Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, August 12, 2014

DUNIA YANGU-15

Inspecta akawa na hamasa ya kulichunguza tukio la kifo cha muheshimiwa, na kila hatua akajikuta anakutana na mambo mengi makubwa, na leo akawa amepangilia kwenda hospitali kukutana na docta aliyempima na kumpa dawa marehemu kabla ya kifo chake, na akiwa njiani akawa anamuwaza msaidizi wake ambaye alionekana kupingana.

‘Kwanini Inspecta mwenzangu haniungi mkono kuwa muheshimiwa anaweza kuwa hakufa kifo cha kawaida... ngoja nikikutana naye nitajaribu kuona maoni yake kuhusu haya niliyoyagundua, lhata hivyo kama hatakubaliana na mimi, mimi mwenyewe nitalifuatilia hili jambo hadi nione mwisho wake, akubali asikubali....’ akawa anawaza, na mara akafika kwenye hoteli moja anayopenda kuingia kupata chochote.

Alipofika akakutana na muhudumu mmoja anayependa kuongea naye mara kwa mara, na alimwambia kuna tatizo liliwapaat kuhusu jamaa yao aliyepotea kimiujiza, na mara kwa mara analalamika kuwalaumu polisi kwa hawalifuatilii, na wakati anapata chakula, akamuomba amsimulie ilivyokuwa;

Tuendelee na kisa chetu..

************

‘ Siku hiyo nilikua kwenye zamu ya kuwapokea wateja, na nikiwa nimeshachoka, mara akaingia Msichana mmoja mrembo , alikuwa mrembo kweli, nikavutika naye, lakini kwa hali niliyokuwa nayo msichana kama yule kwangu ni ndoto...ni matawi ya juu, hata hivyo nikajibaragua na kumfuata kwani ilikuwa moja ya majukumu yangu kuwakaribisha kwa siku hiyo.

‘Samahani dada, nikusaidia nini dada yangu mpendwa.....’nikamuuliza na yule dada akanitupia jicho la haraka na kusema;

‘Nataka kukaa kwenye meza ile, kuna mtu namsubiria, akija nitakuambia nina shida gani, unanielewa...’akasema huku akielekea kwenye hiyo meza, na ile meza aliyoionyesha ilishachukuliwa na watu maalumu, walikuwa na kashughuli kao kadogo tu , lakini kwa mrembo kama huyo kumkatalia ikawa ni shida kwangu, nikasema;

‘Nitakutafutia meza nyingine, kuna sehemu nyingine nzuri zaidi ya hapo, unaonaje, maana kama unavyoona ile meza imeshawahiwa ndio maana imepambwa vile...’nikasema

‘Yaani kupamba meza mpaka kuwe na mtu na shughuli maalumu, au..manichekesha kweli..?’ akasema kwa dharau na huku akiendelea kuelekea kwenye ile meza bila kujalia maelezo yangu, sikuwa na jinsi ya kumzuia, lakini nikamfuata na kusema;

‘Ok, tuelewane mpendwa wangu, utakaa kwa muda, natumai huyo mtu wako akifika mtakwenda kukaa kwenye meza nyingine, au sio mpendwa..tutakuandalia kama vile vile ukitaka...unaonaje mpendwa?’ nikamuuliza na yeye akaniangalia kwa macho ya dharau, pamoja na kuniangalia kwa dharau, lakini uzuri wake ulikuwa sio wa kawaida, .....’akasema 

‘Je huyo binti huwa anafika mara kwa mara, au ulishawahi kumuona kabla?’ akauliza Inspecta

‘Hapana ilikuwa mara ya kwanza kumuona,sura hiyo ni ngeni kabisa kwangu...na kama ningeliwahi kumuona kabla ningelishamtafuta na kuongea naye, mimi nawajulia wasichana kama hao, pale alinidharau kwa vile nilikuwa kwenye vazi la kikazi zaidi...’akasema akijikagua

‘Lakini nikitoka hapa huwezi amini kuwa nafanya kazi kwenye hoteli hii, na kama nimetokea kumpenda mrembo kama huyo, ni swala la kumgharamikia tu...nikiamua sishindwi, ila sasa pesa ni shida, nikiwa nazo, nikiamua nampata...unajua ninachofanya ni nini,  nitakodi gari la kifahari kwa siku moja tu inatisha,, nakodi hata nyumba ya maana...nahakikisha siku hiyo anaingia kwenye hilo gari, na akilogwa akiingia kwenye hiyo nyumba ya kukodi, amekwisha, mimi ni mtoto wa mjini bwana...’akasema

‘Endelea na kisa cha jamaa yako ikawaje?’

