Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, February 28, 2014

BAADA YA DHIKI FARAJA-19


Nilipotoka kazini, sikwenda moja kwa moja nyumbani, nilielekea mitaa ambayo nafahamu ndipo anapoishi mdada, nikaitafuta nyumba kama nilivyoelekezwa, na haikuwa vigumu sana kuipata, kwani ilikuwa karibu na barabarani, na nyumba kubwa yenya kila sifa ya nyumba nzuri, ina geti kubwa na mlinzi, nikagonga geti la hiyo nyumba , na haikuchukua muda nikafunguliwa;

‘Samahani nimemkuta mdada?’ nikauliza

‘Wewe ni nani kwake?’ akauliza mlinzi wa getini niliyemkuta, akawa analiangalia pikipiki langu.

‘Ni mfanyakazi mwenzake’nikasema.

‘Ohoo, kumbe, eeh, sijawahi kukuona kabla, wafanyakazi wenzako walikuwa mara kwa mara wanakuja hapa,...Haya hebu subiri hapa nikamuulize, umesema jina lako nani?’ akaniuliza huku akiendelea kuliangalia pikipiki langu.

‘Mhasibu wake, wewe mwambie hivyo ataelewa...’nikasema

‘Mhasibu wake,...mmh, kweli yawezekana kuweka mhasibu wake, maana mdada huyu anaingiza pesa, sio mchezo, ...kwahiyo umemletea pesa...?’ akaniuliza na mimi nikacheka kidogo na kusema...
‘Hapana....’nikasema na yeye akatikisa kichwa na kusema;

‘Niambie bwana, maana najua kama umekuja na pesa leo ni furaha, dada yangu huyu akiwa na pesa hana hiana..na mimi nina shida, na njia ya kumuingia ni wakati ana pesa...’akasema.

‘Hapana sijaleta pesa, nimekuja na maswala mengine ya kazini..’nikasema.

‘Anadaiwa eeh, mmh, maana kama anadaiwa hata huko ndani siendi, huyu dada akiwa na madeni, ni vyema ukawa mbali kabisa na yeye,na siku akiwa hana pesa ndio kabisa hata ukimsalimia haitiki,...’akasema.

‘Mimi sijui kama anadaiwa, nimekuja na maswala mengine usiwe na wasiwasi...’nikasema.

‘Hata hivyo nimemuona leo akiwa na furaha sana, nahisi kapata bingo, sijui nikachomekee shida zangu huko...’akasema akawa anajikuna kichwa kama anawaza.

‘Kamwambie basi kuna mgeni wake...’nikasema

‘Ohoo, haya bwana,....lakini nikuulize kitu kimoja,wewe ni mhasibu wake, eeh, mimi nataka mkopo nifanyeje?’akaniuliza.

‘Wewe ongea naye kwanza, akikubalia atakupa....’nikasema.
‘Jana alikuja jamaa mmoja, nilimuonea huruma, huyo jamaa ni mtu mkubwa sana, huwa anatembea na magari ya kifahari, lakini jana...nikasema kweli wanawake sio mchezo...’akasema na mimi nikaona kuna jambo, ngoja nimchokonoe.

‘Huyo jamaa ni nani...?’ nikamuuliza

‘Humjui wewe, yule jamaa tajiri, mwenye pesa kama nchi yake, anapenda kusema milioni ni vijisenti kwake, pesa kwake ni mabilioni, pesa kwake ni dola, sio madafu, jamaa ana dharau yule...’akasema na moyo wangu ukaanza kunishituka, ina maana ni huyo jamaa.

‘Yule wa mamlaka ya ushuru wa magari?’ nikauliza

‘Haswa, lakini jana alikuwa mdogo kama piritoni, alipofika tu, akasimamisha gari na kuniuliza mdada yupo nikamwambia asubiri, nilipokwenda kwa mdada, mdada akasema ni mwambia kachoka amelala, ....nikarudi kumwambia akaanza kuniomba, nimwambia kaja kwa dharura, ...nikamwambia mdada huwa hana kauli mbili, akisema kasema,...’akatulia kidogo akiangalia ndani.

‘Ikawaje?’ nikamuuliza

‘Jamaa akawa ananibembeleza, kweli karibu kunipigia mgoti, sio kawaida ya huyo jamaa, mwisho akatoa nyekundu mbili, akanihikisha mkononi, akasema nenda kamwambia huyo mgeni ana mzigo wake...’huyo mlinzi akaruka ruka.

‘Nyekundu mbili shaaah, nikasema hapa ulaji, nikakimbilia ndani kufika namkuta mdada yupo kwenye dirisha kumbe alikuwa anatuangalai kwa ndani,nikasinyaa, maana aliona nikipewa hizo pesa, nikaanza kujiuma uma.

‘Ndio kazi yako siku hizi wakija wageni wanakuhonga, unakuja kunisumbua...’akasema

‘Hapana mama, ...unajua..unajua..nikawa sina cha kumwambia, akaniogelea na kusema;

‘Sikiliza kamwambia kama kaja na mzigo wangu akupe uniletee, sina muda wa maongezi na yeye...’alisema maneno hayo kwa hasira nikatoka mbio, hadi kwa huyo jamaa.

‘Kasema niende kumuona?’ akaniuliza

‘Kasema unipe mzigo wake kwanza...’nikamwambia hivyo, na huyo jamaa akaingia kwenye gari alke akatoa bahasha, imetuna, nikajua ni pesa, akanipa, na mimi kwa haraka nikakimbilia ndani nikamkabidhi mdada...mdada akaziangalia akaniambia ziweke hapo mezani , nenda mwambie tutaongea sehemu nyingine sio hapa nyumbani kwake...’akatulia kuniangalia.

‘Umesema una haraka, au?’ akaniuliza.

‘Ikawaje?’ nikamuuliza

‘Hapa koo linawasha kweli kweli, nina kiu kama ya soda vile..., nikipa soda itakuwa vizuri, sio lazima maji...’akasema na mimi kwa haraka nikaingiza mkono mfukoni, nikatoa pesa iliyoguswa na mkono wangu na kumkabidhi bila kuangalia ni shilingi ngapi.

‘Sasa hapa maneno, naweza kuongea mpaka kesho...’akasema

‘Ikawaje...?’ nikauliza

‘Jamaa hakutaka kuondoka, akasema nimwambia hawezi kuondoa mpaka waonane, ikabidi nirudi ndani kumwambia, na niliporudi nilimkuta mdada akiwa kashkilia ule mzigo huku anazunguka huku na kule, akaniangalia

‘Mama kasema hawezi kuondoka mpaka uonane naye...’nikasema na mara mdada akachukua simu yake, sijui alifanya nini, mara kwa nje, nikasikia mtu akitoa kilio, nikakimbilia nje, nilipofika nilimkuta jamaa kashikilia simu yake huku kapiga magoti....’akatulia .

‘Kwanini alifanya hivyo?’ nikamuuliza

‘Sijui..nilijarinu kumsogelea lakini alisimama kwa haraka na akaanza kuelekea ndani nikamzuia, lakini hakutaka, baadaye mdada akatokeza mlangoni na kuniambia nimuache, na huyo jamaa akapiga mgoti mbele yam dada, akimuomba,...’akasema

‘Alikuwa akimuomba nini?’ nikamuuliza

‘Eti ampe picha..kitu kama picha, anataka apewe zote na yupo tayari kufanya lolote kwa huyo mdada, na mdada alipoona ninasikiliza akamshika huyo jamaa tai yake na kumvutia ndani..ilikuwa picha, na ikaishia hapo, maana jamaa alipotoka alikuwa kakonda, hana raha, akaingia kwenye gari lake akaondoka...’akatulia,

‘Kwahiyo mdada unafikiri alimfanya nini huyo jamaaa...?’ nikamuuliza

‘Mimi sijui, kwanza nimeongea sana, huenda yupo dirishani anatuangalia ngoja nikamuone...’akasema na kutembea huku akionyesha wasiwasi,...kulipita kitambo kidogo, na baadaye akatoka huku akiwa kakunja uso, na kuonyesha wasiwasi, akaniangalia halafu akasema;

‘Mhh, mimi nakushauri usiende kumuona, nahisi mambo yake hayapo sawa...niliwahi kusikia kuwa akiwa katika hali kama hiyo, hutakiwi kumsogelea,....mimi sijawahi kumuona hivyo, mwenzangu wa mwanzo aliacha kazi, eti akimuogopa huyo mdada....’akasema

‘Kwanini amuogope..?’ nikamuuliza

‘Hata mimi sijui ni kwanini, mrembo kama huyo,....mtu unaogopa kufanya kazi naye, cha muhimu ni kumjulia mtu, mimi nimeshamjulia, akikasirika na kuwa mbalia naye, akiwa na raha, nakuwa akribu naye, maisha yanakwenda, watoto wanakwenda choo...’akasema.

‘Kwahiyo unasemaje,...?’ nikamuuliza

‘Mhh, hali niliyomkuta nayo..niliogopa hata kumshitua,...sasa mimi sijui,...uamue mwenyewe, kwa vile wewe ni mhasibu wake, na huenda umekuja na mambo mazuri, jaribu kwenda...’akasema akionyesha wasiwasi.

‘Kwani anaumwa, yupoje,..kalala, ...?’ nikauliza

‘Wewe nakushauri rudi, utampigia simu, zaidi mimi sijui, maana hata hivyo, miomi bado ni mgeni sana kwake, sijamjua vyema...’akasema akawa anatembea kuelekea sehemu yake ya kukaa, nikasimama nikijiuliza nifanye nini.

Baadaye sana, nikaona kwanini nisiende kumuona, kwanza ni mfanyakazi mwenzangu, kama ana tatizo itakuwa vyema kumsaidia, pili ni mtu ambaye nimejaribu kuwa karibu naye, na tatu, leo nimeamua kuwa iwe mwisho wa majanga anayotaka kunitumbukiza..

‘Nikaelekea kwenye mlango, sikugonga maana ulikuwa nusu wazi, nikaingia ndani

********

Asubuhi, nilichelewa kwenda kazini, kwani ilibidi nifanya mpango wa kuzipeleka hizo pesa za magumashi huko kijijini, kama alivyoniagiza mdada; na nilipoingia ofisini nikachuku gazeti nikawa nasoma, lakini akili yangu haikuwe kwenye gazeti, nilikuwa nakumbuka yaliyotokea jana nilipofika nyumbani kwa mdada bila kutegemea;

‘Unasema nini, huzitaki hizi pesa, na zile nyingine unataka kuzirudisha, haya nipe na uondoke hapa haraka ...kwanza sijui kwanini umeingia bila ruhusa yangu,...’akasema kwa hasira.

‘Sijakuja na hizo pesa nyingine, lakini mimi naona ni heri nifanye hivyo, maana pesa hizo hazina heri kwangu,naona naingia kwenye machafu yako,...’nikasema na yeye akaniangalia kwa macho yaliyojaa hasira halafu akageuka kama anataka kuondoka, baadaye akasema;

‘Unajua mimi nilidhania wewe ni mjanja,..na huenda ukawa mmoja wa watu watakao weza kubadili maisha yangu...nimekuona tofauti na wanaume wengine, na...sijui ni kwanini, ...kama nisingelisikia hayo ya kuwa una mchumba, nahisi......sijui, sijui....’akatulia kidogo na kushika kichwa chake akainama chini kama anaangalia kitu.

‘Ni hivi katika maisha haya ya bongo tunaweza kusaidiana ili angalau na sisi tuwe karibu na mafisadi, hivi nikuulize hawa mafisadi wanakula nchi  yetu, wanakupa angalau pesa ya soda, au kazi yao ni kututimulia vumbi kwa magari yao...au kusimamishwa kwenye foleni wakipitishwa na ving’ora na magari ya kodi ya walala hoi....’akasema.

‘Mimi siwajui hao watu, ...’nikasema

‘Sikiliza nikuambie kwanini nafanya hivyo, ..nafanya haya angalau kuchukua hicho kidogo wanachotuibia sisi wavuja jasho, ..hizo pesa kama tusingezichukua kwa huyu jamaa unafikiri zingekwenda wapi, kama sio kwenda kwenye miradi yao, au kutumiwa kuchezewa kamari, umalaya, na ufisadi, ... hawa watu, hawa, wanaoitwa wanaume,...hawajali, hawana huruma kwanini tuwaonee huruma...’akasema

‘Mimi sielewi hayo unayozungumza...’nikasema na yeye akaniangalia halafu akashusha mikono kama kukata tamaa

‘Leo nimejisikia vibaya sana, nimekumbuka maisha yangu, ....hata alipoingia mlinzi kanikuta sipo duniani,..tarehe kama leo, hawa watu wanaoitwa matajiri,mafisadi, wanaume....nyie wanaume,...kama ningelikuwa na uwezo ningeliwamiminia risasi hadi nihakikishe hakuna mwanaume aliyebakia hapa dunia...’akasema

‘Kwanini..?’ nikamuuliza

‘Kwanini,...naogoa kukusimulia maana nikikusimulia, unaweza ukawa marehemu...’akasema

‘Kwanini?’ nikamuuliza

‘Kwasababu wewe ni mwanaume na wanaume wote hawana tofauti...ni sawa na shilingi, japokuwa ina huku na huku, lakini shilingi ni hiyo hiyo...’akasema

‘Sijakuelewa...’nikasema

‘We acha, tarehe kama ya leo, ni siku ambayo, sitaisahau katika maisha, yangu, na ikifika tarehe kama hii ninakuwa kama mgonjwa...angalau leo, nimeweza kuvumilia, na ssijui kwanini leo nipo hapa nyumbani, nilitakiwa niwe sehemu itkayonifanya nisiikumbuke kabisa tarahe kama hiyo...’akasema na kutulia baadaye akauliza

‘Ina maana mlinzi hukuonana naye, sijamuambia aruhusu mtu....’akasema

‘Aliingia kuja kukuona...’nikasema

‘Huenda alipofika, alinikuta nimezimia,....’akasema.

‘Umezimia, kwanini uzimie, acha mambo yako mdada, mbona unanielezea mambo ambayo hayapo...mdada, mimi nimechoka,  usiponiambia ukweli, siwezi kukuelewa, kwani wanaume walikufanyia nini,...ulikuwa unajiuza, ulikuwa....mimi sikuelewi,..hebu niambia,ilikuwaje mpaka uwachukia wanaume kiai hicho, halafu sasa unajifanya eti ulipoteza fahamu, kwasababu ya madawa yako ya kulevya au?’ nikamuuliza nikiwa nimekasirika

 Mdada akainua uso na kuniangalia, aliniangalia kwa makini bila kupepesa macho,...bila kusema neno kwa muda..halafu akageuka, hakuniangalia kwa muda, badaye akageuka kuniangalia akahema na akawa kama anahangaika, akashika kichwa, akaniangalia machoni na kusema;

‘Kama unataka nikusimulie mikasa iliyonipata labda uchukua kamba unifunge, na si kamba, labda unifunge kwa minyororo wenye nguvu sana, maana huenda hata huo mnyororo nikaukata, ...kwani nachelea mabaya yatakayokukuta....

 Nikamwangalia na kutabasamu nikicheka kidogo, halafu nikamwangalia nikiwa nimebadili muonekano, ikutaka utani na yeye niliona nimbadilikie kabisa, nikamuonyesha uso wa hasira nikasema;

‘Mimi nataka niusikie huo ukweli....maana bila kuufahamu sitaweza kuvumilia, na hata hivyo nimechoka na mambo yako, imetosha, na usiponiambia ukweli kwanza kwanini unawachukia wanaume, pili kwanini unanifanyia hivi, sitakuelewa...’nikasema na yeye akaniangalia kwa macho yaliyojaa uchungu, na baadaye akasema

‘Mhh, siwezi,...sitaki,...nakuonea huruma...hapana, kwanini unaniuliza hivyo, kwanini unataka nikusimulie jambo ambali huenda utakuja kujijutia, au mimi mwenyewe nitakuja kujijutia,..siwezi na sitakiwi kabisa...hapana, ....’akawa anashika kichwa kama vile anahisi maumivu.

‘Usiponisimulia, mimi nitakwenda kulipeleka hili swala polisi, ni bora ni kose yote, lakini ukweli ujulikane, ni bora nifungwe, ni bora...’nikasema na mara sauti kama ya mwanaume ikasema

‘Upo tayari eeh, ...’sauti litoka kwa mdada, kwanza nilihisi kuna mtu mwingine kaingia, nikamwangalia mdada, nikahisi ananifanyia mzaha, maana huyu mdada kwa mzaha humuwezi, na mimi nikasema

‘Nipo tayari..’nikasema na ghafla, mdada akaondoka, na kuingia kwenye chumba, nahisi ni chumba chake cha kulala, au cha kuhifadhia vitu, baadaye akatoka na mnyororo kama ule wanaofungia magari, na kuniambia

‘Nifunge huu mnyororo, haraka....’akasema huku akiwa ahniangalii usoni, na mimi nikawa nimeshikwa na mshangao, maana sauti niliyoisikia sio ya mdada, ilikuwa nzito na kukwaruza kwaruza

‘Eti nini...!?’ nikauliza  nikionyesha mashaka.

*****

‘Mdada hali yake ni mbaya sana...yupo hospitalini ....’akasema bosi alipoingia ofisini na kunikuta nimeshikilia gazeti, mimi nikajifanya sijui lolote, kwani jana nilikimbia mapema, na sikujua ni kitu gani kimetokea tena huko nyuma.

‘Kafanya nini, kapata ajali?’ nikauliza kwa mashaka, nikawa sasa nahisi kuna baya limetokea nilipoondoka pale, nilijifanya sijui chanzo ni nini, au sijui kilichotokea mdada.

‘Huyu binti ana matatizo makubwa sana, na nilishamkanya siku kama hiyo, tarahe yake ya kuzaliwa, ajifanya kama haipo, ....na hata siku moja asijaribu kumsimulia mtu maisha yake ya huko nyuma...’akasema bosi na kunifanya nianza kuogopa, kumbe chanzo cha hayo yote ni mimi.

‘Hata dakitari wake alimshauri hivyo, kuna dakitari , mtaalamu wa mambo ya fahamu, na maswala kama hayo, yeye alishamuasa na kumwambia ajaribu kabisa kujizuia na mambo yatakayomkumbusha mambo ya nyuma, ....na ndio maana unaona wakati mwingine anakunywa sana, na huko kunywa alikatazwa pia, lakini tatizo lake ni mbishi,...kwanini umuhadithie mtu mambo yako, ambayo unahisi ni hatari kwako, watakusaidia nini hao watu.............’akasema bosi.

Mimi nikawa nimeduwaa, na moyoni nikawa najalaumu, lakini sikuwa nafahamu hayo yote, mimi niliona akinisimulia huenda na mimi nitakuwa kwenye nafai nzuri ya kushauriana naye,..ndio maana nilimuuliza anielezee maisha yake ya huko nyuma.

‘Jana ni siku yake ya kuzaliwa, na siku kama hiyo, wakati anashrehekea akiwa na miaka tisa, ndipo yalipomkuta mabaya,...ooh, naogopa hata kuyasimulia,...hata sijui kwanini alitaka kumsimulia huyo mtu aliyemuuliza, maana hali kama hiyo hutokea akijaribu kumsimulia mtu...na baya zaidi awe ni mwanaume ...’akasema bosi.

‘Kwani bosi, ...tatizo laki hasa ni nini?’ nikauliza

‘Usije ukamuuliza mdada, kuhusu maisha yake ya nyuma, ....atakuua,...’akasema bosi na kunifanya nikumbuke yaliyotokea jana, kama isingelikuwa mlinzi, huenda kama bosi anavyosema ningelikuwa maiti, lakini sikuamini, ...ina maana mdada angeniua mimi, nikamwangalia bosi na kuuliza.

‘Bosi ina maana wewe mdada aliwahi kukusimulia?’ nikamuuliza

‘Ndio , na mimi ndiye niliyechukua hatua kubwa ya kumsaidia maana watu walishamuona kuwa kachanganyikiwa, ...na wengine wakakimbilia kumuona kuwa eti ana mashetani, yale sio mashetani, ni athari ya matatizo aliyokumbana nayo akiwa binti mdogo...’akasema bosi.

‘Natamani sana kuyajua hayo.....lakini sikuweza, ilibidi nikimbie...’nikasema na bosi akawa kama kashituka na kuniangalia kama mtu aliyesikia jambo ya kulitisha, akasema;

‘Ina maana wewe jana ulikwenda kwake, hujui ndio siku yake ya kumbukumbu ya kuzaliwa na siku kama hiyo kwake inakumbusha mengi, na huenda kwa kiherehere chako, ukamuuliza maisha yake ya huko nyuma?’ akauliza bosi, na mimi hapo nikasita baadaye nikasema;

‘Ndio mimi bosi, nahati nzuri jana nilimtembelea nyumbani kwake, na tukawa tunaongea nikataka kujua ukweli, maana kila mara anawalaani sana wanaume, na kuonyesha hali ya kuwachukia wanaume,....nikawa najiuliza sana, wanaume wamemfanyia nini huyo mdada,!’ nikasema.

‘Kwa tahadhari, usije kurudia tena kumuuliza maswali kama hayo, utakufa, mdada atakuua.....usije ukajidanganya kuwa kwa vile yeye ni mwanamke utaweza kumzidi nguvu, huwezi na hamtaweza...’akasema na kutulia kama anatafakari jambo.

‘Nikuambie ukweli, hali kama hiyo ikimuanza, na akianza makeke yake, hakuna anayeweza kumshika..hata waje wanaume wenye nguvu kumi, hawamuwezi....na hatakiwi mwanaume kumsogelea...’akasema bosi na kuingia ofisini kwake,ilionyesha hakupendezewa na kitendo hicho cha mimi kumuuliza mdada.  Baadaye bosi aliniita na mimi nikaenda ofisini kwake, na kwa vile ikuwa na kazi nyingi siku hiyo, akasema;

‘Tuendelee na kisa chetu kidogo, baadaye nitakwenda kumuona mdada nione anaendeleaje, ...’akasema bosi akiangalia saa yake.

‘Au una kazi nyingi...?’ akaniangalia na mimi nikasema

‘Sina kazi nyingi, ila kama unakwenda kumuona mgonjwa, kwa vile ni stafu  mwenzetu, naona tuongazane na mimi nikamuone huyo mgonjwa...naona twende huko hospitalini pamoja.....’nikasema

‘Tuongazane mimi na wewe,...?’ akawa ananiuliza akiniangalia kwa mshangao, na mimi nikawa nashangaa pia,  kwani kuna ubaya gani mimi na yeye tukienda pamoja kumuona mgonjwa,nikawa sielewi, bosi aliniangalia kwa makini kwa muda, mpaka nikatahayari na kuhisi nimetenda kosa kumwambia hivyo, baadaye akasema;

‘Unasema twende pamoja, ina maana hukunielewa, ..ohooo, wewe sasa unatafuta kifo chako, na na kuonya tena na tena, usifanye kosa hilo, kwa hivi sasa hatakiwi mtu anayeitwa mwanaume kumsogelea huyo mgonjwa, labda kama unataka kufa mapema...mimi huko nitakwenda peke yangu, nitakujulisheni anaendelea vipi...’akasema

Unakumbuka tulipoachia,...

Kuwa nilipata mtu mwenye gari, akajitolea kumpeleka mtoto hospitalini, na muda huo mvua bado ilikuwa ikinyesha, na sio mvuo ndogo, ni mvua kubwa....

‘Haya tuendelee na simulize letu...’akasema bosi

‘Basi kwa msaada wa yule baba alinipeleka hadi hopitalini, na ukumbuke hospitali iliyokuwepo karibu ni ya kulipia, sina pesa, na hata kama nitarudi dukani, kuchukua akiba yangu isingelitosha kwa matibabu, pesa iliyokuwepo nilishanunulia vifaa.

‘Lakini mungu mkubwa kwani kwa msaada wa yule msamaria mwema, nilifanikiwa kulipia matibabu ya mtoto na daktari alipomwangalia mtoto jinsi alivyo, akasema;

‘Huyu inabidi alazwe, hali yake io nzuri...’akasema docta na wakaanza kumchunguza na kumpa ile huduma ya kwanza kabla hajaanza matibabu, walimuwekea kifaa caha kupumulia, ni cha oksijeni kwani pumzi zilikua za shida.  Na huku wakiendelea na vipimo vingine.

Nilimshukuru sana mwenyezimungu kwa kunikutanisha na huyo baba ambaye alikuwa na moyo huo wa huruma anakanisidia bila kusita nilimshukuru naye akiendelea kuonyesha ubinadamu wake na kunilipa shilingi 20,000 kama za kunisaidia na baadaye alipohakikisha kuwa tumelezwa akaniaga.

‘Sijui nikushukuru vipi baba yangu...’nikasema nikimwangalia bila kuamini, maana katika dunia ya leo watu kama hawa ni adimu kabisa.

‘Usijali, kwa binadamu yoyote mwenye utu , angelifanya hivyo hivyo, hali ya mtoto inasikitisha..’akasema akimwangalia mtoto, na baadaye akaondoka.

Nilikaa wiki moja nikiuguza mtoto huku na mie nikiwa na homa kali, ikabidi na mimi muuguzaji niwe mgonjwa, na nianza matibabu na ukumbuke nilikuwa na mimba na mimba inakua kwa majanga hivyo hivyo.

Baada ya wiki moja ya kulazwa, nilirudi nyumbani,na uamuzi niliouchukua ni kuwa hata kama nipo dukani, nitaenda na mtoto wangu,niwe nashinda naye huko huko dukani mpaka hapo jioni , na jioni narudi naye.

Katika kuhangaika, tukawa pia tunapika vyakula, na pia kama kuna sherehe tunachukua hiyo tenda ya kuwapikia wageni, bahati nzuri, mwezi tisa kukawa na harusi harusi, na tukaweza kupata nafasi ya kuwapikia watu.

Mwezi huo wa tisa ndio mwezi wangu wa kutazamia, lakini hata hivyo, ilinibidi nihangaike ili kupata riziki, nakumbuka ilikua ni majira ya saa kumi na moja alfajiri nikahisi uchungu, yakiambatana na maumivu makali, nikajua muda umefika.

Uchungu ulikuwa mkubwa sana , hata hivyo ikutaka kumsumbua mume wangu kwenye  kwani na yeye alikuwa mgonjwa,  alikuwa naye anaumwa, yupo kitandani,  nilivumilia mpaka saa nne hali ikazidi kuwa tete, na mume wangu akaniona nikigugumia maumivu;

‘Mke wangu ni bora uende hopitalini....’akasema na mimi kwa hali niliyokuwa nayo sikupinga ,  nikajiandaa kwenda hospitali, huku uchungu umenikamata kweli kweli hata kusimama siwezi, nasimama huku nimepinda, nikajitutumua hivyo hivyo, nikujiandaa.

Tukiwa tunasubiria usafiri, akaja mtu kutuambia gari walilolitegemea limeharibika, limefika njiani na kuzimika,...

‘Oh mungu wangu, mbona hii adhabu...’nikasema na mume wangu akanipa moyo kuwa nivumilia watajiathidi kutafuta gari jingine.

Gari lilipopatikana lakini hapo nilipokaa, nilikuwa sijiwezi, nilihisi kama ninaweza kujifungulia hapo hapo nyumbani,

‘Gari limefika haya inuka twende nje...’akasema mume wangu,

Nikajikakamua na kuinuka kwa shida, yaani zile hatu hadi kufika mlangoni ilikuwa ni kama mwendo wa maili wa kupanda mlima,...haya nikatoka nje, kwenye hiyo nyumba tunapokaa kuna ngazi za kushuka kidogo.Sio ngazi kubwa saana, lakini cha ajabu ngazi sikuweza kuinua mguu ili niteremke, watu waliokuwa wakiniangalia ambao hawajui uchungu ulivyo, hata kama wanajua, lakini kwa vile sio wao yaliyowakuta, wakaanza kunicheka.

‘Wifi na wewe bwana...ina maana hata kushuka hizo ngazi leo hii huwezi...’akaanza kusema wifi yangu na wote wakaangua kicheko.

‘Anadeka huyo, kwasababu mume wake leo yupo,nani asiyejua kuzaa ...wewe uliona ni raha eeh...hehehe...’akasema huyo wifi mwingine ambaye hata kuzaa hajazaa, anajisemea tu, na wote wakaangua kicheko.Nikajitutumua kwa shida na kwa jinsi nilivyokuwa natembea hao mawifi zangu na shemeji zangu wakawa wananicheka kweli kweli, hawana mbavu.

Mimi sikutaka hata kuongea nao, kwani hata hiyo hamu ya kuongea nao ninao,, ila moyoni nilisema kweli duniani hamna ubinadamu hata huruma hata kuniuliza, au kunisaidia kunishika mkono hakuna.

Nilijitahidi nikashuka zile ngazi, na nilipofika chini, nikakaa chini, sijiwezi kabisa, maumivun yalikuwa makali sana, hapo sasa nikawa nalia, siwezi kuinuka kabisa, siwezi kutembea migumu imegoma, hakuna aliyejitolea hasa akina mama kuja kunisaidia mpaka mume wangu japokuwa ni mgonja, akaamua kuja kunibeba na kuniingiza kwenye gari.

Nikapelekwa hadi hopitalini, nilivyofika tu hospitali kitengo cha clinic ya wazazi, daktari alimuambia mume wangu akimbilie begi na beseni kwani kichwa cha mtoto kilikua kimesha anza kutoka...

‘Kwanini mumemchelewesha huyu mtu hivi...’akasema yule dakitari akionyesha wasiwasi, na niliposikia docta akisema hivyo nikajua mambo sasa yamekuwa mabaya, ni yale yale ya kuambiwa ni mimi au mtoto.

Waliniweka kwenye hilo beseni na kunikimbiza leba na hapo kiakili nikawa mimi na mungu wangu , kipindi hicho mume wangu alikuwa katumwa kwenda kununua baadhi ya vifaa vilivyohitajika kwenye duka lao, japokuwa alikuwa anaumwa lakini kutokana na hali yangu ilibidi kuumwa kwake akusahau.....

NB: Je ilikuwaje


WAZO LA LEO: Usifurahie kupata kitu amabcho sio halali yako, ukijua kabisa kuwa hujakipata kihali, na kupata kwako ni kumdhulumu mwenzako, ...huenda umekipata kwa ujanja-ujanja na hadaa za namna kwa namna huku ukisema; ‘hii ni riziki yangu, hii ni halali yangu....’ hiyo sio halali yako, hilo ni deni, kwani huyo uliyemdhulumu, anaposononeka moyoni, familia yake ikateseka kwa ajili hiyo, huo ni mzigo wa madhambi kwako. Tujitahidi kuchuma na kupata riziki ya halali, chumo linalotokana na juhudi zetu za halali.

Ni mimi: emu-three

No comments :