Nesi akiwa nyumbani kwake....ulikuwa ni muda wa mapumziko na wakati anataka kujipumzisha mara
akasikia simu yake ikiita,kwa haraka akaichukua simu yale ilikuwa mezani, na
kuangalia ni nani aliyemmpigia, akakuta ni ile namba ya nje, akaipokea kwa
hamasa, akiwa amesimama, akasema
‘Halloh nani mwenzangu…’akauliza akiwa anajaribu kuwaza ni nani
huyo
‘Mimi mliyekuwa mkimuita Docta Kijana…’sauti ikasema na nesi
kusikia hivyo akapanua uso kwa furaha na ha akajikuta akisema;
‘Mhh, Docta Kijana,
hatimaye nimekupata....!’ nesi akajikuta akisema hivyo huku akitabasamu
kama vile anamuona huyo anayepiga simu akajaribu kuvuta taswira ya dakitari
huyo…
‘Unasema hatimaye umenipata, ...kwa vipi?’ sauti ikauliza na nesi akatikisa
kichwa kama anakubali kitu, kuwa ndio mwenyewe, akasema;
‘Ni siku nyingi docta na nimekuwa anikikutafuta sana lakini sikuwa
na namba yako..yaani ulichonifanyia, unaondoka bila kuniaga, nilikukosea nini
..’akasema nesi, na kukawa kimia kidogo.
‘Samahani kwa hilo, yaliyotokea ilikuwa ni ghafla..na sikuwa
na nafasi ya kuagana, …yaani we acha tu,
binadamu wana roho mabaya sana…hapa nilipo mawasiliano ni mabovu, kwahiyo
..hatutasikilizana vyema…’akasema
‘Sasa namba yangu uliipataje..kama uliweza kuondoka bila kuniaga
na bado ulikuwa na namba yamngu muda wote huo kwanini usinipigie simu kuniambia
?’ akauliza nesi
‘Mimi nilipewa namba yako na….nesi yule rafiki yako..’akasema
‘Oh, kumbe mnawasiliana naye?’ akauliza nesi akiwa anakunja uso
kwa kutokufuraha kauli hiyo
‘Hapana…imetokea kila nikipiga simu hapo hospitalini anayepokea ni
huyo sister...na jana ndio kaweza kunipa namba yako..’akasema.
‘Sawa najua yule ni rafiki yako sana…’akasema nesi akiwa
keshatahayari.
‘Hapana sio rafiki yangu….,kama alikuambia hivyo
amekudanganya..siku ile ya mwisho alikuja kuniambia hivyo kuwa ananipenda..anataka
tuwe wapenzi,..nilishangaa kidogo, alisema mengi..lakini sikuwa na muda wa
kuongea naye, maana nilikuwa na mambo mengi kichwani, ..nilifurahi tu kwa vile
ni yeye aligundua barua yangu ikiwa imefichwa..’akasema
‘Ilikuwa imefichwa na nani?’ akauliza nesi
‘Mmmh, ni hadithi ndefu, …ni huyo aliyekuwa mkuu wa hiyo hospitali…sijui
kwanini alifanya hivyo, na bahati nzuri huyo nesi rafiki yako akaigundua hiyo
barua na kuniletea,..ilionekana ilifika muda tu, na huyo mkuu akawa kaiweka
kwenye droo za meza yake..nilipoipata nikamuuliza kwanini kafanya hivyo akadai
yeye hajawahi kuiona..basi nikaona hakuna shida, …ndio huyo nesi akatumia
nafasi hiyo kuniambia ammbo yake…’akasema
‘Oh pole sana kumbe ndio ilikuwa hivyo..huyu mtu kumbe mbaya sana
..ndio maana akanifanyia visa na kunitega….kumbe, ningelijua nisingelikubaliana
naye..’akasema
‘Alikufanya nini?’ akauliza
‘We acha tu,….ila kanisaidia nikaenda kusoma…’akasema nesi
‘Hongera, najua sio bure..yule mtu hafanyi kitu bila gharama, kwa
muda mfupi niliokaa hapaoo nilimgundua kuwa ni mtu mbaya…mbinafsi, anacheka
mdomoni lakini moyoni ana roho mbaya….nilikuja kugundua kuwa anafanya biashara
ya dawa, nilimfuma siku moja akishirikiana na yule nesi mkuu, akaniambia eti
wanazipeleka bohari zina makosa…kumbe ndio biashara yao,….wanaiba dawa za
hospitalini na kuziuza kwa wenye mahospitali au maduka ya dawa mitaani’akasema
‘Mhh, …kumbe ulikuwa unajua hilo, na kumbe walikuwa wakishirikiana
na nesi mkuu..ohh, ndio maana kumbee…’akasema nesi akionyesha mshangao.
‘Yah, yule alikuwa mtu wake wa karibu sana, na ndiye aliyekuwa
akimkuwadia….najua yote hayo, lakini niliona kwangu haina maana, …nikawa kimia,…niligundua
kuwa hiyo hospitali ina viongozi wabovu, wenye tamaa binafsi, …ndio maana
nilitaka usome uhame hapo,..’akasema
‘Mhh, mbona hukuniambia hayo mapema..’akasema nesi .
‘Sikutaka kukuingilia maisha yako, na kujiingiza kwenye umbea,
sikuja hapo kwa kazi hiyo…na yule rafiki yako ndiye alikuwa akijaribu sana kuwa
karibu na mimi, nilimkwepa sana…hadi siku ya mwisho aliponieletea hiyo barua…unajua
nilimshukuru sana, maana bila yeye ingekuwaje, lakini sikuwa na muda naye..ni
hivyo tu…’akasema
‘Mhh, mbona kaniambia kuwa mnaelewana sana..’akasema
‘Sio kweli….mimi nilishakuambia msimamo wangu..sasa sister
sikiliza naona muda utakwisha kabla sijakuambia la msingi…, mimi nilikuwa
nakupigia simu kukuulizia maswala ya yule mtoto… na kumbukumbu nyingine na ….’akasema.
‘Mtoto gani , mtoto wetu…?’ nesi akajikuta akisema
hivyo.
‘Mtoto wetu!?’ akauliza docta kwa mshangao.
‘Wewe umesemaje..?’ akauliza nesi
‘Kuna yule mtoto uliyemchukua wewe ukasema unampeleka kwa dada
yako. Unakumbuka?’ akasema Docta Kijana,…
‘Mhh, ndio nakumbuka…..’akasema nesi huku akikaa vyema kwenye kiti,
na kukunja nne.. moyoni akiwa na hamasa ya kutaka kujua mengi na kuongea mengi
ikibidi.
‘Ni kweli ni siku nyingi, lakini hata mimi nilikuwa nahangaika
kukutafuta….kwanza nilimpata nesi mwenzako, ..naona kila nikipiga yeye anakuwa
hewani, yeye ndio mpokeaji simu siku hizi…?’ akauliza
‘Mhh..hapana anasaidia saidia tu kama yule muhusika hayupo,..’akasema
nesi
‘Basi ….yeye mara ya kwanza nilimuomba niongee na wewe akasema upo
masomoni, na ….wewe na huyo mkuu ni ..marafiki,..au….nikamwambia anipe namba
yako akasema hana…na komputa yangu niliyokuja nayo huku ambayo niliweka namba zenu
na kila kitu ilinigomea, imeharibika…nahisi wakati naondoka kwa haraka
niliigonga mahali….’akatulia
Nesi, aliposikia hivyo kuwa hata huyo dakitari alikuwa akimtafuta moyo
wake ukawa unamdunda isivyo kawaida…kumbe mwenzake aliwahi kuambia atoe namba
yake lakini hakupenda kuitoa…akawa na fundo, akapanga akitoka hapo atakwenda
kupambana na huyo aliyekuwa rafiki yake kwanini alimfanyia hivyo…alijikuta
badala ya kusikiliza anachoulizwa akajiona anajawa na hasira, na alipoligundua
kosa lake akasema kwa sauti ya kukwaruza hadi iakbidi akohoe kwanza….
‘Sijui hata nisemeji, nina hamu sana ya kuongea na wewe nina mambo
mengi ya kukuambia, mimi nilijua umeshanisaahu,..kumbe ni huyu aliyekuwa rafiki
yangu, ngoja, nitakutana naye…hebu nikuulize hujaoa mke wa kizungu huko, ...?’akajikuta
amesema hivyo.