‘Basi yule msichana alikwenda na kukaa kwenye kiti, kabla ya kufanya hivyo, alipiga simu yake ya mkononi na nilimuona akiongea kwa madaha, nikajua anaongea na huyo mtu wake anayetarajia  kuja kuonana naye, na nilivyoona hivyo nikahisi moyo wa wivu moyoni, unajau ukipenda kitu hata kama sio chako moyo unajawa na wivu ukijua kina mtu mwingine...’akasema jamaa huyo ambaye anapenda sana kusimulia vituko.

Mara nyingi inspecta amekuwa akipata mambo kwa kupitia kwa jamaa huyu, ni muongeaji mchunguzaji na mfuatiliaji wa mambo ya mjini, ukimpatia pesa kidogo, au kinywaji ukamsifia, anaweza kuongea jambo utafikiri yeye alihusika, ..na ukifuatilia utaona ni kweli tupu,...inspecta akiwa na mawazi anakuja kwa huyu jamaa.

‘Baadaye huyo binti akaniita na kuagiza kinywaji na kuanza kunywa huku akicheza na simu yake nahisi alikuwa akiandikiana ujumbe na huyo jamaa yake na mara kwa mara nilimuona akitabasamu nikajua huenda anawasiliana na huyo jamaa yake na mara kwa mara nilimuona akiangalia saa yake ya mkononi, nikajua kweli kuna mtu anamsubiria.

Mara akafika ndugu yangu...ni jamaa yangu wa akribu tu, japokuwa hatukuzaliwa tumbo moja,...ila ni ndugu wa ukoo...na jamaa yangu alipofika kwa vile nilishawasiliana naye na alikuwepo hapo kabla, alijua wapi anastahili kwenda, meza anaifahamu ipo wapi.

‘Kwahiyo akaingia, na kuikaribia ile meza, kwa muda huo nilikuwa upande wa ndani nikimuelekeza mteja mmoja wapi pa kukaa, hata hivyo, kila mara nilitupa jicho kule kuona kinachoendelea, na yule ndugu yangu alipomuona yule binti kakaa kwenye ile meza nilimuona akionyesha kushangaa, na kugeuka kutizama kule nilipo, lakini nilikuwa spo upande ule, hakuniona ila niliweza kusikia wanachoongea;

‘Ulikuwa umbali gani mpaka usikie walichoongea...?’ akaulizwa

‘Sio mbali, kama angeligeuka upenda nilikuwepo angeliniona, lakini ilijua kaguswa na kile kilichonigusa kwa binti huyo, ndio maana hakuhangaika sana kunitafuta...’akasema

‘Niamuona jamaa yangu huyo akimgeukia yule msichana na kusema;

‘Hii meza imeshachukuliwa na watu, ……’akamwambia na yule binti akajifanya kama anasimama na kusema;

‘Usijali, nilikuwa napoteza muda tu, kuna jamaa kaniahidi kuwa atafika, lakini hadi sasa sijamuona, kwani nyie mna tarajia kuitumia kuanzia saa ngapi?’ akauliza huyo binti akirembua yale macho yake, wewe...ndugu yangu kuna watu wameumbika, ...ungemuona mwenyewe ungenisaidikisha ....’akasema.

‘Muda  huu...wewe huoni nimeshafika mwenyewe, kuna watu wangu watafika…muda huu huu, naomba utafute sehemu nyingine,maana tuna mazungumzo nyeti....’akasema na mara muda huo wakaja jamaa wawili mwanamke na mwanaume wakiwa wameshikana tete-atete, siunafahamu huo mtindo, wa kushikana kwa wapendanao, basi wakafika hadi kwenye ile meza, na yule binti akasimama kuwapisha na kuuliza;

‘Ndio hawa?’ akauliza na wale wapendwa wawili walionekana kama kutokujali, kama vile haliwahusu hilo la kuwepo huyo binti asiyealikwa, wao walikuwa wakionyeshana yale yanayosimuliwa kwa wapendanao wa ukweli. Ungewaona ungeliwapa ushindi wa bure, afande kuna watu wanajua kuigiza...huwezi amini..

‘Ndio wenyewe, samahani lakini…ni bora ukatafuta sehemu nyingine sijui huyu jamaa yangu kwanini hakukuambia...’akasema huyo jamaa yangu, na yule binti akageuka huku na kule na kuuliza;

‘Kwani na wewe mwenzako yupo wapi?’ akauliza yule binti,na yule ndugu yangu akamtupia tena jicho yule binti, na safari hii niliona ile tamaa yake machine, akajitahidi kutokuonyesha kumjali yule binti, lakini kwa jinsi nimjuavyo huyo jamaa yangu, kama asingelikuwa na jambo muhimu angelishaanza mambo yake kwa huyo binti, nikasikia akisema;

‘Aaa, mimi sihitaji mwenzangu, kwani mmhi, nina maongezi na hawa watarajiwa tu, ni jamaa zangu, nilisoma nao, kuna jambo muhimu wanataka kulifanya, sasa ni vyema ukaondoka, tutaongea, wapi unakwenda kukaa, nitaka tuonane kama hutojali, maana kukutana hivi hivi tu,...…’akasema na akawa anasita kuendelea kuongea na yule binti akasema;

‘Basi unaonaje wakati namsubiri mwenzangu niwe mwenzako hapa kwa muda kama hutojali, maana kwa hivi sasa nipo peke yangu nah ii hoteli ilivyo, ukikaa peke yako unajisikia mpweke…siounaona palivyo, au...’akasema yule binti

‘Kama huna tatizo hakuna shida, ilimradi ujue kuwa mimi ni mume wa mtu, na ya kuwa hawa wenzangu wana jambo lao, mmh,…’akasema huyo jamaa na kuwageukia wale jamaa na msichana wake kuona kama watapinga, lakini wao wakatikisa kichwa kukubali, huku wakiendelea kupeana yale mambo ya wapendanao...’akasema huku akionyesha vitendo;

‘Nashukuru sana msiwe na wasiwasi kwani hata mimi ni mchumba wa mtu, tatizo ni  kuwa mchumba wangu ana mambo mengi sana, na huenda keshajisahau,…akiendelea hivii mimi nitamuacha kwenye mataa…’akasema na vinywaji vikaagizwa na mazungumo ya watu hao yakaendelea.

Mimi kwa muda huo nilikuwa nimeshafika sehemu yangu ya kukarisbisha wageni,sikuwa na kazi ya kuwahudumia wao, kazi hiyo ilikuwa kwa wahudumu wengine, ila nilivutika kutaka kujua ni kitu gani kinaendelea hasa kwa yule msichana, kwahiyo nikawa nimetega sikio sikutaka hata neno moja linipite.

‘Wakati wale wapendwa wakifanya vitu vyao, vya kutambulishana na kuvalishana pete, hivi na vile na mpiga picha akichukua kumbukumbu hizo, mimi nikawa naangalai ile picha kwa makini, ilinasa kwenue ubingo wangu kila hatua ya lile tukio nalikumbuka, na walipoamaliza ikawa ni mazungumzo tu ya kawaida.

Ikawa ni zamu ya kutambulishana, kwani tangu awali hilo zoezi lilikuwa halijafanyika, wapendwa wale walihamanika na zoezi la kuvishana pete, na mbwembwe za kuonyesha kuwa kweli wanapendana, sasa niliposikia wakisema ni vyema kujuana, na mimi nikawa na hamu ya kumjua yule msichana anaitwa nani na anafanya kazi wapi...lakini halikuwahi kutokea....

‘Labda nianza kujitambulisha mimi mwenyewe, hasa kwako shemeji, nimefurahi sana umemkubalia rafiki yangu kuwa wako mtarajiwa, alishanielezea zaidi kuhusu wewe, na leo akaniomba niwe kama shahidi yake wenye hili tukio,....nimefurahi sana, na natarajia nyie mtakuwa mke na mume mwema, siku hiyo ikifika, na sioni kwanini msilifanye hilo haraka iwezekaanvyo....mnaonaje?’akasema huyo jamaa yangu.

‘Usijali shemeji, kila kitu na wakati wake, hili la leo ni muhimu na nimefurahai kuwa kweli mwenzangu ananipenda kama ninavyompenda mimi, ...na kwa vile limefanyika, tutaona huko mbele itakuwaje...’akasema huyo msichana, na yule msichana mwingine akasema;

‘Lakini shemeji mimi nahisi niliwahi kukuona mahali....’akasema yule msichana akimuuliza jamaa yangu na jamaa yangu akatoa lile tabasamu lake...anajua hayo mambo mimi ni cha mtoto.

‘Hata mimi nilishawahi kukuona mahali fulani?’ akasema yule msichana aliyevishwa pete.

‘Ni kweli, wengi wananifahamu ila mimi siwafahamu, …kutokana na kazi yangu ilivyo…’akasema jamaa yangu kwa kujitutumua, jamaa yangu huyo anapenda sifa, na ukimsifia umemloga, ila kiukweli anachojisifia anacho, anakipaji huwezi amini...’akasema

‘Kwahiyo wewe upo kwenye kampuni gani?’ akauliza yule msichana aliyevikwa pete hapo

‘Nipo kwenye kampuni ya mitandao ya simu za mikononi…’akasema jamaa yangu ni kweli yupo huko na alikuwa jembe lao la ukweli, wanajutia kulikosa, had leo ukienda hapo na kutaja jina lake, wanasikitika sana...’akasema

‘Oh nimeshakukumbuka, nilifika siku moja nikiwa na simu yangu ikiwa na matatizo, wenzako walihangaika sana, lakini ulipofika wewe tu, uliirekebisha kwa dakika moja…’akasema

‘Oh, huo ndio utaalamu wangu,…ni ujuzi ambao naufahamu sana, namshukuru sana mungu, na kampuni yangu inanitegemea sana,…na wengi wananitafuata, lakini siwezi kuondoka hapo , hata siku moja, nina malengo yangu ya kujiendeleza tu hapo hapo nikitoka nina changu, sio kuajiriwa tena, ....’akasema kwa  kutamba.

‘Wanakulipa vizuri lakini?’ akaula yule mwanaume aliyemvika pete mwenzake

‘Mhh,kwa hivi  sasa kwangu inatosha kabisa, sijawa na familia....’akasita kusema ana mke na mtoto, nilijua hilo hawezi kuliongelea, akakatisha hapo na kusema;

‘Mimi kawaida yangu sitaki makuu, nikitaka zaidi kampuni yangu hiyo wanaweza kunilipa lakini sitaki papara, unajua tena ukiwa mtaalamu, huhitaji kujishushia hadhi kwa kuombaomba nyongeza, yenyewe itajipa. Na mimi sina tamaa…’akasema

‘Kwahiyo unafanya hapo ukiwa umerizika kabisa, kwanini usitafute sehemu nyingine, ukapata pesa nyingi, ukasomeshwa,…kuna watu wanakutafuta kwa udi na uvumba?’ akaulizwa

‘Hapana sina tamaa sihitaji kabisa kuondoka hapo kwa sasa...kwanza nikasome nini nischokijua...ni kweli , kuna mfadhili mmoja alinitaka, nikamtolea nje, ....namfahamu sana yule jamaa, ana mambo ambayo sipendezwi nayo, na mimi sitaki maisha ya namna hiyo.....’akasema

‘Kweli, ina maana umepata bahati hiyo ukaitolea nje...?’ akaulizwa

‘Kwani kama ni kusoma kampuni yangu haiwezi kufanya hivyo, ...hapana, sina haja na kwenda popote, Hata hivyo kampuni yangu naipenda nimetoka nayo mbali, na nimeshawaahidi kuwa sitatoka kwa sasa hivi, kwanini nifanye hivyo. Mimi kwa matarajio yangu baadaye nikitaka nitaanzisha kampuni yangu  mwenyewe, na nitaachana na kuajiriwa kabisa.....’kasema

‘Kwani lengo la huyo mtu tajiri aliyekutaka ni nini na kwanini alitaka kukuchukua, mimi naona ni mwema kwako, kwani angelikusomesha zaidi?’ akaulizwa yule msichana ninayemtamani, na yule jamaa yangu akasema;

‘Mhh, huyo jamaa ana malengo mengi,kubwa ni kutaka kuteka soko la mitandao ya simu,na ana mipango mingi tu, mingine ya kibinafasi ambayo hata  huwezi kuyaelewa, anayaelewa ni yeye mwenyewe na ndoto zake, mara kwa mara ananichukua namuelekeza mambo fulani fulani anayoyataka, zaidi , na ni mwepesi kukariri, akiona unafanya jambo, analishika kwa haraka, kiukweli ana kipaji, lakini sio mtu wa aina yangu…’akasema

‘Kama ingelikuwa mimi,ningemkubalia tu,ninaimani atakulipa pesa nyingi sana…mtu kama huyo anachojali ni utendaji, pesa kwake sio tatizo, nimeshasikia sifa zake..’akasema yule mwanaume aliyemvika pete mwenzake.

‘Hutaamini hadi muda huo hakuna aliyewahi kutaja jina lake, japokuwa walikuwa kwenye sehemu ya kutambulishana, kwahiyo pale niliyekuwa namfahamu ni huyo jamaa yangu tu, wengine ni sura tu...’akasema

 ‘Waliendelea kunywa na mara yule jamaa yangu akatoka kidogo, na mimi nikamfuatilia huko alipokwenda kujisaidia nikasalimiana naye nikamuomba samahani kwa kuingiliwa kwenye meza yao na yule binti, lakini jamaa yangu huyo alisema;

‘Oh, ungelijua, ..yaani ndege yule kajileta mwenyewe ...lakini kwa pale inabidi nijiheshimu kidogo, nitahakikisha namchombeza huyo binti mpaka nimjue,kwani umafahamu ...?’akaniuliza na mimi moyoni nilitaka kumwambia hata mimi nimempenda huyo binti, lakini jamaa yangu huyo kwa haraka akaondoka, na kurudi kwa wenzake.

Baadaye nikarudi sehemu yangu ya kupokea wageni na nikawa bado nawaangalia, kuona kinachoendelea, muda mwingi jamaa yangu akawa anaongea na huyo binti, na niliona ile meza imgeuka kuwa ya kila mtu na wake, haikichukua muda,jamaa yangu nikaona kama amelewa kupita kiasi, sio kawaida yake kulewa hivyo, mimi namfahamu sana, wale wenzake walipoona jamaa kazidiwa wakambeba na kuondoka naye……

‘Huyo si jamaa yako wewe hukusaidia na kuhakikisha anafika nyumbani kwake salama...?’ akauliza Inspecta.

‘Mimi sikuwa na wasiwasi nao, nilijua kuwa hao ni wenzake marafiki zake, kwahiyo sikufuatilia sana, nilikuja kumpigia simu baadaye lakini hakuweza kupatikana kabisa...’akasema

‘Ikawaje...?’ akaulizwa

‘Ni ikawa ndio mwisho wa kuonekana kwa huyo jamaa yetu,hadi leo tunamtafuta lakini hatujui kapotelea wapi,….tulitoa taarifa polisi, na wao wakasema watachunguza lakini hakuna jibu la muafaka, mpaka tumekata tamaa kabisa...’ Akamalizia kuhadithia huyo muhudumu wa hoteli, na Inspecta akamuuliza

‘Je wale jamaa wengine uliwahi kuwaona wakija tena kwenye hii hoteli, hukuwahi kuwaona kabla au baada ya tukio hilo?’ akaulizwa

‘Sijawahi kuwaona, inaonekana kama ni jambo lilipangwa,na hao jamaa walitumwa kwa kazi hiyo, wakijifanya ni wachumba, kumbe walikuwa na lengo moja kumteka huyo jamaa yetu, na wameyeyuka, sijawahi kuwaona tena....’akasema.

‘Kwani hao jamaa hawakuwa wanafahamiana na huyo jamaa yako...mbona yaonekana kama walikuwa wakifahamiana kutokana na maelezo yako?’ akaulizwa

‘Yule mwanaume na jamaa yangu walisoma pamoja sekondari, wakaachana kwenye vyuo, lakini wakaja kukutana kwenye kazi zao za hapa na pale, na huyo jamaa ndio akaja kumuomba huyo jamaa yangu awe shahidi kwenye hilo tendo la kuvishana pete....

'Kiukweli..., ndivyo nijuavyo , zaidi sifahamu jinsi walivyokuja kujuana kiasi hicho,….lakini nahisi waliona njia ya kumpata huyo mwenzao ni kutumia huo ujanja, kama kweli ni ujanja au ni bahati tu imetokea hivyo..sijui kabisa, kazi hiyo tulijua polisi watatusaidia lakini hakuna kitu kilichofanyika, sijui kama wewe unaweza kulifuatilia hilo jambo, ila kama familia tumeshakata tamaa....’akasema

Na mara akaingia dada mmoja akiwa na mwanaume, yule dada alikuwa kavaa mawani, na alipoingia akayavua maar moja na kuyavaa kwa haraka, na huyu muhudumu aliyekuwa akiongea na Inspecta akasema;

‘Ndio yeye......’akasema kwa shauku huku akimkodolea yule mdada, ambaye kwa muda huo alikuwa akiongea na mwenzake, anayeonekana huenda ni rafiki yake wa karibu.

‘Ndio yeye nani...?’ akauliza Inspecta ambaye kwa muda huo alikuwa kavalia kiraia kama askari kanzu, ni kwa wale wanaomfahamu tu wangeliweza kumtambua.

‘Yule msichana niliyekuambia nimevutika naye,...ooh ndio yeye my God,..., lakini sasa ana mtu,ooh, sijui, nifanye nini, na sijui kama anaweza kusaidi akujua alipo ndugu yangu au siku ile ilitokeaje,  ...’akasema huku akizidi kumtolea macho yule binti, na kwa vile walikuwa hatua chache, hawakujua kuwa kuna watu wanawaangalia kwa hamasa hiyo.

Inspecta alimuangalia yule msichana akiongea na jamaa yake, wakafika kwenye meza na kuagiza walichoagiza, wakawa wanakula na kunywa na walipomaliza, haikuchukua muda wakainuka kuondoka, na Inspecta akajiandaa, akageuka kumuambia huyo muhudumu;

‘Basi tutaonana, nitakuja tumalizie kisa chetu....’akasema lakini yule muhudumu hakuwa  makini na inspecta macho na mawazo yake yalikuwa kwa huyo binti, na hata Inspecta alivyoondoka huyo muhudumu hakuwa amefahamu mawazo na akili yake ilikuwa kwa huyo binti.

Inspecta akawaangalia wale jamaa wakiingia kwenye gari, na yeye akachukua pikipiki yake na kuwafuatilia kwa nyuma, aliwafuatilia kwa muda, na alihakikisha hawawezi kumtambua, na hiyo ni moja ya kazi yake, anajua jinsi gani afanye hasa anapomfuatilia mtu kwa lengo maalumu.

Lile gari likafika kwenye kampuni moja, ni ile kampuni kubwa ya Warembo, inayomilikiwa na mdada mmoja, na lile gari lilisimama, na yule binti akateremka, aliteremka peke yake na lile gari likaondoka, na yule binti akaingia kwenye jengo la hiyo kampuni.

Inspecta akahisi huenda huyo binti kaja kujilimbwende, na atatoka, lakini ilichukua masaa mawili hakuona dalili ya huyo dada akitoka , walitoka wanawake kadhaa, lakini huyo mdada anayemtaka yeye hakutokea, baadaye akaona aende kuteta na yule mlinzi wa pale.

‘Mlinzi habari yako....’akasema na kuvua mawani na yule mlinzi akamuona na kumtambua;

‘Oh, ni wewe afande, sikukutambua kabisa, vipi afande kuna mtu wako umemleta hapa nini, maana hapa ni kiboko ya warembo, akina mama wakiingia hapa wakitoka huwezi kuwatambua tena, wanapambwa na kupambika na hata kujibadili sura....’akasema

‘Mhh, ndio kuna mdada mmoja nilikuwa namtafuta kuna dada mmoja alifika na gari jekundu, gari halikuingia, yeye alingia peke yake na nina imani hajatoka, nataka kuongea naye....’akasema

‘Gari jekundu?!,..mmmh, unamuongelea binti mrembo ‘Jemba,..’. hahaha, na wewe afande bwana umeingia anga za huyo binti, utaumia afande...hiyo sio anga yako afande hayo maji marefu...’akasema na kucheka.

‘Hahaha, mimi tena, hakuna mwanamke anayeniweza kuniumiza, unasikia, kwanini wanamuita jembe huyo binti?’ akaulizwa

‘Mmh, afande mambo ya hapa yaache kama yalivyo, maana ukiyachunguza sana unaweza kuumia, huyu binti ni mmoja wa watendaji wakuu wa hii kampuni, kukiwa na jambo la muhimu, wanamtumia huyu binti, na hafanyi makosa hata siku moja, .....’akasema na kuonyesha wasiwasi akiangalia huku na kule kama kuogopa mtu asimsikie.

‘Jambo kama lipi...?’ akauliza Inspecta akiwa ameshavaa mawani yake na alihakikisha hapo aliposimama haonekani, na yule mlinzi akaonyesha wasiwasi sana, na alitaka hata kumwambia huyo afande aondoka, lakini alichelea kusema hivyo, akasema;

‘Afande unajua mimi ni mfanyakazi wa hapa na sitakiwi kutoa siri za kampuni yangu, nimekuambia wewe kwa vile ni afande wangu na umenidhamini sehemu nyingi...lakini kwa hali hii utanifukizisha kazi wenyewe wakijua...’akasema

‘Ndio maana nakuuliza wewe kwa vile nakuamini, na mimi siwezi kukuangusha , siri yako ni yangu, na nitahakikisha na kulinda kwa lolote lile, lakini pia ukumbuke kama kuna tatizo ukaniificha, na mimi nikaja kuligundua utapoteza kazi na nitakufunga....hilo nakuhakikishia maana siwezi kukuuliza jambo lkama halina umuhimu...’akasema

‘Afande kwani huyo binti ana tatizo gani maana mambo yao mengi ni ya starehe, kufurahishana na kuwakomoa wabaya wao, na hawajafanya jambo baya la kuvunja sheria, wanajua ni nini wanachokifanya, hata siku moja sijasikia wameingiliwa na polisi kwa kuvunja sheria, kwani kuna tatizo afande?’ akauliza akionyesha wasiwasi wa wazi.

‘Hapana usiwe na wasiwasi kabisa, mimi nimependezewa na huyo binti, tu, ila usije kumwambia, nitajua jinsi gani ya kumpata na kuongea naye, ila umenitajia jina likanivutia ni kwanini wanamuita jembe, na mara nyingi wanamtumia kwa kazi gani?’ akauliza huyo Inspecta la swali hilo lilimkera sasa huyo mlinzi, lakini akawa hana jinsi akasema;

‘Afande hapa kuna mengi, usione kuna mambo ya urembo, lakini kuna mambo mengine ya chini kwa chini, mimi mwenyewe nilikuja kuligundua lakini sio kiubaya sana, ni kwa wale wanaume wakware, wanaochepuka njia, hapa wana kitengo cha kuwaadhibu watu kama hao, ukiwa na mtu kama huyo unawalipa wao wanajua jinsi gani ya kufanya, kisheria, 
hakuna baya kabisa

‘Hata ukiwa na mtu unamtafuta, mara nyingi wanawalenga wanaume, labda wanamtaka kwa jambo fulani, basi kuna wasichana wanapewa kazi hiyo na mmojawapo ni huyo wanayemuita mrembo jembe....’akasema

‘Anaishi wapi...?’ akaulizwa

‘Masaki, alipangiwa nyumba huko siku nyingi, na sasa hivi nasikia anajenga nyumba yake huko maeneo ya Mbezi, nasikia ana jengo  sio mchezo...’akasema huyo mlinzi

‘Na yule aliyemleta ni mchumba wake?’ akaulizwa

‘Mhh, hapana, yule ni mlinzi wake...ukiwaona wapo wawili ujue kuna kazi wanaifuatilia...’akasema na mara kwenye jengo akatokea dada mmoja akiongea na simu, na yule mlinzi akasema;

‘Jembe hilo. ndio huyo keshajibadili mwendo wa kawaida,...huwezi kujua kuwa ni yeye tena, ndiye yule binti aliyeingia muda uliopita ila mimi nawafahamu hata wajibadili vipi...’akasema na Inspecta hakuamini kuwa ni yule dada aliyeingia muda ule.

Huyo dada alikuwa tofauti kabisa kutoka chini hadi juu, hadi sura, sasa hivi anaonekana maji ya kunde kidogo,kichwani nywele za Kiafrika, zaidi, sio kama mzungu alipoingia awali,ila urembo wake ulikuwa pale pale, macho tofauti na yale ya awali,...sasa nyusi sio nyingi kivile....yaani hakufanana kabisa na yule msichana aliyemfutailia...

‘Una uhakika ndio yeye..?’ akauliza afande

‘Hahaha, ni jembe hilo linajigeuza kama kinyonga....ndio yeye’akasema huyo mlinzi akielekea kufungua mlango,kwani kwa nje kulikuwa na gari linataka kuingia.
Mlngo ulipofungulia likaingia gari la njano, na huyo binti, akalifuata pale liliposimama,akaingia kwenye hilo gari, na hilo gari likaondoka taratibu.

Inspecta akawapa dakika mbili , na baadaye akalifuata akiwa anaendesha hiyo pikipiki yake, na aliwasiliana na jamaa, alipofika mbele kidogo, ikaja pikipiki, na Inspecta wakabadilishana pikipiki na huyo jamaa, sasa akawa na pikipiki ndogo ya kawaida, na moyoni akasema;

‘Ni lazima niwe makini na hawa watu......’ huku akiendelea kulifuatilia hilo gari...

JE NI NINI KITAENDELEA...

WAZO LA LEO: Dunia sasa inarejea enzi zile tulizozisoma kwenye maandiko matakatifu,kwani yaliyoandikwa yatajitokeza, kwa njia moja au nyingine, matendo tuliyowahi kuyasoma kuwa ni mabaya hadi kukatokea gharika, maangamizi, ndio hayo hayo yanayotokea hivi sasa, tena kwa kiasi kikubwa kwa ubaya uliokirihisha.

Huu nii wakati mzazi na familia yako mnatakiwa mkae na kuhakikisha malezi bora yanakuwepo, msiige na kufuata yale ambayo hamna uhakika nayo, tuwe makini na vishawishi na mawakala wabaya hasa vyombo vya mawasiliano tv nk, hivi ni vitega uchumi vibaya kama tusipokuwa makini.

Pia kuna ndugu na jamaa wanaotutembelea majumbani, tuwe makini nao hasa kwenye malazi, tusipende kuwachanganya watoto wetu na watu baki, ambao pia wanaweza kuwa ndugu, lakini hatujui nyoyo zao zina nini, wanaweza wakawa miongoni mwa mawakala hatari. Dunia imeharibika, na wanaoiharibu ni walimwengu. Kosa dogo kwa watoto wako ndio umemuharibia maisha yake ya baadaye.


Hebu jiulizeni kuna haki gani ya kibinadamu ya kutetea mambo yanayokwenda na kinyume na maumbile ya kibinadamu, kama huo sio ushetani, tuweni makini na hawa wanajiona ni watawala wa dunia, hao tunaoona ni matajiri, tutaangamia, na tutaingamiza dunia kwa maasi yetu wenyewe.

Ni mimi: emu-three

No comments :