Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, July 11, 2014

DUNIA YANGU-4


 Diamu akiwa pake yake kwenye ofisi yake, na kitabu chake bado kikiwa mezani, alianza kuweka wazo lake kwenye maandishi, hakutaka mtu awe karibu naye kwa muda huo, japokuwa mara kwa mara akiishiwa na kinywaji alikuwa akimuita mrembo wake, hii kwake ni kazi na dawa.

Leo ndio siku muhimu aliyoipanga kuhitimisha wazo lake kimaandishi kabla hajaliweka mezani kwa watu wake, ilikuwa simu muhimu ya kuanza kufungua kitabu chake muhimu, na yeye aliiona hii siku kama yaliyomo kwenye kitabu chake cha wazo la ndoto yake...ni siku pia ya maamuzi ya kile alichokipanga miaka mingi nyuma, alitaka aanze mara moja, bila kumuogopa mtu, hakutaka kabisa ushauri mwingine, kwanza kama kawaida yake akaitisha kinywaji chake akipendacho, na mrembo wake akafika;

Mlango ulifungulia na mrembo huyo akasimama mlangoni kwa pozi analolijua yeye, mrembo huyo alifanya hivyo makusudi, alitaka bosi wake amuangalie kwa makini, alishamfahamu bosi wake anachotaka ni nini, hasa akiingia mlangoni...wanaume wana siri yao... , na kweli bosi akaacha alichokuwa akiandika, akawa anamtizama huyo mrembo, halafu akatabasamu na kusema;

‘Unanifanya nihisi nipo sehemu nyingine, maana macho yanaburudika, hilo vazi la leo, mmh, hongera...nataka na masikio nayo yaburudike, hebu niimbie kidogo...’akasema

Hapo akawa kachokoza, kwani kwa kuimba binti huyu sio haba, kajaliwa sauti, yule binti alianza kuimba kwa sauti nyororo, na bosi akawa kama anafumba macho, akisikiliza sauti hiyo, hadi yule binti akamaliza

‘Mhh, mambo si hayo, masikio nayo yameburudika ....’akasema bosi

‘Ushindwe tu mwenyewe bosi...’akasema huyo mrembo

‘Hahaha, tutakaa baadaye , ila kama nilivyokuambia,nataka uende shule maalumu, kuna mtaalam mmoja, ninamkubali, nataka ukafundwe naye, na huku unasoma masomo ya kiofisi, uive vyema, isionekana kuwa wewe hujui kitu,, ...’akasema

‘Bosi naye bwana, mimi ni kitu gani nisichokijua, ukatibu muhutasi nimeusomea naufahamu vyema, mambo mengine mimi nayafahamu sana, labda mimi nikawe mwalimu wao...’akasema

‘Nataka uwe nitakavyo mimi,...kufundwa huko sio unavyokujua wewe, utaona mwenyewe, kuna mtaalamu mmoja, kanisomesha, na nimeshamuweka kwenye watu wangu, anajua ni nini cha kukufundisha, mwenyewe utaona....kuna mambo ya ukatibu muhutasi ambayo huyafahamu,, kuna mambo ya kila namna utajifunza, pia hata kutumia silaha...’akasema

‘Kutumia silaha!..... hapana mimi naogopa sana silaha, sipendi kabisa bunduki...’akasema

‘Utafundishwa, na hutaiogopa tena, utafundishwa kupigana karate, na mafunzo ya kila namna nataka ukiwa nami nijue nina mtu , sio mti.....Nataka ukiwa karibu yangu uwe kweli mtu wangu, ujue kunilinda kwa hali na mali...’akasema

‘Sawa bosi, mimi nipo kwa ajili yako tu....’akasema huyo mrembo

‘Upo kwa ajili yangu kwa vile unatafuta pesa, hahaha, usinifanye mimi mjinga, nakufahamu sana, mbele ya pesa unaweza kufanya lolote...’akasema

‘Sio hivyo bosi, unajua tulikotoka, wewe na mimi hatutupani,hata kama ungekuwa huna pesa, ningelifanya hivi hivi ...’akasema huku akishika kichwa kuonyesha aibu kwani huo ndio ukweli wenyewe, kinachoangaliwa hapo ni pesa tu.

‘Ni kweli, wewe na mimi hatutatupani, kama ni kufa tutakufa sote, nataka uwe karibu yangu kiukweli,...’akasema Diamu

‘Usikonde bosi, mwenyewe utafurahi....’akasema na kuweka beseni lenye gilasi na kinywaji ,mezani, na akamimina kinywaji na kumnywesha bosi wake, baosi wake akanywa fundo moja, halafu akasema;

‘Inatosha, wewe acha kila kitu hapa mezani, nenda kaendelee na shughuli zako, nitakuita baadaye kwa mazungumzo yetu....’akasema na huyo binti, akatoka kwa madaha akimuacha bosi wake akiendelea kumuangalia

‘Hii ndio nataka...’akasema huyo bosi huku akifunua kurasa kwenye kitabu chake

‘Hii ndio nataka, kazi na dawa, siumizi kichwa,....ni lazima huyu binti nimjenge vyema, atauwa hazina ya mambo yangu, kwanza akasome, akimaliza masomo, atakuwa zaidi ya hivyo,....atakuwa akitembea na dogo dogo wengi pembeni yake, kila mmoja akiwa na kazi yake maalumu, nitakuwa mfalme, anayelindwa na mabinti wazuri....hahahaha...’akasema na kukuna kichwa akiwazia ndoto yake hiyo.

‘Sasa ngoja niliweke wazo langu sawa sawa...’akasema

 ‘Wazo langu ni pana sana, lina mambo mengi, lakini nia kubwa ni kuhakikisha naweza kuitawala dunia kinamna yangu, dunia nitakavyo mimi, sitaki kufungwa na mtu, mara hiki sio sahihi, hiki sitaki hapana, nataka niwe na nafasi ya maamuzi yangu ..niwe na namna ambayo nitaweza kufanya lolote , mahali popote bila kuwa na wasiwasi, au kikwazo,...’akaandika hivyo

‘Hii inawezekana, ukiwa na pesa na akili kama zangu, nahisi wengi wataniona mimi ni mwehu, au labda nimeleweshwa na pesa za urithi, pesa zipo lakini zikae tu, hapana lazima zifanya jambo, na jambo nitakalo mimi nataka liwe la kipekee, nataka uzalishaji wa pesa za mkupuo, nikitaka pesa zinamwagika tu...hahaha, waache wasema ni ndoto za Alinacha

‘Hamna ndoto hapa, siku nikikamilisha hili zoezi, kila mtu atanivulia kofia...’akasema kimoyo moyo

‘Mimi wazo langu ni kuwa nataka niwe na mamlaka ya kila jambo, nataka niwe na dunia yangu, nitakavyo mimi....’hapoa akatulia kidogo akiangalia ile picha ya dunia iliyozungukwa na mikono, akaigusa, na mara ile mikono ikatawanyika, na kila mkono ukawa unafanya shughuli fulani,.....halafu kukaanza kumwagika pesa nyingi tu na baadaye ikatokea picha yake akiwa kazikalia hizo pesa...

Aliangalia ile picha kwa muda, ikijirudia rudia badaye akasema;

‘Yah, wazo langu ni hilo kwa kifupi, niwe na dunia yangu nikavyo mimi....’akakuna kichwa na kuangalia ile picha ya dunia iliyozungukwa na mikono mingi ikijikusanye tena

 ‘Katika dunia hiyo nawataka wataalamu wa aina zote, yaani kila nyanja, nimpate bingwa wake, niwapate wataalamu waliozidi utaalamu unaojulikana hapa duniani, ni pesa tu, na nitawawezesha zaidi...lakini kazi ipo hapa, nikikamisha hili, nikawakusanya hawa mabingwa, nimemaliza kila kitu, hapa natakiwa nitumie pesa kweli kweli, ...’akasema

‘Kwanza , namtaka dakitari bingwa wa kila kitu kinachomuhusu binadamu...docta bingwa, huyu ataweza kunisaidia kumiliki mambo yote ya hospitalini, huku kuna umuhimu wake,..maana mtu akipelekwa huko, anaumwa, na ni mtu wangu, nitajua jinsi gani ya kumfanyia lolote, huyu anaweza kumtengeneza mtu akawa sivyo ndivyo, hahaha, hili tutakuja kuliona huko mbele.....

‘Dakitari huyu nataka awe anacheza namba nyingi...inawezekana asiwe peke yake, atakuwa na wasaidizi wake, lakini wenye mtizamo wetu,... kukitokea hata mauaji, huyu ataweza kuandika tutakavyo sisi, ukweli unabakia kwetu, uwongo unakwenda huko kwa wanaochunguza, hata hivyo, huko nako kwa wachunguzi, kutakuwa na watu wetu...hapo imeleweka,

‘Sasa huyu dakitari natakiwa nimpate haraka iwezekanavyo, maana tukianza mambo ni lazima kutakuwa na purukushani za hapa na pale, ...nataka kwanza watu waniogope, na wataniogopa vipi,kama sikufanya jambo,...huyu ni muhimu sana na anahitajika kwa haraka...’akakuna kichwa na kuwawazia marafiki zake madakitari.

‘Nikimuacha dakitari, pia namtaka mtaalamu wa komputa ambaye kichwa chake ni zaidi ya computa zote duniani. ...hahaha huyu atakuwa akichunguza kila kinachotokea duniani, na kila linalofanyika linakuwa mikononi mwake....huyu ni mtu muhimu sana...nitashirikiana naye, maana ni mtu wa usalama, atakuwa anamlinda kila mtu wetu...’akakuna kichwa akiwaza kazi nyingina za huyu mtu, lakini akasema

‘Huyu kwa vile nitakuwa naye sambamba, sihitaji sana kuandika kazi zake..ni msiri wangu muhimu...’akasema na kutulia kidogo.

‘Mhh, namtaka mkemia, mtengenezaji madawa ambaye anaweza kutengeneza madawa ya kila namna, kitengo chake kitakuwa sambamba na watu wa silaha za kemikali,..hapa nataka, silaha na kila kitu ambacho ni muhimu kuangamiza kila atakayeleta fyofyoko, bila hata mtu kufahamu...hahaha, lakini mimi sio muuaji, kitakachofanya hivyo ni hizo kemikali, sio mimi....mmh, nitakuwa mbali kabisa, .....’akatabasamu.

‘Haya , pia namuhitajia mtaalamu wa mashine, mtaalamu wa magari, mtaalamu wa kila aina ya ufundi, nyumba, vitasa, na kila aina...na kwanini natafuta utaalamu wa magari , ni kwasababu kuna mihangaiko ya hapa na pale, gari likifanya jambo, linahitajika kubadilishwa haraka iwezekanavyo, kinamna yoyote ile,leo walione hivi kesho vile polisi wakilitafuta waishie patupu...hahaha, mimi kichwa bhwana....’akasema huku akionyesha kwenye komputa yake jinsi gari linavyobadika, kutoka muundo huu na kwenda kwenye muundo mwingine.

‘Pia namtaka mtaalamu, ….mtaalamu wa ...’ akawa anawataja watalaamu wa kila fani zilizopo duniani, na alihitaji wale waliobobea kwenye hiyo fani, nia ni kuwa juu ya kila fani ili aweze kumiliki kila utendaji kwenye hiyo fani, alipomaliza kuainisha watalaamu anaowahitajia, akacheka kicheko cha dharau,

‘Hahaha hawa ndio wataniwezesha, nifanye kile nilichokitaka. Nahitaji mikono mingi ya wataalamu...yah, hili ndio wazo langu...’akasema huku akinywa mafundi mawili ya kinywaji chake

Nikifanikiwa hilo, basi nitakuwa na dunia ninayoitaka mimi, dunia ambayo naimiliki mimi kina mna yangu,...hahaha, ukiwa na akili na pesa, bhwana, dunia unaweza kuiweka mikononi mwako,...lakini kwanza ni lazima nipate mikono ya wataalamu mbali mbali, ambao watakuwa wakifuata amri yangu, hawa watasaidia kuijenga dunia niitakayo mimi...’akatulia na kutabasamu.

‘Hahaha, kweli nikifanikiwa hili, nitakuwa nimewezesha ndoto yangu, ndoto ya kuwa na  dunia yangu...pesa itaongea, na mapesa yatakuja kwa wingi, ni siri ndogo tu, wenyewe wataona.

‘Nikisema dunia yangu, watu wataniona nimekufuru, hapana, mimi sio hivyo, hili neno wasilitafsiri vibaya, mimi similiki dunia, sina uwezo huo katu, mwenye uwezo huo ni mungu, ila mimi ninachotaka ni kuwa na namna niitakavyo mimi, utaalamu, uwezo wa kufanya mambo nipendavyo mimi, yaani niwe na namna dunia inayokwenda kwa matamanio yangu.....labda nitaeleweka kidogo...’akakuna kichwa.

‘Haya ndio mawazo yangu,....’akasema Diamu akifunga kile kitabu chake, na kujizungusha kwenye kiti chake.

Haya ndiyo mawazo ya kijana Diamu, na wakati anawaza haya, alikuwa ameshapitishwa kuwa raisi na mumiliki wa makampuni yote aliyoacha baba yake, japokuwa kulikuwa na upinzani wa hapa na pale, lakini baadaye ikapigwa kura na yeye akashinda.

Alishaongea na wazee, na wahusika wakuu, na baadhi ya wawekezaji akawaahidi kuwa hatawaangusha, ila baadhi ya wazee walisusia hicho kikao, wakijua kuwa hakina ajenda nzuri kwao, hata hivyo zaidi ya nusu ya wajumbe walifika, na kikao kikaendelea

Baada ya ushindi wake, ikaja zamu ya kuchagua wasaidizi wake, aliwachagua marafiki zake, na kuhakikisha kuwa safu ya wazee wote waliohanganika na baba yake hawapo kwenye wasaidizi wake, aliwachagua wawikilishi wa wazee, ambao alijua wapo upande wake, na cha kusangaza zaidi, msaidizi wake wa karibu akawa mrembo wake.

‘Huyu mtu ataweza kweli hii kazi, anaonekana ni muhuni tu, mlevi, na malaya...’akasema mzee mmoja

‘Ngoja tuone, maana baba yake alisema alishamuandaa kushika hatamu, na kuna waraka uliandikwa na baba yake kuwa mtoto wake huyu ndiye mrithi wake, hapo huwezi kuweka pngamizi lolote, ikizingatiwa kuwa wao ndio wenye hisa kubwa,...ni ujana, utaisha tu, akipata mshauri mnzuri, nahisi mambo yatakwenda vyema...’akasema.

‘Nasikia sisi wazee katusahau, kashindwa kujua sisi ndio tuliohangaika na baba yake kubeba matofali, hadi hapa, wanaona matunda yake,...leo hii anaingia madarakani anakosa shukurani, naona tamaa zimemzidi, yeye anajifanya kijana , hajui wazee tupo, tutapambana naye tu, mimi nakwambia sitatulia mpaka nione mwisho wake ....’akasema mzee mwingine.

‘Hayo sio ya kuongea hapa, tutakutana na wazee wenzetu tuone tutafanya nini,..’akasema mwenzake

‘Wala mimi sisubiri hicho kikao chenu, nakwenda kufanya yangu, siwezi kukubali jasho nililopoteza hapo sio dogo, ujana wangu wote uliishia hapo,leo hii ndio imekuwa hivyo.....’akasema huyo mzee

‘Yote yana mwisho, walianza wengine leo wapo wapi....nasikia ana ndoto yake ya kuleta mabadiliko,...sijui ni ndoto gani...’akasema mwingine

‘Ndoto, mwisho wake ni kuzindukana, atalala ataona, akizindukana, dunia ipo pale pale...’akasema mzee mwingine

‘Labda ana dunia yake, huwezi kujua...’akasema mzee mwingine

‘Anajidangaya.....

********

Siku zilivyokwenda ndivyo watu walivyoanza kumtambua huyu kijana, kwa mbwemwe zake, akipita mahali, akiwa na walinzi kila upande, na gari lake liliongozwa kwa king’ora, na hata polisi wakamfahamu.

Watu wakaanza kumuongelea kila kona ya jiji hili, kuwa ni mmoja wa matajiri kijana, na  tajiri mdogo hapa duniani, ...ikawa kila akipita watu wanamuita,, Diamu....Damu....

‘Hahaha kila kona ya huu mji wananitaja mimi,....na hata magazeti, ...’hapo akakumbuka jambo, akafungua kitabu chake na kuandika

‘Pia katika watu ninaoawahitaji, ni pamoja na mtaalamu anayejua propaganda, uzushi,fitina, huyu atakuwa karibu na magazeti yote, pia tunahitajika kuwa na magezti yetu mengi, hasa ya udaku, hapa kuna biashara nzuri tu, hawa waheshimiwa na matajiri wanzizi, nahitaji pesa yao kwa wingi tu,...na ili nifanikiwe hili ni lazima na sisi tuwe na chombo cha mawasiliano..yes hili ni muhimu.’akatulia akiwaza

‘Lakini mimi sitaki nionekane popote, sura yangu nataka iwe siri, na nikionekana mahali isiwezekana kupigwa pichwa, hii miwani itafanya kazi yake.....’akaivua ile miwani, ile miwani alipewa kama zawadi, ukipigwa pichwa ukiwa umevaa hiyo miwani picha hatoki, na ikitoka haionyeshi sura, ni lazima kutakuwa na mawingu ya kuziba muonekano wa uso...

Akawa sasa anakiwazia kitengo cha fitina,...ni jambo ambalo aliliona linaweza kumletea pesa, kama ataliweka sawa.

‘Katika kitengo hiki cha fitina, propaganda na uzushi,, nataka mtu aliyesomea uandishi, anayejua kuandika kitu kikakubalika, lakini pia awe intelegensia,...kuna hawa watu vyuoni walikuwa wakiitwa father punch,...nitamtfauta jamaa yangu, nitampeleka shule ya kiaina yangu,,...

‘Mmmh,halafu nimekumbuka kitu, kuna biashara nzuri ya silaha, hili nitaongea na jamaa yangu huko majuu zinapotengenezewa silaha za moto, aliniambia kipindi  cha nyuma biashara hii ilidorora sana kwani siasa imekuwa haina chokochoko sana ndio maana vita vimetulia kidogo, ila wanasema wamejipanga upya, wameona sehemu inayoweza kuingilika na kuweka fitina ni kwenye makundi ya kidini, huko wamejaribu na inaonekana kufanya kazi, sasa na mimi kama naweza kuifanya hii biashara ni muhimu niwe na kitengo mahususi cha fitina

 ‘Yes, halafu sasa kuna hii, propaganda ya magaidi..., yes, hapa naona kuna pesa, hawa watu wanaoitwa magaidi, wanatafutwa kila kona, lengo ni biashara ya silaha ipambe moto, hizi silaha zimetengenezwa za nini, ni kuulia watu, sasa zitauzwaje,...wakagaundua hii propaganda ya magaidi,...imeweza kulipa kwa kiasi kikubwa, kila kukitokea tatizo linaelekezwa huko, kwa magaidi....watu wajanja,

‘Nimegundua jambo, watu wengi hawapendi kufanya utafiti, wanakurupuka tu, wakisikia jambo, wanalichukulia kama lilivyo,....hahaha, magaidi, magaidi kumbe kuna watu wana malengo yao .....mmh, ni lazima na mimi nijikite huku nione kama na mimi nitapata kitu, niunde tume mahususi ya fitina, nipandikize watu wangu kwenye hawa watu wenye kuchukiwa...

‘Nitawafunda watu, wajifanye watalaamu wa imani za dini, wazame kwenye makundi ya kidini, huko watafiti kuna nini, wanahitaji nini, na wakishajua udhaifu wao, tunapandikiza fitina,....likitokea tatizo, najua makundi hayo yataelekezwa kidole,watakamatwa wakubwa zao, wakikamatwa, watu wangu wanaendelea kutia fitina, kunatokea vurugu wakitaka viongozi wao waachiwe, vurugu zitazaa chuki, chuki itazaa vita, hawa watawachukia hawa, baadaye watahitaji silaha, ...hahaha lakini hili ni lazima niliangalie kwa makini...nitaua hata ndugu zangu...

‘Lakini ngoja kwanza, nitaongea na jamaa yangu atanielekeza jinsi ya kufanya, wao ni wazoefu wa biashara hii, ...lakini ni lazima nijikite katika biashara hii ya silaha za moto, silaha za kemikali sio tatizo, nitakuwa na wataalamu wataziunda....hili nitalifanyia kazi pia

‘Mhh, lakini hizi za moto, tutahitajika kununua nje,....hata hivyo huwezi kununua kitu kikae tu, ni lazima upate wateja, au sio.....ni lazima tujenge fitina kuwe na vita, na fitina ni kipaji, kwahiyo anahitajika mtalaamu wa fitina, huyu atapatikana tu,...hahaha, watu hawajui kuwa kila kipaji na mtaji, hahahaha....unacheza na kichwa wewe.’

‘Nikifanikiwa haya yote, najua wataanza kunitaja, sio tu kwa utajiri, lakini pia watajua kuwa mimi ni mmiliki wa dunia ya aina yangu, dunia nitakayoweza kuiendesha kwa kiona mbali, wenyewe wanaita `remote control,’

‘Yes, ndio maana nataka nisionekane, ndio maana natakiwa sura yangu iwe ni adimu machoni mwa watu, nitakuwa sehemu nimejichimbia, huko huko majuu, ukiwa na pesa huko unakaribishwa kwa mikono miwili,nitaona jinsi gani ya kufanya.....’ akashika kichwa akiwaza, halafu akanyosha mikono yake mbele na kusema;

‘Kwa hii- hii mikono yangu nitaweza kuyumbusha, kunyoosha, kuelekeza, kuratibu,na kufanya lolote niwezalo,...kwa mikono yangu hii hiii nitafanya dunia ya aina yangu,...ila ni muhimu nitumie pia mikono ya watalamu wa dunia nzima, lakini wawe wakinifuata mimi...’akakohoa kidogo

‘Najua haya mambo ni hatari kidogo, nitatafutwa sana, lakini mimi sitaonekani kirahisi, nitakuwa mbali na wao kukitokea tatizo, lakini nitakuwa karibu na wao nikifanya vitu vyangu, nikivuna kile nilichopanda,  ni lazima niwe mtu wa aina yake `invisible man’, hahaha.........’akacheka sana, na baadaye akaiangalia ile picha ya dunia ikizungukwa na mikono, na kusema.

‘Hii ndio dunia yangu....’

NB: Hii ni nyongeza ya sehemu iliyopita, tutakuja kuona jinsi jamaa huyo alivyoweza kukamilisha ndoto yake hiyo, ambayo ni sababu ya mambo mengi yanayotokea sasa hivi kwenye hii dunia, fitina, ...

WAZO LA LEO: Utajiri, na mali ni mtihani, watu wanaweza kutumia pesa zao na mali zao kuwarubuni wengine, wakajenga fitina, wakapandikiza chuki, na kwa pupa ya wanadamu wakachukulia kama inavyosemwa, kumbe ni malengo ya watu wenye nia mbaya, wanaotumia mali na pesa zao vibaya au wanatumia mali kupata mali kwa migongo ya watu wengine.


Muhimu tunaposikia jambo, au kukitokea tatizo, tusikurupuke na kunyosheana kidole, tuweni makini, tuchunguze kwanza, tujiulizeni kwanini iwe leo, mbona jana na juzi haikuwa hivyo. Fitina ni mbaya sana.


Ni mimi: emu-three

No comments :