Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, April 28, 2014

BAADA YA DHIKI FARAJA-46


‘Wewe Mhasibu.....’nikasikia sauti ikiita jina langu, kwanza nikajifanya sikusikia, lakini ile sauti ikaita tena , na safari hii kwa msisitizo.

‘Wewe mhasibu ina maana hunisikii au unanizarau.....’ikasema hiyo sauti

Niligeuka taratibu kwa kujihami na kumtafuta huyo aliyeniita jina langu, ilikuwa ni sauti ya kike, na pale sauti ilipotokea kulikuwa na kina mama watatu na wanaume wengine, wakiwa katika pilika pilika za biashara, na hao akina mama walikuwa wakihudumia chakula, kuonyesha kuwa wanauza bashara ya mama Ntilie.

Nikajaribu kukisia ni nani kati ya wale wawili aliyeniita , sikuweza kutambua, lakini kabla sijachukua hatua nyingine mama mmojawapo akasema;

‘Nakuita mara mbili unajifanya hujanisikia je unatokea wapi mwenzangu?’ akaniuliza huyo mama, nikamwangalia kwa makini kama niliwahi kuonana naye kabla lakini sikuweza kumkumbuka vyema nikaamua kumuuliza kabla sijamjibu swali lake;

‘Samhani kwani wewe ni nani unayeniuliza hivyo?’ nikauliza nikiwa nimesimama nikimwangalia na wale akina mama wengine walikuwa wakiendelea na shughuli zao, bila kujali kinachoendelea kati yangu na huyo mama aliyeniita jina langu.

‘Ajabu kabisa wewe unataka kumuoa binti yetu halafu hunifahamu, mhh, ni kweli kabisa nilishawaambia wenzangu kuwa wewe humfai binti yetu, na hilo nimalisema baada ya kufanya uchunguzi wangu mwenyewe, nikagundua kuwa kweli wewe hustahili kuoa katika familia yetu...’akasema

‘Niliwaambia kabisa wakufunge baada ya kumharibu binti yetu ili iwe fundisho, wakapinga kabinti kakajifanya kanakupenda kipo wapi...na kaka naye akashinikiza kuwa atakutumia kwa  mambo yake,...hamna kitu hapa....’akasema akinionyeshea kidole juu chini.

‘Sasa unaonaeeh,a wanaanza kukumbuka ushauri wangu...’akasema sasa hivi akiwa keshaondoka pale walipokuwa wenzake na kuja hadi pale niliposimama.

‘Sijakuelewa mama, kwani wewe ni nani,.?’nikauliza sasa tukiwa tumeangaliana. Macho ya mama huyo yalikuwa makali, hayaogopi aliniangalia moja kwa moja usoni bila kupepesa, akasema;

‘Mhh unajifanya hunifahamu eti,...basi kwa taarifa yako mimi ndiye shangazi wa mchumba wako..’akasema na kunifanya niiname chini kwa aibu nikanyosha mkono kumsalimia, lakini akanipuuzia, hakunyosha mkono kabisa akawa kaangalia pembeni na mimi nikasema;

‘Oh, samanahani shangazi, mimi nilikuwa sikufahamu, hatujawahi kuonana kabla, unisamehe sana....’nikasema nikijibaragua lakini yeye akakunja uso kwa hasira na kusema;

‘Hebu niambie ina maana binti yetu hakuwahi kukuambia kuwa hapa mjini yupo shangazi yake, na ulipoambaiwa hivyo, kama kweli ulikuwa na nia njema ya kumuua, natumai ungenitafuta....’akasema

‘Kwakweli Binti, hakuwahi kabla kuniambia hivyo, sikumbuki kabisa kusema kuwa kuna shangazi yake huku mjini....’nikasema

‘Haya alipokuja hapa mjini, hakuwahi kukuambia kuwa yupo hapa na anaishi kwa shangazi yake?’ akaniuliza

‘Ni kweli safari hii aliniambia hivyo lakini..’nikasema nayeye akanikatisha na kusema

‘Na uliposikia hivyo ukawa kimiya, hukutaka hata kuja kunisalimia, kwasababu unanifahamu kuwa nakutambua kwa tabia zako chafu, pinga kama huna tabia chafu za ulevi na uhuni...’akasema.

‘Shangazi, nilipolijua hilo, nilitaka kuja kuonana na wewe lakini ndio kipindi nilikuwa kwenye matatizo, ’nikasema.

‘Matatizo ya kujitakia  mwenyewe, ...unajua nyie vijana mnauingia mji kwa pupa mnatuhribia amani, mnakuja na tabia zenu chafu na kuanza kuiga hata yale yasiyofaa,...nikupe ushauri wa bure, ukiingia mji hebu jaribu kuulizia wenzako waliotangulia jinsi gani maisha hapo yalivyo ....’akasema na mimi nikatulia kimiya , alipoona hivyo akasema;

‘Hivi wewe katika wasichana wote, .....mdada, ndio uliona anakufaa, kuondoa tamaa zao za kimwili...?’akaniuliza na mimi nikashituka kidogo na kusema
‘Kwanini unasema hivyo shangazi, huyo unayemtaka ni mfanyakazi mwenzangu tu...’nikasema.

‘Haloooh, mfanyakazi mwenzako eeh,, ...sawa anaweza akawa mfanyakazi mwenzako, kazi na dawa sio, hahahaeeh , mimi hunidanganyi kitu, jinsi mlivyokuwa mnachukuana mnaingia hapo hotelini, mankunywa, mpaka mnapitiliza na siku nyingine kulala humo humo nilikuwa nawaona....’akasema.

‘Mhh hapana sio hivyo shangazi, tulikuwa tunafika kwa maongezi, na wakati mwingine kuna kazi tunafanya...’nikasema

‘Kazi za usiku eeh, mumekuwa umiani, eeh, hahaha, hivi unaniona mimi mtoto mdogo eeh,  haya hebu niambie una mpango gani na binti yetu?’ akaniuliza kinigusa kwa kidole kifuani, na kunifanya nirudi nyuma kidogo, nikasema;

‘Mbona kila kitu kipo wazi shangazi, ....’nikasema nikiwa sasa nanyenyekea

‘Unafahamu taratibu na mila za kabilazetu, na sio kabila letu tu, ni karibu mila nyingi za Kiafrika, shangazi na mjomba ndio watu muhimu katika maswala ya kifamilia hasa ya ndoa,..mimi usinione napika mama Ntilia hapa, ukanizarau nina biashara nyingi tu, leo nipo hapa kesho nipo kwenye shughuli nyingine, nina watu nimewaajiri, lakini hata hivyo, siwezi kukaa na kukunja nne, bila kujishugulisha, nafanya kwa vitendo ili kuwaonyesha wafanyakazi wangu kuwa kila kazi naifahamu, kwahiyo usinizarau kabisaaah...’akasema

‘Sijakuzarau shangazi....’nikasema

‘Nimekuwa nikikufuatilia nyendo zako hatua kwa hatua, na ndio maana niliwaonya ndugu zangu kuwa tunampotezea binti yetu muda wake, na hata leo wakiniuliza kuwa wewe unafaa kuwa mume mwema wa binti yetu, nitasema hufai, niulize kwanini’akasema

‘Kwanini shangazi?’ nikauliza

‘Kwanza huna msimamo, mnafiki mkubwa wewe, ....wewe ni wale wanaume wasiojua kusimamia familia zao, na ni rahisi kurubuniwa... na kwa kuthibitisha hilo, angalia ni janga gani uliloliingiza kwenye familia yetu,....’akasema

‘Shangazi mbona mimi sijakuelewa....’nikasema kujitetea

‘Hujanielewa, si ndio maana nikasema wewe ni wale wanaume bwege, wasio na msimamo, unajua wewe sasa hivi umechangia sana kuiharibia familia yetu  na maisha yetu, pamoja na kaka yangu kujitolea kwa hali na mali kukusaidia wewe kukutafutia kazi, hebu angalia malipo yake, hivi wewe unataka ubebwe vipi....’akasema

‘Mimi nimefanya nini kibaya shangazi ...’nikasema nikiangalia saa yangu

‘Kaka yangu sasa hivi anaumwa, yupo mahututi, kapatwa na gonywa la kiajabu ajabu, ghafla kadondoka chini,  kapoteza fahamu, mara mwili mzima hauna nguvu kabisa , niliwaambia wewe ni muumiani umekuja kunywa damu zetu , utatumaliza mmoja baada ya mwingine  , sasa wanaanza kuona,...chanzo ni wewe na kundi lako..’akasema

‘Shangazi mbona mimi sina habari na hilo...’nikasema

‘Huna habari na nini?’ akaniuliza

‘Kuwa baba mkwe anaumwa...’nikasema

‘Uwe na habari usiwe na habari, kwani kinakuuma nini , wewe siuonaona umepata, wajinga ndio waliwao, au sio...?’ akawa kama anauliza

‘Sasa sikiliza kama mumeamua kufanya hivyo, ujue na sisi hatujalala, tutapambana chini na juu, siunafahamu kabila letu lilivyo eeh, ...sisi hatuogopi, tunapambana ana kwa ana, mimi mwenyewe, sitalala mpaka nihakikishe na nyie mnakumbana na shughuli nzito, na utanifuta ..wewe siunajifanya kijogoo, tutaona kama bakora yako itaweza kazi , tupo....’akasema na kugeuka kurudi kwa wenzake.

Mimi nilibaki nimeduwaa kwa muda halafu nikaangalia saa nikaona nimezidi kuchelewa, nikageuka kumwangalia yule mama, lakini hakuwepo tena kwenye lile kundi, nikaona nisizidi kupoteza muda nikageuka na kuanza mwendo wa kurudi hotelini.

Nilitumia njia ile ile ya kificho na kuingia ndani huku nikijiuliza maswali mengi kichwani, na sikujua kabisa nifanye nini,...

‘Huu sasa msala , naona nikifika ndani cha kwanza ni kumpigia simu mchumba wangu nijue ni kitu gani kinachoendelea...’nikasema nikiharakisha kuelekea kwenye chumba chang

***********

‘Niambie unatoka wapi?’ sauti ikanishitua pale nilipofungua mlango wangu na kuingia kwenye chumbani ninapoishi hapo hotelini, ni chumba kikubwa chenye kila kitu, kwa kipato changu nisingeliweza kumudu vyumba vya hadhi hiyo.

Niliposikia hiyo sauti, nilishituka karibu nidondoshe ufunguo, nikageuka na kumuona mdada akiwa kakaa kwenye sofa kakunja nne, akiwa kabadili muonekano wa nywe zake, na alikuwa akifanya kitu kwenye simu yake.

‘Oh, umeingiaje humu ndani na .....?’ nikauliza nikiwa nimeshikilia ufungua wa hicho chumba, na yeye akabetua mdomo bila kuniangalia, alikuwa akiandika kitu kwenye simu yake, na alipoamaliza akasema;

‘Hilo sio swali la kuniuliza, unafahamu fika mimi ndio mdhamini wako mkubwa, na zaidi ya hapo mimi ndiye mtarajiwa wako.....hahaha, nikitaja hivyo, mtarajiwa, unajifanya kushituka, usijifanye hulitaki hilo, kama moyo wako uneglifungulia ni wazi kabisa ungenionyesha mimi, kuwa ndiye chaguo lako, nasema uongo...?’ akaniuliza akiniangalia kwa uso unaoonyesha kuwa hataki mchezo.

‘Hayo unasema wewe...hata kama ni hivyo, lakini ujue mimi nina mchumba wangu, ambaye ni mama wa mtoto wangu , unafikiri mimi hapo nitafanya nini...’nikasema

‘Kwa minajili hiyo, ujue kabisa kuwa mimi ninaweza kuingia humu ndani wakati wowote nitakavyo,...’akasema akiwa anacheza miguu yake na safari hii akiniangalia moja kwa moja usoni. Na nikawa kimiya, nikiwa nacheza na ufungua mkononi akauliza

‘Haya niambie umetoka wapi, toka muda wote huo?’

‘Nilitoka kidogo..kupoteza mawazo...’nikasema

‘Kwanini hukuniambia unataka kutoka..ki-do-go kupoteza mawazo, kwani ningekukataza, lakini ni muhimu nifahamu ili nijue jinsi gani ya kuhakiki usalama wako...’akasema huku akiyatamka maneno hayo kwa mzaha

‘Hamna shida, mimi nilijiamini kuwa hakutakuwwa na baya lolote, nimechukua tahadhari zote...’nikasema

‘Niambie ulikwenda kuonana na nani?’ akaniuliza akibadili sauti na kuongea kwa sauti ya ukakamavu.

‘Nimesema nilitoka kwenda kupoteza mawazo, sio kwenda kuonana na mtu, sikuwa na lengo la kuonana na mtu...’nikasema

‘Sikiliza, ....mimi sio mjinga, nafahamu kabisa kuwa ulitoka hapa kwa minajili ya kuonana na mtu, niambia ni nani huyo uliyekwenda kuonana naye, na kwanini hukutokea mlangoni,ukatoka kwa kujificha?’ akauliza

‘Sikutaka mtu afahamu kuwa nimetoka, ni kwa usalama tu, nilifanya hivyo kwa ajili ya kuchukua tahadhari...’nikasema

‘Ninataka kumfahamu huyo mtu uliyekwenda kuonana naye ni nani.....’akasema

‘Nimesema sijatoka kuonana na mtu, ...’nikasema

‘Usitake kunichanganya.....unasikia, unafahamu kwanini ninayafanya haya yote, ....,mimi najitolea kwa ajili yako, bado unafanya mambo kinyume na makubaliano yetu, ...kama usiponiambia huyo mtu, nitahakikisha nayaweka machafu yako hadharani, na unafahamu ni kitu gani kitafuata baada ya hapo..’akasema

‘Kwanini unalazimisha kuwa kuna mtu nilikwenda kuonana naye, kwanini huniamini, au kuna jambo jingine una wasiwasi nalo....’nikasema na yeye akatembea hatua mbili kunikaribia na kama vile kasahau jambo akageuka na kunipa mgongo, akasema;

‘Ni kwasababu nina uhakika kuwa kuna mtu alikuita mkaonane naye, ....ila sijamfahamu ni nani, katumia namba ya kibandani, nitamfahamu tu, lakini kwanini usiniambie ukweli, kwanini wewe unakuwa mgumu kuelewa....’akasema na mara simu yake ikaita..’akaipokea na kusikiliza kwa muda, halafu akageuka na kuniuliza

‘Huyo mwanamke uliyekuwa ukiongea naye ni nani?’ akaniuliza

‘Ni shangazi ya mchumba wangu....’nikasema

‘Mlikuwa mkiongea nini na yeye huyo mwanamke mwanga?’ akaniuliza

‘Alikuwa kiniuliza msitakabali wa ndoa yangu na mchumba wangu....’nikasema

‘Wau wau..mstakabali wako na mchumba wako, bado neno mchumba wako lipo moyoni, bado hujanielewa, anyway, haina haja kwa sasa maana familia hiyo sizani kama inakuhitajia tena baada ya hayo yaliyotokea, sizani kama watakupokea kwa mikono miwili....’akasema

‘Kwanini unasema hivyo?’ nikauliza

‘Kwa taarifa yako tu, wenzako hao wameshakutenga...sasa hivi wewe kwao ni adui namba moja....’akasema

‘Wenzangu akina nani?’ nikauliza

‘Usijifanye kuwa hufahamu, baba mkwe wako yupo taabani, hali yake ni mbaya sana, na kauli yake ya mwisho kabla hajapoteza fahamu ni kuwa wewe umemsaliti....umekuwa upande wa maadui zake,...na hayo aliyaongea mbele ya binti yake,na binti yake akaapa kulipiza kisasi kwa lolote litakalotokea kwa baba yake, na sasa hivi wameitana kikao,  ....’akasema

‘Kwanini , kwani mimi nimefanya nini?’ nikauliza

‘Ndio maana nataka nifahamu nyendo zako, ulipotoka hapa zaidi ya huyo shangazi uliongea na nani mwingine?’ akaniuliza

‘Hakuna mtu mwingine niliyeongea naye....sikuwa na haja ya kuongea na mtu, nilikuwa na mambo yangu kichwani ya kutafakari...’nikasema

‘Nitakuja kulifahamu hilo...ila kwasasa, nahisi cheo ulichoahidiwa kimeota mbawa,na huenda ukajikuta ukikamtwa tena kwa kosa lile lile...japokuwa kuna utata mwingine umejitokeza, ...’akasema

‘Utata gani?’ nikauliza nikifikicha macho yako maana akili ilikuwa sio yangu mambo yanatokea mengi wa wakati mmoja mpaka kichwa kinashindwa kuhimili, mdada akaniangalia kwa makini akiwa katulia , akaangalia simu yake baada ya ujumbe kuingia, akausoma, halafu akasema;

‘Mlinzi wangu kapotea siku ya pili sijamuona,...na polisi wanamtafuta, inavyosadikika ni kuwa,  kumbe ndio yeye aliyeingia ndani na huenda ndiyo yeye aliyefanya hayo yote, akishikirikiana na mtu mwingine, huyo mtu mwingine alikuwa kabakia getini, sasa huyo mtu mwingine ndiye kitendawili...’akasema

‘Ni nani huyo mtu mwingine,na huyo mlinzi kaenda wapi?’ nikauliza

NB: Mengi yanaanza kujitokeza, na mwisho wa yote ni ukweli kujulikana,kwani kile chenye mwanzo hakikosi kuwa na mwisho tupo pamoja


WAZO LA LEO: Utajiri na mali sio kila kitu, utaji na mali ulivyovichuma kwa dhuluma vinaweza kugeuka kuwa silaha ya kulipiza kisasi kutokana na dhuluma zako. Vilio vya wale uliowadhulumu, vinasikiwa na kisasi kinakuja kutoka kwenye mali yako mwenyewe.
Ni mimi: emu-three

No comments :