Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, January 28, 2014

BAADA YA DHIKI NI FARAJA-3


Siku hiyo mimi nilichelewa kidogo , kwani kuna kazi nilipewa na bosi, kwahiyo nikajikuta nipo mwenyewe ofisini, nikaharakisha mpaka nikamaliza ile kazi, nilipomaliza, simu yangu ya mezani ikalia, na ni ilionyesha ni namba za humo humo ofisini, kuashiria kuwa kuna mtu mwingine yupo ofisini nikapokea nijua pengine ni walinzi wanataka kujua kuwa bado nipo na wanakagua usalama.

‘Hujamaliza kazi zako wewe mwanaume, mimi nakusubiria....’sauti ile ilinishitua na kunifanya mwili uishiwe na nguvu,  sikutarajia kabisa kuisikia sauti hiyo kwa muda kama huo,  kwani nilijua siku hiyo imepita salama, na nimeshaikwepa ile ahadi ya mdada kuwa tuwe naye kwenye chakula cha usiku, nilishamwambia kuwa haitawezekana kwa vile nina kazi nimepewa na bosi.

‘Kazi gani hiyo ya kufanya hadi usiku wa manane?’ akaniuliza

‘Kazi za kawaida, nikitoka hapo nitakuwa nimechoka, sitataka kwenda mahali popote...’nikamwambia.

‘Tutaona, ...ukimaliza mapema ni lazima tuonane...’akasema

‘Sijui...’nikasema nay eye akasonya na kukata simu.

Nilipoiskia hiyo sauti, ikavuruga ubongo wangu, nikawa sipo kawaida, na hapo hapo nikaanza kujiuma uma na kuongea kwa kigugumizi.

‘Ina maana na wewe ..ba-bado..u-upo ofi-sini, unafanya nini?’ nikauliza nikishikwa na kigugumizi.

‘Haya yote nimeyafanya kwa ajili yako, leo mwili wangu unakuwaza wewe, siwezi siku hii ipite hivi hivi, bila kuguswa na wewe,...’akasema.

‘Sasa unafanya nini ofisini muda kama huu, yaani umekaa hapa ofisini kwa ajili yangu?’ nikamuliza.

‘Wewe usiwe mjinga, mimi sio mtoto kiasi hich, kulikuwa na kazi ya bosi kanipa niifanye,nikaichelewesha makusudi, niliposikia kuwa wewe una kazi umepewa...kwahiyo leo upo na mimi wewe mshamba...’akasema na kucheka kwa dharau.

‘Hivi wewe kwanini unanitakia matatizo...?’ nikauliza.

‘Matatizo gani wewe, ...ina maana wewe hunitamani huu mwili wangu wenzako wanapigana hata kutaka kujiua kwa ajili yangu, ina maana wewe hujisikii lolote kwangu, usinidanganye, nakuona jinsi gani unavyopata taabu ukiniona, sasa, unaonaje mipango ilivyojileta yenyewe, nataka kuuona huo uanaume wako, maana nilishakutilia mashaka...mshamba mkubwa wewe’akaniambia huku akiendelea kucheka kwa kulainisha sauti.

‘Kwahiyo unataka kufanya nini, ina maana kweli umedhamiria mambo yako ya ajabu ajabu, kweli wewe mwanamke, wanawake wenzako wanajiheshimu, mbona wewe upo hivyo...usinitakie balaa....’nikajitetea huku nikianza kuwazia sura ya huyo mchumba wake, na kauli ya bosi kuwa huyo jamaa sio mtu wa mchezo, ikinijia akilini. Nilikaa kimiya mara huyo binti akasema;

‘Umemaliza kazi nije huko, au unakuja hapa nilipo..?’ akauliza na mimi nikajikuta nikimuuliza

‘Kwani wewe upo wapi....?’ nikamuuliza nikitaka kujua yupo ofisi ipi, ili nitafute upenyo wa kumtoroka, kwani nilifahamu kabisa hayupo sehemu yake ya mapokezi, lakini nafahamu anahitajika nimchukue na pikipiki yangu hadi kwake, kama hajamuambia mchumba wake ampitie.

‘Nipo chumba cha mikutano, kuna kazi nilikuwa naifanya kwa ajili ya mkutano wa kesho, wewe unaweza ukaja tukakiwekea baraka hiki chumba, nimefanya kazi kubwa sana, na sasa hivi nimetoka kuoga, nilikuwa najiweka sawa, ili ...mmh, ushindwe mwenyewe...’akasema kwa sauti ya kulegeza.

‘Wewe mwanamke una balaa...’nikasema huku nikiharakisha ili nitoke haraka mle ofisini nikimbilie nje, nikamsubiria huko,nafahamu huko walinzi wapo, hataweza kunifanyia vituko vyake, na nilipohakikisha nimezima taa na kila kitu kipo sawa, nikafungua mlango wa ofisi yetu na kutoka nje, kulikuwa kimiya, ni kama muda wa saa moja moja moja hivi kwahiyo huko nje giza lilishatanda.

Nilipomaliza kufunga mlango nikageuka kwa haraka sasa nikijiandaa kukimbilia nje, nikajikuta naangaliana uso kwa uso na huyu mdada, akiwa kajiiremba sijui hiyo kazi kaifanya muda gani, na ajabu alikuwa kavaa khanga moja, sijui kama hiyo khanga alikuwa nayo, au ndio hizo alizokuwa akiztumia kwa ajili ya kupambia huko ukumbi wa mikutano.

‘Hivi wewe..wewe. ...mbona umevaa hivyo,  kama upo nyumbani kwako, huoni kama ukionekana hivyo, utafikiriwa vibaya, na kwanini unafanya hivyo..?’ nikauliza huku macho yakivinjari ule mwili uliokuwa unaonekana kupitia kwenye ile khanga nyepesi. Macho yakawa ya kwanza kutekwa na ibilisi.

‘Nimeshakuambia siku ya leo nimejiandaa kwa ajili yako, ....ushindwe mwenyewe, kama wewe ni mwanaume kweli...’akasema akinisogelea, nilikuwa kama nimeshikwa na bumbuwazi,  sikuweza hata kusogea nyuma, na wakati huo mdomo ukawa mkavu, nikapitisha ulimi kwa haraka,na lile tendo likamfanya huyo binti atoe taabsamu lake ambalo lilikuwa likizidi kuniumiza.

Sio siri huyu binti alikuwa kajaliwa uzuri wa hali ya juu, ni kama wale warembo wa dunia, kaumbika vyema, na kila anachokifanya ni kama kimepangiliwa, ..nashindwa kuelewa kwanini msichana mrembo kama huyu anafanya mambo ya aibu kama hayo.

Tabasamu lake likanitoa akili ya kawaida ya kibinadamu, ni kama alifahamu kuwa akifanya hivyo, atakuwa kanilogezea, akili ikawa sio yangu, na kwa muda huo  akawa ananisogelea karibu na taratibu akaweka mikono yake laini kunishika kiunoni, na mkono wake ukawa umegusa mkono wangu kabla haujashika kiun changu, ule mguso wake, ulinifanya niwe kama mtu aliyeguswa na umeme, nikatetemeshwa mwili mnzima, nikazidi kupotewa na ufahamu wa kupambana na majairibu hayo,..

Huyu binti alipoona nimetulia, akatoa mikono yake kiuononi, akaanza kunifungua shati langu vifungo, huku analivuta kulitoa nje, nilikuwa nimechomekea vizuri  shati langu, na mara nyingi nipo hivyo,wakati huo akili ilikuwa sio yangu, nilikuwa kama nimezama kwenye giza nene, na akili haikuwa inafanya kazi.

Wakati ibilisi anataka kuniteka akili yangu, mara mlango wa nje ukagongwa, kwa haraka akili ikanirejea, nikawa kaam nimezindukana kutoka kwenye ndoto ya ajabu, na kwa haraka nikageuka na kutizama huku na kule, na yule mdada, akawa ananitzama usoni kwa macho yake malegevu, hakujali huyo aliyegonga mlango.

Mimi kwa haraka kama mtu aliyefumaniwa japokuwa hatukuwa tumefika mbali, lakini shati langu lilikuwa limeshafunguliwa vifungo, na sehemu kubwa ilikuwa imechomolewa, kwahiyo nikawa nafanya akzi ya kuichomeka vyema huku nahangaika kufunga shati langu vifungo,  lakini kabla sijafika mbali ule mlango ukafunguliwa, na aliyekwua kasimama mlangoni ni yule yule mchumba wa huyo binti, akiwa na mavazi yake ya kikazi na mknoni kashika silaha..

********

Kumbe jamaa huyu ni polisi kweli, siku zote akija hapa ofisini kumleta huyu binti anakuwa kavalia kiraia, na uutamfahamu kuwa anafanya akzi hiyo kutokana na gari lake, na ukakamavu wake, alikuwa na mwili ulioshupaa, na kuonyesha misuli yenye nguvu, na macho makali...

Mimi nikawa nimesimama kama mtu aliyepigwa na ganzi, nilijikuta natoa macho ya uwoga, yule jamaa hakusema neno, akasogea kati kati ya chumba, kwanza akanitupia mimi jicho, huku akinishangaa kwa jinsi nilivyokuwa nimemuangalia kwa macho ya uwoga,  halafu akageuka kuangalia kule alipkuwa kasimama mchumba wake, na alipomuona jinsi alivyovaa, akageuka kuniangalia, akasema;

‘Hebu niambieni ni kitu gani kinaendelea humu ndani, ndiyo kazi mliyokuwa mnafanya..eeh, ni uvaaji gani huo, kama watu wapo chumbani, angalia hili lijamaa, linaonekana kabisa limetokea kufanya ufusuka...?’ akauliza huku akiniangalia halafu akageuka kumwangalia huyo mchumba wake.

‘Mimi nilikuwa na kazi zangu bwana sivyo kama unavyofikiria wewe, sio kila mtu ni fusuka, naomba uniombe radhi....’nikasema.

‘Nikuombe radhi, ...nikuombe radhi wewe, fusuka mkubwa wewe, angalia shati lak linavyokuhukum, hata vifungo vyako hujavifunga vyema umefunga juu chini kama mtu aliyefumaniwa...utanitambua,subiri hapo,niongee na huyu malaya....’akasema akimuendea huyo binti huku silaha yake kaiweka begani.

‘Sikiliza mkuu, mimi nilikuwa ofisini kwangu, nimemaliza kazi zangu, na nilikuwa antoka , ...na kwa vile kuna joto, nilikuwa nimeacah shati kifua nje, sikujua kabisa kuwa nitaweza kumkuta huyo binti, na wakati nataka kundoka, na  huyo mchumba wako akatokea kama alivyo.....’nikageuka kumwangalia mdada, ambaye alikuwa anatikisa mguu kama vile anafuata mdundo fulani, huku kaangalia chini, na mikono yake kaweka kiunoni, akionyesha hana wasiwasi.

‘Na ndio mkaona mjipongeze kidogo, kazi na dawa au sio...aah, mimi sina neno,...ninachotaka ni ukweli, kwasabbu siku nyingi nimekuona ukimwangalia mchumba wangu kama fisi aliyona mfupa,...sasa leo nimakufuma kwa macho yangu mwenyewe,huna cha kujitetea hapa, ninachotaka kwasasa ni ukweli, niambie ukweli mlikuwa mnafanay nini?’ akauliza huyu jamaa akinikagua shati langu lilikuwa nusu wazi, na limechomolewa, na huo ulikuwa ushahidi kuwa kuna lolote lilikuwa linaendelea kati yangu na huyo binti.

Kwa kweli, moyoni nikawa najilaumu kwanini nilishindwa kuyakabili hayo majaribu japokwua sikuwa nimefanya lolote baya, zaidi ya huyo binti, kuanza kunifungua shati na kulivuta nje, na akilini nikawaza isije huyo binti alifanya hivyo makusudi ili huyo jamaa yake aje anifume, lakini kwa ajili gani....

‘Hapana, huyo ana mamb yake, alikuwa akifanya kazi ya kusafisha chumba cha mkutano ndio maana unamuona hivyo, hata mimi nilipomuna hivyo nikashituka ndio maana nikawa natoka nje kwa haraka ...’nikasema na yule jamaa akawa anamwangalai yule binti huku anatabasamu, na kusema;

‘Hivi alivyo , alikuwa anafanya usafi, kwanini unamtetea, acha aongee mwenyewe, au mumepanga kusema hivyo,....’akasema akitoa sauti ya mzaha, na watu husema huyo jamaa akiongea utafikiri anakutania kumbe mwenzako kakasirika, na kipigo chake ni lazima ulazwe hospitalini, kama hujavunjika kiungo cha mwili.

‘Nilipoona anamsogelea yule binti, mimi nikachukua mwanya huo kuanza kutoka kuelekea nje, na kabla sijaufikia mlango, nikasikia sauti ya kipigo,...

‘Wewe malaya, ulikuwa unafanay nini na huyo malaya mwenzako...?’ sauti ikauliza.

‘Malaya ni wewe mwenyewe, wewe mwenyewe hujioni, unabadili wanawake kama nguo, au unafikiri mimi sifahamu siri zako, kwanza kwanini unanipiga, mimi sio mke wako,..kuwa mchumba wako isiwe taabu, ninaweza kuvunja huo uchumba...’akasema kwa sauti ya kukasirika.

‘Unasema nini, unataka kuvunja huo uchumba kwasababu ya huyo malaya mwenzako, ngoja niiharibu hii sura yako unayojivunia nayo, tuone kama kuna mwanaume atakupenda,...’sauti ikasema na mlio kwa kibau ukasikika, na kilio cha huyo mdada kikatawa.

‘Mamaaa, kwani unanipiga, mimi sio mke wako, shetani mkubwa wewe nenda kampige mkeo na kuanzia leo tusijuane...’akasema na wakawa wanashikana kupigana, na mimi nikaingiwa na moyo wa huruma nikataka kugeuka kwenda kuwasaidia,

‘Samahani ndugu yangu yangu acha ghadhabu huyo binti hajafanya kitu kama unavyofikiria wewe...’nikasema nikiwa nimewakaribia, kilichoniziba mdomo ilikuwa ni teke lililonipata vyema tumboni, jamaa alikuwa mwepesi ajabu maana teke hilo lilikuja kama umeme,  na hata kabla sijaka vyema nikigugumia maumivu, nikapigwa kigoto cha puani,damu na kamasi vikaruka hewani,

Sijui hivyo vitendo vilitendwa vipi kwa haraka kiasi hicho, maana muda huo huo nikajiona nipo hwani, nikazungushwa kama gurudumu la gari na kutua chini, kama gunia la mkaa na kabla sijatulia, nikasindiliwa na buti la tumboni, karibu nitapike vyote nilivyokuwa nimekula,...na kama asingelikwua huyo mdada kumpiga kichwani huyu jamaa na mashine ndogo ya kutobolea karatasi, nahsi huyo jamaa angeliniua.

Ile mashine ilimpata bara bara, akapepesuka, na kabla hajadondoka chini akayumba huku akionyesha tabasamu la dharau,la kiuaji, na akayumba akapiga magoti, akashika kichwa, kilikuwa kinavuja damu, mimi nilipoona huo mwanya nikasimama, na kwa haraka nikakimbilia nje na walati natoka nje nikakukutana na walinzi, wakija kwani walishasikia kilio cha huy binti.

‘Kuna nini huko ndani?’ wakauliza.

‘Sijui naona huyo mwanaume kaingia na kuanza kutupiga, yeye anafikiria huenda nilikuwa na nia mbaya na mchumba wake...’nikasema na huy mlinzi kwa haraka akanikagua shati langu lilivyokuwa, limetoka nusu na vifungo havijafungwa vyema,.....’nikasema huku nikiharakisha kwenda kuchukua pikipiki langu, na kuliwasha na kuondoka kwa mwendo wa kasi, sikugeuka nyuma hadi nyumbani kwangu, nilipofika kabla sijafungua mlango simu yangu ikaita, nilipoangalia nikaona ni namba ya bosi wangu.

‘Bosi habari za saa hizi ..’nikasalimia huku nikihema.

‘Upo ofisini au upo nyumbani ?’ akauliza

‘Nipo nyumbani...’nikasema

‘Mbona nimesikia kuwa upo ofisini, mnapigana na yule mchumba wa mtu?’ akauliza

‘Hapana, mimi niliondoka mapema tu, nilipomuona huyo jamaa akiingia , nilijua akiniona humo ofisini na mchumba wake atanifikiria vibaya..’nikasema

‘Ina maana muda wote mlikuwa na huyo mwanamke, alikuwa hajamaliza ile kazi, nilimwambia ikifika saa kumi na mbili kama hajamaliza aondoke?’ akaniuliza

‘Mimi nilikuwa sijui kama yupo humo ofisini, wakati natoka ndio nikakutana naye..’nikasema

‘Mkaanza maongezi, au mapenzi?’ akaniuliza

‘Alianza kunisemesha, na mimi nikaona sio muda mnzuri wa kuongea naye, na wakati naondoka ndio huyo mchumba wake akaingia’nikasema

‘Lakini nimeambiwa huyo mwanamke amevaa nguo za kuashiria mabaya, ...sikiliza nimeshakukanya maswala ya mapenzi ofisini, na hili litakuwa mara ya pili linatokea ofisini kwangu, mimi nimesema  sitaki uchafu huo ofisini kwangu, ...mimi kesho nitafanya uchunguzi  wa kina kama nikagundua kuwa kulikuwa na jambo kama hilo, utawajibika..’akasema kwa hasira.

‘Bosi natumai unaniamini, mimi sijawazia kufanya hilo, ninachokuambia ndio ukweli wenyewe, kama ningelifahamu kuwa huyo binti yupo humo ofisini, nisingelikaa humo, ningelikwenda kuifanyia hiyo kazi nyumbani..’nikasema

‘Sawa, tutaongea kesho, ila nimesikia kuwa, huyo mwanadada kaumizwa vibaya sana  yupo mahututi hospitalini, na jamaa yake, kashikiliwa na wenzake,... sasa sijui, kesi ya ngedere kupelekewa tumbili,...sijui ni kitu gani kilitokea, siwezi kukifuatilia kwasasa hadi kesho.....’akasema

‘Saw bosi tutaongea kesho....’nikasema na bosi akakata simu.

***********

Asubuhi kukawa na kikao kikali, bosi alikuwa kakasirika sana, na bila kuficha akaniita mbele ya wafanyakazi na kunihoji, mimi nikajieleza kama ilivyotokea, na kwa vile yule binti alikuwa hayupo, kukawa na hakuna maswali mengi zaidi, lakini walinzi walisema kuwa, dalili walizoziona ziliashiria kuwa mimi na huy binti tulikuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi.

‘Bosi nakuomba uniamini, mimi sijafanya kama wanavyodai hawo walinzi, huyo binti alifanya hivyo kwa nia ya kunitega, na nahisi alifanya hivyo, ili bwana wake aje anifume, lakini mimi nikamshitukia, na shati langu lilichomoka tu, na kwa vile nilifahamu nipo peke yangu sikujali kuliweka sawa...’nikasema.

‘Kama unasema wawili hawo walipanga iwe hivyo,  mbona basi huyo bwana wake alimpiga huyo binti, ...sizani kama walipanga hivyo, lakini nitalifanyia uchunguzi wa kina, na nakuonya tena, ikitokea mara ya pili, mimi sitavumilia nitakufukuza kazi kwa kukiuka sheria na mkataba wako wa ajira...’akasema na mimi nikamuahidi kuwa nitajitahidi kuwa mbali kabisa na huyo binti, kwani naona hana nia njema na mimi.

‘Na iwe hivyo kweli..vingenavyo utamsikia kwenye bomba wakati upo mitaani, au jela ukinyea kopo, na ukikiuka ahadi yako hapa kwangu,nitahakikisha unasota mitaani, au jela, kwani sifa zako zitakuwa zimesharibika...’akasema.

Hali hiyo ikapita ikabakia minong’ono, na wengi wakidai kuwa nimefumwa, nikizini na mchumba wa watu, lakini sikuyatilia maanani na wala sikutaka kubishana na watu nikawa kimiya nikimuachia mungu anisaidie.

‘Ngoja tuendelee na kisa changu, hayo ya mapenzi yenu tuyaache kwanza, nitalifanyia uchunguzi,..’akasema aliponiita ofisini kwake,.

‘Kinachonishangaza ni hii tabia chafu inayoendelea kwenye ofisi yangu, hili sasa linakuwa ni tatizo, na nikigundua kuwa huyo binti ndiye chanzo cha hay a yote itabidi nimsimamishe  kazi kwa muda, hata kama baba yake ana hisa na mimi..’akasema

‘Ina maana kumbe baba yake ana hisa kwenye kampuni yako?’ nikamuuliza

‘Ilibidi nifanye hivyo, kwa ajili ya kibiashara zaidi, lakini sio kwamba kwa vile ni mtot o wa mshirika wangu wa biashar ndio niache afanye atakavyo, mwenyewe anamfahamu vyema mzazi wake huyo hana mzaha kwenye kazi, ...’akasema

‘Sawa bosi tuendelee na kisa chetu, au?’ nikasema na bosi akaniangalia kwanza kwa makini na kuniuliza swali.

‘Umempenda sana huyo binti?’ akaniuliza

‘Hapana bosi,..niamini bosi..’nikasema.

*********

‘Sehemu iliypita ulianza kuona masiha yangu na mama wa kambo,  sasa tutaingia zaidi kuona masiha hayo, na jinsi gani nilivyotaabika na mama wa kambo,na siku ile nilishaamua kumwambia baba kuhusu mateso hay japokuwa kaka yangu alinizuia nisimuambie baba, akijua kuwa baba hatatusikiliza.

‘Mdogo wangu jaribu kuvumilia, ..’aliniambia kaka yangu lakini kwa vile mimi ndiye niliyekuwa nikiteseka zaidi nikaamua kumwambia baba.

‘Baba , kazi za hapa nyumbani zimekuwa nyingi sana, tunasoma kwa shida, inabidi kuamuka asubuhi kufanya kazi za ndani kabla ya kwenda shule na ukurudi nyumbani halikadhalika, hata kazi za masomo ya nyumbani sipati muda wa kuzifanya..’nikaanza kulalamika

‘Mbona mama yenu anasema nyie hamfanyi kazi, sana sana wanaofanya kazi ni ndugu zenu tu, na nyie mnakuja kuongea mambo mengine kabisa..’akasema baba

‘Mama anasema kuwatetea watoto wake tu, lakini wao hawafanyi kazi kabisa, kazi zote tunazifanya sisi, akinisaidai kaka yangu ..’nikasema

‘Ngoja nitamuuliza mama yenu na kama ni uwongo, nitawadhibu kweli kweli..’akasema na kabla hajamaliza mara mama akatokea na alipotuoa tunaongea na baba akahisi kuna jambo, kwanza akauliza

‘Wenzenu wapo wapi?’ akauliza

‘Wanacheza nyumba ya jirani..’akasema kaka

‘Ina maana ile kazi waliyokuwa wakiifanya wameshaimaliza ..’akauliza na hapo nilijua ananiuliza mimi kazi aliyoniambia niifanye nimeshaimaliza , na mimi nikasema

‘Nimeshaimaliza mama ile kazi, sio wao....’nikasema

‘Sasa mnafanya nini hapa?’ akauliza huku akimwangalia baba , halafu akaniangalia mimi.