‘Sister acha utani wako , mimi nipo huku kwa ajili ya kusoma, ….bado
muda wangu wa kuoa kabisaaa..bado sana….’akasema na mara kukawa na mawasiliano
mabovu, na docta akawa anaita halloh, na nesi naye halloh, na baadaye, docta
akasema;
‘Halloh, sister upo,..naona kuna mawasiliano mabovu, …ila cha
muhimu nilikuwa naulizia kuhusu yule
mtoto…je hajambo?’ sauti ikauliza tena lakini nesi akawa hakusikia vyema,
akajua anasalimiwa, ila alisikia kitu kama mtoto, akasema;.
‘Sijambo docta,….unasema nini, kuhusu mtoto, …yupi ooh..mtoto wetu…?..aah
yule mtoto, tena hilo ndilo nataka kuongea na wewe…?’akasema nesi
‘Ana matatizo yoyote?’ akauliza docta
‘Hana matatizo, yupo kwa dada yangu… analelewa na watu wenye
upendo, kwahiyo hilo lisikutie wasiwasi, ila nilitaka kukuulizia kuhusu yule
mama, aliyetoroka hospitali, mama mzazi wa huyo mtoto, kumbukumbu zake zipo
wapi…’ akauliza harakaharaka.
‘Kwanza nikuulie kwanini unarudia kusema mtoto wetu,..kwani tulikuwa na mtoto mimi na wewe, mimi ninayemzungumzia ni yule mtoto ambaye
alizaliwa na yule mama, halafu mama yake akatoweka.....hivi ilikuwaje badaye?’akaulizwa.
‘Yule mama …..mm hata sijui nikuambie nini…yametokea mengi sana…’akasema
nesi na mara kukawa hakuna mawasiliano, na baadaye mawasiliano yalipokuwa
shwari docta akasema
‘Oh, nimkuelewa…,japo mawasiliano sio mazuri....’akasema docta
‘Sasa docta mimi huku kuna tatizo …na tatizo hilo linahitajia zile
kumbukumbu za yule mama na mtoto wake zipo wapi?’ akauliza
‘Kumbukumbu zile nilikuambia kuwa niliziweka kwenye kabati
linalohifadhiwa nyaraka muhimu…lilikuwa kabati namba tano , yale makabati
yalikuwa na namba…na huyo mama imekuwaje?.’akasema na kuuliza lakini swali la
mwisho nesi hakulisikia vyema, nesi akasema;
‘Makabati yale yalihamishwa na nyaraka karibu zote zimepotea..na
zilizopo zimeharibika kabisa… na umeulizaje tena..?’akasema nesi
‘Mhhh...hilo sasa ni tatizo , hata sina jinsi nyingine ya
kuzipata, maana nilijua hiyo ndio sehemu salama....nahitajia kumbukumbu za yule
mama ndilo muhimu …’akasema docta.
‘Lakini wewe siulisema…kwenye komputa yako kuna kumbukumbu..ooh,
ndio umesema imeharibika, bahati mbaya, sijui itakuwaje…’akasema nesi, na
alihisi kama hakuna mawasiliaono akawa anasema halloh, hallow na mara , docta
akasema;
‘Halloh, nipo, nasema hivi…kama waliondoa kumbukumbu zilizokuwemo
kwenye lile kabati.. basi kuna mahali wamezihifadhi, labda kwenye maboksi ya
kumbukumbu za zamani mwambie muhusika akajaribu kuzitafuta huko atazipata
tu…’akasema
‘Hazipo….na hapo kwenye store ni nyumba ya panya,..kiujumla
kumbukumbu hizo zimepotea kabisa....’akasema nesi.
‘Oh, nesi kuna siku niliwapigia hapo hospitalini, kuhusu
kumbukumbu za zamani kipindi kidogo, kwasababu komputa niliyokuwa nimehifadhia
hizo kumbukumbu iliharibika, na kulikuwa na kumbukumbu zangu nyingi,..na
zinenisaidia kwenye masomo yangu,..wakasema watanitafutia…..lakini kila
nikipiga inakuwa jibu ni hilo hilo…’akasema!
