Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, February 11, 2015

NANI KAMA MAMA -31


 ‘Nimesema nataka mtoto wangu….kama hutaki kunipa mtoto wangu nitamchukua mwenyewe, ni mtoto wangu….mimi  nataka mtoto wangu, unanisikia…’akasema huyo mama kwa msisitizo.

‘Mhh…wewe mama una maana gani kusema hivyo, ..utafungwa, isije ikawa ndio nyie mnaoiba watoto, huyo mtoto wako ulimpa nani, au ulimpatia wapi..?’akamuuliza na yule mama kwanza akatulia halafu akasema;

‘Nilimpatia mbinguni,…unasikia nimetoa mbinguni,..na wewe ukamuiba mtoto wangu….mimi nimesema nataka mtoto wangu, nipe mtoto wangu haraka…’akasema akinyosha mikono miwili kama anataka kumvamia huyu mdada, na huyo mdada akawa anarudi nyuma kumkwepa huyo mama,

Mdogo mtu, alipoona hali sio shwari akageuka kutaka kumkimbia huyo mama, na huyo mama akawa keshamshika sehemu ya nguo yake kwa nyuma, mdada akawa najivuta ili huyo mama amuachie, lakini yule mama akawa ameshikilia sehemu hiyo ya nguo vyema, wakawa sasa wanavutana…

‘Wewe mama vipi hebu niachie utachana nguo yangu….’akawa analalamika

Mdogo mtu huyo kuona vile akawa anarudi kinyume nyume kufuata jinsi anavyovutwa na huyo mama, kwa nyuma huku akijaribu kuvuta nguo yake, huku akichelea isije ikachanika…. na watoto waliokuwepo hapo wakawa wanashangilia kama vile wameona mchezo..yule mama akawa anavuta huko akisema;

‘Nataka mtoto wangu, nipe mtoto wangu, umeniibia mtoto wangu….’yule mama akawa anasema hayo kwa hasira na watoto nao wanamuigizia, huku wakiruka ruka…

Mdogo mtu kuona hivyo, akawa keshatahayari maana sasa anakuwa kama anasutwa,na kuabishwa, …

Alichofanya ni kama kukubalia anvyofanya huyo mama, akasogea kinyume nyume adi akamkariia huyo mama, na huyo mama akaachia hiyo nguo na kusema;

‘Haya nipe mtoto wangu…’akasema

‘Yupo wapi huyo mtoto wako..?’ akamuuliza

‘Unaye….umemficha..namtaka haraka…’akasema

‘Nimemficha wapi?’ akamuuliza

Yule mama, akamsogelea na kwa sauti ya kunong’ona akasema

‘Najua wapi ulipomficha, nitakwenda kumchukua….’akasema

Mdada akageuka huku na kule, akiogopa watu wasije kumuelewa vibaya ionekane kuwa kweli yeye kamuibia huyo mama mtoto,… japokuwa alishasikia kuwa huyo mama anamfanyia hivyo kila mtu.

Kwa haraka akanyosha mkono kwa mtu wa bajaji, aliyekuwa akipita, na huyo mtu wa bajaji akafika,na kumsaidia kumuachanisha na huyo mama, na wakati anaondoka yule mama akasema kwa sauti;

‘Umenisikia eeh, nitakwenda kumchukua huko ulipomficha…’akasema na wakati huo bajaji ilishaanza kuondoka kwa mwendo wa kasi…

‘Huyo mama balaa, mimi simuamini, ….’akasema dereva wa bajaji

‘Anatokea wapi?’ akauliza mdada.

‘Nani anajua…mimi nahisi kachanganyikiwa tu, japokuwa watu wanadai kuwa ni mama sijui kutoka mbinguni lakini…..ni mwehu tu….ila maadui wake wakubwa ni akina mama…hawapendi akina mama..’akasema.

‘Kwanini anasema kuwa anataka mtoto wake?’ akauliza

‘Inavyoonekama alizaa halafu watu wakamchukau mtoto wake kwa vilekachanganikiwa, maana hali kama hio ataweza kulea mtoto…’akasema mwenye bajaji

‘Ulishawahi kumuona sura yake?’ akauliza

‘Mhh, ukitaka mkosane, jaribu kumfunua, kuna mtu alijaribu kufanya hivyo, alichokipata hata kisahau,…anaugulia macho…yupo kitandani mpaka sasa….’akasema

‘Alifanywa nini…?’ aakulizwa

‘Huyo jamaa hataki hata kusema….kawa kama kachanganyikiwa, na huyu mama akisema nitafanya, au utapata tatizo ulani , ujue litatokea, ndio maana wanamuita mama kutoka mbinguni…..’akasema huyo dereva wa bajaji

‘Oh, sasa naona hii ni hatari, ngoja niwapigie ndugu zangu simu….’akasema huku akichukua simu yake kwuasiliana na dada ake na shemejiye.

Tuendelee na kisa chetu…..

***********

Huku kwa mama yaani dada mtu, hali ikaendelea kuwa shwari…japokuwa mawazo ya hapa na pale ylikuwa yakitokwa hasa akiwa peke yake hana kazi, anajaribu kuwazia yale yaliyotokea hasa kuhus mtoto na kufanana kwake na mumewe lakini alifikia hatua akaona ni kudra ya mungu ipo siku atajua ukweli.

Alikumbuka pia kuwa alipokea simu kutoka kwa mdogo wake siku alipoondoka kuwa wawe makini na huyo mama, ..simu hiyo iliwafanya wawe walinzi, na kila akitoka alikuwa akicha onyo kwa mfanyakazi, kuwa mama huyo akifika hapo, ahakikishe mtto yupo ndani salama..

‘Kama atajaribu kufanya fujo piga kelele, na simu hii hapa nipigie haraka…unasikia…’akaambiwa mfanyakazi.

Kwahiyo kipindi cha siku tatu wakawa wanaishi kwa mashaka, lakini hakuna lolote liliwahi kutokea,  na hata kule kupita pita mitaani kwa huyo mama akiimba kukawa kumepungua kwa kiasi kikubwa, mama huyo akawa anaonekana mara chache chache, hadi wiki mbili zikapita. Watu wakaanza kumzoea, na kumuona ni wa kawaida tu.

Wiki mbili zikapita, familia hii ikawa ni familia yenye mtoto, na kila aliyekuja alitambulishwa kuwa huyo ni mtoto wa familia hiyo, wamempataje, ikawa siri yao, kwani hakuna mtu aliyewhi kumuona huyo mama akiwa na mimba.

‘Mimba nyingine hazionekani wazi..huyu mama muda wote huwa anavaa gauni pana huenda alikuwa mja mzito, mimi niliwahi kumtania kuwa ana mimba akaniambia aipate wapi…sasa sijui kama alikuwa akinitania au…’watu wakawa wanaongea.

‘Haiwezekani..mimi hilo sikubaliani nalo, labda kama mtoto huyo kaletwa,na-nasikia kuna siku mdogo wake aliwahi kufika kwa siri, mimi nahisi mdogo wake alijifungua akaona amleta huyo mtoto hapo kwa dada yake…’akasema mwingine.

‘Kwanini afanye hivyo, kwani yeye hawezi kulea..au kuna siri gani kati yao…?’ akauliza mwingine.

‘Tunasema kama huenda mdogo wake alifanya hivyo, lakini sina uhakika, nimejaribu kumuuliza huyo mama, lakini anadai ni mtoto wake alijifungua usiku…unakumuka alikuwa anaumwa umwa…’akasema

‘Yawezekana, …halafu kinachofanya tuamini kuwa ni mtoto wao, ..mtoto huyo anafanana sana na mume wa huyo mama..kabisa kabisa…sasa hapo utasemaje…’akasema mwenzake.

‘Mhh, mimi sijawahi kwenda kumchunguza..kama ni hivyo basi yawezekan kuwa ni kweli,hata hivyo iweje mtu ajifungue na kuendelea na shughuli zake kama kawaida, ndipo hapo tunamtlia mashaka, mzazi akijiungua angalau siku sana anakaa nyumbani….’akasema

‘Na pia yawezekana ikawa kuna jambo jingine…mimi nahisi kuna jambo limetokea ndani ya hiyo familia, lakini wameamua kuliicha kifamilia, wewe unawaonaje hao watu…’akasema mwenzake

‘Umeanza..jambo gani hilo jingine…mimi nawaona kama kawaida tu..kwani wewe unahisi kuna nini kimetokea, zaidi ya huyo mtoto?’ akauliza mwenzake.

‘Hawa wapendwa wamekaa siku nyingi bila kuzaa, huenda walipanga huyo mume aende kujaribu sehemu nyingine mbali, …halafu akizaliwa mtoto wamchukue..hilo lawezekana pia, au nikuambie kitu huyo mdogo mtu anaweza akatembea na shemeji yake akapata mtoto kwa siri, akamleta kwa siri, wewe waonaje hilo….’akasema

‘Mhh, hilo mimi sijui…na achana kabisa na hizo tetesi zisizi na mshiko,wakikusikia wenyewe, utafungwa..unaifahamu ile familia haitaki majungu kabisa, na yule mama mimi namuheshimu kweli, ukiwa na lako anakupasha waziwazii, unabakia kuaibika, mimi nakushauri haya yaache kama yalivyo…’akasema mwenzake.

