Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, January 29, 2014

BAADA YA DHIKI NI FARAJA-4


Hali ya ofisi ikatulia kidogo maana bosi alikuwa kachachamaa na wafanyakazi wakawa kila mmoja anajituma kwenye meza yake, na ile tabia ya urafiki wa kimapenzi, ukapungua, kama ilitokea inakuwa nje ya ofisi,hata tabia kutoana chakula cha mchana haipo tena, ikawa kazi ni kazi.

Baada ya wiki moja, Mdada, akarudi kazini, uso ukiwa na makovu, akawa kavalia mawani makubwa kujaribu kuficha uso wake.

 Siku alipofika bosi akamuita ofisini kwake wakaongea kwa muda mrefu, halafu akatoka, na alipopita kwenye meza yangu akaniachia ujumbe kwenye karatasi

‘Nataka tuongee baadaye....’nikasoma na kwa hasira nikakichana kile kikaratasi huku nikisema huyu mwanamke hajakoma tu, sitaki kuonana naye.

Ilipofika jioni nikpata ujumbe kwenye simu yangu, kutoka kwa huyo binti, ukisema;

‘Nitakusubiri unipe lifti ya piki piki yako,...’
Na mimi hapo hapo nikamjibu

‘Samhani kuna mtu kaniwahi, ..’ yeye akaandika ujumbe mwingine,

‘Basi njoo mara moja nataka tuongea na wewe ni muhimu sana, ni kuhusu yule jamaa, alivyoniambia, nimeshavunja uchumba na yeye kwa ajili yako....’akaandika.

‘Mimi hayo hayanihusu, nakuomba tujuane kikazi si zaidi ya hayo...’nikaandika.

‘Mimi nimeongea na bosi nikamwambia ukweli....’akaandika.

‘Ukweli gani?’ nikamuuliza

‘Kuwa mimi  kweli ninakupenda wewe, ...’akaandika.

‘Mimi sitaki mahusiani na wewe...’nikamjibu.

‘‘Ina maana hunipendi?’ akauliza.

‘Mimi sio aina yako, sikuwezi...’nikaandika

‘Wewe sio mwanaume?’ akauliza.

‘Hata kama mimi ni mwanaume, lakini sio kwa ajili yako...’nikamjibu.
‘Basi mimi nitakufundisha uwe wa aina yangu,kama kweli wewe ni mwanaume ...’akaandika.

‘Sitaki, urafiki na wewe nakuomba tafadhali...’nikamwandikia.

‘Sikiliza wewe mwanaume, kazi ni nzuri, unaonaje ukienda mitaani, bila kazi,...’akaandika

‘Una maana gani?’ nikamuuliza kwenye ujumbe wa simu

‘Unaelewa vyema, ...sasa tuonane tuongee, ...kama unamuogopa bosi wako basi tukutane nyumba ya wageni ya kajificheni..’akaandika bila aibu.

‘Sina nafasi hiyo na mimi sina tabia ya kwenda nyumba za wageni..’nikaandika.

‘Mimi nitafika huko kukusubiri na usipofika, nitamwambia bosi wako yote yaliyotokea siku ile kuhusu wewe....’akasema.

‘Kuhusu mimi! Mimi nimefanya nini, wakati wewe ndiye uliyetaka kuniingiza kwenye matatizo?’ nikamuuliza.

‘Nina siri zako nyingi, nikimuonyesha bosi wako, sizani kama atakuvumilia, ...ulipokuwa ofisini siku ile, kuna picha nimechukua tukiwa tumekumbatiana,...au nikutumia...’akaandika.

Mimi nakumbuka kabisa siku ile hakuwa na kamera wala simu yake, je picha hizo alizichukua muda gani, na wakati nawaza hivyo, ujumbe ukaingia kwenye simu,

‘Hebu angalia hiyo picha, je unaweza kusema mimi ndiye niliyetaka kukuingiza kwenye majaribu...’akaandika, na mara ujumbe wa kuonyesha kuwa kuna picha ukaingia. Nilianza kuhisi wasiwasi, huku nikifungua hu ujumbe.

 Picha iliyonekana ilikuwa ni wakati ule Mdada huyu akajiribu kunibusu, na kweli kwa jinsi alivyoichukua, inaonyesha kabisa na mimi nilitaka kufanya hivyo, sijui alichukuaje, kwani ilionyesha wazi nilikuwa nataka kumbusu, hapo nikahisi mwili ukiisha nguvu, nikazima simu yangu  kwa hasira.

 Siku hiyo kabla muda wa kuaondoka kazini haujafika, bosi akaniita ofisini kwake, na alihisi sipo sawa akaniuliza nina tatizo, nikamwambia hakuna tatizo.

Yeye akaniambia;

‘Unafahamu Mdada alikiri kuwa anakupenda sana na ampepanga kuachana na mchumba wake, ili muwe marafiki,..’akaniambia

‘Haiwezekani, mbona mimi nimemkatalia..hatujawahi kuongea hilo, hapana bosi kakudanganya’nikasema.

‘Sema ukweli wako ina maana na wewe humpendi huyo binti...?’ akaniuliza

‘Huyo si aina yangu, ni mkorofi, sitawezana naye...wewe mwenyewe unafahamu hilo...’nikasema.

‘Huyo atatulia tu, ...huo ni wakati wake wa kuruka ruka, lakini atakuja kutulia, ...’akasema.

‘Bosi kwanini unasema hivyo, mimi sizani, kama nitawezana nay eye, nimeshamuona hanifai...’nikasema.

‘Umeshamuona, hakufai, ulimuonaje hakufai wakati huna mahusiano nay eye?’ akaniuliza

‘Kwa jinsi nilivyomuona tu, na kwa tabia zake, nilivyosikia kwa watu, hata wewe bosi unamfahamu hivyo..’nikasema

‘Kasema usimpomkubalia yeye, hatahitajia mwanaume mwingine .....anaonyesha wazi kuwa anakupenda sana...’akaniambia bosi.

‘Bosi hivi kweli hata wewe unanishauri niwe na mwanamke kama huyo , kweli ndi ushauri wako huo, nilitarajia wewe kunikanya nisiwe karibu naye,kama ulivyonishauri mwanzoni!’ nikasema kwa mshangao.

Mimi sijakushauri hivyo, ila nakuelezea alivyosema mwenzako, ..nashukuru hata hivyo, kuwa ofisi sasa kumetulia,mimi nilikuwa nakupima uoni wako na je upo tayari na huyo binti, na kwa jinsi ulivyonijibu inaonyesha wazi hata wewe una kitu moyoni kuhusu huyo binti, ila nakuonyeni, fuateni sheria na taratibu za kazi ...’akasema bosi.

‘Bosi tutafanya hivyo,...’nikasema kwa sauti ya unyonge.

‘Na wale jamaa niliowasimamisha kwa muda walifika jana na barua zako za kujieleza, wewe ulikuwa umetoka, ...wakaniomba msamaha, kwahiyo kesho watakuwepo ofisini...’akasema.

‘Mhh, sijui kama kutakuwa na amani, labda wakifika wataendeleza ushindani wao...’nikawa kama najiuliza.

‘Ndio maana nikakuuliza kuwa unampenda huyo binti, kwani sitavumilia mapigano na mvutano wa kimapenzi kwenye ofisi yangu, kama mpo na uhakika wa kweli,wa kuwa wachumba, naomba  mliweke wazi, tuwachumbie..mimi nitakusaidia ili muweze kuishi kama mke na mume....’akaniambia.

‘Bosi....’ nikataka kujitetea na yeye akaniangalia huku akitabasamu kimzaha

‘Kama huna nia na yeye kiukweli, basi haina haja ya kushindana na wenzako kwani nina imani wenzako wakija, kutakuwa na ushindani dhidi ya huyo binti, na hiyo ndio furaha yake...’akasema

Moyoni nilianza kuhisi wivu, ina maana hao jamaa wakija, binti huyo hatakuwa na urafiki na mimi tena, nikikumbuka msimamo wake wa mwenye kisu kikali ndiye atakaye kula nyama, na kama nilivyosikia kwa wafanyakazi, jamaa hawo wana pesa na wanajua kuzitumia, kwahiyo mimi sitakuwa na nafasi tena na huyo binti.

‘Sijui kwanini nilijisia hivyo, ina maana kweli nilishampenda huyo binti au ni tamaa tu za kimwili?’ nikajiuliza kimoyo moyo na aliyenishitua kwenye dimbwi hilo la mawazo alikuwa bosi.

‘Naona una mawazo sana, unawaza nini, unamuwazia huyo mdada,umeshapenda wewe,....’akasema huku akicheka.

‘Hapana bosi....’nikasema

‘Ninachokuasa ni kuwa achana na mawazo ya namna hiyo, waza mambo ya maendeleo ambayo ukiyafanya watu watakupenda hata bila ya kushindana, watu watakuthamini na kila mmoja atatamani kuwa na wewe. Hata siku moja usipende kuwaza mambo ya anasa kabla hujafanikiwa ...anasa inakuja kwa ziada...

‘Ukweli ulivyo, huwezi kuwaza anasa kabla hujachuma, anasa kabla ya machumo ni uzembe, na uzembe ni sumu ya maendeleo. Maendeleo hutokana na juhudi sio kuota ndoto za mchana,..nikuambie ukweli ukifanikiwa kila kitu kitajileta chenyewe, kwahiyo hakuna haja ya kuota ndoto, fanya kazi,kwa bidii utafanikiwa,...’akasema na mimi nikaitikia kwa kichwa

‘Haya ngoja tuendelee na kisa chetu...’akasema bosi

‘Unakumbuka pale tulipoishia, wakati mimi na mdogo wangu tuliporejeshwa tena kwa mama wa kambo, na sisi kama watoto tusingeliweza kupinga amri ya wazazi, lakini mimi sikupendelea kabisa kurudi tena huko mjini, mama akatuambia baba kaahidi kuwa safari hii atahakikisha hatunyanyaswi au kuteswa.

‘Je ni kweli baba alitimiza ahadi yake,...?’ nikamuuliza bosi na bosi akanitizama halafu akasema;

`Tuendelee kuanzia hapo, utajionea mwenyewe...’

********

Sijui ilkuwaje, kweli tulipofika kwa mama akatupokea kwa shangwe, na tulimuona kama kabadilika, akatuonyesha sehemu ya kulala, na kutuandalia chakula,

‘Wanangu karibu sana mjisikie mpo nyumbani, ..’akasema.

‘Tunashukuru sana mama, naona umebadilika sana...’nikamwambia

‘Kwanini mwanangu, mimi ni mama yenu, nawapenda sana, msisikilize maneno ya wambea kuwa nawatesa, mimi ninachofanya ni kuwajenga ili muwe watoto wema, nawaonyesha jinsi gani ya kuishi maisha mema..’akasema.

Kwakweli tulimuona kabadilika kidogo,akawa anatulea vizuri,siku za mwanzoni, sio kama ilivyokuwa awali, lakini siku zilivyozidi kwenda akaanza kubadilika, kumbe ilikuwa ni kama  geresha, ubinafsi wa huyo mama haukupotea, bado alikuwa na kinyongo na mimi na wala sikufahamu kwanini alikuwa akinichukia kiasi hicho.

Ile hali ya utumishi na kufanya kazi ikawa ipo pale pale, na ile hali ya kusingiziwa makosa hata kama sijayafanya ikawa ipo pale pale, maisha ya dhiki, dhahama kusimangwa, ikawa ndio tabia ya nyumba hiyo,na baba akawa kama anamwamini mke wake kuliko hata utetezi wangu,, mama akisema jambo, baba anakimbilia kuniadhibu tu, watoto wake wakikosa, wananisukumia mimi kuwa ndiye niliyefanya hilo kosa, na sikusikilizwa hata pale nilipojaribu kujitetea.

Nakumbuka ni kipindi tulipomaliza mtihani wa darasa la saba wa taifa nimemaliza na kuelekea nyumbani nilivyoingia tu nikaanza kupewa kipigo na baba bila kuambiwa napigwa kwa kosa gani,baba siku hiyo alinipiga sana, kama vile mtu anayepiga mnyama, na alipotosheka an kipigo hicho, akaniambia nindoke mbele yake.

‘Huyu adhabu yake, asipewe chakula, atabakia hivyo hivyo...mimi siwezi kukaribisha udanganyifu katika nyumba hii...’akasema

‘Jamani kwani mimi nimefanya nini....mbona mnanipiga hata bila kujua kosa langu ni nini...?’ nikauliza na hakuna aliyeniambia kosa langu ni nini.

‘Unajifanya hujui eeh, kwa vile umezoea kufanya hivyo, unamdanganay nani, unafikiri siri zako zitajificha...’akasema mama

Baada ya kukaa masaa kama ma nne nikiskilizia maumivu na njaa ndio napata habari kuwa baba ameambiwa eti nilikua nameibia kwenye mtihani, na hiyo ndio tabia yangu nikiwa darasani, nikashikwa na mshangao mkubwa, mbona hilo alipo na halijawahi kutendeka, mimi huwa natumai akili zangu. Nikajaribu kujitetea nilivyoweza lakini sikusikilizwa, baba alikataa kabisa kunisikiliza.

Mambo hayakuishia hapo, kwani mama aliona njia nzuri ya kunipata ni kunisingizia uwongo, anatuma watu wanakuja na uwongo huu au ule, hapo nyumbani kesi zikawa haziishi kila siku natungiwa jipya na kuzidi kuchukiwa na baba.Baba akawa sasa ananichukia kama vile mimi sio mtoto wake, akawa haniamini tena,  ikawa sasa ni kipigo kejeli, masimango.

Siku ikafika ya mahafali ya kutuaga darasa la saba ambayo kila mtu alikua anafuraha ya kipekee isipokua mimi maana hata ruhusa ya kuhudhuria sherehe za mahafali hayo sikuweza kuipata kirahisi, baba alikuja kuamua baadaye kuwa na mimi niende, na hata hivyo hakuniamini, ikabidi nipewe na walinzi. Japokuwa ilikua siku ya furaha kweli kwa kila mwanafunzi lakini haikuwa kwangu mimi.

Wenzangu walinionea huruma sana, hasa wale wanaofahamu maisha yangu na familia yangu, hata walipjaribu kuniliwaza, niliona kama wananizishia machungu, nikawa nipo peke yangu nimejikunyata kama mkiwa. Niliwaangalai wenzangu wakicheza na kufurahi na kujiuliza moyoni, hivi mimi nimekosa nini katika hii dunia, kwanini nabeba mateso nisiyokuwa na sababu nayo, nimewakosea nini hawa watu.

Nikiwa nimekaa peke yangu, machozi yakaanza kunitoka huku nikimkumbuka mama yangu, ambaye hakuweza hata kufika kuja kunipongeza kutokana na nakama za kimaisha. Nilikaa hivyo hivyo, hadi ikafika muda wa kukabidhiwa vyeti, na nilipokipokea tu, wale walinzi kwa kufuata masharti waliopewa, wakaniambai turudi nyumbani haraka. Wenzangu wakaendelea kushereheka. Nilirudi jela, maana nyumbani kwangu ilikuwa kama jela, sina raha, sina uhuru.

Kwa kawaida wazazi humpongeza mtoto wao anapomaliza darasa la saba, nilitarajia itakuwa hivyo kwa wazazi pale nilipowaonyesha cheti changu, lakini hawakutaka hata kukiangalia, baba ndio kabisa aligeuka pembeni akisema;

‘Huyu ni kupoteza muda tu, sijui kama atafaulu, mtihani wenyewe nasikia umefanya kwa kuibia, umenitia aibu sana,...’akasema akikumbushia siku ile alipoletewa taarifa za uwongo kuwa mimi nilionekana nikiibia kwenye mtihanii huo wa kumaliza darasa la saba, kitu ambacho sio kweli, na sikujua ni nani alileta uwongo huo, nikamuachia mungu, maana sikujua nijitetee vipi.

‘Atabakia hapa nyumbani, afanye kazi za nyumbani akipata mume aolewe, kama basi atampta huyo mume, kwani kwa tabia yake hii ya uhuni, hakuna mwanaume atakaye mtaka, wanaume wanataka wanawake wenye tabia nzuri, wachapakazi, lakini wewe uvivu, mzembe, muhuni, tabia zote chafu,...’akasema mama wa kambo

Marafiki zangu waliwahi kunitembea waliumia sana na walitaka kujua tatizo ni nini mbona sina raha, nipo kama mkiwa, lakini sikuweza kuwaambia ni nini kinachoendelea ndani ya familia yangu, niliwaambia ni mambo ya kawaida tu.

Siku zikaenda na muda wa matokea ya mitihani ukafika, na taarifa zikaja kuwa nimefaulu, nilikimbia kwa haraka kuwafahamisha wazazi wangu, nikitarajia furaha na kupongezwa, lakini sura niliyoiona ilinikatisha tamaa, kumbe wao walishajua hayo matokea lakini hawakunifahamisha, walikuwa na yao mengine kichwani.

‘Wewe hatukuamini, hata kama umefaulu, ukienda huko sekondari pake yako utazidi kututia aibu....’akasema baba

‘Kwanini baba?’ nikauliza.

‘Wewe ni muhuni, huna adabu, nafahamu kabisa ukipata mwanya kama huo, utautumia vibaya na kufanikisha mambo yako ya kihuni, na mimi kama mzazi nitakuja kuaibika, na kuizalilisha hii familia...’akasema baba, na sikumuelewa ni kwanini aniite mimi muhuni, ni uhuni gani huo niliowahi kuufanya, maana mimi sina tabia kama hiyo, sijawahi kuwa na mpenzi, nab ado nilikuwa mdogo wa kuwazia hayo..

Muda wa kujiunga na sekondari ukafika baba akaendelea na msimamo wake huo huo, kuwa mimi sitaenda kusoma sekondari, akasema;

‘Huwezi kwenda sekondari peke yako, ni lazima uwe na mtu wa kukuchunga, kwahiyo utasubiri hadi mdogo wako akimaliza shule ya msingi, akifaulu mtaenda naye,sikuamini,...ina maana nikae mwaka mnzima hadi mdogo wangu huyo, mtoto wa mama wa kambo, amabye walimuamini, amalize darasa la saba, kwani muda huo yeye alikuwa darasa la saba.
‘Baba mimi sio muhuni, nitasoma kwa bidii, ....’nikasema.

‘Mimi nimeshasema, itakwua hivyo, sisi tunakufahamu kuliko wewe unavyojifahamu, tabia yako hiyo, inahitaji uwe na ndugu yako karibu, ukiwa peke yako utafanya mabaya zaidi...’akasema na kweli akashikilia msimamo wake huo. Nilimuwazia mama yangu huko kijijini, kama angelikuwa hapa, angelinitetea, lakini mama yangu wa kambo, akawa na msimamo huo wa baba, na kusema.

‘Na hata huko kusoma ni kupoteza muda tu, ni aheri akae hapa nyumbani, akipata mume ataolewa..’akasema mama huyo wa kambo.

Ukawa ndio msimamo wa wazazi wangu hao, na kweli nilikaa nyumbani, nikifanywa mfanyakazi wa nyumbani hadi mdogo wangu alipomaliza darasa la saba, na kweli akafaulu kujiunga na sekondari ndipo hapo nikaruhusiwa na mimi kujiunga na sekondari kidato cha kwanza, baada ya wao kuniombea na kukubaliwa.

Kwasababu maksi zangu za ufaulu zilikuwa za juu kuliko hata za huyo mdogo wangu, mimi niliwekwa chumba cha watoto werevu, kutokana na walimu wenyewe walivyopanga, na mdogo wangu huyo, ambaye alikuwa mtoto wa mama wa kambo, akawekwa chumba kutokana na maksi zake, hali hii ilijenga chuki fulani kwa ndugu yangu huyo, na alipomwambia mama yake , mama yake akasema ni uhuni wangu ndio uliofanya walimu wanipendelee.

Pamoja na yote hayo, maisha magumu, kusakamwa, kunyanyapawa, lakini hata hivyo, bado nilikuwa napenda sana kusoma, na darasani nilikuwa na juhudi sana, na nilikuwa miongoni mwa wanafunzi walikuwa wakifanya vyema darasani, na hali hiyo ilijitokeza pale tulipofanya mtihani wa kuingia kidato cha pili, kwa kuwa miongoni mwa wanafunzi waliofanya vizuri.

Matokeo ya kuingia kidato cha pili yalipotoka, nilikuwa miongoni mwa wanafunzi waliofanya vyema, tofauti na mdogo wangu, yaani mtoto wa mama wa kambo, yeye japokuwa aliweza kuingia kidato cha pili, lakini alama za ufaulu wake zilikuwa za chini, na hali hiyo ilimfanya mdogo wangu huyo azidi kujenga chuki ya chini kwa chini dhidi yangu, akawa ananipalilia fitina, iliyokuja kuharibu maisha maisha yangu.....

NB: Je ni nini kitatokea kwa mpendwa huyu


WAZO LA SIKU: Tunapoishi na watoto wa wenzetu, tuwatimizie mahitaji sawa na watoto wako, ukiwatendea watoto wa wenzako vibaya, ukawadekeza watoto wako, ujue unaowaharibu ni watoto wako, kwani unawajengea maisha mabaya siku zijazo,kumbuka mtoto umleavyo ndivyo akuavyo.

Ni mimi: emu-three

No comments :