‘Huwezi kuzipta, hilo mimi nakuambia, naona kama ni njama za
kuhakikisha kumbukumbu zote za zamani hazipatikani..’akasema
‘Njama, kwanini njama?’ akauliza docta
‘Kuna mambo mengi yametokea, hata wale viongozi wa zamani hawapo
tena..ni kutokana na utawala wao mbovu, …na mengi hata sitaweza kukuambia kwa
leo..’akasema nesi
‘Oh, basi itabidi niingie gharama tu ya kuitengenezesha komputa
yangu ya zamani…maana kuna mambo yangu muhimi sitaki yapotee…na humo nitaweza
kupata kumbukumbu zote za huyo mama…mimi nilijua tu, huo uatawala utakuja
kuondoka, …kulikuwa na mambo machafu hapo, nilijaribu kutoa ushauri ndio nikawa
adui….’akasema
‘Pole sana…docta sasa hebu niambie yule mama….anafananaje usoni…?’
akauliza nesi
‘Macho…’sauti ikakatika..na simu ikawa haipo hewani, akarabi kuita
lakini wapi, akaweka salio akapiga ikawa haiptaikani kabisa.
`Macho yana nini….?’ Akauliza nesi akiwazia ni kitu gani docta
alitaka kumuambia, na akaanzia na neno macho.
‘Macho….ana maana gani alitaka kuniambia nini kuhusu macho…?’nesi akawa anajiuliza, akaona arudi wodini tena
kumuangalia yule mama mwingine anayemshuku kuwa huenda …maana huyo mama
wanaymezngumiz ani marehemu, na haikuwa n hata haja ya kumuuliza docta,
akakumbuka kuwa hakuwahi kumuambia huyo docta kuwa huyo mama ni marehemu,
alihis huenda alishaambiwa na hao aliowapigia mwanzoni.
Kwa vile siku hiyo aliipanga rasmi kwa kuongea na huyo mama
mwingine ambaye aliungua na moto alitaka kujua kama alikuwa na mahusiano yoyote
na yule mama aliyewahi kufika hapo akapotea, na kujulikana kuwa amefariki kwani
kwa uoni wake wanafanana sana.
Basi akaingia wodini, na kwa muda huo huyo mama alitoka nje, yeye
alikuwa hajifuniki kujificha maana hata yeye alikuwa na makovu ya kuungua
usoni, na uzuri wa huyo mama, yeye aliweza kutembea tembea, basi alipoona
hayupo, akaona atoke nje, atarudi baadaye kwani yule mama wa mitaani alikuwa
amelala, hakutaka kumsumbua, akamtupia jicho la haraka na kuondoka humo wodini,
na wakati anatoka akakutana na huyo mama mwingine akiwa anarudi huko alipokuwa,
na mazungumo yakaanzia hapo.
Nesi akajaribu kumuelezea kuhusu kitu anachotaka kumuulizia,
kuwa hapo kipindi kidogo kulikuwa na mama alifika hapo kujifungua ,lakini mama
huyo alitoroka na baadaye wakapata taarifa kuwa amekufa, sasa je hakuwa an
ndugu wa namna hiyo
‘Hapana..mimi kwetu ndiye mkubwa na wengine wote ni watoto wa
kiume, bahati mbaya nikaja kuolewa na mume mkorofi mlevi..ndugu zangu wa kiume
walinikata sana nikawa mbishi, na matokea yake ndio haya..’akasema kwa uchungu.
‘Mhh, mnafanana sana na huyo mama nilijua ni wewe..’akasema nesi
‘Hapana siwezi kukudanganya sio mimi…nilisikia mkiongea na
yule,..yule mama ana matatizo gani, maana usiku anapiga kelele..na jana na juzi
akilala, anakuwa kama anaongea peke yake, masikini mdada naye kaungua kama
mimi,….’akasema kwa uchungu
‘Kwani unamfahamu huyo
mama…’ akauliza nesi
‘Namemfahamia hapahapa tu..huwa namuita dada…’akasema
‘Hivi niambie kwanza wewe ilikuwaje..mana sijawahi kupata muda wa
kuongea na wewe vyema, huenda ukanisaidia jambo?’ akauliza nesi
‘Mimi niliunguzwa na maji ya moto na mume wake, mume wake akilewa
anakuwa na hasira za haraka haraka, …ameshauriwa asinywe, lakini ndio
hivyo..basi siku hiyo, aliporudi toka ulevini, akakuta chakula hakijaiva na
maji ya kusongea ugali yapo jikoni yakiwa yanachemka..’akatulia akikunuja uso,
kama kuhisi hiyo hali.
‘Basi mume wangu kutokana na ulevi wake, na hasira akayachukua
yale maji kutoka jikoni akanimwagia…na yeye katika kunimwangaia yakamwagikia..maana
aliungua mkono,…akahisi kuungua vidole, akaachia sufuria, maji yakamuunguza na
yeye mwenyewe, halafu akapepesuka na kudondokea jikoni, akaungua vibaya sana
hata kuliko mkewe ..’akasema huyo mama.
‘Kaadhibiwa kwa ubaya wake..’akasema nesi
‘Ni zaidi ya kuadhibiwa ukimuona utamuonea huruma..’akasema
‘nimeshamuona , sikujua ndio mume wako….ni yule mwanaume
aliyeungua vibaya sana na ana pingu mkononi?’ akauliza nesi
‘Ndiye mume wangu ndio ana pingu mkononi kwani ana kesi ya kujibu….,
sasa hivi nilitoka kumsalimia, lakini ndio hivyo yupo kwenye ulinzi, …siunajua
tena mambo ya kisheria, …najua akiruhusiwa tutayamaliza kienyeji maana
aliyafanya hayo kwa ulevi tu…mimi nimeshamsamehe’akasema huyo mama kwa sauti ya
upole, anaonekana ni mama mpole sana.
‘Yaani upo tayari myamalize kienyeji, ..kwa jindi alivyokufanyia
hivyo…? mtu kakumwangalia maji ya moto, huoni angekupofua kabisa…., hapana
usikubalia, kwanini nyie akina mama mnaonewa halafu mnakuja kukubali kirahisi
hamuoni mnafuga huo ugonjwa,..?’ akadadisi yule nesi.
‘Mhh…sasa mtu nimeshazaa naye…na hata nikirudi kwa ndugu zangu
hawatanipokea tena..na nikifanya hivyo watoto wangu watakuja kuishi na mama
mwingine huenda asiwepende…hapana ni heri yaishe kienjeji, najua atakuja
kujirudi na kuacha huo ulevi, …na nitarudi kwanini, maana nilishawageuka ndugu zangu tulipanga
nisiolewe, mimi nikatoroka..,..sikuwasikiliza, ni bora tu niishi na mume wangu maana nimeshamzoea, tatizo ni
ulevi tu… na ipo siku litakwisha tu…’akasema
‘Haya hilo ni lako, kama upo taayri kufa kwa ajili ya huyo mlevi
usija kujutia baadaye…Hebu niambia kuhusu jirani yako pale pembeni unamuonaje?’
akamuliza nesi, na yule mama akamuangalai nesi kama vile anataka kujua ni nani,
lakini akakumbuka jirani yake humo ndani ni mmoja tu, akasema;
‘Oooh , yule mama, unajua mwanzoni alikuwa haongeia kabisa, lakini
amekuwa rafiki yangu maana kila ninacholetewa ninampa nay eye….sasa kawa rafiki
yangu kweli, na jana akanisimulia kuwa ana uhakika alikuwa na kichanga’akasema
‘Kichanga, una maana mtoto?’ akauliza
‘Ndio …lakini mazungumzo hayo hayakuoendelea , kwani wakati
tunaongea dakitari alikuja, tukakatisha mazungumzo na sikuwahi kumuulizia tena…nakumbuka
kitu kama hicho…’ akasema huyo mama
‘Alisema aliwahi kujifungua hapa, kwenye hii hospitali? ….au
ilikuwa hospitalini nyingine…?’ akauliza nesi akiwa na shauku sana.
‘Mimi sijui, sikuweza kumdadisi zaidi..kama nilivyokuambia
dakitari alifika, basi ikabidi tukatishe mazungumzo yetu…, kwani vipi mbona
unamuulizia sana mambo yake…’ akasema huyo mama.
‘Mhh, unajua huyu mama ananichanganya, hata kama alipoteza
kichanga, kwanini aninyoshee kidole mimi na hakuwahi kukuambia alipotezaje,..au
ilikuwa mara ya kwanza kuongea naye mazungumzo kama hayo..?’ akauliza nesi
‘Si kama nilivyokuambia kipindi cha nyuma alikuwa haongeai
kabisa..sasa kuanza kuongea ni juzi na jana, ..juzi ilikuwa kuulizana hali tu...jana
ndio kasema hayo, na sikuwahi kumdadisi zaidi..’akasema..
‘Mhh, kuna kazi, nilijua nitayamaliza hayo,…. lakini kama bado
anaendelea na msimamo wake huo nahisi kuna jambo,..’akasema nesi na yule mama
akawa anageuka kutaka kuondoka, na nesi akamuuliza
‘Pamoja na hayo ana kitu gani kingine cha ajabu, na je uliwahi
kumuona sura yake?’ akamuuliza
‘Sura yake hapana…anajichunga sana asionekane sura yake…ila anaota
sana usiku anakuwa kama anaongea na mtu hivi
‘Anaota, unajuaje kuwa anaota….?’akasema
‘Maana unasikia sauti na mazungumzo..mara anambembeleza mtoto…wkati
mwingine kama anajibishana na watu…., husiki sauti ya mtu mwingine unasikia
yeye akijibu au kuongea na mtu, ukiangalia huoni huyo mtu mwingine..sasa hapo
naona kama anaota..’akasema
‘Mhh, ndio zake hizo docta ansema ndio dalili za kurejea
kumbukumbu zake…je hakuna wimbo wowote anaimba..? ’akauliza nesi
‘Kuimba wimbo!?’ akauliza huyo mama kwa mshangao
‘Huwa alikuwa kama anaimba wimbo hivi akisema anamtaka mtoto wake…’
akasema
‘Anaongea kitu kama hicho, na docta alipokuja jana wakakaa wakawa
wanaongea vizuri tu, na alikuwa akimsimulia kuhusu huyo mtoto wake..na
inaonekana wanaelewana vyema na huyo dakitari…kiujumla huyo mama kabadilika
kabisa, anaongea kama kawaida….’akaambiwa
‘Kuhusu huyo mtoto, ina maana hata docta keshamini kuwa huyo mama
ana mtoto na kachukuliwa hapa?’ akauliza
‘Kwa jinsi nilivyosikia …docta keshaamini kuwa kweli huyo mama ana
mtoto, na docta akaahidi kuwa mtoto wake atapatika tu,..sasa sijui ni hapa au
ni wapi…’akasema huyo mama, na nesi akahisi kuchanganyikiwa, akageuka kuangalia
kule wodini, akasema
‘Ngoja nikaongee na huyo mama aniambie mwenyewe kuhusu huyo mtoto
maana sasa atanichanganya, mimi sijawahi kumchukua mtoto wake…kwanini aendele
kusema mimi ndiye nimechukua mtoto wake…sasa ataniambia kama kachanganyikiwa
itaonekana wazi..sikubali…’akasema na kugeuka kurudi wodini.
Na kabla hajaingia ndani kabisa akamuona yule dakitari mkuu, akija
na yule dakitari alionekana kunyiosha mkono kama ishara kuwa huyo nesi amsubirie
na nesi ikawa kama hamsikii akawa keshaiingia wodini tayari kwenda kupambana na
huyo mama…
Na wakati anakaribia kitanda cha huyo mama mara simu yake ikalia,
akawa anaipuuza lakini alipoona inaita sana, akaitizama maana alikuwa nayo
mkononi, akaona ni namba ya ndugu zake kijijini, akawa kasha fika kitandani,
akaona ngoja aisikilize kwanza;
‘Halloh, …’akaita na aliyekuwa hewani ni dada yake, akasema;
‘Nina habari nzuri…lakini pia tunataka kuja kukutembelea na mtoto, ..tumeona tuje mtoto amuone mlezi
wake. Maana analia lia sana...’wakasema
‘H-h-hapana…’akasema na mara docta akawa ameshafika,…
WAZO LA LEO:Kutoa taarifa za uwongo ili kujipatia
kitu, au kuonekana wewe ni zaidi au kwa ajili ya kujulikana na watu ili kupata
kura, umaarufu… au jambo lolote huo ni wizi, na sio tabia njema, na tabia hiyo
inaonyesha wewe humuogopi mungu, wewe sio mwaminifu..na haufai kuongoza jamii.Kuna
watu wana tabia hizo na wanaona ni jambo rahisi tu kumzulia mwingine uwongo, au
kuzua jambo, kuahidi uwongo,… ili tu kuonekane tunaweza…au sisi ni zaidi, ..au
kitu fulani hakifai , kisipitishwe, hii ni tabia iliyojengeka sasa ya
propaganga potofu, tukumbuke tabia hiyo ni unafiki na njia za mnafiki ni fupi
tu..
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment