Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, January 30, 2015

NANI KAMA MAMA-26



‘Unasema alilala hapo upenuni mwa nyumba yetu?’ akauliza mkewe akionyesha mshangao

‘Atakuwa huyo huyo, ….. kuna kauli kuwa ni mama wa kutoka mbinguni, kaja kuleta neema, na akifika kwako ujiandae kupokea neema, kama alilala hapa kwetu mmmh…’akasema akionyesha furaha usoni, na mumewe akajizuia kucheka

**********
‘Unalia nini mke wangu?’ ni swali aliloulizwa mke wa mtu, na mke akajibu hivi;

‘Mume wangu, wewe hujui tu,  kama wamemfukuza mdogo wangu kazi , wale wazee wangu watalelewa na nani….., na mimi nakuonea huruma wewe mume wangu maana unabeba jukumu kubwa zaidi ya uwezo wako, je  kipato tunachopata kitaweza kuwasaidia na wazee wangu….’akasema

‘Mke wangu lakini hawajasema kuwa shemeji kafukuzwa kazi, kama nilivyoelewa vyema ni kuwa bado wapo kwenye uchunguzi,…’akasema

‘Lakini kasema anakuja huku, ,..na kama ni hivyo mpaka uchunguzi ukamilike, ni miaka, kama ni miaka kazi ipo tena, ……’akasema mkewe.


‘Kasema kuna jambo anataka kuja kujadiliana nasi, ambalo wamekubaliana huko, ….na ni muhimu, ..na sijui anakuja lini, akifika tutajua la kufanya, hayo mengine tumuachie mungu,.usianze kujitwika mzigo kabla haujafika kichwani...utchoka mapema…muhimu tufanye subra’akasema mume mtu.

‘Haya mume wangu nimekuelewa,….’akasema akimkabidhi mumewe simu yake, na mumewe akataka kupiga kuongea na shemeji yake tena ili apate ufafanuzi, lakini ….

‘Nasikia kama mngurumo wa gari….’akasema mke mtu

‘Yah, …labda kuna mtu kakosea njia, sijui huku anafuata nini, tulishawaambia huku hakuna barabara ya magari, watatogongea watoto…..’akasema akielekea dirishani kuangalia nje na mara  gari likafika na kusimama nje ya nyumba yao, wanandoa hawa wakawa wanaangaliana, kila mmoja akiwaza lake, labda ni polisi wamekuja kuwakamata, sasa kwa kosa gani, au…..

‘Mhh, hili sasa laonekana ni tatizo…sio polisi hao,’akasema mke mtu

‘Nahisi…..’akasema mume mtu akichungulia dirishani kwa mashaka.

‘Basi mume wangu nenda kawasikilize…’akasema mke

‘Niende…hapana, ngoja tusubiri, kwani hatuna uhakika ni akina nani, mimi naingia chumbani wakipiga hodi waambie mimi sipo….’akasema mume mtu akianza kuelekea chumbani.

‘Mume wangu….’mke akataka kulalamika lakini akanyamaza, akijua kuwa ni wajibu wake kutii amri ya mume wake, akasogea yeye dirishani kuchungulia…akaona sehemu ndogo ya gari kwa nyuma,....’na mara mlango ukagongwa

Tuendelee na kisa chetu…

***********
Mlango uligongwa tena,

 Mke japokuwa alikuwa na uwoga, lakini alijua wajibu wake kama mke wa nyumbani,  alitamani mume wake ndiye awasikilize hao wageni, lakini akashindwa kusema lolote kwa muda ule, alichofanya ni kutii amri ya mume wake,  na sasa mlango umeshagongwa tena, hana jinsi, ….ikabidi ajitume  akasema;

‘Karibu…nani mwenzangu…’akasema akionyesha wasiwasi huku akihisi kama mlio wa kitu kudondoka, hakuweza kujua ni mlio huo umetokea wapi, nje au ndani,mawazo yake kwa muda ule yalikuwa kwa hao watu waliofika ni askari au….

 Aliogopa kusogea mlangoni, kwani litakiwa aufungue yeye ili kuwakaribisha hao wageni, akabakia pale amesimama, na mara mlango ukafunguliwa…

Mke wa familia akawa sasa moyo unamdunda, akijua ni askari, wataingia kwa nguvu na kuanza kumzoa zoa,..au kutembeza kipigo, au vitisho….lakini sasa je wakimuuliza mume wake yupo wapi atasemaje, atawadanganya, na kama akiwadanganya wakaingia chumbani na kumkuta, itakuwaje…’akawa anajiuliza maswali mengi.

Mlango ukafunguliwa lakini hakuna aliyeingia kwa mara moja, na pale aliposimama mke wa familia hiyo asingeliweza kuona huko nje eneo la mlangoni, hata kama angelichungulia dirishani asingeliweza kuona vyema, kwani gari lilisimama upande ambao sio muelekeo wa dirishani.

Mama akavuta subira huku akiwaza mengi, hakusogea, akawa anawaza jinsi jirani yao alivyokuja kuchukuliwa na polisi, ilikuwa hivi hivi, tukio limetokea huko mjini, …mara askari wakaja kijijini, kwa kosa la kijana wa wazee hao. Kijana wao alikuwa kaajiriwa huko mjini, ikasadikiwa kuwa kaumuibia muajiri wake, akakimbilia kijijini, na inavyosaidkiwa ni kuwa alikimbilia kujificha kwa wazazi wake.

Polisi walipofika hapo kijijini, wakawavamia hao wazazi kwa kushitukizia, na kuanza kutembeza kipigo,…alikuwepo askari polisi mmoja na askari mgambo. Wazazi hawakuelewa ni nini kimetokea,,  kwani wazazi walipoulziwa walisema hawajui, na kweli walikuwa hawajui;

‘Huyu ni kijana wenu na tumeambiwa kakimbilia huku kijijini…’wakasema

‘Mbona hatujamuoana akija hapa…’wazazi wakasema kwa mshangao

‘Tuna uhakika amefika hapa kijijini…na nyie mnafahamu wapi alipo, msipotuelezea wai alipo, nyie mtapata shida , mtafungwa….’wakasema askari.

‘Mbona hajafika huku, kwani kuna nini huko mjini, kafanya nini?’ wazazi wakauliza wakiwa hawaelewi kinachoendelea.

‘Mtoto wako ni mwizi, kamuibia muajiri wake, na taarifa za ukweli ni kuwa kaja huku, tuambieni yupo wapi…’wakauliza askari.

‘Hatujui,….’wazee wakawa wanajitetea kwa uwoga, askari kuona hivyo wakaingia ndani na kuanza kutafuta kila sehemu ya nyumba, walipomkosa wakawachukua wazazi hao wangu wangu, na kuondoka nao….

Kilichoawapata wazazi hao mpaka sasa ni siri yao, kwani walirudi baada ya siku tatu, na waliporudi hali zao zilikuwa mbaya sana …..hata kutembea hawajiwezi, walikuwa wagonjwa wa kitandani karibu mwezi  mnzima.

Mtoto wao hajaonekana mpaka leo…

‘Oh mungu wangu  yasije yakanikuta ya majirani zangu…’akawa anajisemea mwenyewe moyoni, huku keshaanza kutetemeka, na kabla hajamaliza kujisema moyoni, mara akamuona mtu akiingia mlangoni….alikuwa, mwanadada mrembo, akiwa amebeba mtoto mchanga mkononi na mkono mwingine kitenga chenye nguo za mtoto mchanga na vitu vingine.

Mama wa familia,akapandisha mkono usoni kufuta macho hakuamini alichokiona, akabakia kaduwaa, akajaribu kupikicha tena macho, kama kweli anachoona nis ahihi, lakini ni kweli alichokiona, akakunja uso kwa hasira, lakini akakunjua ..akili ikawa imeganda, hakujua hata aseme nini….

‘Dada nimewaletea mtoto, najua mna hamu sana ya kuwa na mtoto, sasa, nawaambia hivi duwa zenu, mungu kazisikia na mungu kawabariki bila hata ya kupata shida….huyu hapa kuanzia leo ni mtoto wenu…’ Ilikuwa ni kauli ya kwanza ya huyo mwana dada aliyeingia, hakukuwa na salam kama ilivyo ada.

‘Umetuletea mtoto…!?’ akauliza mke wa familia akiwa bado hajaamini na hiyo kauli ilimuweka njia panda.

‘Dada, shemeji yupo wapi, ….nataka tuliongee hili akiwepo, ….’akasema mdada huyu akiangalia huku na kule.

‘Oh, mbona umenishitua, ….shemeji kapumzika ndani….’akasema  na huyo mwanadada akasema;

‘Dada usijali,…hili nimelifikiria kwa makini, nikaona ni sawa tu…najua ni kitu ambacho ni kigeni, na hamkutarajia, ila imetokea na ni muhimu muikubali tu…’akasema

‘Sijakuelewa….’akasema mke wa familia akimtupia macho yule mtoto mchanga huku akilini akiwazia mbali, aliwazia kuwa ndio yeye katoka hospitalini akiwa keshajifungua na akaja hapo na kichanga chake na kila mtu anamshangaa.

Alimuangalia yule mtoto mchanga akamuona kama anafanana na mume wake, na akilini akasema;

‘Watu wangelinipokea kwa furaha na kwa vile mtoto anafanana na mume wangu yaani ingelikuwa ni raha tupu, ooh, mungu wangu, hivi hii Bahati nitaipata wapi, ina maana kweli sitaweza kupata mtoto kama huyu….nampenda huyu mtoto, utafikiri nimemzaa mimi mwenyewe…’akawa amawaza, na wakati huo , huyo mdada aliyeingia akawa anazidi kuongea;

Shikamoo dada, maana kwanza nimeshau hata kukusalimia…’akasema na dada yake akaitikia kama ada,  na kabla hawajaongea zaidi, mdogo mtu aliyekuwa na hamasa akasema;

‘Unajua dada kubeba mimba miezi tisa sio mchezo,…wewe sikia tu, waulize wenzako,… tena hata ikifika siku ya kujifungua bado unakuwa huna uhakika kuwa kweli utajifungua salama, sasa mungu kaisikia duwa yenu, tumepata mtoto…huyu hapa ni mtoto wenu,..kabisa kabisa…’akasema mdada sasa akimuelekeza huyo mtoto kwa mke wa mke wa familia ili ampokee,

‘Unamuona mtoto alivyo mnzuri, mtoto wenyewe mzuri , afya tele, hebu mshike umuone…’ akampa dada yake yule mtoto, ambaye alikuwa katulia kimya.

Dada mtu akiwa na mashaka akampokea yule mtoto, huku amemwangalia mdogo wake kwa uso wa kutahayari,…ina maana ndio maana alikuwa hafiki huku kwa muda mrefu, kumbealikuwa mja mnzito….’akawa anawaza na kukumbuka safari ya mwisho kuwatembelea alikuwa kapendeza sana, na yeye akamuuliza kwa utani.

‘Mdogo wangu mbona umependeza hivi, au umeshampata shemji maana nyie vijana wa siku hizi hamcheleweshi, hamtaki hata kufuata taratibu, mnajiozesha wenyewe, bila baraka za wazazi…’alimtania na alijua ni utani kweli.

‘Dada na wewe bwana, mbona wanichuria, kupendeza kupo wapi, mbona ni kawaida tu…’akasema mdog wake.

‘Nimekuona ….lakini haya mapenzi hayana siri, uwe makini usije ukaniabisha…nataka uolewe kisheria, wazazi wetu wahudhurie ndoa yako…’akamuasa.

‘Na ndio lengo langu dada..hilo usiwe na shaka nalo, siwezi kuwaabisha wazazi wangu, …’akasema ndugu yao huyo.

Na alipoondoka, wakawa wanawasiliana kwa simu, mara kuna kazi nyingi, mara mwenzeka kasafiri kwahiyo anamshiki anafasi zake, basi ikawa kuna sababu za hapa na pale, na karibu mwaka ukapita hivi hivi bila kuonana na ndugu yake huyo, kitu ambacho hakikuwa kawaida siku za nyuma.

Sasa ndugu yake huyu kabeba mtoto mchanga, na haoni mume akijitokeza, huenda kabakia ndani ya gari, akiogopa, …au pamoja na yote huenda yeye na mume wake hawajaelewana,….sasa na hayo matatizo ya kazini na mtoto mchanga itakuwaje, atalelewa vipi au ndio maana akasema anakuja huku ili kuliongelea hili, ili wao waweze kumlelea mtoto wake, yeye akiendelea na kesi yake.

‘Lakini mbona mtoto anafanana sana na mume wake…’akajikuta akiwaza kwa hisia nyingine, na mshipa wa wibu ukasimama, akainua uso kumuangalia mdogo wake, hakujua hata asema nini, labda…lakini lini, au ndio maana mume wake alikuwa hajali, alikuwa kuna nini kitakuja!

`Wewe hebu niambie nini kimetokea, maana mara simu ya kuwa utakujakuja nyumbani na mgeni, mgeni mwenyewe hatumuoni, sisi tulizani unatuletea shemeji, aje ajitambulishe tupange mahari na nda na harusi,…sasa kumbe mumeshafanya yale yale tuliyokuwa tukikuasa, hebu …’akasema sasa akiangalia mlangoni.

‘Dada uvute subira…maana na wewe kwa kutunga hadithi kichwani umo, na sijui kwanini huandiki kitabu…’akasema mdogo mtu akiwa haonyeshi wasiwasi.

‘Mhh, unajua kwanza ni vyema nijue  ukweli, huyo mume wako, au sijui bwana wako yupo wapi,…’akasema dada mtu akichungulia mlangoni, alihisi kuna watu nje, lakini hawaingii ndani.

‘Kwanza shemeji yupo wapi, maana hili nataka tuliongee tukiwa wote , maana hili sasa halina hiyari, ama kama hamukubaliani nalo, basi na kazi sina. …mimi kwa dhana yangu nimeona kuwa labda hili limetokea ili iwe faraja kwenu,..’ akakatisha maneno baada ya kusikia sauti nje.

‘Na-na-nataka mtoto wangu…’ na sauti hiyo ikakatishwa na kilio cha mtoto, dada mtu akamshika na kumbembeleza, huku anamuangalia mdogo wake afungue gauni vyema ili mtoto anyone, lakini cha ajabu mdogo wake akafungua kitenga kidogo na kutoa chupa yenye mazima.

‘Kuna vipimo vyake nitakuelekeza….kwanza sasa hivi anatakiwa kunyonya,…’akasema mdada na kuanza kutayarisha maziwa ya huyo mtoto.

‘Wewe vipi , kwanza nyie ndio mnatakiwa kuonyesha mfano,…mtoto mchanga hatakiwi kunywa maziwa ya kopo, mnyonyeshe…’akasema dada mtu akionyesha uso wa kushangaa, na hata akimuangalia mdogo wake, haoni ule ukubwa wa matiti, moyoni akamuonea huruma.

‘Mdogo wangu wewe una matiti madogo, ukizaa mtoto atapata shida sana…’alikumbuka siku moja alimuambia mdogo wake huyo.

‘Wewe hujioni, nahisi sisi tumerithi kutoka kwa mama, na hushangai, mbona mama anasema pamoja na udogo wa matiti yake, lakini aliweza kutunyonyesha hadi miaka miwili ..’akawa anawaza jinsi walivyokuwa wakitaniana na mdogo wake huyo, huwa wakiwa wawili utafikiri walizaliwa siku moja, japokuwa wamepitana miaka mine.

‘Dada bwana eti nimnyonyeshe, …ngoja nikuonyesha jinsi ya kumtengenezea maziwa yake, maana huyu kazaliwa bado….ila keshatimia, hana tatizo kabisa, unasikia dada, huyu kwa kipindi hiki kumpa maziwa mengi sana haitakiwi…unaongeza kipimo kila umri unavyoongezeka, sio kila akilia unampa, hapana, unampa kwa masaa, nitakuonyeshea…’akasema mdogo mtu akikoroga yale maziwa.

Dada mtu akawa anamuangalia mdogo wake kwa uso wa kujiuliza, …

Alipomaliza, akaanza kumpa mtoto..huku akisema;

‘Dada nafahamu wewe ni mkubwa kuliko mimi, lakini kwa hivi sasa inabidi unisikilzie mimi, maana nina uzoeu wa kuelea watoto kitaalamu, kuna jinsi ya kumnyonyeshea mtoto kama huyu ili ajihisi ananyonya maziwa ya mama yake, unamshika hivi….’akaanza kuonyesha mfano.

‘Halafu unachukua hii chupa unaiweka hapa…’akawa anaonyeshea jinsi gani ya kumnyonyeshea , na kichanga kile kikawa kinanonya huku kimeweka mkono karibu na sehemu ya titi la yule nesi, na dada mtu alipoona vile akahisi machozi yakimlenga lenga, akilini akiwazia kuwa huyo kweli ni mtoto wake.

‘Unaona kanavyonyonya, kanahisi kananyonya maziwa ya mama yake…’akasema huku akiendelea kumnyonyesha kwa chupa.

‘Mdogo wangu unajua mimi bado sijakuelewa,..kauli yako siielewi, kamahisi kama kananyonya…. hebu niambia ukweli, kwanini hutaki kumnyonyesha mtoto, unaogopa kuwa maziwa yatadondoka, au…usije kupata dhambi kwa kukwepa majukumu…hebu niambie ukweli…huyu mtoto umezaa na nani, au…kuna kitu gani mnanificha?’ akauliza

‘Dada nimekuuliza shemeji yupo wapi, maana sitaki kurudia rudia maelezo, ni muhimu tukianza kuongea muwe pamoja,..’akasema

‘Leo hii unaona aibu kuniambia siri zako,toka lini mimi na wewe tukafichana ukweli, ina maana ulipofanya madhambi haya, unameshabadilika, au kuna nini na hayo yaliyotokea huko kazini kwako, ni mambo gani, au yanatokana na haya madhambi, ujue ukitenda dahmbi usipotubu, madhambi mengine kuhukufuata…..’akasema akimuangalia mdogo wake kwa uso wenye kuonya kama mama anavyomuambia binti yake maneno yanye kuonya.

‘Dada acha kutunga hadithi, nitakuambia ukweli wote..usiwe na shaka kabisa…ila muhimu naona nikianza kuwaelezea nataka hata shemeji awepo, maana hili ni jukumu letu sote…na siku moja nakumbuka mlishawahi kuniulizia kama hili linawezekana, na bahati, tumejaliwa, tumempata huyu mtoto….nataka niwaelezee akiwepo shemji ili nikiondoka hapa jukumu hili linabaikia mikononi mwenu..mimi narudi kupambana na hiyo kesi,….’akasema.

‘Kwanini mpaka awepo shemji…kwanini usiniambia ukweli …’akasema

‘Kwasababu yeye linamuhusu sana…..’akasema

‘Kabla hajafika shemeji yako, swali langu muhimu, nataka unijibu kama dada yako na hapa nasimama sehemu ya wazazi, sitaki utani, nataka uniambia ukweli, baba wa mtoto huyu ni nani..na yupo wapi?’ akauliza dada mtu akionyesha kukasirika.

‘Dada bwana…kwanini unataka kuvuruga mpangilio..nimesema nitakuambia ukweli wote, na nataka nikilielezea hili na shemeji awepo, kwani shemeji leo kaenda kazini, leo si siku ya mapumziko, yeye hana mapumziko….’akauliza huku akikwepa kuangaliana na dada yake, na hiyo dalili, ilimfanya dada mtu ahisi kuna jambo.

‘Nauliza tena, baba wa mtoto huyu ni nani,…nahisi wewe na shemeji yako mumenizunguka,…sitaki utani, udugu utakufa mara moja, sitajali wewe tumezaliwa tumbo moja, kama kweli mlifanya hili ili eti tupate mtoto,…ohooo,’akasema akionyesha kukasirika.

‘Dadaaah…yaani umefika huko..?’ akasema mdogo mtu akionyesha mshangao.

‘Nakuambia ukweli unielewe,  kama kweli ninavyohis ni sawa udugu utakufa,…’akasema huku mdogo mtu akimuangalia kwa uso wenye mshangao, hakuelewa kabisa dada yake ana maana gani, na mara nje kukasikika kelele..

‘Na-na-nataka mtoto wangu…nataka mtoto wangu…’ wakasikia kelele nje

‘Hivi hawo ni akina nani, naona watoto wengi hapo nje, kuna nini…’ akauliza mdogo mtu na dada mtu akakunjua suo ulianza kujaa hasira na kuongea sauti ya kawaida, akasema;

‘We acha tu leo siku ya tatu, kila siku `na-na-nataka mtoto wangu, nataka mtoto wangu..’ ndio wimbo ulioenea hapa mitaani, na aliyeuleta ni mama mmoja, nafikiri sijui kachanganyikiwa, hatujui katokea wapi, hatujawahi kumuona maeneo ya hapa kabla, wengine wanadai katokea mbinguni…’ akaelezea dada mtu wakati mdogo mtu anajaribu kuchungulia dirishani, lakini hakuweza kumuona huyo mama, kwani alikuwa kasogea nyuma ya nyumba.

‘Katokea mbinguni..na nyie bwana, na wewe ukaamini hivyo, yupoje mapaka muamini hivyo?’ akauliza

‘Haeleweki, unaweza kumuona hapa ukigeuka kuangalia upande mwingine ukigeuka kumuangalia anapotea…imetokea kwa shemeji yako….’akasema

‘Na shemeji kaamini, mbona haaminigi mambo hayo…?’ akauliza

‘Wewe..haya mabo unaweza ukajifanya huamini, lakini yakikufika …utaamini tu…’akasema

‘Kwani ….’akasema, mara akakatishwa na sauti ya hodi

‘Hodi hapa…’ Dada mtu na mdogo mtu wakashituka.

‘Ni nani huyo, sio sauti ya shemeji mbona umesema yupo ndani..?’ akauliza mdogo mtu akijaribu kumfunika mtoto, na kitendo kile cha kumfunika mtoto kama anamficha, alikiona dada mtu, na akilini mwa dada mtu akajua ni lazima kuna jambo kati ya mdogo wake na mume wake…

‘Kwanza mtoto anafanana kabisa na mume wangu, halafu kwanini mdogo wangu hataki kuniambia ukweli, na wakati kwenye maisha yake na mdogo wake huyo hawajawahi kufichana jambo, wanaambizana siri zao, …hapa kuna jambo, na kama ni kweli, sijui kama udugu utakuwepo tena..’akawa anawaza.

Wakati anawaza hayo,..akili iliingiwa na mawazo mengine, maana anachojua yeye ni kuwa mume wake yupo ndani...mume wake, alimuambia anajificha ndani , kwani walijua kuwa hao waliofika ni maaskari, sasa anashangaa kusikia sauti ya mumewe ikitokea nje.

‘Huyu mtu vipi…’akasema dada mtu, huku akichungulia mlango wa chumbani.

‘Kwani vipi dada….?’ Akauliza mdogo mtu naye akiangalia mlango wa chumbani na kugeuka kuangalia huko hodi ilipopigwa.

'Si ulisema shemeji yupo ndani kapumzika, mbona....'akauliza mdogo mtu

‘Ndio shemeji yako yupo chumbani,.. sasa naona ajabu kusikia sauti yake, au ni nani kaigiza sauti yake …..’akasema sasa akisimama kuelekea mlango wa chumbani, lakini kabla hajaufikia huo mlango wa chumbani mlango wa nje ukafunguliwa na huyo aliyepiga hodi akaingia…

NB: Kidole kinauma


WAZO LA LEO: Tabia ilivyo, kukitokea jambo mtu hukimbilia kujenga dhana, inawezekana ikawa dhana njema au mbaya. Tuwe makini na hili, kwani wengi wetu hupenda kuwadhania wenzao dhana mbaya hata kabla ya ushaidi. Muhimu kukitokea jambo, tusubirie uchunguzi,  tusikimbilie kunyosheana vidole kutokana na tofauti za kiitikadi au ushabiki, tukasahau ukweli na haki. Dunia sasa hivi imegubikwa na dhana potofu kwa maslahi binafsi na wengine bila kuchunguza tunashabikia tu, hatujali tena haki na ukweli, na matokeo yake watu wanafarakana, amani inapotea.
Ni mimi: emu-three

2 comments :

Anonymous said...

buy online prescription viagra without [url=http://achatpriligyfrance.com]priligy in europe[/url] viagra ordergeneric viagra toronto [url=http://newmedicforum.com]Buy Priligy[/url] viagra eye pressurekamagra by ajanta pharma [url=http://shopsildenafilus.com]buy super kamagra[/url] kamagra supplies uklevitra price uk [url=http://shoplevitra.com]best price on levitra[/url] how does levitra workcialis commercial music [url=http://fast-tadalafil.com]Cialis Online[/url] generic cialis canadian

Anonymous said...

I am in fact grateful to the owner of this web page who has shared this impressive article at here.