‘Ilikuwa ndoto ya ajabu kweli…’akamalizia
kuongea dada mtu na mdogo mtu akasema;
‘Hayo ni Mawazo dada, hayo ni mawazo yako
kuhusu mtoto, inabidi dada sasa uyapunguze na ikibid uyaondoe kabisa, kwasababu
sasa mna mtoto, japokuwa hamkumzaa nyie, lakini kuanzia sasa ni mtoto wenu
kisheria….’akasema.
‘Ni kweli kisheria inawezekana akawa ni
mtoto wetu, lakini je mwenyewe akiwa mkubwa, akijua kuwa sisi sio wazazi wake
wa kumzaa, unafikiri mapenzi yatakuwa ni yale yale….’akasema dada mtu.
‘Hivi ni waulize, ni nani mwenye thamani,
mzazi wa kukuzaa, ambaye hakukulea, kwasabbu hizi na zile, au mzazi wa kukulea,
ambaye alijitolea kwa nguvu zake zote kukulea, hadi kufanikiwa katika maisha
yako..?’ akauliza.
‘Mhhh, inategemea, …ukumbuke kuna hatari
za mimba, hujui huyo aliyekuzaa kateseka vipi, ..lakini yote ni sawa tu,
inategemea mtizamo wa mtoto mwenyewe , cha muimu ni kutimiza wajibu wako, maana
unaweza ukamzaa, ukamlea vyema, nab ado asikuthamini..’akasema dada mtu.
‘Umeliona hilo, eeh, sasa dada usiwaze
sana, kumbe yote yawezekana unaweza ukazaa, ulea ukatimiza wajibu wako, nab ado
usithaminiwe, na unaweza ukalea, ukahangaika weee, mtoto akakutahamini zaiei ya
yule aliyemzaa,..muhimuu ni kutimiza wajibu wako, sasa sisi tutimize wajibu
wetu…’akasema mdogo mtu.
‘Kwahilo usiwe na shaka nalo, hata kama
kuna sintofahamu ya huyu mtoto, maana mpaka sasa hujatuelezea ukweli wake,..kama
wazazi wake walikuwaje, ..sisi tutamlea sawa na mtoto tuliyemzaa wenyewe,
..nakuahidi hilo mdogo wangu, na hata ukifika huko kazini kwako ujue kuwa mtoto
kafika sehemu sahihi….’akasema dada mtu.
‘Ndio maana nilipokabidhiwa hilo jukumu,
mungu akanilekeza kwenu…muhimu sasa dada usiwe na mawazo ya mtoto tena,, mtoto
huyo unaye huyo ni mtoto wanu, au sio shemeji…?’’akasema mdogo mtu, akimchukua mtoto kuondoka naye kuelekea
chumbani
Shamji mtu hakujibu kitu alitikisa kichwa
tu, akilini hakuwepo hapo kabisa, akili likuwa imekwenda mbali, na hata shemji
yako alipondoka na kubakia yeye na mkewe, bado alikuwa akiwaza yake.
Sasa wakabaki mke na mume,…, kimiya
kikatanda, kila mmoja akiwa na mawazo yake kichwani, mume akiwa anawaza tukio
zima na historia ya maisha yake ya nyuma, ambayo hakutaka mtu aijue, na mkewe akawa kila mara anamtupia jicho mumewe
kwa jicho la kujiiba. Mke alikuwa na yake kichwani, alikuwa na maswali mengi ya
kumuulizz mumewe, yaliyohitaji majibu, alitaka kujua ukweli…lakini hakuweza
kutamka neno, akawa kimiya, huku akiendelea kumtupia mumewe jicho la kujiiba, kimia
kikatanda, utafikiri hawajuani.
Mara mume akawa ni kwanza kufungua mdomo,
na kuanza kuongea…
Tuendelee na kisa chetu.
******
Baada ya ukimia wa muda, mume ndiye akawa wa kwanza kufungua
mdomo, akasema;
‘Mke wangu …’akaita huku akitabasamu, mke wake akainua uso na
kumuangalia, yeye hakustabasamu, kinyume na kawaida yake.
‘Mke wangu, unajua nimeliwaza sana hili tukio, ni moja ya tukio
kubwa katika historia ya ndoa yetu..’akasema na kutulia akitafuta maneno mazuri
ya kumfanya mkewe angalau atabasamu.
‘Unajua mke wangu, mimi nakupenda sana…sijui nikuambieje..kila
mara namshukuru sana mungu kwa hilo kwa kunipataia mke mwema…’akamtupia mkewe
jicho kuona kama kuna mabadiliko, lakini hali ilikuwa ile ile.
‘Kwa hili tukio nimejifunza mengi,..kuwa nafsi ya mwanadamu
inaweza kubadilika kwa kitu kidogo tu..kitu kidogo kinaweza kumfana mtu
akabadilika, na akawa hana amani tena, kumbe..wakai mwingine ni shetani tu…’sasa
hakujali kama mke wake atatabasamu au la,..akaendelea kuongea.
‘Mimi kiukweli, sikutarajia
kuwa itafikia muda mimi na wewe tusiaminiane tena….nimeogopa sana ..namshukuru
mungu kaliona hilo na kutusaidia,…hivi kweli ningeuweka wapi uso wangu, kama
..mtu angesikia hizi shutuma…mke wangu, nakuomba uniamini, mimi nakupenda na
siwezi kukufania hayo unayohisi wewe….’akamuangalia mke wake, ambaye alikuwa kakaa
kimia tu.
‘Lakini sawa, kwa yoyote angelizania hivyo, siwezi kukulaumu, mimi namshukuru mungu, kuwa mambo yameenda salama ukweli umejiweka
wazi wenyewe.…..’akasema mume mtu na mke akawa kimia hakujibu kitu kwanza.
‘Mke wangu,…’akaita na kumuangalai mke wake ambae aliinua uso na
kumuangalia, alihisi kama mke wake anataka kulia, akaona abadili muelekeo
akaona leo sio siku ya kuongea hilo alilolitaka kuliongea, akasema;
‘Ni kweli kwa muda mrefu tumekuwa tukitamani kuwa na mtoto,
..tulifikia hatua ya kutaka hata mtoto wa kulea…’akasimama alitamani aende pale
alipokaa mke wake, lakini akaona sio wakati muafaka akawa kasimama vile vile
akaendelea kuongea.
‘Mimi nakumbuka kuna siku ulilitamka hilo wewe mwenyewe, …kuna
unahitaji hata mtoto wa kurithi, kama wanavyofanya wazungu….nikakuambia nani
kakuambia hutozaa…unakumbuka hilo…’akamuangalia mke wake, mke wake akatikisa
kichwa kukubali, akaona eehee, anaanza kuelekea.
‘Tena ulitamka hilo mbele ya mdogo wako, mimi nikakuambia, tuvute
subira maana hujui mungu kapanga nini, kila jambo huja kwa wakati wake,…nielewe
hapo, kila jambo hufanya nini…huja kwa mapenzi ya mungu… hatutakiwi kulazimisha…unakumbuka
siku ile?’akasema na akawa kama anauliza, mkewe bado akawa kimiya alikuwa
kinama chini.
Mke wake alikuwa akiwaza yake, alikuwa akiomba mumewe afunguke,
azungumze ukweli wote, alihisi bado kuna ukweli umefichwa…lakini aliogopa
kusema hisia zake isje ikawa kama alivyomuhisi mdogo wake vibaya, japokuw
akiundani, aliona kuna jambo, haiwezekani mtoto afanane na mume wake…labda…na
sijui iwe vipi, maana ndugu za mume wake anawafahamu, hawafanani kabisa na mume
wake..iweje hii..au kuna ndugu mwingine hamfahamu..hapana kuna jambo hapa.
Akili ya mkewe ilikuwa na
shauku kuwa mtoto huyo anaweza akawa ni damu ya mumewe, huenda mungu kamleta
hapo ili kujua ukweli, kuwa mume wake yupoje, …lakini huo ukweli hautakuwa na
maana kama mume wake hakukiri,..na kwanini hakuwahi kumuambia hilo, … kama
ataendelea kukaa kimia hivyo itamtesa sana moyo wake.
‘Moyo wangu unataka ukweli….aniambie tu…’akawa anaongea kimoyo
moyo
‘Kwanza nisikie ukweli wote, kuwa kweli mume wangu alifanya hilo akakiuka miiko
ya ndoa katika kutafuta mtoto, ..halafu ndio atajua la kufanya…lakini baada ya kuusikia huo ukweli…sijui kama anaweza kumsamehe,..sijui, lakini kwanza
asikie huo ukweli.
