Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, March 19, 2014

BAADA YA DHIKI FARAJA-29




Niliposikia bosi anataka kuongea na mimi nikaanza kuhisi owoga fulani, na moyoni nikawa nikijilaumu, kwanini nakuwa mwepesi sana kumkubalia mdada, hata kaam naona ni kujiweka kwenye matatizo.

Nilijua bosi anaweza akakata tamaa ya kunisaidia na huenda asiniamini tena, na kwa mtaji huo, huenda hata kibarua hakipo tena, kwani bosi kajitahidi kunitafutia wakili, lakini sikuweza kutoa ushirikiano,na kesi yenyewe ni mauaji, huenda ikachukua muda
Kwa mkono wenye kusita,nikaipokea ile simu kutoka kwa wakili, halafu nikaiweka hewani, nikaanza kwa kusema;

‘Habari za saizi bosi...’nikasalimia nikionyesha kuchoka na kukata tamaa.

‘Habari nzuri kiasi, mtoto wangu anaumwa, imebidi nimuhangaike kwenye hospitali kubwa, huko mjini, bado nipo huku  mjini huenda nikarudi kesho au keshokutwa, ndio maana ukaniona nipo kimiya....’akasema

‘Hkuna shida bosi...nakuamini sana huwezi kunitupa...’nikasema

‘Ndio maana sijaweza kuja kukuona, lakini hata hivyo, niliacha maagizo yote kwa wakili wetu huyo, nikijua ataweza kukusaidia ili kwanza upate dhamana, ambayo ni muhimu kwa afya yako, unafahamu huko gerezani kulivyo, ...lakini pia ni kuangalia jinsi gani kesi ilivyo, kupata ukweli wote, ili aweze kukutetea,...’akatulia kidogo

‘Lakini cha ajabu nashangaa kusikia wakili akisema hutaki kutoa ushirikiano, akama anavyokuuliza, hebu niambie tatizo lipo wapi?’ akaniuliza

‘Bosi mimi nimejitahidi kumuelezea jinsi ilivyokuwa, lakini naona kama haniamini, na mimi sijasema jambo la kuonyesha kuwa sitoi ushirikiano, nikijua kuwa mimi ndiye nahitaji msaada...mimi sijui anataka nimwambia nini zaidi....’nikasema

‘Yeye kama wakili anahitajia kufahamu kila kitu, ili aweze kujua ni jinsi gani ya kuiingilia hiyo kesi,hasa chanzo cha hayo yote, anahisi huenda unafahamu mengi, lakini unaogopa kusema,...kajaribu kukuuliza baadhi ya maswali anayohisi huenda yana chachizo la hayo mauaji, lakini hutaki kumuelezea, sasa atawezaje kukusaidia vipi kwa hali kama hiyo...?’ akauliza

‘Bosi mimi ndiye niliyekuwepo humo ndani,japokuwa sikuona jinsi gani huyo muuaji alivyompiga risasi marehemu, na nimemuelezea yote hayo, lakini yeye anang’ang’ania nimuelezea mahusiano yangu na mdada, kama nina kazi niliwahi kufanya naye....yaani anayoniuliza ni mbali kabisa na tukio lenyewe, nahisi ana ajenda ya siri na mdada....’nikasema

‘Unahisi ana ajenda gani ya siri na mdada!?’ akauliza akionyesha mshangao

‘Nihisia tu, kwa jinsi anavyouliza maswali yake, nahisi, kuwa pengine wanamsuguano yeye na mdada, na huenda wakili huyu anataka kunitumia mimi kufahamu mengi kuhusu mdada, kitu ambacho mimi sijui, siwezi kujua kila kitu kumhusu mdada, na kwanini aniulize maswali mengi kuhusu mdada, kwani yeye ndiye muhusika mkuu...?’ nikauliza

‘Wewe na mdada ndio wahusika wakuu ndio, ndio maana polisi wamewashika nyie, kwahiyo ni muhumu kuwafahamu, nyendo, na tabia zenu, huenda katika mahusiani yenu kuna kitu mnakifahamu kinachoweza kuufichua ukweli...kwanini uogope kusema kile anachokuuliza...’akasema

‘Sijaogopa, nisichopenda ni jinsi anavyonitaka niongee kila kitu, ....mengine naona ni mambo binafsi...’nikasema

‘Kila wakili ana njia yake ya kuliingilia tatizo, huenda yeye kaona njia iliyorahisi ni kupitia kwa mdada, kumfahamu , ili ajue ni kwanini huyo marehemu alifika hapo, kwanini aje na bastola,...hata mimi hapo naona kuna hoja...’akasema

‘Ndio maana nikamuuliza anijulishe ni kipi ni muhimu kwa ajili hii kesi, kama ni hivyo, basi nitamuambia yale ninayoyafahamu kuhusu mdada, na siwezi kumuambia yale nisiyoyafahamu, ....’nikasema

‘Nikuulize kwanini mdada anataka kukutafutia yeye wakili?’ akaniuliza

‘Mhh, yeye anasema kwa vile hilo tukio limetokea wakati tupo tunamsaidia, na yeye anataka kulipa fadhila kuhakikisha haki inatendeka, ndio akaona anitafutie wakili mzoefu wa mambo hayo,...nilishamkatalia,..lakini akasisitiza kufanya kutaka kufanya hivyo...mimi ningefanyaje..’nikasema

‘Kwa hali hiyo, basi mimi itabidi nimtoe wakili wetu, ..sioni haja ya kugonganisha watu, mimi namuamini sana huyo wakili wetu, kwa sababu pamoja na mengine ni mtu anayejua kutunza siri, nimefanya kazi naye kwa muda mrefu, na hutaamini, hajawahi kuniangusha...’akasema

‘Yeye ni wakili wa maswala ya kazi na sheria za kazi, au sio ..na...’akanikatiza

‘Na hapo ndio maana nakuambia huyu mtu ni msiri sana, keshawahi kufanya kazi za kesi hizo za mauaji, na hakuna kesi aliyowahi kushindwa, kwasababu msimamo wake, ni kujua ukweli wa tukio, na akishalijua anakushauri kuwa kesi hii ipoje, na inawezekana kutetewa vipi....hachukui kesi kwa kutafuta pesa tu, lakini pia analinda heshima ya kazi yake...’akasema

‘Ina maana pia ana utaalamu wa kesi za mauji?’ nikauliza

‘Ndio kitu alichosomea awali, lakini kwa vile alitaka kumrizisha mzazi wake, akaacha hicho alichosomea na kujikita kwenye mambo ya sheria za kazi...lakini kesi za mauaji ndiyo fani yake...’akasema

‘Oh, mimi nilikuwa sijui, hata mdada halijui hilo ndio maana akataka kumtafuta mtu aliyebobea kwenye fani hiyo, ya kesi za mauaji..’nikasema

‘Mdada ana ajenda yake ya siri,...nimejaribu kumpigia simu, lakini kazima simu yake, nahisi hataki kuongea na mtu,...sasa uamuzi ni wa kwako, je unamataka wakili huyu, au unasubiria wakili wa mdada...nakuachia wewe hiyo kazi hadi kesho, .....’akasema

‘Sasa bosi ukisema hivyo unaniacha kubaya kwani, mpaka sasa wakili ninayemfahamu ni huyu uliyenisaidia, nijuavyo mimi, mdada alitoa hilo kama ombi tu la kunisaidia akijua kuwa huenda wakili wetu huyu hana uzoefu wa kesi kama hizi za mauaji. Mimi naona leo akinipigia simu nitamuhakikishia kuwa huyu wakili wetu anaweza kunisimamia bila matatizo, nafikiri atatuelewa...’nikasema

‘Hilo nakuachia wewe....na sijui kama mdada anajua hayo zaidi yangu, msijidanganye,...kumbuka hiyo ni kesi ya mauaji, sio mchezo wa kuigiza, utakuja kujuta siku ukisikia unahukumiwa kifungo cha maisha kama sio kunyongwa,....’akasema bosi na kunifanya moyo unilipuke

‘Bosi usiseme hivyo, kweli naogopa sana, nakutegemea sana wewe bosi...’nikasema

‘Haya wewe nipo huyo wakili niongee naye.....’ akasema na mimi nikagonga meza kumpa ishara wakili huko nje alipo kuwa aje, na haikuchukua muda akaingia na kuuliza

‘Vipo umemaliza kuongea na bosi wako?’ akaniuliza

‘Bosi anataka kuongea na wewe...’nikasema na kumkabidhi simu, akaishika na kuiweka sikioni, halafu akasema

‘Mbona hayupo hewani,...’akasema na kuanza kumpigia, lakini ilionekana kama simu ya bosi haipatikani , akajaribu tena na tena, lakini haikupatikana

‘Inaonekana simu yake imekwisha chaji, sasa, kwa hali ilivyo, mimi nitaondoka, na kesho nitawasikiliza nyie, vinginevyo, nitajua kuwa sihusiku katika kuisimamia hii kesi, nijipange kwa ammbo mengine...’akasema

‘Tumeongea na bosi wewe ndiye utasimamia hii kesi yangu...’nikasema

‘Ni hapo utakapokubali kuniambia ukweli wote...’akasema

‘Nitakuambia, ukweli kuhusiana na tukio zima, na sijui kuna kitu gani sijakuambia, labda tuende kwa mtindo wa maswali, ili niweze kukumbuka zaidi...’nikasema

‘Vyote ni sawa, cha muhimu ni kuhakikisha unaongea ukweli wote, na mimi nilitaka kuanzia kwenye mahusiano yako na mdada, kwani tukio lilivyo, inaonekana marehemu alikuja kwa nia ya kukutana na mdada, kwanin...kuna nini kilikuwa kinaendelea, je wewe  unahusikana vipi na mdada, unafahamu lolote..ndio lengo langu...’akasema.

‘Kama ni hivyo mbona nimeshakujibu, ....’nikasema

‘Hayo tutayaona kesho, sasa nakwenda kuonana na watu wangu, najua wameshapata taarifa za kutosha kutoka huko polisi, na asubuhi nitadamkia kukupigania, upate dhamana, hilo ni muhimu sana, vinginevyo watakupeleka gerezani, na huko sio kuzuri sana...’akasema

‘Naomba tafadhali jitahidi kufanya hivyo,..’nikasema

‘Yote inategemea wewe, kuna jamaa yenu mmoja wa pale ofisini, kulitokea wizi nilimwambia hivyo hivyo, aniambie ukweli, kuhusu anavyowafahamu hao watu anaofanya kazi nao,...yeye kwa ujumla alikuwa hahusiki, lakini kwa vile alikuwa kitengo hicho na siku hiyo alikuwa zamu, akajikuta anaunganishwa kwenye hiyo kesi,...

‘Nilimshauri sana, kuwa ili niweze kuimaliza hiyo kesi ni muhimu nifahamu nyendo na tabia za watu anaofanya kazi nao, maana wizi, mauaji, hayaji kwa bahati mbaya, mara nyingi ni vitu vya kujipanga, ...labda iwe ni ajali tu...akajifanya hafahamu, kumbe anafahamu

‘Hapa na hapa akajikuta yupo gerezani, alikaa wiki mbili, alipotoka hutaamini, alikuwa kaisha, na wiki moja baadaye akaanza kukohoa, kifua kikuu kikamuandama, ...huyo jamaa alikwenda kuponea kwao, ....ilikuwa akribu tumzike...sasa nikuambie ukweli, gerezani sio kuzuri, ...’akasema

‘Tfadhali nakuomba sana, nisaidie, nisiende huko...’nikasema huku nataka kupiga magoti

‘Yote inategemea wewe, ninachotaka kutoka kwako, ni kuniambia ukweli kuhusu mdada, nyendo na tabia zake, pili kuhusu marehemu, na tatu, wewe ulikuja vipi ukawa karibu na mdada....na tukio la siku hiyo itakuwa ni kumalizia tu....ni kazi rahisi je upo tayari...?’ akaniuliza na kabla sijamjibu simu yake ikaita, na kwa haraka akaipokea

‘Nani mwenzangu?’ akauliza

‘Mdada, unataka nini tena?’ akauliza na akawa anasikiliza kwa muda, bila kusema neo na baadaye akageuka kuniangalia na kusema;

‘Mdada anasema keshampata wakili ambaye ataweza kusimamia kesi yako, na anakuja kesho asubuhi kuonana na wewe.....’akaniambia

‘Lakini....’nikaanza kusema

‘Sikiliza nikushauri kitu, nafahamu hali uliyo nayo kwa sasa, sasa nakushauri hivi,wewe usikatae moja kwa moja ....., kesho akija huyo wakili aliyemtafuta mdada, kwanza jifanye kama unamkubali, uone anataka kukuhoji nini, ...uwe na akili ya haraka ya kutafakari...’akasema na kunifanya nimwangalia moja wa moja usoni.

‘Uwe makini sana na maswali yake, na akimaliza mwambie unahitajia muda wa kufikiria, nikija mimi utaniambia ni kitu gani kakuhoji, nitajua lengo lao ni nini, sasa hapo na mimi nitakushauri je uendelee naye au vipi,....’akasema

‘Lakini kwanza nataka kufahamu je wewe kweli upo tayari kunisimamia kwenye hii kesi?’ nikamuuliza huku nikimwangalia kwa makini na yeye akiwa haonyeshi dalili yoyote usoni, akasema;

‘Mpaka nisikie na kujua ukweli wote, kama nilivyokuambia,.... kwa hivi sasa siwezi kukupa jibu la moja kwa moja, kwani nimeshaanza kuingiwa na wasiwasi na jinsi gani unavyonificha mambo muhimu...nahisi kuna kitu unaficha, ambacho kinahusiana na hayo mauaji, na hiyo ni hatari sana kwako...’akasema

‘Sio kweli, ...sikufichi kitu muheshimiwa, ....mengine unayoniuliza ni mambo yangu binafsi,ambayo sio lazima na nina uhakika hayahusiani na hii kesi..’nikasema

‘Na kama ni mambo binafsi,na yana mahusiano na mdada, nahisi, huenda ndio chanzo cha hayo mauaji, ...’akasema

‘Kwanini unasema hivyo...?’ nikauliza kwa mshangao.

‘Mdada ni mtata sana...nimeshakuambia mimi namfahamu sana, hata hivyo ni binti mjanja sana, anafahamu kuuma na kupilizia...na huwa hafanyi jambo bila malengo, na faida,...sijui kwa hili alikuwa na malengo gani....’akasema

‘Maisha ya mdada, au maisha yangu binafsi, yanaingilianaje na hayo mauaji, mimi ina uhakika hayahusu kabisa hayo mauaji,...niamni hivyo....’nikasema

‘Wewe unasema kwa kukwepa jambo, lakini mimi nikifahamu hayo ninayokuuliza,nitaweza kujua undani wa hili jambo,ninahisi kuna kitu kilichosababisha hayo mauaji, na hayo mauaji hayakutokea kwa bahati mbaya, kuna sababu kubwa iliyofikia hapo, ....nakuambia hili kwa manufaa yako, namfahamu sana mdada, nahisi kuna kitu anataka kisijulikane, ....kwahiyo mimi naondoka, nasubiri maamuzi yako , hiyo kesho...’akasema na kuanza kuondoka na baadaye akakumbuka jambo na kusema;

‘Ukumbuke pia polisi wa upepelezi anataka kukuona hiyo kesho....’akasema na kunifanya nizidi kuishiwa nguvu.

`Mhhhh...’ nilipumua kwa muda nikijinyosha, na hatimaye nikaingia kwenye chumba cha mahabusu, na nilivyokuwa nimechoka, nikashikwa na usingizi mzito,....na asubuhi iliingia kama mchezo, na askari akaja na kusema;

‘Kuna mgeni wako....’nikajua ni huyo wakili wa mdada

NB: Je wakili yupi ataweza kunitetea


WAZO LA HEKIMA: Maamuzi ya hekima ni yale yanayolenga ukweli na haki, pia busara na hekima ya kulitatua hilo jambo. Siku hizi, ushabiki, ubinafsi , na masilahi ndio unaotawala maamuzi ya watu hata katika sehemu nyeti, ambazo zinahitajia utaalamu wa hali ya juu. Tuwe makini na hili, kwani unachofanya leo, ujue kinaweza kuathiri mustakabali wa kizazi hadi kizazi, na historia itakuja kukuhukumu.

Ni mimi: emu-three

No comments :