‘Mimi nimesema tu, wala…simuambi mtu mwingine nimekuambia wewe tu na mume wangu…na wewe ukimuambia mume wako shauri lako..mume wako hana dogo….’akasema

‘Acha majungu wewe..mimi sipendi hiyo tabia yako…mume wangu hana dogo umemjulia wapi kuwa ahan dogo, mama nanihii hiyo tabia yako tutakosana, kaa na mume wako, achana na waume wa wenzako, achana na familia za wenzako kila mtu anajua mambo yeka….nimekukanya siku nyingi, tutakuwa hatuongei tena mimi na wewe…’akasema mwenzeka, na huyo mama akaonyesha ishara ya kufunga mdomo, na wakaachana na mwenzake.

Kwahiyo siri ya mtoto huyo ikawa ndani ya familia hiyo hata mfanyakazi wa ndani alijua kuwa mtoto huyo ni wa huyo mama, hakutakiwa kusema zaidi, hata pale alipomdadisi huyo mama kwanini hamnyonyesi huyo mtoto.

‘Matiti yangu yana matatizo…nimeshauriwa kuwa nisimnyonyeshe maziwa yangu, atakuwa akitumia maziwa hayo ya unga…’akasema mama mwenye nyumba.

‘Lakini matiti yako hayafanani kama mtu aliyewahi kuzaa..na iweje ujifungue nab ado uwe na nguvu za kufanyakzi, mimi nasikia mtu akijifungua anaakaa nyumbani siku…40, au….?’akasema huyo mfanyakazi na akawa kama anuliza.

‘Kwanza wwe uliwahi kuyaonea wapi matiti yangu?’ akauliza mama mwenye kwa uso wa mshangao.

‘Wakati mwingine wewe huwa unavaa khanga, na nguo ya kuonyesha , matiti yako yanaonekana bado madogo, tofauti na akina mama waliojiungua karibuni…’akasema

‘Acha kabisa hiyo tabia, mambo ya hapa ndani yaache kam yalivyo, wewe umekuja kwa kazi sio kuchunguza chunguza ammbo ya humu ndani, mimi mwenyewe nimeamua kuwa hivyo sio lazima kila mwanamke anayejifungua kupumzika hizo siku inategemeana na afya na mazoea ya mtu….kumbuka nikuambie, nyumba hii haitaki majungu ..umenielewa..’akaonywa, na kweli huyo mfanyakazi akawa kimia hakuwahi kuhoji tena kuhusu huyo mtoto au familia hiyo.

Kwahiyo ikawa ni siri ya familia, na ikajulikana hivyo kuwa familia hiyo ina mtoto na mtoto huyo huenda kazaliwa kimuijiza, mambo ya kijijini yakaenea hivyo na kufifia hivyo.

Mama wa kufikia, akawa amejipanga vyema katika shughuli zake, miradi yake ikawa inaendelea vyema, ikawa na baraka, wateja wengi,…utafikiri neema hiyo ililetwa na kuja kwa huyo mtoto, kwa kuongezeka kwa biashara na wateja, mama huyo ikabidi atafute mtu wa kumsaidia katika baishara zake, na hapo akawa anapata hata nafsai ya kurudi rudi nyumbani kuona kinachoendelea.

  Basi mama huyu akiona kwenye biashara yake kupo shwari, anamuachia huyo msaidizi wake kazi za kuendelea na biashara yeye anakimbilia nyumba mara moja kuona kinachoendelea nyumbani kwake,   alifanya hivyo kuhakikisha kuwa huyo mfanyakazi hafanyi makosa…na bahati nzuri mfanyakazi huyo alijua nini cha kufanya kwa wakati gani…akawa muda wote yupo nyumbani na mtoto.

Na, siku zikapita,…mawiki , yakapita, inakaribia sasa mwezi …

Siku moja wakati anarudi nyumbani,  akashangaa, kuwa yule mfanyakazi wa ndani kakaa nje na yule mama wa ajabu wakiongea! Siku hiyo alipata mshutuko wa aina yake, akakumbuka onyo kutoka kwa mdogo wake, akajiuliza kulikoni!

Kwanza hakutaka kuwashitua, akaingia ndani na kufanya shughuli zake, alipotoka hakumuona huyo mama wa ajabu, siku hiyo hakusema lolote, siku ya pili yake ikawa hivyo hivyo, na ilipotokea hivyo siku ya tatu, mama huyu akaona amuulize huyo mfanyakazi wake,..kwani siku hiyo ya tatu alimuona huyo mama wa mitaani akiwa kambeba mtoto wao.

‘Vipi wewe, mbona unampa huyo mama mtoto, hujasikia nilivyokuambia, unamfahamu huyo mama alivyo huwa anadai kuwa anataka mtoto wake, na kila mwenye mtoto mdogo anadaiwa kuwa kamuibia huyo mama mtoto, sasa kwanini hutaki kunisikia ….?’ Akamuuliza huyo mfanyakazi na huyo mfanyakazi akasema;

‘Mama, huyu mama wa ajabu, anampenda sana huyu mtoto wako, na hutaamini, kila mara huyu mtoto akilia sana, mama huyu hutokea, na akimshika huyu mtoto kichwa, basi mtoto hutulia kabisa….’akasema huyo mfanyakazi akonyesha uso wa furaha kama vile hilo aliloambiwa halina maana kwake.

‘Mimi nimeshakukanya, kama hutaki kazi usema,..huyo mama anadai kuwa anataka mtoto wake kwahiyo kila mtoto mchanga ni wake…anaweza akaondoka na huyo mtoto unafikiri utamapata wapi, unafahamu wapi huyo mama katokea, nakuambia ukweli, siku mtoto akitoweka, ujue unakwenda kuozea jela….’akasema

‘Ni kweli kila mahali kwenye mtoto mchanga, mama huyu hufika na kumbeba mtoto, nimeulizia kwa majirani wenye watoto, lakini hafanyi lolote baya, ndio hivyo mtoto akilia tu huyu mama akifika akamshika huyo mtoto kichwani, mtoto anatulia…mimi sioni ubaya wake….’akasema.

‘Kwahiyo sio hapa tu, anafika popote kwenye mtoto mchanga?’ akauliza mama mwenye nyumba.

‘Ndio mama, sio hapa tu, ..anafika sehemu yoyoye yenye mtoto mchanga,..ni kipenzi cha watoto, sio wachanga tu….na sikutaka kukuambia mapema karibu siku nyingi huyu mama anafika hapa…’akasema

‘Sasa kwanini hukuniambia….’akasema mama mwenye nyumba kwa hasira.

‘Mama sikukuambia tu, mtoto wako anakuwa analia sana ukiondoka,  kila nikimpa maziwa hataki, lakini akifika huyu mama…mtoto ananyamaza, ….hutaamini, mama huyu anamchukua anamnyonyeshwa maziwa anamshika kichwa, mtoto ananyamaza kabisa utafikiri ….’akasema

‘Anamnyonyesha maziwa! Maziwa gani hayo?’ akauliza kwa mshangao

‘Hayo tunayomtengenezeaga kila siku…’akasema kwa wasiwasi akionyesha  kuogopa.

‘Yaani umeamua kumpa yeye hata maziwa, ina maana wewe umeshindwa kumnyonyeshaa mtoto wangu, si ndio kazi niliokuchukua nayo, kwanini unafanya hivyo…?’ akauliza mama akiwa kakasirika kweli.

‘Mama wewe hujui tu, ..sio kwamba nimeshindwa kufanya hivyo, mbona nafanya siku zote, ila inatokea tu,…mtoto akianza kulia, hata ufanye nini hanyamzi, ni mpaka huyo mama afike,….’akatulia

‘Eti nini….?’ Akuliza mama mwenye nyumba kwa mshangao.

‘Yani akianza kulia, hanyamazi,…mpaka huyo mama aje…na inabidi akifika nimpe yeye ndio anamfanya ananvyomfanya, basi ananyamaza,…’

Anamfana nini mtoto wangu, mbona unanitisha….?’ Akauliza

‘Mama mtoto akianza kulia mwenyewe utamuonea huruma,…na anayeweza kumtuliza ni huyo mama…’akasema

‘Mbona hujaniambia …kuwa mtoto ana tatizo hilo?’ akaulizwa

‘Kulia kwa mtoto ni kawaida, na kama huyo mama kambembeleza akanyamaza, mimi sikuona haja ya kukuambia…kwahiyo nikaona akianza kulia namtafuta huyu mama anakuja, anampakata, na hapo ndio naweza kufanya kazi zingine  vinginevyo, hata sijui ningefanyaje..’akasema

‘Mmi hata sikuelewi..kwanini hjaniambia hapo ndio naona umekosea maana nilishakuambia kama kuna tatizo lolote, kama kuna mabdiliko yoyote kwa mtoto uniambie….haya kaam mtoto ana tatizo, mimi ningelijuaje hayo…’akasema

‘Mama mimi sikuona kama ni tatizo, kwani kama ingelikuwa ni attizo, angeliendeela kulia, huyo mama nahisi ana karama…anajua kwanini analia, akimpakata anajua jinsi gani ya kumfanya, na mtoto hutulia,..ipo siku mwenyewe utaona,..kiukweli, mama huyo hana tatizo,watu wanamuelewa vibaya bure, ukikaa naye ndio utamgundua, anaongea vizuri tu, anapenda kuimba nyimbo za kubembeleza watoto,….’ akasema yula mfanyakazi wa ndani.

