Kisa chetu kinajaribu
kutukumbusha wajibu wetu, kama familia
na jamii kwa ujumla, mapungufu yaliyopo na athari zake. Kuna baadhi ya
wanaume wanachukulia vibaya tafsiri ya mwanamume kuwa kichwa au kiongozi wa
familia. Tafsiri hiyo hupotoshwa na kutumiwa sivyo ndivyo.
Kama wewe ni kiongozi wa
familia je unajua wajibu wako kama kiongozi, usitumie mabavu na nadharia za
imla, kuwa wewe ni kila kitu, hapana, uongozi unahitajia hekima, sasa wewe
mwanafamilia kama unalijua hilo kuwa wewe ni kiongozi, hebu jaribu kutafakari kwa
kila jambo unalolifanya, faida na hasara zake.
Katika jamii zetu, wapo
baadhi ya watu wamediriki kuvuka mipaka na kufanya mambo ya aibu, kupiga,
unyanyasaji, na imani za kishirikina, haya yapo na yanahitajika kuelimishana.
Katika kisa hiki
tunaendelea kuona hali hiyo, inayowakumba akina mama, kama wahanga wakubwa wa
madhila ya imani zisizofaa, ubabe uliokithiri, na unyanyasaji usiojali utu wa
binadamu.
Ndoa ambao asili yake ni
kuunganisha udugu, na kuleta chimbuko jingine kwa ajili ya kuendeleza vizazi,
wengine wanaichukulia kama sehemu ya uatawala wa kiimla. Ndoa ikijengwa vyema,
ikawa na mahusiano mazuri, ndiyo inakuwa chanzo kizuri cha jamii, na kinyume
chake ni kuwa na jamii iliyojaa chuki, uhasama, na mwisho wake ni ukosefu wa
amani.
Kama ni hivyo basi, kumbe
tunawajibu wa kuwaelimisha wana ndoa wajue wajibu wao, mume na mke, kila mmoja
kwa nafasi yake, ili wakijaliwa kupata watoto, wawe walimu wazuri wa kwanza
kwani mzazi ndiye mwalimu wa kwanza wa kiumbe kinachozaliwa.
Lakini pia tukubali kuwa,
ndoa inaweza ikawa na mitihani yake, inapotokea hivyo, wanandoa kama wanadamu
wenye utu, wajaribu kuikubali hali, lakini baada ya kushauriana, kufanya
utafiti wenye tija, kuona tatizo lipo wapi.
Kwenye kisa hiki tumeona
tatizo la kukosa kizazi, wanandoa wengi wanapofikiwa na mtihani huu, mtu wa
kwanza kunyoshewa kidole ni mwanamke, hivi kweli mwanamke anapenda, au alipenda
iwe hivyo….tuwe makini. Lakini pia kuna hawa watu wenye elimu nyingine elimu ya
kiasili, ambao wanatumia vipaji vyao kujaribukutatua matatizo ya kijamii, hawa
wanaoitwa waganga wa asili.
Katika kila hali kuna watu
wengine huitumia hiyo hali kwa ubinafsi wao, waongo, wahadaaji, ambao huingilia
Nyanja fulani wakati hawazifahamu vyema, nia na malengo yao ni kuharibu au
kunufaika kusipo halali.
Tanzania sasa hivi
inasfika kwa imani hizo za kishirikina, na chanzo ni kutoka kwa hawa waganga wa
kienyeji, ambao wamejivika nguvu ya kutoa riziki, nguvu ambayo hawana.
Wanawahadaa watu kuwa wakitumia viungo vya wanadamu wanaweza kutajirika, hili
haliiingii akilini kwa mwenye utu na hekima.
Sasa kama jamii tufanyeje,
hili ni swai la kila mmoja wetu, kwani, haya yote yanatokea ndani mwetu, sisi
ndio tunaokwenda kwa waganga kwa siri kutaka kujua, au kuelekezwa namna ya
kupata jambo. Kama ni hivyo basi kumbe sisi wenyewe ndio asili ya tatizo, na
kama sisi ndio asili ya tatizo, kumbe pia tunaweza kulimalizia hili tatizo.
