nao pale ulishakwisha, nikamwambia akija kuchukua vipimo tutaongea naye zaidi….’akasema docta.

‘Kwahiyo vipimo vinasemaje….najua hutakiwi kutuambia lakini kwa ajili ya hawa watu ambao lengo lao ni kuwasaidia watu walioathirika…..ingewasaidia sana…’ sauti ikasema

‘Majibu yake yalishatoka, na hutaamini, hana tatizo la ukimwi kabisa ...., nilitaka akija nimuombe tumpime tena…na kwa vile yupo hapa tutampima tena tuhakikishe hilo, lakini tuna uhakika asilimia mia kuwa hajaathirika, na vipimo vingine halikadhalika havionyeshi  kuwa ana matatizo makubwa…ni matatizo madogo madogo tu ….’akasema yule dakiatari.

Mara ikasikika sauti ya kike,

‘Docta vipimo vya huyu mgonjwa hivi hapa,…..’ kukapita ukimia fulani halafu sauti ya docta ikasikika ikisema

‘Ok,….x-ray, inaonyesha kuwa hajavunjika mahali popote , hana matatizo makubwa zaidi ni hiyo michubuko tu…labda nesi, chukua vipimo vya damu na docta hapa atakuandikia ni nini zaidi kinahitajika, kwa upande wangu mimi nimemalizana naye….’akasema docta

‘Ok, nipe hiyo karatasi….’sauti ikasema na kukapita muda kidogo, halafu sauti nyingine ikauliza

‘Kwahiyo sasa docta sisi tunaweza kuondoka maana  sisi tuna safari, itakuwa haina haja kwetu tena kuendeela kusubiria, kwa sababau tulimgonga kwa bahati mbaya akiwa katikati ya barabara, sio kosa letu…sijui ana mawazo gani… na kama atakuwa muathirika, tunaomba tupate taarifa, tutajitahidi kurudi lakini hatuna uhakika ni lini….’ nikasikia sauti ya mtu mwingine ikisema

‘Mimi naona bado tunahitajika kumsaidia huyu mtu,  hata kama sio muathirika,  nahis atakuwa na tatizo jingine kubwa, kuna kitengo chetui kingine cha kusaidia watu wasiojiweza, kwahiyo tutalifikisha kwa wenzetu…’sauti ikasema

‘Mimi nitakuja kulishughulikia,….mimi nipo kwenye kitengo hicho,’sauti nyingine ikasema

‘Mhh, lakini hatuwezi kusubiria, tunakwenda na muda, tutakuja kurudi, au wewe unasemaje, maana ni lazima tuongezane na wewe…’sauti nyingine ikasema

‘Mimi nahisi huyu mtu ana matatizo ambayo yamemzonga, huenda ana ugonjwa haujagundulikana au kuna jambo…’ sauti ikasema na kukawa na ukimia fulani, muda huo nilijaribu kufungua macho tena

Docta ambaye alikuwa karibu nami nikamuona akinishika mkono, na nilihisi kuwa wamehisi kuwa nimezindukana. Macho sasa yaliweza kufunguka, yalikuwa yanaona vyema, na niliweza kuwaona wote waliokuwepo mle ndani. Kulikuwa na madakitari wawili, na watu wengine ….kama waaa-nne hivi, mwanamke mmoja.

 Mmmoja wa wale madakitari akanisogelea zaidi na huku akiangalia mashine iliyopo ukutani ambayo inaonyesha mienendo ya mwilini akatikisa kichwa, na kuwaambia wale watu;

‘Huyu mgonjwa keshazindukana, ila bado akili haijakaa sawa. ..’akasema huyo docta

Akanisogelea na kunifunua mboni za macho, akashangaa namwangalia.

‘Vipi upo safi, …’ akaniliuliza

‘Nipo safi kwaaa-ni ooh, kichwa,..ooh, kwani vipi,nimefanya nini….docta, kwani nina nini, na hapa ni-ni-po wapi…oooh’ nikakumbuka kitu kichwani, nilikumbuka neno moja nikajikuta nikisema ;

`Mama yangu…docta mama anahitaji msaada wangu, na…aanhitajika kupelekwa India.’nikasema


 ‘Mama yako…yupi huyo…, hebu subiri kwanza , bado unahitajika kupumzika…wewe tulia kwanza…’ akasema docta.

‘Docta..kwani nimefanyaje..?’ nikauliza

‘Wewe umesema mama yako, …anahitajia msaada ni mama gani huyo na yupo wapi?’ akaniuliza

‘Mama…..mimi nimesema mama….mmh, docta mbona sikumbuki kitu….’nikasema nikijaribu kukumbuka

‘Basi tulia usiwe na wasiwasi….’docta akasema na akasogea akawa anaongea na mwenzake kwa sauti nisiyoisikia vyema.

Nikabakia najiuliza kwanini nimesema mama, anahitajia msaada wangu ni mama gani huyo inawezekana ni mama yangu, kwani mama yangu ni nani….’nikawa najiuliza maswali mengi lakini sikuweza kukumbuka vyema.

‘Ina maana kumbukumbu zilipotea..?’ nikamuuliza rafiki yangu

‘Kwa muda huo sikuwa najua kitu, kuwa labda nimepotewa na kumbukumbu, na sikuwa najifahamu…’akasema, wakati wale madocta wanaongea wale jamaa wengine mmoja akanisogelea na kusema name;

 ‘Sikiliza ndugu, sisi ndio tuliokugonga kwa bahati mbaya…samahani sana, na docta kasema hujaumia ni mshituko tu uliokupata, lakini tunaona kuwa huenda una matatizo mengine ambayo tungependa kuyajua ili kama inawezekana tukakusaidia  kwani sisi p tunashughulika na kampuni ya kusaidia wenye matatizo mbali mbali, hasa waathirika, na …’ akasita kuongea.

‘Kwani mimi nimeathirika…?’ nikauliza

‘Hapana..hujaathirika, ..ila tunakuambia tu kuwa sisi ni shirika binafasi linashughulikia matatizo mbali mbali, mojawapo ni kuwasaidia wale walioathirika, wewe kwa mujibu wa dakitari, sio muathirika, lakini kutokana na hali uliyo nayo, tunahisi una tatizo kubwa, unaweza kutuambia ni tatizo gani..?’ wakaniuliza

‘Tatizo…mmh mimi sijui kama nina tatizo, kwani ….mimi ni nani..ooh, samahani …docta kwani nimefanyaje,….kwanini nipo hivi?’ nikawa namuuliza docta na wale watu wakawa wananiangalia kwa mashaka.

‘Lakini wewe umesema sasa hivi kuwa mama yako anahitajia msaada wako, mama yako yupo wapi na ana matatizo gani..?’ wakaniuliza

‘Nani, mama yangu, mama yangu ndio nani…yupo wapi, kwani ….mama anahitajia msaada wangu nimesema hivyo…docta kwani mama yangu yupo wapi,..?’ nikauliza nikijaribu kukumbuka.

‘Usihangaike, wewe tulizana tu, ni kawaida ..’akasema docta na wale jamaa mmojawapo aaknisogelea na kuniambia

‘Hebu tuambie mama yako ana tatizo gani la kuhitajika hadi apelekwe India…?’
akasema mwanaume mmoja na kabla sijamwambia lolote, mara simu ya huyo mtu ikaita, ikabidi awaangalie wenzake halafu akaniomba msamaha na kuipokea ile simu.

‘Docta niambie naona nina bahati kubwa kupigiwa simu na mtu mashuhuri kama wewe, …ndio , ndio kazi yetu docta, pesa zipo bwana, lakini tunahitajia zaidi kutoka kwa wadau, wasamaria mwema wenye kujitolea,… hapa nchini wapo wafadhili wengi wamechanga,..lakini bado, unajua wengi hawajatufahamu lengo letu ni nini….’akatulia

‘Na unajua wapo watu wanahitaji kusaidia wenzao lakini nani wa kusaidia ndio tatizo, ndio maana sisi tukaanzisha hili shirika, kuwa mtu kati, wanaotaka kusaidia na wale wanaotaka kusaidiwa,….ndio, uaminifu, na kuaminiana ndio lengo letu, sisi ni waumini,…kwahiyo hatuwezi kuwatapeli watu….’akasema

‘Mpaka sasa hatujajitangaza zaidi ya kupita mahospitalini,…tutakuja kufanya hivyo, ila kwa sasa tuliona tuhakikishe tumejipanga vyema, kwa maana tukiamua kujitangaza kwa sasa wanaweza wakaja hata wale wasiostahili hii misaada…binadamu sio watu wema..’akasema akiongea na simu

‘Sasa hebu niambie una watu wangapi hapo hospitalini kwako, wanaohitaji misaada,…?’ akauliza

‘Mhh, kuna wanaohitajika kwenda India kwa upasuaji, wapo wangapi…wanaume wanne, na mwanamke mmoja, ….mmh, kwanini wanawake…ni wachache ina maana kweli hakuna wanawake wanahitika kwenda huko..?’ akauliza
‘Ok, basi mimi nitakuja hapo kumuona huyo mwanamke… …yupoje…?, ok…basi tukitoka hapa tunakuja huko.., na hao wanaume wapo hapo hapo au kwingine,…ok, …haina tatizo ngoja kuna tatizo naliweka sawa hapa, nipo na wenzangu wa kitengo cha kusaidia walioathirika kuna sehemu tunakwenda, mimi naweza kuachana nao, nikaja huko..ok tunakuja.. ok, bye’ akakata simu.

 Akawaangalia wenzake na kuonyesha saa mkononi …akanisogelea na kuniambia kuwa wamepata dharura, lakini wakirudi watakuja kuona kama wanaweza kusaidia hilo tatizo la mama yangu …kwani ni  moja ya kazi yake …nisiwe na wasiwasi watanisaidia…wapo kwa ajili ya kusaidia watu kama hawo wasio na uwezo wa matibabu, nisitie shaka.

‘Mama, nina mama ..mbona sikumbuki, anahitajika kwenda India…mmmh, mbona sikumbuki…’nikawa nababaika sikumbuki kitu.

‘Wewe usijali, tutarudi , huenda tukirudi utakumbuka vyema…’wakasema.

‘Muda gani mtarudi maana hapa sijui nini kinaendelea….’nikasema nikijaribu kukumbuka lakini akili ilikuwa butu haikumbuki kitu, ni kama akili isiyo na jambo, umetoka usingizini, hukumbuki hata kuota na hujui upo wapi na kitu gani kimetokea.

‘Docta kwani mimi nina tatizo gani,na kwanini nimefungwa hivi…docta nipo wapi…’nikawa naongea ovyo.

 Na docta akahisi kitu na akaongeza dawa fulani kwenye yale maji ya drip niliyotundukiwa, na …haikuchukua muda nikajikuta kwenye usingizi mzito!

Hali yangu kiafya ikabadilika ghafla, nikawa mgonjwa kwelikweli, na kumbukumbu zikapotea kabisa…na nikawa na hali mbaya, joto likawa kali,,na mara kwa mara nikawa napoteza fahamu,…, nikizinduka, hali ni ile, ile..joto linakuwa kali, mara mapigo ya moyo yanakuwa na kasi ya ajabu…, hali ikawa sio shwari, wakagundua kuwa nina upungufu wa damu, shinikizo la damu, hata sukari…nikajua sasa siku za kuishi duniani zimekwisha.

Katika hali hii ya kuumwa, kupoteza kumbukumbu, kwahiyo sikujua nipo wapi, ila nilisahjua kuwa nimepatwa na ajali, ilikuwaje sikumbuki, nimetokea wapi sikumbuki, na mara kwa mara wakawa wananiuliza kuhusu mama, wanasema huwa nikilala naongea kuwa nina mama, anahitajika kwenda India, anahitajia misaada ya watu, na wanasema nongea hayo nikiwa kwenye ndoto.

Hali ilizidi kuwa mbaya , wakaona nihamishiwe kwenye hospitali kubwa zaidi

Nilihamishiwa hospitali ya Muhimbili, na huko nikakutana na wataalamu ambao walinisaidia sana, mpaka hali ikaanza kurejea vyema, lakini kumbukumbu ikawa ni tatizo kwangu, wakati mwingine naweza kuongea na mtu akirudi namuuliza kuwa yeye ni nani na tuliongea nini…

‘Tatizo hili ni la muda tu, litaisha , kwasababu ubongo wako umepitia mambo mengi, na ule mshituko wa kugongwa na gari ulileta athari ambayo haikugundulika mapema, una bahati sana, kwani athari ile haikugusa ubongo,…lakini hali inatengamaa usijali..’ docta akaniambia, nami sikuwa na wasiwasi  sana, niwe na wasiwasi na kitu gani…sielewi, na kwanini nililetwa pale sijui kabisa!

Na kweli siku zilivyozidi kwenda ndivyo hali ilivyokuwa na matumaini, nikiwa naona mabadiliko , na nilianza kukumbuka kumbuka kidogo kidogo, na kumbukumbu nyingi zilikuwa za muda mfupi, kumbukumbu za zamani nilikuwa sizikumbuki kabisa. Mpaka nikawa naona kero, mtu hujui umetoka wapi wewe ni nani

‘Hili tatizo ni la muda, litakwisha usitarajie kuisha kwa haraka, lakini sio tatizo la kukuumiza kichwa, na usijichoshe kwa kuwaza sana….’akaniambia docta

‘Docta unajua nashangaa, kwanini nisikumbuke, hivi ina maana sina ndugu, mbona….ooh,..na huyo mama mnayemtaja mbona haji kuniona au..’nikawa nashika kichwa kujaribu kukumbuka.

‘Ndugu zako wapo usijali, ….na mama wewe ndiye unayemtaja mara kwa mara kwenye njozi inaonekana kweli utakuwa na mama anayehitajia msaada, tumejaribu kuwasiliana na hospitali mbali mbali lakin hatujaweza kugundua mama kama huyo…’akasema docta na kuniacha nikiwa najaribu kuwaza ni kitu gani kilitokea,….na mimi nimetokea wapi, na huyo mama ni nani , na atakuwa wapi…sikuweza kukumbuka.

Mwezi ukapita, nikaonekana sijambo jambo…ila kumbukumbu bado zilikuwa hazijakaa sawa, na madakitari wakaona haina haja ya kuendelea kulazwa, ila natakiwa niwe nafika hapo hospitalini kila baada ya wiki moja, …

‘Sasa tunaoan tukuruhusu uende ukatulie nyumbani kwako, na utakuwa ukirudi hapa kila baada ya wiki,..na tutaona huko mbele….kiafya huna tatizo sana, ila kumbukumbu bado hazijaa sawa, zitarudi tu usijali..’akasema docta

‘Nyumbani kwangu  ni wapi? ‘nikauliza na docta akajifanya kama ananishangaa…

‘Ndugu yangu ina maana hujui kwako ni wapi…!’ Akaniangalia kwa makini halafu akatabasamu ni kuniambia;

‘Kama hujui kwako ni wapi inabidi ukalale polisi..’akasema kwa utani

‘Kweli docta mimi sijui kwangu ni wapi, niende wapi sasa..’nikasema

‘Mhh, usijali, kuna ndugu zako kila siku wanakuja kukuangalia, naona siku mbili hizi sijawaona, …ngoja wakija nitaongea nao, usijali, utapelekwa kwako..’akasema

‘Ndugu zangu, wale wanaosaidia watu au ni nani….ni wale waliofika siku ile..hao nawakumbuka lakini wao sio ndugu zangu, walisema wao kazi yao ni kusaidia watu, nakumbuka hilo sana..docta mimi sikumbuki kuwa na ndugu kama wale..’nikasema

‘Mhh, yah, utakumbuka tu, na muhimu akija mke wako nataka  nikae naye nimpe maelekezo jinsi gani ya kuishi na wewe, hadi hapo hali yako itakaporejea kama kawaida..’ akasema docta.

‘Mke wangu!? Ni nani huyo?…mke wangu alishawahi kuja hapa…?, mbona simkumbuki…hivi mimi nina mke kweli….?!’ nikawa nashangaa, kwani sikuwa na kumbukumbu zozote za kuwa na mke.

‘Atakuwepo tu, sidhani kuwa huna mke,…huwa anafika na hao jamaa zako mara kwa mara,  ngoja jamaa zako wakija tutaongea nao, wewe tulia hapo kitandani, usiwe na wasiwasi…’akasema docta

‘Mke wangu….!?’ Nikabakia nikijiuliza

NB: Tatizo lileee kama la mama yake mnakumbuka mama yake alipoteza kumbukumbu, kumbe ni kizalia, sasa mama yake imekuwaje..Jamani leo nimeona nitoe sehemu hiyo ndogo, maana akili haijatulia kidogo, tukutane sehemu ijayo tuone jamaa atakumbuka vipi na huyo mke wake ni nani



WAZO LA LEO: Tuheshimu na kujali rasilimali watu kutokana na nguvu kazi yao, wewe kama muajiri, wewe kama una bahati ya kuwa na watendaji wako unaowalipa,. Hakikisha unajali sana jasho lao, usitumie ujanja kuwanyonya, usiwanyanyapae, au kuwanyanyasa , maana wanatoa jasho kwa ajili ya kipato chako, hata kama wapo vipi, ilimradi ni watu wako na una dhamana nao, ni muhimu sana kuweka mbele `utu’…kuliko ‘masilahi’ utu utalinda mali yako na familia yako, utu utakuongezea baraka na huo utu, utakuongezea kipato. 

Ni mimi: emu-three

No comments :