Huyu mama kusikia hivyo akaona afanye uchunguzi mwenyewe wa kina,….siku moja akarudi mapema, wakati huyo mfanyakazi yupo nje na mtoto, alianya hivyo akihakikisha huyo mfanyakazi hajui kuwa yupo ndani, …akiwa ndani akijaribu kujipumzisha kitandani, mara akisikia mtoto akianza kulia, yule mfanyakazi akawa anambembeleza, lakini mtoto hakutulia kulia, kile kilio kikampa mashaka mama mwenye nyumba, akataka kutoka nje aone mtoto kwanini analia.

Wakati keshajiandaa kutoka, mara akasikia sauti

‘Na-nataka mtoto wangu..’ akajua ni huyo mama wa mitaani, akachungulia dirishani, na yule mfanyakazi kwa vile hakujua mama mwenye nyumba yupo, akawa anaongea na huyo mama, kama vile wamezoeana,…lakini hakusikia wanaongea nini.

Mara yule mama akamsogelea yule mfanyakazi akiwa anamchukua mtoto kutoka kwa yule mfanyakazi…kuna hali ilitokea kama vile huyo mfanyakazi anasita kumpa huyo mama mtoto, akawa anaangalia huku na kule, kama kuhakikisha kuwa hakuna mtu halafu akampa yule mama wa ajabu huyo mtoto.

Yule mama wa ajabu akamshika yule mtoto akawa kama anambembeleza, akatafuta sehemu akakaa na huyo mtoto, akaonekana akimshika kichwa huyo mtoto,na yule mtoto akanyamaza!

Baadaye yule mfanyakazi akampa yule mama wa ajabu chupa ya maziwa, na yule mama akaipokea, na kuanza kumnyonyesha yule mtoto, huku akionekana kama kuimba kwa sauti ya chini, au kumbembeleza mtoto, badaye yule mama wa ajabu akamuashiria yule manyakazi amchukue mtoto, mtoto alikuwa amelala.

Yule mfanyakazi akamchukua mtoto na kwenda kumlaza kwenye kitanda chake cha kutembea kilichokuwepo hapo nje…ikatokea wakati huyo mfanyakazi akataka kuingia ndani, akaonekana kuongea na yule mama…hili likampa mashaka huyu mama mwenye nyumba, kuwa kama huyu mfanyakazi anaweza kumuachia huyu mama mtoto ni hatari.

Huyu mfanyakazi akaingia ndani,  na wakati anaingia ndani ndio huyu mfanyakazi akagundua kuwa mama mwenye nyumba yupo, akataka kugeuka kutoka nje, kwenda kumchukua mtoto, na huyu mama mwenye nyumba akawa kasimama pale pale dirishani akiangalia nje, hakumumini kabisa yule mama wa mitaani, alitaka kuhakikisha huyo mfanyakazi anatoka nje kumchukua mtoto;

‘Oh, kumbe umefika..sikukuona ukiingia ndani…’akasema huyo mfanyakazi, baada ya kutoka nje na kumchukua mtoto na kuingia naye ndani

‘Hamna shida, huyo mama wa ajabu keshaondoka?’ akauliza huyo mama akijaribu kuficha hasira zake, na huyo mfanyakazi akawa kama kashituka na kusema;

‘Eeeeh, kaondoka….’akasema na huyo mama mwenye nyumba hakusema neno kwa muda ule, ila akilini alijawa na mawimbi ya hasira akitamani amfukuze tu huyo mfanyakazi,…, alijiuliza kwanini mfanyakazi wa ndani hatekelezi hilo, mengine akiambiwa anatekeleza , na anajituma kweli , kila kitu anakianya vyema, lakini hilo la mtoto na huyo mama wa mitani linakuwa gumu.

Mama huyu akataka kufanya utafiti zaidi, kabla hajachukua maamuzi mengine au kumuambia mume wake, siku nyingine akafika tena, bila mfanyakazi kujua, akiwa ndani akasikia mtoto akilia sana…kilia cha sasa kilikuwa kikali kweli,  kilio kama mtoto kaumwa na kitu…, mama mwenye nyuma akakurupuka kwa haraak kutaka kutoka nje kwa haraka, ili akamchukue mtoto, amuangalia kama kuna tatizo, kwa muda huo mfanyakazi wa ndani alikuwa kambeba anambembeleza…..

Mama huyu alipofika mlangoni kutaka kutoka nje, huyo mama wa mitaani akatokea, akiwa kajifunga uso wake kama kawaida, huku akiimba nyimbo yake akiwa na watoto wachache ambao walipofika hapo kwenye aneo la hiyo nyumba, wao wakasimama, na kuafuta sehemu ya kukaa mbali mbali kidogo na hapo, wakimsubiria huyo mama, na huyo mama alipoona huyo mtoto analia, akamkimbilia yule mfanyakazi na kunyosha mikono kama kutaka kumpokea huyo mtoto.

Yule mfanyakazi, akawa anaendelea kumbembeleza huyo mtoto, lakini hatulii kulia, mwisho wake huyo mfanyakzi akageuka na kutaka kumpa huyo mama huyo mtoto, mama mwenye nyumba , pale aliposimama akatamani amkemee yule mfanyakazi , kuwa anafanya nini ..mbona anarudia yale…lakini mdomo ukawa mzito kusema kitu.

Cha ajabu kabisa, yule mtoto alipokuwa mikononi mwa huyo mama, mtoto akapunguza sauti ya kulia, ni kama vile mtoto anapojua yupo kwa mama yake na sasa kinachofuatia ni kupewa nyono….yule mama akampkata vyema, akamweka karibu na sehemu ya matiti, kama wafanyavyo wazazi wakitaka kutoa titi , ili kumnyonyesha mtoto.

Akainua mkono wake na kumshikwa yule mtoto kichwani na huyu mtoto akanyamaza ghafla, kama vile kaamiwa nyamaza, akatulia kimiya. Na yule mama wa mitaani alimbeba kwa muda yule mtoto na yule mfanakazi alikuwa kashikilia chupa ya maziwa, alitaka kumchukua mtotoa mnyonyeshe mwenyewe, lakini yule mama wa mitani akaonekana kutaka kumnyonyesha yeye mwenyewe.

Yule mfanyakazi kuona vile, akaona isiwe shida, akampa ile chupa na yeye akakaa karibu yake, akiangalia huyo mama anavyonyonyesha huyo mtoto,  akawa anamnyonyesha yule mtoto, na yale maziwa yalipoisha yule mama akamuinua ule mtoto na kumweka begani kwa muda, akawa anamkanda kanda mtoto mgongoni, halafu akamweka kama alivyokuwa kwanza wakati aanmnyonesha, hadi mtoto akalala.., halafu yule mama akamrudishia yule mfanyakazi wa ndani mtoto, na akataka kuondoka.

Yule mfanyakazi wa ndani akampa yule mama kipande cha mkate, kwani kwa muda ule alikuwa akinywa chai, yule mama akakataa na kusema yeye kashiba, ila labda awape wale watoto aliokuja nao, akapokea kile kipande cha mkate nakuanza kuwagawiwa wale watoto waliokuwa nao,  na baadaye yule mama wa ajabu akaanza kuondoka zake na wale watoto aliokuja nao,..lakini baada ya kuhakikisha kuwa yule mtoto kalala!.

Baada ya yule mama wa ajabu kuondoka mama, mwenye nyumba akajitokea pale mlangoni, akaenda pale aliposimama yule mfanyakazi wa ndani, na yule mfanyakazi wa ndani alipomuona mama mwenye nyumba,akawa katoa macho ya uwoga, akijua sasa kazi hana…

‘Nipe huyo mtoto…’akasema mama mwenye nyumba

‘Aalikuwa analia sana nikashindwa kuvumilia nikaona bora nimpe tu huyo mama, kama ungeliona…ungejua kuwa kweli huyo mama sio mtu mbaya….’akasema na mama mwenye nyumba hakusema neno.

Mama mwenye akamchukua mtoto akiwa amelala, akaingia naye ndani akamkagua vyema kuhakikisha hakuna tatizo kwa mtoto akaona yupe salama kabisa, akamlaza kitandani,  na yeye akalala pembeni yake, huku akiomba mungu kusije kukatokea jambo baya kwa huyo mtoto, kwani moyoni keshampokea kama mtoto wake.

Toka pale mama wa kufikia wa huyu mtoto akawa na mawazo sana na huyu mama wa mitaani, akajiuliza kuna nini kuhusiana na huyu mama, mbona hafanani kabisa kuwa kachanganyikiwa ki hivyo. Na kwanini muda wote huwa kajifunika uso wake na hataki kujifunua na huwa haachani na wimbo wake huo wa kusema anataka mtoto wake, na mara nyingi huwa ana kundi la watoto kama walinzi wake.


‘Hili jambo lazima niongee na mume wangu, maana lolote laweza kutokea, na isje ikatokea jambo baya nikaja kulaumiwa mimi  kuwa kwanini niliona hivyo na sikusema…na pia, lakini ngoja kwanza niongee na mume wangu..’akawa anaongea mwenyewe kimoyo moyo

 Siku huyo mume wake aliporudi, akiwa na nia ya kumuambia lakini kukatokea mambo mengine akasahau kabisa kumuambia mume wake, na alipokumbuka ikawa ni siku ya pili yake,..akasema nitamuoambia tu akirudi… na siku hiyo akatembelewa na mgeni, alikuwa mama mmoja ambaye alijifungua karibuni.

‘Oh, mzazi umeamua kuja mwenyewe, umeona kimia sijaja kukupa pongezi ya uzazi….’akasema

‘Oh, hapana jirani, …najua utafika tu,..nasikia hata wewe ummejifungua lakaini mengi yanasemwa kuwa mimba yako ni ya ajabu hata kujifungua ni kwa ajabu..hawakuwahi kuona mimba yako…hapa kijijinikuna mambo….’akasema

‘Achana na hayo mambo ya hapa kijijini , kila mtu anajua maisha yake,..nimehsjaifungua na mtoto wangu yupo salama ndilo la muhimu…..’akasema

‘Ni kweli muhimu ndio hilo, usalama …na afya, sasa mimi nimefika kwa shida..’akasema

‘Shida gani mpendwa, mpaka unijie mimi, hebu niambie maana ni bahati hiyo,mzazi kukutembelea na shida…haya hebu nambia una shida gani jirani yangu..?’akasema na kuuliza.

‘Unajua nina tatizo la maziwa, matiti yangu yana vidonda,nashindwa kabisa kumnyonyesha mtoto wangu….imekuwa ni taabu, nikaambiwa nimpe maziwa mbadala, kwanza wengine alinishauri niwe nayakamua amziwa yangu kwenye chupa…lakini wewe..nauma kweli kweli..

‘Basi nikaambiwa, kuna maziwa maalumu ya watoto wachanga,..nimeyanunua, lakini matumizi yake yananipa shida, nikaulizia watu wakaniambia kuwa wewe unamnyonyesha mtoto wako kwa maziwa kama hayo…..’akatulia

‘Ndio tunamnyonyesha mtoto wangu, kwa maziwaya kopo..unafikiri ni kazi kubwa sana, hapana muhimu ni kuangalia vipimo, maji safi ya uvuguvugu…basi…unakoroga..hutakiwi kuyachemsha kama haya ya maziwa ya ngombe….’akasema na kuanza kumuelekeza.

Alipomaliza hayo maelekezo huyo mama akawa anataka kuondoka, lakini akawa kama kakumbuka jambo, akiwa kasimama, akasema …

‘Jamani mwanangu jana hakulala,…siku nyingine inatokea hivyo, lakini cha jana kilikuwa kilio cha aina yake…kalia karibu maasaa matatu, hadi sauti inakauka,…kulia huko sio kwa kawaida,…. siunajua tena, maziwa yana vidonda, siwezi kabisa kumnyonyesha, huku kwenye chuchu kunauma kweli, na mtoto akawa anazidi kulia karibu usiku kucha

‘Tulihangaika usiku huo maana siku zote analia, tunatafuta njia nayakamua maziwa kwenye chombo tunampa aanakunywa analala, lakini usiku huo hakulala kilio na  yeye,…mimi na mume wangu tukaona sasa hilo ni tatizo, tutafute njia za kwenda hospitalini, sasa usiku huo utakwenda wapi…tuhangaika huku na kule, ..nilitamani nimnyonyeshe hivyohivyo, lakini wee…akigusa chuchu..mungu wangu….sikuweza, kwani kunakuwa kama kidonda..hooo ..’

‘Mhh pole, sana unavyoelezea nasisimuka mwili mnzima, lakini hukuwahi kwenda kwa dakitari, na kama mlikwenda dakitari alisemaje hakuna dawa a kutibu hayo matatizo…?’ akaulizwa.

‘ Tulikwenda, kuna siku tulikwenda, mwanzoni tatizo lilipoanza, …Dakitari alivyoshauri, kiusalama nimuanzishie haya maziwa.

‘Kama dakitari alisema hivyo mimi sioni ni tatiz na kulia kwa mtoto ni kawaida, muhimu ni kuona kama hajakojoa..au tumbo limembana, mnamlalisha tumbo chini ili hewa itoke…utumbo wake unakuwa umejaa hewa..au umabena kma vile unamweka begani, tumbo linalia sehemu hi ya begani,..unakuwa kama unamkandamiza kidogo mgongoni hivi….’akawa anamuonyeshea kwa vitendo…

‘asi kama sio tatizo kubwa,..atanyamaza tu….akizidi sana ujue kuna tatizo, kesho yake mpelekeni hospitalini..’akasema

‘Ohh, tulitaka tufanye hivyo, unafikiri ilikuwa na haja tena…’akasema

‘Kwanini..?’ akaulizwa

‘Unajua huyu mama wa mitaani, kumbe wakati analia,huyo mama alikuwa kalala upenuni mwa nyumba huko nje, si unajua huyu mama, hana makazi maalumu, hulala popote wanadai akilala kwako kuna baraka.

‘Mhhh..hata mimi nasikia hivyo.

‘Ndio baraka ilitushukia, maana alivyokuwa analia mtoto ningelienda wapi, huko nyuma ya nyumba alilala huyu mama wa mitaani.  Mara mtoto alipokuwa kilia, tukasikia hodi, tukawa tunashangaa, kumbe huyo mama alikuwa kalala nyuma ya nyumba yetu, sijui kelele za mtoto zilimkwaza,…

Akabisha hodi na kusema, `namataka mtoto wangu..’ tukashangaa, toka lini mtoto huyu akawa wake. Tukamdharau kwasababu huu ndio wimbo wake.

Wakti huo mtoto akawa analia ile ya kutisha, na huyu mama akawa anagonga mlango kwa nguvu, tufungue. Nilitamani nitoke nimfukuzilie mbali…maana sisi tunahangaika angalaua mtoto alale, …sasa huyu mama anakuja na usumbufu wake.., lakini baba watoto kwasababu ya joto akaamua kufungua mlango, atoke nje na mtoto huenda, analia kwasababu ya joto..mimi nikamkataza, nikasema nitabakia na mtoto ndani.

Muda huo kila mtu keshajichokea tumekata tamaa, kabisa….baba watoto bika kujali akafungua mlango, alipoona huyo mama anaendelea kubisha hodi.

 Huyo mama mlango ulipofunguliwa tu akaingia ndani, na tukashindwa hata kumzuia, akaja moja kwa moja pale nilipokaa na mtoto, wote tumeduwaa. Kumzuia tunashindwa, tukabakia kimya…Akaja pale nilipokaa, akamwangalia mtoto anavyolia, akasema `mtoto wangu nyamaza eeh..’

Akainua mkono wake, sijui alikuwa akisema maneno gani, akamshika mtoto kichwani….mara mtoto kimya, na baada ya muda mfupi mtoto akalala. Halafu yule mama bila kusema kitu huyo akatoka nje na kwenda kulala pale alipokuwa kalala mwanzoni…’Akahadithia huyo mama na kuwaacha wenzake wakiwa wameduwaa, na kabla hawajamuuliza kitu zaidi, huyo mama akaaga kuwa anamuwahi mtoto wake.

‘Mhh..sasa naanza kuhisi ..yawezekana kweli huyu mama sio mama wa kawaida…’akasema na mfanyakazi wake akasema;

‘Mimi nimekuambia mama..huyo mama hana matatizo ni mama pekee mwenye karama…ukikaa naye utalijua hili…’akasema

‘Mliwahi kuongea naye, akakuambia alitokea wapi, na uliwahi kuuona uso wake anafananaje..?’ akamuuliza..

NB habari ndio hiyo, mama wa ajabu, mara mama  wa mitaani, je ni mama gani huyu..yapo maswali mengi bado anahitajia majibu, kisa kinaendelea, tuzidi kuwepo.

WAZO LA LEO: Dharau ni kiburi cha shetani..usiwe na tabia ya kudharau wenzako, maana dharau, inamuumiza yule asiye nacho kisaikolojia, kama una uwezo wako, una utajiri wao, cheo chako, ni majaliwa yako,…kwanini umdharau yule ambaye hakujaliwa,..


Jiulize, wangapi wangapi walikuwa navyo, cheo, mali…nk, …na wengine wakafikia sehmu wakawa hawana navyo tena, ama kwa kuharibikiwa, kupoteza kazi, kufirisiki,a au kufa, hawapo tena duniani, yote hayo yachukulie kama majaliwa ya mungu kuna kupata na kukosa, yule yule aliyemfanya huyo unayemdharau asiwe nvyo ndio huyo huyo aliyekupa wewe na anaweza kufanya vinginevyo. Wewe unachotakiwa kufanya ni kumshukuru mungu kama umejaliwa kupata, ….na usione soo kumsaidia yule ambaye hajajaliwa, huo ndio ubinadamu , na huo ndio utu mwema.

Ni mimi: emu-three

No comments :