Inspecta
Maneno alikuwa akiongea na mkuu wake wa kazi, akitoa taarifa ya
safari yao ya kwenda kumuona mama wa huyo anayemiliki hoteli ya Paradise, na
akaanza kuelekezea;
‘Mkuu
yule mama ni kiboko, pamoja na kuchanganyikiwa kwake, lakini mama yule anaonekana ni jasiri
kweli, hutaamini kuwa ni mzee, ana amri, vitisho, ….’akasema.
‘Kwani
imekuwaje, mumepata nini cha kusaidia kujua ukweli wa hilo kundi?’ akaulizwa
‘Yule
mama sizani kama anaweza kutusaidia lolote, yeye kasema kweli mtoto wake amekufa,
na yupo huko kaburini kwake, na tukamuuliza hilo kaburi lipo wapi..’akatulia
‘Kwani
kaburi lake halijulikani lipo wapi?’ akauliza huyo mkuu
‘Kiukweli
hakuna anayefahamu wapi alizikiwa japokuwa kwenye taarifa za dakitari
aliyethibitisha kufa kwa huyo mtu zinaonyesha kweli, huyo mtu alishafariki,
sasa alipofariki alizikiwa wapi, imekuwa ni kitendawili kingine..’akasema
‘Hakuna
ndugu au jamaa yoyote wa familia hiyo anaefahamu, au wawekezaji wake , ina
maana alipokufa hakuna watu waliohudhuria mazishi yake?’ akaulizwa
‘Kwa
taarifa za juu juu tu, wanasema kifo cha mtoto huyo kinahusiana na mambo ya
kishirikina, alipokufa hakuna mtu aliyeruhisiwa kufika kwenye huo msiba,
walikuwepo ni wazee wachache kutoka huko kijijini kwao, na kundi la vijaba
kutoka hko huko kijijini kwao, ambao walikuja na hao wazee kusaidia mazishi, na
kilichoendelea hapo hakuna anayejua…’akasema
‘Lakini
walizikia hapa hapa mjini?’ akaulizwa
‘Ndivyo
inavyoaminika hivyo, …ni jambo lililofanyika kisiri sana, na baadaye wanasema
hao ndio pekee walitakiwa kufanya hivyo, na kaburi lake halitakiwi
kulitembelea, ukitaka kwenda huko kuna msharti yake…..’akasema
‘Masharti
gani?’ akauliza
‘Huyo
mama anasema ni mpaka ufe…’akasema na mkuu huyo akacheka kidogo, na kusema
‘Msilete
mzaha kwenye kazi, ina maana mlishindwa kumshawishi huyo mama kujua wapi kaburi
hilo lipo..mumeogopa hayo masharti, hamuoani kuwa alikuwa akiwaogopesha tu….’akasema
kwa sauti ya ukali.
‘Mama
huyo kachanganyikiwa, hatuwezi kupata msaada wowote kwake,…’akasema Maneno.
‘Tutaliona
hilo baadaye, ni lazima ukweli wote ujulikane, nahisi kuna jambo limejificha hapo,…’akasema
**********
‘Mkuu
mimi naona hilo halitatusaidia sana kuupata ukweli, inabidi tutumie njia
nyingine, na kuhusu hilo kundi, huenda ni wahuni tu walijifanya kuanzisha kitu
kama hicho kikakuzwa na midomo ya watu,…sio uhalisia wake….’akasema
`Cha
muhimu kwa sasa ni kuwa kesi ya mauaji ya mke wa Inspecta Moto , kesho yake
inafikia mwisho wake, na mujibu wa ushahidi ulipelekwa mahakamani ni kuwa rafiki yako hana hatia na huenda kesi
ikafutwa kabisa.
‘Nilishamuambia
kuwa hana hatia, na mimi nitajitahidi kumsaidia kuhakikisha haki inapatikana,
akawa mkaidi, matokea yake ni ndio anapambana na watu wasijulikana, hivi huyu
mtu yupo sawa kweli,…?’ akauliza
‘Hilo
ni swala jingine, cha muhimu ni kuwa kesi dhidi yake haipo tena, ila kuna utata
katika hilo, inavyoelekea ni kuwa kweli mke wake aliuwawa, hata kama sio yeye,
lakini kuna mtu alihusika katika mauji yake, kwahiyo kwasasa kinachotakiwa
kufanyika ni kumtafuta muuaji wake ni nani…?’ akaambiwa
‘Haiwezekani,
ni nani katoa maneno hayo, mimi mwenyewe nimeongoza upelelezi wake na kuhakikisha
kuwa kweli mke huyo alijiua mwenyewe, mnataka nini tena,…mbona mnataka kuharibu
mambo, ina maana mnataka kesi hiyo ifufuliwe upya, wakati tumeshaimaliza?’
akauliza.
‘Kwa
ushahidi mpya uliopatikana mke huyo aliuliwa,..’akaambiwa
‘Ushahidi
mpya, una maana gani kusema ushahidi mpya, na ni nani aliyemuua,…?’ akauliza
‘Inavyooneka
aliyepo nyuma ya hayo yote ni hilo kundi haramu…’akaambiwa
‘Haiwezekani,
ina maana hamuniamini mimi, hamuamini upelelezi wangu nilioufanya?’ akauliza
‘Sio
swala la kukuamini wewe na upelelezi wako, hili ni swala la ushahidi, ambao
inavoonekana kulikuwa na njama za kuufisidi, kama ulivyosema awali, unakumbuka
ulisema mwenyewe awali kuwa kundi hili lina mbinu nyingi, na moja ya mbinu zao
ni kugeuza ushahidi, kugeuza mambo kwa masilahi yao, na kwa vile wana watu wao
kila idara hilo kwao inakuwa ni kazi rahisi tu…’akaambiwa
‘Ni
nani aliongoza upelelezi huo hadi akafikia kupata huo mnaosema ni ushahidi?’
akauliza, na kabla hajajibiwa mara mlango ukafnguliwa kwa kasi;
‘Ni
mimi hapa bwana Maneno….’sauti ikatokea mlangoni na jamaa mwenye midevu akiwa
na mawani makubwa machoni akaingia na kukabiliana uso kwa uso na Maneno.
************
Ni
siku ya mahakama ambapo kesi ya kuhitimisha kesi ya kifo cha mke wa Inspecta ilikuwa
ikisikilizwa, japokuwa kulikuwa na fununu kuwa kesi hiyo inaweza kuanza tena
upya, kutoka na baadhi ya wanafamilia kuja juu na kutoa madai kuwa binti huyo
aliuwawa, na hakujiua mwenyewe, na wao wanataka haki itendeke
Cha
ajabu kilichotokea ni kuwa hakimu aliyekuwa akiendelea na kesi hiyo toka awali
aliamua kujitoa kwasababu ambazo hazikutajwa, na baadaye akawekwa hakimu
mwingine, na huyo hakimu mpya, na siku ya kesi hiyo huyo hakimu mpya akaanza
kuelekezea kesi hiyo ilipofia na kusema hatua iliyofikia ni kwa wahusika kutoa
ushahidi wao kuwa kweli mke huyo alijiua mwenyewe kinyume na ilivyoletwa awali.
Kesi
hii imekuwa na utata mwingi, na sisi kama mahakama, tumeliona hilo ndio maana
hatukukimbilia kutoa hukumu, na kama tulivyowaagiza waendesha mshitaka kuwa
waje na ushahidi unaothibitisha maamuzi yao, tunawahitajia leo watoe ushahidi
wao kamili…’akasema hakimu.
Muendesha
mashitaka akaanza kuelezea na kuanza kutoa vidhibiti mbali mbali vikielezea
tukio zima lilivyokuwa na hadi mke huyo akafikia kujiua.
Upande
uliokuwa unatetea ambao kwasasa umewashangaza wengi kuona unashinikiza kuwa
mshitakiwa afikishwe mbele ya mahakama ili waweze kumtetea na kuhakikisha kuwa
kweli hakuhusika;
‘Inavyoonekana
wote sasa mnamtetea mshitakiwa lakini kwa njia tofauti, …’akasema hakimu
‘Sisi
muheshimiwa hakimu tunachohitajia ni wao wamleta mtu wetu mbele ya mahakama,
maana hatumuoni, na tuna uhakika kashikiliwa na hao waendesha mashitaka kwa nia
ya kuharibu uhalisia…’wakasema watetezi.
‘Kuharibu
uhalisia gani, kama kesi ipo hapa mbele ya mahakama, sheri itaangalia uhalisia
na ukweli wa jambo hilo, hiyo ni kazi ya mahakama sio wewe….’akasema hakimu.
‘Huyu
mtu yupo lakini tumemuhifadhi kwa usalama, …’wakasema waendesha mashitaka
‘Sisi
ndio watetezi wake na ndio tuliobeba dhamana yake, inakuwaje waendesha
mashitaka wageuke kuwa wao ndio watetezi wake, je hii sheria gani muheshimiwa
halimu.?’ wakahoji
‘Kwasababu
nia yenu sio kumtetea mlifanya hivyo kwa masilahi binafsi, na tuna ushahidi
kuwa kuna watu walitaka kumuua, ili kupoteza ushahidi…’wakasema waendesha
mashitaka
‘Shutuma
hiyo ni nzito sana, je waliotaka kumuua ndio hao watetezi wake?’ akauliza
hakimu
‘Hatujasema
ni hao watetezi wake, ila kuna watu ambao walitaka kumuua kwa sumu, je kama wao
ndio watetezi wake mbona hawakuweza kumlinda kwa hilo, na alipotoweka walianya
juhudi gani za kumtafuta, ndio maana tukachukua jukumu hilo la kumlinda hadi
hapo haki itakapopatikana na waliohusika wakafikishwa mbele ya mahakama hii
tukufu…’wakasema
‘Ushahidi
wenu umeishia hapo?’ wakaulizwa na hakimu
‘Ndio
muheshimiwa hakimu, kutokana na ushahidi huo na vielelezo tulivyotoa,
tumejirizisha kuwa kweli mshitakiwa hana hatia, na mke wa Inspecta alijiua
mwenyewe kutokana na msongo wa mawazo kuwa mume wake alikuwa na mahusiano na
mwanamke mwingine, lakini kumbe mume wake alikuwa katika harakati za kufanya
kazi yake…’wakasema
Hakimu akageuka kuteta na wasaidizi, na wakati
wanateta, mara mlango wa kuingia mahakamani kukaonekana kama kuna msogomano,
ilionekana kama kuna watu anataka kuingia na kwa vile nafasi ilikuwa n indigo
kukawa na kusukama, na hakimu akauliza;
‘Kuna
zogo gani linaendelea huko mlangoni?’ akauliza
Na
kabla hajajibiwa mara mtu mmoja mwenye mandevu mengi akaingia na kumsogelea
muendesha mashitaka wakateta, na hakimu akasema
‘Ni
nani wewe unayengilia mahakama yangu bila mpangilio…?’ akauliza
Muendesha
mashitaka akasema;
‘Samahani
muheshimiwa hakimu, huyu aliyeingia sasa hivi ndiye mshitakiwa waliyekuwa
wakimuulizia wenzetu, na kaja rasmi,…’akasema na watu wakawa wanashangaa kwa
kutoa sauti ya mguno
‘Kiutaratibu
anatakiwa kukaa sehemu ya mshitakiwa, na kwa vile maamuzi yameshafikiwa huku
mbele kuwa hana hatia, hatuoni kama kuna haja ya yeye kuja kukaa hapa mbele
tena…kuanzia sasa yeye ni mtu huru , hana hatia…’akasema hakimu
‘Muheshimiwa
hakimu, mimi nimefika kwa lengo moja, kuwa mke wangu hakujiua mwenyewe,
amuuwawa….’akasema huyo mtu mwenye ndevu.
Watu
wakaanza kuguna na kila mmoja akawa anongea lake.
‘Kwanini
unasema kuwa hakujiua mwenyewe wakati ushahidi upo wa kutosha kuwa amejiua
mwenyewe?’ akaulizwa
‘Ushahidi
huo ni wa kutengenezwa,……’akasema
‘Una
uhakika na hilo unalolisema, maana wewe ndiye uliyekuwa ukishukuwa na mauaji
hayo, na wewe ndiye uliyekuwepo hapo siku hiyo, hakuna mtu mwingine aliyewahi kuingia humo kabla , kwa namna hiyo unataka kusema nini, kuwa wewe sasa unakiri kuwa kweli ndio wewe uliyemuua mke wako...?’ akaulizwa
WAZO LA LEO: Hata siku moja
huwezi kufuta haki na ukweli kwa hadaa, kwa kufanya hivyo ni kujenga jamii
isiyo aminiana, na matokeo yake ni
jamii hiyo kuishi maisha ya ujanja ujanja, utapeli ulaghai na rushwa.
Usitegemee amani kuwepo katika jamii ya namna hiyo.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment