Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, October 16, 2014

DUNIA YANGU-49


'Ndio twendeni nikawaonyeshe wapi alipo mwanangu,….ili na mimi nife kwa amani, …’akasema huyo mama.

‘Twende wapi mama,watu wamefika huko wanasema hakuna mahali ambapo mtoto wako aanweza kupatikana, ni wapi mtoto wako yupo, anawezaje kuishi huko makaburini….?’ akaulizwa.

‘Mnaogopa eeh, nilishawaambia sharti la mtu kufika hapo alipozikwa mtoto wangu ni moja tu….hahaha. mumeanza kuogopa eeh....'akasema akitikisa kicha

'Lakini kwa sasa tuliache hilo, ...... muhimu ni nyie mfike huko mkutane na huyo mnayemtafuta , au sio, na…na ..na tukichelewa, hatutamuona tena, na wote waliopo naye huenda ikawa ndio mwisho wao wa kuonekana hapa duniani…..twendeni haraka…..’akasema.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, tunahitaji kibali chako, mahakama hii ihamie huko makaburini ili tuone ukweli wa hili tukio…..’akasema muendesha mashitaka, lakini watetezi wa hiyo kesi, wakakataa hilo ombi, na kusema hayo ni mambo ya kishirikina, hakuna mtu anayeweza kuishi makaburini na huyo mama kacjhanganyikiwa hajui anachokiongea…

Hakimu akatulia kwa muda na baadaye akauliza;

‘Je askari waliokwenda huko wanasema nini?’ akauliza

Akafika Moto na kuteta na muendesha mashitaka, na waakti wanateta yula mama akasema kwa hasira;

‘Twendeni mbona mnachelewa,msije mkanifanya nife kifo kibaya,twendeni ili nife kwa amani, twendeni haraka, mume wangu huyoo, anakuja kunichukua, twende askari wangu kabla muda haujaisha….’akasema na kugeuka huku na kule akasema;


‘Askari wangu yupo wapi jamani,....nataka  mimi mwenyewe nitangulie mbele, kama nyie mnaogopa, mwaogopa kufa nyie eeh, ….'akasema huku askari wake akimuendesha kutoa nje ya mahakama.


Haya tuendelee na kisa chetu....

************

Kutokana na unyeti wa kesi yenyewe, watu walizuiwa kuongozana na msafara uliokuwa ukielekea huko makaburini, hata hakimu mwenyewe ilimchukua  muda sana kukubaliana na shauri hilo, la kuhamishia mahakama makaburini, lakini  baadaye akasema;

‘Natumai waendesha mashitaka  mnajua dhima mnayoibeba,  hatutakubali kupoteza muda wetu bure, na muwe na uhakika kuwa kweli huko tunapokwenda tutamuona huyo mtoto wa huyu mama…na kweli mna uhakika kuwa mama huyu ana akili timamu kama mlivyosema...sitaki kuwakumbusha kuhusu sheria, kuwa mtoa ushahidi ni lazima awe na akili timamu....’akasema Muheshimiwa hakimu.

‘Muheshimiwa hakimu, pamoja na utu uzima wa huyu mama, pamoja na kuchanganyikiwa kwake, lakini sio wakati wote anakuwa kachanganyikiwa, na haya anayoyaongea kwasasa yana ukweli muheshimiwa...'akasema kutulia kidogo.

'Ndugu muheshimiwa hakimu sisi tuna imani kubwa sana kuwa huyu mama alichosema kinaweza kutufikisha mwisho wa kundi hili haramu….’akasema muendesha mashitaka, na watetezi wakasimama kuipinga hoja hiyo wakisema;

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, sisi bado hatujakubaliana na maamuzi ya waendesha mashitaka, kwa vile huyo mama kisheria anafahamika kuwa ni mgonjwa wa akili, na sheria haimlazimshi mwenye matatizo ya akili kutoa ushahidi mahakamani, lakini wenzetu wamamlazimisha huyo mama, lakini pia kiukweli hebu tuliangalia hili jambo kwa makini, itakuwaje mtu aishi makaburini…muheshimiwa hakimu hawa watu wanataka kupoteza muda tu......’watetezi wakahoji.

Muheshimiwa hakimu akageuka kumuangalia muendesha mashitaka, na watetezi wakawa wanaendelea kuongea;

‘Lakini pia muheshimiwa hakimu sheria na taratibu za kimahakama zinaendana na kumbukumbu na ushahidi, hapa tuna kumbukumbu zote zinazoonyesha kuwa huyo mtoto wa huyo mama alifariki na kuzikwa, na stakabadhi zote tunazo, tunahitajia ushahidi gani mwingine, sisi  tunaona ni upotezaji wa muda wanaotaka kuutumia hawa wenzetu….’wakaongea upande wa utetezi na muendesha mashitaka akajibu hoja hiyo kwa kusema;

‘Hizi ni mbinu za hili kundi, yote hayo yalifanyika kiujanja ujanaj, ili mtu huyo aweze kufanya mambo yake bila kupatikana, sisi tuna uhakika na tunachokifanya, kwahiyo tunaona  ni vyema tukaenda huko ili tuhakikishe sote, sioni kwanini kuwe na kigugumizi kwa hilo, labda na nyie mnaogopa kuwa ukweli utajulikana….’wakaambiwa watetezi .

‘Hatuogopi lolote tunachohitajia sisi ni sheria zifuatwe, ndio maana wakati wote tumekuwa tukidai kuhusu sheria zinasemaje tusiwe wa kwanza kuzivunja sheria …hebu tujiulize,je sio kweli kuwa mtu aliye na matatizo ya akili haruhusiwi kutoa ushahidi mahakamani,  je huyo mama hana matatizo hayo, nab ado tunataka kupoteza muda muhimu wa mahakama ...’ wakazidi kujitetea. watetezi.

‘Nani kawaambia nina matatizo ya akili, nyie watoto mnafikia hatua ya kunitukuna mbele ya mahakama yenu, muishie hapo hapo, mimi nina akili zangu timamu, na sitaki muendelee kunitukana, mimi sio mwenzawazimu, uwendawazimu huo wamekuwa wakiniletea hawa watu kwa kundunga madawa yao ya ulevi...sasa twendeni huko tuone ni nani mwendawazimu nyie au mimi...’akasema huyo mama.

‘Muheshimiwa hakimu.....’watetezi wakawa hawajakata tamaa,...

Hatimaye muhehimiwa hakimu akaongea na wasaidizi wake, wakakubaliana mahakama ihamishiwe huko kwa muda, na safari ya kuelekea huko mhakamani ikaanza, watu wanaostahili kwenda wakaanza kuingia kwenye magari chini ya ulinzi mkali.

Yule mama akaingia kwenye gari lake na walinzi wake, na Moto akaingia kwenye gari lake, lakini alihisi wasiwasi, hakupenda Yule mama abakia na walinzi wake tu, lakini hakuwa na la kufanya kwa vile mambo yote yalikuwa yanasimamiwa na mahakama.

Moto akiwa ndani ya gari lake tayari kwa safari ya kuelekea huko mahakamani, akaanza kuwasiliana na watu;

‘Mambo yanakwendaje huko?’ akauliza Moto, kuwauliza vijana wake.

‘Mpaka sasa hakuna jipya, …’akaambiwa.

‘Je zile simu za hao watu, bado mnazo?’ akauliza.

‘Ndio mkuu, lakini kuna kitu cha ajabu sana, kwenye hizi simu….’akaambiwa

‘Kitu gani cha ajabu…?’ akauliza.

‘Ulituambia tuzizime na kuhakikisha hazifanyi kazi, lakini tunaona kuna kitaa kidogo kwenye hizi simu, hakizimi kabisa…’akasema.

‘Hakikisha kuwa mumezizima kabisa, toeni mpaka betrii yake…’akasema moto.

‘Sawa mkuu……’akatulia na baadaye akasema.

‘Tumezizima, na hata kutoa betrii, lakini kuna taaa ndogo inaonekana kuwaka wakati wote….’akasema huyo askari.

‘Hakuna jinsi ya kuizima hiyo taa, kitakuwa kinawaka kwa kutumia nguvu gani, hebu zichunguzeni vyema, Toani betri kabisa, na hakikisha hiyo taa haiwaki kabisa….’akasema Moto, na ilichukua muda na baadaye akasikia mtu wake huyo akiongea.

‘Ni ajabu kabisa, hata baada ya kutoa betrii, lakini bado kitaa hicho  kinawaka nahisi kinatumia solar….’akasema.

‘Ziwekeni ndani ya mfuko wa palasti na mpeni askari mmojawapo azipeleke chumba cha uchunguzi, nina wasiwasi na hizo simu, inaweza ikawa ni chombo cha kunasia matukio…’akaambiwa namoyoni akasema;

‘Inawezekana ikawa ni bomu…lakini sizani’ kukawa na ukimya Fulani baadaye akaambiwa;

‘Tumeshazitoa kwa kijana wetu aziwahishe huko ofisi ya uchunguzi, lakini mtalaamu tuliye naye hapa anasema sio bomu, ila inawezekana kabisa ikawa ni chombo cha kunasia matukio, kwahiyo inavyoonekana muda wote hao watu walikuwa wakituona…’akasema

‘Kama mlikuwa naye kwanini hamkumuuliza mapema?’ akaambiwa

‘Ulituambia tusimuhusishe mtu yoyote mpaka utuambie mkuu, tumefuata amri yako mkuu…’akajitetea huyo askari.

‘Halafu huyu mtaalamu wetu, kasema kwa kutumia hiyo simu,  wanaweza kutambua wapi walipoweka vyombo vyao hivyo vya kunasia hayo matukio, na wameshaanza kufuatilia…’akasema

‘Sawa hilo lifanyike haraka sana, kwani hatuna muda wa kupoteza tena…’akasema Moto.

Ni wakati magari sasa yanaanza kuondoka, na king’ora cha polisi kikaanza kulia ili masafara huo uweze kupita, mara simu ya Inspecta ikaita hakukuwa na namba yoyote kuashiria kuwa mpigaji hakutaka atambulikane, Inspecta akaweka kiwambo cha kunasia sauti, na kuiweka hewani

‘Ni nani mwenzangu?’ akauliza

‘Kwenye hilo gari la huyo mama kuna bomu…msimruhusu mama huyo aingie humo,..fanyeni juhudi..huyo mama akifa nitapambana na nyie, aaaah’ kukawa kimiya, na Inspecta Moto akaamrisha gari lao lisimame,akawa anataka kuwasiliana na mkuu wa msafara,  lakini hata kabla hajamaliza kusema, kukasikika mlio mkubwa mbele yao …..

WAZO LA LEO: Unapotoa kwa nia kusaidia, hakikisha unatoa kile kilicho kizuri, kile unachokipenda wewe mwenyewe na usitoe kwa ria, kwa nia ya kujionyesha kuwa unazo. Hili pia ni pamoja na pale unapofanya jambo kwa nia ya kuwasaidia wenzako iwe jamii  vikundi, au hata kwa mtu mmoja, fanya hivyo kwa nia njema ya kusaidia.

Unajua, wakati mwingine kujitangaza kuwa umesaidia watu au kundi, au mtu,  unakuwa kama unawazalilisha wapokeaji, hujui wanajisikieja moyoni mwao,  japokuwa ni kweli huenda hao watu , au kundi au mtu wanastahili kusaidiwa, swali hapa ni kwanini mpaka tujitangaze, au kuwatangaza wanaosaidiwa….





Ni mimi: emu-three

2 comments :

Anonymous said...

Jamani unatubania unaweka kiduchu sana, hata ivo twashukuru na hongera sana

Anonymous said...

Kwakweli Kisa kinazidi kunoga haswa,nasubiri muendelezo wa kesho,all the best