Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, February 27, 2015

NANI KAMA MAMA-38


Katika kupata ukweli wa tukio zima, askari hawa waliotumwa waligawana katika makundi matatu, nia hasa ni kutafuta ukweli na chanzo, cha watu kuuwawa ovyo, hasa wazee na akina mama kupigwa hadi kuumizwa, na kwanini kunakuwa na ajali za moto za mara kwa mara.
 Tulishaliona kundi la kwanza , ambalo liliingia kumchunguza mmoja wa wahanga wa moto ambaye ni mama wa mkono wa karama, au wengine kama wanavymuita, mama kutoka mbinguni, na wale wasiompenda wakamuita, mama kutoka kuzimu…na kundi la tatu lilikuwa na kazi ya kuchunguza chanzo cha moto.

Katika kundi hili la pili, ambalo kazi yake ilikuwa kuwahoji watu ili kujua kinachoendelea hapo kijijini, …na kuhusiani na hilo tukio la moto uliotokea karibuni hadi kueleta maafa.

Askari hawa wakiwa wanaendelea kumhoji, baba mwenye nyumba maswali mbambali na kwa muda huo walikuwa wakitaka kufahamu huyo mama mhanga wa moto ni nani…..

Akiendelea na maswali, askari kanzu akamuuliza baba mwenye nyumba swali ambalo kwao lilikuwa na umuhimu wake, japokuwa alitarajia kupata maelezo kutoka kwa kundi la kwanza lakini kutokana na utata uliopo, akaona amuulize baba mwenye nyumba ambaye aliweza kuishi na huyo mama kwenye nyumba moja kwa muda sasa…akamuuliza swali;


‘Je wewe uliwahi kuiona sura ya huyo mama…maana nasikia muda wote kajifunika usoni?’ akaulizwa baba mwenye nyumba,  na baba mwenye nyumba kwanza akatulia akijua hilo swali sasa linamuingiza kwenye mtihani, na pia inawezekana ni mtego kwake, akasema;

‘Mwenyewe umesema kuwa mama huyu muda wote huwa anajiunika,sasa kama muda wote anakuwa amejifunika, mimi nitawezaje kumuona sura yake..’akajibu akiwa kakereka na maswali ya mwanzoni ambayo hakuyaenda.

‘Hivi ni kweli mtu mumeishi naye nyumba moja karibu miaka mingapi,…akawa anakulelea mtoto wako…mkazoeaan akawa kama mmoja wa familia yako, ina maana haikutokea hata siku moja kuiona sura yake au ni kwa vile hutaki kutoa siri zake, labda kwa kujali utashi wake…?’ akaulizwa.

‘Nikuambie ukweli, akina mama kama hao wanakuwa makini sana…inaweza ikatokea bahati mbaya kama unavyosema,..kwa bahati mbaya,na kwa vile ni kwa bahati mbaya huwezi kuwa makini kumuangalia …’akasema.

‘Tunataka hiyo bahati mbaya,…maana wewe kama baba wa nyumba,una jukumu la ulinzi na usimamizi wa nyumba na familia yako , huwezi kumpoeka mtu tu, humjui, hujui sura yake, hujui jina lake..haya limetokea kama hili janga, tunahitajia ukweli na unatakiwa kusema ukweli wote li tuweze kuhakikisha kuwa haki inatendekea, na pia tuweze kumaliza hili tatizo linaloendelea haapa kijijini kwenu..’akasema

‘Lakini hamuwezi kulimaliza kwa kupitia kwangu tu au…?’ akauliza baba mwenye nyumba.

‘Chanzo kimoja kinaweza kuwa sababu ya vyanzo vyote, hapa tumeona ndipo pa kuanzia, na kwa jinsi ilivyo, hawa watu waliofanya hivi hapa ndio hao hao wamekuwa wakifanya kila siku sehemu mbali mbali za hapa kijijini,…sasa ukituficha inawezekaan tukahisi kuwa unashirikiana na hao watu….’akasema askari.

‘Ndio tatizo lenu hilo..mtu akijitolea kusema ukweli anaweza akapata taabu hata kuliko muhusika mwenyewe au muhalifu mwenyewe mnayemtafuta…sawa mimi sikatai kushirikiana nanyi kuupata ukweli, maana hata mimi kama raia mwema wa hiki kijiji napenda tuishi kwa amani..lakini sio kwamba kila kitu nitakifahamu mimi..’akajitetea

‘Ndio maana tunakuuliza maswali ambayo tunahisi wewe unayafahamu na sio kwamba tunahisi lakini kiukweli haya maswali tunayokuuliza, tunaamini wewe unayafahamu..hasa kuhusu huyu mama…’wakasema

‘Haya mnataka mimi niseme nini?’ akauliza

‘Utujibu swali letu tulilokuuliza awali , au niulize tena, je, wewe uliwahi kumuona huyo mama sura yake,…usoni,… hata kwa bahati mbaya tu…?’ akaulizwa

 ‘Mhh..,hata kwa bahati mbaya tu, mmh….?’ Akauliza huku akisita kusema kitu na kumbukumbu la tukio la nyuma likamjia akilini na kujaraibu kuwazia sura ya huyo mama, akawa hakumbuki vyema  ….maana mara zote ilikuwa kwa bahati mbaya na kwa haraka.

Wakati baba mwenye nyumba anatafakari akilini akahisi kuonywa, kuwa asiseme, akisema atakufa au kupatwa majanga kama yalivyowapata wengine…lakini kwa upande mwingine akawa anajipa matumaini, akisema; mmh huenda ndio yeye, kama ndio yeye kwanini niogope kusema ukweli, lakini hata hivyo, mwenyewe hakutaka sura yake ionekane kwanini mimi niwe mtoaji wa siri zake,…

Tuendelee na kisa chetu

****************

Baba mwenye nyumba akakumbuka tukio wakati alipoingia kuhakikisha kama kweli huyo mama kateketea na moto uliounguza chumba hicho alichokuwa akilala huyo mama…na kwa kumbukumbu zake tukio hilo ndilo lililomuwezesha kumuona huyo mama, japo, sio kwa uhakika sana,.. ni kwa muda mchache sana, na kilichotokea pale alipoivua ile nguo iliyokuwa imefunika kichwa, alijikuta akipata msituko na akili yake kuwa kama imeganda.

Akili ilikuwa kama imeganda kwa kutokuamini kwa yale aliyoyaona ambayo mengine hataki hata kuyakumbuka, sembuse kuyasema..macho na akili ikawa kama haiamini kile alichokiona…na mengi yalipita kichwani na hata hakuweza kukariri vyema kile alichokiona..

Ilivyotokea ni kama vile umepita njiani ghafla ukaona kitu cha aajabu au kisichochofaa, ukakwepesha macho yako kwa haraka usikiingalie, na kwa tabia ya macho hutuma taarifa kwenye ubongo, na ubongo hutaka uhakika, kwahiyo utageuza kichwa kuangalia kile kitu tena….ndivyo inavyokuwa kwenye akili ya kibinadamu na ndivyo ilivyotokea kwa huyu mjamaa….

  Akajaribu kukumbuka…na kuvuta akili, kuanzia pale alivyomfunua….na nguo ya kichwani ilipotoka, uso ukaonekana, ..kwa kumbukumbu za uhakika, kilichotanda usoni kilikuwa ni damu na majeraha yakuonyesha kuwa mama huyo alikatwa na mapanga, na damu bado zilikuwa zinavuja….

‘Hawa watu jamani ni wanyama..’akajikuta akisema kimoyo moyo

Lakini pia aliona kitu kingine cha ajabu ambacho kilimfanya ashindwe kuamini, kilimkumbusha jambo, jambo ambalo hakutka alikumbuke tena,..na kwa mchanganyiko wa yote hayo, akili ikashindwa kuhimili, kilichofuatia hapo ni yeye kudondoka chini…macho….macho

‘Macho, macho yana nini?’ akawa anajiuliza bila kupata jibu

Akakumbuka kuwa aliposimama ili kuangalia tena, kama akili ilivyomtuma, akakuta ile nguo iliyomfunika huyo mama usoni, ilikuwa imerudi kama ilivyokuwa, uso umefunikwa,…hiyo iliashiria kuwa kumbe mama huyo kwa muda huo alikuwa bado yupo hai,…. akataka kujaribu tena kumfunua, huyo mama akazuia…na baadaye kukaja dalili za kuonyesha kuwa huyo mama anakata roho…

Sasa hapo atawaaambia nini hao askari kuwa huyo mama yupoje…?

‘Afande,… huyu mama alijitahidi sana kujifunika, alijitahidi sana kuhakikisha hata mimi, hata mke wangu, hata mfanyakazi wa ndani ambaye wamezoeana sana, hakuna anayefanikiwa kumuona sura yake…’akasema

‘Unajua unaongea na nani?…sisi sio watoto wadogo….ni lazima kuna siku ulimuona huyo mama,…sisi tunachotaka ni uhakika tu, je huyo mama yupoje, na kwanini watu wanafikia kumuona sio mtu wa kawaida,…’akasema askari.

‘Mhh,sijasema huyo mama sio mtu wa kawaida, maana anakula anafanya kila kitu tunachokifanya, najua wengi wamehadaika na huo uvumi kuwa huyo mama ni mama wa mbinguni,..mimi sijui, maana kwangu mimi nilimuona kama mwanadamu tu….ila..tofauti yake ni hiyo kuwa matendo yake yalikuwa na utofauti kidogo na watu wengine, kwa jinsi walivyozoea..’akasema baba mwenye nyumba

‘Tunakuuliza tena hili swali kwa kumbukumbu zetu, maana kama itatokea kuwa ulimuona..na unatuficha, sheria itachukua mkondo wake, sikufichi ndugu, hapa tunaongea kirafiki, lakini ukifika kwenye anga zetu…hutaaamini…utajuta kuzaliwa..’akasema

‘Ina maana mnanitisha?’ akauliza.

‘Sio kwamba tunakutisha…, ila tunakuambia ukweli, sisi tuna njia nyingi za kupata ukweli..kuna njia hii ya kirafiki tu, kwa raia wema wanashirikiana nasi tunapata tunachokitaka basi mambo yanaishia kwa usalama kabisa lakini kwa wale wanaojifanya vichwa ngumu,..hatuna jinsi….tunakwenda kama wanavyotaka wao..hujawasikia watu kaam hao, hujawaona…..?’ akauliza

‘Afande, huko unapokwenda sio sahihi, tangu mwanzo nimejaribu kuwajibu maswali yenu, na nikawajibu kwa jinsi ninavojua, nikasema ukweli wote, ili kusaidia kama raia mwema…, kwanini sasa msiniamini kwa hili, na surayake itasaidia nini kwenu..mimi hapo sielewi ina maana na nnyie mnaamini kuwa huyo mama hakuw amtu wa kawaida….ni..ni …?’ akauliza huku akishindwa kumalizia hicho alichotaka kusema.

‘Sisi tunajua kwanini tunakuuliza hivyo na wajibu wako kutujibu,…je kama huyo mama alikuwa mhalifu sehemu fulani, na sasa kaamua kuja kujificha hapa ili asionekane…’akasema huyo askari

‘Lakini huyo mama yupo hapa,…na kwa urahis kabisa mnaweza kumuona, kwasababu keshakufa, hawezi kuzuia kumuona, au…. kama mnataka kuthibitisha kwanini msiende kumuona wenyewe,…mnaogopa nini..’akasema kwa sauti kubwa kidogo.

‘Unajua sisi tunakuuliza maswali mengine kukupima ulivyo, je wewe ni mkweli, …unaona eeh…tunaweza hata kukuuliza swali wewe ukaliona ni la kitoto, lakini sisi tuna malengo yetu..nia ni kukupima ukweli wako, ….’akasema

‘Najua….mnataka kunibambikia kesi ..nyie ndio kawaida yenu mkishindwa kupata ukweli, mnalazimishia mambo…acheni hizo bwana…’akasema

‘Ndugu, sisi tunajua ni nini tunachokifanya..naona tukuambie ukweli…ili ujue hilo,sio kwamba tunaogopa kwenda kumfunua na kumuona huyo mama, …marehemu..kwanza kwanini, tuogope, na wenzetu wapo wanaifanya hiyo kazi, tulichotaka kutoka kwako ni kujua ukweli kutoka kwako,..ukweli wao tutakwenda  kuulinganisha na ukweli halisi kutoka kwa wenzetu..sasa kama umeamua kuficha basi….’akasema

‘Mama huyo kwa shida sana, na sio kwa usahihi,  nilimuona nilipokwenda kuona kama kateketea kwa moto…’akasema.

