Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, April 16, 2014

BAADA YA DHIKI FARAJA-41


Mdada alipoingia alipiitiliza hadi kwenye kiti kirefu, anapokaa bosi wa hiyo ofisi, akakaa na kuanza kujizungusha kwenye kile kiti, utafikiri yupo ofisini kwake, alifanya hivyo mara tatu, na wote tukawa tunamwangalia yeye, na alipoona wote tunamwangalia yeye, akatulia na kusema;

‘Jamani ubosi mnzuri, au vipi mhasibu, kwanza nikupe hongera zako mhasibu,unaona mambo yalivyo eeh, sasa usahahu fadhila ....’akasema

‘Tuanzeni muda ni mchache sana....’akasema yule wakili waliyeingia naye huku akifungua makabrasha yake na huku akimtizama mchumba wangu kwa mashaka, na mdada alipoona hivyo naye akamtupia jicho huyo mchumba wangu, halafu akachukua mkoba wake.

Kwenye ule mkoba wake, alitoa simu yake, na akapiga namba akawa anaisikilizia, ilionekana haijibiwi au ana maana yake kufanya hivyo, alisikiliza hivyo kwa muda, huku akiwa kaangalia pembeni muelekeo wa dirisha huku akiwa kaweka miguu yake mmoja juu ya mwingine.

‘Ok, tupo tayari...’akasema  baada ya kusikiliza hiyo simu kwa muda bila kusema neno, halafu akaizima ile simu na kutugeukia huku akibenua mdomo, na kusema kwa sauti ndogo;

‘Mambo yameiva....mzee mzima anaumbuka kiutu uzima, hakuna jinsi, ok, mimi nipo tayari...’akagauka na kutuangalia mmoja baada ya mwingine, halafu akageuka kumwangalia mchumba wangu, na kusema;

‘Kwanza kabla hatujaanza, natumai, huyu mwanamke hastahili kuwemo humu ndani...’akasema akiniangalia mimi huku akionyesha kidole kwa mchumba wangu.

‘Ndio anaondoka hamna shida, ...’nikasema nikimuangalia mdada kwa mashaka, maana ile sura aliyoionyesha sio ya kawaida, alikuwa kama askari akiwa kwenye mapambano, na mchumba wangu aliposikia hivyo, akasema;

‘Kwanini!! kwani mimi sistahili kuwemo humu,kuna ubaya gani ....?’ akauliza mchumba wangu.

‘Niambie sababu za kuwepo kwako humu ndani,...’akasema mdada

‘Kwani wewe hujui...’akasema mchumba wangu akiweka mguu mmoja juu ya mwingine,na kushika kidevu kwa zarau.

‘Mimi sijui, ndio maana nakuuliza je, una sababu gani za msingi za kuwemo humu ndani, je unafahamu ni kitu gani tunataka kukiongelea...?’akasema mdada kama anauliza.

‘Yanayoongelewa humu yanamhusu mchumba wangu, nina haki ya kuyafahamu....’akasema na mdada, akamwangalia huku akitabasamu, halafu akaniangalia mimi, halafu akageuka kumwangalia mchumba wangu, na kusema;

‘Hayo ya uchumba wako, ni huko nje, sio hapa,hapa tuna mambo muhimu sana na nyeti, ...nakuomba usipoteze muda, kazi huko imeanza, usitake tukaharibu....tafadhali toka, ili tupate nafasi ya kuongea mambo nyeti....’akasema

‘Mambo gani nyeti ambayo yanamuhusu mchumba wangu, na mimi sistahili kuyasikia, au una lako jambo....’akasema mchumba wangu.

‘Mchumba mchumba.....hahaaaae, kweli masikini akipata matako hulia mbwata,...unajiona ukitamka hivyo,..ok, ngoja sisi tuongee, tukimaliza kama bado unahitajia kuongea na mtu wako, basi mtaongea tu, lakini kwa sasa haya tunayotaka kuongea hayakuhusu, tafadhali, naomba nakuomba utoke kwa amani, nakuomba ten asana, unielewe hivyo,au sio wakili, ninafanya makosa kumtoa huyu mtu, niambie...?’akasema mdada kwa sauti ya utulivu, na kumgeukiwa wakili, na wakili akasema;

‘Ni kweli kwenye ajenda zetu hatuna mtu mwingine, mimi naona ajabu yeye kuwepo, sijui labda tumuulize mhasibu, kwanini ameongeza mtu bila ya kutufahamisha, kwani hiki kikao ni rasmi, kina wajumbe wameorodheshwa hapa, hatuwezi kuongeza mtu bila utaratibu, ....’akasema na kuniangalia mimi.

‘Anaondoka jamani, .....’nikasema nikimuashiria mchumba wangu asimame , aondoke, lakini hakutaka haat kuniangalia, macho yake yalikuwa kwa mdada

‘Kwanini mnifukuze, na huyu mwanamke ananifukuza mimi, yeye ni kama nani?’ akauliza mchumba wangu

‘Siwezi kukueleza mimi ni kama nani, haina haja,na hata nikikuambia hutanielewa, maana inavyoonekana umeshajenga hisia fulani kichwani mwako,ambazo hazina maana kwa sasa, cha muomuni ni wewe kutii sheria, kama alivyosema wakili, au sio jamani  ..?’ akawa kaam anatuuliza na mimi nikamwangalia mchumba wangu lakini yeye hakutaka hata kuniangalia mimi.

‘Msipoteze muda wenu, endeleeni, kama hataki kuwa mshiriki wa kuongea, basi mimi nitasikiliza tu...’akasema

‘Mbona huelewi....wewe mtu ni wa wapi,tunakuomba tafadhali utoke nje, tuna mambo makubwa ya kujadili hapa, ...’akasema na mchumba wangu akakaa vyema, na kuweka mikono kifuani kama vile hasikii. Mdada akaniangalia kwa macho ya kushangaa na kusema;

‘Hivi ni nani alimleta huyu mwanamke humu ndani, mhasibu umemuokotea wapi huyu mtu, mbona mkaidi hivi, tutafika hivi kweli, tufanye mambo kienyeji enyeji tu...?’ akauliza mdada akiniangalia mimi.

‘Aliruhusiwa na waheshimiwa aje anione,...na tumeshaongea, na alikuwa mbioni kuondoka ....’nikasema

‘Waheshimiwa, waheshimiwa, ....ok, sasa...?’ akawa kama ananiuliza

‘Ndio tulikuwa tunaagana na nyie mkaingia...’nikasema

‘Basi kama ni hivyo,natumai mumemalizana au sio..., anaweza kuondoka, au kama bado mnataka kuagana rasmi, basi inuka, muagane kimahaba, labda ndivyo anavyotaka, na kama bado mna  mazungumzo yenu sisi tuondoke, mkimaliza mtatuita...’akasema mdada akitaka kusimama na kumwangalia wakili.

‘Tumeshamaliza kuongea, anaondoka....’nikasema nikimuangalia mchumba wangu ambaye alionyesha kama hatusikilizi. Nikasema;

‘Tafadhali, Binti, nakuomba uondoke, tutaongea zaidi baadaye...’ nikasema na mdada akaniangalia halafu akamuangalia Binti, na binti akamuangalia mdada kwa macho yaliyojaa hasira, zarau na chuki ya wazi, na kusema;

‘Mnapoteza muda wenu bure, nimeshasema humu ndani sondoki,....kwani nikisikiliza hayo mnayoyaongea kuna ubaya gani?’ akauliza akimuangalia wakili na wakili akawa kimiya tu.

‘Kwasababu tunayotaka kuongea yameshapitishwa kuwa waongeaji ni kadhaa, na wameandikwa tayari kwenye ajenda za hiki kikao, ni mambo ya kisheria, sio ya kienyeji enyeji, sio tunajitungia, ....kwa kifupi hayakuhusu, tafadhali ondoka...’akasema mdada, sasa kipandisha sauti na kuniangalia mimi

‘Hebu mwambie huyu mtu wako atoke nje...’akasema mdada

‘Wewe mwanamke, usianze kunichefua, sio mtuu- waake, mimi ni mchumba wake..unasikia, kama ulikuwa hufahamu vyema, elewa hivyo, mimi ni mchumba wake wa halali, na ni mama wa mtoto wake...’akasema na wakili akasema;

‘Ni muhimu ukaelewa taratibu za vikao kama hivi, kuna wahusika wameshaainishwa kwenye makatasi yetu haya ya ajenda ya hiki kikao, kuwa mimi kama wakili nitaongea na nani, ....sasa wewe haupo kwenye muhutasari wetu, sio kwamba unafukuzwa tu, bali ni taratibu, na unapoakaidi, unavunja sheria, utakuwa unaleta vurugu za kikao halali...’akasema wakili kwa sauti ya busara.

‘Lakini wewe kama wakili unaweza kuja kuandika baadaye kuwa na mimi mchumba wake, nilikuwepo, hakiharibiki kitu hapo, maana kuna mambo nimeona yanayokwenda kinyume, kuna mbinu zinatumika kumuingiza mchumba wangu kwenye matatizo, na mimi nimeshazifahamu hizo mbinu,  ni lazima niwepo nisikie kila kitu...’akasema

‘Sawa tumekusikia kuwa wewe ni mchumba wake, haijalishi, chema hujiuza na kibaya hujitembeza su sio...lakini hata hivyo hata kama ungelikuwa ni mke wake hapa huna maana kwetu, kuna taratibu zimeandaliwa, kama ungelihitajika ungeliambiwa, nikuambie ukweli,  ..waliochumbiwa au wake za watu hawahitaji kusema...’akasema mdada na kumfanya mchumba wangu amuangalie kwa jich baya na kusema;

‘Nyie ndio wezi wa waume za watu, badala ya kuhangaika kutafuta wanaume wenu mnakimbilia kuiba waume za watu, unaonyesha kabisa jinsi ulivyo, aongee huyu wakili nitamsikiliza lakini sio mwanamke kama wewe, asiye na haya kabisa.....’akasema mchumba wangu akimwangalia mdada juu chini kwa macho yaliyojaa hasira.

‘Kwanza kwanini hujiulizi, kwanini uibiwe eti mume wako..hujiulizi hilo swali, ni kwanini itokee hivyo, ...’akasema mdada.

‘Si umemlaghai kwa uhuni wako, na madawa ya kumpumbaza....’akasema mchumba wangu .
‘Nikuambie ukweli,...ni kwasababu hujui wajibu wako,nyie ndio mkipata wanaume, mnaona mumefika, mnashindwa kuonyesha ni nini mwanamke afanye kwa mwanaume wake, mume anakuchoka mapema, na basi akimuona mwanamke wa nje anayejua wajibu wa mke kwa mume, anakuona wewe tena huna maana,matokeo yake nini, na huko,kuishia kulalamika, naibiwa naibiwa..., mtaibiwa sana, nikuambie ukweli,kama ungelikuwa unajua wajibu wako usingelizungumza hayo, ...’akasema mdada

‘Unaongea nini hapo wewe, wajibu, wajibu, wajibu gani ambao mimi siujui, ..na wewe utajuaje huo wajibu wa mume wakati hujaolewa,....hujui hata adabu za kuwa na mchumba au mume, wewe unachojua ni uhuni tu, hebu jiulize,umri kama huo hujaolewa, unasubiri nini, ni kwa vile una tabia mbaya...’akasema mchumba wangu na mdada akamwangalia wakili , halafu akaniangalia mimi

‘Jamani huyu mtu anatoka au sisi tutoke...maana sasa anataka kuharibu hali ya hewa’akasema mdada akiniangalia mimi, na mimi nikamshika mkono mchumba wangu, lakini mchumba wangu akaupachua na kusema;

‘Unaona anaanza kunitukana, mimi nimeharibu hali ya hewa, ...unaona wewe wakili, hizo ni kauli gani, sasa sitoki, naona anataka tuanze kupashana, .kwanza huyu mwanamke ni malaya, ni mlaghai, pili anavunja ndoa za watu, na tatu, ni muuaji, mwanga mkubwa...kazi yake kuua watu na kuwapakazia wengine...hiyo ndio tabia yako wewe mwanamke, unisikie sana, ikuogopi, na nipo tayari kwa lolote lile...’akasema akiwa sasa kasimama.

‘Umemaliza eeh, kama umemaliza nakuomba uondoke...’akasema mdada mdada sasa akiwa kamkazia macho mchumba wangu

‘Bisha kama sio wewe uliyemuua huyo mtoza ushuru, ukatumia mbinu ionekane huyu mhasibu ndiye kafanya hivyo, unabisha...wewe ni mwanga ukishirikiana na mashetani yako...unabisha kama huna shetani linalokusaidia kuwahadaa wanaume, kuvunja ndoa za watu, kila mara linahitaji damu za watu, sijui mpaka sasa umeua watu wangapi,...unatumia hadaa za kujiremba remba uonekane mrembo , una urembo gani wewe, kujichubua tu, ili kuwalaghai waume za watu....bisha kama sio kweli’akasema

‘Huna unalolijua wewe, nenda kijijini kalime....’akasema mdada, sasa akijaribu kutuliza hasira zake.

‘Sawa kilimo ni jadi yetu siwezi kukataa, huko ni kwetu ndipo nilipokulia, hamna shida nitakwenda kwa waati wangu, lakini na wewe uhuni ndio kazi yako, kuiba wanaume za watu ndo jadi yako,...ikishindikana unaua, ili shetani lako lipate kufurahia,  mwanga mkubwa wewe,mimi nikuambie ukweli,utaua lakini mwisho wa siku na wewe utakufa tu...’akasema mchumba wangu akiwa kasimama, alionyesha kukasirika, na nilihisi kama hali isipotulizwa lolote linaweza kutokea.

‘Hahaha, sasa naona unakwenda mbali....wakili, hebu, niambie nikichukua sheria mikononi mwangu hapa nitalaumiwa,....’akasema akimwangalia wakili, na wakili akageuka kuniangalia mimi, na mimi nikamwangalia mchumba wangu kwa hamaki, na mdada alipoona hakuna linalofanyia, akavuta kiti nyuma, na kusimama, akasema

‘Hivi wewe mwanamke unanifahamu mimi, ...nimekuvumilia sana...’akasema mdada, akiinuka kwenye kiti...na mimi nikaona sasa hapo linazuka balaa jingine, nikamshika mchumba wangu mkono, na kuanza kumvuta kumtoa nje, ilikuwa kama kuvutana hadi akasalimu amri. Namfahamu sana huyu binti, huwa hakubali kirahisi kushindwa.

‘Niache aje, tupambane, haniwezi kabisa huyu malaya wako...kwanini unanishika...kamshike huyo malaya wako, ...’akasema  na mimi nikatumia nguvu mpaka nikamtoa nje, na tulipofika nje, nikaanza kumuongelesha

‘Sikiliza unachofanya wewe hapa ni vurugu, ni kuniharibia jina langu, na kwa hali kama hii, mimi sitakubali, siwezi kuambiwa nimeoa mke asiye na tabia nzuri...’nikamwambia

‘Kwahiyo unataka kusema nini, kuwa mimi sina tabia nzuri, nafanya haya kukusaidia mtu kama huyo hatakiwi kubembelezwa, namfahamu sana, nimemuota sana, huyo mwanamke ni mwanga, atakuangamiza...sasa wewe unataka kusema nini, unamtetea?’ akaniuliza akiniangalia kwa wasiwasi

‘Ondoka nenda nyumbani, rudi kijijini tutawasiliana...’nikasema

‘Hivi kweli wewe unanijali mimi, badala ya kuwa upande wangu, unanifukuza, kwanza umepata cheo, unatakiwa uwe na mimi wakati unasimikwa,unalifahamu hilo,....au hulijui kuwa wakati unapewa majukumu na mimi nahitajika kuwepo kama msaidizi wako,ndivyo wanavyofanya wenzako, ni lazima uonyeshe uungwana kuwa una mtu wako, ....’akasema

‘Lakini kwanini unafanya hivyo, na hata kama ni hivyo, wewe ni mchumba wangu tu, hatujafunga ndoa bado...’nikasema na kauli hiyo inaonyesha ilimkera, akaniangalia kwa jicho baya na kusema;

‘Hatujafunga ndoa eeh, lakini umenizalisha, hiyo ina maana gani, nakushangaa sana, kusema maneno kama hayo,...badala ya kuniunga mkono, tukamkomesha huyo mwanga, unanifukuza eti nirudi kijijini, kumbe ni kweli eeh, .....’akasema

‘Ni kweli kuhusu nini?’ nikamuuliza

‘Kuwa huyo mwanamke anakuendesha kama gari bovu,..keshakufukiza madawa, hujielewi kabisa, hapo ulipo, kila anachosema yeye wewe huna ujanja unakubali tu, angalia kafikia hadi kukuweka jela, na kesi haijaisha bado unazidi kuwa mtumwa wake...hiyo kesi haijaisha kabisa wameifunika tu, ili upate hiyo kazi, wasema ndicho ulichokuwa ukikitaka, umuue, ili upate hiyo nafasi....’akasema

‘Sikiliza hayo ni maneno ya watu hayana msingi, mimi nakuomba urudi kijijini utulie huko huko,nitakuja huko tutaweka haya mambo sawa,...ukiwa hapa mjini, nahisi mtagombana sana na huyo mdada, na sipendi kashifa kama hizo...’nikasema

‘Umeoanaeeh, kuwa tutagombana na huyo mdada, ni kweli tutagombana kiukweli, mpaka umuambie mbele yangu kuwa hana lolote, mimi ndiye mchumba wako wa halali, ....kwanza jiulize kwanini tugombane naye kwa vile ni mke mwenzangu au sio?’akaniuliza huku akiwa kashika kiuno

‘Nani kasema mambo ya mweka mwenzako hapa, mbona hunielewi,....sikiliza sasa naongea kwa mara ya mwisho, ondoka rudi kijijini,...’nikasema na kuanza kutembea nikimuacha akiwa kakasirika, na yeye akasema;

‘Mimi kijijini sirudi, nimeshaongea na baba, kuwa niwepo kipindi ukisimikwa hicho cheo, ni lazima niwepo kama mtarajiwa wako...’akasema akionyesha kutaka kurudi huko ofisini.

‘Sawa muda ukifika nitakuita uje, hilo mbona halina tatizo....sioni ni kwanini tuanze malumbano yasiyo na tija, wewe rudi huko kijijini, tumalizane na haya yaliyopo mbele yetu,nakuomba sana  usilete ubishi usio na maana, utaharibu kila kitu, achana kugombana na mdada, ....’nikasema

‘Kwa mtaji huo bora niharibu, na nakuambia kiukweli, nitaharibu kweli kweli usiponijali mimi, kwanza ngoja nikutane na huyo mwanamke wako, ameshanionyesha dharau na kiburi, sasa ni vyema tupambane naye anifahamu kuwa mimi ni nani....’akasema

‘Halafu utapata faia gani kwa kufanya hivyo?’ nikamuuliza

‘Mimi sipendi shari, ni mvumilivu sana, nimevumilia mangapi huko kijijini,....nimeambiwa mangapi huko kijijini, nikayavumilia,...lakini hizi zarau za huyu mwanamke, sitaweza kuzivumilia keshanipandisha hasira, atanijua kabila langu ni nani...’akasema akichezesha chezesha miguu.