‘Watoto wanalalamika kuwa unawafanyisha wao kazi nyingi, na watoto wengine kazi ya ni kucheza tu hawafanyi kazi, kazi anayefanya ni huyu na kaka yake tu...’akasema baba.

‘Ndivyo walivyokuambia ehe, na ukawaamini ....?’ akauliza huku kashika mikono kiuononi, na kabla mume wake haajsema neno, akaendelea kuomngea.

‘Watoto hawa ni wanafaiki wakubwa,  siumesikia nikiwauliza wenzao wako wapi, ina maana kuna akzi niliwapa kila mmoja na kazi yake, na unaona wenzao wameshamaliza kazi zao,na hawa kwa uvivu wao walikuwa bado waanjivuta vuta....’akasema mama .

‘Huyu mtoto ni mvivu, wenzao walishamaliza kazi zao, sasa yeye anajifanya kuwa alikuwa akiifanya hiyo kazi peke yake, sio kweli, ..ukiwasikiliza hawa watoto, tutakuja kukosana wenyewe humu ndani...watoto hawa, ni wanafiki hawana lolote..’akasema na baba akatuambia tuondoke mbele yake, maana eti sisi ni waongo.

Maisha yakawa hivyo, na muda wetu wa kupumzika ni ule tu wa kwenda shule, na mara nyingi tulikuwa tukitamani kukaa huko huko shuleni, japokuwa mchana tulikuwa tuna muda wa kurudi nyumbani kupata chakula cha mchana, lakini mimi niliona ni bora nikae shuleni na njaa yangu kuliko kurudi nyumbani, kwani hata nikirudi nyumbani chakula chenyewe naweza nisikipate, nitaishia kufanya kazi, na hata shuleni naweza kuzuiwa nisirudi tena.

**********

Baba muda mwingi alikuwa kwenye mgahawa wake, ambapo kulikuwa na biashara ya chai, na vitafunio vyake  kama maandazi, vitumbua, chapatti na sambusa, ikatokea siku moja pesa ikapotea na aliyepoteza alikuwa ni dada yangu wa kambo, na  dada yangu huyo akanisingizia mimi kama kawaida yao, kuwa mimi ndiye niliyepoteza;

Mama alikuwa amekasirika, na baba akawa yupo wanatuuliza kwa pamoja

 ‘Huyu atakuwa kaziiba, na sasa anasingizia kupoteza....’akasema mama na kunifanya nibakie mdomo wazi, kwani katika maisha yangu sijawahi kuiba, mama alishatukanya kabisa tusje kuchukua pesa bila idhini ya wazazi, na sisi wote tunalifahamu hilo.

‘Mama mbona mimi sijachukua hizo pesa, aliyekuwa nazo ni huyo...’nikamtaja dada yangu huyo wa kambo, akiwa pembeni yangu na haraka bila aibu huyo dada yangu akasema;

‘Muongo huyu, nilimuona akiziiba akaondoka nazo, ananisingizia tu...’akasema huyo dada wa kambo, na mama aliposikia hivyo akasema;

‘Mbona mlipokuwa hampo haijawahi kupotea pesa, huoni kwamba nyie ndio mumeanzisha hii tabia, na huyu mtoto mtoto anatabia mbaya sana ya wizi, nilikuwa sijamuamboa baba yako aheri leo kajionea mwenyewe ...’akasema mama.

‘Mimi sijachukua pesa....nilikwenda huko mgahani mara moja, tukiwa na mwenzangu na yeye ndiye aliyechukua hizo pesa akisema wewe ndiye uliyemtuma...’nikasema.

‘Unaona jinsi gani alivyo muongo,sasa anasema mimi ndiye niliyemtuma huyo ndugu yake, kwanza tukuulize huko mgahawani ulifuata nini?’akaniuliza mama na baba wakati huo alikuwa kakasirika kweli.

‘Nilikwenda kuchukua ufagio...’nikajitetea

 ‘Unaona hebu muulize toka lini ufagio wa huko mgahawani ukatumika huku nyumbani, huku kuna ufagio wake, kwanini ulikwenda kuchukua huo ufagio wa huko,...ni ujanja wako wa kupata mwanya wa kudokoa pesa, mimi nilishakuambia huyu mtoto ana tabia mbaya, na kila siku nalalamika pesa zinapotea, kumbe ni mwizi wet yupo humu humu ndani....’akasema mama

‘Hebu niambie vizuri pesa hiyo umeipeleka wapi?’ akauliza baba kwa hasira akinitolea macho yaliyojaa hasira...mimi nikaanza kulia, niliona ninaonewa, sikuweza hata kujitetea zaidi, sikujua hata niongee nini tena, nikajikuta nalia tu huku nikuita mama yangu;

‘Mama yangu njoo nisaidie, nimekosa nini , mimi mama,hawa watu hawanipendi , kila siku wananisingizia uwongo, mimi sijaiba jamani ...’nikawa nalia.

‘Mama yako ndiye aliyekutuma uje uuibe pesa, unaiba ili umtumie hizo pesa...?.’akasema huyo mama wa kambo kwa hasira.

‘Baba mimi sijachukua pesa,..mbona hamniamini mimi, sijawahi kuiba katika maisha yangu, kwanini nije kuiba huku...’nikajitetea, lakini baba hakuniamini tena, akaanza kuniadhibu, kwa kunichapa, na alipomaliza mama akaona hiyo haitoashi akanichukua, sikujua ananipeleka wapi, wakati huo nalia sana, maana naonewa, sijafanya kosa naadhibiwa tu, na wadogo zangu, yaani watoto wa mama wa kambo wakawa wanashangilia wakisema

‘MwIzi huyo mwizi huyo....’hata yule ambaye ndiye aliyepoteza hizo pesa akawa ndiye anashabikia zaidi...’

Mama alipoona kuwa baba kanichapa kidogo tu, yeye kwa hasira akanishika mkono huku akisema;

‘Huyu tusipo mpa fundisho, tabia hii hataiacha, wewe uanmgusa gusa na fimbo, watu kama hawa wana adhabu yao...’akasema huku akivuta kunipeleka ndani wanaposagia nyama ya sambusa kisha akachukua kidole changu na kukitumbukiza ndani kisha akaanza kusaga japo hakikusagika sana, kilichofika juu, juu, ulikuwa huu mkono wa kushoto, unana hapa kidole changu hakipo sawa.

Baba muda huo alikuwa karudi kwenye mgahawa wake, mama akawa anaendelea na adhabu zake akaona hiyo haitoshi, akachukua pasi, akaiwasha ikapata moto

‘Mama mimi sijaiba mbona mnanionea...’nikawa nalia hata kaka yangu nilimuona machozi yakimtoa, lakini hakuwa na la kufanya, mama akachukua ile pasi yenye moto, akashusha nguo, yangu na mara pasi ikabadika mgongoni, maumivu niliyyasikia, ilikuwa karibu kupoteza fahamu nikadndoka chini, huku hata sauti ya kulia haipo tena

Mama alipoona nimedondoka chini, akahisi nimekufa, akaichukau ile pasi na kuweka pembeni, akakimbilia nje, na aliyetoka haraka kwenda kumtafuta baba alikuwa kaka yangu, na baba akaja haraka na kuuliza;

‘Kuna nini tena,....’akaniona nipo sakafuni, nimetulia nikiwa nimeishiwa nguvu kabisa ya kulia tena, nilikuwa kama mtu aliyepoteza fahamu.

‘Amaefanya nini huyu...?’ akauliza baba, na mara mama akaja kwa haraka, na yeye akauliza

‘Kwani kafanya nini...?’ akauliza

‘Kaungua na pasi...’akasema binti wa mama huyo

‘Kaungua vipi mgongoni,?’ akauliza baba akionyesha mshangao huku akiangalai lile jeraha, naona hata yeye aliingiwa na wasiwasi maana lilikuwa ni jeraha kubwa.

‘Hawa watoto bwana, hapa nikumpeleka hospitalini, hakuna haja ya kuuliza uliza tumuwahishe hspitalini...’akasema mama na haraka wakaniinua na kunibeba na kunikimbiza hspitalini

Walipofika haspitalini wakadai kuwa ni utoto, tuliunguzana wakati tunachezea pasi ya umeme. Docta alinikagua lile jereha, na kusema jereha hilo ni kubwa sana, ni lazima nilazwe.

‘Watoto hawa watundu kweli kweli, wakati wanajifanya wananyosha nguo na mwenzake kwa bahati mbaya mwenzake akapitisha pasi mgongoni mwa huyu ndio akaungua kiasi hiki..’akasema mama akimwambia dakitari, na mimi sikuwa na la kusema, niliogopa sana kusema mama ni muongo, nikanyamaza kimiya huku nikimshukuru mungu tu.

‘Lakini jereha hili linaonyesha ni kama mtu alidhamiria, akawa kaikandamiza pasi, huoni limeenda ndani sana..’akasema docta.

‘Ni utoto, nafikiri sasa watakoma ubishi kuchezea pasi tena...’akasema mama.


Nilikaa hospitali kama wiki mbili mpaka hapo nilipopata nafuu nikaruhusiwa. Baba akajaribu kutafuta undani wa tukio zima na ukweli ukadhiri, baba mzazi akajua ukweli ulivyokuwa,hapo baba akaona ili kuepusha shari ni bora turudishwa tena kwa mama yetu mzazi huko kijijini.

Siku ya pili yake ,tulirudi mimi na kaka yangu,mama aliptona jinsi tulivyokonda na kumuhadithia yaliyotukuta, akakasirika sana, na kusema hata siku moja hatarusu mtoto wake kwenda huko mjini tena, mama akaendelea na kazi sisi huku ndugu wa tatu tunaendelea na masomo katika shule ya serikali ya hapo kijijini.

Kwa vile kwa asilimia kubwa mama alikuwa ndiye anayetulisha kwa kiasi kidogo anachopata kwenye mshahara wake, maisha yalikuwa ni magumu sana, lakini hata hivyo, mama hakukata tamaa, akawa anajitahidi kwa hicho kidogo anachokipata.

Maisha huko mjini kwa mama wa kambo yakawa ni ya shida, ikabidi baba na mama huyo warudi hapo kijijini kwa muda, na mama akawa ndiye anayetegemewa na kipato chake kidogo cha mshahara wake anachopata, na kwahiyo maisha yakazidi kuwa mabaya zaidi. Na mama huyo wa kambo alipokuwa hapo, utafikiri kama sio yeye, alikuwa mpole, anajifanya anatupenda.

Baadaye baba akahangaika, na akafanikiwa tena kuweza kufufua ile biashara yake huyo mjini, kwahiyo wakaondoka na mke wake, yaani huyo mama wa kambo.

Maisha huko mjini yakawa mazuri, na baba akaja na kuongea na mama, akamwambia kwa vile maisha huko mjini ni mauri na hapo kijijini hali ni ngumu, basi ni bora mimi na mdogo wangu wa mwisho twende tukasomee mjini.

‘Watot wangu waende huko mjini tena, hapana, ...’akasema mama, lakini baba akasema mama kesabadilika, baada ya kumsema sana, hawezi kuwatesa watoto tena, na yeye mwenye atahakikisha tunaishi bila shida.

Mwisho wa siku mama akakubali, apo tena ikaamuliwa kwenda kuishi huko mjini,, safari hii alinichukua mimi na mdogo wangu wa mwisho na kutupeleka tukasomea huko mjini, na kipindi hicho mimi nipo darasa la sita.

‘Mama mimi siendi huko mjini...’nikasema nikikumbuka yaliyonipata kipindi kile.

‘Mimi nitakwenda kama hutaki,...’akasema mdogo wangu, yeye alikuwa mdogo sana, hakuwa anafahamu ni nini anakwenda kupambana nacho huko, hata hivyo huyo mama hakuwa akiwanyanyasa sana watoto wa kiume ni mimi tu alikuwa akiniandama sana sijui ni kwanini.

Mama akaniagalia na kuniambia,

‘Mtoto wangu mimi nataka ukasomee huko mjini, ili ufaulu masomo yako, shule hii ya hapa kijijini hutaweza kufaulu, na masmo ni muhimu sana katika maisha yenu...’akasema mama.

‘Lakini mama , huko mjini ninvyofahmu mimi, naenda kufanyizwa kazi tu, sitapata hata muda wa kusoma...’nikalalamika.

‘Nimeongea hilo na baba yako, kasema safari hii atahakikisha hamteseki tena, usiwe na wasiwasi mwanangu ni muhimu sana mkawa mnamtii baba yenu...’akaniambia, japokuwa ilionekana kabisa hakupenda iwe hivyo, hakutaka kabisa kuachana na watoto wake hasa huyo mdogo wetu, lakini hakukuwa na jinsi ikabidi twende tena huko mjini. Nikimuomba mungu hali ile ya mateso isirejee tena...

NB: Je hali ni ile ile, au kutakuwepo na mabadiliko kama alivyoahidi baba

WAZO LA LEO: Majaribu na mitihani ya kimaisha ni mingi, ya kila namna kwa wanadamu, yanapotukuta tunahitajika kupambana nayo, tusikate tamaa, wala kuyakimbia kwa visingizio mbali mbali, kwani yote hiyo yapo kwa ajili ya kupima, taaluma zetu, imani na misimamo yetu, tujitahidi kupambana nayo, na silaha yetu kubwa iwe ni elimu, elimu ndiyo silaha ya mambo mengi ya kimaisha. Tusome, tufanya utafiti wa kina, kabla ya kufikia maamuzi...

Ni mimi: emu-three

No comments :