Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, January 8, 2015

NANI KAMA MAMA-15



‘Tumeua……’wakasema kwa pamoja mume mtu na mkewe, huku wakimuangalia mama akiwa kalala kwenye miba, uso hautambulikani, ni damu tupu...

‘Hili sasa tatizo, ……’akasema mume akionyesha wasiwasi baada ya hasira kumuisha, akawa anapikicha macho kama haamini vile, mkewe alipoona hivyo akamshika mumewe bega na kujigemeza kimtindo.

‘Ni kuambie kitu mume wangu, huyu keshakufa, cha muhimu tukamtupe huko mabondeni, ataliwa na fisi ……na hakuna atakayejua kuwa ni sisi tumemuua...’akasema mke  wake huyo huku akimtupia jicho mumewe la pembeni.

Mume bila kufikiri akaona ni wazo zuri,...akaangalia huku na kule, na kwa vile giza lilishaanza kuingia hakukuwa na watu wakipita, au kushuhudia hilo tukio, na kwanza watu walishachoka kuamua ugomvi kwenye nyumba hiyo, kwahiyo hata wakisikia kelele, hawasumbuki tena.

Watu wawili hawa kwa pamoja wakambeba mama, kwa kushirikiana, ilikuwa kazi kumtoa kwenye zile kuni zenye miba, na ukizingatia kuwa mama alikuwa mja mzito, basi na uzito wake ulikuwa mkubwa.

Hawakujali, akuhurumia wakati wanamtoa, miba ikazidi kumchana hata nguo zikawa ni kambakamba tu..wakamtoa pale na kuanza kumbeba kuelekea bondeni

Ili kurahisisha hiyo kazi hapo nyumbani kulikuwa na torolo la kubebea mizigo, wakampakia hapo na kuanza kulisukuma hilo torili, wakiwa wamefunika, kwahiyo hata kama mtu angeliwaona angelijua wamebeba gunia la taka, wanakwenda kutupa bondeni.

Walifanya haraka wakafika kwenye hilo bdone na kumtupia mama.....

Je mama keshakufa, au ilikuwaje, tuendelee na kisa chetu


****************

`Wewe ndio umemuua mke mwenzako, …’akasema mume mtu wakati wakirudi nyumbani.

‘Nyamaza bhana watu watatusikia,….’akasema mke mdogo akionyesha wasiwasi kwa kuangalia huku na huku.

‘Mungu wangu, ina maana mke wangu kweli ameshamekufa…’ akawa analalamika baba bila kujali onyo la mwenzake.

‘Sikiliza mimi nipo nitakuzalia watoto, cha muhimu ni sisi kuhangaika,  tutakwenda kwa mganga atairejesha nyota yangu, maana mchawi wetu ameshaondoka una shaka gani tena…’akasema mke mtu.

‘Mhh, tatizoo lako huelewi, ….’akasema na huku akikuna kichwa kwa kasi

Bwana alikuwa kama kachanganyikiwa, akawa anashika kichwa, mara anaruka ruka, na mke mdogo akimsogelea yeye anamsukuma, na hali hiyo iliendelea hadi wakaenda kulala.

Usiku ulikuwa wa maruerue kwa bwana mtu, hakuweza kulala, kila akijaribu kupata usingizi, anajikuta akiota ndoto za kutisha, mara anatokewa na mke wake, kwa maumbo toauti ya kutisha, akiwa kalowana damu au kicha kimekatika, ….na wakati mwingine anamuona mke wake mdogo akimjia na kisu kuwa anataka kumuua na yeye….akashituka na kukaa kitandani

Aalikaa kwa muda, huku akitafakari, akaona hakulaliki, akaretemka kutoka kitandani na kutembea hadi eneo la dirisha la pili, akasmama hapo kwa muda baadaye akageuka kumuangalia mke wake mdogo ambaye alikuwa kalala fofo alikuwa anakoroma usingizini bila wasiwasi.

Mke wake mdogo alimuoa akijua atatatua tatizo la kupata mtoto, na hilo alilifanya baada ya kupata ushauri kwa watu na pia baada ya kumuendea mganga wake anayemuamini….lakini matokeo yake ndio hayo.

Akazidi kumuangalia mke wake mdogo ambaye bado alikuwa usingizini, na hakuonekana kuwa na wasiwasi, akamlinganisha na mke wake mkubwa, akakumbuka siku alipomoa mke wake kubwa, baada ya kutoa ng’ombe wengi, na ilikuwa kazi kumpata….sasa ndio huyo ameshakufa, akashindwa kujizuia, machozi yakamtoka.

Alisimama pale kwa muda, akishindwa kujua afanye nini, na mara akakumbuka jambo, akageuka, na kutoka chumbani na kuelekea sebuleni, huko akaangalia pembeni ya kabati anapoweka kinywaji chake, akaikuta chupa ina chochote kitu, akapiga mafundo matatu ya harakaharaka, alikunywa kwa harakaharaka, na kujikuta akikohoa mfululizo.

Kikohozi kilipokwisha akakaa kwenye kiti na kutuliza kichwa, na huku gongo likifanya kazi yake. Akajipa moyo, kuwa kama kaua nani atajua, kama ikibidi ataoa mke mwingine…

‘Lakini mimi sikutaka afe, mbona kila siku ninampiga, tena sana, zaidi ya kipigo hiki, lakini hakuwahi kufa….aaaah,hili eeeh, lazima kuna sababu….’akasema na kuinua chupa, akagundua haina kitu akainua juu nakujaribu kumimina yakadondoka matone mawili.

‘Mhh, …..nani kamaliza pombe yangu…’akasema na kuitupa hio chupa pembeni. Akakumbuka kitu na kuinuka pale alipokuwa kachuchumaa,na kwa akaelekea chumbani.

Alipofika chumbani akakuta mke wake kalala vile vile, ila sasa kaelekeza kichwa juu, akikoroma

‘Wewe mwanamke, nimeshajua kuwa , ulipanga uje hapa ili umuue mwenzako…’ akasema na mwenzake alikuwa kimia akiendelea kukoroma.

‘Hunisikii, unanizarau eeh, yaani mimi naongea wewe unaendelea kunywa uji,..koroo-koroo….nitakubamiza…’akasema na kugonga kitanda kwa mguu, na kwa kufanya hivyo akajigonga ugoko, na kupata mauimvu, akainama kujishika kwa hasira.

‘Mhh, ….sasa utanitambua…maana siku zote naishi na mwenzako hapa, tunapigana, hafi , sasa umekuja hapa kwa nia ya kumsaidia kumbe ulikuwa na lako jambo, na umesababisha mwenzako kufa, sasa na wewe hulali, dawa ya muuaji na yeye ni kuuliwa…’ aliposema hivyo akasogea pale alipolala mke wake mdogo na kulivuta shuka kwa nguvu.

Mke akawa analalamika usingizini, akageuka upande wa pili, na jamaa kuona hivyo akaona kama kazarauliwa akaanza kumpiga mangumi,….akarusha teke kama kawaida yake na badala ya kumpiga mtu akawa anajigonga kitandani, na alipopata maumivu, hasira zikazidi kumpanda.

Mkewe mdogo akawa sasa kashituka kutoka usingizi, akakaa vyema kitandani.

‘Kwani kuna nini tena….?’ Akauliza bado akiwa anapiga miayo.
‘Kuna nini tena…wewe ni muuaji, …..yaani mimi nashindwa kulala, wewe unakoroma,…’akasema

‘Sasa nianyeje , usiku maana yake ni nini, mbona …..unanipiaga, tulale bwana….’akasema akijaribu kujilaza, na bwana mtu akamfuata pale na kuanza kumzaba vibao.

‘Mungu wangu,…mbona unanipiga…’akasema na kuinuka pale kitandani, tayari kwa kupambana alishajua kuwa kuna shari, na yeye kwa shari hajivungi, kwani na yeye sio mtu wa kukubali kuonewa akajiweka sawa na kumwangalia mume wake anataka kufanya nini.

‘Hivi wewe una akili sawasawa, usiku kama huu unataka kuleta fujo, nani kaua, situmekubaliana tukae kimya, ukianza fujo hapa huoni majirani watajua…’ akasema huku anasogea mbali na mume wake.

Kabla hajatulia vyema akaisikia kibao kikipiga nyuma ya shingo, alishangaa jinsi mume wake alivyokuwa mwepesi kiasi kile, ule umbali aliosimama, hakuzani kuwa mume wake angeweza kuruka na kumzaba kibao cha haraharaka, akapepesuka, na yeye hakukubali akageuka na kurusha ngumi ikampiga mumewe puani, akaishia kusikia maumivu yeye mwenyewe na kuupuliza mkono wake.

‘Unajifanya unajua kupigana sio, ngoja sasa na wewe uione njia aliyoondokea mwenzako..’ kabla mke hajajibu kitu, akawa kavamiwa, na kipigo alichokipata ilikuwa kama yeye ni gunia tu, sio binadamu. Mume alipotulia kupiga, kwasababu aliona mke hajibu mashambulio, akamuachia, na mke huyo akadondoka kitandani…kimya,

‘Nimeua tena…..’akasema kimoyo moyo

Hee vipi tena, wewe ulikuwa unajifanya mwamba, mbona kipigo kidogo umelegea, kumbe hamna lolote, alizoea mke mkubwa ulikua akipiga , na kupiga, lakini , mtu yupo pale pale, sasa huyu kagusa kidogo, …oh, akatizama chini pale alipodondoka mkewe kwa woga, huku akili ikisema ‘nimeua tena..’

. Akamtikisa mkewe, akamuona kakauka kimiyaaa, akatikisa kichwa kuondoa mawimbi ya pombe, akasimama huku akishika kichwa….

‘Huu mkosi…..’akasema, na kugeuka, akarudi sebuleni, akatafuta ile chupa, akaiona,akaweka mdomoni, hakuna kitu…

Kwa hasira akaibamiza ile chupa ukutani…., akaanza kukohoa mfululizo, huku akisema akilini , mbona siku hizi nakohoa namna hii, kuna sababu. Akakaa kwenye kiti chake na kutulia..haikuchukua muda usingizi ukamchukua ghafla….

Hakujua alilala pale muda gani, kwani alijikuta shingo inamuuma kwa kuegemea upande mmoja, na bega , akajaribu kuinuka kujinyosha, akaona kichwa kinamgonga, maumivu ya kichwa…na dawa yake ni kuzimua

Akasimama akiyumba yumba,akasogea pale anapoweka chupa yake, akakuta haipo. Akatuliza kichwa kufikiria nini kimetokea, na kwanini kalala pale kwenye kiti. Akaanza kukumbuka kwa mbali , japo kidogo, matukio ya jana, akakumbuka kuwa alikuwa na kazi ya kumalizia chumbani, akaita jina la mke wake wa kwanza, akaona kimya, akaita tena kimya.

‘Hivi nipo wapi,….mke wangu namuita hanitiki…..’akasema akitembea kuelekea chumbani.

Alipofika chumbani , akakuta kitanda kipo shaghala baghala na shuka, hata godoro lipo chini, akaangalia pale alipokuwa kalala mke mdogo, akaona shuka limefunika kitu, akajua ni mke wake mdogo kalala, na kwanza akasimama.

‘Wewe umeuata nini huku…..’akakumbuka akatikisa kichwa,

‘Ohoo, wewe jana ulijifanya bondoa, nikakupiga moja tu, nikakutoa knock-out….sasa sijui na wewe umekua au, kwanini toka jana hujaweza kuinuka..’akasema.

Akasogea pale kitandani akainama kumtaka kutoa lile shuka, lakini
Kabla hajafanya hivyo, akasikia sauti za watu kwa mbali, akaona sasa kama wanakuja humo kwake atashindwa la kujitetea.

‘Hili sasa ni balaa….huyu naye atakuwa amekufa…hao watu wanakuja hapa…ohooo….’akasema akageuka na kuangalia dirisha, akatikisa kichwa

‘Hapa ni kukimbia tu….’akasema, na akageuka kwa haraka akaliendelea kabati anapoficha salio lake, akakuta bado lipo,akachukua baadhi ya nguo zake na kuzifutika kwenye mfuko,  halafu akaelekea mlangoni.

Akasikia watu wameshafika eneo la numba yake, wanaongea, na moja ya sauti aliyoiskia ni ya mjumbe,…akageuka, na kuelekea dirishani, hakupoteza muda, akapanda dirishani na kwa haraka akarukia nje, na wakati anaruka akasikia jina lake likitwa kwa nje.

Hakusubiri…..taratibu akachekupa njia inayoelekea vichakani. Mkononi alikuwa na kifurushi kidogo cha nguo na rungu lake la dharura.

‘Duuh, ina maana nimeua wake zangu wote wawili nitaenda wapi leo. Akaongoza njia ya porini, akikusudia kukimbilia kijiji cha karibuni, halafu atatafuta usafiri na kwenda kokote, mbali kabisa wasipomjua.

Alihakikisha kachukua akiba yake ya pesa na vitu vya kumsaidia njiani, na wakati anaingia njia ya uchochoroni, kwenye kimsitu kidogo, akasikia sauti nyuma, akajibanza pembeni ya mti na kuangalia wapi sauti inatokea asubihi hii. Kwa mbele akaona kikundi cha watu wanne, akajaribu kuwatizama vyema ajue ni akina nani na nani. Ajabu akaona wanelekea kwake. …

Aliyetangulia hakumuona vyema, lakini alionekana ni mtu wa makamo, ila aliyekuwa karibu naye, alionekana mrefu, na pande la jitu, mkononi kashika rungu. Mungu wangu ni nanihii…oooh, shemeji yake….

‘Mhh, shemeji huyo,….’akasema ni kweli alikuwa kaka wa mke mdogo. Mtu kama yule utamjua popote alipo, kwa umbo na ushari wake. Alianza kutetemeka kwa woga, licha ya kuwa yupo mbali na wao. Huyu shemji yake ni kiboko wa kijiji, anaogopewa kama simba, akakumbuka kauli yake siku anamuoa dada yake.

‘Oya, umekubali kumuoa dada yangu kwa hiari yako mwenyewe, ole wako nisikie umemtoa damu, najua kupiga kidogo sio mbaya, lakini umtoe damu…umvimbishe mahala, … utakumbukwa hapa kijijini..’hiy ilikuwa suti ya njemba hilo.

‘Usijali shemeji siwezi kumtoa damu, nampenda sana dada yako….’akamwambia.

‘ Dada yangu nampenda sana, na kama wewe unampenda kama ninavyompenda mimi, ukae naye kwa salama na amani, la sivyo, watakuhadithia jinsi maiti yako itakavyoharibika sura…’ akampiga na kiwiko cha mkono ubavuni, maumivu aliyoyapata siku ile bado anayakumbuka hadi leo. Anakumbuka alikaa wiki nzima kila akihema anasikia hayo maumivu…

Akawa anawaangalia wale watu hadi walipofika nyumbani kwake, na wakakutana na kundi lile la mwanzo, ambapo alikuwepo mjumbe. Walikuwa wanagonga mlangoni, na kwa vile mlang ulifungwa kwa ndani hawakuweza kufungua, na sauti ya shemeji yake ikasema;

‘Vunja mlango huo, haina haja ya kupiga hodi…’ akasikia sauti ya shemeji yake akitoa amri.

Alinekana mjumbe kama hakubaliani na hilo wazo lakini yule shemeji mtu hakusubiri, akajirusha na alichosikia ni kishindo cha mlango wake ukivunjwa.

‘Wameshanitia hasara ya mlango….lakini sio muhimu kwa sasa….’akasema pale alipojificha.
Pale kwenye lile kundi alimuona mwanamke. Akajaribu kutizama vyema, na kugundua kuwa mwanamke yule anafanana sana na mke wake mdogo. Akajiuliza ni mke wake mdogo au ni mdogo wa mke wake, kwani mke wake na mdogo wake wanafanana sana.

 Lakini akakumbuka kuwa, mke wake alikuwa kitandani hadi wakati anaruka dirisha kukimbia, mke wale alikuwa kafa usiku, haiwezekani awe ndiye yeye, …akajaribu kutizama kwa uangalifu, lakini ule umbali na majani ya miti hayakuweza kumsaidia kuona vizuri. Inawezekanaje ndugu zake wajue kilichotokea, inawezekana kuwa mke wake huyo mdogo hakufa, na alikimbia kwao kutoa taarifa kuwa kapigwa…

‘Haiwezekani…’akasema akijaribu kutafakari, akajaribu kukumbuka matukio ya jana baada ya kumpiga mke mdogo, akajua keshaua, akaenda varandani akitafuta kinywaji, akakuta hakipo, akavunja chupa…akakumbuka kuna muda aliamuka kwenye kiti…akitaka kujisaidia, ….akatoka nje na kujisaidia mlangoni, hakuenda mbali….

‘Mimi nilifungua mlango kweli au ulikuwa upo wazi…?” akajiuliza

‘Nakumbuka ….kweli nilifunga mlango vyema nilipoingia, ila wakati natoka, mlango …..mmmh, wakati natoka sikumbuki mlango nilifunguaje….’akawa anawaza lakini hakupata jibu.

‘Sikumbuki kabisa kumuona mke akitoka, kwanza mfu, angetokaje…..aaah,kichwa kinauma’akawa anawaza.

‘Aaah hilo sio muhimu kwa sasa,…..yule mwanamke atakuwa ni dada yake maana dada yake ni mshari kama alivyo ndugu yake, kaja kushabikia tu, akijua kaka yake yupo…’akasema

Mara akasikia sauti, wale jamaa walioingia ndani kwake, walikuwa wametoka nje….hawakuwa na kitu chochote, alitarajia angeliona wamebaba mwili,au wanasubiri polis wafike….akata kusikia lolote kuhusu mke wake, lakini hakusikia kitu kama hicho, alichoskikia ni…;


‘Huyu mfu mtarajiwa hayupo humu ndani, katoroka, tumtafuteni , hajaondoka mbali huyu…’, akasikia sauti ya shemeji yake ikitoa amri. Na aliposikia hivyo kuwa yeye sasa ni ‘mfu mtarajiwa’ hapo akaona asipoteze muda akaingia msituni na kuanza kukimbia….

**************

Hebu sasa turudi kwa mama yangu, unakumbuka alitupwa kwenye bonde, je yupo hai…ukumbuke bonde alipotupwa mama sio bonde dogo, limekuwa likichimbika kwa mvua za mara kwa mara, kwahiyo limeenda ndani sana. , lilikuwa kubwa.

Hilo bonde mara kwa mara kipindi cha mvua wanakijiji wamekuwa wakilitumia kulima mpunga. Baba na mke mdogo wao walipomfikisha hapo, walijua kuwa wameshaua. Kwa muda ule wao walikuwa wanajua kuwa wamebeba mzoga, kwahiyo walimtupa tu kama gunia, na mama aliserereka kuelekea chini kwa kubingilika kama gunia hadi chini ya bonde, na kutua kwenye lundo la majani ya mpunga. 

NB: Tutaendelea sehemu ijayo

WAZO LA LEO: Kuna watu huwa wanapenda kuchukua sheria mikononi mwao, …kupiga, kuua, kwao ni jambo la kawaida bila kujali sheria.

Kuna matuko kadhaa watu wameuwawa, wakidhaniwa kuwa ni wezi, baadaye inakuja kugundulikana kuwa hao waliouwawa hawakuwa wezi, hawakuwa wachawi nk…waliokuwa wezi waliwahi kukimbia, au hao waliodhaniwa kuwa ni wachawi ni uwongo wa mganga wa kienyeji.


 Hebu jiulize wewe uliyeshabikia, au kutenda kosa kama hilo la kupiga hadi mtu akafa, utakuja kusema nini mbele ya mungu…, kuwa eti ni `bahati mbaya’ ya bwanawakubwa ambao wakiua husema ni Bahati mbaya…..tusihukumu kabla sheria haijasema hivyo…hilo ni kosa kubwa.

Ni mimi: emu-three

No comments :