‘Kwani nitakosa nini nikichukua maamuzi magumu,..kwanza hatuna
familia, sina mtoto wa kuniumiza kichwa kama nitaamua kuondoka, sina cha
kupoteza hapa…angeniambia ukweli tu, ili nisiendelee kuumia, nai kama
ataendelea kuni ficha hivi nikaja kugundua mwenywe, sijui kama nitaweza
kumsamehe tena… siku akigundua tu
itakuwa siku ya kuagana mimi nay eye..lakini mmh, mume wangu nampenda
sana, kwanini haya yatokee, ooh, mungu wa ngu nisaidia, …..’akainua kichwa
kumuangalia mume wake ambaye alikuwa bado anaongea.
‘Unajua mke wangu kila nikiliwaza hili nahisi kweli, kuwa mungu
kasikia kilio chetu na sasa katupatia mtoto..bila hata kuhangaika, na ilivyo na
bahati mtoto anafanana na sisi kabisa, unajua kufanana, hii ni miujiza kweli…’akawa
kama kamshika mtoto akimuangalai usoni.
‘Yaani, …sura utafikiri…..ooh,
mtu hawezi kuuliza. Hivi mke wangu umemchunguza vyema huyo mtoto, sio tu
anafanana na mimi, lakini pia anafanana
na wewe..’akasema na mkewe akacheka, na kicheko kile kilimfanya mume mtu
akatize kuongea na kumuangalia mke wake, alitaka iwe hivo, mke wake acheke….lakini
kicheko kile ni kma sio chake, sio kicheko halisia.
‘Sasa mke wangu tujipange jinsi ya kumlea huyu mtoto,…mtoto wetu, maana hili ni kama limetushitukizia, japokuwa
tulikuwa tunaliombea litokee hivyo, lakini
kihali a maisha yetu, a kuganga njaa…hili limekuja hatujajipanga.
‘Mimi hapa naona jambo muhimu ni kujua jinsi gani ya kumlea kwanza….unaona
hapo, ulezi,..najua wewe upo utamlea,..lakini..mmmh, hapana hapa ni lazima
tutafute mfanyakazi,, tunahitaji mfanyakazi wa kutusaidia, …’akasema na kugeuka
kumuangalia mke wangu, na mkewe akawa bado yupo kimia, kajiinamia vile vile.
‘Nasema hivi kwasababu, kuna hizo shughuli zako ambazo zinatusaidia
hapa na pale, siwezi kusema uziache, uje ukae hapa nyumbani tutegemee hicho
kipato kidogo ninachopata, cha mkono
twende mdomoni..hapana hilo halitakuwa jambo la busara…’akamuangalia mkewe akitaraji
maelezo au kauli kutoka kwa mke wake, lakini mke wake alikuwa vile vile.
‘Nimekuwa nikiwazia hilo kwa muda huu mfupi,…mimi naona tutafute
mfanyakazi, haraka iwezekanavyo,..maana ukikaa nyumbani, shughuli zako za
vibiashara vyako zitasimama…si unaliona hilo mke wangu…sasa hapo tufanyeje, …,’akamuangalia
mke wake akisubiri mchango kutoka kwa mke wake, alipoona kimia akasema.
‘Vinginevyooooh, oh, labda utafute mtu wa kutufanyia hizo
biashara, awe anakuuzia biashara zako, lakini mmmmh,… hapo ina maana kumlipa
huyo mtu, ni yale yale sawa na kutafuta mfanyakazi wa ndani …unasemaje mke
wangu…hebu changia kidogo mke wangu…acha mawazo mengine hili ni muhimu sana,
unasemaje kwa hilo?’ akauliza mume mtu na mke akaendelea kuwa kimia.
‘Mke wangu naongea na wewe…’akasema na mke akakumbuka ile kauili
ya nyuma ambayo kwa mara ya kwanza mume wake alimuita `wewe mwanamke..’hasira
za ndani kwa ndani zikawa zinajisokota tena, akatamani akae kimia au…... Kauli
hiyo ilimuuma sana, sijui ataisahau vipi, yeye kwake ilikuwa kama zarau. Mke
alipoona mume wake katulia anamkodolea jicho yeye, akasema;
‘Yote sawa…ilimradi tumeafikiana kumchukua huyo mtoto,..vyovyote
itakavyokuwa ni sawa tu…kwani hata mtoto kupatikana kwake, yalikuwa maamuzi
yako asu sio…sasa mimi niseme nini …’akasema.
‘Maamuzi yangu….hapana, …ni maamuzi ya mdogo wako, kaona sisi
tunahitaji mtoto, ndio akamleta hapa….au
ulikuwa una maana gani?’ akauliza
‘Mhh,…kwahiyo vyovyote iwavyo kwangu sawa tu, … ‘akasema na moyoni
akawa anasema ngoja nisubiri ipo mume
wake atamuambia ukweli, muhimu kwa sasani zubira japokuwa inauma sana..ila akichelewa
kumuambia akaja kugundua mwenyewe, sijui kama kutaeleweka.
‘Mawazo yako ni sawa…tupo pamoja..’akasema akinyosha, hakuona
sababu ya kukaa kimia akiumia moyo wake, akaamua kuliacha hilo kwa muda, na
mumewe akasema:
‘Kama ni hivyo basi, tutafute mfanyakazi wa ndani…hilo la
kumtafuta najua utalifanyia kazi wewe mwenyewe, mimi nijipange jinsi gani ya
kuongeza kipato ili kupatikane cha kumlipa huyo mfanyakazi, je unaweza kumpata
lini huyo mfanyakazi wa ndani?’ akauliza
‘Hata leo anaweza kupatikana..’akasema mkewe kwa lugha ya mkato,
akijaribu kundoa mawingu yaliyokuwa yametanda kichwani.
‘Kweli mke wangu! Ina maana kumbe ulishajipanga kwa hili…mmmh mke
wangu…nashukuru sana!’akasema mumewe kwa kuonyesha mshangao.
‘Mhh! …ni kweli, nilishajipanga…sisi wanawake unafikiri tuna
shida,..tunawasikiliza nyie waume wa nyumba, nyini ndio waamuzi, …sisi tumeolewa
tu…’akasema mkewe kwa sauti ya unyonge. Na kauli hii ilimfanya mume wake aone
kuwa mke wake bado ana dukuduku linalohitajika kusawizishwa, lakini kwake yeye
aliona muda utakuja kulisawazisha, hana haja ya kuhangaika nalo kwa sasa.
‘Sasa mke wangu tufanyeje,..mimi
naona wewe uwasiliane na huyo mtu, maana unaweza kusema yupo kumbe keshapata
sehemu nyingine, mpigie simu…au…. au utakwenda kwao, kwani ni mbali sana,…maana
nionavyo mimi muda ni huu huu, ili mdogo wako akiamuka tu tunamfahamisha, ili
aondoke akijua hilo, au sio mke wangu..?’ akauliza.
‘Mhh, ni sawa, hata mimi naona iwe hivyo, ….mfanyakazi wa
kutusaidia nimuhimu sana,sitaweza kuiacha ile biashara ya sokoni maana
nimeshaijengea jina na inasaidia sana hapa nyumbani…mimi nilionelea kama
tungelipata mfanyakazi wa muda tu ingelifaa zaidi, akinishikia kwa muda, lakini
kuna mfanyakazi ninayemfahamu mimi anahitajia kazi,…yeye anataka sehemu ya
kukaa wakati wote, sijui kama tutaweza kumlipa…’akasema sasa akiwa katuliza
kichwa.
‘Mambo si hayo mke wangu…mimi naona hilo limekuja na heri zake, ….mimi
naona tutaweza tu, tutahangaika tutapata mshahara wake, mimi sioni ubaya wake….’akawa
anatafakari jambo mke akainua kichwa kumuangalia mume wake, na mume waka
akasema;
‘Sawa tu…unafikiri kutakuwa na tofauti ya malipo,….yaani wa muda
na wa kukaa muda wote…., sizani kama
itakuwa kubwa saana tutaoana huko mbele, …mimi naona kama yupo ufanye mpango wa
kuongea naye, maana huyo wa wakati wote hutakuwa
na wasiwasi ukiwa kwenye biashara zako. Unaweza ukawa kwenye biashara zako
ukatingwa, lakini unajua kuna mtu nyumbani. Sasa muhimu tu ajue jinsi gani ya
kulea mtoto kama huyu- mtoto mchanga, je unaweza kuwasiliana naye sasa hivi….?’
Akauliza mume mtu.
‘Usijali hiyo ni kazi ndogo sana kwangu, kuna binti mmoja alikuwa
anatafuta hiyo kazi, aliwahi kufika hapa mara mbili, alikuwa akitafuta kazi za
nyumbani kama hizi, na niliwahi kumhoji kuwa anataka kazi za namna gani akasema
kazi zozote za ndani..’akatulia kidogo.
‘Sawa kabisa anafaa…ukimuona anweza kulea mtoo mchanga maana hapo
tuwe makini.’akasema mume mtu.
‘Nilimuuliza hilo, aah,, … akasema kuwa anaweza kulea mtoto hata kama
ni mtoto mchanga kwani yeye ana upendo sana na watoto…., nikamwambia kama
nitasikia sehemu wanahitaji mfanyakazi wa ndani nitamfahamisha, ….jana alikuja tena
kuulizia ..’akasema.
‘Alikuja tena..ooh, hiyo ni bahati, ni mungu alipanga iwe hivyo,
unaona mke wangu…mungu ana njia zake zakuelekeza…sasa…’akataka kuongea zaidi na
mkewe akamkatiza na kusema;
‘Ni mara kwa mara anakuja kuulizia, maana nilimuahidi kuwa
nitamsaidia kutafuta mtu anayetafuta wafanyakazi wa ndani…’akasema.
‘Unaona mke wangu jinsi ilivyo…, kila kitu huja na bahati yake,
haya yote kayapanga mungu…ni muhimu tumshukuru mungu na tusiwe na kinyongo
chochote, kila jambo litakuja kujieleza lenyewe,…nakuhakikishia hilo mke wangu…hutaumia
moyo wako….’akasema na mke akamtupia jicho mumewe, na mumewe akakwepa hakutaka
waangaliane moja kwa moja usoni, mkewe akasema.
‘Hamna shida, ….ni kweli kila alipangalo mungu huwezi kuliepuka,
na yeye anafahamu ya siri na dhahiri,…na sisi kama wanadamu subira ni muhimu
sana, mimi kama mke wako, nitasubiri tu….mume wangu….’akasema mkewe akawa
anasimama na mumewe akasema;
‘Nimefurahi kusikia hivyo mke wangu,…. sasa ndio unataka kwenda
huko kwanini usimpigie simu kwanza, kuhakikisha kuwa yupo, maana naona tusipoteze
muda..’akasema mume we akiwa kashika simu mkononi.
‘Hilo siumesema unaniachia mimi…, ni jukumu langu hilo, wewe tulia
tu, kila kitu kitapatikana kwa wakati wake..mtoto kapatikana kwa wakati wake,
na hata mfanyakazi atapatikana tu, kwa wakati wake, au sio…’akasema mke wake na
mume akasema;
‘Haya nenda kamuambie aje aanze kazi mara moja,…maana ni kweli akija
akamkuta na mdogo wako yupo…aah, kila kitu kitakuwa shwari….maana mdogo wako
ataweza kumuelekeza yeye mwenyewe kila kitu ambacho ni muhimu kwa mtoto huyo,
wewe utakuwa msimaizi tu…sasa itabakia kujua kiasi gani cha mashahara wake…’akasema
mume wake.
‘Swala la malipo yake,..tutaona huko mbele….mara nyingi wafanyakzi
hawa wa ndani hawahitaji malipo makubwa, maana anaishi kama mwanafamilia, kula
kulala na huduma za kawaida ni hapa hapa na atapata bure, muhimu ni posho yake,
maana kaja kwa kazi, sio kama mwanafamilia,inabidi alipwe, kwa makubaliano,
tusimsononeshe,…
‘Na nijuavyo mimi, wafanyakazi hawa wa ndani, wengi wanalipwa kutegemeana
na hali zetu, kama kipato ni kikubwa ni wajibu alipwe vizuri, kama ni kidogo,
basi atalipwa hivyo hivo, na kwa vile mwenyewe hali anaiona atarizika tu, ila
tusimuonee, akaona kama yupo utumwani…kazi nyingi nitazifanya mimi mwenyewe…’akasema
mke mtu, huku akianza kuondoka.
‘Haya kila la heri nataraji utamkuta hajaondoka, ukimkosa inabidi
kuulizia sehemu nyingine…’ akasema mume mtu.
‘Siwezi kumkosa, yupo ananisubiria..hilo nina uhakika nalo, ….muhimu
….’akasimama kwanza.
‘Mimi kichwa hapa kinaniuma…nawaza sana,….’akasema
‘Kuhusu nini tena mke wangu….?’ Akauliza
‘Sawa…nitasubiri tu…ila sitaweza kusubiri sana,…nataka nikirudi
tuongee hili kwa mapana…au tusubiri mdogo wangu aondoke tukiwa na nafasi naomba
hili tuliongee kwa uawazi, mimi ninachohitajia ni ukweli tu….’akasema
‘Mke wangu hebu tuachane na hizo hisia zako kwanza, hili lina
umhimu kuliko hizo hisia zako…’akasema mume wake.
‘Lina uhumhimu, ina maana hujali hisia zangu..?’ akauliza mke
wake.
‘Sio hivyo mke wangu,..mimi nimeshakuambia ukweli utakuja
kujielezea wenyewe, si umeona mwenyewe, ooh, mdogo wangu una mtoto, ooh, mdogo
wangu umenisaliti..ooh wapi…si umeona
mwenyewe, na hilo litakuja kujionyesha lenyewe, usiwe na shaka kabisa, utakuja
kufurahi , hakuna ubaya wowote kama unavyofikiria wewe…’akasema mume mtu, mke
mtu hakusema neno hapo.
‘Unajua mke wangu…usipende kutunga hadithi…….utaumiz akichwa chako
bure, mwishowe utakufa kwa kihoro uniache nikiteseka kukuwaza, na mimi sipenzi
uniache mke wangu ni heri nife mimi kabla yako….unasikia mke wangu mimi….sipendi
wewe…..’akawa anaongea akijua mke wake bado yup ndani.
Mke mtu alikuwa keshaondoka akimuacha mumewe akiendelea kuongea, hakutaka
kumsikiliza zaidi, na mume ambaye kwa muda huo alikuwa anaongea akiwa kageukia
upande mwingine hakujua kuwa mkewe ameshaondoka.
Mke mtu akiwa na mawazo akawa anatembea kuelekea kwenye hiyo
nyumba ambapo huyo msichana anaishi kwa muda, … lakini mawazo yake yakakatishwa
na kundi la watoto, na yule, mama, safari hii akaonana na huyo mama ana kwa ana,
japokuwa yule mama alikuwa kajifunika usoni kama kawaida yake. Yule mama
alipomuona huyu mke mtu yeye mwenyewe akamsogelea na kuanza kusema;
‘Na-na-nataka mtoto wangu….’akasema kwa sauti ya kukasirika, na huyu mke mtu akatulia na sijui
ni kitu gani alijikuta na yeye akisema;
‘Nataka mtoto wangu….’akasema na watoto nao kwa wakati huo wakawa
wameitikia hivyo hivyo, huyu mama akarudi nyuma hatua moja, kama vile anaogopa,
alirudi kinyume nyume,…na kumfanya mke
mtu kubakia na mshangao, ni kama vile hiyo sauti ilimshitua ule mama, lakini
baadaye yule mama akasimama akamsogelea tena huyo mke mtu,na kusimama karibu
naye.
‘Nimekuambia…nataka mtoto wangu…’akasema na safari hii mke mtu
akajua huyu mama anaongea kionyesha dhamira hana utani, ndipo akamjibu;
‘Kwani mimi nina mtoto wako?’ akamuuliza
‘Ndio una mtoto wangu, wewe huoni,….mimi namtaka mtoto
wangu….nitakuja kumchukua mtoto wangu….’akasema
‘Mimi sina mtoto wako, ulinipa lini mtoto wako…, kwanza wewe ni
nani mbona unajifunika, kwanini hutoi hiyo nguo usoni tukuone ulivyo….?’
‘Unataka kuiniona eeh..hahaha…’akacheka halafu akasema;
‘Nataka mtoto wangu, wewe unaye mtoto wako, na mimi nataka mtoto
wangu…’akasema
‘Ninaye mtoto yupi…?’ akauliza
‘Mtota wako unye tumboni kwako,..huyo uliyemchukua ni mtoto wangu….nitakuja
kumchukua mtoto wangu…’akasema na kugeuka kuondoka, akamuacha mke mtu akiwa
kaduwaa..
‘Mhh, ….mimi nina mtoto wangu tumboni,…! ‘akainama kujiangalia
huku akiwazia ile ndoto.
‘Mhh mbona hii kauli yake inafanana na ile ya kwenye ndoto…’akasema
akiwa anaangalia huko mama huyo anapokwenda lakini hakumuona tena, keshatoweka.
‘Mhh,..mbona makubwa…’akasema kwa sauti, akawa sasa anaanza
kuingiwa na mawazo kuwa huenda kweli huyo mama ni mama kutoka mbinguni,
anafahamu siri za watu, na jinsi alivyotoweka haiwezekani akageuka huku na kule
kumtafuta lakini hakuwepo kwenye upeo wake wa macho…akawa kasimama pale akiwaza,
hakujua kasimama pale kwa muda gani, lakini baadaye akakumbuka kuwa alikuwa na
kazi ya kufanya, akaanza kutembea kuelekea huko alipokuwa akienda.
Alipofika nyumba ya jirani,
akamkuta huyo binti yupo,akiwa anafua nguo…na huyo binti alipomuona huyo mke wa
mtu, akaonyesha uso wa furaha na swali likawa;
‘Je umesikia kuna mtu anatafuta mfanyakazi wa ndani, maana mimi
najiandaa kuondoka, kesho naondoka zangu, narudi huko kwetu kijijini, nitakuja
tena siku nyingine..’akasema
‘Usiwe na shaka, kazi imeshapatikana..’akambiwa na kumfanya yule
binti kuacha akzi aliyokuwa akiifanya na kumsogelea huyo mama
‘Wapi huko…ooh, ndio maana jana niliota nafanyakazi nalea mtoto
mchanga…nikajua huenda kweli nitapata kazi, napenda sana watoto wachanga, siku
nikipata wangu, sijui itakuwaje…umesema kazi imepatikana wapi, kwa nani?’
akauliza
‘Nyumbani kwangu….’akasema na huyo binti akawa kama kakata tamaa,
akasema
‘Lakini uliniambia kuwa wewe huhitaji mfanyakazi, na huna mtoto
mchanga na pia ulisema kutokana na shughuli zako hutaweza kunilipa..’akasema
‘Usijali, nitakulipa tu….kama upo tayari twende…’akasema na huyo
binti akasema
‘Mimi kwasasa nipo tayari kwa kazi oyote maana nilishakaa na
kukata tamaa..hapa nilikuwa najiandaa kesho kuondoka, mwenyeji wangu nilishamuaga
maana nikaa tu sema katoka kidogo..oh, bahati …., yule pale unamuona ..anarudi,
ngoja nijiandae tuondoke, …’akasema.
‘Sawa wewe chukua kila kitu hutarudi tena hapa…’akaambiwa na
mwenyeji wa huyo msichana akafika akaelezewa , yeye akawa hana kipingamizi,
akatoa baraka zake.
Basi wakaondoka na huyo binti hadi nyumbani kwake alipofika, mdogo
mtu alishaamuka, na mdogo mtu aliposikia kuwa huyo ni mfanyakazi wa mtoto
kwanza alisita lakini baadaye akakubaliana na hilo, ikawa ni kazi ya kuelekezwa
jinsi gani ya kumlea huyo mtu, kumtengenezea maziwa.
‘Hii kazi ya mtoto, utaifanya tu pale nikiwa sipo, na nitajitahidi
sana kabla ya kuondoka kila kitu kipo tayari, usiwe na wasiwasi tutasadiana na
kama sipo ukiona kuna jambo hulielewi au mtoto analia sana, nipie taarifa
haraka, tafadhali….’akasema dada mtu akimuelezea huyo mfanyakazi na mdogo wake
akawa anatikisa kichwa kukubaliana na hilo.
Dada mtu akamwambia mdogo wake asiwe na wasiwasi na hilo, imebidi
kumtafuta huyo mfayakazi kwa vile ana biashara zake na wakati mwingi huwa anakuwa
hayupo hapo nyumbani…lakini kwa sababu ya huyo mtoto atajipanga jinsi gani ya
kufanya.
Pamoja na sintofahamu uliyojitokeza, lakini tukio hili likaoneka
kuwa litaleta faraja ndani ya familia, na ilikuwa kama vile, dada mtu
kajifungua mtoto, japokuwa bado kulikuwa na kitu nafsini mwa mke mtu kwa mumewe…lakini
kila hatua hali hiyo ilikuwa ikipungua.
Kesho yake mdogo mtu akarudi kazini kwake, na wakati anaondoka
akakutana na umati wa watoto, wakimfuatilia yule mwanamama, akaona ajaribu
kumwangalia huyo mama ni nani. Akawa anamuendea pale aliposimama na watoto, na yule
mama alipoona mtu anamjia, akageuka kuondoka…akatembea hatua kama tatu halafu akasimama, akasubiri…
Mdogo mtu, alipoona huyo mama kasimama,…akatembea kumsoegelea…alipomkaribia
akasita, lakini alishafika karibu yake, sasa akawa anafikiria amuambieje huyo
mama, yule mama akaanza kutembea kuelekea sehemu nyingine alipoona aliyekuwa
akimfuata hasemi neno, huyo mdogo mtu akasema;
‘Samani mpendwa, nataka kuongea na wewe…’akasema huyo mdogo mtu.
‘Na-na-nataka mtoto wangu…’akasema huyo mama na watoto wakaitikia
‘Unataka mtoto wako,…yupo wapi huyo mtoto wako?’ akauliza
‘Wewe unafahamu wapi alipo, tena ndio wewe, unayeiba watoto wa
watu …nataka mtoto wangu,…mimi nitakwenda kumchukua mtoto wangu….’akasema.
‘Utamchukua wapi huyo mtoto wako, kwani mimi nilikuwa na mtoto
wako, umeniona wapi nikiiba watoto?’ akauliza huyo mdogo mtu.
‘Nimesema nataka mtoto wangu….nitamchukua mwenyewe mtoto wangu….nitamchukua
mtoto wangu, nataka mtoto wangu, unanisikia…’akasema
‘Mhh…wewe mama una maana gani kusema hivyo, ..utafungwa, isije
ikawa ndio nyie mnaoiba watoto, huyo mtoto wako ulimpa nani, au ulimpatia wapi..?’akasema.
‘Wewe ndiye umeiba mtoto wangu nataka mtoto wangu, nipe mtoto
wangu…nimesema nataka mtoto wangu, …nipe mtoto wangu haraka…’akasema akitaka
kumvamia huyu mdada, na huyo mdada akawa anarudi nyuma kumkwepa huyo mama,
Na alipoona hali sio shwari akageuka kutaka kumkimbia huyo mama,
na huyo mama akawa keshamshika sehemu ya nguo yake wakawa wanavutana…mdogo mtu
huyo kuona vile akawa anarudi kwa nyuma huku akijaribu kuvuta nguo yake, isije
ikachanika…. na watoto waliokuwepo hapo wakawa wanashangilia kama mchezo vile.
‘Ntaka mtoto wangu, nipe mtoto wangu, umeniibia mtoto wangu….’yule
mama akawa anasima
Mdogo mtu kuona hivyo, akatahayari maana sasa anakuwa kama
anasutwa,…kuwa yeye kamchukua mtoto wa huyo mama, japokuwa alishasikia kuwa
huyo mama anamfanyia hivyo kila mtu, akaona
hapo hapakaliki akaita bajaji na mwenye bajaji alipofika akamsaidia
kumuachanisha na huyo mama, na hapo akapata upenyo, akaingia kwenye hiyo
bajaji, wakaondoka kwa haraka.
Alipofika njia akachukua simu na kumpigia dada yake……
NB: Je huyu mama kwanini anadai kuwa anataka mtoto wake…je huko kazini
kwa huyu mdogo mtu kuna nini kinachoendelea, tuwepo sehemu ijayo.
WAZO LA LEO: Kuna vitu ambavyo kama vingelikuwa ndani
a nafsi ya kila mtu, utu na ubinadamu ungelikuwepo , na dunia hii ingekuwa ni
kisiwa cha amani, lakini vitu hivyo ni nadra sana kuwepo ndani ya nafsi ya mtu,
kwani kila mtu amejawa na ubinfasi, vitu hivyo adimu ni upendo
na huruma. Ikimuuliza mtu anaweza kujinadi kuwa anvyo vitu hivyo, lakini je
ni kweli, Mtu kujipima kuwa kweli ana upendo na huruma , ajaribu kujiona jinsi
gani anavyoweza kutoa kile alicho nacho kusaidia wenzake bila kinyongo.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment