Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, January 5, 2015

NANI KAMA MAMA-13


Mwanangu, Baba yako hakuwa na kufanya, akakubali kwa shingo upande kwani wazee wa kimila wanaheshimiwa sana huko kijijini, na hata hivyo akasema anasubiri mtoto akizaliwa kama ana sura ya huyo jamaa atahakikisha anamletea huyo raiki yake kiwiliwili kisicho na kichwa na mke atakuwa kiwete. Na rafiki yake akamjibu naye kwa maneno ya kejeli;

`Na hata akizaliwa sura kama yako, namchukua huyo mtoto kwangu, kwani hustahili kuwa na baba kama wewe anayepinga uhalali wake, hivi utapata wapi mke kama huyo anayejiheshimu, mke ambaye amejitahidi kulinda heshima yak oleo hii umadhania ubaya….wewe ni mtu wa ajabu sana…’akasema rafiki yake
‘Najua wewe utamtetea sana, si mpenzi wako, sioni ajabu….’akasema baba yako

‘Hivi kweli, mimi nitembee na mkeo, shemeji yangu, mtu na muheshimu kiasi hicho, na kwanini mimi nitembee na mke wako, wakati mke wangu unamtambua kwa uzuri wake, na wao wawili ni kama ndugu, kamuulize mke wangu kama anaweza kuamini maneno yako...’akasema

‘Kama mke wako angekuwa ni mzuri kama unavyodai wewe, kwanini uekuja kuzini na mke wangu, na unaweza kumdanganya mke wako lakini sio mimi, mimi nina akli ya kutambua, sio kama mkeo, mdanganye yeye, na ipo siku nitakunasa tu, na, subiri mtoto azaliwe ushahidi utabainika…’akasema

‘Kwahiyo unaamini kuwa wewe huzai ni tasa….?’ Akasema rafiki yake.

‘Umeanza, unafikiri mimi nitajali hao wazee, nitaliwasha hapa na wakija kuamua utakuwa hautamaniki..’akasema.

‘Thubutu, wewe kai yako kukimbilia rungu, pigana na mikono mitupu uone kazi yangu…sema mimi sipendi ugomvi, kupigana sio ani yangu…’akasema rafiki yake.

‘Ndio ujue sasa, kuwa kama wewe ni mtaalamu wa kuiba wake za wenzako kuna wataalamu wa mengine, nab ado, hii kesi wamenionea, ila nikikupatia hawatakuwa na kesi a kujibu, utakuwa maiti…wewe utaona….’akasema

‘Kwa kauli yako sitaki urafiki na mtu kama wewe, na ole wako, ukanyage kwangu, na huyo mtoto akizaliwa sio halali yako hata kama mnafanana naye, na kama atakusaidia, hatafanikiwa, maana hustahili msaada wake, kwani umeshamkana…’ akaambiwa na rafiki yake.

‘Utajua mwenyewe, ….ngoja azaliwe, utaona maajabu yangu…’akasema

‘Huyo umeshamkana, sio mtoto wako tena huyo ni mtoto wa mama,maana hakuna mama anayeweza kumkana mtoto wake, hakuna mzazi anayekana mtoto wake, wewe ni mtu wa ajbu sana, unamkana hata mtoto, hata kabla hajazaliwa..…’ rafiki yake akasema.

`Tatizo lako unafikiri mimi ninatania, we subiri uone, labda kama sio mimi…wewe unanionaje mimi, mimi siwezi kulea mimba za watu, azaliwe mwanaharamu mimi nilee tu, utakuja kuchukua kinyago chako, kikusaidie wewe…’ baba yako akasema na kuondoka hapo kwenye kikao.

Mabiashan hayo yaliendelea hata bada ya kikao, ikaonekana kuwa marafiki hao sio marafiki tena, wameshakuwa maadui..

Tuendelee na kisa chetu….

                    *************

Kikao kiliamua kuwa mama bado ni mke halali wa baba yako, na baba yako anastahiki kuhudumia mimba hiyo, kama mke wake, mwanzoni baba yako alipinga,lakini baada ya wazee kuja juu, akakubali kwa shingo upande na wanafamilia hao wakarudi majumbani kwao.

Mama aliendelea kuishi kimashaka na mume wake, hawakuwa na maongezi ya mke na mume,mume akija, kunakuwa kama hakuna mtu, kila mtu kanuna, mume bado ana hasira zake, mke naye keshajenga chuki kwa mumewe ikichanganya na matatizo ya mimba.

‘Nilimchukia mume wangu wangu kupita kiasi, sikutamani hata kumuona, na kila nikimuona mume wangu, nasikia kutapika, na wakati mwingine natapika kabisa…’akasema mama.

Moyoni nilihuzunika sana, kwani siku ile nilipotoka kwa dakitari nilitarajia iwe mwanzo wa furaha katika familia, kwani sote tulikuwa tunahitajia mtoto, sasa mungu kasikia maombi yetu, lakini cha ajabu ikageuka kinyume chake, taarifa hiyo ikazua mambo mengi, kiujunla kila nikitathimini nakuja kuona kuwa mchonganishi mkuu ni mke mwenzangu, yeye ndiye alijenga hiyo fitina japokuwa alikana kwenye kikao cha wazee.

Nilipoongea na watu, wengi waliniambia wao walisikia kabisa kutoka kwa mke mwenzangu, wakasema;

‘Mke mwenzako ndiye aliyekuwa akipita mitaani na kutangaza kuwa wewe unatembea na rafiki wa mume wako….na alisema, alishamuelezea  mume wako kuwa rafiki yake hufika hapo nyumbani, kila akitoka kwenda kwenye shughuli zake, na wakati mwingine rafiki yake huyo hushinda..’akaambiwa.

‘Mume wako nasikia kwanza alisema hana shaka na rafiki yake huyo lakini mkewe huyo akamwambia, kwanini rafiki huyo ashinde humo ndani, na akitoka anashindikizwa kwa kicheko cha kimapenzi….’

‘Jamani toka lini huyo rafiki yake akashinda nyumbani kwangu, sikumbuki kitu kama hicho maana yeye husalimia tu na kuondoka,ina maana mwenzangu aliamua kunisingizia mimi kwa kisa gani …’akajitetea mama

‘Basi ndio hivyo fitina haichanganui ukweli, na uwongo, kama vyote vinaharibu, vitasemwa tu, na ujue fitina ikijengwa husambaa kama ugonjwa wa kuambukiza,kwahiyo uwe makini na mke mwenzako huyo…’akaambiwa.

‘Mimi sikujali sana, nikamuachia mungu, na hata nikikutana na mke mwenzangu namsalimia, yeye huitikia kama hataki, sikujali.....’akasema mama

 Basi toka siku hiyo ya tukio rafiki wa mume wangu, akawa anapita bila kusalimia, kwasababu ndio njia yake, akilekea nyumbani kwake, akawa amekata urafiki na baba yako kabisa, na hata hivyo bado chuki za chini kwa chini , chuki hizi zikazidi kuendelea hadi kufikia familia, familia kwa familia zikaanza kuchukiana.

‘Lakini nyie watu wawili mlikuwa marafiki kwanini mfikie hatua hiyo?’ rafiki huyo akaulizwa siku moja na mzee mmoja

‘Hata mimi sipendi, lakini kama mwenzangu kalikoroga atalinywa yeye mwenyewe, mimi sijali tena,….’akasema

‘Mimi sikuwepo kwenye kikao, na nilisafiri, niliporudi nimesikia juu juu hivi ilikuwaje mpaka mkakosana na mwenzako, maana katika kijiji hiki mlikuwa mfano wa marafiki , watu mlioshibana mpaka mkasaidia kwenye ndoa zenu, leo hii nasikia mumekosana, kuna kitu gani kikubwa kimetokea?’ akauliza huyo mzee.

‘Mzee hata mimi mpaka siamini, lakini imebidi iwe hivyo, ni ajabu siku hiyo, maana mimi nilikuwa sokoni, nikamuona shemeji yangu…, alikuwa akinunua bidhaa zake, nikamsalimia akasema anaumwa, katokea hospitalini, basi kwasababu njia ni moja nikaone nimchukue na baiskeli, sasa kumbe hilo ni kosa….’akasema

‘Kwanini ni kosa mbona wengi wanafanya hivyo,...hilo sizani kama ndio tatizo lazima kuna jambo jingine, lakini hata hivyo kwa vile unamfahamu rafiki yako, kwanini ubebe wake za watu kwenye baiskeli yako si unamfahamu huyo jamaa alivyo…’akasema huyo mzee kwa mzaha.

‘Lakini mbona sio mara ya kwanza, …maana huyo ni rafiki yangu, …na kijijini hapa ni jambo la kawaida, na kama ulivyosema hilo sio chanzo, nasikia aliambiwa kuwa mimi natembea na shemeji yangu huyo...’akasema

‘Mhh, wewe utembee na mke wa rafiki yangu,labda umebadilika,..sijui au na wewe umeshikwa na ibilisi ukajikuta umefanya hivyo, maana binadamu unaweza ukatekwa na shetani bila kujijua....?’ akauliza huyo mzee.

‘Hapana mzee, mimi sikufikia huko...namuheshimu sana shemeji, na rafiki yangu huyo, hizo ni fitina zilijengwa na watu, na mwenzangu bila kufahamu akatekwa na hizo fitina, hakutaka kuchunguza vyema...’akasema

‘Kwahiyo alipokuona umemchukua mke wake kwenye baiskeli akakuvamia mkaanza kupigana?’ akaulizwa

‘Ilikuwa kama mzaha vile, mimi nilimpa lifti shemeji yangu huyo, nikamfikisha nyumbani kwao,...muda kama huo mara nyingi rafiki yangu anakuwa hayupo, lakini siku hiyo nilimkuta nyumbani, akatuona, sikuwa na shaka, mimi nikamsalimia kama kawaida, nikashangaa haniitikii, mimi nikajua mwenzangu kwa vile ana matatizo yake, nimuache tu, nikaondoka zangu…’akasema

‘Nikiwa nyumbani kwangu, mke wangu akaniambia kuwa, kuna jamaa mmoja ana ng’ombe mweusi kama alivyomtaka rafiki yangu, niliposikia hivyo, nikapanda basikeli yangu na kukimbilia kwa rafiki yangu,....’akasema

‘Ukajirudisha, ...huoni kwamba ulijitakia mwenyewe...’akasema mzee.

‘Unajua yule ni rafiki yangu, matatizo yake ni yangu pia, kwahiyo niliposikia kitu kama hicho nikaona matatizo ya rafiki yangu yatakwisha. Nilikwenda kwake, nikijua hiyo itakuwa taarifa nzuri kwake. Mke wangu alipoona naondoka akalalamika, maana tulikuwa na safari muhimu na yeye, nikamwambia;

‘Mke wangu huyu ni rafki yetu, ni muhimu tuwahi huyo ng’ome asije akachukuliwa na mtu mwingine, nikamuacha mke wangu ambaye alitaka twende sehemu muhimu kwenye shughuli zetu za kibiashara..unaona mzee, nilifanya hivyo kwa kujali urafiki wetu, kumbe najipaleka kweney matatizo…’akasema.

‘Unajipeleka ndio, ungetumia akili kidogo, siku hiyo ikaisha, ulivyomsaliamia akakataa kuitikia ina maana ana hasira,je hukuwahi kusikia tetesi kama hizo kabla kuwa watu wanasema unatembea na mke wake....!?’ akauliza mzee kwa mshangao

‘Mzee sikuwahi kusikia, ningelisikia ningelishaangea naye, kumuweka sawa, kuwa hizo tetesi sio kweli, ....na ningelijua kuwa imefikia hapo, hadi yeye kuamini, nisingelikwenda, maana mimi namfahamu sana huyo rafiki yangu, akiamini kitu, kumrudisha nyuma ni kazi ya ziada...’akasema

‘Sasa si unaona, ....lakini ilipangwa itokee ....Ehee ulipofika ikawaje?’ akauliza mzee

‘Nilipofika, nikapiga hodi,....kwanza sijui kwanini, maana nilipokaribia eneo lao, nikahisi mwilini ukinisisimuka, nikahisi hakuna amani, moyoni nikasema labda shemeji kazidiwa, maana nilipomla lifti, alisema katokea hospitali anaumwa, ....’akasema

‘Anaumwa! Alikuambia anaumwa nini?’ akauliza mzee.

‘Alisema hajisikii vyema, mwili mzima unama, tumbo,..alisema ni karibu kila kitu, mimi nikamtania au ndio dalili zenyewe nini, akacheka tu, hakuniambia kuwa ana ujazito....’akasema rafiki

‘Ujauzito....?’ akauliza mzee kwa mashangao.

‘Nilimtania tu, sikuwa najua loloye mzee, na niliona ajabu yeye kusema katokea hospitalini, wakati mume wake, niliongea naye alisema kwanza hapendi kutibiwa hospitalini yeye na mkewe, lakini pia kutoka na masharti ya dakitari, mkewe au yeye hatakiwi kwenda hospitalini ...’akasema

‘Mhh, mbona hiyo mpya, hata akizidiwa, hata akiiumwa?’ akauliza mzee

‘Sasa kumbe nilipokutana na mke wake alikuwa katoka hospitalini kwa kujiiba kupimwa,...uone jinsi gani hali ilivyojikoroga, mume akisikia hivyo, anaweza kuhisi kuwa na mimi nimeshiriki kumshawishi mkewe akatibiwe, na hata nilipomsalimia akakataa kuitikia, nikajua huenda...huenda, sikuwa na uhakika na hilo...’akasema

‘Ina maana mume wake alijua kuwa mkewe ana uja uzito?’ akaulizwa

‘Hakuwa anafahamu, hata mkewe mwenyewe alifahamu baada ya kwenda hospitali kupimwa, hata mimi sikuwa nafahamu, maana mkewe ahakuniambia kuwa ana uja uzito, ...’akasema

‘Ohooo, kumbe...nimeshaanza kuelewa....’akasema mzee

‘Sasa ikawaje,...maana habari inaanza kunoga, maneno ya mitaani yanatiliwa chumvi zaidi, nimesikia kutoka kwako naanza kuelewa..’akasema mzee

‘Mzee nilipofika nikiwa na furaha, nikapiga hodi, mlango ukafunguliwa uso kwa uso na rafiki yangu, kumuona sura yake nikajua kuna tatizo,...nakaribishwa moja kwa moja na kauli ya shutuma, oooh, nimesikia wewe unatembea na mke wangu, oooh, ….sikuelewa, nilipoona shutuma zinazidi nikaamua kuondoka, ile nageuka tu, rungu likanikosa,…sijakaa sawa mateke ngumi,….nikaona sasa vita, ikabidi na mimi nijjihami, tukaanza kuzipiga kweli…..’akasema

‘Mkewe akakutetea, ndio akapigwa au ilikuwaje mpaka yeye apigwe na kupoteza fahamu..?’ akaulizwa

‘Wakati naingia mkewe alikuwa kalala sakafuni kapoteza fahamu, kumbe alishapigwa hadi kupoteza fahamu...kwahiyo hadi tunapiagana mkewe hajui.....’akasema

‘Rafiki yako ana hasira sana, lakini hasira hizo ni kwa vile hajapata mtoto kwahiyo ni pamoja na wivu, hata hivyo alitakiwa kuipokea hiyo taarifa ya mkewe kwa furaha, na kama anahisi vinginevyo angesubiri mkewe ajifungue kwanza….’akasema mzee

‘Anasema hataki kulea mimba za wenzake, yeye ana uhakika kuwa mtoto sio wa kwake....’akasema

‘Oh, anasema ana uhakika kuwa mimba sio yake!? Huo uhakika kaupatia wapi,...ujue yeye anajijua mwenyewe yupoje, kama kafikia kusema ana uhakika, .....huoni kuwa kuna jambo, ...halafu anasema wewe umetembea na mkewe ukampa mimba, mmmmh, hilo lazima lina sababu, ..kuna kitu kimemfanya aamini hivyo sizani angelishikilia wazo hilo bila sababu...’akasema mzee.

‘Mganga wa kienyeji ndiye aliyemfanya aamini hivyo, hakuna sababu nyingine mzee....huyu jamaa yangu anaamini sana waganga wa kienyeji, na alipofika mitaani, maneno ya mitaani yakazidi kumchanganya, akaambiwa kuwa mimi natembea na mkewe basi kwa akili yake fupi, ikamfanya aamini hivyo, hakuna jingine ni fitina na uvumi usio na ukweli mzee wangu...’akasema

‘Ohooo, nilijua tu...hawa waganga wa kienyeji wa ramli, usipokuwa makini, unaweza ukaghilibika,...mimi najiuliza kwanini asingelienda kwanza hospitalini akajihakikishia, kwanini akakimbilia huko...’akasema mzee

‘Hata mimi nilimshauri hivyo hakunisikia, mzee, jamaa yangu huyo huwa hapendi kwenda hospitalini kabisa, yeye anaamini kuwa tiba nzuri ni hiy ya waganga wake.....’akasema

‘Mimi sikatai, kuna tiba nzuri za miti shamba, lakini kuna waganga matapeli vile vile, na kuna washirikina, ambao lengo lao ni kujenga fitina kwa watu.Unaona hao wanaoua maalibino, unajua wamepata wapi hayo, ni kutoka kwa hao waganga wa kienyeji...’akasema

‘Mzee, hayo kamuambia huyo jamaa, hamtaelewana...’akasema

‘Huyo ni sawa na ha wanaodanganywa, wanaambiwa miili ya watu inaleta utajiri, kwanini yeye asikate mwili wake, akaupta huo utajiri ...mimi sijui kwanini watu hawaelemiki,...na kwanini hamuuliza huyo sijiu mganga au mtaalamu, kuwa, kwanini yeye asifanye hivyo akawa tajiri..binadamu ana akili ya ajabu sana....’akasema mzee.

‘Mzee pamja na imani zake hizo, lakini kubwa zaidi ni kuwa yote hayo yamefikia hapo,  kwa vile kachelewa kupata mtoto...’akasema rafiki huyo

‘Mtoto, mtoto, hivi yeye hajui kuwa kupata watoto ni majaliwa ya mungu hakuna anayependa iwe hivyo,...huwezi kumlaumu mke, au kutupia lawama kwa wengine,na tatizo jingine mke wake mdogo naye hajatulia, namfaahmu sana yule binti...lakini tuyaache hayo, muhimu rafiki yako anatakiwa awe makini hasa na mke wake mdogo, mimi nikikutana naye nitamshauri hivyo…’akasema huyo mzee

‘Utakosana naye, hataki ushauri kuhusu maisha yake, mimi ni rafiki yake, lakini inapofikia kumshauri kuhusu maisha yake na wake zake, tunakosana....’akasema

‘Mhh, kama ni hivyo kuna tatizo...’akasema mzee

‘Mimi sasa nimeahidi, kama atanileta vurugu tena, safari hii nitapambana naye kiukweli, haniwezi kwa kupigana yule, kazi yake kukimbilia rungu, mimi niachieni huyo mtu, keshanichokoza, nitamtengeneza barabara, mimi sichezewi na watu kama hao, mimi ni mpole sana,lakini mtu akinichokoza vita yake haiishi, atakuja kukimbia hiki kijiji, mwenyewe utaisikia…’ hayo yalikuwa maneno ya rafiki mtu.

‘Hapana usifikie hapo, huyo anahitajia ushauri....sijui tutafanyaje, lakini tukiliachia hivi hivi linaweza kuzua balaa jingine, namuonea huruma huyo mke wake mkubwa...sijui wataishije...ana mtihani...’akasema mzee , na kuagana na rafiki huyo.

                      ******

Usuluhisho wa kimila ulishapitishwa ulitakiwa uheshimiwe,….lakini chokochoko zikawa zinachangia kila mmoja akawa anatia neno, na neno huwa maneno, na yakiwafikiwa wahusika huzidisha hasira jamaa wakawa mahasimu kweli. Wazee waliposikia kuwa bado kuna uadui wa chini kwa chini kwa watu hao, ikabidi wakuu wa koo hizo mbili waitwe, ili kusije kukavuja damu tena.

`Kama bado hamjatosheka na hukumu hii, tutaingilia sehemu ambayo mtakuja kujuta wenywe, tunatoa onyo kali…’ akasema mzee wa kimila, na mzee huyo huheshimiwa sana na wengi wanamuogopa kwa karama zake.

Wakiambiwa hivyo wanatulia, lakini choko choko za watu, wafitina, zikawa bado zinapalilia chuki.

Mvutano huo uliendelea chini kwa chini na baadaye ukafifia, baada ya kuona hakuna ushahidi wa moja kwa moja. Miezi ikapita na mimba ya mama ikawa inakuwa, japokuwa ni kwa shida kwani mume mtu alikuwa hajali kuwa mkewe ni mja mzito na anastahili kuhudumiwa , yeye akikasirika bado anaendeleza vipigo.

Mama aliomba kama baba hana uhakika na uhalali wa hiyo mimba basi amuache arudi kwao, lakini hoja hiyo ilipingwa kabisa na mumewe na hata wazee walikataa hilo kwenye vikao vilivyopita, aliambiwa;

‘Kisheria mke anapokuwa mjamzito ni wajibu wa mume husika kumlea mkewe hadi ajifungue, haruhusiwi kumuacha, ….’akaambiwa.

‘Lakini sasa nitaishije kwa hali hii, mimi namchukia kweli mume wangu, na akija hana subira na mimi, akiona kuna jambo anakimbilia kunipiga bila hata kujali kuwa mimi ni mjamzito…’akasema mama

‘Tunahitaji ushahidi akukupiga waite watu, piga ukelele, watu waje washuhudie, na sisi tutachuku hatua…’akaambiwa, lakini tatizo la mama alikuwa mvumilivu sana, anapigwa anakaa kimiya.

Matatizo ya familia hii yakawa yanaendelea, baadaye wazazi wa pande mbili wakakutana kulijadili kiundani hili tatizo, maana mume bado anashikilia kuwa hiyo mimba sio yake, na akiulizwa sababu gani muhimu, anadai kuwa keshachunguza, na anajua kabisa hiyo mimba ni rafiki yake, sio mimba yake.

Wazazi wa mume walionekana kuwa upande wa mtoto wao kuwa kwa dalili zilizojionyesha na sababu za mtoto wao, kwasababu yeye ni mume, na yeye anamfahamu zaidi mke wake kwahiyo huenda kuna ukweli, kwahiyo wakawa wanamsikiliza mtoto wao jinsi anavyosema, lakini hawana uhakika wa moja kwa moja…

 ‘Mkisema hivyo mnakosea, hawa ni watoto, na tukisikiliza maneno ya mitaani tutayumbisha hiyo ndoa yao, sisi tunamfahau binti yetu , hana hiyo tabia kabisa, lakini muhimu ni kuwasuluhisha, na sio kusimamia upande mmoja…’wakasema wazazi wa kikeni.

Mwisho wa kikao hicho wakafikia muafaka kuwa,waache mpaka mtoto azaliwe halafu watakuwa na ufumbuzi kamili…

‘Na kama ni kweli mtalipa mahari yangu….’akasema mume wangu.

‘Ukishazaa naye mahari haipo tena hapo….’akaambiwa baba yako.

‘Haipo wakati sijazaa naye, hiyo mimba sio yangu….mnataka niwaelezeje…’akasema baba, kuonyesha kabisa hajakubaliana na hiyo mimba kuwa ni yake.

Kwa vile alishajenga hiyo hoja kuwa mimba si yake, akawa akifika kwa mkewe huyo mkubwa anaanzisha visa, na mkewe kwa vile naye keshajenga chuki, basi inakuwa ni uhasama kati ya mke na mume, na mume hacheleweshi kupiga.

Kwahiyo mama bado akawa anapigwa, anasimangwa, na hilo la kuonekana kuwa mimba sio ya familia hiyo likawa limeshika kasi kweli, mawifi wakawa wanamsimanga mama kuwa kazaa nje ya ndoa.

‘Mwanamke gani Malaya , anakwenda kuzaa nje ya ndoa…kalichafua jina la familia, anataka ili kaka yetu aonekane hazai kumbe kisa ni yeye….’akawa anaambiwa. Mama akavumilia akijua kuwa akijifungua ukweli wote utabainika, na hayo yatakwisha.

‘Mimi namuachia mungu, tusubiri nijifungue na mtathibitisha huo umalaya wangu…’akawa anawaambia.

Jinsi mimba ilivyokuwa inakuwa, na ndivyo mama alivyozidi kuchoka, ikawa kazi nyingi haziwezi, wenzake bila huruma wakawa wanamsimanga kuwa yeye ni mvivu, kazi yake kutaka kulala na kula tu.

‘Kama hawezi kazi amtafute mfanyakazi wake…na kwanini mwenzake asimsaidie kazi…..’wakawa wanasema mawifi.

‘Hayo watajua wenyewe, yeye kama mke anawajibika sio kulala tu asubiri kupikiwa, ….’akasema mama

‘Kaka katuambia tuwe tunakwenda kumsaidia kazi, sisi tumechoka, ukifika ndio anajilegeza kabisa, na sisi tunashughuli zetu….’wakawa wanalalamika mawifi.

Kucha na kuchwa, mateso yalikuwa yanazidi na hakuna aliyejali ile hali yake hadi ikitimia mimba ya miezi nane.

Siku moja baba mtu alirudi nyumbani akawa amefika na mke mdogo, ilikuwa kama ajabu kwa mama, kwani mke mwenza alikuwa hafiki hapo kwake mara kwa mara hakutaka kuuliza kwanini leo imekuwa hivyo akawasubiri asikilize nini kimewaleta.

‘Nimemleta mwenzako awe anakusaidia kazi kwasababu ya hali yako,sitaki iwe sababu, nataka ujifungue ili nione ukweli, kwahiyo sitaki mkorofishane hapa..’ akasema mume mtu hakuataka hata kusikia mama atasema nini , yeye akaondoka zake. Mama hakuamini hayo, kwani yeye alishafikia hatua kuwa kama inawezekana akakae kwao mpaka ajifungue. Lakini hiyo ikapangwa ili mama asiende kwao, hakujua wenzake wana malengo gani.

Mke mwenzake akawa anafika hapo asubuhi kwa nia ya kusaidia kazi, lakini cha ajabu akawa akifika hapo hafani kazi yoyote, hatoi msaada wowote, anaweza akafanya kazi ndogo ndogo nyingine akaacha na kulala, hata chakula akawa hapiki.

‘Vipi mwenzangu sasa tutakula nini?’ anauliza mke mkubwa

‘Unaniuliza mimi, hapa ni kwako, wewe ndiye ujue utakula nini, na wewe ndiye una tabia ya kuchagua chakula, pika unachoona kinakufaa…’akasema mke mwenza kwa nyodo

‘Lakini si umekuja hapa kunisaidia kazi , mbona tangu ufike hapa hakuna kazi unayofanya, sana sana unafanya kazi ndogo, ukachukua mkeka na kulala, si bora ungejikalia nyumbani kwako tu.....?’ akauliza mama.

‘Nilizofanya zinatosha,....maana hata kwangu kuna kazi za kufanya ni nani atanisaidia kazi zangu, yaani mimi nikufanyie wewe kazi zao nichoke, niende kwangu kazi zangu za nyumbani zinanisubiri, na mume anahitajia,...sijaolewa kuja hapa kuwa mfanyakazi wako….’akasema mke mdogo.

‘Lakini mpaka kuja kwako kwangu, mimi nilijua mumekaa mkakubaliana, ukakubali kuwa unakuja kunisaidia kazi au sio?, kama huwezi basi kwanini usisema ili mimi niende kwetu, maana mimi kwa hali hii kiukweli nahitaji mtu wa kunisaidia kazi…’akasema.

‘Kwenda kwenu hilo mtajuana wewe na mume wako...najua unachokitaka, ili ukajifungulie kwenu, ufiche ukweli,ndio maana nikakubali, nije kukusaidia, sipendi ila, nataka  ukweli ujulikane, ..maana watu wanasema mimi ni muongo nimekufitinisha, nataka uzalie hapa mtoto aonekane…’akasema mke mdogo.

‘Mhh kumbe ndio nia yako....basi ngoja nizae, ukweli utawaumbua,...’mama akasema, na mke mdogo akamuangalia mke mwenzake kwa mashaka, halafu akawa kama kakumbuka jambo, akatoka nje.

Mama akaamua kujifanyia kazi zake na hata chakula akawa anajipikia mwenyewe,…na mume akija wakati mwingine anamuona akifanya kazi, haulizi kisa ni nini, …lakini baadaye mama akaona ni bora aseme ukweli, akamueleza mume wake kuhusiana na hiyo tabia.

Alipoulizwa mke mdogo kwanini hafanyi kazi kumsaidia mwenzake, akasema;

‘Huo ni uongo, kila nikifika asubuhi nafanya kazi zote, yeye hataki nipumzike, na kila ninachofanya anakitoa kasoro, nikipika chakula hataki kula, anasema ni kibaya, mara haikaiva, mara kinanuka, anamkaripia kama mfanyakazi wake, anafikia kunisimanga kuwa mimi sizai…’akasema hivyo mke mdogo

‘Jamani hayo yote yametoka wapi, mimi niliongea hivyo…?’ akauliza mama

‘Sasa unakataa sio, au niseme yote uliyoniambia….’akasema huyo mke mwenza, na mama hakujua mwenzake anataka kusema nini tena.

‘Useme yote yapi hayo, nimekuambia nini mimi, mbona wewe mwanamke mshari, kwanini humuogopi mungu wako, unazua uwongo,….’akasema mama

‘Mshari ni wewe, uliyeanza kunisingizia kuwa mimi sifanyi kazi, hayo yote umeyaanza wewe, sasa nitasema yote uliyoniambia, wewe siunajifanya unajua kuema wenzako, ….’akasema na mama akakaa kimia.

‘Amekuambia nini unachoogoap kusema?’ akauliza mwanaume.

‘Ameniambia mengi sana, na hata mengine sitaki kuyasema kwani nimeshayazoea, nilishawahi kuyasikia kwa watu nikayazarau, lakini sasa nimeyasikia moja kwa moja kutoka kwake, kaniambia mwenyewe, kwa mdomo wake…’akasema

‘Kakuambia nini….?’ Akauliza mume mtu, kwa hasira, na mke mdogo akamuangalia mama, na kumuuliza;

‘Niseme, …au ukiri kuwa hayo uliyomwambia mume wetu umetungia mwenyewe, ….?’ Akamuuliza

‘Kwani mimi nimekuambia nini, …wewe mwanamke, muogope mungu wako, unajua kusema uwongo ni dhambi,…’akasema na mke mdgo akabenua mdomo kwa dharau, na kuinama chini.

‘Nataka kuyasikia hayo aliyokuambia, vinginevyo nitakuadhibu wewe mwenyewe uliyeanza kuongea, kama nu uzushi wako ..kakuambia nini …?’ mume akamsogelea mke wake mdogo kwa hasira, na mke mdogo akaonekana kuogopa, akasema;

‘Kasema kuwa yote hayo ya wewe kutokuzaa, anayafahamu na….na amefanya hivyo kwa kiherehere chako cha kutaka kuoa mke mwingine, na alicho kifanya, alishajua kuwa wewe hutazaa tena, ndio maana akaenda kutembea na mume mwingine…’akasema mke mdogo bila kuogopa, na mume akawa kama kapigwa na shoti ya umeme, akasema.

‘Na hiyo ni siri ya yeye na rafiki yako.....kama utambana vizuri rafiki yako atakuambia..kwani yeye kafanya kama kukusaidia, usiadhirike...’akazidi kusema.

‘Nini amesema nini….!?’ Mume mtu akajitanua kifua na kupumua kwa nguvu, akamgeukia mke mkubwa na huku akitetemeka kwa hasira, akasema;

‘Hivi, wewe mwanamke unanitaka nini mimi, kumbe yote hayo sababu ni wewe, unajua kuwa ni kweli, sasa unaongea kwa kujiamini kwa vile una uhakika kuwa wewe unazaa, wewe sio mgumba tena, na mimi umeshaniharibu, ili nisizae, eeh, ...hata nikikuacha huna hasara au sio…’akasema akimuangalia mke mkubwa kwa hasira.

‘Sio kweli mume wangu, huo ni uwongo…’akaweza kusema maneno hayo lakini akajikuta hawezi kuendelea, alihisi vibaya, kutapika, akawa anajizuia, na mke mdogo akadakia na kusema;

‘Ndio hayo aliyoniambia mume wangu muulize, aliniambai na sio mara moja, muulize si huyo hapo….?’ Akasema akimuangalia mume wake kwa macho ya namna yake, na mume mtu akaguna, halafu mke mdogo akamgeukia mke mkubwa na kumuambia;

‘Je, ni kweli si kweli, je hukuniambia hivyo....?’ akauliza mke mdogo na mama alijikuta hawezi kutamka neno, ilikuwa kama kapigwa sindano ya ganzi, akabakia kaduwaa, mdomo wazi haamini hayo aliyoyasikia, anajisikia vibaya, pumzi inakuwa ndogo.

Mume akawa anamwangalia mama asema neno, lakini mama akawa hawezi hata kutamka neno, akiwa haamini…., na kukaa kwake kimia, mume mtu akaamini ni kweli…’ na kabla mama hajarejewa na fahamu na kuanza kujitetea baba akaingia ndani….

Mke mdogo akamuangalia mwenzake kwa zarau, akasema;

‘Unaona umelitaka mwenyewe kwa umbea wako...’akasema mke mdogo huku mama akiwa kashikwa na butwaa, hasira, na akahisi kama mwili unamuishia nguvu, akaanza kujisikia vibaya...akasimama na kuanza kutoka nje....

NB Haya haya mambo hayo


WAZO LA LEO: Hakuna kitu kinachoumwa kama kusingiziwa uwongo wa nguoni, kusingiziwa imani za kichawi, wizi ...kusingiziwa vitu ambavyo vinagusa hisi za binadamu, ...ndugu zanguni tuwe makini katika kutoa kauli kama hizi,....`wewe mwizi, wewe mchawi, wewe malaya...wewe ni...’ kauli hizi huumiza sana nyoyo za watu ikizingatiwa kuwa kauli hizi nyingine ni uzushi, sio za kweli, hebu fikiria unamwambia mtu kama huyo kuwa yeye ni mwizi, yeye ni malaya, yeye ni muongo, na kumbe hana kabisa tabia hizo, utakwenda kujibu nini mbele ya muumba, tuache kabisa kauli hizo...
Ni mimi: emu-three

No comments :