Docta aliponiambia kuwa mama yangu ana
uvimbe ndani ya ubongo, uvimbe ambao nilijua kabisa umetokana na madhila ya
watu, mama kupigwa kichwani na hata pale aliposukumwa na mke wangu akadondokea
kichwa, vinaweza kuwa ni sababu ya uvimbe huo lakini sikuwa na ushahidi wa
kumnyoshea mtu kidole.
‘Docta Sasa tutafanyaje kuhusu huo
uvimbe..?’ nikamuuliza dakitari nikitaka kujua kuwa huenda kuna dawa inayoweza
kumtibia, lakini jibu nilipopewa lilinikatisha tamaa,
‘Uvimbe huo huondolewa kwa kufanyiwa upasuaji,
na tatizo ni kuwa upasuaji kama huo, hauwezekani hapa kwetu,..’akasema docta
akiangalia faili la mama kama vile anasoma kitu ili anielezee nilipoona yupo
kimia nikamuuliza.
‘Una maana gani, …sasa kwahiyo docta mama atatibiwaje…?’
nikauliza
‘Kama nilivyokuambia uvimbe kama huo
unahitajika kufanyiwa upasuaji, ni bahati mbaya kuwa sisi hapa nchini hatuna
upasuaji wa namna hiyo…’akasema
‘Upasuaji huo unafanyiwa wapi….?’ Nikauliza
‘Upasuaji huo unafanyiwa India..lakini
kwanza hebu subiria vipimo vingine maana bado kuna vipimo hapa havijakamilika,
vikikamilika..utakuja kuambiwa kila kitu …’akasema na kuanza kuondoka, nilitaka
kumsimamisha lakini hata nikimsimamisha nitamuambia nini….
Basi siku ile nikabakiwa kuwaza na
kuwazua, nikalia na kulia, …lakini yote hiyo haikusaidia kitu..
Tuendelee na kisa chetu
*********
‘Mnakumbuka pale nilipowahdithia, kuwa mimi na mama tulikwenda
kuomba kwenye nyumba moja kwa mama mmoja ambaye alikuwa na asili ya mtu kutoka
India,…na akaingia ndani, baadaye kukaja gari la landrover ndani yake kulikuwa
na askari mgambo na polisi..?’ akatuuliza rafiki yangu
‘Ndio tunakumbuka, kwani ilikuwaje…?’ nikauliza
‘Tukio hilo siku hiyo ndio tukio lililonitenganisha mimi na mama yangu…’akasema
‘Mhh, ina maana huyo mama mwenye asili ya kihindi, aliwapigia simu polisi…?’ nikauliza
‘Ndio…kwasababu taarifa zilishasambazwa kuwa kuna mama mmoja
jambazi, gaidi, anatafutwa na polisi, mama huyo huwa anajifunika uso wake, yeyote atakayemuona atoe taarifa polisi, kwani mama huyo ni hatari…’akasema
‘Mhh..yaani ilifikia hapo, mkaitwa magaidi….?’ Akauliza jamaa
mwingine.
‘Kuna usemi wa wenzetu kuwa ukitaka kumuua mbwa, cha kwanza mchukia yule
mbwa, halafu umuite majina mabaya…na ndivyo ilivyotokea kwetu, hatukutakiwa
kabisa maeneo hayo, tulionekana ni uchafu…kwahiyo ili zoezi hilo likamlike,
tukapakaziwa ubaya, kuwa sisi ni wezi, sisi ni mjambazi, sisi ni magaidi…’akasema
‘Mhh, kweli dunia haina wema..’akasema mmojawapo
‘Ndivyo ilivyo…mnyonge hata siku moja hana haki, hasa
anaposhindana na mwenye uwezo, mwenye mali….wewe una nini, utafanya nini mwenzako ana pesa ataajiri wanasheria wa kumtetea, wewe atakutetea nani…na ndivyo
ilivyotokea kwetu, ...'akatulia
'Kuna raia walilalamika kuwa wanamiliki maeneo kuzunguka eneo hilo toka mababu zao, lakini hawakusikilizwa, kwa vile hawakuwa na hati miliki, ..muwekazaji akafuata sheria zote, akapata haki miliki...utashindana na yeye.....na sisi tukatumbukizwa kwenye mkumbo, kwani tulikuwa tukitumia eneo hilo kujihifadhia...
'Basi tukio hilo ndilo lililonitenganisha mimi na mama yangu , linanikumbusha mbali na ni tukio nisiloweza kulisahau, na nikiwa hapo hospitalini nikakumbuka
maneno ya mama akiniambia….
‘Mwanangu hapa naona hakuna
usalama, na kama kutatokea fujo kimbia moja kwa moja hadi mfichoni kwetu
usijali litakalo tokea….mungu atakulinda…’
Nililikumbuka sana tukio hilo siku hiyo wakati nipo nasubiria
vipimo vya mama ambavyo niliambiwa havijakamilika,…nililikumbuka kwani ni tukio
lililonifanya nitengane na mama yangu, na sasa tena naambiwa mama yangu ili
apone anatakiwa apelekwe India,…sina pesa, sina chochote,hali yatu ni dhalili…nani
atatusaidia..ni tukio ambalo sitaweza kulisahau…
‘Kwani ilikuwaje walipofika hao mgambo…?’ nikamuuliza
Siku ile walipofika hao mgambo, utafikiri walimpania mama, kwani
kwa pamoja walimkimbilia mama, wakaanza kumpiga, wakati huo mimi nimekamatwa,
askari mmoja alikuwa kanishika mkono kuhakikisha sitoroki. Wao walishaniona
kuwa eti mimi ni tishio, ni mkorofi, ni mtoto wa nyoka…yaani kama alivyo mama,
basi hata mimi mbaya naweza kuleta
maangamizi.
‘Nyie ndio wakaidi eeh, mnadiriki kuwaumiza walinzi, …..mumewaumiza
askari mgambo wawili….mnajifanya magaidi eeh….’akasema askari huku akiangalia
jinsi gani mgambo wale wanavumpiga mama..kipigo cha hasira kipigo cha kulipiza
kisasi,…mama hakuwa na la kufanya alitulia kimia huku virungu mabuti yakitua
mwili mwake, bila kujali wanapiga wapi, na mimi nilibakia kulia tu nikiita
‘Mama..mama..mnamuua mama yangu…’lakini kilio changu hakikuwa na
maana kwao.
‘Lazimz iwe fundisho kwenu…mnavuruga amani,..hamtaki kutii sheria…mama
yako atakuwa fundisho kwa wengine…’akasema huyo askari
‘Mama…msimuue mama yangu…jamani mama mnamuua mama yangu…’nikawa
nalia na huyo askari akawa anatabasamu tu.
‘Muache afe kwani ana faida gani,…san asana ni kutuletea shida,
sisi tunahitajia mendeleo, wawekezaji wanataka kujenga kiwanda hapa, kitakacho
waajiri watu wengi, nyie mnaleta ukaidi mnawaumiza watu wa usalama….hamuoni
kuwa nyie ni wakorofi…’akasema
‘Sisi hatujafanya hivyo….sisi ni omba omba tu afande..’nikasema
‘Omba omba…kwani muombe, kwani nyie hamuna mikono ya kufanyia kazi,
mama yako ana mapungufu gani, kwanini asiende kulima,….’akasema
‘Mama haan shamba, ..shamba kanyang’anywa..’nikasema
‘Acha uwongo…funga domo lako…’akasema na kuminya mkono mpaka
nikawa nasikia maumivu.
Jinsi walivyokuwa wakimpiga mama bila huruma, moyoni nilijawa na
chuki , nikajisemea mwenyewe hivi kwanini binadamu tunakuwa hatuoneani huruma,
watu wazima na akili zao hawaoni kuwa kitendo kama kile kinamuumiza binadamu
mwenzao, na hawajui kwanini mama anaishi mazingira kama yale, hawajui na
hawataki kujua, sana sana tunaonekana ni uchafu…nikakumbuka yanatokea huko dunia
nyingine ambapo mtoto anashuhudia mateso hayo kwa wazazi wake, unafikiri mtoto
kama huyo akiwa mkubwa atafanay nini…ni chuki zisizoisha na matokea yake mtoto
anabadilika na kuwa gaidi wa ukweli.
Wakati mgambo wamehakikisha kuwa maa hajiwezi tena, mara likatokea
lori jingine likiwa limebeba watu, nikagundua ni wale ombe omba, na watoto
wasio na wazazi, wakiwa wamebebwa kwenye hilo lori, na nikajua huo ni mpango
maalumu wa kuhakikisha sote tunaondolewa eneo hilo ili muwekezaji aweze kuweka
vitega uchumi vyake, wazawa tukawa hatuna haki,..na hata kama tungekuwa na
haki, sis tungewekeza nini, san asana tulionekana ni udhia wa mji…
Lile lori lilipofika mama akabebwa kama gunia na kutupiwa ndani ya
hilo lori na baadaye kuondoka likiongozwa na landrove mbili za polisi moja
mbele na nyingine nyuma,…
Hapo sikujua wanapeleka wapi mama, mimi nikiwa nimeshikwa mkono na
mgambo mmoja aliyebakia nyuma, yeye hakuondoka na wenzake, labda alibakizwa kwa
ajili yangu. Baadaye ikakaja gari aina ya pick-up, yule mgambo akaniongoza kwenye
hilo gari akanipandisha nyuma, na ndani yake nikakutana na watoto kama mimi na
wengi wao nilikuwa nikiwajua. Wote walikuwa watoto wa mitaani na omba omba kama
mimi!
‘Sasa tunapelekwa wapi…’ mmoja wa watoto akauliza, na yule mgambo
akasikia na kutuangalia kwa jicho baya. Mimi nilikuwa nawaza wapi wamempeleka
mama yangu, na hali kama ile, maana alivyopigwa ni lazima atakuwa na hali mbaya.
Nilililia sana kisirisiri, na kila mgambo akiniangalia nilijifanya najikuna
machoni, niliogopa nikilia sana atanipa adhabu kwani sura yake naikumbuka
vyema, ni yule yule mgambo niliyempiga kigogo kichwani siku ile …, wakati
akimkanyaga mama yangu.
Tulisafirishwa hadi mbali kidogo na mji, gari lilikatisha katikati
ya mji na kutokea sehemu nyingine nje ya mji, na kuingia eneo la msitu halafu
tukatokea eneo lenye miti mingi, halafu kwa mbele yetu tukaona jengo kubwa kama
shule, na majengo mengine madogo madogo yaliyokaribu yake, na eneo la pembeni
kidogo kulikuwa na uwanja wa michezo mbalimbali.
‘Hapo mnapopaona mbele yenu kutakuwa ndio nyumbani kwenu, kuanzia
leo, na ole wenu mmoja atoroke ,…narudia tena kusema ole wenu..mtu ajifanya
anajua kutoroka, atakuja kupambana na kifo…’akasema huyo askari.
‘Unaona huu msitu….kuna wanyama waakli , kuna simba, chui…mkijifanya
wajuaji kutoroka mtaenda kuliwa na wanyama wakali…, cha muhimu ni kukaa
shuleni, kwani hapa ni shule, ni kambi itakayokulea ili baadaye uwe na maisha
mazuri kuliko kuzurura mitaani….’ Akasema jamaa mmoja, ambaye tulikuja kujua
kuwa ndiye mkuu wa kambi.
Tulifika hapo kambini , na kuwakuta watoto wengine wakiwa
wanafanya kazi mbalimbali, wengine wananyweshea bustani, wengine wanaweka
mbolea, ..na kazi nyingine nyingine, na wote wamevaa sare moja, nilivutiwa
kidogo na manthari hiyo, …lakini kila mara mawazo yangu yalikuwa yakimuwaza
mama yangu.
Ilipofika usiku tulionyeshwa sehemu ya kulala, na usiku kulikuwa
na vibweka vyake maana wapo wale waliotangulia ,wenyeji wa siku nyingi, wao
walikuwa watukutu, sisi wageni tulianza kuteswa, eti tunakaribishwa kambini, tulilazimishwa
kuimba, kuruka kichura…
Ilikuwa ni kero nyingine, sikujua kuwa hata sie watoto tuna roho
mbaya, kwani walichotufanyia hakikustahiki, lakini wao walijiona wanajua zaidi,…vitendo
hivyo viliendelea hadi saa nne, …na hapo ghafla, tukaona wale wote waliokuwa
wakitutesa wakirukia vitanda mwao na kujifunika gubigubi , na kuifanya
wamelala…
Mara akaingia mbaba mmoja na kirungu, huyu alikuwa mmoja wa
walezi, au mwalimu wa zamu wa kambi , akawa anazunguka huku na kule bila kusema
neno, alifanya hivyo kwa muda na sisi wageni tulikuwa tumekaa sakafuni,
hatukujua tufanye nini…
‘Mlikuwa mnafanya nini, siliwaambia kuwa kila mtu kitandani kwake
hapa mnafanya nini..?’ akauliza yule mlezi
‘Walikuwa wanatutesa, wanatuimbisha, wanaturusha vichura…na…’
akasema mmmoja wetu
‘Eti nini ni nani anafanya hivyo, silishawakataza hii tabia,
…kesho mutanionyesha ni nani anayewanyanyasa wenzake…tabia hii siitaki kabisa,
huyu aliyefanya hivyo namtaka kesho ofisini. Wewe na wewe kesho utanitajia ni
nani, … atakiona cha mtema kuni…’alikagua vitanda na kuita majina , halafu taa
ikazimwa akaondoka.
Alivyoondoka wale watoto watukutu wakainuka, kama vile hawajali,
wakawa wanatupitia vitandani na maji, wanatumwagia na huku wakitoa onyo kuwa
atakayemtaja yoyote kati yao kesho kuwa alikuwa akiwanyanyasa atatoa macho ya
yoyote atakayefungua domo lake.
‘Ulizeni wenzenu hapa, mimi ndio nani, nitawatoa macho wote mbakie
vipofu, na nitawafanyizia kitu mbaya ambacho hamtakisaahu maishani mwenu…oooh,
…’ akatamba mmojawapo…na, baadaye tukalala.
Utukutu huu haukuishia hapa vijana hawa walikuwa wanatumwagia maji
kitandani ili tuonekane tumekojoa vitandani, na asubuhi yake tunaishia
kuadhibiwa kwa kudeki na kufua, na adhabu nyingine, …kwakweli ikawa ni shida
juu ya shida na hali kama hii ikawa inanikumbusha sana mama yangu, nikiwa peke
yangu ninalia sana, lakini hata nilie ingesaidia nini. Tuliogopa kabisa
kuwashitaki hawa watoto watukutu, kwani walikuwa wakubwa na inavyoonekana
walikuwa wakiogopwa na watoto wengine!
Siku zikaenda, miezi miaka, umri ukawa mkubwa, lakini siku moja
wakaja wale mgambo na askari polisi, walipokuja nikaitwa, nikijua kuwa labda
kuna taarifa nzuri kuwa mama atakuja kunitembelea au kunichukua, lakini maswali
niliyoulizwa yalinikatisha tamaa;
‘Wewe mtoto mama yako mara nyingi anaishi wapi na jamaa zake ni
nani?’ nikaulizwa
‘Mimi sijui jamaa za mama , mama hana jamaa zake … sisi hatukuwa
na nyumba, kwani mama yupo wapi…?’ nikauliza
‘Mama yako siku anapelekwa mahakamani kwa kumjeruhi askari akiwa
kazini,… aliruka kwenye gari, na sehemu aliyoruka ni karibu na daraja, akazaam
majini, ..tulimtafuta bila mafanikio…’akasema
‘Mama yangu…ina maana mumemuua mama yangu..’nikalia
‘Mama yako ni mkaidi,a liruka mwenyewe..hakuna aliyemuua, tunahisi
atakuwa katokea upande mwingine wa mto…, ndio maana tulikuwa tunakuulizia kama
unajua wapi mama yako huwa anapenda kwenda au kama kuna jamaa au ndugu
utuambie, ili tuwe na uhakika kuwa yupo salama au …?’ akasema yule mmoja wa
askari.
‘Mimi sijui jamaaa yoyote..’nikasema
‘Na ule mto ni balaa umejaa mamba, viboko, sasa yeye alijifanya
mjuaji akaruka, akijua katoroka mkono wa sheria kumbe anakwenda kuliwa na
mamba…sasa wewe hapa utulie kabisa….’akasema askari.
‘Namataka mama yangu..’nikasema kwa hasira.
‘Mama yako, kwa ukadi wake atakuwa kaliwa na mamba, na wewe
ukijifamnya mkaidi utaliwa na simba, ole wako ujaribu kutoroka, ..humo msituni
kuna simab, chui, mamba…’akasema askari mmoja.
‘Sisi bado tunamtafuta mama yako, maana mama yakoa naonekana ni
gaidi, kwanza tuambe kwanini anajifunika uso wake,..huoni kuwa ni mkosaji, alifanya
makosa sasa anaficha sura yake….’akasema na mimi nikawa kimia moyoni nikiwa
hasira
‘Sasa, kama kweli unajua wapi jamaa zako wanaishi na hutaki
kutaja, tutakuja kukuchukua ukafungwe gerezani, unasikia…?’ akasema yule askari
mwingine hata bila huruma.
Alipofika kusema hivyo mimi sijua kabisa nini kilinipata, nilishikwa
na kitu kama kwikwi, mfulululizo, huku natingishwa mapaka nakosa pumzi. Ikabidi
nipelekwe kwa dakitari, lakini hali yangu ikawa mbaya, ikabidi nisafirishwe
kupelekwa mjini. Na nilipofikishwa hospitali nikalazwa kwa siku tatu.
Nikiwa hapo nilikiwa kila mara nikiwaza sana, na usiku naota ndoto
nikiwa na mama, tukipambana na mgambo, basi naamuka kwa kupiga kelele, na hali
hii iliniandama sana, lakini baadaye ikatulia, na usiku mmoja nikaona ni bora
nitoroke, lakini kabla sijapata njia ya kutoroka, jamaa wakaja wakanichukua na
kunirudisha kambini.
Kule kambini jamaa watukutu wakazidi kutuandama , sisi kundi
lililokuja mwishoni kuwa eti tumewachongea na sasa hawana kazi ya uongozi, na
mmmojawapo alikuwa kaka mkuu akaachishwa kazi ya ukaka mkuu, kwahiyo kisasi
chake kikawa dhidi yetu…hasa mimi.
Kwakweli hali hii ya mateso nikaona haivumiliki na niliambiwa kuwa
huyo jamaa anasema kweli alishamtoa mtoto mmoja macho na hakuna aliyemsema kwa
wakubwa, kwani ukisema anakutoa macho na wewe au anakuumiza sehemu ambayo
utapata shida sana, kwahiyo wanamuogopa sana. Basi nikpata wazo la kutoroka.
Huwa mara kwa mara kuna gari la kubeba bidhaa , vyakula na vifaa
vingine , lori hili huja mara mbili au mara tatu kwa wiki, na kila likija,
baadhi ya watoto wanapewa kazi ya kuliosha,basi katika kulichunguza sana,
nikagundua kuwa kwa chini kuna nafasi ambayo ukiweka maboksi vizuri na ukafunga
kitu kama kamba unaweza ukalala, ukasafiri bila shida,..
Nikikumbuka baadhi ya filamu nilizowahi kuona, nikakumbuka
makomandoo walivyokuwa wakifanya, basi kila gari likika nafanya zoezi la kuweka
maboksi na kufunga vyema, nikafanya hivi mara mbili, kuweka boksi wakati
linasafishwa , halafu nalala pale wakati linasogezwa kuweka karibu na stoo,
nikagundua kuwa inawezekana kusafiri …
Kitu kilichoniogepesha ni kuwa barabara tulizopitishwa wakati
nakuja ni mbaya sana, na sehemu nyingine kuna vumbi, lakini nikasema kwasababu
mara nyingi magari hayo kama nilivyoambiwa huwa yanasafiri usiku, mimi nitaweza
kujifunika na vile vifaa tunavyotumia wakati tunafagia kwenye mavumbi.
Nikatafuta kifaa kimoha ambacho unaweza kukivaa vyema kabisa nikakificha.
Jamaa yule aliyefukuzwa ukiranja mkuu, akawa ni adui wangu mkubwa,
tulikorofishana naye , kwani wakati mwingine na mimi sikukubali kuonewa, kuna
siku nilimshitakia, ..basia kajua mimi ndiye chanzo cha yote hayo, japokuwa
nilikuwa mdogo, lakini sikukubali kuonewa, kuna muda na mimi nilikuwa najitutumua
hivyo hivyo,…kama alivyokuwa mama, huyo jamaa akaahidi kuwa usiku atakuja na kuhakikishaa ananitoa
macho yangu..niliogopa sana.
Basi siku ambapo jamaa huyo alipanga kunivamia …kama
nilivyodokezwa na wenzangu , nikaona ndio siku nitoroke, kwani marafiki zangu
waliniambia kuwa wamesikia jamaa huyo akipanga na wenzake kuwa atakuja kunivamia
usiku na atahakikisha amenitoa macho yangu kiukweli.
‘Yule jamaa huwa hatanii, na anajuana na wakubwa wa hapa, hata
ukimshitakia huwezi kuaminika,..si umeona tumemshtakia, lakini amefanywa
nini..kafukuzwa ukiranja mkuu baada ya watu wengi kulalamika….’akaambiwa
‘Nitajua la kufanya…’nikasema na sikuwahi kumwambia mtu mpango
wangu huo, nilikumbuka mama aliwahi kuaniambia kwa ukiwa na jambo la siri
usimuamini yoyote yule, kwani huyo unayemuamini anaweza akawa ndiye adui wako..
Ilipofika usiku wa saa sita…nikawaona wale jamaa watukutu
wakiongea, na baadaye wakalala, niliujua kabisa wameshapanga kunivamia, basi
kulipokuwa kimya, nikatoka nje, kama nakwenda kujisaidia, nilijua kabisa kuwa
bado mapema, lakini niliwaogopa sana wale watukutu, wanaweza wakaja kunivamia
nikiwa nimelele, nikaona heri nikalale pale kwenye gari, …, nikafika pale ,
nikiwa nimevaa sweta la baridi na vifaa vyangu vingine nilishaviweka kwenye ile
sehemu, matunda kidogo na maji ya kunywa.
Bahati nzuri mlinzi alikuwa kalala, basi nikajisokomeza ile sehemu
na kujilaza vizuri kabisa na kulala, nilikaa kwa muda mpaka nikafikiri labda
gari halitaondoka, ila baadaye nikashikwa na usingizi, na ndani ya usingizi,
niliota napaishwa juu, huko juu nikakautana na upepo mkali wenye vumbi, ngurumo
kama ya simba nikawa nakohoa sana, nilipaa wee, baadaye nikadondoka kwenye
shina la mti…baadaye nikazinduka, nilipoangalia nikasikia mngurumo wa gari ,
mara nikawa natingishwa sana.
Nilipokumbuka kuwa nipo nyuma ya lile gari , nikajiweka vizuri,
kusubiri gari liondoke, kumbe ndio lilikuwa linakatisha nyika, na sijui wapi
nilipo. Kumbe muda wote niliokuwa nikiota nilikuwa nipo ndani ya lile gari, na
kuota kukohoa ni kwasababu ya vumbi, na kumbe gari limeshaondoka muda na lipo
mbali kabisa na ile kambi.
Nikajiweka vizuri ili nisije nikaonekana. Na ilikuwa dhahiri kuwa
tumeshamaliza barabra ya vumbi, tunaingia barabara ya lami. Nikachukua kile chombo
changu nikakivaa puani,, lakini ilikuwa haina haja tena kwani barabara ya lami
vumbi lake ni kidogo.
‘Ni heri kufa kuliko kurudi kambini….’ Nikasema na kuapa moyoni
Tulisafiri, mpaka kukapamabuzuka, sasa ikawa joto, …ilibidi
nifungue yale maboksi ili nipate hewa, na katika pilika pilika hizi nikajikuta
naharibu ile kamba niliyoifunga kama kinga ya kunifanya nisidondoke, na
nikagundua kuwa nyuma kuna msururu wa magari ina maana watu waliopo kwenye
magari ya nyuma wanaweza hata kuniona. Nilijishikilia kwa shida sana, na mara
usingizi ukanishika. Ndoto zikaniandama tena na ile ndoto mbaya ya kutisha
iliponitokea nikazindukana kwa wasiwasi, nikipiga kelele na kutaka kukimbia, na
hapo nilikuwa nimejisahau kuwa nipo wapi.
Nilishituka nimeachia ile sehemu niliyoishika na ghafla nikabwagwa
chini kwenye lami, …nilisikia maumivu makali, nikaserereka barabarani na huku
nyuma magari yalikuwa yakija kwa kwa kasi, nilichosikia na mlio wa gari
likifunga breki, nikahisi kama napigwa kikumbo kikubwa, …hapo nikaona giza nene
likatanda usoni, sikujielewa kabiasa kuwa kumetokea nini, nikapoteza fahamu
WAZO LA LEO: Utalawa bora ni pamoja na kutoa haki
sawa kwa kila mtu bila kujali hali za
watu, utofauti wao wa kipato, rangi, jinsia au kabila, na kuwe na taratibu
nzuri za kuwahudumia watu kutokana na uwezo wao, wale wenye uwezo wawe ni
chanzo cha kuwawezesha wale wasio na uwezo ili ifikie hatua kuwa kila mmoja
anaweza kujimudu. Hii itasaidia kuondoa utofauti mkubwa wa kipato.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment