‘Kitu ambacho nakumbukakwa huyo mtoto…eeh,
nywele…oh, mara nyingi nywele za watoto huwa hivyo..lakini cha zaidi ambacho ni
muhimu ambacho nikimuona huyo mtoto nitaweza …japokuwa…unajua yule alikuwa bado
mchanga,…ila nilimuona kwa muda mfupi tu…na zaidi nilimuona kwenye ndoto kuliko
siku ile alipotolewa tumboni mwangu…, na kwa vile alikuwa mkubwa, macho yangu
yalimuone vyema, hiyo ni miujuza ya mungu…’akasema mama
‘Nikifiria sana...., kwanini dunia hiyo ya
mwanzo, vitu vilikuwa vikubwa,…sasa nimegundua, hiyo ni miujiza ya mungu
alitaka kila kitu kiwe kikubwa ili niweze kuona vyema…ili niweze kukumbuka kila
kitu, ili niweze kumkumbuka mtoto wangu…’akatulia.
‘Kitu kikubwa ambacho hata leo nikimuona
mtoto wangu kinachoeweza kunithibitishia kuwa huyo ni mtoto wangu…ni
macho…’akasema
‘Macho…!!’ kauli hii ilitamkwa na watu
watatu wakishangaa, docta mkuu, docta bingwa, na sauti nyingine ilitoka mbali
na pale kitandani, na sauti hiyo iliyotoka mbali, iliongezea neno la kushangaa…
‘Khaaa…’ilikuwa ni sauti ya nesi
aliyeshindwa kuvumilia, na kutoa kauli hiyo ya mshangao…sauti ile na kauli ile
ilimfanya mama ashituke, ilimfanya mama ahis kitu kikimshika, akawa kama
kapigwa ganzi, akatulia… na taratibu akawa
anageuza kichwa kuangalia huko sauti ilipotokea…
Tuendelee na kisa chetu
******************
Madocta walipoona ile hali
wakajua sasa amani inaweza kuvunjika, alichofanya yule dakitari bingwa ni
kumsogelea yule mama na kukaa karibu yake ili kuzuia huyomama asimuone huyo
nesi, ili aweze kuendelea kuhadithia
ndoto yake..lakini alikwa ameshachelewa, mama akamuona nesi..
Mama macho yake yakakutana na ya nesi, japokuwa yule mama macho
yake yalikuwa ndani ya ile nguo aliyojifunika , lakini nesi aliyaona, aliyaona
katikaile hali ya hisia kuwa huyo mama akimuangalia macho yake yanakuwa kama
yanaingia ndani ya nafsi yake na kuhisi kila anachokifikiria.
Nesi aligutuka kwenye ule mshangao, akiwa ameshika mdomo kwa
kujizuia, akiwa anahis woga kwa ule mtizamo wa ule mama, akiwa anajiona mjinga
kwa kutokuweza kujizuia, akatembea kuelekea pale kwenye kitanda, na kujifanya
ndio anafika, akasema;
‘Oh mama,…nisamehe, leo nimechelewa kuja kukusalimia, nilikuwa na
majukumu mengine…’akasema na nesi aliyekuwepo hapo akifanya usafi akatoka na
kumuachia huyo nesi akiendelea kufanya yale yanayostahiki
‘Mhhh, najua ulikuwepo hapo, umesimama, ukisikiliza kile
nilichokuwa nikiongea, mukiogopa kuwa nesi akiwepo nitafanya fujo..mimi sio
mleta fujo, mimi sina lengo la kueleta fujo, mimi ninachodai ni haki yangu,damu
yangu, mtoto wangu, nesi niambie mtoto wangu yupo wapi….’akasema na nesi
alikuwa akinyisha nyosha nguo, shuka kwenye kitanda.
