Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, March 18, 2014

BAADA YA DHIKI FARAJA-28


‘Mdada anataka kuongea na wewe kwa kupitia kwa wakili wake,...na anataka muongee naye kwa siri, kama alivyoniambia wakili wake, mimi namwamini sana wakili wake, kwani ni mwalimu wangu, ...sasa kazi ni kwako,...’akasema na kunikabidhi simu yake, na yeye akatoka na kuniacha peke yangu, nikaiweka ile simu hewani na kwanza nikasema

‘Mdada unaendeleaje?’ nikauliza huku nikiwa na hamasa ya kusikia sauti yake, ilikuwa kama vile ni mtu mwenye kiu na maji yake ni sauti ya huyo mdada.

‘Usiwe na shaka na mimi,...muhimu ni hili ninalotaka kukuambia, unisikilize kwa makini...’akasema na mimi nikatulia

‘Kwanza hakikisha kuwa upo na mimi,...ninachoongea mimi kiwe sawa sawa na unachoongea wewe,unanielewa hadi hapo?’ akauliza na mimi nikaguna hata sikujua niseme nini.

‘Na ili iwe hivyo, uache kabisa kupanua domo lako kupita kiasi, elewa lugha yangu hiyo, elewa kuwa ukiropoka ovyo, mimi sipo na wewe tena..., kama ulivyosikia, mimi sina lolote kuhusu hayo mauaji,...sikujijua na sijui kilitokea nini,...hilo linajulikana sio dhamira yangu, japokuwa sizani kama mimi ndiye niliyefanya hayo mauaji,....’akasema

‘Nasema sizani, kwani,nisingeliweza kufanya hivyo, halafu nijipige kitu kichwani kwa nyuma, na kupoteza fahamu,..., dakitari wangu atathibitisha hilo,na muda wa kilichotokea ni muhimu sana, muda ndio ngao yetu...’akatulia.

‘Sasa wewe ukifungua domo lako na kusema mambo yasiyokuwepo, utajikuta unaingia matatani, mimi nafikiria sana kuhusu wewe kuliko mimi, ....’akatulia kidogo.

‘Kinachojulikana ni hivi, huyo mtu alikuja kwangu akitaka nimlipe pesa zake za gari, wewe hulijui hilo, ....na nilishangaa alipoingia na wewe akiwa kakuwekea bastola nyuma, sasa sijui kwanini alifanya hivyo, na sijui kwanini alitaka nimlipie nyumbani na sio kazini kwake, hayo wewe huyajui, hujui chochote,...unanielewa...?’akatulia

‘Nilikubali kufanya hivyo, kuwa akija nitamlipa pesa yake, ...kama watafutailia maongezi yangu kwenye simu watasikia hivyo, ....sasa kinyume na nilivyotaajia, kuwa anakuja na mzigo wangu, ambao ni pesa, yeye akaja na silaha, akiwa kakunyoshea wewe, mimi 
nilipoona hivyo ndio hasira zikanishika, nikabadilika, na kilichotokea baadaye mimi sijui...hapo unaachiwa wewe uwanja wa kuongea....uwe makini sana hapo’akasema

‘Sasa mimi hapo nitaongea nini, maana ulipobadilika hukuwa na urafiki na mtu hasa mwanaume, ukaanza kunivamia na mimi, nikakimbia,...nilipopata fahamu, kwani kuna kitu kilinigonga na kupoteza fahamu sijui ni nani ...ni wewe ulinigonga?’ nikauliza

‘Hicho kitu nilikipata wapi, unakumbuka nilikuwa na kitu mkononi, kabla ya hapo...sijui, na sikumbuki kuwa na kitu, ambacho polisi wanasema ni kitu kama nondo, je uliniona nikiwa na nondo humo ndani,...?’ akauliza

‘Hapana kwa kumbukumbu zangu sikukuona na kitu kama hicho, na ...’nikatulia nikijaribu kukumbuka

‘Ueleze kilichotokea, kwani hukumbuki kulitokea nini,wakati huo..?’ akaniuliza

‘Ndio hivyo najaribu kukumbuka...’nikasema

‘Sasa sikiliza sema ulivyoona, sio ulivyosikia, au wanavyotaka watu useme, usilishwe maneno, hapo kila mtu ana dhamira yake, na huenda wengine wana lengo la kunimaliza,..’akasema

‘Kwanini...?’ nikauliza

‘Kwanini, kwanini...haina haja kwa sasa, cha muhimu hadi hapo, mimi na wewe hatufahamu kitu, usiongee sana, kuongea kwako sana, kunaweza kukuponza. Unasikia wanaofahamu zaidi ni mimi na wewe kwasababu ndio tuliokuwepo humo ndani, sasa wasikudanganye watu useme watakavyo wao...unanielewa hapo?’ akawa kama anauliza

‘Ndio hivyo nataka niwaambie ukweli, ...’nikasema

‘Ukweli eeh, sema ukweli, usiohatarisha maisha yako ya baadaye, ukijikanyaga, kitanzi kipo shingoni mwako, mengine ya nyuma, mimi siyajui, na wewe huyajui, au kuna kitu unafahamu, ambacho mimi sikijua, kama kipo niambie?’ akauliza na kabla sijajibu akasema

‘Jibu ni kuwa hufahamu chochote au lolote...sawa...sasa ropoka ukaozee jela, mimi sipo, mimi nina kinga, je wewe unayo, jiulize mara mbili kabla hujaropoka...’akasema

‘Pili, kama huna wakili mwaminifu useme,mimi naweza kukutafutia wakili atakayeweza kukulinda, mimi nawafahamu wengi tu, hakikisha wakili wako sio mbabaishaji wa kukulazimisha kuongea kila kitu hata kama hakihusiki...umenielewa, usiogope kutishiwa jela, wewe ni mwanaume bwana...’akasema

‘Huyu niliye naye ni wakili anafahamu zaidi yangu ni wajibu wake kuniambia kipi nimueleze na kipi nisimueleze, na hapa alipo hajui tukio lilivyokuwa, natakiwa nimueleze ilivyokuwa, ...’nikasema

‘Inategemea....sikiliza usiongee kila kitu, mengine yanahusu nini, nafahamu kabisa hao watu , wengine lengo lao ni kukuchimba kwanza ili baadaye aje kukuweka mikononi mwake...mimi nawafahamu sana hao watu, sio kila kitu unahitajika kuwaambia, utakuja kuumbuka baadaye, ....’akasema

‘Kwahiyo...unataka niseme nini..?’nikauliza na yeye akasema;

‘Una maana gani kuniuliza hilo swali, wewe mjinga kweli, unataka nikufundishe cha kusema, ..nimeshakuambia uwe makini, usiropoke kila kitu ambacho ni siri za maisha yako, ambayo usingelipenda kuyaongea, ongea yale yanayohusiana na hiyo kesi, na kesi iliyopo mbele yetu ni ya mauaji, ni nani kaua,ulionaje, alikuja kujaje ...mengine hayawahusu, unanielewa..?’ akasema

‘Mhhh...lakini...’nikataka kusema na yeye akasema;

‘Kazi ya muhimu ni kumtafuta huyo aliyemuua huyo jamaa,...kumpata kabla hawa askari hawajakata tamaa, maana wakikata tamaa, wanaweza kukubambikia kosa ambalo sio lako,...mimi nina uhakika, huyu mtu aliyefanya hivyo ni mmoja wa watu wenye nia ya kunimaliza, na mimi natakiwa kumgundua ni nani mapema iwezekaanvyo,...’akasema

‘Watu gani hao,ina maana kuna watu wanaotaka kukumaliza kwanini na ni akina nani? Nikamuuliza

‘Hilo halikuhusu, mimi nina wapinzani wengi, wasiotaka maendeleo yangu, natakiwa nipate muda wa kuwachuja, nitawapata tu,...’akasema

‘Ina maana wewe hukumuona huyo mtu aliyeingia na kufanya hivyo...?’ nikamuuliza

‘Ningemuonaje, siwezi kukumbuka kilichotokea baada ya mimi kubadilika, I wish ingelikuwa hivyo,....huyo mtu inawezekana alipoingia, alijua sehemu ya kunipata ni kunigonga kichwani, akaniwahi, nahisi alinipiga na kitu kizito kisogoni, kama walivyosema kuwa ni chuma kama nyundo nzito,...nikapoteza fahamu, ...ningemuona asingeliniweza,...naapa nitampata tu, na nikimpata nitambeba juu kwa juu hadi kwa hao polisi...’akasema akionyesha hasira, nikaogopa asije akabadilika, japokuwa sikuwa karibu naye.

‘Mbona polisi wanasema bastola ina alama za vidole vyangu na vya kwako, na mimi sikumbuki kabisa kuishika hiyo bastola,...?’nikamuuliza.

‘Hapo na mimi ndipo ninapojiuliza, ...huyo mtu alichofanya ni kuhakikisha kuwa alama za vidole zangu na zako zinabakia kwenye hiyo bastola,....ni ujanja wa kijinga, kwasababu hata polisi, hawawezi kukubali hilo kirahisi,...kama kweli mtu alikuwa na nia ya kuua...’akasema

‘Kama ni hivyo kwanini wamenishikilia mimi..?’ nikauliza

‘Huenda ni kwa usalama wako...’akasema

‘Kwa usalama wangu, kwa vipi?’ nikauliza kwa mshangao

‘Huwajui hao watu,...hawafanyi kosa, hukutakiwa uwe hai, ....hata mimi siku zangu zinahesabiwa, kama wataona sina umuhimu nao tena.....sema na mimi sio mchezo , kama wamenikosa hapo, hawanipati tena.....’akasema

‘Inaonekana unawafahamu hao watu...?’ nikauliza

‘Ningeliwafahamu ningelishawamaliza....lakini dawa yao inachemka, iogopi kufa, ila kabla sijafa, nitahakikisha na wao wameonja kifo..’akasema

‘Mhh, kwahiyo ....wanakata mimi nisote jela, hata kufungwa kwa kosa nisilolifanya kwanini?’ nikauliza

‘Ndio lengo lao hilo, ili uwe hatiani, ionekane mimi na wewe ndio tuliofanya hivyo,...sasa ndio maana nakuambia uwe makini na maelezo yako, mimi nitafanya uchungzi nitamgundua huyo mtu kabla kesi haijaanza, nakuhakikishia hilo..’akasema

‘Una uhakika gani?’ nikamuuliza

‘Usijali, hiyo kazi kwangu ni ndogo sana, nasubiri kibali cha hawa watu, maana wananilinda utafikiri mimi ni jambazi, wangelijua wasingelifanya hivyo ....lakini usimwamushe alieyelala, maana akiamuka mtu kama huyo, hujui itakuwaje...umenisikia, huyo wakili wako ni nani?’ akaniuliza

‘Yule wakili wetu wa kampuni...’nikamwambia

‘Ohooo, ...yule na kesi ya mauaji wapi na wapi, yeye ni mtaalamu wa sheria za kazi, na utawala, lakini anyway, labda anataka kupanua wigo wake,....okey ngoja mimi ,nitaongea naye,kama ni huyo, nitajua jinsi gani ya kumweka sawa ...’akatulia kidogo nahisi alikuwa akiongea na mtu halafu akasema;

‘Cha muhimu, uwe makini na huyo jamaa ni mjanja sana, kwa watu kama nyie,....umenielewa eeh?’ akauliza na mimi nikaguna halafu yeye akasema

‘Umenielewa, kama hujaelewa niambie...au una lolote la kusema?’akasema na mimi nikamuuliza

‘Hii ni kesi ya mauaji, na kwa maelezo yako ni kama wewe unataka kuvuta muda, bila kujua kuwa mimi nipo rumande na sasa nasubiria kwenda, gerezani, na hapo ina maana mimi ndiye nitakayepata shida kwa vile wewe unachukuliwa kuwa hukuwa unajua ni nini kilitokea kutokana na matatizo yako,...’nikasema

‘Kwahiyo wewe unaogopa kwenda jela huogopi kwenda kunyongwa eeh, juhudi ninayofanya kwa sasa ni kukuokoa wewe na kitanzi, kunyongwa au kufungwa maisha, hiyo ya kwenda gerezani kwa muda sio tatizo kwa sasa...wewe ni mwanaume, ukomae, unafikiri maisha ni lele mama eeh, masikini mhasibu...’akasema kwa sauti ya kunibeza.

‘Mimi hapo sikuelewi, unasema nisiropoke kwa wakili wangu, na kwa hali hiyo ina maana nitashindwa kumwambia yote ambayo huenda yakamsaidia katika kazi ya kunitetea mimi,...hapo unaniweka pagumu nashindwa kuelewa ni nini na kipi nisimwambie, na yeye kama wakili anahitajika kujua kila kitu, ili ajue jinsi gani ya kunitetea,..au sio?’ nikamuuliza

‘Sikiliza wewe mtu, hakuna kitu kama hicho, kuwa umwambie wakili wako kila kitu, kwanini umwambie kila kitu, wakati wewe mwenyewe kwa akili zako unafahamu hiki kinahusiana na hiyo kesi na hiki hakihusiani, je unamwamini vipi kuwa ataweza kulinda masilahi yako mpaka mwisho, huyo huyo anaweza kukugeuka baadaye..je yeye na baba yako mkwe hawajuani,...uwe makini.’akasema.

‘Hapo unaniweka pabaya,...mpaka sasa sijajua msimamo wangu ni upi, na wakili wangu ndiye anayeweza kunisaidia, ...’nikasema

‘Hivi wewe mtu hujanielewa,...cha muhimu ni kuwa makini , usiropke ovyo, sina la kukuambia zaidi, akili kichwani kwako, kama unataka uozee jela, na huku mchumba wako akikusuta na kululaani kwa kumharibia maisha yake, na hapo hapo baba mkwe wako akitamani asikuone tena katika maisha yake wewe, ropoka ovyo, ....niamini mimi nitahakikisha upo salama....’akasema na kukata simu.

Nilikaa kwa muda nikitafakari, huku nikimuwazia huyu mtu, je ni huyo huyo mdada niliyesikia kuwa yupo mahututi, kwa jinsi alivyokuwa akiongea hapo haonyeshi kabisa kama alikuwa na hali mbaya.

Baadaye wakili akaja, na kuniangalia kwa muda, halafu akasema;

‘Nafikiri mdada keshakugeuza mawazo yako maana huyo mdada namfahamu sana ni mjanja kupita kiasi, lakini hili tatizo lililopo mbele yako,sio la ujanja-ujanja, ujue hii ni kesi ya mauaji, hauna ujanja wa kuongea .....ujanja wake ni kuwa na ushahidi utakaokuweka mbali na tukio hilo,...sasa ni wakati wa kulifikiria hili kwa makini, je utamsikiliza huyo mdada, ambaye kwa jinsi ninavyomfahamu atakuwa na malengo yake, ujue na yeye ni mshukiwa kwahiyo hapo alipo, anatafuta njia ya kuitetea nafsi yake...je una uhakika ana uwezi wa kutetea na nafsi yako?’ akaniuliza.

‘Mimi sijui, na kiukweli mimi simuelewi kabisa mdada...’nikajikuta nikisema

‘Ndio hivyo,..kwani kakuambia nini?’ akaniuliza na mimi kwa haraka nikasema;

‘Alichoniambia yeye ....eeh, ni kujaribu kunikumbusha yale yaliyotokea mle ndani,na yeye akataka kujua ni kitu gani kilitokea baadaye, baada ya kuanza kuchanganyikiwa, kwani hapo hakumbuki kama unavyomfahamu akichanganyikiwa anavyokuwa, huwa hawezi kukumbuka ni kitu gani kinatokea kwa muda huo aliochanganyikiwa...’nikasema.

‘Mhasibu ujue hii ni kesi ya mauaji, sio rahisi kihivyo, mdada hapo alipo anahangaika kujiokoa, na usizani ataweza kuangalia mstakabali wake na wako kwa wakati mmojO.Nikuambie ukweli, yeye hapo alipo hajijui hatima yake itakuwaje,kuwa hivyo kuwa ana matatizo ya akili sio tija, kunahitajika ushahidi wa hali ya juu, ili aweze kujiokoa, na kukubalika kwa hakimu...sijui kama unaliona hilo kwa mapana yake, au unafikiri hii ni kesi ndogo ndogo tu,...’akasema

‘Naliona hivyo,...na ninaogopa kweli, lakini unataka mimi niseme nini, nikiri kosa ambalo sijalifanya, au unataka niseme nini, hebu niambie maana labda mimi nashindwa jinsi ya kujielezea...’nikasema huku moyoni nikishauri nifanye nini, kwani kama alivyosema mdada, nikiropoka, huenda aibu yangu yote itajulikana, na nikajikuta kwenye kesi nyingine ya mambo ya mdada...na sijui ana mambo gani zaidi.

‘Sawa ngoja mimi niongee na bosi wako, maana alikuwa anasubiria nitoe jibu langu kuwa nitakusimamia au la....’akasema na mara simu yake ikaita na kuipokea hapo hapo

‘Ni nani mwenzangu?’ akauliza

‘Mdada...!?’ akauliza kwa mshangao halafu akasema

‘Mdada unataka nini kwangu...una wakili wako au sio?’ akauliza na kuanza kusikiliza alionyesha kutokufurahishwa na hicho anachoongea mdada,lakini kila akitaka kuongea kitu mdada hakuwa akimpa nafasi, na mwisho wake akauliza;

‘Kwahiyo unataka mimi nifanye nini?’ akauliza na kusikiliza kwa muda na baadaye akageuka kuniangalia , halafu akasema;

‘Nitaongea na bosi wake, na yeye atajua la kufanya lakini mimi siwezi kufanya hayo unayotaka wewe, mimi ni mwanasheria nafahamu kazi yangu ni nini, huwezi kuniamurisha nifanye unavyotaka wewe...nisikilize mdada, kuongea sana hakusaidii..eti nini,...nilishakukanya kuhusu hilo..kumbuka kesi mlio nayo, sio ndogo, ni kesi ya mauaji,....sikuelewi...na huwezi kunitisha kwa hilo....’akakata simu kwa hasira.

‘Huyu binti vipi,..mbona simuelewi...’akasema

‘Kwani vipi tena?’ nikauliza

‘Ukicheza na hii kesi wewe utaozea jela,...utafungwa, na huenda kikawa kifungo cha maisha mwenzako sijui anataka nini...mimi sijamuelewa hadi hapo, lengo lake hasa ni nini...’akasema huku akifunga funga vitu vyake

‘Sa-sa—sa, mbona unaondoka?’ nikauliza

‘Mdada kasema atakutafutia wakili mwingine...mimi naona bora iwe hivyo, kwa hali kama hii, sitawaweza kukusaidia, maana wewe mwenyewe hutaki kuniambia ukweli,....na sasa huyu mdada analeta mambo mengine, nyie watu, siwaelewi, hamjuia kuwa kesi hiyo ni mbaya sana, ni kesi ya mauaji,...okey, mimi nitawasiliana na bosi wako, nione tutafanya nini, ...’akasema na kuanza kuondoka.

‘Tafadhali, usimsikilize mdada, wewe ndiye tegemeo langu, ukiondoka mimi nitafanya nini...’nikaanza kulalamika

‘Mtajua wenyewe....siwezi kuzalilika kwasababu ya watu wasiojitambua, na huyo binti, anataka kunichezea, nilishamkanya kuhusu mambo yake, anafikiri mimi siwezi kumfanya lolote eehe..huo mchezo wake utamtokea puani, nahisi sasa huko anapokwenda ni kubaya...’akasema huku akiondoka, akionekana kukereka sana.

Nilibakia pale nimetulia nikijiuliza ni nini hatima yangu, maana sasa kesi yote imaniangukia mimi, na sijui kweli mdada anaweza kunisaidia, na hata akimtafuta wakili ni nani atamlipa, ni mdada...kwanini afanye hivyo...

Na wakati naendelea kuwaza mara yule wakili wa kampuni  akarudi, na kuniangalia kwa muda kabla ya kusema neno, baadae akasema

‘Ongea na bosi wako...’akasema akinikabidhi simu.

NB: Haya wapendwa kwa leo ndio hayooooh


WAZO LA LEO: Matendo ni dhamira ya kweli, kuliko maneno ya kupendeza. Wengi hujiona wanajua sana, kwa vile wanajua kuutumia mdomo wao, kwa kuongea sana, lakini kwenye matendo yao inakuwa ni kinyume. Huku ni kudanganyana, matendo yako mema ndio ushahidi wa kweli.

Ni mimi: emu-three

No comments :