‘Huyo mama ni nani, na anatokea wapi….?’
Akauliza shemeji mtu.
‘Huyu mama mnamfahamu sana…’akasema mdogo
mtu na kuwafanya hao wanandoa wawili kuangaliana.
‘Tunamfahamu kwa vipi, ..?’ wakauliza
‘Hamtaamini nikiwaambia kuwa huyu mama mliishi
naye kwenye nyumba moja, na huyo huyo ndiye kaja hapa kudai kuwa mtoto wake
nimemchukua mimi..’akasema
‘Mama gani huyo..?’ akaulizwa
‘Yule mama wa mitaani,..’akasema mdogo mtu,
na wote wakamtolea macho kila mmoja akionyesha uso uliojaa maulizo
***********
‘Mama wa mitaani, ni mama gani huyo….?’ Shemeji mtu akataka
kuuliza lakini akakatisha, kuonyesha kakumbuka jambo, akageuka kumuangalia
mkewe lakini mkewe akatangulia kusema;
‘Mimi sijaelewa ni mama gani huyo?’ akauliza dada mtu naye
akigeuka kumuangalia mumewe, na akawa kakumbuka jambo, na kugeuka kumuangalia
mdogo wake, na mdogo wake akaona asipoteze muda, akasema;
‘Ni yule mama mliyekuwa mkiishi naye, aliyekuwa akiitwa mama wa
mitaani, akaja kuitwa mama wa mkono wa baraka, ambaye aliletwa hapa kutibiwa kutoka
huko kwenu akiwa kaungua…ndiye huyo anayedai kuwa mimi nimemchukua mtoto wake…sasa
mtoto huyo ni nani, kama sio huyo mtoto wenu….’ akasema nesi
Nesi akatega sikio akahisi kama kuna mtu alikuwa anakuja hapo
ofisini kwake, lakini hajasikia mtu akigonga, akataka kusimama kwenda kufungua
mlango na kuona ni nani kasimama hapo, lakini akasita.
Kwa muda huo dada mtu alikuwa katoa macho, akamwangalia mume wake
, na mume wake naye alibakia mdomo wazi, na nesi akanyamaza kwa muda
akitafakari nini cha kuwaambia zaidi hawa watu ili wamuelewe vyema,na huku
akijiuliza ni nani kaja hapo mlangoni na hajagongwa au kuonyesha kuwa kaondoka.
Shemeji mtu ambaye alikuwa kakaa sasa akasimama, na kuanza kukuna
kichwa mfufululizo, akainama akiwaza jambo, halafu akainua kichwa na
kumuangalia mkewe, akatembea hatua moja mbele, halafu akasimama…
Mkewe ambaye alikuwa kasimama, sasa akarudi kwenye kiti alichokuwa
kakaa mwanzoni, na kukaa, na hakusema neno kwa muda huo, akainamisha kichwa
chini, aliona mwili umemuishia nguvu, akawa katulia vile vile akiwa kainamisha
kichwa chini, kama anawaza jambo…
Mume mtu akasogea hadi pale alipokaa mkewe, akasema;
‘Twende zetu….’hiyo sauti ikawafanya wote sasa wajitambue, mke mtu
akainua kichwa kumuangalai mumewe, na mumewe, akawa kageuka kumuangalia nesi na
nesi aliyekuwa katulia, akiangalia ile
hali, akijua sasa keshawapa nafasi ya kuliwaza hilo akataka kusema neno,.lakini
sauti ya shemeji yake ikasikika ikisema….
‘Nimesema inuka tuondoke..’akasema mume mtu akiwa kabadilika sura,
utafikiri kala pilipili.
Nesi akaona asipoteze muda, akasimama na kuelekea mlangoni
akafungua mlango na kuangalia nje, hakuona mtu, akaangza huku na kule hakuona
mtu, lakini alikuwa na uhakika kuwa kuna mtu alikuwa anakuja hapo,na baadaye
kukawa kimia, alipotosheka kuwa hakuna mtu akaufunga huo mlnago na kurudi pale
alipokua amekaa akwa anawaangalia ndugu zake hao.
‘Twende wapi mume wangu, ngoja tusikilize kinachoendelea maana
mpaka sasa sijaelewa kitu…na tukiondoka hapa tutakuja kusema nini, tutajua ni
kitu gani kimeendelea huku, je…tufanyeje, ngoja tuyamalize hapa hapa tujue moja….’akasema
mkewe na kukatisha maneno kwani alihisi kuumia pale aliposhika mumewe kwenye
bega.
‘Aaaah, unaniumiza..’akalalama mke mtu.
Mume mtu sasa akawa anatetemeka mwili mzima kwa hasira, na kila
akitaka kusema neno anaishia kushikwa na kigugumizi, na mkono uliokuwa umeshika
bega la mkewe ukawa unaliminya lile bega na kumfanya mkewe ahisi maumivu na
ndio akasema;
‘Aaah unaniumiza…’ na kuutoa mkono wa mumewe kwa nguvu , na mkono
ulivyokuwa umeganda kwenye bega ilikuwa kama sumaku imenasa kwenye chuma..
Hali hii ilimshitua sana
mke wake ambaye licha ya kushikwa na mshangao, lakini aliponuona mume wake
akibadilika ghafla, mawazo yake na hisia zake zikamlenga mume wake, kwa wasi
wasi kuwa ana tatizo jingine la kiafya, ambalo linahitaji msaada!
‘Vipi baba nanihii…baba ….’ Akauliza mkewe huku akisita kumtaja
mwanae, kitu ambacho sio kawaida yao, kwani nyumbani, walikuwa wakiitana kwa
jina la mtoto, mama nanihii au baba
nanihii ….
Nesi akaiona hiyo hali, akajua kuwa shemeji yake kapatwa na jambo
na asipofanya kitu , shemeji yake huyo anaweza kupatwa na shinikizo la damu au
hata kiharusi, akasimama kwenye kutoa msaada,…
************
Huku wodini chumba maalumu
, dakitari bingwa alikuwa akiongea na mgonjwa wake, baada ya heka heka za
kumtuliza, na mama akakubali kutulia, na walikuwa wamekaa kitandani kwa huyo
mama.
‘Sikiliza mama mpendwa, mimi ni dakitari wako kwa sasa, nataka
nikusaidie , lakini sitaweza kukusaidia kama sitajua undani wa tatizo lako,
kwahiyo naomba unielezee kuhusu huyo mtoto wako, ulimpataje..mume wako ni nani,
hujaweza kukumbuka hilo…?’ Docta akauliza.
‘Docta hilo sio la kuniuliza mimi kwa sasa wa kuulizwa na huyo
nesi wenu, muulizeni huyo mtoto kampeleka wapi…’akasema
‘Lakini una uhakika gani kuacha hiyo ndoto,kuna ushahidi gani
mwingine kuwa huyo nesi alimchukua mtoto wako..akiwa hai..?’ akaulizwa na huyo
mama aliposikia kauli hiyo akainua kichwa na kumuangalai docta akasema;
‘Acha uchuro..sitaki kusikia tena hiyo kauli, …eti akiwa hai..mnataka kusema nini…haya hata
kama ni maiti, nipeni hiyo maiti yake basi, au nionyesheni hilo kaburi lake..’akasema
kwa hasira.
‘Tatizo ni kuwa hilo tukio limetokea siku nyingi, na waliokuwepo
kipindi hicho hawapo….’akasema
‘Hawapo , unauhakika na kauli yako hiyo, huyo nesi hakuwepo siku
hiyo..?’ akauliza
‘Nasema madakitari,…’akasema
‘Hilo mnalijua nyinyi, nyinyi ndio madaktari mliopo sasa na
mnachukua majukumu hayo..mimi nawaona sasa lenu moja, …..’ akasema huyo mama.
‘Ndio, sisi ni madaktari, na tunachukua hilo jukumu, lakini
hatuwezi kufanya lolote mpaka tupate msaada kutoka kwako, tunahitajia ushahidi
wa kutosha…’ akasema yule dakitari na kabla hajamaliza, yule mama akainuka, na
yule dakitari akashituka akijua huyo mama anataka kukimbia
Mara yule mama akavuta nguo, sehemu ndogo inayoonyesha sehemu ya
tumbo, na kuonyesha pale aliposhonwa, na haraka akajifunika…
‘Huu ni ushahidi mmojawapo,….unataka nini zaidi..’akasema
Docta alipaona na alishaambiwa
na dakitari mwenzake kuhusu hilo , lakini bado alihitajia maelezo zaidi kutoka
kwa huyo mama, na akitoka hapo atakwenda kuongea na nesi ili kusikia kauli yake
juu ya hilo.
‘Mama hiyo peke yake haiwezi kusaidia,maana utaulizwa ni ushahidi
gani kuwa ulijifungulia kwenye hii hospitali,…unaona hapo, kwahiyo sisi bado
tunahitajia kumbukumbu zako zaidi.’akasema docta.
‘Mkitaka usahhidi mwingine ni huyo nesi,..na kama ataendelea
kukaidi, basi msija kunilaumu, uvumilivu una mwisho wake…mulizeni kilichomtokea
asubuhi, …’akasema
‘Kwani kilitokea nini?’ akauliza docta
‘Kamuulize mwenyewe, na hao washirika zake, waulizeni huko njiani
walipokuwa wakija walipatwa na majanga gani….’akasema
‘Washirika wake..?’ akauliza docta.
‘Mhh, tatizo hata …..mimi,….’akashika kichwa huyo mama kuonyesha
kuwa kinauma, docta akaliona hilo, akagundua kuwa mama huyo kuna dawa aliakiwa
kuzipata na yeye alimchelewesha akitaka kumhoji kwanza.
‘Chukua dawa hizi zimeze….’akasema huku akimpa huyo mama hizo dawa
akachukulia maji na kumpa, yule mama akazipokea na kuzimeza, na haikupita
muda,huyo mama akawa kashikwa na usingizi.
‘Washirika wake..ni akina nani hao..?’ docta akawa anajiuliza
akitoka chumba kile kuelekea kwa mkuu wa hiyo hospitali, lakini kabla hajafika
huko akaona aende kuonana na huyo nesi ajaribu kumshawishi kama anaweza kupata
lolote kutokakwa huyo nesi.
Akiwa anatembea kulekea huko, akiwa anamuwaza huyo nesi , ni
kwanini anasita kuelezea tukio ambalo alisema linafanana na huyo mama, je
huenda huyo nesi anafahamu kuwa huyo mama ndiye huyo aliyekuwepo kipindi hicho….’akawa
anajiuliza
‘Basi kama hataki kuelezea hilo tatizo ni lazima kuna jambo, ni
lazima kuna kitu anajaribu kukiwepa…na je huyo mtoto anaye kweli, je huyo mtoto
alifariki….hapo tunahitaji majibu sahihi kutoka kwa huyu nesi….ngoja nikaongee
naye …’akasema huku sasa anakaribia mlango wa huyo nesi.
Alipofika mlangoni akasikia watu wakiongea, akajua nesi huyo
anawageni, akageuka kutaak kuondoka lakini kauli aliyoisikia ikamfanya arudi na
kuegemea mlango kusikia kinachoongewa huko ndani.
‘Mama wa mitaani, ni….?’ Ilikuwa sauti ya kiume
‘Mimi sijaelewa ni mama gani huyo?’ Sauti ya kike.
‘Ni yule mliyekuwa mkiishi naye, aliyekuwa
akiitwa mama wa mitaani, akaja kuitwa mama wa mkono wa baraka, ambaye aliletwa
hapa kutibiwa kutoka huko kwenu akiwa kaungua…’ Hiyo ni sauti ya nesi
Kumbe…..hao wageni ndio waliokuwa wakiishi na huyo mama, sasa
nimeanza kuelewa,….ni lazima nionane na hao wageni niongee nao, watakuwa
wanafahamu vyema kuhusu huyu mama.
Hakutaak kusbiria zaidi akaondoka pale mlangoni na kwenda kuongea
na mlinzi kuwa hao wageni wa nesi wakitoka waambiwe wanahitajika kwa maongezi
kwa dakitari mkuu wa hiyo hospitali, na yeye akaelekea huko kuongea na mkuu
huyo kumuelezea alichosikia.
NB Tutaona yaliyoajiri
WAZO LA LEO: Mshukuru mola wako kwa kila jambo, kwani yote
anayajua ni huenda heri ikapatikana katika shari.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment