Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, March 11, 2015

NANI KAMA MAMA-43



Nesi akiwa na jukumu la kutafuta ukweli kuhusu huyo mama,  kama alivyokuwa ameleekezwa na docta bingwa,..kuwa ajitahidi kupata ukweli kuhusu historia ya huyo mama…ikiwa na pamoja na kuongea na ndugu zake ili kama wanafahamu lolote kuhusu huyo mama, …lakini cha ajabu ndugu zake hawakuweza kuja tena hapo hospitalini.

Ikabidi siku ya pili yake alipokuwa mapumziko, kuchukua jukumu la kwenda huko kijijini, pamoja na kusalimia, lakini pia alitaka kujua kama atapata lolote kuhusu huyo mama, lakini hakuna jipya alilolipata.

Leo ni siku ambayo nesi huyu alitakiwa kutoa taarifa kwa mkuu wake wa kazi wakitengo cha watu wenye matatizo ya ufahamu,ubongo ,akili, na kuchanganyikiwa (Neurologists and General Psychiatrist ).

Akiwa ameshikilia kabrasha la huyo mama mkononi, aliingia ofisi ya huyo docta, na kumkuta docta huyo akiwa na msaidizi wake, wakiwa na karatasi za x-ray, ambayo walimpiga huyo mama,…na walikuwa wakionyeshana kitu kwenye hiyo xray, na ilikuwa dhahiri wanamuongelea huyo mama, na walipomuona huyo nesi, wote wakageuka kumuangalia;

Docta bingwa ambaye alionekana siku hiyo kama hayupo ofisi kwani alikuwa hajavalia mavazi ake ya kazi akasema;

‘Karibu nesi…utuambie uliyoyaata huko kijijini, kwani nataak kutoka kidogo …ni hili ni muhimu sana..., maana imefikia hatua huyu mama anakuonyoshea kidole wewe…’akasema docta

‘Ananinyoshea kidole mimi, kwa lipi?’ akauliza nesi akionyesha wasiwasi.

‘Kaa kwenye kiti kwanza tusikie uliyoyapata huko kijijini….maana huyo mama anaongea mengi…ni kuonyesha kuwa huyo mama alipatwa na jambo likaziba ufahamu wake wa kumbukumbu za nyuma…sasa anaanza kukumbuka kidogo kidogo....kwahiyo mengi yatasemwa, na huenda yakawa na ukweli…hatutakiwi kuyapuuzia...’akasema docta bingwa.

‘Anadai wewe umechukua mtoto wake..’akasema docta msaidizi..na nesi akakaa kwenye kiti huku akili ikianza kuchemka.

Nesi akiwa hata hajui atasema nini kwani pamoja na juhudi zote za hata kufika huko kijijini alipokuwa huyo mama, lakini hakuweza kupata msaada wowote, zaidi ya kuchanganywa akili..na vitisho zaidi,…kwani imefikia hatua watu wengine wanaogopa hata kumuongelea huyo mama.

Akasalimiana na mabosi wake,, huku akili yake ikikumbuka yaliyotokea pale alivyokwenda huko kijijini…, ilivyokuwa;

********

‘Mhh, mimi hata sitaki kumongelea huyo mama,…huyo mama hata… kuna watu wameshaanza kupata mabalaa kwa kujifanya wanamuongelea huyo mama, ….mhh, hapa mimi sijui lolote..’aliambiwa na mtu ambaye inasadikiwa kuwa ndiye aliyekuwa mtu wa kwanza kumuona huyo mama alipooneana hapo kijijini.

‘Lakini nasikia wewe ni ndiye uliyemuona huyo mama kwa mara ya kwanza,lipoonekana hapa kijijini au sio…je ulimuona akitokea wapi?’ akaulizwa

‘Nimekuambiaje mimi sijui lolote kuhusu huyo mama…unasikia jirani, wewe ni ni binti tumekulea wenyewe kwanini nikufiche ukweli…hayo yaache kama yalivyo,….’akasema huyo mama ambaye ni muongeaje sana, lakini kwa swala la huyo mama akakataa kata kata kuliongea.

‘Unasikia nikuambie kitu jirani, …hili ninalolifanya ni kwa nia njema, mimi nahisi kama nilivyosikia, waliopata madhara ni wale wanaomuongelea huyo mama kwa ubaya, mimi ni nesi, na nipo kwenye hospitali aliyolazwa huyo mama, lengo langu ni kumsaidia huyo mama atokane  na tatizo alilo nalo..huyo mama inaonekana kapotea, huenda huko alipotokea ndugu zake wanamtafuta hawajui wapi alipo..’akasema nesi.

‘Nani kakuambia huyo mama kapotea..huyo mama hajapotea,huyo mama anajua ni nini anachokifanya…kaja kulipiza kisasi, ni wale akina mama waliokufa kwa kuonewa, kudhulumiwa…’akatulia.

‘Mhh, hizo ni imani tu..huyo mama hakuwahi kufa, kama angelikuwa ni mfu tungelimuona huko hospitalini, anacho kila kitu kama binadamu..lakini kama unavyosema huenda alitendewa ubaya, huenda…alipatwa na ajali, huenda…na atahari hizo ndizo zikafikia kuharibikiwa….’akasema nesi huku akionyeshea kwa mkono, na jirani akawa katulia huku kaangalia chini.

‘Mhhh….’akaguna huyo jirani kuonyesha kutokukubaliana na hayo maneno ya nesi

‘Kuna matatizo mengi yanayoweza kumuathiri mtu akawa kama kachanganyikiwa, ..sasa sisi kwa huruma zetu, maana hiyo sio kazi yetu kuhangaika hivi, lakini tumeona tumsaidie huyo mama kwa vile alikuwa mwema kwenu..na pia kwa namna nyingine ni wajibu wetu inapobidi kama hivi…, na ili tufanikiwe hilo tunahitajia msaada wenu..’akasema nesi.

‘Jirani,… mdogo wangu…Wewe unajitakia matatizo, hebu nikuulize kitu; Kwanini polisi walishindwa..?’ akauliza

‘Polisi hawajashindwa,… wao wametimiza wajibu wao,..na kama kuna tatizo wangelipelekewa ili walifanyia uchunguzi…unajua polisi wana mipka yao..hawawezi kujitungia kesi…. na huenda badoo wapo kwenye uchunguzi, siwezi kuwasemea…’akasema nesi.

‘Mdogo wangu hata kama umesoma..eeh, lakini kuna mambo mengine huyajui…nakutolea mfano tu kwa hao polisi,..hii kazi unayoifanya ilitakiwa ifanywe na polisi ni kweli si kweli..?’ akauliza

‘Mhh…sio kweli inategemea unaongelea upande gani, mimi nafanya haya ili kuwezesha mgonjwa kutibiwa…’akasema nesi.

‘Nisikilize,…nyie na polis ni ni nani mwenye mamlaka ya kuchunguza ukweli kuhusu huyo mama,..kama kapotea, kama anatafutwa..kwanini alitaka kuuwawa.. ina maana polisi wamepatwa na jambo ambalo limewaogopesha…kuna askari wawili , tumesikia kuwa wamechanganyikiwa…sasa wengine  wameogopa…unasikia mdogo wangu..’akasema huyoo jirani.

‘Inawezekana wamechanganyikiwa na jambo jingine, lakini kwa vile limetokea muda huo wa tukio ni lazima watu wataliunganisha hapo….’akasema nesi.

‘Mdogo wangu…nikuambie ukweli, mimi ninaona mengi ambayo huwezi kuyaona licha ya kuwa wewe umesoma…. sasa naona na wewe huko unapokwenda yanaweza kukuta hayo ya polisi..japokuwa naona nyota yako ni kali…lakini nakuonya kama mdogo wangu, achana na hayo, achana na huyo mama, huyo mama ni adui yako…atakusumbua sana, utakuja kuniambia..’akasema huyo mama.

‘Adui yangu kwa vipi…kwani mimi nimemfanya nini?’ akauliza

‘Inaonyesha hivyo…kazi kwako utapata shida, huyo mama atawasumbua sana….usipoangalia…mmmh, sitakiwi kukuambia hayo, …’akatikisa kichwa na kupiga chafya.

‘Kama ni kupata shida kwa ajili ya waginjwa kama hao, tumeshapata sana..lakini hatuwezi kuvunjika moyo..maana ni moja ya jukumu letu jirani yangu…..’akasema

‘Mengine mnajitakia ..hasa hilo la huyo mama,…utakuja kuniambia..’akasema.

‘Jirani, sisi tupo na huyo mama wakati wote tunamuuguza na sasa angalau anaanza kuongea na watu..lakini tatizo hana kumbukumbu za nyuma…hayo mengine na mambo ya kukuza tu, hayana ukweli…’akasema nesi.

‘Nani kakuambia hana akili..akili anazo sana, ..lakini hatakiwa kuongelea yaliyopita maana ni machungu na shubiri kwake, yamefichwa, anachotakiwa kukifanya kwasasa ni kutimiza lengo la ujio wake….unasikia, hataongea ya nyuma mpaka lengo lake litimie…’akasema

‘Jirani hebu niambie, wewe unasema hivyo kwa ushahidi gani?’ akaulizwa nesi akimuangalia huyo mama ambaye wamezoea kumuita jirani maana zamani waliwahi kuishi nyumba ya kupanga pamoja, na hata walipohamia kwenye nyumba zao bado wakaendeleza kuitana hivyo.

‘Kutokana na wataalamu,….na mimi huwa ninapatwa na njozi , zinanielekeza, si unakumbuka wakati tunaishi pamoja kwenye ile nyumba…sasa kuna watu wananijia, na wananiambai mengi…sasa hao, siwajui ni akina nani, wameniambia hivyo...huyo mama sio mwanadamu wa kawaida, ….’akatulia na kuangalia hewani kama vile anaona kitu.

‘Hao wanakuambia hivyo ni watu, unakutana nao..au ndio hayo majini…?’ akauliza nesi akionyesha tabasamu mdomono la kudharau.

‘Unajua nikufunulie kitu…majini ,mashetani,  vibwengo wanaweza kujigeuza na kuwa maumbile ya wanadamu wakiwa na malengo yao…sasa huyo mama…muone hivi hivi…mhhh, najua hutanielewa, wewe si msomo bwana…’akatulia akageuka kuangalia huku na kule. Na nesi akaiona hiyo hali akauliza

‘Nakuona kama unaogopa kitu…, huyo mama yupo huko mjini hospitalini, kama ndio yeye unayemuogopa…nakuona kama unawasiwasiwasiiih…’akasema nesi akitabasamu.

‘Ahahaha….mdogo wangu…mmmmh, sio kweli, huyu mama yupo hapo nje…’akaema huyo mama, huku akiwa kakodoa macho kuangalia mlangoni, na nesi akashangaa..kwanza kwa jinsi huyo mama alivyotoa macho, na pili kusikia hiyo kauli yake, kuwa huyo mama yupo nje, lakini hakutilia maanani maana anamahamu sana huyo mama akazarau na kusema;

‘Jirani, sikiliza nikuambie..hivi hujaacha yale mambo yako..mara unaona wachawi, mara umeona hiki au kile..sisi wala hatuvioni..hayo yatakuharibu akili…., ‘akasema

‘Mhhh…acha..acha..namuona huyoooo’akasema na kutikisa kichwa.

‘Jirani vipi tena…nakuambia ukweli, mimi ndiye ninayeshughulika na huyo mama kwa sasa, sijawahi kuona dalili yoyote ya hayo unayofikiria wewe na hizo ni hisia zenu tu huku kijijini,…mumezijenga akilini, na zitawaathiri sana, hayo sio mambo ya kuyajenga kwenye ubongo….huyo mam a nimemuacha hospitalini, hawezi kuja huku…’akasema nesi, lakini alimuona huyo jirani yake akitikisa kichwa na akawa kama anaweweseka mdomoni.

‘Mhh, jirani huyo mama yupo hapo nje….kama unabisha hebu toka hapo nje umuone..’akasema, na nesi akageuka kuangalia nyuma akafikiri na baaadaye akasimama,…

Hakutaka kubishana na huyo mama, akatembea taratibu kama kunyata, hadi mlangoni kabla hajashika mlango kufungua, akasikia mlio wa nyago, kama mtu anakimbia. Nesi akafungua mlango kwa haraka na kutoka nje, akatizama huku na kule hakuona mtu, na kwa mbali akaona kama mtu…ni mwanamama, kajifunika kama vile alivyokuwa kajifunika yule mama,..na kwa umbali ule hakuweza kuona zaidi na huyo mtu akapotea…

Nesi akapikicha macho…akatizama tena, hakuona kitu, akatulia na akajaribu kutizama tena na tena hakuna dalili tena ya mtu, akatulia kuwaza, akageuka kutaka kurudi kuongea na huyo wanayemuita jirani, lakini akaona haina haja, taratibu akaondoka zake hata bila kuaga….

*********

‘Unajua..huko nilipokwenda  kwa yule mama mliyeniambia kuwa ndiye aliyemuona huyo mama wa mkono wa baraka kwa mara ya kwanza mhh, nimeondoka bila kuaga..…’nesi akawa anaongea na ndugu zake, muda huo alishajiandaa kuondoka, kurudi mjini.

‘Mhh kakuambia nini…maana yule mama naye sijui ana mshetani, anaweza kuona vitu msivyo viona.. naye ana makarama yake…’akasema jirani wa dada yake ambaye alikuwepo hapo akimuaga nesi , na kwa vile wamezoeana sana alitaka pia kufahamu maendeleo ya mgonjwa.

 Nesi huyo alipofika hapo kijijini, akasalimiana na ndugu zake, halafu akataka kujua kwanini hawakurudi tena kumuona mgonjwa, wakasema mwenye nyumba hataki, kwahiyo wametii amri ya mume wa nyumba, japokuwa walikuwa na hamu ya kurudi kumuona mgonjwa.

‘Sasa kwanini shemeji kakataa, kama yeye hataki, basi angewaruhusu nyie mje mumuone mgonjwa....maana yule mama alikuwa mwenzenu, mkaishi naye hapa kwa wema au sio, na mumesema alikuwa akiwasaidia watoto wenu wenye matatizo...na pia docta alitaka kuongea na nyie…kwani shemeji kwanini hataki muende kumuona mgonjwa…’akasema nesi.

‘Hataki, na hataki kutoa sababu…, na unasema docta anataka kutuona, kwanini docta anataka kuonana na sisi heri basi hatukufika maana tungelisema nini kuhusu huyo mama, na shemeji yako angesikia kuwa tumeongea na docta… lolote kuhusu huyo mama mmh, kungechimbika….’akasema dada mtu.

‘Mimi ningekuja mwenyewe, lakini yanayoendelea hapa kijijini yanatisha..nikaona kwanini nijitakie matatizo, mume wangu hajanikataza….’akasema huyo jirani, na nesi akaona ndipo pa kuanzia.

‘Kwani kuna nini kinachoendelea hapa kijijini maana sasa mnatia aibu, kila siku visa vya kuua, kuchomeana moto.., kuumizana ….ukiuliza ni imani za kishirikina, wivu…unyanyasaji kwa akinamama, imekuwaje jamani…hivi niwaulize, dini mumepeleka wapi..?’ akauliza

‘Mhh, ya hapa kijijini yaache kama yalivyo, ..usije kuingia matatizoni,..’akaambiwa

‘Hapana kama ni kuhusu huyo mama ,…hilo ni moja ya ajenda zangu za kuja hapa, …naaah, ni nani anaweza kuniambia yote kuhusu huyo mama,…nataka kujua ..au kuonana na ambaye alimuona huyo mama kwa mara ya kwanza…ili tujue katokea wapi?’ akauliza

‘Mimi nakushauri …japokuwa sina uhakika sana,..nenda kwa yule mama mnayemuita jirani yenu…yule yupo mpakani mwa kijiji, na ndiye aliyemuona huyo mama kwa mara ya kwanza….na anajua mengi..japokuwa sijui ufahamu wake kuhusu huyo mama wa mkono wa baraka…maana kila mtu sasa anaogopa kuyaongea hayo ya huyo mama..’akaambiwa na mama mmoja ambaye ni jirani yao hapo.

‘Basi ngoja, mimi nawaacha kidogo…sitaki kusubiri…muda unakwenda..dada mimi nakwenda kwa huyo mama…’akasema nesi na bila kusubiria zaidi akaelekea kwa huyo mama wanayemuita jirani…ni nje kidogo ya eneo hilo… na yaliyomkuta ndio hayo……

*****

‘Haya tuambie umepata nini huko, maana nakuona uso umesawajika….’akamuuliza alipomuona mdogo wake akirudi wangu wangu,  muda huo jirani yao pia alikuwepo , na jirani huyo akawa katega sikio, na kutikisa kichwa kukubalina na hilo.

‘Mhhh…huko eeh, kweli, yule jirani hajaacha yale mambo yake….unajua baada ya kunikatalia kuniambia ukweli kuhusu huyo mama nikatumia ujanja kumuhoji,… na katika kuongea akajikuta anamuongelea huyo mama, akadai kuwa huyo mama nimekuja naye toka mjini…’akasema nesi.

‘Kwa vipi?’ akauliza dada mtu akiacha kile alichokuwa akikifanya na kumuangalia mdogo wake.

‘Hata mimi sijui…anadai kila ninapokwenda huyo mama yupo nyuma yangu na pale hakuweza kuingia, alikuwa nje akinisubiria.’akasema

‘Mumeonaee..huyo mama ana machale..anaweza kumuona mwanga, …mchawi…anaona vitu msivyoviona..ana sijui tuite nini…ana hulka ya uganga wa kienyeji..sijui kwanini hataki kuwa mganga….’akasema huyo jirani.

‘Mhh, usiende tena kwake, ..asije kutuletea mabalaa…mimi sitaki kuongea nay eye, hasa akianza mambo yake….mara akaona hiki, mara yule yupo hivi…hapana , hata mume wangu hataki kabisa yule mama kufika hapa..anaweza kukukosanisha na watu….’akasema dada mtu.

‘Sasa sikilizeni niwaambie ilivyokuwa..’akasema huyo nesi.

‘Mhuuu, tuambie ikawaje?’ akauliza huyo jirani lakini dada mtu hakutaka kusikiliza zaidi..akawa kaangalia mlango wa chumbani, akijua mume wake yupo ndani kalala.

‘Akaniambia kama nabisha kuwa huyo mama hakuja name,  nitoke nje, nitamuona huyo mama akinisubiria..’akaasema nesi.

‘Unaonaeeh..haya ikawaje, ni lazima utamuona huyo mtu kwa vile kasema umuone, vinginevyo usingeliweza kumuona…’akasema huyo mama jirani.

‘Acheni hayo mazungumzo, ukiongea sana hayo mambo yanakuathiri kiakili, utajikuta unaamini mambo ambayao hayafai sio sehemu yetu kuyaamini,..mimi naona tuongee mengine…’akasema dada mtu lakini moyoni alikuwa na hamu kusikia yaliyomkuta mdogo wake alipokwenda huko.

‘Unajua nataka kuwaambia ilivyokuwa sio kwamba nimeamini,… hapana..ila imetokea hivyo,..maana nilipotaka kutoka kwanza nilisikia kama kishindo cha nyayo cha mtu anayekimbia,..nikajua ni mtu tu, labda alikuwa hapo mlangoni akisikiliza mazungumzo yetu, basi kwa haraka  nikafungua mlango n kutizama nje…’akasema

‘Eheee, ikawaje..ukamuona eeh…atakuwa kapotea usingeliharakisha hivyo…, watu kama hao wanajua na kuhisi nyayo zetu, ..wewe uko ndani unatembea yeye yupo nje, anajua kabisa unatembea kuja kufungua mlango, na akiondoka hapo ni kama anapaa huwezi kumuone tena..’akasema huyo jirani.

‘Wewe umejuaje hayo?’ akauliza dada mtu.

‘Niliwahi kuongea na huyo mama,…na mara kwa mara naongea naye, ..ana visa vingi..anawajua watu wote hapa kijijini, ninani mwanga, ni nani….yaani ukikaa naye utaogopa kuishi hapa kijijini…’akasema huyo jirani.

‘Kwahiyo huyo jirani anasema huyu mama aliyekuwa akiishi hapa ni mwanga, ni mchawi…au sio?’ akaulizwa huyo jirani, akageuza kicha huku akiwa kama anafumba macho.

‘Aaah, huko tusiende…mimi sijui, …..nazungumzia huyo mama alivyo , sio huyo mama wa mkono wa miujiza, mimi huko sijui…’akasema an kuonekena kuogopa kumuongelea huyo mama.

‘Au nyie ndio washirika , mlikuza mambo, mkajenga chuki hadi huyo mama wa watu akafanyiwa hayo mabaya..roho mbaya tu…’akasema dada mtu.

‘Jirani…chunga mdomo wako…mimi na huyo mama tulikuwa marafiki..na ingelikuwa kidogo tu, ..mimi ningeliweza kuona sura yake..kidogo sana..lakini siku ile akaja mtu, tukakatisha mazungumzo yetu, yule mama aliniamni kweli, alitaka kunionyesha uso wake..’akasema huyo jirani.

‘Jirani na porojo zake…sikilizeni mume wangu kalala, akiyasikia haya …mmh’akasema dada mtu.

‘Ina maana shemeji yupo ndani, unajua nilishamuaga kuwa naondoka…’akasema nesi.

‘Ndio maana nasema huyu jirani anapenda sana kuongea na kujionyesha kuwa kila kitu anajua,..ukimsikiliza huyu , unaweza ukapotea, wewe wahi usafiri, labda kama unataka kulala..’akasema dada mtu.

‘Aaah, ..jirani ngoja amalizie…hebu tuambie ulimuona huyo mama, akiwa hapo mlangoni?’ akauliza huy jirani.

‘Hapana sikumuona huyo mama…ila niliona mtu kwa mbali sana, ..’akasema nesi

‘Yupoje ni kama huyo mama au?’ akauliza huyo jirani

‘Wanafanana…lakini szani kama ndio yeye maana nilipiga simu hospitalini, wakaniambia huyo mama yupo….ila huyo niliyemuona kwa uvaaji …na sio kweli…maana alikuwa mbali, …na..na alikuwa kanipa mgongoo kwa hiyo nisingeliweza kumuona, siwezi kusema ni huyo mama sio kweli, …’akasema

‘Ulirudi kumuuliza huyo mama ?’ akaulzia huyo jirani

‘Wala sikuwa na haja naye tena, …’akasema nesi

‘Ungerudi angekufunulia mengi….maana angekuwa na uhakika kuwa huyo mama hayupo hapo nje, na anaongea akiwa na uhakika, wewe umeamua kuondoka kwa haraka bure na umekosa uhondo..’akasema huyo jirani.

‘Siku nyingine nitaongea naye..ila sasa naondoka, na hata sijui nitamuambia nini bosi wangu, maana sijapata alichoniagiza..’akasema

‘Haya mtaniagia mtoto…na shemeji tena, japokuwa nilishamuaga….vipi siku hizi mtoto analia lia tena kumtaka mama wa baraka…naona sasa kawa mkubwa, ..’akasema

‘Wala halii tena, huyo mama wa mkono wa baraka kafanya makubwa, wale wote waliobahatika kukutana na huyo mama wanasema watoto wao hawana matatizo kabisa,..sijui kwanini watu wengine waliamua kumfanyia hayo waliyomfanyia, unajua huyo mama angesaidia sana hapa kijijini…natamani arudi tena’akasema dada mtu.

‘Yah, lakini huenda na yeye alikuwa na lengo lake,…hatujui zaidi,..yule mama anasema huyo mama alikuwa na malengo yake, pamoja na huo uzuri wake..’akasema huyo jirani

‘Malengo gani?’ akaulizwa

‘Mmmh, mimi sijui…utakuja kumuuliza huyo mama atakufunulia yote, lakini kwa hivi sasa sijui..maana watu wanaogopa kabisa kumuongelea huyo mama…labda akirudi tena hapa, kama atafikia hapa mtajua zaidi…’akasema huyo jirani.

Mara mlango ukafunguliwa, akatokea shemeji mtu akiwa kashika fimbo yake mkononi, ..kakunja uso kwahasira…akawaangalia waliokuwepo mmoja baada ya mwingine,  japokuwa alikuwa akiwaangalia lakini usoni alikuwa kama hayupo hapo, akainua fimbo juu, na kusema;

‘Hivi niliwaambiaje?’ akauliza sasa akimtizama mke wake , na mkewe akawa kaangalia chini, na kusema;

‘Kwani kuna nini mume wangu?’ akauliza mke mtu sasa akimuangalia usoni, alikuwa anajua ni kitu gani mume wake anauliza lakini hakutaka kukubali mara moja.

‘Nawauliza niliwaambiaje?’ akauliza tena huku akitikisa kichwa

‘Tulikuwa tunaongea tu…’akasema mke mtu, na jirani akiwa kajikunyata kwa uwoga

‘Narudia tena, nauliza niliwaambiaje?’ akauliza sasa kwa sauti ya hasira.

‘Tusimuongelee huyo mama hapa ndani…’akasema jirani mtu.

‘Sasa wewe jirani, ujirani utakushinda..sitajali kuwa wewe ni jirani, na wewe mke wangu ….ina maana mimi nilichoongea unaona ni cha upuuzi,…’akasema kwa hasira.

‘Mume wangu samahani,..hatutarudia tena,..ni mdogo wangu katumwa, anataka kujua jinsi gani huyo mama alikuwa akiihis nasi, katokea wapi…inahitajika huko kazini kwao..’akasema na shemeji mtu akageuka kumuangalia shemeji yake.

‘Mimi nilijua umeshaondoka….’akasema na kugeuka kutaka kuondoka.

‘Sasa shemeji mimi nataka kukuuliza jambo..’akasema nesi.

‘Jambo gani, kama ni kuhus huyo mama, ..sitaki kusikia…unasikia kama unataka tukosane, uniulize kuhus huyo mama…simtaki na sitaki kusikia habari zake…’akasema shemeji mtu.

Nesi akamsogelea shemeji yake na kumshika mkono,….shemeji yake akawa anatembea hakugeuka kumuangalia shemeji yake huyo na nesi, akawa anatembea naye sambamba…sasa akautoa mkono wake mkononi mwa shemeji yake, na kuuweka begani,… wakatoka naye huku akionyeshea ishara kwa nyuma kuwa yeye anaondoka.

‘Haya safari njema…’akasema dada mtu, na jirani akawa anataka kutoka, nia kuwafuatilia hao waliondoka, akionyesha kutaka kusikia wanayoongea…, lakini dada mtu akamshika mkono na kumtuliza kwanza. Na huyo jirani akasema;

‘Mhh mtu na shemeji yake bhana, hivi huoni wivu…?’ akauliza

NB: Tupo pamoja


WAZO LA LEO: Kamwe usikate tamaa na kupambana na majaribu, mitihani na shida zinazokuzunguka, kwani shida hizo au majaribu hayo yasingeliitwa hivyo, shida au matatizo kama yengelikuwa ni rahisi kuyatatua. Kila hatua ya vita hiyo, utajifunza mbinu mpya na njia nyepesi ya kuyashinda hayo majaribu. Jua kuwa Mungu yupo pamoja nawe na  kakupa hiyo mitihani kujaribu imani yako, pambana na mwisho wa siku utafaulu tu.
Ni mimi: emu-three

No comments :