Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, September 30, 2014

DUNIA YANGU-39


Akatoka na kwenda barazani, akachukua kiti, maana lile kabati ni refu, akaweka kiti na kusimama juu yake na hapo akaweza kufikia mwisho wa lile kabati na kuanza kuangalia pale juu, looh,....kile kitu hakikuwepo..

‘Nina uhakika niliona kitu hapa juu…ilikuwa kitu kama bahasha ni nani kaichukua...’akasema

Ni hiki unakitafuta mkuu….’akasikia sauti, iliyomshitua hadi kutaka kudondoka kwenye kile kiti. Sauti anayoifahamu, na sauti hiyo ni ya watu wawili, wanaofanana wakiongea, mmojawapo ni yule muuaji wa kundi ambaye akitumwa kwako ujue wewe ni maiti, na wapili… akagwaya….

Na pale alipokuwa kasimama kwenye kiti aliogopa hata kugeuka, akilini akijaribu kuhakiki, kuwa kweli sauti hiyo ni ya mtu anayemfahamu, na kili hapo ilifanya kazi kwa haraka sana, akasema;

‘Wewe ni nani, umetumwa kuniua sio…..’akasema na kwa haraka akaruka hewani na kujiviringisha kisarakasi hewani kutoka kwenye kile kiti na kutua chini tayari kwa mapambano….

Tuendelee na kisa chetu....

*****

Inspecta Maneno alipofika sakafuni akajiviringirika kiaskari, na kwa haraka sana akasimama akiwa kwenye kisimamo cha kurusha teke, lakini alipopepesa macho yake kwa haraka, kuangalia wapi pigo litue, akajikuta yupo peke yake, hakuona mtu, akatuliza kichwa na kutega masikio, hakusikia chochote,..

Alitembea mwendo wa kuvizia akiwa tayari kwa lolote huku bastola ikiwa tayari mkononi, akiwa na bastola, ni kama wapo kumi, ….hadi muda huo alijua kuwa labda adui yupo sehemu kajificha, lakini pale chumbani hakuna sehemu mtu anaweza kujificha.

Humo ni chumba cha kulala, kuna kitanda, kabati kubwa, na meza ya kusomea, na meza nyingine ipo kwa pembeni ikiwa na luninga hakuna sehemu mtu anaweza kujificha kabisa, lakini hata hivyo hakuamini, huyo mtu kama ni yeye, anaweza kutumia kila mbinu, akajificha sehemu isiyofichika,….mmmh.

Haraka akagundua kitu, Mlango ulikuwa wazi, kwahiyo huyo mtu alishatoka kwa haraka…..basi huyo mtu ni mwepesi sana, akawaza hivyo.

Akatoka kuelekea barazani , kwenye chumba cha maongezi akijua huenda huyo mtu yupo hapo anamsubiria sehemu yenye nafasi kwa mapambano,lakini alipofika hapo, akasikia kwa nje ni sauti ya pikipiki ikiondoka kwa kasi..akasonya, na kusema;

‘Huyu mtu atakuwa ni nani…’akatoka nje kwa haraka, lakini pikipiki ilishatoka nje ya geti, na hakumuona huyo mtu , na hata mlinzi alikuwa hayupo,…akaangalia huku na kule, na kusema;

‘Huyu mlinzi kaenda wapi…?’ akajiuliza, lakini hakupata jibu, akajaribu kukumbuka sauti ya huyo mlinzi kama ni yeye aliyeingia humo ndani, lakini sauti ya yule mlinzi haifanani kabisa na hao watu anaowafikiria yeye…kwahiyo atakuwa ni huyu huyo jamaa anayemfikiria yeye…

‘Atakuwa ni ‘Kifo…’akasema kimoyo moyo

‘Kifo’ ni mmoja wa watu kwenye kundi ambaye kazi yake kwenye kundi ni moja tu, kumaliza maisha ya maadui. Akipewa kibali hakosei, na kawaida yake haonekani  ovyo, akionekana kwako ujue ndio kifo chako.

Hata Inspecta alimuona mara moja siku alipotambulishwa kwake, na akaambiwa wazi huyu akija kwako tena ujue ni umauti wako,…

‘Huyu anakuja kwangu tu…..akija kwako ujue anakuja kukumaliza…’akaambiwa.

Lakini walikuwa wakiwasiliana naye kwa simu, na kuweza kuizoea suati yake hasa pale alipokuwa akitakiwa kumuelekeza wapi mtu fulani anayetakiwa kwake au anayetakiwa kumalizwa yupo…

‘Mbona sauti yako inafanana na ya mtu ninayemfahamu…?’ siku alipotambulishwa kwake alimwambia wakat wanaongea.

‘Huenda mtu huyo tuna tabia zinazofanana, lakini sizani kama sauti yangu inafanana na mtu mwingine, mimi najijua kuwa nina sauti ya kivyangu…’akasema

‘Inafanana kabisa na sauti ya rafiki yangu mmoja, ukiongea wewe utafikiri ni yeye anayeongea….’akasema

‘Basi uwe makini na hilo…’akaambiwa, na hakukaa naye sana akaondoka, na ikawa ndio 
mwisho wa kuonana naye uso kwa uso.

Alipokumbuka hayo mazungumzo, akasema;

‘Huyu mtu hakunifuata mimi, kama angenifuata mimi angelishaniua, inawezekana alikuja kuhakikisha kuwa Inpecta Moto hayupo, na kama yupo ammalizie, atakuwa ni yeye tu…’akasema

Na mara akamuona mlinzi akitokea chooni, huku anafunga funga suruwali yake vifungio, na akawa anakuja muelekeo wa getini kwake, na alipokaribia pale aliposimama Inspecta akageuka kuangalia pale lilipokuwapikipiki ambalo kwa muda huo halipo tena.

‘Mbona sielewi, nimesikia pikipiki ikiondoka, nikajua ni wewe umeondoka nalo…?!’akauliza kwa mshangao.

‘Una uhakika hakuna mtu aliyeingia humu, wakati nipo ndani…?’ akauliza Inspecta akimuangalia yule mlinzi akiwa kamkazia macho.

‘Nina uhakika mkuu, na sijakaa sana humo ndani, nimeingia sasa hivi tu, na masikio yangu yalikuwa yanasikia kila kitu…hakuna mtu aliyeingia, nilichosikia sasa hivi ni sauti ya hilo pikipiki likiondoka. …’akasema.

Mlinzi huyu ni mzee wa makamo, aliwekwa hapo kusaidia ulinzi, katika kusaidiana, mwanzoni aliwahi kulitumia jeshi, akastaafu, na wakaona kwa vile bado ana nguvu basi katika kusaidiana awe anakuja kufanya hiyo kazi hapa na pale.

‘Sasa ni nani kachukua pikipiki langu na kuondoka nalo..na huyo mtu anatumia funguo za bandia, au aliwahi kuiba ufunguo wangu na kuchongesha, basi ni mtu anayenifahamu,… siwezi kuelewa, kwa jinsi alivyoweza kuingia, na kuchukua na uharaka wake wa kufanya haya….ooh, atakuwa ni yeye tu…’akasema

‘Ni nani,…ina maana unamfahamu, lakini mbona unanichanganya, mbona sikuona mtu akiingia hapo getini mkuu, nikiwa chooni, kuna tundu pale nachungulia muelekeo wa getini, hakuwahi kuingia mtu na niliposikia pikipiki likiondoka, nikawa sina wasiwasi tena, nikajua ni wewe umeondoka na pikipiki lako…’akasema

‘Umefanya makosa sana kuondoka kwenye lindo lako ukijua hakuna mtu aliyeshika nafasi yako..na uzoefu wako wote leo umeharibu…’akasema Inspecta.

‘Mkuu, hakuna mtu aliyeingia, mimi nina uhakika labda awe kapitia sehemu nyingine, lakini sio kupitia getini…’akasema

‘Angepitia wapi sasa, kuwa aliruka ukuta, haiwezekani, ukuta huu mrafu halafu una nyaya za umeme, …..’akauliza akikagua kwa macho ukuta unaozunguka hiyo nyumba, lakini hakuweza kupata sehemu ambayo mtu angeliweza kuruka na kuingia ndani…

‘Yawezekana aliruka kupitia nyuma,…kule nyuma kuna sehemu ina uwazi kuna nyaya hazikuunganishwa, kwa wenye uzoefu wa kazi za namna hiyo wanaweza kupitia hapo, hata hvyo kwanini afanye hivyo, na kama alifanya hivyo …angelipitaje na kuingia mlangoni mimi nisimuone…’akasema

‘Kwanini wewe uliingia chooni muda gani ….?’akauliza

‘Nimeingia sasa hivi nikijisaidia haja ndogo, hebu fikiria haja ndogo inachukua muda mrefu….’akasema akiangalia saa yake

Inspecta akachukua simu yake na kupiga namba yake ya siri, akasubiri na mara sauti ikawa hewani na akajitambulisha kwa maneno yao, halafu sauti ikauliza

‘Kwanini umenipigia, tulipanga nini na unafanya nini?’ akaulizwa

‘Nauliza ulimtuma `kifo’  kuja kwa Moto…..?’ akauliza

‘Nimetume kuje kwa Moto? Mbona sikuelewi, mbona kazi hiyo nilikupa wewe, kwanini nimtume mtu mwingine au umeshindwa, nimpe kazi huyo jamaa, na ujue sisi tunasubiri utupe taarifa kuhusu huyu mtu wako, siwezi kutuma mtu, hususani Kifo, kama umeshindwa hiyo kazi nitamtuma yeye, lakini kwanza atapitia kwako kwasababu umenisaliti….’akaambiwa

‘Bosi…’akataka kujitetea

‘Uliitwa kwenye kikao maalumu cha watu wenu, hukutoa taarifa ya muito huo, na pili ulizima kinasa matukio unachotakiwa kuwa nacho kila mahali, kwanini ulifanya hivyo, kama sio nia ya kusaliti kundi, unafikiri nitamwambiaje bosi mkuu..?’ akaulizwa

‘Sehemu kama ile huwezi kuingia ni kifaa chochote, utagundulikana tu, ndio maana nilifanya hivyo,….’akasema

‘Hicho kifaa hakiwezi kugundulikana kwa mashine yoyote, nina uhakika na hilo, na sisemi bila ushahidi, nilishawahi kutuma watu wangu wakaingia nacho, na hawakugundulikana kuwa na kifaa kama hicho, kwa hilo usinidanganye…’akasema

‘Bosi ina maana sasa huniamini….?’ Akauliza

‘Kukuamini kwangu ni hapo utakaponiletea kichwa cha Inspecta Moto, na pili nataka huyo inspecta Mpya asalimu amri ….kwa kila njia kama umeshindwa useme, na ukishindwa wewe najua una njama za kutusaliti, na umekiuka masharti tuliokubaliana. Na mimi sioni kwanini 
'Kifo' asikutembelee, ila kwa sasa nimetuma kazi moja, muda wowote atakurudi, akirudi ujue ni mgeni wako..’akaambiwa.

‘Kaenda wapi bosi mimi nina uhakika alikuwa hapa kwa Moto…’akasema

‘Sio yeye..na kwasababu wewe umevua kile kifaa cha ulinzi, hatuwezi kujua ni nani aliyefika huko,na unakumbuka hapo tulishaondoa vifaa vyote vya kuonyesha matukio,kwahiyo imekuwa shida kujua lolote ..’akasema huyo anayeitwa bosi.

‘Ninachotaka kujua ni je Kifo alifika eneo hili?’ akauliza.

‘Atafikaje huko bila kibali changu, atarudi karibuni, na akirudi kazi ya kwanza nitakayompa ni kuhusu nyie wawili, hilo nakuthibitishia, vinginevyo umalizie kazi uliyopewa hasa kuhusu huyo rafiki yako…nakupa nusu saa niskie matokea zikipita utakutana na Kifo…’akaambiwa

‘Bosi nina uhakika ni yeye, sasa kama sio yeye ni nani…’akawa anajiuliza

‘Mimi sijui hilo na sina haja ya kulijua hilo kwasasa, maana halina umuhimu kwakngu, la muhimu kwako , nataka huyo mwenzako apotee , nashindwa kuelewa kwanini ile sumu haikufanya kazi kama ilivyofanya kwa wengine ni nani kagundua jinsi ya kuitoa hiyo sumu mwilini, hakuna dawa inayoweza kuiondoa hiyo sumu, nahisi kuna tatizo,…’akasema

‘Hata mimi bosi nashangaa sana..sielwei maana nilitarajia kusikia mwili wake umeokotwa huko alipoenda kutupwa…..’akasema

‘Naona haikufanyika hivyo, huenda huyo mtu mliyempa hiyo kazi, hakutumia sindano inayostahiki,…sasa basi kama sumu haikufanya kazi, mimi nataka uniletee kichwa cha huyo mtu, au kama huwezi basi nataka kichwa chako…’akasema

‘Bosi, kwasasa haitawezekana…’akasema

‘Ok, kama haitawezekana kwako wewe, nitampa kazi huyo uliyemtaja, …naona nyote wawili kwasasa ni tatizo kwa kundi, hata hivyo kazi mliyohitajiwa kwenye kundi mumeshamaliza, kubakia na nyie ni mzigo tu,…na kwa vile umemuota Kifo kuwa kakujia basi kwanini hiyo ndoto yako sasa isiwe kweli,…kifo atakuja kukutembelea hilo nimelithibitisha rasmi, kazi kwako ….’akasema na simu ikakatika.

‘Oh,….’akaguna, akijua huyo bosi akisema neno ni lazima linatimizwa, ndio sera yake, kwahiyo anatakiwa kujiandaa na umauti wake.

‘Sikubali siwezi kufa hivi hivi…nitafanya atakavyo….’akasema na kuelekea barabarani kutafuta usafiri, akakuta pikipiki ipo barabarani…akamwambia mwenye pikipiki,

‘Nipeleke hapo kituo cha polisi..’akasema

‘Sawa bosi….’akashituka, sauti ni ile ile aliyoisikia kule ndani, akataka kumuangalia yule mtu, lakini yule mtu akawa ameshavaa kofia la waendesha pikipiki, hakumuona sura yake, na kabla hajasema neno, akahisi kitu kikipenya mkono wa kushoto, ….akajua hiyo ndio ile, sindano ya umauti. Kifo keshafanya kazi yake…..

WAZO LA LEO: Dhamira mbaya kwa wenzako, chuki, na husuda ni udhaifu usio na tija. Ukiona mwenzako kaendelea kafanya maendeleo, basi mpe hongera na kwa nia njema unaweza kuomba ushauri kwake ili uwe kama yeye au zaidi.


Lakini wengi wetu tunaishia kujenga chuki, kuona wivu, na hata kuhisi vibaya kwa huyo mtu. Ni kweli , huenda kaupata utajiri huo, au maendeleo hayo kwa njia mbaya, kama una uhakika na hilo, basi chukia matendo hayo, usiyafuate, lakini kama kaupata kihalali, basi ungana naye, pata ushauri kwake, na huenda ukifuata alivyofanya yeye kwa nia njema unaweza kufanikiwa, lakini kamwe usifuate matendo mabaya yenye dhuluma kwa nia ya kupata utajiri, utajiri huo hauna mwisho mwema.

Ni mimi: emu-three

1 comment :

Yasinta Ngonyani said...

Hapa duniana baadhiyetu tunapenda kupata kirahisi . Hatufikirii aliyepata amepataje...wazo la leo ni ujumbe mzuri sana kwa jamii