Inspecta
Moto alitolewa nje ya eneo lile la choo, wakapita eneo la chumbani kwake,
akatupa jicho kwa haraka kuona kama kuna chochote anaweza kukipata kama
ushahidi, lakini kwa hali ile ilivyokuwa asingeliweza kufanya lolote, akasema;
‘Hapa
ni nyumbani kwangu nahitaji kupaacha kukiwa salama, nipeni nafasi niweke
mazingira ya nyumba yangu vyema…’akasema.
‘Usiwe
na wasiwasi na hilo, walinzi watakuwepo
muda wote hadi hapo tutakapomaliza kazi yetu ya uchunguzi, tukishamaliza,
utaruhusiwa kufanya upendavyo, hatutaki uvurugike ushahidi wowote, nasikia wewe
ni mjanja sana….’akasema kiongozi wa kile kikosi cha kumkamata.
‘Mimi
ni askari mwenzenu, nafahamu fika kuna mtu kahusika na hili, …..’akasema na
yule inspecta mgeni akasema.
‘Mimi
hilo sijui nimeletwa hapa kuhakikisha utaratibu wa kikazi unarejea mahali pake,
kwan kuna malalamiko mengi ya utendaji wenu usirizisha, na hili limethibitisha
hayo, anayway, usiwe na shaka, hakuna
kitakachoharibika, …nitahakikisha kila kitu kipo salama na ukweli wote
utabainika, huwezi kutudanganya kwa lolote lile, wewe kuanzia sasa upo chini ya
ulinzi, ni vyema ukafuata taratibu ili tusije kulaumiana,…’akasema
‘Ipo
siku utagundua ukweli wa haya,..na nitahakikisha ukweli wote unabainika, hata
kama nitakuwa kifungoni, ….lakini waliyofanya haya yote watajuta…..’akasema
‘Mtoeni
huyu mtu humu ndani, tunataka kumaliza hii kazi haraka iwezekanavyo….’akasema
mkuu huyo.
Inspecta
akatolewa nje ya kile chumba cha choo na bafu, na sasa akapitishwa kwenye chumba
chake cha mapmziko, hapo akamkuta Inspecta Maneno, akiwa kakaa kwenye sofa
kakunja nne huku kainamisha kichwa
chini. Na alipowaona wakitokeza, akasimama…..
‘Mumeshamaliza
….?’ Akauliza
‘Tumemkamata
, lakini inaonekana tumechelewa,…’akasema huyo kiongozi wa huo msafara.
‘Oh,
hili sasa ni tatizo kubwa,…..’akasema, na kumsogelea Moto, akamuangalia kama
anataka kumuambia jambo, lakini hakutoa kauli, akampita na kuingia ndani huko
walipo wenzake kuendelea na shughuli za kiaskari baadaye akatoka na kwenda pale
alipokuwa kashikiliwa Inspecta Moto, akiwa chini ya ulinzi, akamsogelea na kwa
sauti ya chini akasema;
‘Pole
sana rafiki yangu, sijui ni kitu gani kilikufika hadi ukashikwa na hasira kiasi
hicho, imekuwaje, hebu nielezee ili nijue jinsi gani ya kukusaidia, maana hili sasa
ni tatizo zito sana, kuna kila ushahidi kuwa wewe umemuua mke wako…sielewi kwanini
umafikia hatua hiyo, kwanini umefanya hivyo?’ akauliza.
Inspecta
Moto, akainua kichwa na kumuangalia, kilichofuata hapo ni machozi mengi yaliyokuwa
yakimtoka Inspecta Moto…., hakuweza kusema akatulia kimiya.
‘Wewe
ni askari na mwanaume unatakiwa ujikaze, kwasababu huo ndio ubaya wa hasira,
kama askari ulitakiwa ujue madhara ya hayo yote, sasa unaona ulichofanya,hasira
yako itagharimu vibaya sana, hata sijui nitakusaidieje, …..’akasema
Inspecta Moto akawa kimiya tu, na Inspecta Maneno
akauliza;
‘Ok,
sasa je una lolote la kusema ili niweze kukusaidia, maana nataka kuongea na
wenzangu kabla hatujapeleka taarifa kwa wakubwa?’ akauliza.
Inspecta
Moto, aliendelea kuwa kimiya, huku moyo akijitahidi kuvumilia, alijua akianza
kuongea hapo ataongea kauli mbaya, akatulia, lakini baadaye akainua kichwa na
kumuangalia Inspecta Maneno, na safari hii ulikuwa uso ulijaa makunjazi ya
hasira na chuki,…akamuangalia Inspecta Maneno moja kwa moja usoni, wakaangalia
kwa muda.
Inspecta
Maneno, akiwa anasubiri kauli ya Inspecta mwenzake, lakini hakuna kauli
iliyotoka zaidi ya kuangaliwa kwa hasira, hadi Maneno akahisi vibaya, akageuka
kutaka kuondoka, na ndipo akasikia mwenzake akisema;
‘Tutaona, labda mniue kabla, lakini wewe na
dunia yako tutapambana, hilo naahidi…’ ilikuwa kauli ya Inspecta Moto,
iliyomfanya Maneno kugeuka na kumuangalia mwenzake, halafu akajitahidi kutabasamu
na kusema;
‘Mimi
sikuelewi unachokiongea, naona mshituko umekupoteza akili yako, usijali, tutaona
itakavyokuwa…..’akaondoka kwa haraka kukutana na wenzake.
********
Taratibu
za mazishi zikafanyika, baada ya kukamilika taratibu zote za uchunguzi, na
Inspecta Moto, akatolewa jela, kushiriki kwenye hayo mazishi ya mkewe, japokuwa
familia ya mkewe, haikutaka kabisa Inpsceta huyo ashiriki, lakini baada ya
kuombwa sana, wakakubali, na hata kwenye mazishi hayo, hakuna aliyekuja kumpa
pole huyo inspecta, alangaliwa kama muuaji, na baada ya mazishi akasindikizwa
kurudi jela..
Na
siku moja baadaye baba wa mke wake akafika kuongea naye kitu ambacho Inspecta
hakukitarajia,wakaa kwenye chumba kidogo cha maongezi, kama mzazi alionyesha
zile chuki za wazi, akasema;
‘Ina
maana nilikuozesha mtoto wangu uje umfanyie hivyo, haya sasa umemuua, umepata
faida gani, ndio sasa unataka kumuoa huyo malaya wako…’akasema
‘Mzee,
….’akasema.
‘Nisikilize
kwanza, nikuambie niliyoja hapa, aitaki ukaidi wako, ujue hapa naongea kwa
hasra sana, mimi nakuambia hivi, hili halitaishia hapa, kwanza nataka
nihakikishe kitanzi kinapita shingoni mwako, na kama hawatafanya hivyo, mimi
mwenyewe nitalipiza kisasi cha binti yangu….’akasema kwa hasira.
‘Mzee
amini ninayokuambia, mimi sijamu-ua binti yako, sijamuua mke wangu, hilo
nakuambia, kama mzazi ulielewe, yote hayo ni viini macho tu, ni mambo
yaliyotengenezwa, ipo siku utayaamini maneno yangu,..lakini kama huamini, siwezi
kukulaumu, maana yamepangwa yawe hivyo, li muamini hvyo, kwa hivi sasa
ninachoweza kusema mungu yupo pamoja nami…’akasema Inspecta huyo, na maneno
hayo yakamgusa mzee, na huyo mzee akasema;
‘Mara
nyingi hakuna mhalifu anayekubali kosa lake, hasa kosa la mauaji, lakini wewe
ni askari, na ni mtu ambaye nakuamini sana, hadi sasa sijaelewa, ni kitu gani
kilikupata hadi ufikie hatua ya kufanya hivyo, …..sijaamini kama kweli ni wewe
umefanya hivyo, nitachunguza mwenyewe, na kama ni kweli umefanya hivyo,
tutapambana mimi na wewe…’akasema mzee huyo.
‘Baba
niamini mimi, nilifika pale na kukuta mke wangu yupo kwenye beseni la kuogea
keshajiua….sina uhakika kama alijiua mwenyewe au kuna mtu kafanya hivyo. Lakini
ninahisi kuna mtu kafanya hivyo, kama ningelipewa nafasi kwa muda ule
ningeligundua hilo ….ila ninahisi kuna mtu kamuua, na imepangwa makusudi
ionekane , kuwa kajiua au mimi nimemuua…’akasema
‘Inavyoonekana
ni wewe umemuua, ushahidi wote unaonyesha hivyo,…labda itokee vinginevyo, maana
kuna kauli za utata kwa wetu wenu, …sijui wewe kwa kujitetea utasema nini,
sijui ni nani ataukubali utetezi wako,…hebu nambie ilikuwaje, nataka nijue wapi pa kuanzia?’ akauliza mzee
huyo ambaye awali alikuwa askari mpelelezi, aliyefikia hadi hatua za juu za
uongozi na kabla ya kuastaafu kwake.
‘Siku
hiyo kweli nilikuwa hotelini, nikiwa katika mbinu za kupambana na hilo kundi,
na walichofanya ni kunitega ili wapate cha kufanya, wakatafuta kila mbinu, na
mojawapo ni kuhakikisha nalewa, walijua nikilewa, huwa nakuwa na hasira sana,
kwahiyo walipoona nimeshalewa, wakaanza kunikasirisha, kuhusu mke wangu, na
nahisi nilitoa kauli za vitisho, na ndicho walichokitaka kutoka kwangu, na nahisi
waliweka kitu kwenye kinywaji changu , na hii sio mara ya kwanza…..’akasema
‘Ina
maana walishawahi kukufanyia hivyo kabla, na safari bado ukakubali, usiniambie
ulifanya hivyo tena kwa minajili ya kufanya uchunguzi wako, …?’ akaulizwa,
‘Ni
mlolongo mrefu mzee wangu, lakini yote hayo yamefanywa ili niweze kutii matakwa
yao, na hapo hotelini ilikuwa mbinu zaidi ya kunulazimisha nitii matakwa yao
mzee, sikumuua mke wangu, hata kama ningelikuwa na hasira kiasi gani,
nisingeliweza kufanya hivyo….’akasema.
‘Hebu
niambie ni watu gani hao?’ akaulizwa.
‘Inaonekana
ni kundi kubwa, lililojijenga kitaalamu zaidi, sizani kama wewe peke yako
unaweza kupambana nalo, nakuomba usijiingize huko, sitaweza kubeba lawama
nyingine…mzee hilo kundi ni hatari la lina kila utaalamu wa kisasa na wakubwa
wengi wamo humo,…..hata hujui ni nani yupo na nani hayupo…’akasema.
‘Hilo
sitaacha, hadi hapo nione haki imetendeka, na kama wewe wameshakunasa na umeshajiingiza
huko, ujue tutapambana, sasa niambie ukwel, wewe ilikuwaje mpaka ukawa
unatembea na huyo Malaya?’ akauliza
‘Zote
hizo ni mbinu zao za kuninasa, na huyo mwanamke, ametumika kama chambo, ni mtu
wao, katika mbinu zao wapenda sana kuwatumia mabinti warembo, ulevi, madawa ya
kulevya, na kuharibu itikadi njema, na pia wanatumia sana mitandao kujenga
itikadi chafu, ni mbinu za hali ya juuu za kimataifa, ikiwemo pia blackmail…...na
ikishindikana wanakumaliza kinamna ambayo haitaonekana kama umeuwawa, itaonekana
umekufa kwa kifo cha kawaida tu..’akasema
‘Nimeliona
hili kwenye uchunguzi wangu, nimegundua kuwa kuna jambo kubwa sana, nimeshaanza
kukupata, sasa, mimi sitajishirikisha moja moja, sitaki kabisa ijulikane kama nafanya
uchunguzi, najua jinsi gani nitafanya, ila narudia tena, kama umehusika kwa
namna yoyote ile kwa kifo cha mtoto wangu, mimi mwenyewe nitahakikisha
natumbukiza kisu tumboni mwako kama ulivyofanya kwa binti yangu…’akasema.
‘Nakuhakikishia
mzee, sijafanya hivyo, na kama ukipata ushahidi huo, …kama ni kweli,
nitakukabidhi kisu ufanye hivyo utakavyo,..ila kwa sasa ninachoweza kusema mungu
wangu ndiye shahidi kwa kauli yangu hiyo, …’akasema na yule mzee akasimama
akitaka kundoka, Inspecta akasema.
‘Mzee
wangu, hata mimi statulia hadi nimpate aliyefanya hivyo, najua hawatanipa hiyo nafasi,
ila nikitoka hapa sitatulia mpaka niwapate wote waliofanya hivyo,…’akasema
‘Kama
usemayo ni kweli, tupo pamoja…nashangaa mbona kauli yako na ya mwenzako
zinafanana, utafikiri mlipanga kuniambia hivyo, ila mwenzako sijamuambia kuwa
nitafanya uchunguzi wangu, nimemuambia ajitahidi kufanya uchunguzi ili agundue
muuaji wa kweli ni nani kwahiyo akikujia ujue yupo katika kutekeleza ahadi yake….’akasema.
‘Mwenzangu
yupi una maana Inspecta Maneno…sitaki hata kumuuona, na akija sijui kama
kutakuwa na usalama humu ndani, labda wanifunge pingu nikiongea naye, na
nitaongea naye nini, msaliti mkubwa yule…..amesema atakuja kuonana na mimi?’
akauliza.
‘Sina
uhakika hilo la kuja kuonana na wewe, lakini kama ndiye anafanaya uchunguzi ni
lazima akuhoji, au alishafanya hivyo, kiukweli mimi simuamini huyo mtu tena,
…kabadilika kabisa, siku hizi ni tajiri , nashindwa kujua pesa hizo kapatia
wapi, na mtu ukishajikita kwenye utajiri, hasa usio wa halali, ubinadamu
unapotea kabisa,….’akasema.
‘Kwakweli
hata mimi simuelewi, na sijui, kwani sijakaa kumchunguza maana nimekuwa
nikimuamini kama rafiki yangu, sasa kama unavyosema, basi kuna haja ya kuwa
makini naye, maana adui sasa anaweza kuwa hata rafiki wako wa karibu, hata
ndugu, kwa jina la utajiri, sijui sasa katika dunia hii utamuamini nani,…..’akasema
Inspecta.
‘Ndio
maana nimekuambia mimi sitajihusisha moja moja, na kama nitakuja kwako, ujue
nakuja kwa mambo mengine, na nitachomeka mambo yangu kinamna…’akasema na kuanza
kuondoka Inspecta akasema;
‘Na
naomba umwambia mama kuwa hili ni pigo letu sote sijui utamshawishi vipi
akubaliane na hiyo hali, kwani nahisi keshanichukia kiasi kikubwa, najua fitina
zimeshapandikizwa vichwani mwa watu, na kila mtu ananiona kuwa kweli mimi ndio
nimeua,…’akasema
‘Hata
magazeti ya udaku yameandika hivyo, na yametoa picha mbali mbali za ushahidi ,
nyingine zinaonekana ukiwa na akina dada warembo ukistarehe nao, lakini cha
ajabu huyu Malaya wako, hawajamuonyesha sijui ni nani hasa….’akasema mzee
‘Hizo
ni mbinu zao, kuhakikisha kuwa naonekana mbaya, wanatumia hiyo mbinu kuwa
ukitaka kumuua mbwa kwanza umuite huyo mbwa majina mabaya, ili chuki zizidi
moyoni….’akasema
‘Mzee
unajua kabisa moyo ukijazwa chuki, na ubaya ambao kila siku unarudiwa rudiwa
dhidi yako…ni lazima watu watakuchukia, na hata hukumu ikitoka, kila mmoja
ataona n halali yako, ….lakini mimi nina imani haki na ukweli una nguvu,…kwa
vile sijafanya huo ubaya, mungu yupo pamoja nami, …..’akasema Inspecta na yule
mzee akageuka kumuangala, halafu akageuka na kuanza kuondoka kwa hatua ndogo
ndogo, kama vile hatak kuondoka, huku akisema;.
‘Twende
kazini, ila uwe makini huku jela ulipo, na pa uwe makini na watu wako maana
hata sijui ni nani wa kumuamini kwa sasa, ..’akasema
‘Na
wewe uwe makini mzee wangu, usimwambie yoyote hata mama usimwambie lolote kuhusu
utakayoyagundua hadi hapo ushahidi utakapokamilika,….’akasema Inspecta,na mzee
akaondoka sasa kwa hatua za haraka.
Inspecta akabakia pale, akiwa kajiinama, na akijaribu
kutuliza mawazo yake, alitaman apate mahali alale kidogo, ili akili itulie,
akasogea hadi kwenye ukuta akakaa, lakini kabla hajajtuliza, akaja askari mlinzi
na kusema kuwa kuna mgeni wake mwingine kaja
‘Nani
….’akauliza akiwa hana hamu ya kuongea na mtu mwingine tena
‘Inspecta
Maneno….’akaambiwa
NB:
Haya haya, twende pamoja
WAZO LA LEO: Watu wakiwa katika
harakati za kutafuta, hutumia mbinu za kila namna kuhakikisha wanafanikiwa, na
hata inafikia watu kukengeuka, na hata wale waumini au vongozi wa dini
wanadiriki hata kuyageuza maandiko kwa masilahi yao, yote hii ni kutaka
kuchuma, kupambana na hali ngumu, lakini sio hali ngumu tu, bali pia ni kutaka
kujitajirisha,lakini tukumbuke dunia ni mapito tu, na muda wa kuishi ni mchache
tu, siku itafika kila mmoja atarejea kwa mola wake, na hapo hakimu wa kweli
atafanya kazi yake.
Kuchuma
tuchume, lakini liwe chumo la halali, na kila mmoja akifanya hivyo, mbona Baraka
itapatikana tu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment