Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, May 8, 2015

NANI KAMA MAMA-73


 Mlango wa chumbani ulifunguliwa, na aliyejitokeza pale mlangoni alikuwa mke wa nyumba, na mume wake aliyekuwa akiongea akakatiza maneno na kugeuka kumuangalia mke wake, kitendo hicho cha kugeuka kuangalia huko kwenye huo mlango kilitendwa na wote waliokuwemo humo ndani.

Mke wa mwenye nyumba taratibu akajongea kuja eneo la mazungumzo,  alikuwa kajifunga khanga mbili, akionyesha kuchoka, tofauti na anavyotoka nje , huwa akitoka nje huvaa gauni pana ambalo huwezi kujua yupoje….

Nesi ambaye alikuwa kaupa mgongo huo mlango, naye akageuka kumuangalia huyo aliyetoka huko chumbani alifahamu ni nani, alijua ni dada yake, lakini alikuwa na hamasa kujua hali ya dada yake, ambayo ilishamtia mawazo, akiwa akijiandaa kusimama kwa adabu ya kumsalimia dada yake, akajikuta akishikwa na butwaa, 

Kwanza hakuwa na uhakika, lakini anamfahamu dada yake alivyo, hata akifunga khanga, maumbile yake anayafahamu vyema, akapepesa macho yakiwa hayabanduki pale yalipokuwa yakiangalia, sasa akawa kama kagandishwa, nusu kukaa na nusu kusimama. …

‘Hivi ni kweli au ni macho yangu…’akawa akijuliza…

Tuendelee na kisa chetu

***********

Nesi alipohakiki macho yake na kubaini kuwa hicho alichoona ni kweli, akasimama kwa haraka,  na kuelekea pale aliposimama dada, japokuwa ni karibu tu, kwa hali ile kwake yeye alipaona ni mbali,..lakini akajitahidi, hakuweza kuvumilia..

Na wakati huo huo , kiadabu, wote waliokuwemo humo ndani walisimama hasa walipoona mwenyeji wao, nesi kasimama. Na docta naye alikuwa kasimama kusalimia, yeye alikuwa karibu na ujio wa huyo mama, kwahiyo akawa wa kwanza kunyosha mkono wa salamu, lakini mkono huo ulichelewa.

Nesi aliinuka kwa haraka ili awe wa kwanza kumfikia dada yake,akawa kama anaruka, huku akiendelea kumkagua  dada yake kwa macho, na tabasamu tele mdomoni, …akatikisa kichwa, halafu akainuka mikono juu, akimshukuru mungu na kwa haraka za ajabu bila kujali kuwa docta alikuwa kanyosha mkono kumsalimia dada yake,…hakujali yeye akamkumbatia dada yake!

`Dada kwanini mumenificha kiasi hiki, hata mimi mdogo wako, nimekukosea nini…’ akawa kamshikilia dada yake, lakini huku akiogopa kumkumbatia zaidi…ni ada yao wawili hawa wakikutana kusalimia kwa hivi, kuonyesha jinsi gani walivyozoeana kila wakikutana husalimiana kwa kukumbatiana, ila hili la leo lilizidi zaidi.

Dada yake akiwa na tabasamu mdomoni, akamshikilia mdogo wake, huku akimuangalai docta, na kwa haraka akamuachia mdogo wake, na kunyosha mkono kusalimiana na docta…

‘Samahani sana mgeni, ..huyu mdogo wangu, hajali kuwa wewe bosi wake unatakiwa kupewa kipaumbele zaidi…wewe hebu niachie nisalimiane na wageni… docta eeh, hujavaa zile sare zako lakini nimekukumbuka..’akasema mama mwenye nyumba sasa akisalimiana na huyo docta.

‘Ndio mama docta..usijali ni kawaida, yaonyesha siku nyingi hamjaonana na ana hamu sana ya kukutana na wewe…ni kutokana na majukumu,..alikuwa akijaribu kuomba ruhusa tunamkatalia…., natumai haujambo, tumeambiwa ulikuwa na …..una matatizo ya kiafya.., naweza kujua shida ni nini hasa japokuwa nikuonavyo, hali kama hiyo hutokea sana…?’ akauliza docta.

‘Nani kasema nina matatizo…ni kawaida tu…..’akasema huyo mama akionyesha aibu fulani

‘Mueleze huyo ni docta …huoni hiyo ni bahati, kaja hadi nyumbani…’akasema mume wake..

‘Nimesema sina matatizo,…mimi najijua, kama ningelikuwa na matatizo ningelikwenda hospitalini kwake..’akasema mama akisalimiana sasa na mlinzi.

Walipomaliza kusalamiana, akageuka kumuangalia mdogo wake, ambaye alikuwa nyuma yake akiendelea kumfuatilia, tabasamu tele mdomoni akiwa habandui macho yake pale alipokuwa akipatizama muda wote na dada yake akawa kama anamzarau sasa…, akasema;

‘Karibuni wageni,…’akasema akigeuka huku na kule, kuna kitu alikuwa akikitafuta, lakini hakusema, akatafuta sehemu akakaa, na mdogo wake akasogea na kuja kukaa karibu naye.

‘Samahani mdogo wangu, kila mara tukitaka kukuambia , kunakuwa na kipingamizi, ila wewe kama nesi nilidhania umeshanigundua, kwasababu kama unavyoona hali haijifichi, ..nakumbuka siku ile tulipokuja tulikuwa na lengo hilo la kukuambia, najua nilikuwa nimevaa nguo pana usingeligundua..lakini kwa nesi au docta mzoefu unaglinigundua…hukuwa na shaka shaka….? ’akauliza

‘Nilikuwa na shaka hiyo, ….lakini sio mara ya kwanza , nakumbuka kuna kipindi nyuma ilitokea hivi, …na haikutokea…. lakini hii sasa naona ni heri…na inaonyesha ni ya muda, ..yani muda wote huo msinishitue..’akalalamika nesi.

‘Samahani sana mdogo wangu, mimi na mwenzangu hatukutaka watu watufahamu mpaka ifikie mahali ambapo hakuna jinsi…na..wewe tulitaka tukuambie kwa wakati muafaka, tulitaka iwe kama sepriziii, ….si unakumbuka ile ya mwanzo, wasiwai wetu ulikuwa isije ikawa hivyo tena…’akasema na kuwa kama anacheka.

‘Dada furaha niliyo nayo haielezeki…sijui nisemeje ….’ Akamkumbatia tena dada yake huku machozi yakimlengalenga, moyoni akisema , hii ndio miujiza ya mungu, una furaha machozi yanakutoka, una huzunu huku unacheka….mmh, hatimae familia ina furaha.

‘Haya naona tukiwaachia nyie mtaongea utafikiri hakuna wageni wengine, shemeji wewe ni mwenyeji, angalia taratibu za kuwakirimu wageni…’akasema shemeji mtu na mke wake akamuangalia mumewe kwa jicho la kumuonya.

‘Kwanini, mbona unaingilia anga zangu, wewe nesi tulia, mimi sijashindwa kuwakirimu wageni, sijachoka, siumwi…sina tatizo lolote…tulieni kidogo, tulikuwa tunasalimiana kwanza, mambo sasa hivi….mfanyakazi kaenda kwao, kwahiyo tupo wenyewe,…lakini hatuna shida, …tafadhali nawatoka kidogo…’akasema mama mwenye nyumba na kusimama..na nesi kwa haraka naye akasimama na kutembea na dada yake huku akinyosha mkono wa ushindi

Kwa pamoja mama mwenye nyumba
wakaelekea jikoni.

**********

‘Samahani sana baba mwenye nyumba, lakini sina budi nikuulize hili,  kwani mimi ni docta ambaye pamoja na fani yangu nahitajia sana msaada wa watu, ..kiufupi mimi ni docta ninayemuhudumia huyo mama mliye-eeh, …mwenye matatizo…’docta akaanza kuongea.

‘Mhh, sawa niulize tu…’akasema baba mwenye nyumba , huku akionyesha ana furaha fulani tofauti na ilivyokuwa awali.

‘Huyo mama anahitajia msaada mkubwa, mimi kama docta nimejitahidi kadri niwezavyo kutokana na utaalamu wangu, ni ni kweli sasa anajitahidi na sasa kilichobakia ni mambo machache ambayo yanahitaji msaada wa jamii… ‘akatulia kidogo

‘Yah, serikali ipo itamsaidia,…mimi sio tajiri…’akaanza kusema na docta akamkatiza.

‘Nisikiliza kidogo hapo….kutokana na matatizo yaliyomtokea huyu mama, ambayo kakumbana nayo, yalisababisha yeye kupoteza kumbukumbu zote za nyuma, ninaposema kupoteza kumbukumbu nina maana akili yake ilisahau, haikumbuki kabisa kile kilichotokea huko nyuma, kamsahau hata huyo mume wake..hata ndugu zake, hata yeye mwenyewe alikuwa hajijui ni nani…’akatulia

‘Hilo ni tatizo na linajulikana kitaalamu, na linatibika…ni swala la muda, na pia linahitajia usaidizi wa namna moja au nyingine, linahitajia ushauri nasaha, kauli nzuri,…’akatulia

‘Kwa jinsi alivyokuja hapa,…hata kama ingelikuwa wewe ungelikasirika…’akasema

‘Ndio hivyo yeye hapo alipo ni mgonjwa , na hiyo ni moja ya athari za hilo tatizo, …anahitaji kusaidiwa, wewe hushangai kuwa pamoja na kusahau, pamoja na kumsahau mume wake, lakini wewe kakumbuka haraka..’akasema kama anauliza

‘Mhhh, labda ni kutokana na hayo aliyonitendea huko nyuma, na yamepita…’akasema huku akikunja sura tena kutoka kwenye furaha na kuingia kwenye huzuni.

‘Yawezekana ndio…lakini pia yawezekana yeye bado anakupenda na yaliyotokea huko nyuma hayakuwa kusudio lake, ..kama unavyoona, mtoto wake alikuwa kichwani mwake muda wote, kwasababu gani …ni kwasababu ya upendo wa mama kwa mtoto, upendo huo hauna …angalia hata wanyama , ndege huwezi kufanya kitu kwa watoto wake, ni lazima atakurukia…ni upendo wa asili…’akatulia

‘Ahaaa, una maana kanikumbuka kwa kuwa ananipenda, hahaha..leo hii ndio akumbuke hilo, hapana…hilo la kupenda halipo..na kiukweli ni kujidanganya, hilo..asinidanganye, …pendo langu mimi nay eye limeshapitwa na wakati..’akasema baba mwenye nyumba

‘Ndio, …kakumbuka kwasababu ya pendo la asili… , kupenda huko sio lazima kuwa anataka mje mrudiane,..hiyo sio lazima,… mnaweza mkapendana hata kama kila mmoja kaoa na kuolewa, lakini zile hisia za kweli haziishi moyoni…, hayo ni maumbile ndugu yangu, hata wewe hili lipo moyoni mwako,…’akasema docta.

‘Sijui…’akasema baba mwenye nyumba huku akitikisa kichwa.

‘Huo ndio ukweli ndugu yangu…, ndio maana hata wewe mpaka sasa huwezi kulisahau hilo tukio, …ndio maana mpaka sasa unajiona kama una kovu lisiloponyeka…unafikiri kwanini…’akawa kama anaulizwa

‘Mhh, ni kwasababu alinijeruhi moyo mwangu…’akasema

‘Kwanini akakujeruhi moyoni mwako,…ina maana kulikuwa hakuna wanawake wengine, wazuri..ambao wangeliweza kuzina nafasi yake…?’ akaulizwa

‘Wapo..mmojawapo si mke wangu, kazina hiyo nafasi na nimesha msahau yeye..’akasema

‘Hata kama atapatikana huyo,…lakini kama kulikuwa na yule mliyewahi kupendana naye kwa dhati , pendo la asili, lisilo na masharti, moyoni hatanduka,…sasa huyu mama kakumbuka, kuonyesha jinsi gani alivyokupenda..’akasema

‘Sijui…’akasema baba mwenye nyumba.

‘Ndugu Yangu, huo ndio ukweli, .. nyie mlikuwa na pendo la asili pendo lisilo na mipaka, lakini ikatokea ilivyotokea mkatenganishwa….nikuambie kitu ,yale wanayoonyesha kwenye filamu za mapenzi kusalitiana, kutengana…, sio maigizo tu , kuwa watu walipendana, wakatenganishwa na sababu mbali mbali, wakaja kukutana baadaye…zile ni nadharia zinazotokana na uhalisia..yapo, yanatokea…’akasema docta

‘Kwahiyo unataka kusema nini…?’ akauliza mwenye nyumba akimuangalai docta.

‘Kwanza umsamehe, pili uangalia jinsi ya kuwa naye karibu, ili naye ajisikie kama binadamu…au sio docta, samahani nachangia kidogo, nisiwe tu msikilizaji…’akasema mlinzi, na docta akatikisa kichwa kukubali. Baba mwenye nyumba akamuangalia yule mlinzi akonyesha uso wa kutahayari, halafu akatikisa kichwa, akasema;

‘Simuombee mtu vibaya,… lakini ili mjue jinsi gani nilivyoumizwa hiyo siku, sio hiyo siku tu ..ni miezi , hadi, mwaka, miaka ikapita..nateseka moyoni, najiuliza, kwanini…kwanini…nyie acheni,…ili mjue nilivyoteseka, ingelifaa na nyie muipitie hiyo hali..inatesa…lakini nashukuru mungu…’akasema akiangalia juu.

‘Ni kweli inatesa, ni kweli inaumiza sana..lakini mwenyewe umekiri kuwa kutokana na hilo ukampata mwenzako mwingine ambaye alikuja kukupa mapenzi ambayo umeona huenda usingeliyapata kutoka kwa huyo mwenzako mliyetenganishwa naye, huoni kuwa ni mipango ya mungu…’akasema mlinzi.

‘Ni kweli…hilo nimeliona..na nashukuru kwa …japokuwa siwezi kusahau, na swala la kumsamehe, mbona mimi nilishamsamehe zamani tu..na sina kinyongo naye saana..japokuwa ukikumbuka bado unaumia..na kiukweli sikupenda kuja kukutana naye tena…maana nilijua hili litatokea, nilijua tukikutana anye hakutakuwa na amani…’akasema huku akitikisa kichwa.

‘Mungu kapanga mkutane ili yeye akuelezee ilivyokuwa kwa kinywa chake, ili akuombe msamaha, japokuwa alichofanya …hata kama angelikuwa ni mtoto wako, usingelipenda aende kinyume na matakwa yako au sio..chukulia angelikuwa ni binti yako, unafikiri ungelifurahia akuhini, akatae ombi lako, akijua nyie mpo hataraini ya kufanywa watumwa, kunyanyasikia, na ukumbuke wazazi hao waliyayafanya hayo kwa ajili yenu watoto, mpate kula, nk…hebu angalia hilo kwa mfano huo..’akasema docta.

‘Unajua …nyie hamunielewi, nyie hamfahamu ilivyotokea,..tulishakaa naye kabla, tukaliongelea hilo kwa marefu na mapana yake…, na tukaliona hilo…tulijua ubabe wa huyo mtu, lakini kwanini tumuone kama mungu, kuwa kila akitakacho yeye hupata, kwasababu yeye ni tajiri basi tumpigie magoti,…hapana hicho ni kiburi, na kama ni kiburi,ilitakiwa mtu afanye kitu ili ajione yeye ni sawa tu na wengine, sasa ni nani wa kulifanya hilo….tukasema sisi tuonyeshe mfano, tujitoe mhanga…’katulia

‘Mliongea hivyo mkakubaliana hivyo..?’ akauliza mlinzi

‘Ndio…ndio maana inaniuma,..tuliliongelea hadi .. mpaka tukala kiapo, japo ni kiapo cha ujana…si unajua tena..tuliahidiana kuwa hakuna atakaye msaliti mwenzake, tukaagana, tukitakiana kila laheri, kumbe ilikuwa kuagana kwa ukweli…mwenzangu akafika huko, sijui waliongea nini, akanigeuka…unajua nyie kwasababu mnalisikia hilo tukio kijuujuu, hamuwezi kulielewa…’akasema

‘Nakuelewa sana…na nafahamu sana jinsi gani ulivyoumia, hilo ni moja ya mambo ambayo yakimkuta mtu yanaumiza sana….lakini cha kushukuru mungu ni kuwa mwenzako , na wewe mwenyewe mpo hai, na mungu kawapa nafasi ya kutubu, kuombana msamaha,..kuongea tena, na mnaweza kuongea kwa wema tu mkayasahau hayo kwa wema tu, maanayaliyopita, yamepita muyaone kama majaliwa tu…’akasema docta

‘Docta..mimi nimekuelewa saana tu.., na mimi moyoni eeh, nimeshamsamehe saana tu, lakini sina muda wa kuongea naye tena..hilo mnielewe…, maana yeye ana mume wake, na mimi nina mke wangu, tutaongea ili yasaidie nini..hebu angalia haya yaliyotokea, kaja hapa simjui, kajifunika kabisa huenda ili nisimfahamu,..kapatwa na nini…nyie hamlioni hilo….hapana mimi na yeye basi….arudi huko kwa mume wake…hivi kweli mnanishauri kitu kama hicho….’akawa kama anauliza

‘Aaah, lakini kujifunika huko bado ni utashi wake, hakuna anayefahamu ni kwanini anafanya hivyo, yawezekana ni kutokana na hayo majereha, huko kuharibika sura..lakini pia yawezekana kuwa imani yake inamtaka kufanya hivyo…na sio kwamba mrudiane,….’akasema docta.

‘Hahaha, imani yake..hahha, hilo halipo,…mimi namfahamu bwana… labda hilo la kuficha huko kuharibika sura, lakini pia yawezekana hakutaka nimfahamu..’akasema

‘Hapana hilo la kutaka usimfahamu sio kweli, ….maana kitaalamu imethibitisha kuwa mama huyo alipotewa na kumbukumbu, na sasa hivi ndio anaanza kukumbuka, nab ado hajawa sawa, bado yupo kwenye mapambano , ndio maana nataka unisaidie kwa hilo..’akasema docta na baba mwenye nyumba akamtolea jicho na kusema;

‘Ni kusaidie  nini…?’ akauliza

‘Nataka mimi na wewe tushirikiane, tuweze kumsaidia huyo mama aweze kurejea katika hali yake ya kawaida, aweze kukumbuka kila kitu, aweze kusimama kwa miguu yake mwenyewe, na ikiwezekana tuweze kumpata huyo mwanaume wake aliyemfanyia hivyo…hilo ndio ombi langu kwako..tafadhali mkuu…’akasema

‘Eti nini…?’ akauliza baba mwenye nyumba.

‘Ni ubinadamu tu…, hebu jaribu kukumbuka enzi zile wewe na yeye mlipokuwa wapenzi, kumbuka yale mema mliyotendeana, kumbuka …upendo wake kwako,..usikumbuke hilo tukio lililokuumiza, ili tumsaidie huyo mama, unatakiwa uondoe hasira, uondoe chuki, umueweke mungu wako mbele, kuwa hayo ni majaribu na yeye keshajifunza, na kuumia kupita maelezo…hivi wewe humuonei huruma kwa hali aliyokuwa nayo…’akasema docta.

‘Sikiliza docta, nimeshakuambai huyo ni mke wa mtu, na mimi ni mume wa mtu, tumeshaweka mipaka,…hivi nikuulize kama inatokea mume wake anafika halafu anikute mimi nipo na huyo mke wake tunaongea, unafikiri atafanya nini…?’ akauliza

‘Ni mpaka huyo mume wake awepo, kwa hali ilivyo, na kwa hali huyo mama alivyotendewa, sizani kama huyo mume wake ana haja tena na huyu mama…muhimu amkumbuke na ikibidi sisi tukutane na huyo mume wake…’akasema docta

‘Wewe hujui tu, ..wewe hujui hili kabila letu lilivyo..haya tuachie sisi wenyewe, ….huyo mume wake kwa jinsi ninavyomfahamu, hata kama kitu ni cha kutupa, hawezi kumpa mtu..hata kama kakitupa akaona adui yake kakiokota, anaweza kupata sababu ya kukuumiza…mimi namfahamu sana yule mwanaume ….’akasema

‘Sisi nia na lengo letu ni kusaidia, na ingelikuwa ni bora sana tukampata huyo mtu,hiyo ni moja ya kazi zetu kuwanasihi hao watu, kuwaelimisha, ili waweze kukumbuka ubinadamu, tumeshakutana na watu kama hao saana, na wengi wamejirudi, …huwezi ukamtesa binadamu mwenzako kiasi hicho,….hilo halikubaliki…yule mama kateseka sana, kumbuka mateso hayo yatakuwa yamempata kipindi akiwa mja mzito…’akasema docta.

‘Ni kweli hata mimi nimesikitika sana…lakini ..mmh, mimi siwezi kukaa na huyo mama tukaongea naye tena, naomba mnielewe hivyo …’akasema

‘Mnaweza….tu..’akasema docta

‘Ili iweje,..eti tumtafute mume wake, kwa kipi ninachokitafuta kwa huyo mwanaume,…natafuta vita..au nipate faida gani,…mimi siwezi kulifanya hilo, na nimesema huyo mtoto wake mumrejeshe kwa mama yake, mimi siwezi kumlea huyo mtoto tena,..nichofanya kinatosha, kwanza shukurani yake ipo wapi…hapana,  mimi sipo tayari kukaa na huyo mtoto….’akasema na kukatizwa na sauti ikisema.

‘Baba….’ilikuwa sauti ya mtoto iliyokatisha mazungumzo na wote wakageukia kuangalia huko sauti ilipotokea,  ilikuwa ni mlangoni, na kabla hawajasema neno sauti nyingine ikasema;

‘Mimi nipo tayari kukaaa naye, hadi hapo mama yake atakupokuwa na uwezo wa kuishi naye..’ilikuwa kauli iliyotokea mlangoni.


NB: HAYA ndugu zanguni wapendwa, niambieni hapo…najitahidi kuwaletea haya, lakini nipo kwenye mitihani, mitihani ya kimaisha,…natafuta jinsi gani nitaweza kuwekeza kwa hii kazi, ili niweze kutoa vitu bora zaidi ya hivi, ...mwenye wazo, njia asisite kunitumia maoni.

WAZO LA LEO: Tunapokuwa kwenye mazungumzo ya watu wawili au zaidi , tupende kupeana nafasi ya maongezi, ni kweli kuna wataalamu wa kuongea na wakiongea ni rahisi sana kueleweka na kufikisha ujumbe kwa wengine, na pia kuna ambao hawana utaalamu wa kuongea sana, lakini wanaweza wakawa wanafahamu hilo jamb mnaloliongelea huenda zaidi ya huyo muongeaji.


Cha muhimu kwenye hadhira, au kwenye maongezi, kupeana nafasi hata ikibidi kumuongoza huyu ambaye sio muongeaji, maana anaweza akawa anafahamu jambo lenye faida kubwa kuliko mnavyofahamu. Tusidharau kauli za wengine kwenye maongezi, tisidharau watu kutokana na jinsi walivyo, tusipende kukatiza watu wanapoongea tunaweza kukosa faida kubwa.

Ni mimi: emu-three

No comments :