Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, September 17, 2014

DUNIA YANGU-33


  Usiku inspecta hakuweza kulala kabisa, mawazo, huzuni upweke vikawa vinamuandama,akili ilikuwa ikimuwaza mkewe, na yote yanayoendelea, hakupendezewa kabisa kwa hayo waliyofanya wenzake, ambao wanadai kuwa kweli kuna ushahidi wa kutosha kuwa mke wake alijiua.

Kuna muda alitamani atoke kwenda kwenye ukumbu wa starehe, akapoteze mawazo, lakini aliogopa kuwa akienda huko ni lazima atashawishika kunywa, na alijua udhaifu wake kuwa akinywa na hasira alizo nazo anaweza akafanya kitu kibaya, na hasa kama atabahatika kuwa na silaha, akaona avumilie hovyo hivyo.

Akaelekea kitandani na kujilaza, ilikuwa kama humo kitandani kuna mashetani yamelala humo kwani kila alipojaribu kupitiwa na usingizi, alijikuta akikutana na ndoto zakutisha, mara anaota anatokewa na mkewe, akiwa na sura ya kutisha, mara anaona watu wanataka kumuua, ikawa anapata taabu, mpaka ikafika saa sita usiku sasa kichwa kikawa kinamuuma.

Akawa anajaribu kukumbuka matukio ya mchana ili kupoteza mawazo, na ndipo akakumbuka ujio wa mama mkwe, ambaye alipofika, walipata muda wa kuongea, mama mkwe alikuwa tofauti kabisa na alivyokuwa siku za nyuma.

********

‘Mwanangu nimekuja kwanza kabisa nataka hata kupiga magoti kukuomba msamaha, nisamehe sana mwanangu, maana unajua tena, ….’akasema huku machozi yakimlenga lenga.

‘Mama usijali, …nilijua tu ipo siku utagundua ukweli, kuwa mimi siwezi kumuua mke wangu,…mke wangu nilimpenda sana, licha ya mitihani ya hapa na pale, lakini nisingeliweza kufanya huo unyama…’akasema

‘Yaani hata siamini, lakini kwanini ilifikia hapo, mpaka aamue mwenyewe kujiua, kuna nini kilitokea kati yenu,…na kama ni hayo ya wivu kuwa aliambiwa kuwa una mwanamke mwingine, ndio ifikie hatu ya kujiua…’akasema.

‘Mama mengi yatasemwa, na kwa vile mke wangu hayupo duniani, hataweza hata kujitetea na kujieleza, lakini mimi nina imani kuwa ukweli wa kifo chake bado haujajulikana vyema, sina uhakika wa hilo la kujiua, huenda ndio hivyo,….’akasema.

‘Ndio hivyo mwanangu, nimeonyeshwa ushahidi wote, …jamani inatisha, lakini kwanini akafanya hivyo, mungu amsamehe madhambi yake, …’akatulia, akionekana akisononeka moyoni.

‘Mama, hili jambo, niachieni mimi, nataka nilichunguze mwenyewe kiundani, maana mimi ndiye ninayemfahamu sana mke wangu, japokuwa wewe ni mzazi wake, lakini mimi niliishi naye ukubwani, na nimemsoma na kumjua vyema mke wangu, hilo la kujiua, halijaniingia akilini…’akasema Inspecta.

‘Mwanangu ndio hivyo,… huo ndio ukweli, nimethibitisha, na sina shaka na hilo,…muhimu ni kumuombea mungu tu, kwani hiyo imekuwa ndio sababu ya mwisho wa maisha yake, na kila mmoja ataondoka kwa sababu yake …’akasema na kushika shavu.

‘Na mwanangu nakuomba na wewe utulie umuombee mwenzako mema, aishi pema peponi, na wewe pia utubu dhambi zako, kwasababu yote yalitokea akiwa na dhana kuwa wewe una mwanamke wa nje…’akasema.

‘Lakini mama…’akataka kujitetea.

‘Mimi nafahamu kuwa kutokana na kazi zenu unaweza kujikuta ukiwa na mwanamke, hapa na pale, na cha muhimu kwa kazi zenu ni kujua mipaka ya ndoa yenu..mimi na mume wangu tuliishi hivyo hivyo…’akatulia kidogo na baadaye akasema;

‘Mwanangu siwezi kukuficha kuwa sisi tulivumiliana kihivyo…hapana, kuna kama hayo yalishawahi kutokea kwa mume wangu, unamkuta kabisa akiwa na mwanamke mwingine…unaumia, mnagombana kweli, mnafikishana mpaka kwa wazee, lakini baadaye tunasuluhishwa, na ukikaa na kuja kuchunguza, unagundua kuwa ni kweli kumbe alifanya hivyo katika kutekeleza majukumu yake….’akasema

‘Mama kwa hili la kifo cha mke wangu, kuna mengi yamejificha, nakuomba tu, unielewe hivyo….’akasema lakini mama yake akawa kama hamuelewi, akaendelea kuongea kwa kusema;

‘Kazi zenu hizo zina mtihani mingi, na kiukweli ingelikuwa ni uwezo wangu nisingelipenda mtoto wangu aifanye hiyo kazi yenu, siipendo, siipendi …maana ni sawa na waigizaji, unaona kabisa kuna tendo chafu linafanyika, lakini ni katika kuleta ujumbe, halikadhalika kwenye kazi zenu kuna muda unalazimika kuingia kwenye matendo machafu ili kupata ukweli fulani…..’akasema.

‘Ni kweli wakati mwingine tunakumbana na mitihani kama hiyo, na wakati mwingine mitihani hiyo inaletwa kama mitego tu,..yote hayo ndio yananifanya nishindwe kuamini kifo cha mke wangu kama kweli kilikuwa ni cha kujiua… bado kabisa sijakubaliana na hilo, kama ilivyo kuwa kifo cha muheshimiwa….nahisi, kuna kitu kipo nyuma yake….’akasema Inspecta.

‘Niliwashauri wasikuonyeshe huo ushahidi walionionyesha mimi,….maana utakuumiza sana, japokuwa hata mimi kuna sehemu wamenificha kama mzazi, wakisema ushahidi huo utaniumiza zaidi, lakini huo mchache nilioonyeshwa, na uchunguzi wangu mwenyewe, nimethibistisha kuwa kweli binti yangu alijiua mwenyewe, sitaki kusikia zaidi…’akasema, na kabla inspecta hajasema neno, mama huyo akasema;

‘Na hiz shutuma kuwa kajiua kwa wivu kuwa wewe ulikuwa na mwanamke wa nje, nimeufanyia kazi, nimegundua mengi, na hili nisiwafiche nyie wanaume mnajiendekeza, pamoja na kuwajibika kwenye kazi zenu, wakati mwingine mnatumia visingizo vya kazi, kujinufaisha na tamaa zenu za kimwili, hilo mnalo….’akatulia

‘Mama ni kweli lakini…’akasema,lakini mama akamkatiza na kusema;

‘Ilibidi nifanye hiyo kazi ya kupeleleza mwenyewe, maana hata mimi nilipitia pitia huko, japokuwa nilikuwa mwalimu, na nlipofanya uchunguzi, nimegundua kuwa kweli ulikuwa na mwanamke wa nje…usikane, huo ndio ukweli….’akasema

‘Ama kama ulikuwa naye kwa ajili ya kuwajibika, hilo ni jingine...nilipogundua hilo, sikutaka kujua zaidi, ila mwanangu nakukanya, hata kama nikufuatilia jambo, jitahidi sana kuchunga mipaka ya ndoa yako, usitumie visingizio, utaua wengi bila kupenda, maana hata mimi nilitamani kujiua…’akasema mama.

‘Ni kweli mama,…mnisamehe sana,..ni kweli mama hilo nimeliona, hata hivyo,kama nlivyokuambia hili tukio lina mambo mengi yamejificha,…nahitaji muda wa kutuliza kichwa kuyaangalia haya matukio kwa mapana yake…’akasema.

‘Mwanangu nikushauri jambo, achana na hilo..hata kama utakesha, utalia, utachunguza kupitiliza, binti angu hayupo tena duniani, na hataweza kurejea tena..muhimu ni wewekujipanga upya, jiangalie maisha yako…unasikia, wewe umebakia duniani, li uwajibike, mungu kampenda yeye akapumzike huko mbele ya haki, sasa wajibika ….’akasema.

‘Unajua mwanangu, kuna siku niliongea na marehemu , binti yangu,…maana kuna siku tunakaa kama mtu na rafiki yake, akaniambia jinsi wenzako wanavyojiendeleza, akasema wewe muda mwingi upo katika kazi yako tu,..hutaki hata make na mwenzko mshauriane maisha yenu ya baadaye, ….sikatai kazi ni muhimu, lakini ujue kazi pekee haiwezi kukufanya ukawa na maendeleo….’akasema mama.

‘Mama ni kweli, lakini….’akataka kujitetea lakini mama akaendelea kusema

‘Mimi na baba yako, tuliishi maisha ya dhiki sana, yeye alikuwa kama wewe, kazi na yeye, hasi anafikia kustaafu, bado tu anang’ang’ania kuendelea kufanya kazi, akawa hana mbele wala nyuma, kiinua mgongo alichopewa, hakikuweza kumsaidia lolote, ashukuru mungu kuwa mimi na ualimu wangu, ndio uliotufanya hadi tuweze kusonga mbele, vinginevyo, tungeumbuka….’akasema.

‘Mhh, hongereni sana…’akasema.

‘Sasa nyie wakati wenu huu mna uhuru wa kufanya shughuli nyingine, kipindi chetu hukuruhusiwa kama muajiriwa kujibidisha na ajira nyingine, na kama mna uhuru huo,utumieni vyema kwa kujiendeleza, ongea na mwenzako, inspecta mwenzako ana akili kweli, ya kuona mbali, unajua kanisaidia sana hata mimi, hadi sasa naweza kusema, sina shida, kanipa mawazo, kanionyesha njia….’akasema.

‘Pamoja na uzee wangu huu kumbe ninaweza kufanya jambo, ninaweza kuzalisha, nikawa siwategemei tena watoto,…siku nyingi amekuwa akituelimisha jinsi ya uwezekazaji, kuna walimu wao, wanajua sana kuelimisha watu, tumeanza miradi na sasa tupo mbali,…’akasema.

‘Ina maana mumeanza muda kufanya hayo aliyowaelekeza rafiki yangu?’ akauliza

‘Tatizo lako, wewe ni sawa na mume wangu, muda wote unafikiria kazi, jipange mwanagu wakati ndio huu , huku kazi huku unaangalia maisha yako ya baadaye, usije ukafanya makosa kama ya mume wangu. Mume wangu hadi sasa anaota kazi, japokuwa kastaafu, maongezi yake ni kazi yake ilivyokuwa, angepata nafasi angelifanya nini…yaani yeye na kazi…, kazi, kila jambo,kazi, yaani atakufa akikumbuka kazi, kazi ambayo imeshamtema, keshastaafu, atafanya nini tena na uzee ule..’akasema.

‘Lakini huo ndio uzalendo, kupenda taifa lako na watu wake, uzee sio tija ya kuacha kueleza, na kuelekeza, tukiwatumia wazee kama wao, tunaweza kufanikiwa zaidi,…tatizo ni kuwa watu kama hao hawathaminiki, kwa vile hawajui kuongopa…ukweli, haki na kujitolea kwao, unaonekana kama hadithi za Alinacha…’akasema Inspecta.

‘Hahaha, mwanangu ni kweli, hayo hakuna duniani tena…’akasema mama.

‘Ukiwa mkeli, ukatenda yaliyo haki…, unaonekana kama kuvaa kanzu tu…vitu kama hivyo, havithaminiki tena,…ujanja-ujanja, udhalimu, ufisadi ndio sifa ya siku hizi, ukiwa navyo umesoma sana, utapata kazi, utapata mshahara mkubwa, wewe unaona mbali, ukiwa navyo, wewe unafaa katika mikutano, katika uongozi, …sijui kama kweli dunia itakuwa na amani kwa hali hiyo…’akasema Inspecta.

‘Ndio hivyo mwanangu, bora uwe mjanja, ujiandae kwa maisha yako ya baadaye, maana hakuna atakayeangalia maisha yako na familia yako zaidi ya wewe mwenyewe, hakuna atayekutetea kuwa ulikuwa mfanyakazi bora, hakuna…hilo nakuambia, sifa zaitakwenda kwa yule aliyekuwa mjanja, akajijenga, hata kama ni kwa dhuluma, hata kama ni kwa ufisadi, lakini sasa ana miradi,ana maisha mazuri,…huyo atasifiwa, wewe uliyejifanya mchapakazi, una maisha magumu, unaaibika kwa kutembea na ndala huku na kule ukiomba omba, utazaraulika tu….’akasema.

‘Sawa lakini mimi nina imani kuwa haki , ukweli, ndio msingi wa maisha, na hivyo vingelipewa nafasi, dunia ingelikuwa na amani, kusingelikuwa na vita, watu wangelipendana, dunia inagubikwa na vita kwasababu hakuna haki, wale wanao-onewa, hawana wa kuwatetea,…’akasema Inspecta.

‘Ndio wakati wake huo mwanangu, ….’akasema mama na Inspecta kwa sauti ya taratibu akasema;

‘Mama huo ndio ukweli, ndio maana kunatokea makundi yenye siasa kali, imani kali, makundi haya yanajaribu kutoa hisia zao kwa kupitia maeneo yao yanayowazunguka, wao sio wajinga, wana yao yamewatinga, lakini hawapewi nafasi ya kusikilizwa, …’akasema

‘Ndio hivyo mwanangu na wenzao wajanja, mafisadi, wenye nafasi zao, ambao ndio waligeuza haki kuwa batili, wanatumia mwanya huo huo, wa hayo makundi, kuwekeza fitina, …wanazidi kumwagia mafuta kwa manufaa yao…biashara ya silaha inashamiri, ubeberu unarudi kwa mtindo mwingine umasikini unazidi duniani..hayo yapo, ni wakati wake…’akasema mama.

‘Unaona eeh mama, sasa kwa mtaji huo hebu niambie tutafika wapi…’akasema Inspecta.

‘Mwanagu sasa kwa hali hiyo utafanyaje, inabidi na wewe uangalia muelekeo, maana ukijifanya mcha mungu saana, utaachwa kwenye mataa, ni vyema uwe bega kwa bega na wenzako ili na wewe uende na wakati….ni hilo tu mwanangu, mimi nakushauri, kaa na mwenzako, akuonyeshe njia, yeye ni mjanja, yeye anajua maisha, ….mtumie, utafanikiwa, vinginevyo, naogopa kusema unaweza kuishia kubaya….kwaheri mwanangu, na natumai tumesameheana…’akasema.

‘Mimi mama sina kinyongo na wewe, na nashukuru sana, kuwa umelewa, na umenisamehe na mimi, kwani kama binadamu huwezi kuwa mkamilifu,….nina mapungufu yangu, na ndivyo tunahitajika kuishi hivyo, kukubali ukweli kuwa kila mmoja ana mapungufu yake, na tukikosea, tusameheane, …’akasema.

‘Ni kweli, lakini pia tukosoane tukikosea au sio, tuonyesheane njia tukipotea au sio, na mimi nakushauri umshike mwenzako bega akuonyeshe njia, kabla hujapotea…..’akaambiwa

‘Mama, mimi hayo nayafanyia kazi, kama kuna ukweli, nitafuata njia, lakini kwanza mpaka nijua ukweli, maana njia nyingine ni mtihani, zimejengwa kiujanja-ujanja kwa masilahi ya wajanja, badala ya kwenda pema, unaelekezwa kutumbukia kwenye moto…’akasema Inspecta na mama akindoka, akasema;

‘Acha mawazo hayo, …kumbuka raha na maisha mema unajipa wewe mwenyewe, hakuna wa kukutafutia….kwaheri mwanangu kaa fikiria, jipange….’akaondoka.

**********

Mawazo yake na mama mkwe, yalimfanya atulize kidogo kichwa, lakini mawazo hayo yalipoisha kichwani, akawa bado hajapata usingizi, na alipoona hivyo, kuwa hataweza kulala, akatoka kitandani na kuanza kuzunguka zunguka mle ndani, sijui ni kitu gani kilimuambia achungulia mvungoni,

Akainama na kuangalia mvunguni, aliona boksi ndogo ni kama vile viboksii wanaotumia watu kuwekea pesa za mchezo,akainua godoro, na kukichukua kile kiboksi, mwanzoni alijua ni mkewe aliweka kwa ajili ya kudunduliza pesa zake, maana kalikuwa kazito.na kimefungwa na ufunguo.

‘Sijui ufunguo wake upo wapi…?’ akajiuliza, akatafuta sana bila mafaniko, akasema;

‘Huenda aliuweka mahali ili asihangaike kufungu mara kwa mara, lakni mpaka nijue humu ndani kuna kitu gani…’akasema.

Akajaribu kukafungua ikawa vigumu, akapanga akivunje, lakini akaona kuvunja ni kosa huenda kuna vito vya thamani ambavyo mkewe aliweka, akakichukua na kwenda nacho varandani, akakaa kwenye sofa, akiwazia afanye nini.

‘Hata ni lazima nikifungue….’akasema, sasa akaenda jikoni na kuchukua pisipisi na nyundo, akarudii na kuanza kazi ya kukivunja, ilichukua muda kidogo hadi kikavunjika, na kufunguka.

Mle ndani kulikuwa kweli na baadhi ya vito vya thamani, lakini pia kulikuwa na bahasha mbili, na moja ilikuwa na vitufe vidogo sana kama vile vya kumbukumbu kwenye simu(memory card), lakini ni vile vya hali ya juu, vinaweza kuweka kumbkukmbu nyingi sana, zikiwemo picha za video.

Kabla hajaamua kufanya lolote na vile vidude vya kumbukumbu, akafungua bahasha ya pili, humo kulikuwa na picha, na hizo picha ndizo zilimfanya ashikwe na mshituko, mshtuko, uliomfanya adondoshe hata lile boksi, akawa kama anaangalia kitu cha kutisha.

Ilichukua muda kutuliza kichwa chake, na baadaye akajipa moyo na kusema;

‘Labda ni mapicha ya kubuni, haiwezekani, na kwaninialihifadhi hiyo picha, akainama na kuzichukua zile picha na kuanza kuangalia, kwa makini, picha ya kwanza, ni ...

‘Oh, haiwezekani…ina maana ..hapana…’akasema na kuanza kuangalia nyingine kama mtu anayeangalia kitu kichafu, na mara akakutana na picha nyingine, akaona sura yake, akasita,

‘Ina maana mke wangu alijua….’akasema na kuiangalia ile picha, ni kweli ilikuwa picha yake akiwa na mrembo jembe….

‘Kwanini, naimefikaje hapa, tulikubaliana vipi na hawa watu…’akasema, akachukua simu yake na kuanza kupiga, na ilichukua muda na kupokelewa, ..ilikuwa sauti ya mdada Jembe
‘Wewe vipi mbona unanipigia simu saa mbaya kama hizi…umeniharbia ndoto yangu nzuri, unasemaje…..?’ akauliza

‘Tulikubaliana nini, mbona kuna picha za ule uchafu wako, zimefika kwa mke wangu?’ akauliza.

‘Mbona sikuelewi unaongea nini, subir tutaongea kesho, nitakuja kuziona, maana mimi sizani kama hawa watu wanaweza kukusaliti, ni lazima kulikuwa na jambo,..una uhakika na hilo?’ akauliza.

‘Ahadi mumeanza kuivunja wenyewe, na kitakachofuata msije kunilaumu, nahisi kuna mengi zaidi ya haya, nitahakikisha naisambaratisha hilo kundi, hilo nakuahidi nilishapanga kufuata masharti, lakini kwa hili, …sitavumilia…’akasema.

‘Sikiliza baby, hilo haliwezekani, huenda hiyo ni picha ya kupanga ilitengenezwa kwa ajili ya kumuweka mke wako sawa, kuna watu walikuwa wakimtafuta mke wako labda kwa ajili ya kupata siri zako, labda, kwa ajili ya kufanikiwa jambo, ndio wakaamua kutumia picha yako, lakini haikutakiwa ibakie huko, nahisi kuna jambo…’akasema.

‘Mimi sijui, waambie mabwana zako labda waniue,…labda nife mapema, lakini ni lazima nitafanya kitu ambacho hawataweza kunisahau…’akasema.

‘Sikiliza baby, kuwa na subira, tatizo lako una jaziba za kitoto, nikuambie ukweli, unachotaka kupambana nacho sio kitu kidogo, ni dude, ….kwahiyo uwe makini, nakuonya tena na tena, uwe makini, tuliza kichwa chako, jipange kama unataka kufanya unachotaka kufanya, ila sizani kama utafika kokote…’akasema.

‘Tutaona, ….’akasema na kukata simu.

Akachukua zile picha zote na kuziweka kwenye mtandao kwa kutumia komputa yake yenye uwezo huo, na kila alichokiona chenye umuhimu akakidurufu na kukiweka kwenye mtandao, sasa akajipanga kuangalia vile vidude viwili, ambavyo alitakiwa kuviweka ndani ya komputa yake ili aweze kuvisoma, na kujua ni kitu gani.

Wakati anavichukua ndani ya ile bahasha, akahisi mwili ukimsisimuka, akajua sasa hayupo peke yake. Akajuta kwanini alimruhusu mlinzi kuondoka, mlinzi, aliomba ruhusa akisema ana matatizo ya kifamilia, yeye hakuona kizuizi, maana mwenyewe yupo, na yeye mwenyewe ni askari.

Alipohisi hivyo, kitu kwanza kukifanya ni kuvirudisha vile vidude (memory card) kwenye bahasha, na ile bahasha akairusha juu ya kabati lake la nguo, na halafu akajifanya anaendelea kupekua, akilini, na hisia zake za ziada zilimtuma kuwa kuna mtu, yupo karibu, mlangoni, au dirishani.

Kwa haraka akatupo jicho dirishani, na akashangaa, kuona lipo nusu wazi, hakumbuki kulifungua kabisa, akajiandaa kwa lolote, akajuta kwanini hawajamrudishia bastola yake, humo ndani hakuwa na silaha yoyote ya moto, zaidi ya visu vya kurusha, lakini vipo mbali, pale alipo hakuwa na cha kujitetea, kama ikibidi.

Akaanza kuhesabu , moja mbili , tatu, akasimama, lakini kabla hajafanya jambo, akahisi kitu kikichoma upande wake wa kushoto,…sindani, iliyorushwa kama risasi, ilikuwa imetokea dirishani, hakuweza hata kuigusa, ilifanya kazi mara moja, akahisi giza likitanda usoni….       


WAZO LA LEO: Tukubali kuwa sote wanadamu sio wakamilifu, kuwa kila mtu ana mapungufu yake, akikosea, tukikosea tusameheane, hata hivyo, pia tukubali kukosoana, kurekebishana  kwa amani na hekima ili tufikie malengo yetu, kwa ajili ya maendeleo yetu.

Ni mimi: emu-three

1 comment :

Yasinta Ngonyani said...

Akahisi giza limetanda usoni....sijui hapo kiliendelea nini...nashubiri. Pia wazo la la ni bonge la wazo ambalo wengi katika jamaii wanasahai..Tena ni bora zaidi palepale unapokosea kuomba msamaha...Ahsante