‘Mama..tulishakubaliana kuwa sisi tutajitahidi kutimiza matakwa
yako, lakini kwanza tunahitajia ushahidi,..tunahitajia kusikia kila kitu
unachokumbuka, hasa kutokana na hiy ndoto yako…’akasema
‘Mimi ninachotaka ni kusikia kauli ya nesi kuwa haya
ninayoyaongea, kuwa kweli mimi nilijifungua hapa, na yeye alikuwepo, na yeye
ndiye aliyemchukua mtoto wangu…’akasema
‘Nesi hebu tamka neno la kumrizisha mama….’akasema docta, na nesi
kwanza akakunja uso, akimuangalia bosi wake, akasema;
‘Bosi…..’akasema
‘Aaah, muhimu tunahitajia ushahidi..na mama anataka uhakika kuwa
mtoto wake yupo…na yupo salama..’akasema, nesi akamuangalia yule mama na
kusema;
‘Mpendwa mama….mimi siwezi kusema lolote kw hivi sasa, najua kama
kweli wewe ni muadilifu,..utanielewa kwanini nfanya hivyo…’akasema
‘Wewe unataka nikuonyeshe nini ili unisaidiki,..maana hujanisadiki
kuwa mimi ndiye yule mama, au sio….?’ Akauliza mama.
‘Mama mpendwa, wewe unasema mtoto wako anafanana na wewe, hasa
macho kwani macho yako yapoje…?’ akauliza na ile sauti ikawa kama imefanya kitu
kwa yule mama, yule mama akakurupuka,….na kukakaa kwenye kitanda, akamgeukia
nesi, akatulia akawa anamuangalia nesi…nesi akawa katulia lakini akihisi
hatari…
‘Ndio wewe….hata sauti yako ni ile ile..ndio wewe….nimekukumbuka
sahihi kabisa...ndio wewe….waambie madocta kuwa ni kweli, wewe ulikuwepo, wewe
ndiye uliyechukua mtoto wangu….ndio wewe, usikane, tafadhali….waambie kuwa ni kweli….’akasema huyo mama akionyesha
furaha fulani
Nesi akawa kimia, hakusema neno, na madocta nao wakawa wanaangaliana
na kuiangalia ile hali, na docta
akasogea pale aliposimama nesi akamwambia;
‘Wewe kubali kuwa mtoto unaye….’akasema
‘Docta mimi nitakubalije kuwa nina mtoto wa huyu mama, …hivi nyie
hamnielewi mama ninayemtambua mimi alifariki, huyu mimi simjui …’akatulia na
yule mama akawa kama anataka kusimama akasema;
‘Hutaki eeh, ina maana ulidhamiria eeh, wewe na yule docta…yupo
wapi yule docta…nani alikuambia nilikufa, kama ningelikufa ningelionekana hapa…wewe
unatunga tu ili umchukue mtoto wangu…’ akasema
‘Mama wewe kwanza unamzungumzia Docta yupi, maana madocta wote ndio
hawa hapa waulize kama waliwahi kukuona... na pili nimekuuliza kuhus macho yako tuonyeshe hayo macho yako ili tuweze kukuamini, ili hatatukumuona huyo mtoto, kama yupo tujue kuwa ni kweli, umeyaonaje hayo macho wakati muda wote umejifunika....’akasema nesi kwa hasira
‘Nesi, najua una nia njema na huyo mtoto, najua mlifanya hivyo
mkiwa na nia njema, lakini nia njema hiyo inaweza kubadilika na kuwa kitu
kingine… ili tuelewane, ili nisikuonne mbaya…nataka kauli ya kujua wapi alipo mtoto
wangu basi…macho yangu huna haja ya kuyaona sasa hivi muda utafika utayaona..lakini sio leo, au kesho,...’akasema.
‘Kwahiyo unataka kuficha sura yako ili umuibe mtoto utokomee...nani atakujua ukienda na kujibadili......halafu kwanza mimi sijui huyo mtoto unayezungumzia ni mtoto gani…'akasema halafu akamgeukia mkuu wa hiyo hospitali akasema
'Bosi unakumbuka, yule mama aliyekuja hapa na kudai mtoto akamchukua mtoto kumbe sio mtoto wake....,
kesi hiyo ipo kwenye kumbukumbu mabosi zangu nawataka muwe waangalifu na akina
mama kama hawa...jiulizeni kwanini hataki kutuonyesha uso wake....’akasema nesi
Mkuu wa hiyo hospitali alipoona hivyo akaingilia kati na kusema;
‘Sikiliza mama, sisi tunataka kukusaidia, na ili tukusaidia,
tunahitaji maelezo yako yote, huyu nesi anataka uhakika kutoka kwako…maana yeye
hajakusadiki kuwa ndiye huyo mama, kwani anavyojua yeye, huyo mama anayemtambua
yeye, alifariki, sasa wewe unayekuja kudai hayo umetoka wapi…ndio maana
tunataka kupata uhakika….’akasema docta.
‘Uhakika eeeh, nimesha mshitukia…huyu sasa nitamuona ana nia mbaya
na mimi..ndio maana akamchukua mtoto wangu, kwanini usizae wa kwako kama unaona
unataka mtoto, au huna kizazi…’akasema kwa hasira
‘Halafu nimekumbuka kitu…nimekumbuka kwenye ndoto nilikuona mahali, ..huyu nesi nilimuona pia kwenye
ndoto akiwa kule....huko nilipopatwa na haya majanga ya kuchomwa moto, nimekumbuka…hebu niambie huko ulifuata nini…niambie..nesi
niambie, mtoto wangu yupo wapi…’akasema huyo mama
‘Uliwahi kumuona huyu nesi wapi?…kwenye ndoto au kweli uliwahi
kumuona huko..?’ akaulizwa. Yule mama akawa anataka kusimama...
Docta bingwa akamuashiria nesi aondoke,….na nesi akawa anasita, lakini
nesi akaona ni heri kufanya hivyo, yule mama akaligundua hilo,naye akakurupuka
kitandani…na docta akamuwahi akamshika akasema;
‘Mama, unajua nia yako njema ya kupata haki yako inaweza
kubadilika, ukashindwa kupata unachokitaka, sisi akiwemo nesi, tunahitajia
ushahidi….nikuambie mama, siku hizi watoto wanapotea,wanaibiwa,
wanauwawa…kutokana na matukio hayo ni lazima tuwe na tahadhari, …’akasema
‘Ina maana hata nyie hamjaniamini..?’ akauliza
‘Tunaanza kukuamini, lakini bado tunahitajia ushahidi zaidi..si
tumekuambia ili kuthibitisha hayo, tutakwenda pamoja hadi huko kijijini tuone
ukweli wa hayo uliyotuambia, lakini pia, ….’akatulia na huyo mama akarudi
kitandani na kukaa, akionyesha kutokurizika
Nesi akatoka pale na kwa haraka akakimbia chumba cha kubadili
mavazi, akavaa nguo nyingine akajifunika uso, na kwa haraka akarudi kwenye
hicho chumba kwa kupitia mlango mwingine akaja na kukaa sehemu ambayo huyo mama
hamuoni, alikuwa kavaa kama yule nesi aliyekuwa akifanya usafi mwanzoni, lakini
sasa akiwa kajifunika uso.
******
‘Mama tuendelee na ndoto yetu….’akasema docta, na yule mama kwanza
alikaa kimia, akiwa kainamisha kichwa, na hata hawa madocta wakajua huyo mama hataki tena kuongea na
wakati wanajiandaa kumshawishi, kama itawezekana mara huyo mama akaanza kuongea kwa kusema;
‘Nikawa naishi kwa wale wafadhili, nikiwahudimia watoto waliokuwa
wakiletwa wakiwa na matatizo huku nikisaida kumlea yule mtoto wa pale..Cha
ajabu kabisa huyo mtoto alikuwa kanizoea kama mama yake, na mimi sikuwa na raha
bila kuwa akribu na huyo mtoto..’akasema
‘Mama wa huyo mtoto hafanani na huyo mtoto , kwa jinsi
ulivyomuona?’ akaulizwa
‘Hawafanani, ..hafanani na baba wala mama…’akasema
‘Na macho yake je..maana ulisema macho ndio ushahidi …’akaulizwa,
na akawa kama kashituka, akawa kama anataka kusimama halafu akashika mdomo,
akashika kichwa, akasema;
‘Mhh, unajua umenikumbusha kitu…yule mtoto,…mmh, mbona sura yake
inanitoka, …docta nahitaji kwenda tena huko nikamuone huyo mtoto
….tafadhali..’akasema
‘Kwanini..?’ akaulizwa
‘Nikamuone tu, nahisi..natamani…nahitaji kumuona tena..’akasema
‘Hilo tutalifanya, lakini kwanza hebu malizia maelezo yako..ya
hiyo ndoto na kumbukumbu zako..’akaambiwa
‘Mhh, unajua umenifanya niwe na mashaka, unajua, yule mtoto ni
kweli ana mama yake na baba yake, kwahiyo sikuwa makini sana kumchunguza, ila
….nahisi kulikuw na hali ya mvuto kati yangu na huyo mtoto..’akatulia
‘Kwanini unasema hivyo, kwani huyo mama hamukuwahi kuongea naye,
je huyo mwenyeji wako hana watoto wengine..?’ akaulizwa
‘Mhh, sikuwahi kuwaona, nahisi wana huyo mtoto tu, na wanampenda
sana, ni kama dhahabu kwako, zaidi ya dhahabu unajua mtu akiwa na mtoto mmoja
anakuwa anapendwa sana anadekezwa..mimi nilijitahidi kuondoa hilo, wasimdekeze,
na muda mwingi nilikuwa naye..’akasema
‘Hayo unaongea kutokana na ndoto au kutokana na unavyokumbuka..?’
akaulizwa
‘Nahisi ni …sio ndoto tu, lakini hata kiukweli nahis ilikuwa
hivyo..’akasema
‘Ukiwa kwenye hiyo nyumba uliishije na wenyeji wako..?’ akaulizwa
‘Walikuwa wazuri, walinijali,….sikuona kuninyanyapaa..ila kwa
hilotukio la kuja watu na kunkata mapanga…na kuchoma sehemu niliyokuwa
nakaa..’akasema.
‘Ilikuwaje..kama unakumbuka…?’ akaulizwa
‘Siku moja nikawa nimelala nje kulikuwa na joto ndani, nikaona
nilale nje…nikiwa hapo nje.., mara wakaja watu, wameshika mapanga…wakaniamusha
na kuniambia `wewe ni mwanga, unatulogea watoto wetu…’ nikashangaa, mimi ni
mwanga, kwa vipi maana mimi nawasaidia watoto wao, wanaoumwa, nawaombea
wanapona sasa hilo la kuwa mimi ni mchawi lilikuwa la ajabu kwangu….’akasema
‘Unajua nimeamini kitu, katika hii dunia sio wote wanaokuchekea ni
marafiki wa kweli, sio wote wanaukuonyesha wanakupenda wana nia njema
kwako..hawa walikuja kuwa marafiki na kuniona mwema, lakini kumbe wengine
moyoni walikuwa wakinichukia, wakaniita mchawi….’akasema kwa uchungu.
‘Hutaamini, sikupewa hata muda wa kujitetea…Yaani walifika na
kuanza kunikatakata na mapanga huku wakisema wewe ni mchawi, wewe ni mwanga…
‘akatulia
‘Ukumbuke hapo nilikuwa nje, nilipiga kelele, lakini sauti ikawa
haitoki, wakanivuta nguo ya usoni, na kuanza kunikata usoni, damu zikanijaa
usoni, hawakuchoka,…nikaona hapa nitakufa, nikakimbilia ndani
wakanifuata,…niliwahi kuingia mvunguni mwa kitanda…hapo hawakuniona, na baadaye
nikajikuta nimezungukwa na moto, sijui ilikuwaje, kwani nilipoteza fahamu, na
nilipozindukana nikamuona mtu akinikagua…nahisi ndiye aliyeniokoa…’akasema
‘Aliyekuokoa na huyo mtu, alikuwa
ni mtu mmoja..au wengi…?’ akaulizwa
‘Niliyemuona alikuwa ni mtu mmoja….sikuweza kuhimili zaidi,
nikaona nazama gizani, nikapoteza fahamu, sikumbuki tena kilichotokea baadaye,
nilipozindukana nikajikuta nipo hapa hospitalini..’akasema.
‘Hebu tukuulize kitu kwenye hiyo nyumba unasema mama hafanani na
huyo mtoto na je baba hafanani na huyo mtoto..?’ akaulizwa
‘Mhhh…hapana…mmh, nahisi kuna namna wanafanana..ndio ..ndio maana
sikuwa na mashaka nao, kuacha macho , kuna namna nyingine niliona kama
wanafanana..lakini hapana, siwezi kusema zaidi, mpaka nirudi nimuone huyo mtoto
tena, nashindwa kukumbuka zaidi hapo nyumbani, nashangaaa kwingine nimekuota
vyema, na kukumbuka vyema… lakini maisha ya hapo ndani na huyo mtoto nashindwa
kuelewa kwanini sikumbuki vyema..’akasema akishika kichwa.
‘Wewe uliwahi kuongea na huyo baba mwenye nyumba, au kuwa karibu
naye, au zaidi ulikuwa ukongea na huyo mama mwenye nyuma?’ akaulizwa
‘Mimi sikuwa karibu na yoyote zaidi ya huyo mtoto ,ndivyo
ninavyokumbuka hivyo, na nilikuwa namuogopa sana huyo baba, …nahisi hivyo,
nilikuwa namkwepa sana, au yeye anani kwepa …hata ikitokea kukutana naye kwa
bahati tunakwepana....nakumbuka kama hatukuwa tunakutana sana na yeye, hivyo
ndivyo ninavyokumbuka, sababu siijui. Kwakweli hapo sijui kwanini,..labda
alikuwa anafanya kazi, simuoni mara kwa mara au ndio baba mwenye nyumba anakuwa
kama mkwe....’akasema
‘Kwahiyo hukuwahi kuongea naye…?’ akaulizwa
‘Nani….?’ Akauliza
‘Baba mwenye nyumba….’akaambiwa
‘Sijui…sikumbuki vyema hapo....ila ninachokumbuka ni kuwa hatukuwa
tunakutana, nilikuwa namkwepa kitu kama hicho, au yeye ananikwepa…nahisi
alifanya hivyo kama walivyokuwa wengi wakiniogopa tofauti na mama mwenye
nyuma…unajua nakumbuka kuwa wengi wao walionekana kuniogopa, sijui ndio hicho
kilichowafanya wanihisi vibaya kuwa mimi ni mchawi..’akasema.
‘Unahisi kwanini walikuwa wakikuogopa…?’ akaulizwa
‘Mhh, ..sijui…..’akasema na kutulia
‘Nani mwingine unayemkumbuka kwenye hiyo nyumba, ..ulikuwa wewe na
hao wanafamilia tu, au kulikuwa na mtu mwingine..?’ akaulizwa
‘Mhh..nahisi..mmh,..hivi kwanini hata kwenye ndoto sikuweza
kuonyesha vyema maisha ya hapo, ni sehemu ndogo ndogo tu , na nyingine nafanya
kama kukumbuka na kuunganisha…’akasema
‘Utakumbuka tu….usijali wewe tuambie hicho
unachokumbuka…’akaambiwa.
‘Mhh, nahisi,…kwakweli hapo
sikumbuki, kwenye ndoto kuna mtu alikuwa akinipokea mtoto, sijui ni nani, sio
huyo mama wa mtoto hapana, nahisi kama kulikuwa na mtu mwingine…lakini
simkumbuki ni nani….’akasema
‘Akikupokea mtoto..kwa vipi?’ akaulizwa
‘Hapo sikumbuki, labda nilikuwa peke yangu….na hao wenyeji…labda
kulikuwa na mtu mwingine….hapo nashindwa kukumbuka, hata ndoto naona kama
iliruka sijui…, au sikukumbuka ilivyokuwa….’akasema
‘Kwahiyo kwa kumbukumbu zako walikuchukua wewe kama yaya wa kulea
mtoto wao..?’ akaulizwa
‘Sikumbuki,….sikumbuki..mmh, kuna kitu kinanijia na kutoka, …kuna
msichana….eeeh,…ndio, nimekumbuka kwenye njozi, eeh, sijui ni kwenye njozi …eeh
ndio..’akatulia
‘Ilikuwaje..?’ akaulizwa
‘Siku moja, wakati napita…nikiwa namchunguza huyo mtoto,..nahisi
alikuwa analia, kitu kaam hicho, huyo msichana, akaniita kuwa nimsaidia mtoto
maana mtoto analia na hataki kunyamaza, na yeye ana kazi, mimi nilitamani sana
nimshike huyo mtoto, sijui kwanini..basi kwa furaha nikampokea huyo mtoto, na
yeye akiwa na mashaka na mimi, akawa kasimama karibu yangu, yule mtoto alikuwa
analia kweli…, nilipomshika tu, akanyamaza..’akasema
‘Akanyamaza baada ya kumbembeleza au ulipomshika tu yeye
akanyamaza..’akaulizwa
‘Nilimchukua nikainua mkono wangu na kushika shika nywele zake
zilikuwa laini kama …singa singa…yaani kama za mzungu, mimi nina nywele za
namna hiyo ni kwa vile hamjaziona..nikasema; `mtoto nyamazaee,..linanitoka
neno, nikasema mtoto wangu nyamazaee..nakumbuka hivyo na hapo hapo akanyamaza
na kuanza kucheka..’akasema
‘Ndio hapo ukajua kuwa wewe una kipaji cha kuwaliwaza watoto
wasilie..?’ akaulizwa
‘Sikumbuki vyema..labda huyo binti…sina uhakika lakini, … nahisi
hivyo kuwa huenda ndiye aliyetangaza kwa watu, …sijui kwanini ilitokea hivyo,
nikajikuta naletewa watoto,…nikiwafanyia kama nilivyomfanyia huyo mtoto,
wananyamaza wanapona…mmh natamani nifike tena huko nikifika huko nitakumbuka
kila kitu...’akasema.
‘Na je huyu mwanaume mwenye nyumba,…unasema ndiye aliyekukuta
wakati upo kwenye hiyo nyumba kati kati ya moto..hawezi akawa ndiye
aliyakufanyia hivyo, maana ulisema unamuogopa, au yeye anakuogopa?’ akaulizwa
‘Kuwa ndiye alipanga nikatwe na mapanga na kuchoma nyumba
moto…hayo mawazo gani, mtu achome nyumba yake, maana hiyo ni nyumba
yake..hapana siwezi kabisa kumfikiria hivyo, pamoja na kuhisi kuniogopa au mimi
kumuogopa,…walikuwa watu wema kwangu…’akasema
‘Je hapo ukiwa hapo kwa wenyeji wako,…uliwahi kujifunua uso wako,
wakakuona maana unaishi nao….unakula nao, unaoga hapo, haikuwahi kutokea
kukuona sura yako?’ akaulizwa
‘Hapana, unakumbuka kwenye ndoto, niliambiwa nikionekana sura
yangu , nikionyesha sura yangu basi yatanipata makubwa,…na imani hiyo
imejengeka moyoni, ..sikutaka yoyote anione sura yangu..’akasema
‘Hakuna aliyebahatika kukuona…?’ akauliza
‘Kwa yule aliyefanya makusudi kutaka kuniona sio kwa bahati mbaya,
cha moto anakiona, niliomba iwe hivyo, maana hiyo sauti iliponiambia hivyo
nikasema je wakinilazimisha kufanya hivyo, ikaniambia kuwa hilo niwaachie
wao,…sasa sijui…’akatulia
‘Ina maana hakuna hata mmoja kwenye nyumba aliyewahi kukuona sura
yako…?’ akaulizwa
‘Mhh, nimekumbuka..huyo mwenye nyumba,..niligundua akichunguza,
hata usiku nikiwa nimelala., ananinyemelea kitandani….’akasema
‘Anakuja kufanya nini?’ akaulizwa
‘Nahisi kutaka kuniona sura yangu,lakini mimi nilikuwa na hisia,
hata kama nimelala, nakuwa kama naona, kila alipotaka kufanya hivyo ,
nilishituka nay eye hukimbia…’akasema
‘Ndio maana tunasema huyo hakuwa miongoni mwa hao waliotaka
kukudhuru…?’ akaulizwa
‘Nina uhakika sio miongoni mwao..’akasema
‘Kwanini..?’ akaulizwa
‘Nahisi ..nahisi…sijui na ndio maana nikamuota,
nahisi…nahisi,..oh, sina uhakika..’akasema
‘Anakupenda…au?’ akaulizwa, na nesi akawa kasimama akisikiliza kwa
makini akajisahau kuwa yeye yupo hapo kama mfagizi, na mama kabla hajajibu
akageuka kuangalia huko alipo huyo nesi…halafu akasema;
‘Unajua umenikumbusha kitu..pale nilipokuwa mvunguni …nilipotewa
na fahamu na nikawa naota…nahisi pale,
ndipo nilipoanza kupatwa na hizi ndoto za ajabu..zakunielekeza
kumbukumbu…nakumbuka pale, nilota nipo
sehemu na nilikuwa na mtu mwanaume, ….na nahisi alikuwa ni mume wangu, sina uhakika, ni mume ,
mchumba au rafiki, akawa ananiagiza jambo, tunapanga jambo,mimi nikamkubalia,
kuwa tutakuja kukutana,….’akatulia
‘Kukutana kwa vipi?’ akaulizwa
‘Sijui, hiyo ndoto imeanza kunitoka…lakini nahisi alikuwa na
urafiki na mimi, maana tulionekana kuwa na furaha, na hatukutaka kuachana…ikawa
kama tunaagana …kitu kama hicho,..sijui sasa maana kwa namna nyingine kihalisia
nahisi niliishi na mume mbaya, aliyenitesa, lakini kwenye hiyo ndoto inakuwa
kinyume…’akasema
‘Kwanini unahis mume alikutesa..?’ akauliza
‘Mhh, ninavyojiona, sizani nilikuwa hivi…kuna kitu, lakini siwezi
kukumbuka kabisa ya nyuma zaidi ya hiyo ndoto, na hiyo ndoto haikuwa
kubwa,ilikuwa kipande tu, nikazindukana…
‘Huyo mume kwenye hiyo ndoto, ulimuona kwa sura na kama ukimuona
tena unaweza kumkumbuka..’akasema.
‘Mhh,…nahisi hivyo, labda…lakini namfahamu,… ndio maana naiona
ndoto hiyo ya aina yake, maana nilipozindukana, huyo niliyemuota kwenye ndoto
ndio huyo niliyemuona akinikagua…’akasema
‘Akikukagua, ndio huyo eliyekuokoa, …kwenye moto au…?’ akaulizwa
na huyo mama akakaa kimia kama anakumbuka jambo
‘ Ni nani huyo …?’ akaulizwa
‘ Ni mwenyeji wa hiyo nyumba...baba mwenye nyuma....’akasema
WAZO LA LEO: Usalama na hatima ya watoto wetu ipo
mikononi mwetu wazazi, kuna wazazi ambao hawawajali watoto wao, watoto wao
wakiamuka na kwenda kucheza au shule hawana habari ya kuwafuatilia, watoto hawa
wanakutana na makundi mabovu, wanaharibiwa kiakili, wanageuka kuwa wakorofi na
wazazi wakioulizwa, wanakuwa wakaidi,..mtoto anakuja kuwa mwizi..mzazi
akiambiwa anakaidi..mwisho wake mtoto huyu unakuwa nini,..kama sio jambazo..chanzo
ni nani , chanzo ni wewe mzazi. Tunaambiwa samaki hukunjwa akiwa bado mbichi,
akikauka hutamuweza tena….
Ni mimi:
emu-three
1 comment :
Great website you have here but I was curious about if you knew of any
user discussion forums that cover the same topics discussed here?
I'd really love to be a part of online community where I can get opinions from
other experienced individuals that share the same
interest. If you have any recommendations, please let me know.
Kudos!
Also visit my blog post kw1 - -
Post a Comment