‘Huyo mama ni nani…?’ wakauliza
‘Huyo ni mtu katumwa kutoka mbinguni,
kuwakomboa akina mama wasio na watoto, ndio maana anaimba hivyo, kuwa mwenye
kutaka mtoto naye aimbe, ‘nataka mtoto wangu..’akasema huyo mwanaume.
‘Nani kakuambia anhitaji mtoto, tulio nao
wanatushinda, fujo kelele, gharama za kuwasomesha, …wewe unataka watoto
tena…’akasema mama mwingine,
‘Wewe hutaki watoto, lakini ukumbuke kuwa
kuna wanaowataka, angalau hata mmoja lakini hawajajaliwa kupata….’akasema mama
mwingine.
‘Sasa ndio hao wameletewa huyo mjumbe,
akisema `nataka mtoto wangu…’ na wewe unayetaka mtoto, unatakiwa uutikie,
uombe, shida zako, ndio maana watu wanamfuatilia huyo mama
wakimuigizia…’akasema huyo mwanaume.
Umbea ukaanzia hapo…
Je ni kweli, mama huyo ni mjumbe kutoka
mbinguni…
Tuendelee na kisa chetu
********
‘Ngoja nitoke mara moja, nikaitikea mara mbili mbili tatu, huenda
nikaipata hiyo Baraka,…’akasema mama huyu, na kutoka kulifuatilia hilo kundi,
na yeye akawa miongoni mwa wanaoitikia,
‘Nata-nata, nataka, mtoto wangu’
Mama yule akawa aanalifuatilia
hilo kundi, halikuwa mbali sana, lakini kwa vile lilikuwa likitembea, na watoto
wamejaa, ikawa ni kazi kufika karibu sana, hasa pale alipokuwa huyo mama.
Na mama huyu akawa na hamasa, ya kumuona huyo mama muimbishaji,
ili apate cha kuongea, kama akiulizwa, sasa akawa anamkaribia huyo mama
anayekuwa kama anaimbisha, lakini kila akimkaribia , huyo mama anakuwa kama
kahisi kuna mtu nyuma anamfuatilia, akawa anaongeza mwendo, au anapinda kushoto
au kulia kumkwepa, na watoto wanamzonga kiasi kwamba anashindwa kumfikia.
Alijaribu tena na tena lakini baadaye akakumbuka kuwa anahitajika
nyumbani, mume wake anaweza akawa karudi,…kwahiyo akakata tamaa kumfuatlia huyo
mama, na kugeuka kurudi huku akisema;
‘Mbona huyo mama anaonekana kama sio wa kawaida, na kwa jinsi anavyoonekana mimi nahisi ana
walakini….’akasema kimoo moyo huku akigongana na watoto wanaomkimbilia huyo
mama.
‘Mhh, na kwanini haonyeshi uso wake,….ningemuona angalau sura
yake, nikajua yupoje, na kwanini watu wanasema ni mama kutoka mbinguni…kwa
kigezo gani, au ni tetesi za uvumi, maana watu hawaachi kuvumisha uwongo….mmmh
mimi, sijui lakini, nitasikia ukweli baadaye….’akatulia kwanza alipoona watoto
wanazidisha ghasia na yeye hawezi kushindana nao.
Mama yetu huyu aliyeota
ndoto, akawa anarudi kwake, huku bado akiendelea kuusikia huo wimbo ukiimbwa,
maana umeshakuwa wimbo tena, ‘Nata-nata, nataka, mtoto wangu …..’na watoto nao huitikia
hivyo hivyo …..’ ‘Nata-nata, nataka, mtoto wangu …..’ hata mama huyu naye akawa
anaitikia hivyo hivyo akipiga piga miguu yake chini kufuatilia jinsi
wanavyoimba, haraka haraka kurudi nyumbani.
Mama alipofika nyumbani
kwake, alikuta mlango upo wazi, alikumbuka aliurudishia japokuwa hakuwa
ameufunga na uungua kwani hakutarajia kukaa sana, na kuuona upo wazi akaanza
kuhisi wasiwasi.
‘Mhh, nisije nikawa nimeingiliwa na wezi….’akasema
Akawa anausogelea mlango wake, na kuchungulia ndani, akahisi
harufu ya mume wake, kila mtu anajua harufu ya mwenzake, mafuta gani
anapendelea kupaka, manukato, na mama huyu anajua kabisa harufu ya mume wake
ipoje, akajua kuwa ni mume wakeyupo ndani.
Akaingia kwa aibu akijua yeye ni mkosaji, kwa kuondoka nyumbani na
tena hakuwa amefunga mlango vyema, hata
hivyo haijatokea kabla , mara nyingi mume wake akirudi anakuwepo ndani, akajipa
moyo kuwa mume wake hatakasirika sana, ni kweli mara nyingi mume wake akirudi
kazini yeye ndiye anayempokea.
Alipoingia ndani akamkuta mume wake amekaa kwenye sofa yao ya
kuanzia maisha, akiwa kajiegemeza, alionekana kuchoka na akawa kama kasinzia,
alimtupia jicho mume wake akamuonea huruma, ….kachoka, ana njaa, …
Mume wake akahis mtu kuingia, akafumbua macho, na macho yake yakakutana
na macho ya mke wake, mke wake alisogea na kusimama mbele yake. Mume huyu
akajiinua na kujinyosha na kumuangalia mke wake, mke wake akatangulia
kumsalimia
‘Za kazini mume wangu….?’ Akamsalimia
‘Nzuri tu, za hapa…’akasema kwa sauti kavu kuashiria kutokuwa na
furaha , mke alijua ni kwasababu ya kuondoka hapo nyumbani, na akataka kugeuka
kwenda kumtayrishia mumewe chakula na mume wake akauliza
‘Niambie kuna nini kimetokea?’ mume wake akauliza sasa akiwa
kasimama akijinyosha, na yeye akaanza kumsimulia mume wake habari za huyo mama,
na mume wake akasema;
‘Wewe nipe chakula niondoke zangu, maana nyie watu msio na kazi
kitu kidogo tu hamtaki kiwapite…..’mume wake akasema.
‘Samahani mume wangu, unajua niliposikia kuwa mama huyo ni mtu
kutoka mbinguni kaja kuleta baraka za uzazi, na kuondoa mikosi kwenye ndoa,
nikaona na mimi nikajionee, tuipate hiyo baraka….’akasema
‘Sasa umeshaipata hiyo baraka?’ mume akamuuliza kwa dharau.
‘Mhh, mume wangu naye…baraka utazipataje na kuziona kwa sikumoja, onaje
si mpaka ipite siku kadhaa, sisi tuombe mungu, ila huyo mama ni mtu wa ajabu
sana, sikuwahi kuona uso wake, hata sijui anafaanaje, bado nina mashaka
naye…’akasema
‘Ohooo, wewe mwenyewe umeshatilia walakini,…imani yenye mashaka
sio kamilifu, hebu niambie kwani yupoje
huyo mama?’ mumewe sasa akawa na hamasa kusikia zaidi.
‘Ni….sijui nimuelezeje, anisamehe nikisema hivyo, ni kama vile hana
akili nzuri , maana anavyokimbizana na watoto, anavyoimba ni kama mtu
hajitambui vile kawa kama mtoto mtoto kivitendo…’akasema
‘Ndio huyo unasema analeta baraka, si nimekuambia kwa vile huna
kazi, basi umeona hilo ni la muhimu, umeacha nyumba bila hata kufunga mlango na
funguo, hivi ungeibiwa ungekuja kulalamika…’akasema mume wake .
‘Mume wangu samahani, nilijua nafika mara moja na kurudi tu,
kwanza nani angetuibia wataiba nini humu, …ila kwakweli mume wangu, mimi
nikisikia jambo linalohusu kupata mtoto, sitaacha kuliendea ilimuradi tu liwe
la halali…’akasema
‘Haya bibiye, maana na wewe na mtoto….hujasikia watu wanatupa
watoto majalalani au chooni, unafikiri wanapenda kufanya hivyo, ni shidaa tu
mke wangu…., watoto wana heri zao, nakubali kweli, mkioana mnatarajia hilo, lakini pia kutokana na nakama za maisha watoto
wanaweza kuwa mzigo….’akasema.
‘Ukiwa nacho ni lazima utasema hivyo, na wanaosema hivyo wanasahau
kuwa kuna watu wanatafuta, hawana kabisa….’akasema
‘Ni kweli mke wangu, kuna wanaotafuta kama sisi, lakini wenye nao,
wana matatizo yao wewe waulize watakuambia, ndio ni kweli watoto ni furaha ya
ndoa, ….hata sisi tunatamani tuwapate, lakini kwanza tumshukuru mungu, kwani,
hujui kwanini mungu ameamua kutucheleweshea kupata mtoto, wewe hujui hekima ya
mungu,….’akasema mume wake.
‘Ni kweli lakini subira hii imezidi, miaka kumi, hatuna hata ,
angalau hata mima ingelitunga na kutoka, hakuna hata dalili,….mmmh, inataka
moyo,….’akasema mke wake na hapo akamuona mume wake kama na yeye kazama kwenye
mawazo, akajua hilo na yeye limempa jakamoyo. Halafu mume wake akainua kichwa
na kumuangalia mkewe, akasema;
‘Kwahiyo unataka kusema nini?’ akauliza
‘Tujaribu upande wa pili….’akasema
‘Una maana gani kusema hivyo, sijakuelewa…?’ akauliza mume wake
akimkazia macho
‘Twende kwa wataaalamu wa tiba mbadala…’akasema mke wake kwa sauti
isiyo ya kujiamini.
‘Mbona tulishaenda huko mara nyingi, au una maana gani ,…kuna watalaamu
wengine zaidi ya hao,…mke wangu mara ngapi tumeenda huko na kupata dawa, hebu
achana na hayo mawazo..’akasema.
‘Ndio tatizo lako mume wangu, tuliowaendea sio wale wataalamu
wenyewe , kuna wale wataalamu wa kuangalizia,…wanagundua tatizo lipo wapi…’akasema
‘Eti nini, umeanza kuwazia hayo, hebu nipe maji ninywe niondoe
zangu, maana nyie wanawake mkiwa hamuna kazi mnadandaganya tu, ….’akasema mume
mtu.
‘Nani hana kazi mume wangu, wewe unafanya kazi huko nje, na mimi
nafanya kazi humu ndani, ni mpangilio tu, hiyo kauli yako ya kusema hatuna kazi
sio sahihi, na sijakaa kuongea na watu ovyo, …’akasema .
‘Sasa sikiliza sitaki hayo mawazo , na nisije kusikia umeenda
huko, unakumbuka mdogo wako alivyokuasa kuhusu watu hao, mdogo wako shule
imemkomboa, ana mawazo mapana, na vizuri kasomea maswala ya afya, mimi
nimemuelewa sana, ..tusubiri mke wangu, achana kabisa na imani hizo, umenisikia…’akasema.
‘Nimekusikia mume wangu….’akasema mke mtu alipoona mume kapandisha
sauti kuashiria kukasirika, na haraka haraka akaondoa vyombo.
Baadaye mume wake aliondoka.
Yeye akawa kakaa pale alipokuwa kakaa mume waks na kushika shabu,
akiwaza, na akashituka pale aliposikia zile kelele zikirudi tena, ilikuwa kama
zile kelele nje zimetoweka, kama vile hao watu walimuogopa mume wake, kwani
mume wake alipoondoka tu, haikupita
muda, mara akasikia kutoka barabarani;
‘Nata-nata, nataka, mtoto wangu …..’, aliposikia hivyo, mama huyu
akasimama na kusogea dirishani, kuchungulia dirishani, sasa watoto
walishapungua, walibakia watoto wachache, akaweza kumuona yule mama, lakini
alikuwa kampa mgongo.
Pale aliposimama yule mama,
kulikuwa na kundi la watoto wamesimama wakimchokoza, na yule mama aliokota
fimbo akawa anawatishia kuwachapa wale watoto , na watoto wakakimbia na baadaye
wanamrudia tena , na wakimfikia yule mama yule mama anawaimbia;
‘Nata-nata, nataka, mtoto wangu …..’ ananyosha mikono kama anaomba
halafau anashika kichwa kama kukata tamaa, basi na watoto nao wanakuwa kama
wameamrisha waimbe na kuigiza vile vitendo, na baadaye wanaruka juu hewani;
‘Nata-nata, nataka, mtoto wangu …..’
Kwa hali ile watoto wengi wakawa hawaondoki karibu na yule mama,
na kila muda ilionekana wakisogea karibu na nyumba ya huu mama, kiasi kwamba na
yeye aliona ni kero. Akashindwa hata kujipumzisha, kwani muda kama huo, wakati
mume wake hayupo hujilaza kidogo, akiamuka huanza kazi za usafi na mapishi kwa ajili
ya chakula cha usiku, lakini kutokana na hizo kelele karibu na nyumba yao
akajikuta hawezi kulala, akasema;
‘Watoto wazuri, lakini fujo
zao…aah, mimi nitatoka hapo nje niwafukuze…’ Akasema na kufungua mlango kutaka
kutoka nje, akiwa na dhamira ya kuwakemea waondoke eneo la nyumba yake, na
wakati anafungua mlango simu yake ya kiganjani ikaita, akatulia kusikilizia iliita ikakatika.
Baadaye tena ikaanza kuita, akajua mpigaji kweli anahitajio na
yeye, Ikabidi arudi ndani pale
alipoiweka simu yake.
Akaichukua, na hakutaka kuangalia aliyepiga ni nani, akaiweka
hewani na kusema …
‘Halloh, nani mwenzangu…’ aliuliza kabla hajaangalia nani
aliyepiga, aliposikia sauti akajua ni sauti ya mdogo wake.
‘Shikamoo dada…’, akasalimiwa
‘Marahaba, hamjambo huko kazini..?’ akauliza
‘Mhh, dada, ….’akaguna na sauti anayotoa sio sauto yake ya
kawaida, na mara mdogo wake akaanza kulia, na aliposikia hivyo kilio, mwili
ukamuisha nguvu, akakaa vyema kwenye kiti, maana kilia kina maana nyingi, na
mara nyingi ni ishara ya msiba.
Kiujumla ndugu hawa wanapendana sana, na kusikia kilio kwa mdogo
wake, ilikuwa ni kama kapigwa sindani ya ghafla, na akilini akaanza kumuwaza
mdogo….
Mdogo wake anafanya kazi hospitali ya mkoa, amehamishiwa huko hivi
karibuni tu, na mara nyingi walikuwa wakimtegemea sana yeye walipokuwa kwenye
hali mbaya, japokuwa na wao ndio waliomsaidia kupata mafunzo hayo ya unesi, na
alipopata kazi, hakuwatupa, akawa ni tegemeo lao kubwa na kwa wazazi pia, hasa
kipindi walipokuwa kwenye mkwamo wa kimaisha.
Sasa hivi angali mume wake ana kibarua wanajiweza wenyewe,
japokuwa kipato sio kizuri sana, lakini siku zinakwenda. Mwanzoni kabisa mume
wake alikuwa na kazi nzuri, kabla hajapunguzwa kazini, na kipindi hicho ndipo
walimchukua huyo mdogo wake alipomaliza kidato cha nne, wakawa wanamsomesha
unesi.
Alipomaliza hayo mfunzo, na kufaulu vizuri akaomba kazi hospitali
ya wilaya, na bahai nzuri akapata kazi, na akawa na juhudi kubwa , akiwa humo
kazini, akawa anajitahidi kujiendeleza na kufikia kiwango kizuri, ikatokea
uhamisho.
‘Dada na shemeji nimepewa uhamisho kwenda kufanya kazi hospitali
ya mkoani, hospitali ya rufaa…’akawaambia
‘Oh, hongera, ina maana cheo kimepanda…’wakamwambia.
‘Ndio hivyo, nashukuru kuipata hiyo nafasi maana huko nitajitahidi
nisome zaidi, nataka niwe dakitari kabisa…’akasema
‘Ni wazo zuri, na juhudi yako itakueletea matunda muhimu ni
kuzingatia kazi, na usifanye mzaha, kama unavyoona hali zetu, …wazazi wetu ,
kwahiyo uije kuharibu kazi, …’akaaswa.
‘Kwakweli kazi kwangu ni muhimu sana, sitafanya makosa, …nitajitahidi
sana, sitawaangusha…’akasema.
Na baadaye kweli akaondoka kwenda kufanyia kazi hospitali ya mkoa
ya rufaa, alipopata uhamisho huo ikabidi atafute chumba huko huko mjini, karibu
na maeneo anapofanyia kazi, na kuondoka kwake mwanzoni ilikuwa kama pigo, kwani
asilimia kubwa walikuwa wakimtegemea yeye pale walipokuwa wamekwama kabisa,
hakuwa na hiana ya kutoa msaada.
Ikawa wanawasaliana kwa simu, na siku akiwa mapumziko anakuja
kuwatembelea mara moja moja, na kuna kipindi anakuwa adimu kabisa kutokana na
kazi zake.
Katika familia yao wamezaliwa wao wawili tu yeye na mdogo wake
huyo, kwahiyo wanapendana sana, na kipindi wanaishihapo pamoja, watu walidiriki kuwaita mapacha, japo
kiumri walikuwa hawaendani, waliwatania hivyo kwa vile kisura wanafanana, ingawaje yeye alishaanza kuonekana mtu mzima
zaidi, na ukichanganya na mawazo, sasa hivi anaonakana mama …
Basi aliposikia sauti ya
mdogo wake akilia..kwanza alivuta pumzi, lakini aliposikia nalia, hata yeye
akajikuta machozi yanamlenga lenga, akavuta pumzi , akisubiria kusikia tatizo,
na hasa inavyoelekea ni msiba….ni nani kafa…’akawa anajiuliza
‘Vipi habari za huko..?’ akaulizi akijaribu kujipa moyo , alihisi
sauti ya mdogo wake, japo anajitahidi lakini yupo katika wakati mgumu, kuna
jambo baya limetokea huko anakofanyia kazi, au kuna taaarifa ya msiba.
‘Habari sio nzuri dada….kuna matatizo…..’akasema na kilichofuata
hapo ni kilio.
‘Unasema kuna matatizo, tatizo gani , kwani imekuwaje, sema basi mbona unaanza kulia, mimi
unanitisha, kuna msiba au kumetokea nini…’ kabla hajasikia vizuri simu
ikakatika.
Alipoangalia akakuta simu yake haina chaji, akakumbuka kuwa
alisahau kuichaji usiku, kwasababu umeme ulikatika, Akakimbilia kuichaji,
lakini akakuta umeme hakuna.
‘Mungu, hili sasa balaa,…huu umeme jamani, kila siku kukatika,
sasa sijui nifanye, maana nahisi mdogo wangu yupo kwenye matatizo makubwa, mume
wangu angelikuwepo tukashauriana, hata ikibid mtu apande basi aende huko, …’
akajikuta anaongea peke yake, mara ningi akasikia kelele sasa zikiwa zinatokea
mlangoni mwake.
‘Nata-nata, nataka, mtoto wangu …..’ mama huyu subira ikamshinda,
akasogea pale mlangoni na kufungua mlango, kwa hasira akasema;
‘Hata mimi nataka mtoto wangu..ondokeni hapo nje, mnanipigia kelele,
nataka mtoto wangu, nataka mtoto wangu, nani kawaambia mtoto wenu yupo hapa, ….’huyu
mama akaongea kwa hasira na watoto wakakimbia, lakini yule mama akawa kasimama
pale pale, akiwa kageukia barabarani.
Mama huyu akamuangalia yule mama akiwa kabakia peke yake…alikuwa kavaa
gauni refu linampwaya, la mistari mistari, kulikuwa na mikanda ya kufunga kati
kati, lakini hakuiunga, kaiacha inaning’inia tu….miguuni hajavaa kitu…, akataka
kumuambia yule mama ageuke amuone sura yake.
Alipoona huyo mama kasimama tu hageuki, akaona asipoteze muda,
kwanza wa nini, wakati ana linalomsumbua kichwani, akageuka kurudi ndani akiombea umeme urudi,
lakini hakukuwa na umeme, akachukua simu
yake na kujaribu kuiwasha tena, bila
mafanikio. Akairudisha sehemu ya chaji na sasa akawa anawaza la kufanya.
‘Mhh, hapa inabidi nikaombe msaada….’akasema
Akatoka nje ilia aone kama atampata mtu wa kumuomba simu, lakini
alichoona ni wale watoto wakiwa wanazidi kujaa eneo karibu na nyumba yake.
Akatoka hadi kwa jirani, jirani yake hakuwepo, akarudi nyumbani akiwa hajui
afanye nini.
‘Hapa inabid niende kupiga simu za vibandani, lakini pesa niliyo
nayo hapa ni ya matumizi ya usiku, haitoshi, …na hata sijui nifanyeje…’akasema
akijaribu kuhesabu pesa aliyo nayo, akagundua kuwa haitawezekana, akabakia
kushika shavu, na mara akasikia mlango ni kukigongwa.
‘Hodi hodi hapa…’ akasikia sauti ya mume wake ikiita kwa nje
Kwanini mume wake akapiga hodi hivyo kwa mbali, sio kawaida yake,
na sauti hiyo inamtisha akikumbuka na simu ya mdogo wake, basi nguvu
zikamuishia, ….’taratibu akawa anatembea kuelekea mlangoni, akashika kitasa na
kufungua mlango, moyoni akiwa kidogo na amani kuwa mwenzake kaja wataongea la
kufanya, lakini bado moyoni hakuwa na
amani, kuna nini kimetokea ….
NB: Tusihie hapa kwa leo
WAZO LA LEO: Mawasiliano ni kitu muhimu sana, japokuwa
wengi siku hizi hawatilii sana umuhimu wa mawasiliano…wengine hutumia
mawasiliano hayo kudanganyana tu, nipo ‘nipo mahali fulani kumbe sio kweli, au
mtu akipokea simu au kupiga simu haweki kipaumbele cha jambo, anaweza kuanza
kuongelea mambo mengine yasiyo na umuhimu, au salamu ndefu, na kuliweka lile
jambo la muhimu baadaye. Tukumbuke kuwa wakati ni ukuta, na umuhimu wa jambo ni
kipaumbele chake. Lipe jambo umuhimu wake, hasa unapoongea kwenye simu, na mengine
yasiyo na umuhimu yaje baadaye, na pia tujali gharama zake.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment