Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, March 26, 2015

NANI KAMA MAMA-49


‘Sasa nesi nilichokuitia hapa ndio hicho, ila kwanza wewe mwenyewe uonyesha upo tayari kwa hilo…na hatua ya pili, ambayo sio shida sana, ni kubadili kila kitu, hilo sio tatizo kwangu…’alisema dakitari mkuu.

‘Unaona, nia ni kuonyesha kuwa huyo mtoto hakuzaliwa hai kwa huyo mama, maana mama mwenyewe hayupo..keshafariki… ,’akasema na kumuangalia nesi, nesi ambaye alikuwa katoa macho ya kutoamini hicho anachosikia.

‘Na nesi kama ulivyosema, dada yako alikuwa akihitajia sana mtoto au sio, mungu kampa mtoto kwa njia rahisi tu, lakini urahisi huo unategemea na wewe mwenyewe,kwahiyo ukikubali basi, dada yako ndiye mama halali wa huyo mtoto, je wewe unasemaje,…kwanza upo tayari kwa hilo?’ akaulizwa, nesi ambaye alikuwa akimuangalia huyo mkuu bila kummaliza akajikuta akisema;

‘Nipo tayari kwa vipi?’ akauliza nesi akiwa katahayari, haamini,…mkuu ambaye anafahamika kuwa ni mtu asiyetaka uzembe, mkali kwa mambo yasiyofuata sheria, japokuwa ana mapungufu yake ambayo nesi mara nyingi alikuwa anaona kama wanamsingizia tu,.. leo hii anatakamka hayo mbele yake…, hakuamini, akawa hata haelewi…kumbe ni kweli…mhh!.

Lakini hata hivyo kwa hali ilivyo hakuwa na la kufanya, kwanza alijiuliza hayo yote yanafanywa kwa ajili yake, na familia yake kwa malipo gani, ina maana kuna kitu atatakiwa kukifanya kufidia hayo, au….akasubiria jibu la mkuu wake…

Jibu ambalo lilimuweka njia panda,…lakini alipotajiwa kwendqa kusoma, ooh, akawa kaswajika, na ndio ukawa mtego wake… na kilichotokea ni kujitoa mhanga..kwa ajili ya mtoto, kwa ajili ya ndugu zake, ambao walishajua kuwa huyo mtoto ni wao…,

Sasa leo siri ya miaka hiyo siri iliyojificha na yenye mambo mengi, siri ambayo akiikumbuka inamtonesha moyoni, na kumpa wakati mgumu…siri ambayo ilitakiwa iwe siri…inahitajika kujulikana….itakuwaje?

Tuendelee na kisa chetu

***************
Nesi akiwa kazama kwenye mawazo, na maneno yenye kumchomo moyo yakawa yanasikika masikiono mwake kwa sauti ya kuwewesa…..

‘Nesi …umesikia, wewe sasa kula maisha, ukiwa na mimi usipate shida….unaonaeeh, sasa unakwenda kusoma, ila kumbuka; …..’ hiyo ila kumbuka ikamfanya ajaribu kukatisha hayo mawazo, lakini sauti ile bado ikawa na nguvu kichwani

‘Nesi…hakikisha siri hii inakaa moyoni mwako, maana ikijulikana tu, mmmh, umeniharibia kazi..na ama kwa mwengu anaweza kukufanyia visa ukafungwa na kupotelea jela..ujue nesi mimi nimeyafanya haya kwa vile nakupenda,…eeh, umeona mpenzieeh… ‘ sauti ikazidi kupenya masikioni mwake, huku machozi yakianza kumtoka. Akasimama na kushika kichwa na kuziba masikio, lakini wapi…sauti ile ikawa inajirudia, …..

‘Siamini..kwanini mimi…’akawa analia, baadaye akatulia, akajiuliza analia nini, maana hayo yalishapita, hata akilia machozi ya damu hayo yalikuwa yameshafanyika, ni kama kutamani maziwa yaliyomwagika ardhini na kunywea mchangani…

 Sasa akatuliza kichwa na kuanza kuingia kwenye hali halisi akajiuliza;

‘Je nilifanya makosa,..ndio ni makosa, lakini kulikuwa na njia gani nyingine ya kuepuka na lile tatizo…sikuwa nalo, sasa…..’

Kiukweli siku ile alijiona kama msaliti, pamoja na kuwa hakufanya hivyo kwa ridhaa yake, maana ilikuwa ni kuona huyu kanifanyia hivi nitamlipa nini, na pia, na kwa ajili ya mtoto, ni kwa ajili ya dada yake…akajuta , lakini majuto yakawa na mjukuu

‘Nimeshamsaliti niliyempenda..’akasema, hata hivyo akajiuliza huyo aliyempenda kweli na yeye anampenda hivyo hivyo…`aaah, hata sijui, …imebakia kuwazia hivyo, tu maana yupo moyoni mwangu namuwaza yeye kila siku, japokuwa kaondoka hata bila kuniaga….sasa huyu mtu kanitega, nimekusaliti mpenzi , usiyependeka…nisamehe…’

Mara ile sauti ya kukera ikasikia masikioni mwake tena, ..ikiwewesa, ikawa na harufu ya ulevi, ikasema;

‘Unasikia nesi, …kama ningeliachia hili liende inavyotakiwa kisheria, basi ujue wewe ungeishia jela, ungefungwa, unaonaeeh, lakini sikukubali, kwa vile mapenzi yangu kwako ni makubwa, …huyu aliyekudanganya yupo wapi, fimbo ya mbali hata siku moja haiwezi kuua nyoka…’kauli yenye kukera ikapenya ubongo wake

Na alikumbuka kuwa alitaka kumuambia kuwa yeye atapenda wangapi maana kauli kama hiyo kaeshaitamka kwa manesi wengi waliowahi kutembea naye.

‘Na ujue nesi hapa hospitalini, wewe peke yako ndiye ninayekupenda sana…wengine wanajipitisha tu kwangu, siwataki kabisa….unaona kama ingeliwezekana kuoa mke mwingine ningekuoa wewe, lakini imani yangu haitaki hivyo…’akasema

‘Lakini unazini je imani yako inataka uzini..?’ akamuuliza, lakini hakupata jibu, alisikia maneno mengine tofauti

‘Na ninachokupendea zaidi ni kuwa wewe ni mtu mwenye huruma sana..na kwahiyo usingelipenda mtoto kama yule aje kuteseka….’akasema sijui hakusikia swali lake au alifanya hivyo kupotezea.

‘Na pia, umesikia mwenyewe alivyosema yule mkuu wa kituo, yule namuamini sana tuna mambo mengi mimi na yeye..unakumbuka alivyosema…, kasema familia ile anapotoka huyo mtoto, alipokuawa kaolewa huyo mama, ni familia yenye maisha magumu…sasa utafurahi huyo mtoto aende kuteseka…unaona kwahiyo umefanya maamuzi sahihi…usihuzunike kwa hili, naomba ubadili muelekeo na kunipenda mimi tu…’akasikia sauti hiyo ikiendelea kupenya kichwani.

‘Nitakupendaje na wewe una mke wako, na imani yako haitakia kuoa wake wawili..?’ akauliza na hata hilo swali halikupatiwa jibu, ni kama anaongea na kitu kilichorekodiwa kazi yake na kuongea yale yaliyomo tu….

‘Sasa mimi na wewe ni kitu kimoja na sitakuangusha…kesho utaondoka kwenda chuoni, ..ukirudi hapa aaah, wewe ni bosi, na tutakuwa karibu karibu,..unaonaeeh, haya ndio maisha…mke wangu hana shida, hatufuatani yeye ana maisha yake na mimi yangu…’sauti ikizidi kumkera akilini

Alipokumbuka hilo tukio, na maneno hayo yakipenya kichwani kwake, akahisi kichwa kinamuuma, akahisi kichefu chefu, anakumbuka siku ile alipotoka pale, alikimbilia maliwatoni akatapika sana…alitapika mpaka nguvu zikamuishia..na toka siku ile kila akikumbuka lile tukioa, akawa anahisi kutapika,..kichefu chefu… ingelikuwa ni mtu ambaye sio mtaalamu angelihisi ana uja uzito.

************

Nesi akijaribu kuziondoa hizo kumbukumbu kichwani, alitoka mle ofisini na kupita chumba cha huyo dakitari bingwa ambaye kwa kipindi hicho pia, alishikilia nafasi kuu kama kiongozi wa hospitali, akajua hatima ya maisha yake imeingia kwenye mtihani mwingine, kwa matu kama yule yule…

Ni kweli ulikuwa ni mtihani,  mtihani ambao unaweza kuwa kama ule, japokuwa sasa anajiamini, hawezi kuingia kwenye mtego mwingine, mwenye akili hafanyi makosa mara mbili,  …

‘Sasa nitafanyaje, na nianzie wapi…’nesi akajiuliza swali, akakumbuka moja ya mafunzo yake kuwa unapojikuta kwenye wakati mgumu wa kufanya jambo, kitu cha kwanza ni kukaa chini na kulitafakari hilo jambo,kama kuna muda wa kufanya hivyo, weka mipango, na mikakati..ikibidi andika utaratibu hatua kwa hatua…kama hakuna muda, chukua hatua na matokea yatakupa muelekeo ulio sahihi…

Kwanza akahakikisha majukumu ya watu yamekamilika akapitia kwa wagonjwa na kuhakikisha kazi zinakwenda sawa, akatizama saa yake akaona ni muda wa kuanza uchunguzi wake, …kwanza akachukua karatasi, na kabla hajaanza kuandika kitu, akakumbuka jambo, ..

‘Oh, kweli,..anaweza akanisaidia, anaweza akakumbuka ngoja niende kwake..’akasema na haraka akaacha kila kitu , akatoka pale ofisini na kwa haraka akakimbilia ofisi ya madakitari wa kawaida,..ambappo wagonjwa wengi hutibiwa hapo, hakujali wingi wa wagonjwa, yeye moja kwa moja akaingia kwenye chumba cha dakitari huyo aliyemkumbuka kichwani.

‘Vipi nesi mbona waingia bila hodi..’akaulizwa na dakitari huyo ambaye kwa muda huo alikuwa akihudumia mgonjwa.

‘Samahani sana docta, kwa hili, limenifanya niwe kama mwendawazimu, hata sijijui nafanya nini, ..’akasema nesi akiwa kasimama mlangoni na yule dakitari mtu mnzima, kutokana na hekima za utu uzima wake akamuelewa huyo nesi, akasema;

‘Basi ngoja nimtoe huyu mgonjwa,…’akasema huyo dakitari ambaye ishara za uzee zilishatanda kichwani mvi, na uonekanaji, kijumla alionekana kuwa ni mtu mzima, na huenda pale kazini ndiye dakitari mwenye umri mkubwa kuliko wote, na wagonjwa wengi wanapenda kuingi kwake kwa vile pamoja na utaaalmu wake, lakini pia ni mzoefu wa magonjwa mbali mbali,na anajua jinsi gani ya kuongea na mgonjwa …

Alipomaliza kumuhudumia yule mgonjwa, nesi akasogea na kukaa kile kiti cha wagonjwa na kumuangalia huyo dakitari,..mawazoni akakumbuka siku dakitari kijana ndio kwanza amefika hapo hospitalini na kutambulishwa kwake kuwa yeye atashirikiana naye katika utendaji , akambiwa yeye ndio atakuwa nesi wake wa karibu…na kuna siku walikuwa wakipata chakula pamoja, akiwemo huyo dakitari na dakitari kijana akiwa pembeni…, na huyo dakitari alisema kiutani;

‘Nyie mnafaa muwe mke na mume….’ Na kauli hiyo iliwafanya wacheke, maana ilikuwa ni mwanzoni tu, na hakuna aliyekuwa akifahamu undani wa mwingine, ndio kipindi dakitari kijana amefika hapo hospitalini na hana mazoea kabisa na huyo nesi zaidi ya kuambiwa kuwa ndiye atakayekuwa nesi wake kwa kazi mbali mbali za hapo.

Nesi alipokumbuka hivyo akasema kimoyo moyo;

‘Oh… kama dakitari kijana angelikuwepo hapa leo ningeliweza kupata msaada mkubwa, sijui nitampataje huyu dakitari…maana hata sina mawasiliano naye tangu aondoke. Huenda keshanisahau, huenda keshaoa mzungu..’akajikuta akiwaza hivyo

‘Mhh natamani sana niisikie angalau sauti yake, kwenye simu, mmmh…., lakini..hio sasa ni kama ndoto na hili tukio mmmh, naliona ni langu peke yangu..aheri na mimi ningelipata uhamisho a kwenda sehemu nyingine…., lakini hata hivyo hapa nimepazoea sana…!’ Akawa anawaza akimuacha yule dakitari amalizie kuandika kile alichokuwa akiandika baada ya kumaliza kumhudumia yule mgonjwa aliyetoka.

‘Docta mimi nina shida kubwa sana, na wewe pekee ndio  naona utanisaidia….’akasema nesi, na huyo dakitari akawa katulia akimuangalia huyo binti usoni, na huyo binti akaendelea kusema;

‘Docta, nakumbuka sana  wewe ndiye uliyenipokea hapa nikiwa bado kabinti…’akasema nesi akitabasamu, na huyo dakitari akacheka na kusema;,

‘Hahaha unanikumbusha mbali kweli, …Ni kweli, nakumbuka kipindi chenu waliingia manesi wengi wadogo wadogo, unajua kipindi chenu, mnaajiriwa mabinti wadogo sana..nakumbuka wewe ulikuwa bado unadeka, unakumbuka kudekezwa na wazazi wako, jambo dogo tu unalia, umeacha kule kulia lia kwako..’akasema dakitari akiendelea kucheka.

‘Hapana docta,… acha utani wako, nilikuwa siliilii ovyo, siunajua tena ujana, utoto…na ilikuwa mara ya kwanza kuajiriwa…hahaha, eti nilikuwa nalia lia..hapana bwana unavumisha sasa…tuache huo utani docta…, nisikupotezee muda wako pia, mimi nauliza, hapa zamani kulikuwa na makabati makubwa ya kuhifadhia kumbukumbu,..hivi wewe unaweza kukumbuka yalipelekwa wapi, na kumbukumbu zake?’ akauliza.

 Ni kweli hiyo ofisi anayotumia dakitari huyu huyu kwasasa haikuwa hivyo kabla…kipindi hicho ilikuwa ni sehemu kubwa, na kulikuwa na makabati makubwa…, lakini sasa imeshafanyiwa ukaratabati, na kugawanywa kuwa ofisi ndogo ndogo za madakitari…

‘Mhh, kwanza ya nini,…. pili unanikumbusha kitu, maana hata mimi kuna muda nilikuwa nahitajia nyaraka zangu, unajua ilitokea kama mshitukizo, mara ofisi zinafanyiwa ukaratabari, tukahamishwa huku na huku…hapa sasa kulikuwa kukubwa eneo lote hili, ..kulikuwa ni kama sehemu ya kuhifadhia kumbukumbu, kulipangwa makabati makubwa tu….mara makabati yakatolewa, sisi wala hatuna habari…unajua sisi tulikuwa tunatumia ofisi zile kule za jengo hilo la sasa ambalo limefanywa kuwa jengo la wagonjwa maalumu…’akasema

‘Nani alifanya hivyo..yaani nani alisimamia hilo zoezi la kuhamishwa hizo kumbukumbu,  maana nijuavyo hizo kumbukumbu ni muhimu sana, na ilitakiwa kuwepo dakitari wa kusimamia…unajua mimi hayo yakifanyika nilikuwa sipo, nilikwenda kusoma?’ akauliza nesi

‘Mhh, sijui kama kulikuwa na mtu wa kusimamia..wenyewe utawala wanajua walichokifanya…basi,  yalitokea mambo ya ajabu kweli, maana sisi ndio tunaoweka kumbukumbu zetu muhimu, tunajua umuhimu wake…sasa wanakuja watu wengine wanajifanya wamesoma wanataratibu mpya za mitandao, komputa sijui..basi wewe..ikawa ni karaha..muda gani utaweza kujua kipi ni kipi ukihifadhi kwenye komputa..walioweza wakafanya hivyo, na wengine wakaacha kama ilivyo…

‘Basi yale makabati yakebebwa, ..ujanja ujana tu, wenyewe waliyataka yale makabati kwenye hospitali zao, wakayachukua kwa kisingizio cha kuchakaa, wakajifanya kupiga manada… hata bila sisi tunayoyatumia kupewa taarifa…’akashika kichwa

‘Sasa inafika muda unakumbuka kitu unakwenda kuangalia …oh, unakuta ofisi inavunjwa kuna ukarabati ukiuliza, unaambiwa kamuone mtunza store,..na mtunza store naye atahangaika weee, kama kakipta sawa, kama hajakipata ndio basi tena…kumbukumbu zikapotea…’akasema.

‘Sasa kuna kitu nataka kukifahamu, ni muhimu, unakumbuka katika kazi za upasuaji wagonjwa, kuna kipindi kile alikuwepo yule dakitari kijana,..’akasema

‘Hahaha..unasema oohm, nimekumbuka yule handsome boy,….yule si alikuwa mchumba wako bhana…, hivi hamkuwahi kuvishana pete, maana aliondoka ghafla, ilikuwaje?’ akauliza huyo dakitari akitabasamu.

‘Aaa, docta achana na huyo mtu,…mimi nataka urudishe kumbukumbu zako kipindi kile….. , unakumbuka kuna mama mmoja alifikishwa hapa hospitalini, wewe ulikuwa kule kwenye kitengo cha upasuji…huyo mama alifishwa akiwa na hali mbaya, akafanyiwa upasuaji, na aliyeshiriki alikuwa huyo dakitari kijana…na ikawa ni ama mtoto au yeye, lakini kwa bahati wakapona wote, unakumbuka hilo tukio?’ akaulizwa

‘Mhh, mbona hayo matukio yalikuwao mengi..sasa sijui ni lipi kati ya hilo,…?’ akauliza.

‘Yupo mama mmoja, ambaye baadaye alitoroka…hukumbuki tukio kama hilo?’ akaulizwa

‘Nakumbuka kuna matukio kama hayo wagonjwa wanakuja kutibiwa na baadaye wanatoroka, unajua mimi nilikuwa kama dakitari msaidizi tu, na kawaida yangu hata ya kimaisha, huwa sitilii maanani sana mambo yasiyonihusu…na kawaida yangu, nikimaliza kusaidia kazi fulani narudi huku kutibia wagonjwa mambo ya huko nayaacha kama yalivyo…maana huku ndio ofisi kwangu mimi ni dakitari wa amgonjwa yote,…siunajua hilo…, japokuwa tulikuwa hatutumii ofisi hii, maana haikuwepo , tulikua kulee….’akasema akionyeshea kidolee

‘Doctaaa…hebu jaribu, kukumbuka bwana…kuna mama mmoja bwana… alikuja kuleta taabu kweli,..alitoroka… mpaka polisi wakaitwa wakafanya uchunguzi ….maana tulijua kuwa kapoteza fahamu na hauenda asizindukane..kwa hali aliyokuwa nayo..lakini cha ajabu akazindukana na kutoroka, na hakupatikana na baadaye wakasema kafariki..’akasema

‘Aaah, nimekumbuka..lakini hata hivyo kwa kumbukumbu zangu kichwani mimi kipindi kila sikuwa na nafasi kubwa ya kufuatilia hayo mambo…nilikuwa nashiriki kwenye upasuaji kama msaidizi tu…na wakati mwingine nasaidiana na nyie kwenye kutumwa lete hiki, naleta…’akasema

‘Lakini siunakumbuka tukiolenyewe lilivyokuwa..?’ akauliza

‘Mhhh, ..sasa kwa yule mama..mmh, namkumbuka…. maana yule mama baada ya kumaliza ule upasuaji, tukawa tunasikilizia tu, tulishamkatia tamaa ya kuishi....na mimi baada ya ile kazi nikaondoka, nilikuwa na dharura fulani, kama sikosei, kwahiyo sikujua kilichokuja kuendelea baadaye, nilikuja kusikia tu…’akatulia

‘Nilikuja kuambiwa kuwa huyo mama alikuja kupona,..lakini akapotea kiajabu-ajabu wengine wakavumisha mengi kuwa ni …mama wa ajabu ….unajua,, lakini mengine zaidi ya hayo sijui ilikuwaje baadaye...ilikuwa sio kazi yangu…na unajua ilikuwa ni kazi kubwa uende kusaidia huko, huku wagonjwa wa kawaida wanakusubiria..oh, sikuwa na muda wa kufuatilia kwa kweli… ‘akasema

‘Oh, mbona shidaah..’akasema nesi.

‘Sasa kuna nini kinahitajika, maana kama ni yule mama keshaoza ni muda eeh…na sikuwa na uhakika kuhusu yule mtoto wake,…sijui ilikuwaje, unajua mimi sina muda na mambo mengine yasiyohusu kazi zangu, nikimaliza kazi zangu haraka nakwenda zangu kwenye shughuli zangu nyingine..sina muda kabisa na mambo ya hapa kazini….ambayo hayanihusu..huo ndio utaratibu wangu, kwahiyo sahamani sana kwa hilo sizani kama nitaweza kusaidia zaidi!’akasema huyo dakitari

‘Unajua docta huyo mama tunavyojua sisi alifariki, lakini cha ajabu kuna mama mmoja kaletwa hapa, huyo mama kaungua vibaya, akatibiwa, na katika kutibiwa akaonekana ana kitu kama kuchanganyikiwa, mara akaanza kudai kuwa tumechukua mtoto wake..mara eeh…’akasema

‘Lakini hiyo ni kawaida wagonjwa kama hao kuchanganyikiwa au..?’ akauliza dakitari akionyesha mshangao, na kuonekana kutokujua ni nini nesi anakihitajia.

‘Sasa wakubwa wanadai kuwa huyo mama huenda, alitibiwa hapa kipindi cha nyuma,..ndio maaana anadai mtoto wake kuchukuliwa hapa hospitalini,..wanadai huyu mama anaweza akawa yule mama wa kipindi kileeeh, nikawaambia huyo mama wa kipindi hicho keshafariki…’akasema

‘Kwani huyo mama na yule mama wa kipindi kile wanafanana, na kwanini waseme ni huyo mama wa kipindi hicho, mimi haliniingi akilini, waambie huyo mama sasa hivi ni mifupa ukifukua kaburi lake sana sana utakuta mifupa, …hao watu wamechanganyikiwa nini , sasa wanataka nini, kuna nini kikubwa kimetokea..’akasema

‘Cha ajabu huyo mama aliyefika sasa anadai kuwa mimi ndiye niliyemechukua mtoto wake..’akasema

‘Kachanganyikiwa huyo achane naye, wewe endelea na kazi yako bwana..aaha, mimi kwanza nimejichokea, naona nistaafu nikaendeleze hospitali yangu, hapa napoteza muda wangu bure…sikiliza nikushauri kitu, achana na huyo mama wewe pambana na kazi, hayo yapo na yanakuwepo…unasikia,..na kama hao wakubwa wako wanadai kuwa eeh, ni kweli…waambie wathibitishe, na kwanini wasikuamini, kwanini wanakuja kumuamini mgonjwa aliyechanganyikiwa, kama vipi waniulize mimi maana nilikuwepo, au sio…’akasema

‘Mhh, hapa nimekwama…’akasema nesi

‘Sasa wewe ulihitajia nini kwenye kumbukumbu za zamani naona kwanza ulivyofika hapa ukaniuliza kuhusu makabati na kumaanisha unahitajia kumbukumbu za zamani , za kumuhusu  huyo mama au sio, ili uweze kuthibitisha kuwa huyu mama wa sasa sio yeye, au sio?’ akauliza

‘Ni kitu kama hicho..’akasema nesi akisimama kutaka kuondoka

 ‘ Sasa wewe ulitakaje kuwa zipatikane hizo kumbukumbu za zamani, na tuchukua kumbukumbu za huyu wa sasa ikibidi tuchukue DNA, ..ndio unataka hivyo, lakini kwanini yote hayo, kuna kesi mahakamani ya madai, au ni kauli tu ya huyo mgonjwa, mimi sielewi hapo…! Dakitari yule akamuuliza

‘Mhh docta sio kesi, ni kauli ya mgonjwa tu, na dakitari bingwa, anataka kuhakikisha kuwa ni kweli au si kweli kuhusu madai ya huyo mgonjwa kuwa mimi nimemchukua mtoto wake

‘Kwani wewe ulimchukua mtoto wake?!..., na kwanini umchukue mtoto wake wa nini,…kujipa mzigo wa bure… mbona hao wakubwa zako naona hawana kazi ya kufanya, waambia kama kazi zimewaishia waje huku tusaidiane, maana wagonjwa siku hizi ni wengii…’akasema

‘Docta mimi nilikuwa nahitajia hizo kumbukumbu na kama unakumbuka lolote zaidi kuhusu huyo mgonjwa zamani, na sura yake kama unakimbuka vyema…’akasema nesi.

‘Sura yake…hapaan siwezi kumkumbuka kabisa…Lakini yote hayo ya nini, unahitajia yote hayo, ili iweje?’akamuuliza

‘Mhh, hata sijui..’akasema nesi

‘Sawa kama unahitajia hizo kumbukumbu za zamani, mimi nakushauri ukamuone mkuu wa bohari, mtunza nyaraka, huenda akawa na hizo kumbukumbu.. kitu ambacho sizani kama utafanikiwa, ..maana hizo kumbukumbu zilichukuliwa kama zimepitwa na wakati …zitakuwa zimeliwa na panya…’akasema

‘Na mtandao..sijui hiyo, komputa waliokuja kuhifadhia baadhi ya kumbukumbu nayo iliharibika, ikawa ni hasara..pesa zimetumika, na kazi iliyofanyika haionekani..yaani watu wanakuja na mambo yao wakiwa na malengo binafsi,..ten parcent hiyo.. aah acha tu, hata sitaki kuongea hayo mambo maana hayatanisaidia kitu.’akasema.

‘Sawa dakitari nimekuelewa..kama nitaona kuna umuhimu , nitafanya hivyo…naona nikuache tu uhudumie wagonjwa…’akasema nesi

‘Lakini mimi bado najiuliza kwani wewe shida yako ni nini hasa kwani huyo mama kashitaki, kwani kumetokea nini zaidi, huko kudai kwa mgonjwa, kachanganyikiwa akipona itakwisha wasiwasi wako ni nini…?’ akadadisi yule dakitari tena.

‘Docta, siwezi kukuelezea kila kitu kwa hivi sasa, ila ni muhimu sana, …’ akasema nesi huku anatoka kuelekea ofisi za mtunza nyaraka na kumbukumbu za hospitalini. Hata yeye hakujua hizo kumbukumbu zitamsaidia nini, ila kila mara alikuwa akikimbuka kauli ya dakitari mtoto ikisema;

‘Nimekuambia tu wewe, kama itatokea kuhitajika taarifa za huyo mama, basi jaribu kukumbuka hivyo kuwa kumbukumbu hizo unaweza kuzipata  kwenye kabati namba 5, hili ni maalumu kwa kumbukumbu nyeti za kwetu kama madakitari, sitarajii kuwa hapo zitaharibiwa....’

**********
Nesi aliachana na dakitari yule wa zamani baada ya kuona hana msaada kwake akaelekea kwa mtunza store na nyaraka wa hospitalini,….

Mtunza store na nyaraka alimkatisha tamaa kabisa, kwani alimwambia, kutokana na kulundikana kwa nyaraka nyingi za zamani, wao waliona kuzipunguza zile za zamani, na nyingi zilikuwa zimeharibika vibaya,..lakini waliogopa kuzichoma, wao wakaona nyaraka zote za zamani zihifadhiwe kwenye stoo ya zamani, na humo hapatamaniki…!

‘Stoo ipi hiyo?’ akaulize nesi

‘Mhh, nesi huko hapaingiliki, kwani wewe unahitaji kitu gani hasa…kuna mtu anatafuta asili au kuna tatizo,..kuna kesi ..au… mbona huna hata barua ya madai au chochote cha kuweza kunisaidia…., kwasababu hiyo ingetusaidia kutafuta visaidizi, hiyo stoo nesi …haiingiliki kwa hivi sasa , tumeomba kibali tuyachome tu hayo mabaki….sasa sijui nitakusaidiaje…’ akasema yule mkuu wa kumbukumbu!

‘Lazima nikalitafute hilo faili…na makabati yaliyotokea ofisi za madakitari yapo wapi?’ akauliza

‘Makabati?!, wewe hukumbuki au hukuwepo, mengi ya makabati ya zamani  yalipigwa mnada, na kumbukumbu zake ndio zikachanganywa na hizo za zamani…lakini kuna baadhi bado yapo,….’akasema

‘Oh,…nimekwama, lakini lazima niende nijionee mwenyewe ..’ akasema yule nesi huku anatoka kwenye ile ofisi, akijua hana msaidizi wa jambo hilo, inabidi alijizatiti mwenyewe.

 Alijisema moyoni kuwa ,ili moyoni ajirizishe na kuweza kujikwamua kutoka kwa bosi wake, basi akiwa na nyaraka za huyo mama marehemu ataweza kuwa salama, akawa anajijutia kwanini alikumbuka tukio hilo, maana mkuu wake kalishikilia bango, utafiri lina umuhimu .Sijui kwanini kalikazania…akawa anajiwazia mwenyewe.

‘Lakini ni muhimu, kwa vile imetokea hivi, basi na mimi nahitajika kujua vyema kumbkumbu za yule mama, maana sisi ndio tunaoishi na huyo mtoto huenda ikaja kutokea huyo mtoto akataka kujua zaidi…sasa inanipa hamasa la kuzitafuta hizo kumbukumbu….’akawa anajipa moyo kihivyo…

‘Kitu ninachojiuliza kichwani ni kwanini miminilikumbuka tukio hilo na kuliongeleaa kwa hao madakitari wakati ilikuwa ni siri….oh sasa nitaumbuka, nimeshindwa kuficha siri….’akawa anajilaumu.

‘Hata hivyo..ni ukweli usiofichika kuwa yule mama alikuja akafanyiwaupasuaji, na baadaye akatoroka na ikaja kuokotwa maiti yake, na akazikwa, sasa……kwanini huyu mama mpya aje kuleta shida, na madai kuwa mimi nimemchukulia mtoto wake..hapa ndio inakuja shida ..hapo ndio maana nikakumbuka kisa cha huyo mama maana kama ni mtoto , niliyemchukua ni mtoto wa yule mama marehemu, sasa huyu mama katokea wapi….mmh hapa kuna kitu , sio bure..’akawa anajiuliza na muda huo akawa anatembea kuelekea ofisi hiyo ya zamani.

Alipofika kwenye stoo iliyowekwa mafaili ya zamani, alikata tama kabisa, kwani lilikuwa kama dampo la uchafu, makaratasi mengi yalishaharibika na mengine panya walishayatafuna kabisa. Akajaribu kupekua pekua na aliambulia kuwatibua panya waliokwisha jenga makao yao, akakimbilia nje huku akipiga ukulele..baadaye akakumbuka siku ile dakiatri kijana alivyomwambia,

‘Kumbukumbu hizi nitaziweka kwenye kabati no 5. ..’ Kabati namba tano, ndio kabati gani hilo, mbona humu ndani hakuna makabati, zaidi ya marobota ya mafaili yaliyofungwafungwa na mengine yamefumuka, na hata hivyo ilikuwa namba tano au mia tano…akawa anajaribu kujiuliza.

‘Na huyu mtunza store anadai makabati yalipigwa mnada..naona hapa kuna baadhi lakini yamechakaa..sizani kama ndio hayo yaliyochukuliwa kule ….haya sio yenyewe mmh, hapaingiliki kabisa…’akasema

‘Kabati namba tano au mia tano…au….mmh hata sikumbuki vyema…’akasema

Alikuwa hakumbuki vyema, maana siku ile wakati wanaongea na dakitari kijana,  akili yake haikuwa kwenye kusikiliza hayo aliyokuwa akiagizwa, akili yake ilitekwa na hamasa za mapenzi, …yeye alitaka angalau asikie neno moja la kimapenzi kutoka kwa huyo dakitari kijana, angalau ajue kama kweli huyo dakitari anampenda, …

‘Sasa nitafanyaje….maana juhudi zangu mwenyewe zimegonga ukuta, siwezi kuingia tena humo ndani, ..hawa wadudu walivyo, macho yao yanatisha,mmmh, panya hapana, namuogopa sana huyu mdudu…na siwezi kuomba msaada, nikiomba msaada zaidi kwa huyu mtunza store, nitakuwa naanza kuitoa siri isiyotakiwa kujulikana…..’akasema nesi akijikagua, na mara akasikia kitu kikiruka akajua ndio hao panya acha atimue mbio kuondoka eneo hilo…


Je itakuwaje, huyu nesi atafanya nini,  au atakaa kimya, ...tuzidi kuwepo!


WAZO LA LEO: Tujengeni tabia ya kuhifadhi kumbukumbu za vizazi vyetu…hili ni jambo ambalo wengi hatulitilii maanani, na vizazi vinatawanyika, na wengine hata hawajui asili yao, lugha yao ya asili na hata utamaduni wao. Ni kweli sababu kubwa ni kutokana na mishughuliko ya kimaisha, lakini kama familia mnaweza kujenga taratibu za kuhifadhi kumbukumbu za asili za vizazi toka kwa mababu kwa ajili ya vizazi vijavyo.

Ni mimi: emu-three

No comments :