‘Sasa kwanini ulikuwa unatuficha..ehe tuambie alivyokuwa..yupoje.?’ wakamuuliza kila mmoja akiwa na hamasa ya kusikia atakachosema huyu jamaa.

‘Nyie mliuliza niliwahi kumuona kipindi nipo naye….sio kwenye tukio la moto, ndio maana nikashindwa kuwajibu, ila…hapo alipokuwa hajitambui mimi nilimfunua nikitafuta upenyo wa kuweka vidole ili kupima mapigo ya moyo kwenye mshipa wa shingoni…kuhakikisha kuwa yupo hai, na ili aweze kupata hewa, maana alivyokuwa kajifunika asingeliweza kupumua vyema..’akasema

‘Eheee, unaona eeeh,ile hamu ya kutaka kumuona, kama ilivyo kwa wengine ikakujia, ukaona kuwa wakati ndio huo..au ulikuwa na sababu nyingine..hebu tuambie ndugu…?’ akaulizwa.

‘Sababu gani nyingine mbona siwaelewi?’ akauliza huku akiwa kakunja uso.

‘Hebu tuambie ukweli, ….wewe na huyu mama hamjawahi kujuana kabla…?’ akaulizwa swali na akajikuta kama mtu kapigwa na kitu usoni, akahisi kichwa kikilia nziiiiiiii, akakunja uso kama kukasirika , akatikisa kichwa kama kuondoa hayo mawingu, halafu akajikuta akisema;

‘Kujuana na huyu mama !?, wapi , mbinguni…au…mbona siwaelewi…?’ akauliza na kabla hajaendelea mara mkuu wa hao askari aliyekuwa kundi la kumchunguza huyo mama akaingia.

‘Samahani kuwakatiza, lakini hili ni muhimu sana..’akasema.

‘Afande hakuna shida, tulikuwa tunamuhoji ndugu yetu na tunaendelea vyema sana, na sasa tulitaka kupata ukweli wake maana yeye ndiye aliyekuwa akiishi na huyo mama, kwa kipindi cha muda,..akawa analea mtoto wake,…walipata bahati hiyo maana wenzake wanakuja kuipata ile baraka ya mkono wake, lakini wao baraka ilikuwa ndani…’akasema

‘Sawa sawa, nimekuelewa, lakini kuna jambo muhimu sana..’akasema mkuu wao huyo.

‘Ndio afande,..’akasema huyo askari aliyekuwa akimuhoji huyo baba mwenye nyumba, akimuangalia mkuu wake wa kazi.

‘Sisi tunamuhitaji huyu mtu huko …kuna kitu tumeona ni muhimu yeye awepo,..’aaksema akimuangalia baba mwenye nyumba.

‘Eti….si wewe uliyemuona huyo mama, yaani wewe ulikuwa mtu wa kwanza kumuona huyo mama baaada ya moto?’ akaulizwa baba mwenye nyumba na akili ilikuwa haijatulia vyema akasema;

‘Unasema…kwenye moto..ndio mimi ndiye niliyemuona…’akasema

‘Mbona unakuwa kama hujiamini, unaulizwa swali na mkuu…je wewe ndiye mtu wa kwanza kumuona huyo mama baada ya moto kuisha, ?’ akauliza yule aliyekuwa akimuhoji kabla

‘Nimesema ndio…kwani nimesema vipi, sijakataa..’akasema baba mwenye nyumba kwa hasira.

‘Usijali, tunachohitajia ni ukweli wako…maana wewe ndiye uliyemuona kwanza, na pia wanasema wewe ndiye uliyethibitisha kuwa huyo mama amekufa, kweli sio kweli?’ akaulizwa na kubakia kimia, akawa anajiuliza akilini ina maana yeye alipotoa kauli ile kuwa huyo mtu keshakufa, hakuna aliyetaka kuthibitisha zaidi…,

Lakini ana uhakika yeye alimuona huyo mama akikakata roho, na dalili zote za kukata roho zilikuwepo, hakumbuki kumchunguza zaidi..lakini hata hivyo..hana shaka yule mama alishafariki, kama ingelikuwa bado muda wote huu angekuwa ameshazindukana, sasa wanataka nini zaidi, ..akawa anawaza.

‘Ni kweli afande, mimi nilipofika nilimpima kwa vidole, mkononi na shingoni,…kwanza alionekana yupo hai, alikuwa hajakata roho, ..lakini baadaye akapiga zile tatu, tatata… za kukata roho, kujivuta mguu, mara tatu, akawa kimia..kimia kabisa..

‘Kwahiyo afande…mmh, na …kwa hali aliyokuwa nayo, mimi niliwaambia mtu huyo mtu keshakufa….mimi niaondoka nikawaachia wao wakiendelea, walitakiwa na wao kuthibitisha hilo…sasa mimi sijui..’akasema.

‘Je hukuhakikisha tena kwa vidole..maana mwenzetu wewe ni mtaalamu, ukajua kuwa kweli keshakata roho..?’ akaulizwa.

‘Lakini kwanini mnaniuliza maswali hayo, huyo mtu yupo mikononi mwenu, mnaye,au si yupo mikononi mwenu…bado tu mnanisakama kwa maswali ni kama vile mnanishuku kwa jambo fulani…je mumeona nini kwake?’ akauliza.

‘Swali uliloulizwa na mkuu, je uliweza kuhakikisha tena kuona kuwa amekata roho, au hizo dalili za kutikisha miguu kama mtu anakata roho, kwako zilitosheleza kuonyesha kuwa ameshafariki?’ akauliza yule askari aliyekuwa akimhoji awali, na yeye akasema;

‘Hivi…mbona siwaelewi, …ina maana huyo mtu kazindukana, kafufuka..kiukweli, hata ingelikuwa na nyie mngajua hilo…sikuwa na haja ya kumchunguza tena kwa vidole, nilijua tu ameshakufa, kwa hali aliyokuwa nayo,…na zile dalili…hata hivyo mimi niliondoka nikawaachie wengine wenye mamlaka,…je wao hawakuthibitisha…walitakiwa kuanya hivyo…’akasema.

‘Wewe uliwahi kuwa docta?’ akaulizwa

‘Nilianza kusomea…, lakini nikaishia kati nikaamua kujiunga na fani nyingine..kwasababu zangu binafsi…’akasema

‘Kwanini ulibadili fani,…hatuhitajiki kuzitambua hizo sababu?’ akaulizwa

‘Niliona hakuna muelekeo,…hasa nilipoona madocta awali walivyokuwa wanalipwa, ..maisha yao ni kama wanavyofanyiwa walimu, nikaona huko hakunifai, nikageuza kibao na kusomea mambo mengine..’akasema

‘Kwahiyo una ujuzi wa kidakitari japokuwa sio kamilifu au sio?’ akaulizwa

‘Ndio nilikuwa nimeanza kusomea,..siwezi kujinadi kuwa nilikuwa na fani hiyo, maana sikuingilia undani wake, ilikuwa ni mwanzoni tu mnafundishwa…aaah nikaona huko hapana sitakuweza, basi nikaamua kubadili mchepuo na kuijiingiza kwenye mchepuo wa masoko na manunuzi(sales and marketing) ‘akafafanua kwa kiingereza.

‘Kwahiyo kwa ujuzi huo mdogo, ukajua kuwa huyo mama amekata roho au sio..ndio mkuu anakuuliza hivyo…’akasema huyo askari.

‘Sio swala la ujuzi,..hata uzoefu tu kwa mtu mzima, ambaye umewahi kukutana na watu wakikata roho utajua huyo mama alikuwa anakata roho….maana alifikia sehemu akazima …watu wakaanza kuja,..muda huo nilishachanganikiwa, nimechoka,nikaona niondoke niwaachie wenzangu waendelee…pale kulikuwa na joto, hewa ngumu, sikuweza kukaa zaidi…ndio hivyo’akasema.

‘Unasema wewe una uzoefu wa kuona watu wakikata roho, ulishawahi kuona watu wangapi wa namna hiyo, yaani wakikata roho?’ akaulizwa.

‘Unajua maswali yenu yananipa mawazo, hiivi mnanishuku nini mimi, siwaelewi…hebu niambieni ukweli kama wanaume, je mimi mnanishuku nini mimi?’ akauliza kwa jaziba.

‘Aaaah, hebu njoo huku…’yule mkuu wao akamshika mwenye nyumba mkono, na kutoka naye hapo kwenye chumba na wale askari wawili wakasema;

‘Ei kama wanaume kweli…hahaha,….sawa mkuu,  sisi tunaendelea na mtu mwingine naona tuongee na mama mwenye nyumba, tuitieni huyo mama…sijui nay eye itakuwa mume kama mke…’wakawa wanaongea wale askari wawili, huku mkuu akiondoka na yule baba mwenye nyumba.

Baba mwenye nyumba aliposikia hivyo, akahisi kama janga sasa linaikumba familia yake, anavyomjua mkewe ataongea kila kitu, na hata kile alichokuwa akikificha yeye…lakini hakuwa na la kufanya, na hakuwa anajua nini mkewe anafahamu zaidi,..na sijui hata mfanyaakazi wao watamuhoji pia,mmh, mungu aepushie mbali ….

‘Lakin nina wasiwasi gani…’akawa anajiuliza, halafu akasema

‘Mimi sina kosa, ..kosa langu ni kulinda utashi wa mtu, kama mwenyewe hakupenda kuonekana akiwa anajitambua, kwanini nitoe siri yake akiwa hajitambui, akiwa keshakufa,..mimi naona nimefanya sahihi, ..sina kosa..’akajipa moyo hivyo

‘Lakini kwanini huyu askari ananishuku..naona kama hawa watu wananishuku, ni kama vile wanajua jambo, ambalo linanihusu na mimi,..je ni jambo gani, kwanini asema; wewe na huyu mama hamjawahi kujuana kabla

Kauli ile ilijirudia rudia kichwani mpaka akahisi kichwa kinamuuma, kichwa, ikawa kichwa akajitahidi kujizuia,lakini ikawa ni shida…na huku akizidi kusikia sauti nyingine na nyingine,..akajaribu kutiliza kichwa na sasa ikaja sauti nyingine ikisema;

Tulikuambia usiseme lolote ..kama ulimuona huyo mama, hutakiwi kusema yupoje, sasa umeanza kusema,..ole wako..utakufa..utakufa…’sauti ile ikawa inasema na ile ya awali ya afande ikawa inafifia,..kwa jinsi ilivyo, akili haipo inawaza mengine, huku kashikwa mkono na fande, anakuwa kama  anakokotwa tu hajitambui.

‘Sasa sikiliza, wewe ndiye uliyemfunua kule….kwenye tukio au sio, ukahakikisha kuwa amefariki au sio...na wewe kwa bahati nzuri una utaalamu wa dakitari au sio..’akatulia akimungalia huyo jamaa, na jamaa alikuwa katulia akiwa kwenye mawazo yake.

‘Sasa,…sisi yupo mtaalamu, ndio..lakini kapatwa na dharura….hajitambui..unemuona yule kalala pale..’akasema na mwenye nyumba akageuka kumuangalia huyo anayeonyeshwa,, akamuona ni yule askari aliyekuwa akaimfunua huyo mama, hapoa akshituka, akili ikaanza kufanya akzi tena, akauliza;

‘Kwani imekuwaje..?’ akauliza sasa akijaribu kupambana na maumivu ya kichwa

‘Aaah, nahisi hajisiki vyema, toka tulipotoka naye huko ofisini alikuwa akidai kichwa kinamuuma, sasa na tukio hili linaonekana limemuathiri sana, unajua huyu mama, haeleweki…kuna mambo tunataka msaada kutoka kwako, wewe ulikuwa unaishi naye na unamfahamu vyema, kwahiyo kwako haitakuwa ni taabu sana..’akasema

‘Kwa-kwa-kwahiyo mnataka mimi nifanye nini?’ akauliza huku akianza kuhisi jambo, akawa anaanza kujihami.

‘Usijali, au kuogopa,..unajau maiti anatakiwa sana sana kukaguliwa na wanandugu kuhakikisha kuwa ni ndugu yao, au sio..lakini pia sisi kama askarii eeeh, tunahitajia kumpiga picha ili kama ikibidi tukatangaze , ili ikiwezekana ndugu zake waje kumuona au kumchukua, au sio..?’ akauliza yule afande.
‘Sasa tatizo ni nini, kwanini hamfanyi hivyo..haina haja ya kuniomba mimi kibali..kwanza hata hivyo mimi sio ndugu yake….sio mtu wake wa karibu..ni watu tulioamua kukaa naye tu…kwani kuna tatizo hapa?’ akauliza.

‘Unamuona yule….yule yupo kitengo cha udakitari ..nilikuwa naye hapa…sasa hajiwezi, kichwa kinamshumba ndio nikaaona nikuchhukue wewe unisaidia,..si umesema wewe umesomea udakitari, unajua jua..nakumbuka uliniambia wakati naingi, si ndio…?’ akauliza

‘Hapana…nitaka..na sikuweza kuusomea..hata hivyo afande, kwani ni tatizo sana kumfunua na kumpiga picha..?’ akauliza

‘Unajua kuna tetesi kuwa huyu mama hakutaka sura yake ionekane na mtu baki..sana sana ni ndugu zake na jamaa zake, hasa nyie mliokuwa mkiishi naye karibu,..nimesikia wenzangu wakisema walikuwa wakikuhoji kama uliwahi kumuona sura ya huyo mama, na ukawa unawaelezea alivyo, au..sio, kwahiyo kwako wewe ni rahisi..au sio’akasema

‘Rahisi kufanya nini,..afande, naona nyie mnakwepa majukumu yenu, mimi, siwezi kufanya mnalotaka …naona kama…hahaha afande, nimeshawashitukia, kama huyo mwenzenu kajaribu kumfunua yaka mkuta yaliyomkuta, mnataka na mimi yanikute hayohayo..mumenoa…siwezi…’akasema huku akirudi kinyume nyume

‘Aaah, wewe si ulikuwa unaishi naye bhanaa..eeh?’ akasema huyo afande kwa sauti ya chini kwa chini.

‘Afande, kwanza kiukweli hata mimi  kichwa kinaniuma sana…naomba nikatafute dawa, …unajua nikuambie kitu kama huyu mama angekuwa hai angekitibu hiki kichwa, hua inatokea hivi, nikisemakichwa kinauma, akikishika tu kinapona…, ‘akasema

‘Oh, kumbe,…kwako haitakuwa ni shida….wewe fanya hivi, mpiga picha yupo wapi tena, tusaidia, jambo, nenda kamfunua halafu mpiga picha atafanya kazi yake na tumemaliza kazi, unasemaje?’ akawa akama anauliza

‘Afande kichwa kinaniuma..sitanii, mara nyingi kichwa changu kikiuma hivi, akinishika kichwa huyo mama kinapona, sasa ndio huyo..’akasema na kugeka kumuangalia huyo mama pale alipolazwa…ile kugeuza kichwa kuangalia,..akashituka, ule mshituka wa kama kuruka,

Na afande aliyekuwa karibu yake, akaruka hatua mbili nyuma kama kukwepa kitu, huku akauliza

‘Kuna nini tena, umeona nini….’

NB: Kidole kinauma, tuonane kesho

WAZO LA LEO:Kuna watu hupenda kukwepa majukumu yao, hasa pale wanapoona kuwa jambo hilo au kazi hiyo ina matatizo, au ni ngumu kwao,…hawataki kusema moja moja kuwa imewashida, au ina jambo ambalo wanaliogopa,… lakini hapo hapo, wanahitajia masilahi yake au faida yake au sifa kutokana na jambo hilo  au kazi hiyo. Wanachofanya watu hao ni kusakiziana, au kuwategea wengine waifanye, huku wakisubiri matunda yake wayafaidi pamoja.


Huu kiukweli sio uungwana, kama kuna jukumu au tatizo liangaliwe kihekima, au litafutiwe njia yenye muafaka kwa kusaidiana…, na sio kukwepa wajibu na kuusogeza jukumu hilo kwa mwingine kwasababu mbambali. Wajibu ni dhima, na kila anayestahiki ana takiwa kuwajibika nao, ndio kujitoa muhanga huko, kwa nia njema na kwa malengo ya kulitaua hilo tatizo, ukikwepa wajibu wako, utaulizwa,..
Ni mimi: emu-three

No comments :