‘Nisikilize ninachokuambia, usiponisikiliza mimi, nitayaachia yende yawavyo, na wewe utakuja kuumia, na kukosa kila kitu...’nikasema

‘Ni bora nikose, lakini tukose wote, mimi sijali, lakini kwanza ni lazima nimkomeshe huyo mwanamke wako...unanisikia, nenda mkaongee, lakini ujue kuwa mimi namsubiri huyo mwanamke wako hapa nje,, kwasababu hajui ulichonifanyia mimi, wewe si umeniharibia maisha yangu, umesahahu kwasababu ya hicho kinyago,...nimevumilia vya kutosha, sasa basi....’akasema na kuegemea ukuta kuonyesha kuwa haondoki hapo.

‘Kwahiyo unataka kusema nini, hutaki kuondoka sio, ....?’ nikamuuliza na yeye akaniangalia na kusema;

‘Namsubiri huyo mwanamke wako hapa nje...wewe nenda mkaongee,lakini mimi hapa sitoki.....’akasema na mimi nikaona napoteza muda nikachukua simu na kumpigia baba yake.

‘Mzee, Binti yupo hapa analeta vurugu, ...’nikamwambia

‘Analeta vurugu....., analeta vurugu gani, hebu nipe simu niongee naye...’akasema na mimi nikampa simu huyo mchumba wangu, kwanza akaniangalia kama vile hataki kupokea, akauliza;

‘Simu ya nini, hata kama ni polisi mimi sitoki hapa....’akasema

‘Ongea na baba yako...’nikasema na aliposikia baba yake, akaipokea kwa haraka na akaanza kuongea naye, kwanza alimsikiliza baba yake akionega kwenye simu baadaye  akasema;

‘Baba huyo hawara yake yupo naye, na kwa kauli yake mwenyewe, huyo mwanamke,inaonyesha kuwa wana mahusiano na huyu mchumba wangu, sasa huoni nikiondoka hapa nitakosa muda wa kuongea naye, ni lazima nipambane naye....’akasema

‘Wapi,....kwani wewe upo wapi,?’ akauliza akionyesha mshangao.

‘Lakini ulisema umerudi nyumbani kijijini,....’akasema kwa mshangao

‘Oh, kwanini, kuna nini kimetokea?’ akauliza na sasa akawa ananiangalia mimi kwa mashaka

‘Baba ....una uhakika na hilo ...wamekugeuka,...akina nani?’ akauliza huku akisikiliza kwa muda halafu akaniangalia wa jicho baya, akasema;

‘Msaliti mkubwa wewe..utaona.....’akanipa simu yangu na kuondoka kwa hasira

NB: Kuna nini  hapa tena:

WAZO LA LEO:Hasira kwa binadamu wakati mwingine hazikwepeki, inatokea hali kama hiyo ukakutana nayo. Unapoona hali hiyo inakujia, jaribu kutafuta njia za kuituliza, ni muhimu kuwa makini sana kwa hali ilivyo sasa,, kwani unaweza kufanya jambo ambalo utakuja kujijutia baadaye au hata kushinikiza mapigo ya moyo, na kuleta athari mwilini.

 Cha muhimu, tuliza kichwa chako kwanza, fikiria kwa makini unachotaka kukifanya, kabla hujachukua maamuzi, ikiwezekana ni bora ukalikwepa eneo la tukio, ukaenda sehemu nyingine ukatulia kwa muda, kumbuka hasira ni hasara.



Ni Mimi: emu-tatu

No comments :