Cha muhimu ni kujua kuwa
riziki, utajiri, hauji kwa kufikirika, hauji kwa kutumia migongo ya wengine,
utajiri wa namna hiyo ni batili na una madhara. Huwezi kupata utajiri kwa
kutumia viungo vya watu, hebu niambia hivyo viungo utaviuza kama nyama,….kwanini
hatuna hekima ya kulitafakari hili.
Huyo anayekuhdaa, je ni
tajiri, …aliwahi kufanya hivyo akatajirika, mbona hali yake ni dhalili zaidi
hata na ya kwako. Huyo ni wakala wa shetani mkwepe, na tafuta njia halali za
kupata utajiri.
Kisa chetu kinaendelea ,
sasa hivi tukielekea moja kwa moja kwenye hospitali ya mkoa, hospitali ya
rufaa, ambapo mama wa rafiki yangu, ambaye ndiye anatusimulia hiki kisa,
alipopelekwa.
Tuendelee na kisa chetu…
************
Walipoika hospitali ya rufaa, wengi
walishakata tamaa, wakijua sasa mama hatapona na huenda wakapoteza mama na
kiumba chake kilichopo tumboni, na hata dakitari bingwa alipoona ile hali ya
huyo mama, alifikia kutikisa kichwa na kusema;
‘Mhh, hapa kuna mawili, …kumuokoa
mama, na kumpoteza mtoto, au kumpoteza mama na kumuokoa mtoto…’ kauli hii
iliwaanya waliokuwepo hasa madakitai wasaidizi kujua kuwa kazi iliyopo mbele
yao ni kubwa, na kila mmoja lihitajika kutumia ujuzi wake wote.
Dakitari bingwa, aliwaita
madakitari wenzake, na kuwaelekza nini cha kufanya. Hili lilikuwa zoezi
lakumuokoa mtoto au mama wa hicho kiumbe kilichokuwa tumboni. Kila mmoja kwa
nafasi yake akaanza kuhangaika, na mama akaingizwa chumba cha upasuaji.
Tukumbuke mama huyu
alifikishwa hapo hajitambui, hata kauli hana. Damu nyingi zilishapotea, kwani
alishaanza kuvuja damu, achia mbali ile damu iliyopotea kwa kuchanwa na miiba
na seng’enge. Ukumbuke pia kuwa mama huyu bado alikuwa na vidonda vya miba
iliyomchoma usoni na sehemu nyingine za mwili.
Majeraha mengine yalikuwa makubwa, kiasi
kwamba, uso ulihumuka na kupoteza taswira yake ya kibinadamu. Na kwasababu
alikaa kwenye maji bila ya matibabu vidonda vilishaingiwa na virusi na vingine
kuonyesha dalili ya kuoza.
‘Hapa tuna mitihani, kwani
mama anahitaji matibabu ya vidonda, lakini hilo sio muhimu kwasasa inabidi
tulitulize kwa dawa maalumu, ila cha muhimu kwasasa ni huyo mtoto aliyepo
tumboni, inaonyesha dhahiri kuwa tusipofanya juhudi za haraka, tutawakosa wote
wakiwa hai, kwahiyo tukimbilie hili kubwa la kumuokoa mtoto. Akasema yule
dakitari kuwaelekeza wenzake.
Kipa umbele kikapelekwa
katika kuokoa kiumbe kilichopo tumboni,…
Ndani ya lile jopo
kulikuwepo na dakiatri kijana, huyu alikuwa kaja pale kupata uzoefu baada ya
kupata masomo yake huko nje. Aliporudii na ujuzi wake,hakutaka kusubiri likizo
imuishie nyumbani tu, aliamua kujitolea kwenye hospitali hiiyo iliyokuwepo
mkoani mwake.
Kazi hii ya udakitari ilikuwa ndoto yake toka
akiwa mdogo, na lengo lake ni kufikia ngazi ya dakitari bingwa wa uzazi. Yeye
alishuhudia wakina mama wakipoteza maisha katika eneo lao, kwa kukosa huduma na
wataalamu, akaweka nadhiri moyoni kuwa atajitahidi asome hadi kiwango cha juu,
ili aje kusaidia katika tatizo hilo na mungu akaikubali nadhiri yake hiyo.
Kwahiyo, pamoja na kupata
ujuzi wa kazi yake, lakini moyoni alikuwa na dhima, na utashi wa kuitenda hiyo
kazi, hakuifanya kwasababu ya ajira, aliifanya kwa wito, na hata kuja hapo
kujitolea hakuhitaji malipo.
Na katika changamoto
mojawapo aliyoiwekea kipaumbele, ni kuwa kama itafikia hatua ya kuchagua nani
bakie hai. Yeye aliahidi kuwa katika kazi yake hiyo, inapofikia hatua ya
kuchagua nani apone, yeye, atachagua wote wapone. Sitaweka kipaumbele kwa mmoja
wapo, nitajitahidi wote wapone
‘Dakitari kijana , jana
tulikuwa tukiongelea swala kama hili, ukasema una hamu sana ya kuokoa mama na
mtoto , pale inapofikia hatua ya kuchagua nani apone, je katika hali kama hii
unaweza ukasemaje, …najua wewe sio mzungumzaji ni mtendaji, naombe ushike
usukani wa kuokoa maisha ya huyu mama au mtoto….hili iwe ni moja ya mtihani
wako wa kutimiza ndoto yako….’akaambiwa.
Katika hospitali hii ya
rufaa, kila muda fulani, kunakuja wataalamu wa kujiunza waliohitmi vyuoni , nia
ni kujenga uzoefu na kuendeleza fani zao, na kipindi hicho, kulikuwepo hao
wataalamu na mmoja wao alikuwepo dakitari kutoka nchi za nje, aliyefika kwa
mualiko maalumu, kwahiyo mama akawa na Bahati
ya kupata wataalamu wa aina zote.
Kutoka na hili hospitali
hii ikawa na umaarufu fulani, japokuwa wataalamu hao wengi wakimaliza masomo
yao hukimbilia nje, kutafuta kipato zaidi, tofauti na walivyo madakitari hao,
dakitari huyu kijana alikataa kwenda kufanya kazi nje, kwani akiwa masomono
huko nje, alipewa na nafasi hiyo.
‘Kwanini hupendi
kufanyakazi huku nje, wakati ukirdi kwenu utakuwa unalipwa mashhara mdogo na
hutapata marupurupu ya maana…?’ akaulizwa na wenzake.
‘Hivi wewe unapoona mzazi
wako anaumwa utafanyaje?’ akawauliza
‘Nitamtautia dawa?’
akamjibu mwenzake.
‘Basi ndicho
ninachokifanya, mimi nimetoka nyumbani nikiwa nimewaacha wagonjwa, wazazi
wangu, nikasema nakuja kuwatafutia dawa, nina uhakiak dawa nimeshaipata, je
nifaneje?’ akawa kama anawauliza.
‘Nikuambie ukweli, watu
kama wewe husihia kufa masikini, na kuja kujijutia baadaye…’wakasema wenzake.
‘Sizani kama kwa kufanya
hivyo nitakua masikini, mimi nitakuwa tajiri kuliko matajiri hao wa mali, …..’akasema
na wenzake wakamcheka na yeye akaendelea kusema;
‘Mjue kuwa kuna utajiri wa
namna mbili, kuna utajiri wa mali na utajiri wa roho, na nadra sana mtu kupata
vyote hivi viwili, ni mtihani …..mimi napendelea zaidi utajiri wa roho, maana
hata nikifa nitakwenda na utajiri wangu, na utanisaidia, sio hapa duniani tu,
lakini pia na maisha ya huko baadaye….’akasema
‘Huko baadaye unakujua
wewe, ni nani alikwenda akarudi akasema kuna maisha ..ukia umekufa tu….’wakasema
wenzake.
‘Mimi imani yangu
inaniambia hivyo, na ninaamini hivyo kuwa nikifa kuna maisha mengine ambayo
mungu katuandalia, lakini yote inategemea maandalizi yako ukiwa hapa duniani…..’akasema
‘Sasa kwanini ukawa
dakitari kwanini hukuwa mtangaza dini…’wakamkebehi.
‘Kila kazi unayofanya ina
imani ya dini, ….mimi nina imani hiyo, ukiwa umemuweka mungu mbele kwenye kazi
zako, basi hutashindwa, kwani yote yanawezekana kutokana na uwezo wake
mungu,..ndio maana mimi napenda kuwa tajiro wa moyo,….nyie tafuteni utajiri wa
mali, lakini kumbukeni utajiri wa mali ukifa, mali utaicha,huwezi kuzikwa na
utajiri wako wa mali…’akasema
‘Hizo ni nadharia za
kiimani tu,…muhimu ni maisha mazuri, mengine ukia mbele kwa mbele…..’wakasema
wenzake.
‘Hahaha, mbele kwa
mbele..niwaambie ukweli, mimi namwamini mungu mmoja, na najua kwake yeye haya
yote tunayofanya ndio muweza, usjione una akili sana, unaweza sana, ukatabakari, na kujiona hakuna zaidi yako, na
mungu hayupo, utakuwa umefanya kosa kubwa sana…’akasema.
‘Hatujasema mungu hayupo,
lakini mungu kwanini katuumba, ni ili tuishie kila mtu kwa juhudi zake,…ukikaa
kumuamini tu, huku hutafuti maisha bora, utachanganyikiwa, na utakufa, na mungu
atakuhukumu kuwa alikupa uwezo, na namna ya kuishi ukashindwa kuutumia….sasa
ndio maana tunakuambia maisha yapo huku, ukurdi nyumbani utakwenda kusota waya…’wakamwambia.
‘Nimeshawaambia mimi
nilitumwa na wazazi nikwatafutie dawa, …wanaumwa, wanasubiri dawa, wanasubiri
utaalamu wangu, siwezi kuwatupa, …..’akasema na kuwashangaza wengi.
Leo kijana huyu mwenye
dhamira ya kweli ya kazi yake, mwenye wito na uzalendo, yupo chumba cha
upasuaji na mbele yake yupo mama, na kiumbe tumboni, na anatakiwa kudhirisha
taaaluma yake….
*****
Tukiwa ndani ya chumba maalumu cha upasuaji,
Chumba hiki kilitengwa pembeni kidogo ya jengo kubwa la hospitalini, na
kilijengwa kwa utalaamu wa hali ya juu, kilikuwa na vyumba vingine viwili vya
upasuaji, ina maana wagonjwa watatu wangeliweza kuhudumiwa kwa dharura za
upasuaji. Moja ya chumba hiki cha upasuaji ndipo alipokuwepo mama
tunayemzungumzia.
Mama alikuwa katika hali
mbaya sana, vile vidonda vilipakwa dawa za kawaida za kutuliza, lakini
vilihitajia matibabu zaidi ya hayo, vidonda vingine vilishaanza kuoza, lakini
muhimu ikawa sio yeye, sio vidonda vyake, muhimu ikawa ni kumuokoa mtoto…jamani
ni nani kama mama!
‘Ni nani kama mama?’….
Alisikika dakitari huyo dakitati
mtoto akimonea huruma yule mama, na hapo akamuomba mungu kuwa amjalie huyo mama
apone, na mtoto wake, ili baadaye mtoto ajue kiini cha mateso ya mama yake, ambaye
alikubali kuteseka kwa ajili yake, na alikuwa tayari yeye kufa ili mwanae
apone, hakukata tamaa, hadi hapo alipo…
Kwa muda huo, ndani ya
hicho chumba kulikuwa kimya na sauti iliyosikika na ya mashine ya kupozea hali
ya hewa. Usingeamini kuwa ndani yake walikuwepo madakitari, wakiongozwa na
dakitari bingwa wa uzazi, wakijaribu kukiokoa kiumbe kilichopo tumboni kwa mama
asiyejitambua, mama ambaye hali yake ilikuwa mbaya sana.
Dakitari kijana akifanya
kazi yake chini ya dakitari bingwa wa akina mama, alikuwa kayaweka mawazo yake
kwa kile anachokuwa akikiifanya, na siri kubwa ilikuwa kichwani mwake…kwani
pamoja na maelekezo ya dakitari bingwa, pia yeye alikuwa akifanya mengine zaidi.
Akiwa anaongozwa kwa kauli
ya msimamizi wake kuwa juhudi zake zote kwasasa ni kumuokoa mtoto, kwani mama
hali yake ni mbaya uwezekano way eye kuishi ni mdogo. Lakini kwa dakitari huyu
kijana haikuwa hivyo, yeye aliomba wote wapone, lakini angelifanyaje, na wakati
wito ulishatolewa kuwa juhudi ziwe kwa mtoto.
‘Oh, sasa hili zoezi
likishindiana, nitakuwa nimeongpa,, kuwa nilikwenda nje kuwatautia akina mama,
wazazi wangu dawa,…’akawa anajisemea moyo huku akiendelea na kazi hiyo. Akinyosha
mkono kuomba hiki na kile, huku dakitari bingwa akiwa pembeni yake kuhakikisha
kila jambo linakwenda kama inavyotakiwa.
Humu ndani kilichokuwa kikongea ni mikono, na
jopo la wataalamu wa upasuajil ilikuwa likijitahidi kila mmoja kwa nafasi yake.
Dakitari kijana alijitahidi kufanya kazi yake kwa makini, huku akimuomba mungu
aweze kufanikiwa, kwani ile ilikuwa moja ya mitihani yake, lakini licha kuwa ni
moja ya mitihani yake, nia yake kubwa ni kutimiza ahadi yake ya siku nyingi!.
Baada ya kazi ngumu ya
kumuokoa mtoto , kama agizo lilivyokuwa, madakitari walitoka chumba cha
upasuaji kwa muda kujadili jambo wakiwa wamekata tamaa,….dkitari mtoto akawa wa
mwish kutoka, kwani kulikuwa na kazi akimalizia, baada ya mtoto kuchukuliwa
kwenye chumba kingine cha watoto kama hao.
Kwa hali ya mtoto ilikuwa
sio nzuri,ilikuwa mbaya sana…, dakitari kijana, akamuangalia yule mtoto na
akilini mwake akahisi uhai wa huyo mtoto, kwa mbali akatabasamu, akawaachia
wengine wakaendelee na huyo mtoto, yeye mawazo yake yakawa kwa huyo mama, kwani
wenzake walishamkatia tamaa.
Wenzake walikuwa
wanasubiria muda wa mama huyo kukata roho, kwani walijua yeye ni marehemu tu,
kutokana na hali waliyoiona toka awali. Kinyume na madakitari wenzake, dakitari
kijana alikuwa na mawazo tofauti alikuwa na yake kichwani ambayo hakupenda
kuwaambia wenzake kwa muda huo. Alimuomba mola wake hicho alichokifanya kizae
matunda.
Anakumbuka wakati
anakifanya dakitari bingwa msimamizi alitaka kumzuia, lakini akawa
keshachelewa, na hakukuwa na muda wa kuulizana, ikawa ni siri yake, na huenda
siri ya huyo dakitari bingwa kama alikuwa makini kuuatilia kile alichokifanya.
Walipotoka nje yule
dakitari kijana akaiinua mikono juu na kumshukuru mungu wake, na tendo hili
liliwashangaza madakitari wenzake iweje amshukuru mungu wakati zoezi lakumuokoa
mmoja kati ya mtoto au mama yake lilinaonekana kama limeshindikana.
Yeye akawajibu huku
akionyesha uso wa furaha, na kusema;
`Halijashindikana, na
hamtaamini kitakachotokea baadaye, nyie subirini ile kazi tuliyoanya ifanye
kazi yake, …' alisema na yeye akaamua kurudi chumba cha upasuaji peke yake.
Alitaka kuhakikisha kuwa alichokuwa kakifanya kwa usahihi, alitaka kuhakikisha
kuwa anayaona matunda ya kazi yake yeye mwenyewe. Akawa sasa anajaribu
kumuhudimia yule mama majeraha yake, hakusubiri muda mwingine.
Baada ya nusu saa miujiza
ya mungu akaanza kufanya kazi yake, mtoto akaonyesha dalili ya kuishi, na kilio
cha kwanza kikasikika,…na madakitari hao wakasimama na kwenda kuangalia pale
walipokilaza kile kichanga, na huduma nyingine zikafuatia.
Wote walikuwa wakisubiria
taaria ya muda gani mama huyo atakuwa kaiga dunia, na hakuna aliyekuwa na moyo
wa kurudi ndani kwenye chumba cha upasuaji, walimuachia kzi hiyo dakitari
kijana.
Dakitari kijana alikuwa peke yake ndani ya
kile chumba , alikuja kuhakikisha kuwa alichofanya kimezaa matunda! Alifikiria
moyoni kuwa kama alichofanya hakikufanikiwa basi, ina maana alichojifunza kina
walakini, lakini hakukata tama, akajipa moyo kuwa itawezekana tu, na kama haitawezekana basi ni
mapenzi ya mungu!
Akamsogelea yule mama pale
alipolala na kutafakari lile alilolifanya kwa yule mama, na alichojifunza
masomoni kama dakitari ni kuweka mbele kufanikiwa, na kama itatokea
kutokufanikiwa, ni muhimu sana kujua kosa lipo wapi, na ulianyie kazi mara moja….
Muda ukawa unakwenda na
hakukuwa na dalili zozote za uhai kwa yule mama akawa anaangalia saa na mashine
ya kuonyesha mapigo ya moyo, kuna muda mistari ilikuwa kama inataka
kunyoooka,na inafika mahali inaanza kujipinda tena
‘Oh, …mungu wangu nakuomba
utoe matunda mema ya kazi hii, sio kwamba ni kwa ujuzi wetu, ila yote
yanatokana na wewe…mama anamuhitaji mwanae na mtoto anamuhitajia mama yake….nakuomba
mola ..’akawa sasa anaomba hadi machoz yanamtoka, lakini hali ikawa ile ile.
‘Nimefanya kaosa gani
mbona nimefuata maelekezo kama ilivyotakiwa…’akawa anasema na kujariu kukakiri
kile alichokifanya na kuona kuwa alifanya vyema zaidi.
Basi moyoni akasema
iliyobakia sasa nakuachia wewe mungu, kwani hata tungelifanyeje kama mungu
hakupenda iwe haitakuwa. Hii ilikuwa moja ya imani zake…Alikumbuka nyaraka zake
alizokuwa keshazitayarisha kuhusina na ugunduzi wake ambao alikuwa hajauonyesha
wazi kwa wakubwa zake kwani alihitajia tukio kama hilo, kama litafanikiwa basi
ataweza kukamilisha ugunduzi wake huo.
Dakitari kijana hakutaka
kutoka nje, kuona nini kinachoendelea kwa mtoto, moyoni alishajua kuwa mtoto
atapona iliyobakiwa ilikuwa kama huyu mama, sasa alikuwa amemaliza kumganga
huyo mama majeraha, akawa anasubiria matokea ya upasuaji, na kile alichokianya,
akawa kakaa kwenye kiti karibu na yule mama akimuangalia;
‘Huyu mama alipatwa na
nini…..?’ akajiuliza
‘Mhh, labda alikutana na simba, akawa amemburuza kwenye
miba., Vinginevyo, kwanini uso uraruliwe kiasi hicho.
Kila mara dakitari yule
alikuwa akikumbuka yale maneno ya yule mama alipokuwa akiweweseka kabla kazi
haijaanza ya kumfanyia hiyo operesheni, mama huyu alisema;
`Muokoeni mwanangu, lakini mimi niachane nife,
na nikifa nileleni mwanangu, msimpe mtu, nileleeni mwanangu hospitalini….'
alijiuliza sana kwanini yule mama alisisitiza sana kuwa mwanae alelewe na
hospitali na wala sio jamaa zake.
‘Kwanza hao jamaa zake ni
wakina nani?’ akajiuliza kwani kuna muda alitoka kuwatauta ili kuwaelezea
kilichotokea, lakini hakukuta mtu.
Alisema moyoni kuwa huenda
ni ile hali aliyokuja nayo yule mama, au huenda kuna ugomvi huko alikotoka, au
aligombana na mumewe,lakini haiyamkini kwa binadamu kuwa na unyama kiasi kile,
kumpiga mama mjamzito na kumchana chana mama huyo usoni kiasi kwamba sura
ilikuwa haitamaniki.
Basi siku ikaisha na
hakukuwa na dalili ya kuzindukana kwa mama, lakini pia hakukuonyesha dalili ya
kukata roho kama walivyokuwa wametarajia hao madakitari wengine. Siku ya pili
ikaingia, hakukuwa na matokeo zaidi, matokea mazuri yalikuwa kwa mtoto
Baada ya siku tatu mtoto
akawa amechangamka na kuondokana kabisa na dalili zozote mbaya, lakini mama mtu
bado alikuwa hajazindukana, na hali hii iliwatia wasiwasi madakitari wakijua
kuwa hawataweza kufanya lolote kumsaidia yule mama kuzindukana. Ilibidi waitane
tena kushauriana ili kama imeshindikana wayaondoe yale mashine ya kumsadia
mgonjwa kupumua,
Lakini dakitari kijana
akakataa, akasema ana imani mgonjwa atazindukana muda mchache ujao.
‘Wewe bado kijana una
munkari na kazi bado, na hili ni jambo jema kabisa, endeela na moyo huo, sisi
kazi hizi tuna uzoefu nazo, hali kama hii…ni ya kupoteza muda tu,……’akasema
yule dakitari bingwa, akiwa na nia ya kumpa yule kijana uzoefu wake wote, kwani
kijana huyo alionekana kuipenda kazi yake vyema. Alisema kichwani, huyu yupo
kama mimi nilipokuwa makamo yake, nilipenda sana kusaidia watu…kama nchi yetu
ingetujali sana,huenda mimi ningekuwa mbali sana, lakini…
Walitoka ndani ya kikao
chao kwa haraka kwani aliletwa mgonjwa mwingine mahututi, sana, na kwa haraka
wakaingia chumba kingine cha upasuaji, na kuanza kazi hiyo, jopo zima
likaelekea kumhudumia huyo mgonjwa mpya.
Wote wakawa katika kazi ya
kuhakikisha wanamsaidia huyo mgonjwa mpya apone, na Ilibidi wamsahau mgonjwa wa
zamani kwa muda,kwani mgonjwa huyo wa zamani, alikuwa anasubiriwa azindukane,
au amalize uhai, na kama atapona kuna kazi nyingine ya ilihitajika dhidi yake
ya kuponyesha majeraha yake, na kama itahitajika upasuaji mwingine. Lakini matumaini ya mgonjwa huyo kupona
yalikuwa hayapo.
Walichofanya ni kumuachia
nesi majukumu ya kuangalia mambo mengine yanakwenda sawa, huku wakimwambia kama
kuna badiliko lolote atoe taarifa haraka iwezekanavyo.
NB: Haya ngoja tuishie
hapa kwa leo,
WAZO LA LEO: Kuna fani ambazo zinahitaji
kujitolea tu, fani ambazo zinagusa uhai na utu wa mtu, fani kama za udakitari. Wengi
wanaujua fani hii, wanaifanya kwa wito, wapo wachache wanaoweka masilahi mbele,
lakini hata ulipwe nini, kutokana na ugumu, na unyeti wa kazi yenyewe ilivyo,
haitaweza kutosheleza. Muhimu kwa vile umeikubali hiyo kazi, basi jitolee kwa
moyo kuwasaidia watu, mengine mungu atakulipa.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment