Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, May 11, 2015

NANI KAMA MAMA-74



`Baba…’ ilikuwa sauti ya mtoto akiwa anatokea chumba alichokuwa amelazwa, chumba ambacho mara nyingi hukitumia nesi akiwepo hapo nyumbani…. kumbe mtoto huyo alishaamuka kutoka usingizini, na alipoona yupo peke yake kitandani akateremka kutoka kitandani na kuja chumba cha maongezi.

Akili yake alianza kujiuliza yupo wapi, lakini alipochunguza kwa makini akagundua yupo sehemu anayoifahamu, akaingiwa na furaha akijua sasa atamuona mama yake na baadaye baba yake atakuja na zawaidi,…akatoka mle chumbani na kuingia chumba cha maongezi,..alipofika chumba cha maongezi wa kwanza kumuona alikuwa ni baba yake,…

‘Baba….’akaita kwa furaha

Kwa muda alipoingia, baba yake yeye alikuwa akiangalia mlango ule wa jikoni, ni kwa muda ule nesi na dada yake walikuwa wakitokea jikoni wakiwa na sinia lililokuwa na maandalizi ya wageni..na baba mwenye nyumba alikuwa akiwaangalia wao,  hakuwa ameangalia upande ule wa mlango aliotokea mtoto, sauti ndiyo ilimshitua,…..na kugeuka kuangalia huko

Baba mwenye nyumba aliposikia sauti ya huyo mtoto moyo ulimlipuka phaaa.., kwanza alijishitukia akitaka kusimama kwenda kumpakata yule mtoto kama kawaida yake, maana ilikuwa kawaida kila akitoka kazini mtoto huja kumpokea na baba huwa anakuja na zawadi, basi hapo humuinua juu akazunguka naye halafu anamweka chini anamwambia nisalimie.
Na mtoto huinua mkono na kushika kichwa cha baba yake na mwanzoni ilikuwa hivyo na baadaye alivyoanza kuongea maneno mawili matatu, akawa anasema `si-kamoo..’

Baba mwenye nyumba akajikuta kainuka kidogo,. Halafu kama vile kakumbuka jambo… kuwa huyo mtoto ni wa nani, akarudi na kukaa akainamisha kichwa , hakupenda kuinua kichwa kumtizama yule mtoto, na alikaa hivyo kwa muda kidogo

Mtoto alitarajia tendo alilolizoea kutoka kwa baba yake huyo..lakini haikutokea hivyo…, alishangaa kumuoana baba yake akiwa kainama chini na kujifanya hakusikia, yeye hakujali akawa anamsogelea baba yake, moyoni alihis huenda baba yake anaumwa… , mara akajikuta yupo kati kati ya watu, kumbe hakujua,..kumbe kuna watu wengine, akageuka huku na kule, sasa akiwa na aibu, au uwoga,…akawageukiwa hao watu, mmoja akamtambua

‘Si-kamoo….’akasalimia docta, na akamuona mlinzi akamsalimia pia.

‘Marahaba, haujambo, umeamuka eeh..?’ akauliza docta na mtoto hakumjali yeye akageuka upande ule alipo baba yake.

Hakumjibu docta, yeye kwa haraka akageuka kumuangalia baba yake, baba yake alikuwa bado kainama chini, kiakili za kitoto, hakujua afanye nini , lakini hakukata tamaa akawa sasa anamwendea baba yake pale alipokaa, baba yake kuona hivyo,..japokuwa moyo ulikuwa umeshatanda huruma, lakini kwa upande mwingine hasira na chuki zikamtawala…kwa haraka akasimama

‘Samahani natoka kidogo…nakuja..’akasema  na kusimama na kwa haraka akatoka kuelekea nje na wakati huo mtoto alishasogea karibu yake akitarajia lile tendo kutoka kwa baba yake..na alivyoona baba yake anasimama akajua  atapakatwa na kuinuliwa juu kwa juu kama kawaida yake, na mtoto alipoona baba yake anatoka nje akasema

‘Si-sikamoo….baba….’

Lakini baba yake alishatoka nje, na hapo akabakia kasimama na alipogeuka upande ule wa mlango wa kutokea jikoni, ndio akawaona nesi na mama yake wakiwa wamesimama na vyakula kwenye sinia kubwa…mama yake huyu alimuangalai kwa jicho la huruma, na mtoto kwa haraka  akamkimbilia, mama yake akisema;

‘Mama..baba..mama taka baba….’akasema

‘Ohh, mwanangu,…umekuja…ohh nimekumis kweli..haujambo mwanangu…’mama mwenye nyumba akamuinua mtoto na kufanya afanyavyo baba yake, na baadaye akampakata na kuanza kumuangalia machoni.

‘Si-sikamoo, mama..’akasalimia mtoto sasa akiwa anafuraha maana yupo mikononi mwa mama yake na nesi hakuweza kujizuia akaona machozi yakimtoka.

‘Marahaba…haujambo, una njaa eeh, ngoja nikupe chakula chako unachokipenda,…’akasema na kumchukua mtoto wakaelekea jikoni, huku nyuma nesi akawa anawaandalia wageni na baadaye baba mwenye nyumba akaingia, na kulionekana kama kuna kitu kimepita maana ukimiya ulitanda zaidi..

********

‘Rafiki yangu naona muda umepita sana…’alisema rafiki yangu akisimama kutaka kuondoka

‘Hapana huwezi kuachia hapo, niambie kwanza ilikuwaje, yule mama kaenda wapi,. Na huyo mtoto alibakia hapo…au ilikuwaje?’ nikamuuliza rafiki yangu

Mkumbuke kuwa kisa hiki anayenisimulia ni rafiki yangu, lakini maelezo hayo aliyokuwa akisimulia hadi hapo ni maelezo aliyoyapata kutoka kwa mama yake..

 `Kwahiyo baada ya hapo mtoto akapelekwa kwa mama yake, au ilikuwaje?’ Nikamuuliza rafiki yangu ambaye alikuwa akitaka kuondoka , na mimi  na jamaa wengine waliokuwepo hapo ambao ilibidi waje na wao wasikilize..baada ya kuona umuhimu wa kisa hicho..na wao walikuwa na hamu ya kujua nini kilitokea baadaye. Nilijua kama nitamruhusu aondoke itakuwa sio rahisi kumpata tena. Nikamganda kwa maswali!


‘Bwana wee, naona nia yako unataka nikuhadithie kila kitu,..kuna sehemu siwezi kuzisimulia hapa tena…na sikutaka mtu ajue hayo yaliyotokea…, kwani kiujumla kumbukumbu zake zinanitia machungu sana…’akasema

‘Lakini umeshaanza kunisimulia,…na ukiachia hapo utanifanya nibakie na dukuduku moyoni…tafadhali endelea umalizie tu….’nikasema.

‘Hapo nilipofikia ndio mwisho wa sehemu aliyonisimulia mama, kutoka hapo hakuweza kusema tena….’akasema

‘Hakuweza kusema tena…kwanini?’ nikamuuliza

‘Mama alikuwa katika hali mbaya, muda wote ananisimulia kisa hicho alikuwa kumbe anaumai ndani kwa ndani..alikuwa akijikaza tu kunisimulia, ikafika sehemu hajiwezi tena,hawezi kuongea…’akasema

‘Oh….’nikaguna.

‘Lakini ngoja nikuanzie maisha yangu na mama, ingawaje niliishi naye kwa muda mfupi kabla ya kutengana naye katika mzingira ya kutatanisha…kumbukumbu zangu zilianza kujua ni nini kinaendelea wakati nipo na mama yangu huyo…’akasema

‘Mama yupi?’ nikamuuliza

‘Mama aliyenizaa..’akasema

‘Ulifikaje kwake…?’ nikamuuliza

‘Hadi hapo, sehemu hiyo,  sikukumbuka ilikuwaje…’akasema

‘Mama hakukusimulia..?’ nikamuuliza

‘Hadi hapo,…hapana…kama unataka nikuhadithie kimtiririko ilivyokuwa …hadi hapo sikumbuki kilichotokea,..’akasema

‘Mhh, sasa…eeh..’nikabakia kutaka kujua, maana sehemu hiyo ni muhimu sana, akaniangalia halafu akatabsamu…akasema

‘Sasa nitakuhadithia maisha yangu na mama mzazi…kipindi hicho nipo naye, ukumbuke mama alikuwa hana kitu, hajui wapi pa kuishi,..hajui atakula nini…lakini pamoja na hayo, mama alinipenda sana, na hakutaka kabisa niachane naye, nilikuwa kama mboni yake ya jicho, lakini ilivyotokea, tukajikuta tumetenganishwa tena…’akasema

‘Sijakuelewa…’nikasema.

‘Sehemu hiyo ya kwanza ya simulizi la mama iliishia hapo, ..’akasema na mimi sikuwa na la kufanya ikabidi nimsikilize anavyokwenda na simulizi yake …

*********
‘Nakumbuka maisha yangu na mama yalikuwa ya kutangatanga, mara leo tupo hapa mara kesho tupo kule …na sehemu kubwa ya maisha ya mama yalikuwa ya kuomba-omba, ili angalau mimi nipate chakula…’akaanza kuongea na machozi hapo yalikuwa yakimlengalenga.

‘Ni…huzuni kwa kweli…ndio maana sitaki kusimilia sehemu hii…’akasema

‘Jikaze kiume bwana….’akasema jamaa mmoja aliyekuwa akifuatilia, alikuwa na hamasa ya kutaka kujua,na mimi nilitaka hivyo hivyo, lakini nilishaanza kumuonea huruma rafiki yangu kwani naona inampa uchungu zaidi.

‘Mhh…katika kuhangaika kwa mama, akagundua kuwa kwenye jalala moja kuna vyakula huwa vinatupwa sana hapo, kwahiyo tukahamia hapo..sikuwa peke yangu, kulikuwa na watoto wengine ambao hawakuwa na wazazi…’akatulia

‘Jalala….ina maana ilifikia hapo…?’ nikauliza

‘Kuna kitu niwaambie , ndio maana mimi nikiwaona akina mama wanaomba omba mitaani,wakiwa na watoto …siwachukii, najua kabisa sio dhamira yao..’akatulia

‘Hawajapenda iwe hivyo…ni ukweli usiopingika kuwa wengi wao hawapendi hiyo hali..ona kama ilivyokuwa kwa mama..alitamani kabisa apate kazi..ili alipwe, lakini ni nani atamkubali kumuajiri…kwanza ile hali yake ya kujifunika, ikawa ni kero kwa wengine,….’akatulia

‘Kuna wakati alikwenda kwa mama Ntilia ili awasaidie kazi, ili angalua nipate chakula…au aoshe vyombo wamlipe, lakini wanamkata, wanamuambia ajifunue kwanza wamuone sura yake…, wanasema watamjuaje, kama ni mwizi…mama hakutaka kabisa kujifunua..

‘Wewe uliwahi kumuona mama yako usoni kipindi hicho..?’ nikamuuliza

‘Kwa muda ule nilioishi naye hapana..sikuwahi kumuona mma yangu akijifunua…, na sikuwa na haja ya kufanya hivyo, mimi nilijua ni mama yangu, na kwanini anafanya hivyo haikuniingia akilini kumuuliza, nakumbuka watoto wengine walikuwa wakiniuliza lakini mimi sikuwa na la kuwajibu..’akasema

‘Muhimu kwangu, ukilinganisha na wenzangu ni kuwa mimi nilikuwa na ufahari maana nilikuwa na mama yangu…wenzangu walikuwa hawana wazazi…kwahiyo kwa namna moja au nyingine walikuwa wakinione wivu…’akasema

‘Hebu kwanza nikuulize uliwezaje kumkubali huyo kuwa ni mama yako..?’ nikamuuliza

‘Kumbukumbu hasa sijui, …unajua nilikuwa bado mdogo…nakumbuka machache sana kutoka kwa mama mlezi hadi kwa mama huyo,..sikumbuki vyema ilikuwaje hapo..ninachokumbuka ni kuwa nilikuwa mikononi mwa mama yangu huyo, na nilishampenda..’akasema

‘Oh, hapo unatuacha kwenye mataa..’akasema jamaa aliyekuwa pembeni yangu akimsikiliza rafiki yangu huyu.

‘Unakumbuka yeye ndiye aliyekuwa akinilea nikiwa na mama wa kunilea…kama alivyonisimulia mama yangu, na nilikuwa nampenda sana..kama alivyokuwa akinipenda mimi, kwahiyo ..hata sikumbuki..ila nilimuona na nikamtambua kama mama yangu..kumbukumbu zangu ndivyo zinavyokumbuka, hadi hapo….’akasema

‘Hukuwa unamkumbuka mama yako wa kukulea..ukataka kurudi kwake..?’ nikamuuliza

‘Kuna muda nilikuwa nakumbuka na nilikuwa nikimuuliza mama yangu huyo, lakini hakukuwa na muda wa maongezi, unajua utoto tena,..tunakutana na watoto wengine tunakimbizana , tunapigana,..njaa inakushika, mama anahangaika kunitafutia chakula…usiku unakuwa umechoka…unajikuta umelala tu…’akatulia

‘Sasa mlikuwa mnapataje chakula,..na kulala mlikuwa mnalala wapi..?’ nikamuuliza

‘Kuna muda tulikuwa tunakosa chakula kabisa…majalala yamechomwa moto, watupaji nao kwa roho mbaya wanakiharibu kile chakula…, mimi naishia kulia..hapo ndio ninakuja kumkumbuka mama wa kunilea, hapo mama mzazi..atahangaika huku na kule,…hata kwenda kupiga hodi majumbani mwa watu, kuniombea angalau mimi nipate chochote, basi kwingine akifika mama anafukuzwa, ..lakini hakati tamaa, mpaka apate kitu cha kunilisha…na wakati mwingine anarudi nimeshalala..lakini atahangaika angalau niingize kitu tumboni…’akatulia akionyesha uso wenye huzuni.

‘Na mlikuwa mnaishi wapi, …ni hapo hapo mjini, au mlirudi huko kijijini..?’ akaulizwa

‘Ilikuwa maeneo ya hapo hapo mjini..na mama alijitahidi kubadili maeneo ili asije akanyang’anywa mtoto wake, kwani kuna muda alikuwa akitafutwa ili nichukuliwe na ustawi wa jamii….hospitali walifanya juhudi hizo, baada ya kuona kuwa mama yangu hataweza kunilea…mama akatoroka mbali, na akawa anabadili maeneo….’akasema

‘Kwahiyo ikawaje..?’ nikaulizwa

‘Kiukweli mama sikuishi naye kwa muda mrefu…kuna tukio lilitokea, …sitalisahau, na ndilo lililonitenganisha mimi na mama yangu, sikuonana na mama tena, hadi nimekuwa mkubwa..….’hapo akatulia na machozi yakawa sasa yanamtoka

‘Naombeni sana niishie hapa kwa leo….nitajitahidi nije niwasimulie sehemu iliyobakia..’akasema na sikuweza kumzuia


WAZO LA LEO: Masikini, wasiojiweza, mayatima…wanastahiki kusaidiwa , sio kwamba wamependa hiyo hali, bali ni kutokana na nakama za kimaisha na huenda kwa kiasi kikubwa nakama hizo zimetokana na udhalili, wizi, na ubadhirifu, wa matajiri, ambao kwa namna moja au nyingine wamafisidi haki za hawa watu. Hata kwenye maandiko matakatifu tumeamuriwa kuwasaidia hawa watu, ..kwahiyo tusiwanyanyapae, tujitahidi kadri tuwezavyo kuwasaidia, hasa watoto…wapo mayatima, wapo waliotelekezwa na wazazi au kwasaabbu ile na ile …hawa watoto wanahitaji huduma yako,…kama una uwezo usione ubahili, kwani utakachotoa kwao, ndilo fungu lako baada ya maisha ya hapa duniani.
Ni mimi: emu-three

No comments :