Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, October 7, 2014

DUNIA YANGU-44


‘Ndugu muheshimiwa hakimu, kutokana na haya yaliyojItokeza tunaomba tuiwakilishe upya kesi hii ya kifo cha mke wa Inspecta, kwani ushahidi uliowakilishwa sasa hivi una uzito mkubwa, na tunaomba tupate muda wa kuupitia vizuri…’akasema mundesha mashitaka.

‘Kwahiyo sasa hivi mnamshitakia nani?’ akaulizwa.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, tunashindwa kuliweka hilo wazi mpaka tuweze kupitia ushahidi wote, na kupitia kila kitu kwa makini, ili kuchelea kurudia rudia tena hii kesi, tuna uhakika sasa hivi tutaweza kuimaliza hii kesi bila kuwepo na manung’uniko…’akasema muendesha mashitaka.

Upande wa utetezi ukaanza kupinga hoja hiyo mpya, na kusema kwa vile kesi ya kwanza imeshaisha, basi kama kuna kesi nyingine iwakilishwe kama kesi nyingine, lakini swala la kuwa mke wa Inspecta alijiua limeshahkumiwa halina kesi tena ya kujibiwa.

‘Kesi inaweza kurudiwa mara nyingi tu, ndio maana kuna kukata rufaa…’wakasema waendesha mashitaka.

Hakimu alisikiliza mabishano ya pande zote mbili bila kuingilia kwa muda, na baadaye akasema;

‘Kwa vile kesi hii ilishafungwa, waendesha mashitaka, wanatakiwa kuwakilisha kesi hiyo nyingine mpya, na natumai sasa hivi hakutakuwa na utata, nataka muelewe kuwa wananchi wanaifuatili akesi hii kwa makini sana, na kwa jinsi mnavyofanya hivi mtasababisha wananchi wasiamini mahakaza zao….’akaongea hakimu kwa muda, na baadaye akafunga kesi hiyo rasmi.

Wakati Inspecta Moto anatoka, waandishi wa habari wananchi mbali mbali wakawa wanamzonga kutaka kujua zaidi kutoka kwake, lakini hakuweza kuongea lolote, na kuingia ndani ya gari alilokuja nalo likiwa na ulinzi wa hali ya juu.

Inspecta Maneno alipotoka hapo alifululiza moja kwa moja hadi Paradise hoteli, kwani alitakiwa kwenda huko kuendelea na uchunguzi kuhusiana na kundi hilo haramu, alipofika alikwenda na kuingia kwenye ofisi moja maalumu.

******

Siku ya kesi ikaanza kwa kishindo, kulikuwa zaidi ya washitakiwa watano pale mbele, wote wakiwa wawekezaji katika hoteli ya Paradise, wakishitakiwa kujihusisha na kundi haramu, na kuendeleza mauji ya raia wasiokuwa na hatia.

‘Kwa pamoja wote wanashitakiwa kwa kesi za kuanzisha kundi haramu, kuendeleza mauaji, na shughuli nyingine, kama za utapeli, unyang’anyi na kunyanyapa watu kwa kutoa mapicha mabaya kwenye mitandao….’kesi ikasomwa.

Kama ilivyotegemewa wote walikana mashitaka, na kwa vile ni watu mashuhuri wenye nyadhifa zao, walikubaliwa dhamana,na ikapangwa siku ya kusikilizwa kesi.

Maneno ambaye alikuwa akihaha huku na kule kutafuta ushahidi alikutana na Moto kwenye ofisi maalumu makao makuu, na aliyeanza kuongea alikuwa Moto.

‘Kwanza hebu sogea huku…..’akamshika mkono na kumvuta kwenye mashine maalumu ya kumchunguza mtu kama ana chombo cha hatari cha kunasia sauti, lakini hakuweza kugundulikana kuwa na chochote.

‘Kwanini unafanya hivyo, …?’ akauliza kwa hasira.

‘Najua ….lakini anyway, hata wakisikia nataka kukupa ukweli wote ili ukae ukijua kuwa wewe unajulikana kuwa ni miongoni mwa kundi hilo haramu…’akaambiwa na Moto.

‘Mimi sikuelewi, hilo la kushutumiwa hivyo lipo na nimeongea na wakuu, nimewaambia yote wanayotaka, ….’akasema.

‘Kama ni hivyo kwanini na wewe hukuwepo kwenye kundi la washitakiwa…?’ akasema kwa hasira.

‘Kwa kosa gani nililolifanya hadi nishitakiwe kama unavyotaka wewe?’ akauliza

‘Wewe hujui kuwa ulikuwa kibaraka wao, hebu niambie huo utajiri ulio nao umeupata wapi kama sio mapesa yao machafu waliyokupa ili uwafanie kazi zao?’ akaulizwa

‘Kumbe ni wivu wa utajiri wangu ndio unakusumbua, kama unataka sema nikuonyeshe njia mimi sina hiana, sasa hivi utabadilika, sasa hivi utakuwa ni tajiri mkubwa, tatizo lako huoni mbali, na hao kama hao, wana yao,na mimi nina yangu, utajiri nilionao hautokani na wao kabisa…’akasema

‘Wewe wataka unifundishe nini mimi, hiyo tabia chafu, au ni zile njia zako za kujiunga na kundi, ili na mimi waniwezeshe au…?’ akaulizwa.

‘Hayo ni ya kwako, na ukiendelea kunisakama kwa shutuma zisio na ushahidi nitakuchukulia hatua …’akasema.

‘Ndio nataka ufanye hivyo…’akasema Moto.

‘Wewe umehangaika kutafuta kila mbinu za kuniharibia jina langu umeshindwa iliyobaki ni kuongea ovyo, hilo halitakusaidia kitu, kumbuka tulipotoka, kumbuka nilivyokusaidia hadi kesi dhidi yako ikafutwa ndio fadhila zako hizo?’ akauliza.

‘Hujanisaidia lolote, ulichokitaka wewe ni kuharibu ushahidi tu, uonekana upo na kazi yako, ili uweze kutoa taarifa kwa watu wako, nakufahamu sana, ila bado nataka nijue ukweli, kuhusu mauaji ya mke wangu, wewe utakuwa ulihusika, hilo bado nalifanyia kazi….’akasema.

‘Endelea mimi sijakukataza, hiyo ni haki yako kutafuta ukweli na ukitaka msaada wangu mimi nipo tayari…’akasema.

‘Unisaidie au unichote mawazo yangu, ili ujue ni jambo gani ninalolifanya….’akaambiwa

‘Kama hutaniamini mimi, ujue hutafanikiwa, hujui jinsi gani ninavyothamini urafiki wetu…nilihangaika sana kukuteta, lakini najua hutaweza kuniamini mpaka hapo utakapofikia mwisho wa upelelezi wako…’akasema

‘Hebu niambie jana ulipotoka mahakamani ulikwenda wapi?’ akamuuliza

‘Nilikwenda kufanya uchunguzi wangu kuhusu kundi hilo haramu linalodaiwa kuwepo…’akasema.

‘Wewe ulipofika Paradise uliongea na nani?’ akaulizwa.

‘Na watu mbali mbali….’akasema.

‘Habe sikiliza maongezi yako na hao watu wako….’akaambiwa na Inspecta Moto akatoa simu yake na kuweka hewani, na maongezi yake aliyoyafanya siku hiyo yakasikika;

***

 ‘Naona kesi ya kifo cha mke wa Inspecta imefufuliwa upya na sasa hivi yaonekana wana ushahidi wa kutosha…’akasema Maneno.

‘Tunafahamu yote hayo, kwahiyo wewe unataka nini kwetu?’ akaulizwa.

‘Kama mlivyoniahidi, nimekuja kwenu kwa kutaka msaada..’akasema.

‘Msaada gani unaohitajia kutoka kwetu?’ akaulizwa.

‘Msaada wa kipesa, maana inabidi kuongea na watu mbali mbali,ili kuweza kupata ushahidi wa kutosha…’akasema.

‘Hilo halina shida,…na wala haikuwa ni kazi yako, ukumbuke kuwa wewe umeshavunja mkataba na sisi, ulitakiwa sasa hivi uwe kaburini, tumekustahi tu tuone jinsi gani utakavyoosha mikono yako, na tumerizika na utendaji wako, tunaangalia jinsi gani ya kukusaidia,na ikibidi kumalizana na wewe kabisa….’akaambiwa.

‘Kwahiyo sasa hivi nifanye nini?’ akauliza kwa hamasa, lakini kichwani akawa anajiuliza hawa watu wana maana gani kusema; `ikibidi kumalizana nay eye kabisa’.

‘Endelea na shughuli zako kama kawaida, usibabaike, inapofikia sehemu ya hatari wewe tuambie tutajua nini la kufanya, japokuwa tunakuona kwa kila unachokifanya...’akaambiwa.

‘Je ushahidi huo mpya ulioletwa mahakamani mna taarifa nao, ?’ akauliza

‘Sisi hatuoni kama una lolote jipya, kwa vyovyote iwavyo tumeshajiandaa, tunajua ni nini cha kufanya, ujue kabisa kama itabidi, ….hasa tukiona unaweza kuingiza kundi kwenye matatizo, hatuna budi kuagana na wewe,…’akaambiwa

‘Una maana gani kusema hivyo?’ akauliza

‘Hilo lipo wazi, ndio maana tulishakuambia uwe makini, na kosa dogo ullolifanya, japokuwa tumeshalisahihisha, limeweza kuingiza kundi kwenye matatizo makubwa, sisi kama wanachama tunahitajia kuliangalia hilo kwa macho mawili, na sheria zetu zipo wazi, najua ulishazielewa vyema..au unataka tukusomee tena upya…’akaambiwa

‘Lakini mkisema hivyo, mimi nina kosa gani, maana yote nilifanya kama kundi lilivyotaka, au sio, sasa nitawajibikaje wakati hayo yaliyotokea ni maagizo ya kundi, mimi nilikuwa ni msimamizi tu…’akajitetea.

‘Swali ni je wewe ulifanya kama ilivyotakiwa ufanye, au ulifanya hivyo  huku ukimlinda rafiki yako, ukilianda masilahi yako, sisi sio watoto wadogo, sisi tuna akili yako mara mbili, tunakufahamu vyema kabisa...’akaambiwa

‘Nilifanya hivyo ili ionekane kuwa namlinda huyo anayeitwa rafiki yangu kumbe natafuta njia ya kumnasa hivi nyie hamlioni hilo…’akasema

*********

Inspecta Moto akazima simu yake na kumuangalia mwenzake usoni, akamuuliza

‘Hebu niambie ni kwanini usikamatwe kwa kushirikiana na hilo kundi haramu, hebu niambie ni kwanini nikuamini, kwanini usikamatwe kama muuaji wa mke wangu….?’ Akamuuliza kwa hasira.

‘Huo sio ushahidi wa kunifunga mimi, na hata hivyo, huoni kuwa hizo ni mbinu zangu za kupata ukweli, bila kufanya hivyo nitawapataje hao watu, hauoni kuwa sasa wote waliokuwa wakishukiwa wamekamtwa, …..’akasema

‘Hao waliokamatwa ni viini macho tu, wahusika wenyewe hawajakamatwa hata mmoja…’akaambiwa

‘Ni akina nani hao wahusika, kama unawafahamu kwanini usiwataje wakakamatwa…?’ akauliza Maneno

‘Mmojawapo ni wewe, na wengine wengi, ambao wamechukuliwa kutokana na taaluma zako….najua jamaa zako wanakusikiliza, ila nataka wajue kuwa mimi nawafahamu wote,….waambie hao mabwana zako…’akasema na Maneno akamuangalia rafiki yake kwa muda bila kusema neno, halafu akasimama na kusema

‘Nimekumbuka nina ahadi ya kuonana na mtu muhimu hoteli ya Paradise unaonaje tukaongozana, nataka uhakikishe mwenyewe kuwa mimi sihusiki, nawajibika tu, ukaonane na huyo mtu niliyekuwa nikiongea naye …’akasema

‘Janja yako…’akasema Moto

‘Ndio nafasi peke yake ya kuhakiki shutuma zako, twende au uje kinamna, ili tuyamalize haya..’akasema

‘Wewe endelea na shughuli zako, mimi sishirikiani na wewe, …’akasema Moto

‘Uwe makini na hayo unayoyafanya…wewe ni rafiki yangu , kuna mbinu za kukumaliza kabisa,..usije ukasema sikukuonya,…’akasema

‘Umejuaje hayo kama huhusiki…?’ akamuuliza

‘Dunia hii haina siri, kama ulivyojua ya kwangu ujue nafahamu mengi ya kwako….lakini mwisho wa siku ni ujanja kupata…’akasema na kuinuka kuondoka.
Inspecta Moto akachukua simu yake na kuandika ujumbe wa maneno.

WAZO LA LEO: Katika shughuli za kikazi ni muhimu kuwa na malengo,na mipangilio mizuri ya pamoja yenye maafikiano kwa wahusika wote.Kusiwe na malengo yenye ajenda binafsi kila mtu akiangalia masilahi yake, kwa kufanya hivyo, itakuwa kama mpo katika ya bahari, mpo kwenye mtumbwi mmoja mnatakiwa mfike ng’ambo, ikiwa mtapiga makasia kwa pamoja kwa mpingalio mmoja, safari yenu itakuwa salama, lakini kama kila mtu atapiga makasia kivyake mjue mtumwbi utayumba, na usalama wetu utakuwa hatarini.


Ni mimi: emu-three

No comments :