‘Hahaha...... unamuwazia mkeo sio, hahaha, ungelijua, kuwa mkeo naye yupo anastarehe na wa
kwake,usingelisumbuka hivyo, hahaha….wanaume bwana, mnaiona wajaaaanja, hujui
kuwa unayestarehe naye ni mwanamke, na kama sio wa kwako wa ndoa ujue ni mke wa
mtu au mchumba wa mtu…hahaha, sasa nataka nikuambia ukweli…
Tuendee na kisa chetu
***********
Wakati
hayo yanaendelea huko hotelini, mke wa Inspecta alifika hapo hotelini na shoga yake,
na shoga yake kuonyesha kuwa ni mwenyeji, akatangulia kuingia ndani ya hiyo
hoteli na kusalimiana na walinzi,
Mke
wa Inspecta, alimuangalia mwenzake kwa mshangao, kwa jinsi alivyokuwa
akisalimiana na walinzi, hana wasiwasi, alionekana kama mwenyeji tu, basi yeye
akawa anamfuatlia nyuma nyuma, akionekana mwingi wa mawazo, kuna muda alikuwa
akijawa na hasira, kuna muda alikuwa akiona amefanya hasira kuchukua hatua hiyo.
'Ngoja tukae hapa kidogo tunywe angalau kinywaji, ....'akasema
'Lakini....'akasema mke wa Inspecta kulalamika.
'Hii ni moja ya mbinu zetu, we niachie mimi,najua ni nini tukakifanya tunatakiwa tuonekane tumefika kihoteli, sio kumfuatilia mtu , unaonaeeh, mjini shule shoga...'akasema na wakakaa kidogo wakiagizwa vinywaji vyepesi.
‘Haya
tumefika, hii ndio Paradise Hoteli, unaiona ilivyo,…ulishawahi kufika hapa
kabla?’ akaulizwa na yeye kwanza akatabasamu, halafu akasema kwa mashaka.
‘Nilishawahi,
….’akasema na akasita kuendelea kuongea.
‘Ulishawahi
kufika hapa?’ mwenzake akamuuliza kwa
mshangao, lakini mke wa Inspecta hakusema kitu akatulia kama vile kaongea kitu
ambacho hakutaka kukiongea, na mwenzake akasema;
‘Kama
uliwahi kufika, utakuwa unafahamu jinsi huko ndani kulivyo, au?’ akaulizwa
‘Shoga,
sikuwahi kuingia ndani,…na ilikuwa jioni
jioni hivi inaelekea usiku,…yaani, siku hiyo, ilitokea tu, …’akasema akiona
aibu.
‘Mhh,
basi kumbe na wewe wamo, eeh, au …?’ akataka kusema lakini mwenzake akamkatiza
na kusema;
‘Hebu
acha hayo, sivyo kama unavyofikiria wewe, alinileta rafiki yake mume wangu,
akinionyesha miradi yake,wakai tunapita hapa ndio, akasema tuje kula na kunywa
kidogo, …lakini sikupenda, hata hivyo, kwa vile ni rafiki wa mume wangu,
nikaona sio vibaya, nikamkubalia …’akasema
‘Hamna
shida, huna haja ya kujitetea kihivyo,…’akasema na kumfanya mke wa Inspecta
kujuta moyoni, kwanini kamuambia aliwahi kufika hapo, lakini hakuona tatizo
sana, na siku hiyo hakuwa makini sana kuichunguza hoteli, kwani alifikishwa
hapo kama kushitukizwa tu.
‘Sasa
kama uliwahi kufika ,basi hutakuwa mshamba sana wa hapa, ila kwa huko ndani kuna
sehemu nyingi, kuna sehemu za starehe, kuna sahemu za mikutano, kuna sehemu
maalumu kwa wanachama tu, sasa sijui mume wako atakuwa upande gani, ngoja
nifanye utafiti…’akasema na wote wakawa ndani sehemu ya mapokezi.
‘Wewe
nisubiri hapa, niongee na hawa watu wa mapokezi, ….’akasema na kusimama kuelekea sehemu ile ya mapokezi, akawa anaongea na yule jamaa wa mapokezi kwa muda, halafu akaja pale
aliposimama mke wa mtu, akasema;
‘Ukiwa
mjanja bwana, hakuna kitu kinakushinda, nimetumia ujanja wa mjini, mpaka
nikajua mume wako anaweza kupatikana sehemu gani, japokuwa hapa huwa hawataji
mtu yupo wapi hasa wanachama wa hiyo sehemu maalumu, ..ukiona wanasita
kukuambia mtu wako yupo wapi ujue ni lazima atakuwa mwanachama na yupo sehemu
ya wanachama tu…’akasema
‘Sasa
wewe umejuaje yote hayo, inaonekana wewe ni mwenyeji kwenye hili jengo,…ni
kiukweli, mimi hapa hata sijui niende wapi, maana jengo hili ni, kwa mapana na
kwenda juu, na huku juu tutapandaje…?’akauliza mke wa Inspecta.
‘Unaona
pale kwenye ukuta,pale kuna maelekezo, ofisi zote zilizomo kwenye hili jengo
zimeorodhweshwa pale, kama ni kwenda juu, tunatumia lifti ile pale, unaona pale
watu wanatoka na kuingia, eheee, sasa twende pale, nina uhakika mume wako yupo
sehemu ya hoteli ya watu maalumu, humo wanaingia wanachama tu, kwahiyo kumuona
itakuwa ngumu…tutaona huko mbele…’akasema
‘Kwahiyo?’
akauliza mke wa Inspecta kwa sauti ya kukata tamaa
‘Wewe
twende huko huko juu, mimi nitajua la kufanya…’akasema akitembea kuelekea
kwenye ile lifti, na mke wa Inspecta akamfuata huku akionyesha wasiwasi,
kichwani akijiuliza atajuaje jinsi ya kurudi mwenyewe, kama mwenzake ataamua
kuondoka.
‘Lakini
si umeniambia unatakiwa kuwahi kazini kwako, vipi tena, mimi naona tuishie hapa
tu, sina haja ya kuendelea zaidi, ngoja nirudi nyumbani…?’ akasema, na mwenzake
akamuangalia kwa macho ya kushangaa,na kusema;
‘Unafikiri
kazini kwangu ni mbali basi, sio mbali sana kutoka hapa,… ni hapo jirani tu,
muda ukifika mimi nitaondoka, kama tutakuwa hutujamuona mumeo wako basi wewe utarudi
nyumbani, au…?’akasita akiangalia huku na kule kama kutafuta jambo.
‘Au
nini tena, umeona nini…?’ akauliza mke wa Inspecta.
‘Hao
wanaonekena kutoka huko juu, nilijaribu kuwaagalia , mume wako anaweza kutoka
tusimuona..’akasema akizidi kuwaangalia wale watu, na ujumbe ukaingia kwenye
simu yake akawa anausoma, halafu akasema
‘Naona
muda unakwenda, twende haraka huko juu, kama tutamuona sawa,kama hayupo humo,
basi watakuwa wamechukua chumba…siunajua tena humu kuna kila kitu….’akasema.
‘Wamechukua
chumba, una maana gani?’ akauliza mke wa Inspecta.
‘Wewe
sio mtoto mdogo bwana, hayo ndio maisha ya waume zetu, wewe kaa nyumbani, pika,
subiri, mwenzako akirudi anakuambia nimechoka kweli, hata sijisiki kula, unarizika
tu…kumbe keshamaliza kila kitu huku wanaposema wanakwenda vikaoni…’akasema
‘Mhh,
hayo makubwa, nahisi kama unataka kunichinganisha tu, mume wangu hawezi kufanya
hivyo….unachoongea kinanitia mashaka hata naanza kuogopa…’akasema
‘Wala
usiogope, mwenyewe utajionea, mimi muda wangu ukifika nitaondoka, mengine
utajua wewe mwenyewe, au vinginevyo, tutarudi pale chini, wewe unaweza kuendelea
kumsubiria nitakuonyesha sehemu ambapo wanapitia watu wote, akipita tu unamnasa…’akasema
akiangalia upande wa pili kuna watu walikuwa wakija muelekeo wao.
‘Hapana
huwezi kuniacha huku juu mwenyewe, mimi hata sipaamini, ..’akasema
‘Hahaha
kweli wewe mtoto wa geti kali, unaonekana wa kijijini..jichanganye mwenzangu,
dunia itakuacha njia panda…lakini si umesema rafiki wa mume wako huwa anakutoa out siku moja moja….au’akasema
‘Mhh,
na wewe bwana, sijasema hivyo, usikuze maneno, na hata hivyo mimi nitajichanganyaje
wakati mume hanipi hiyo nafasi, mimi na kazi za nyumbani, san asana ukitoka ni
kwenda sokoni, siku hiyo huyo shemeji alinipitiza hapa tu kunionyesha miradi
yake na tukitoka naye ni kama katumwa na rafiki yake kunipeleka mahali, na sio
kama unavyofikiria wewe…’akasema
‘Sio
kama ninavyofikiria mimi, usijidanganye bwana, dunia hii haina siri, ipo siku
utaona mambo yenu yote yakiwa hadharani, ndipo utasema, wamejuaje..mmh, usijali
mimi ni shiga yao tu, haya tunaongea tu…ila jua hayo hayo sababu kubwa ni
wanaume,umeonaeeh, kama akikufuga ndani ujue ana mtu wake nje…’akasema.
‘Sio
kweli, na sio wote wana tabia hiyo…’akasema.
‘Hahaha,heeya…mmh,
nimecheka utafikiri nipo mitaani kwetu…’akasema akiangalia huku na kule kama
kuna watu wamemsikia.
‘Mara
nyingi mume wangu ni mtu wa kazi, na kazi zake, zinamruhusu kuja sehemu kama
hiii au sehemu yoyote, siwezi sana kumlaumu, ila hicho ulischosema kwa huyo
mwanamke, kinanitia wasiwasi sana…’akasema.
‘Unaonaeeh,
ndio maana wanaume zenu wanawadanganya, anakudanganya kuwa ana kazi nyingi, ana
kikao sijui, vikao vyenyewe siku hizi vinafanyika mahotelini, unajua kwanini…’akamuuliza
akiangalia simu yake.
‘Kwanini?’
akauliza mwenzake
‘Wakimaliza
kikao mambo mengine yanaendelea humo humo, hakuna kutoka kwenda wapi tena, kama
ni kulala, kama ni nini ni humo humo..hahaha, wewe lala nyumbani tu, endelea
kusubiria ukiota ndoto za mume mwema, mume mwema karna hii hakuna…’akasema.
‘Huo
sasa ni ushetani….’akasema.
‘Kwako
wewe ni ushetani, kwa wenzako ni maendeleo, mwenye kitega uchumi anafaidikia
kwa yote hayo…ndio dunia ilivyo, wenzako wanakuwa na dunia zao akilini, wewe
unabakia gizani tu, umelalaaaa, huamuki, ukiamuka umeshazeeka, nani atakutaka
tena..hahahaheyaah…’akasema na kucheka, mwenzake akazidi kujawa na hasira
moyoni.
‘Mimi
sipendi maneno yako, naona unazidi kunichefua….’akasema.
‘Sasa
sikiliza, twende huko huko juu, hapa sio penyewe, kama tukimkosa kabisa wewe
unaweza kurudi nyumbani mwenyewe au sio…’ akawa kama anauliza na mke wa
Inspecta akawa anaangalia huku na kule kuwaangalia wale watu waliokuwa wakitoka
na kuingia kama atamuona mume wake.
‘Mmm,
hapana huwezi kuniacha hapa mwenyewe, kama ukitaka kuondoka, inabidi wewe unitoe
hadi barabarani,….yaani hapa tu nimeshachoka, hata hamu ya kumuona huyo mume
sina tena….’akasema.
‘Unajua
wewe ni rafiki yangu, sipendi haya wanayotufanyia wanaume yaendelee, lakini
nikikuambia kwa mdomo hutaamini ndio maana nikaona uje hapa ujionee mwenyewe
kwa macho yako mwenyewe..unaonaeeh…’akasema akimshika mkono mke wa Inspecta
‘Lakini
mimi naona haya ya kumfuatilia mtu, nikujisumbua maana mtu hujichunga mwenyewe
hasa mnapokuwa kwenye ndoa, na ukiamua kumchunga mwenzako ni kujiumiza mwenyewe
tu, mmi tabia hii siipendi kabisa,…’akasema mke wa Inspecta.
‘Ni
sawa hakuna anayependa hilo, hata mimi sipendi kuvunja ndoa za watu…ila wakati
mwingine ni muhimu kuhakikisha maana unaweza kusema rafiki yangu ana lengo baya
la kuvunja ndoa yangu, hilo ndio silitaki, sipendi umbea
kabisa,…unaonaeeh,…’akasema na yeye akijifanya anaangalia huku na kule
kutafuta.
‘Mimi
naona tunajisumbua bure tu, naona huyu mume wangu hayupo hapa, labda bado yupo
ofisini kwake…’akasema mke wa mtu.
‘Usijali,
..mimi nina uhakika yupo hapa, ngoja kwa sasa nikupeleke huko wanapokaa watu
wanachama tu, ni sehemu maalum sio hapa, mimi nina uhakika ni lazima atakuwa
huko, ..mara nyingi watu kama hao hawawezi kukaa sehemu hii ya kuonekana na
kila mtu, tukifika huko niachie mimi…’akasema.
‘Kwahiyo
sio hapa tena?’ akauliza mke wa Inspecta.
‘Hapa
pia ni sehemu ya hoteli, ni sehemu ya watu kujibuudisha, hata hapa ukiingia
kwenye mlango ule, unaona pale pameandikwa nini, wanachama tu, lakini hapa ni
kwa watu wengine wakunywa na kula na kuondoka, lakini huko ninaposema mimi, ni
zaidi ya hapa..’akasema.
‘Kwa
vipi, huko kuna nini zaidi?’ akauliza
‘Kila
kitu..’akasema.
‘Kila
kitu kwa vipi?’ akauliza.
‘Wewe
usijali utajionea mwenyewe, tutafika sehemu ya mapokezi kama hapa, utaulizwa
utoe kadi, hapo utaniachia mimi, nitajua la kufanya, ..ila tukishindwa kabisa,
kuna namna nitaongea na jamaa analinda usalama, nafahamiana naye, atajua la
kufanya na hapo utaona maajabu ya hii hoteli…’akasema.
‘Aaah,
mimi naona nirudi nyumbani tu…nakusumbua sana rafiki yangu,…’akasema mke wa
Inspecta
‘Yaani
umefika hadi hapa, unataka urudi nyumbani hivi hivi, hapana, usiniangushe
mwanamke wee, mimi nilijua wewe ni mtoto wa mjini kumbe bado mshamba, hivi
utajuaje jinsi dunia inavyokwenda, wewe twende huko juu ukaona mambo, hatutakaa
sana…’akasema na kumshika mkono na mke wa Inspecta ikabidi wakubali na
wakaingia kwenye chombo cha kupandisha juu…
NB
Haya hayapo….mke katoka kijijini kafika mitaani kwetu, anakutana na wanawake wa
mitaani, anachukuliwa kihivyo, mwishowe unakuwa nini…haya tutaona kutatokea
nini huko mbele...
WAZO LA LEO: Uaminifu wa mtu ni
mtu mwenyewe, kila mtu anapofikia umri wa utu uzima, akafikia hadi kuoa, ina
maana ameshafahamu masharti ya ndoa, kwahiyo mienendo yake, na umanifu wake,
hauwezi kupimwa kwa kuchunguzana, kwani kiapo cha ndoa kinatosha kuwa mchunga,
na kiapo cha ndoa huwa kimeshafika kwa mungu, atakayekivunja, anapingana na
mwenyezimungu, na kwahiyo keshatangaza vita na muumba wake. Tuwe waaminifu hasa
wale waliopo kwenye ndoa, kwa masilahi ya vizazi vyetu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment