Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, May 16, 2014

BAADA YA DHIKI FARAJA-59


‘Masikini mhasibu, nilikuona jinsi ulivyokuwa unajikanyaga pale mahakamani, hahahaha, ujanja wa bure, kumbe huna kitu kabisa, hivi wewe uhasibu huo uliupata pata vipi, au ndio nyie mlioenda shule kukariri tu...’akaanza kunitania mdada, huku akicheka kwa dharau.

‘Yaani badala ya kunipa pole na hongera wewe unanidhihaki...’nikasema

‘Nikupe pole, wakati ulikuwa aribu uvurunde, huna maana kabisa wewe, kumbe wewe huwezi kuwa mwanajeshi...’akasema

‘Kwanini mimi nimekosea nini?’ nikauliza

‘Wewe ngoja uone nitakavyowajibu siku wakinisimamisha kutoa ushahidi,labda wasifanye hivyo...’akasema mdada kwa kujiamini.

‘Kwanini unajiamini hivyo, nikuambie ukweli yoyote atakayesimamishwa pale mbele, ni lazima atakuwa na wasiwasi, ujue pale hujui utaulizwa nini, na hicho unachoulizwa huwezi kuwa na uhakika mwenzako ana lengo gani, sio swala la kwenda shule...’nikasema

‘Nikuambie siri moja ya kumshinda adui yako, usikubali akutishe kwa macho, pili usimpe nafasi ya kuchambua kauli yako, tatu, usimsaidie kufikiri..na ukianza wewe hakikisha hapati pumzi ya kukurudi...’akasema

‘Mhh, mdada mbona kauli yako ni ya kibabe sana, utafikiri wewe ni askari...’nikasema

‘Hahaha, masikini mhasibu, kila mtu ni askari bwana, cha muhimu ni kujiamini..ndio fani hiyo ina wenyewe, kwani ni taaluma inayojitegemea lakini katika maisha ya kawaida kila mtu ana ulinzi binafsi ambao ngao yake ni kujiamini...sasa wewe hujiamini, ndio maana ukawa unajianyaga...’akasema

‘Lakini mdada mimi nilijaribu sana kuwa upande wako, na nimefanya hayo kwa ajili yako, nimeshindwa kusema ukweli wote kwa kukulinda wewe, ina maana mimi hapo nimefanya kosa...?’nikasema kama namuuliza

‘Hahaha, mhasibu usitake turudi nyuma kwenye kauli yangu ya mwanzo, na ujua nasubiri jibu, na hilo jibu litoke kabla kesi hii haijaisha, ukichelewa tu, utakuja kunikumbuka na utakuwa umeshachelewa...fikiria kwa makini na uwe na uhakika nayo, kumbuka maisha yako ni wewe mwenyewe, usikubali kuwa mtumwa wa mtu mwingine, jiamini....na kama kuna mtu unaona yupo upande wako, hakikisha kweli anakutahamini..’akasema

‘Mhh, kweli eeh, ndio maana uliona nilivyokuwa najaribu kuficha ukweli, ukweli ambao ningeliusema wewe ungelikuwa hatiani...’nikasema

‘Mhh, mhasibu, masikini...hata siku moja sifikirii kusaidiwa, mimi huwa anjipigania mwenyewe,...ila ninapenda sana kusaidia watu...wewe unasema umeshindwa kusema ukweli wote, ukweli upi huo, hebu niambie wewe ulitaka useme ukweli upi, ....?’ akaniuliza na kabla sijamjibu akasema;

‘Sikiliza wewe mwanaume, Usije ukajifanya wewe unajua kuongea sana, uaongea tu, bila kuwa na uhakia na hicho unachokiongea, mdomo, utatamka, ..lakini hebu chunga athari ya kile utakachokitamka, linganisha matamshi yako na ukweli wa hicho kitu na athari zake,...sione raha kuongea kitu ukitumaini kuwafurahisha watu, kumbe itu hicho kitageuka kuwa kisu au sumu ya kukudhuru wewe mwenyewe, kuwa makini kwa hilo hasa katika hii kesi, kuna mengi huyajui...’akasema na kutikisa kichwa.

‘Wewe unajua, au unasema tu..’nikasema

‘Mhasibu, usitake niongee sana, ila ninachokushauri ni kuwa makini sana katika kutoa kauli zako hasa mbele ya mahakama, ni bora ukae kimiya au uongee yale uliyo na uhakika nayo tu...’akasema.

‘Mdada mimi inaniuma sana kusema uwongo, na baada ya kumaliza pale moyo wangu ulinisuta sana, nikawa najiuliza ni kwanini wewe hupendi niseme ukweli ulivyokuwa, hasa kwenye lile swala la ndevu, kwanini hutaki niseme kuwa wewe ndiye uliyenivalisha zile ndevu za bandia...?’ nikauliza

‘Mhasibu ngoja nikusaidie mpenzi wangu, hebu chukilia ukweli halisi, kwa mfano,uneglisema hivyo, na ukaja kuulizwa ni kwanini ulifanya hivyo ungelisema nini?’ akaniuliza

‘Nitasema ni wewe ulinishauri hivyo, ili mtoza ushuru asinielewe kuwa mimi ni nani...’nikasema

‘Wewe mwanaume kwanini hujiamini, hiyo kauli ya wewe ulisema, huoni kuwa ni ya kitoto zaidi, jifunze jinsi ya kujitetea, haya, mfano wakakuuliza tena, ni kwanini ujifiche sura yako, kama kweli ulikuwa katika usahihi?’ akaniuliza

‘Mdada, wewe ndiye ulinishauri hivyo, mimi sikujua kusudio lao ni nini, ...’nikasema

‘Hapo umeshaanza ujikanyaga, ...unaona hapo, wahiyo  ni heri huo uwongo kuliko ungelisema ukweli, kwani ukweli huo ungezua hisia nyingi, na wewe ungelionekana mtu wa ajabu sana, bendera fuata upepo, mtu usiyejiamini, ....na uwe makini kwa hilo, kwani kama utaendelea hivyo, basi mwisho wa siku wewe utashukiwa mhalafu,. Ni vyema hilo lisifahamike kabisa kwa yoyote yule, hiyo iwe siri yangu mimi na wewe tu....’akasema na mimi nikabakia kimiya nikiwaza na nikamuona mdada akitaka kusema kitu mimi nikamuwahi kwa swali;

‘Hivi mdada, nikuulize huyu mtu aliyenipiga nyundo mimi na wewe, ni nani?’ nikamuuliza na yeye kwanza akatabasamu halafu akaangalia pembeni na kusema

‘Mimi sijui, hiyo ni kazi yao wao kumtafuta...usipende kubeba mizigo ya wenzako yenye utata, jiamini, nimeshakufundisha hilo’akasema mdada

‘Mimi naanza kuhisi vinginevyo, huenda ikawa ni kweli....’nikasema

‘Ukweli upi huo...?’ akaniuliza

‘Kuwa huenda  kweli ni wewe uliyenipiga na hiyo nyundo...’nikasema

‘Mimi sijui hilo, na wala sijui kulitokea nini kipindi kile, ndio maana sipendi kusimamishwa pale mahaamani, kwani ninaweza nikapandwa na hasira nikaiharibu mahakama yote, ....’akasema

‘Ahaa nimelewa kumbe ndio maana hawataki kukusimamisha weweckutoa ushahidi?’ nikamuuliza

‘Sijui, ....hilo ni kazi yao, kama wapo tayari wafanye hivyo, mimi siogopi kabisa,ila wakinisimamisha wajiandae...’akasema mdada akikunja uso kuashiria hasira.

‘Mdada, hivi wewe unafanya haya yote kwa ajili ya nani?’ nikamuuliza na yeye akaniangalia na kutabasamu akasema;

‘Nfanya yaote hayo kwa ajili ya nani,...hahaha mhasibu, ina maana hujui, ni kwa ajili yangu, ni kwa ajili ya maisha yangu,ni kwa ajili ya kuwakomoa hao wanaojiona wamefika, mafisadi wakubwa, hao wanakula mali ya wananchi, wakavimba kama vifutu, wakati wananchi wao wanakondeana, wakizidi kuambiwa wafunge mikanda na ahadi za maisha bora ya kufikirika,..nilishakuambia hilo, na sijutii kabisa kuwachukulia hao mafisadi mali yao, ...’akasema

‘Mimi nahisi kuna mtu unayemfanyia kazi, sio kama unavyodai wewe, na mimi unanitumia kama njia ya kufanikisha malengo yako...’nikasema na yeye akaniangalia  kwa makini huku akichezesha chezesha macho, halafu akataabsamu, na kusema;

‘Masikini mhasibu,...kwanini unanifikiria hivyo, hivyo ina maana wewe hdi sasa hujaniamini kuwa mimi nafanya haya kwa ajili ya watu kama nyie, na zaidi nafanya haya kwa vile ninakupenda sana...nimefanya mengi wa ajili yako, hata kuwa tayari kuivunja ndoa yako, ili tu uwe mchumba wangu, hebu jiulize wewe una nini cha maana saana, ujue mimi nipo kwa ajili ya masilahi zaidi, sasa wewe una masilahi gani, una nini cha kuitwa tajiri, hebu jiangalia una masilahi gani...’akasema kwa dharau.

‘Mimi sijui, yote hayo unasema wewe..’nikasema na akawa kaangalia mbele na uso wake ulionyesha  kuwazia jambo nahisi kuna kitu kinamkera, halafu akatabasamu, akawa anasita kugeuka kuniangalia, na hali hii ilikuwa ngeni kwa mdada, mdada mara zote tukiwa na mimi huwa anajiamini, na anakuwa kama mtu wa kutoa amri kwangu, lakini leo nilimuona tofauti, akasema;

‘Ujue nimefanya hayo yote kwa ajili yako, huwezi kuamini hilo lakini ipo siku utanikumbuka, na nimefanya haya kwa vile ninakupenda kwa moyo wa dhati, na hao wanaokudanganya , wakajifanya wanakupenda, wanafanya hivyo tu kwa vile tu, imetokea hivyo ilivyotokea, hakuna kingine....’akatulia kidogo.

‘Hata hivyo napenda kuumbusha kuwa mimi sitakubali mtu mwingine akuchukue hivihivi...yaani mimi niumie, halafu niwe mshika pembe, hapana...., labda niwe maiti, labda niondoke...’akasema na kutulia halafu akaniangalia na kusema;

‘Mhasibu, natumai umeyasikia yangu ya moyoni, labda utaniona mwanamke wa ajabu sana, wa kumulezea mwanaume hivyo, wakati mwanaume mwenyewe anajifanya hana habari...nimegundua kitu hasa kutoka kwako, maana wanaume nyie mkipendwa mnajifanya kuringa...sasa , nikuulize na wewe, je unanipenda kama ninavyokupenda wewe?’ akaniuliza sasa akiniangalia moja kwa moja usoni, akiwa hapepesi macho.

‘Mdada, mimi siwezi kukujibu hilo swali, unataka nikujibu nini, kwasababu wewe unafahamu fika mimi nina mchumba wangu tayari,...’nikasema na yeye akawa amaetulia kimiya na nilipoona hasemi neni nikasema;

‘Hebu jaribu kujiweka katika nafasi yake, halafu utendewe hivyo, hivyo unavyotaka wewe, hebu jaribu kuhisi,...utajisikiaje,mdada nakuomba, tujaribu kuwa na moyo wa huruma, namuonea huruma sana huyo binti, .....’nikasema na yeye akageuka na kuniangalia usoni, nilihisi kama kitu kinapita usoni mwake, akatikisa kichwa, na niliona machoni kukiwa na kitu kama machozi, lakini sio machozi, akahema.

Aliendelea kukaa kimiya kama anawaza jambo, halafu akataabsamu,  na taratibu lile tabasamu likaanza kuyeyuka, na uso uliokuwa unavutia ukaanza kujenga sura nyingine, lakini kabla hajafikia kukasirika kabisa akageuka pembeni na kusema;

‘Unanikatisha tamaa mhasibu, kwanini hutaki kutoa kauli ya kunipa moyo, kwanini hutaki kukubali ukweli kuwa hata wewe unanipenda..nafahamu fika kuwa moyo mwako unanipenda na  huyo mchumba wako ni kwa vile tu, ilitokea hivyo, mkaonana kabla yangu,...kweli si kweli?’ akaniuliza na mimi nikabakia kimiya halafu akaendelea kusema;

‘Mhasibu ni vyema ukasema ukweli  kabla hujachelewa, nakuambia hili ili siku moja usije ukajuta, na wakati huo nitakuwa sipo nawe tena,...’akasema na kutulia na kabla sijasema kitu akanisogelea na kuchukua simu yake, akapiga picha tukiwa pamoja akasema;

‘Hebu tabasamu nataka kuweka kumbukumbu ya siku ya leo...’akasema tukatabasamu na akachukua picha, akawa anaiangalia, na mdada akasema;

‘Kwahiyo mimi , nataka kusikia kauli yako, niambie moja kwa moja je kweli na wewe unanipenda kama ninavyokupenda mimi,hebu angalia hii picha tunavyoendana, nakuambia ukweli , utakuja kunikumbuka na unitafute usinione...’ akasema na kuniangalia tena usoni

‘Mdada hilo lipo dhahiri, kupenda kupo, siwezi kukataa, lakini kwa hali ilivyo, mimi sina ujanja wa kufanya lolote, yule ni mchumba wangu tayari na ameshanizalia mtoto, na tumeingia kwenye mkataba naye na ni mkataba mgumu ambao mimi siwezi kuuvunja, unamfahamu vyema baba yake, sasa mimi hapo unataka nifanya nini...?’  nikamuuliza

‘Mhasibu, usitake kunichefua,  au wataka mimi nifanye kweli, ili jamii ijue kuwa wewe na mimi ni wachumba wa siri, mimi nakustahi sana wewe, ..baba mkwe wako niliongea naye, nikajaribu kumuelimisha, hilo na mengineo, lakini kama alivyo, ni mgumu kuelewa, na shauri hilo lipo mikononi mwako, wewe ndiye mwenye maamuzi, hata hivyo, mbona wao walishavunja huo uchumba unaodai wewe, ‘akatulia na kuangalia saa yake.

‘Sijaongea nao, sizani kama uchumba huo utavunjwa kirahisi hivyo, je huo mkataba tuliowekeana nao utakuwaje, unataka nyumba yangu na kila kitu kiwe mikononi mwao...huoni kuwa mimi nitakosa kila kitu...’nikasema

‘Mliandikishana hivyo, unaona hawa watu walivyo..lakini kwa mzazi anaweza kufanya lolote, wewe ulijifanya kijogoo, ukawa unaparamia mitetea, haya hiyo ndio faida yake...’akasema na mimi nikainama chini na kusema;

‘Yametokea sasa ningelifanya nini..hata hivyo hata kazi alinitafutia huyo baba mkwe, unaona kulivyo pagumu hapo....’nikasema

‘Hahaha, hata hii kazi ya mtoza ushuru ni yeye aliyekupigia debe,...alikuwa akikuvuta na alijua akikuweka wewe utafanya kila anachokitaka yeye, lakini sasa maji yamemfika shingoni,familia yake ina haha huku na kule hadi wa waganga wa kienyeji, nasikia wanataka kunitupia juju mimi na wewe, una habari hiyo, sio ajabu maana,kila mchumia janga hula na wa kwao, au sio.....’akasema

‘Nani aumbia yote hayo?’ nikamuuliza

‘Kaa kama ulivyo, na bakia na msimamo wako huo, mchumba mchumba, na safari hii ukiwabembeleza ukamrudia huyo mtu, basi wewe utakuwa mume bwege,...hilo liweke akilini, maana hapo itakuwa sio mapenzi tena, bali ni kulipa fadhila....’akasema

‘Mdada ni lazima niongee na hao watu nijue msimamo wao upoje, siwezi kuamua lolote mpaka sasa, hata kama nakupenda vipi, hata kama wewe unanipenda vipi, lakini ujue kuna ndoani imenasa kooni mwangu...siwezi kumuacha mtoto wangu....’nikasema

‘Haaaah, kumbe, ...nimekuelewa, mtoto ndio kikwazo, au?’ akauliza

‘Sio kikwazo ...ila...’nikasita

‘Mimi nilikuwa nataka kusikia kauli yako tu, ili nijue nipo na mtu ambaye kweli ananipenda kwa dhati, uchumba sio ndoa,...kama mngelikuwa mumefunga ndoa, nisingeliweza kulifanya hili, ...sawa mumezaa mtoto, lakini hiyo ilikuwa kwa bahati mbaya, na unataka kumuoa mtu ambaye huna mapenzi naye, huoni kuwa utajitaia utumwani, maisha yako yatakuwa hayana raha, na ndio mwanzo, wa kuchepuka chepuka...kuwa makini na hilo....’akasema

‘Sasa wewe unataka mimi nifanye nini?’ nikamuuliza

‘Maamuzi ni ya kwako, na ni bora uchukua maamuzi mapema kabla hujachelewa, wani kesi hii ikiisha, utabakia kunikumbuka,...siku ya leo iweke akilini mwako, na uyakumbuke maneno yangu, tuyaache haya, tuongee swala lililopo mbele yetu...’akaangalia saa yake na mimi nikawa nawaza kauli yake hii ya mwisho ana maana gani kusema hivyo;

‘Kwanini unasema nitakuja kukumbuka, kwani una mipango gani?’ niamuuliza

‘Mpelelezi, anataka kuongea na mimi, sijui anataka uniambia nini, na huyu mtu nimemuona ana ajenda ya siri, badala ya ufanya kazi yake, anataka kutumia migongo ya watu, mimi siwezi kumfanyia kazi yake, na kama ananishuku mimi, kwanini hanischukulii hatua...’akasema

‘Kwani siku ile hamukuongea naye?’ nikamuuliza

‘Wewe mtu, kwanza siku ile ulinificha ...hukuniambia kuwa huyo mtu yupo ndani kwako, pili inaonekaan mna ajenda ya siri nyie wawili, ndio hapo nakosa amani, ina maana umeshaanza kunisaliti mimi, mhasibu unakumbuka tulipotoka, ...usitake nifanye yale ambayo utakuja kuniona mbaya, usinilazimishe nifanye jambo nitakalokuja kujijutia....’akasema

‘Pale ilikuwa vigumu kukuelezea lolote maana ningelisema lolote angelisikia, nilijaribu kuonyesha hisia kuwa humo kuna mtu, lakini ukawa hunielewi, unafikiri mimi pale ningalifanya nini...’nikasema

‘Mimi sio mtoto mdogo, kazi hii sikuianza leo, nafahamu kabisa kuwa mnakutana mara kwa mara na huyo mtu, na ameshaupa kazi ya kufanya, kunichunguza mimi ...lakini kwangu mimi hamtapata kitu, mimi natimiza wajibu wangu kwa jamii, ipo siku utalijua hilo, ...kwahiyo msipoteze muda wenu sana kunifuatilia mimi, na nazidi kukumbusha kuwa haya ninayoyafanya kwa namna moja au nyingine yatakuja kukusaidia wewe...’akasema

‘Kwani mliongea nini na mpelelezi?’ nikamuuliza na yeye akatabasamu na akatulia kama anawaza jambo, halafu akaanza kunielezea

NB: Alielezea nini, hebu tukutane sehemu ijayo


WAZO LA LEO: Kutamka nakupenda ni rahisi sana, na wengi wanatamka tu, wakiona ni kauli ya kupita tu, lakini kauli hiyo inatakiwa iwe ni ahadi inayotoka moyoni, ...tulitamke neno hilo tukiwa na yakini ya weli kuwa kweli tumependa, hatuna shaka, vinginevyo, tutakuwa kwenye kundi la wanafiki, ambao mara nyingi kauli zao ni za uwongo.

Ni mimi: emu-three

No comments :