Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, December 11, 2013

Mkuki ni kwa Nguruwe-45


Baada ya kuhakikisha kuwa kila mtu aliyestahili kufika kwenye kikao amefika, na wale ambao hawajafika washatanguliza dharura zao, kikao kikaanza, na kwa vile mimi ndiye niliyekiomba hicho kikao, nilitakiwa mimi nimkaribishe mwenyekiti , lakini kwa heshima, nikamuomba mume wangu aifanye hiyo kazi, ya kumkaribisha mwenyekiti ili kikao kianze.

Mume wangu akasimama kuwakaribisha wajumbe, na kumkaribisha mwenyekiti wa kikao,ambaye ni baba yangu. Baba kaba haajasena neno aligeuka kuniangalia mimi, nahisi kuna kitu alikiona sio kawaida, na, kabla hajasema neno mara mlago ukagongwa.....

Watu wote wakageuka kuangalia mlangoni, kwani haikutarajiwa kuja mtu mwingine, kwahiyo kila mmoja alikuwa na mawazo yake, kuhusu huyo aliegonga mlango, wengine walihisi ni askari, wengine wakahisi huenda ni wafanyakazi wa hapo wananihitajia mimi, ilimradi kwa muda mfupi kila mmoja alikuwa na wazo lake. Mwenyekiti akanigeukia, kutaka kuniuliza, lakini kabla hajasema neno, mlango ukafunguliwa na akaingia mtu akiwa bado na kofia la waendesha pikipiki, kuonyesha kuwa ni mwendesha pikipiki, na mimi nikakumbuka yule mtu aliyenipita, na kunipungia mkono, sikujua ni nani kwa muda ule.

Huyu mtu, alipofungua mlango, akiwa kavalia jaketi la kuzuia upepo mwilini, na kumfanya aonekane bonge, alismama na kutuangalia akiwa na kofia lake lile lile, inaonekana hakutaka kulivua huko nje, labda kwa vile aliona keshachelewa, kama ni mjumbe wa kikao hiki, ambaye mimi sikuwa na habari nay eye,au alifanya hivyo kwasababu zake nyingine. Kila mmoja ndani ya kikao alimwangalia yeye, na yeye alipoona watu wote wanamtizama, akafanya mambo mawili kwa haraka,  kwanza akainama, kama vile anasalimia au kutoa heshima na pili, akageuka kuangalia mlangoni, akalivua lile kofia lake na kuvua koto , halafu taratibu akageukia watu, na kusema;

‘Samahani mwenyekiti, nimechelewa, nilikuwa naweka mambo sawa...jamaa wananifuatilia kila kona...’ akasema huku akiangalia pale alipokaa mwenyekiti, lakini alikuwa hamuangalii moja kwa moja usoni, na mwenyekiti akasema;

‘Huyu amefuata nini kwenye hiki kikao...?’ mwenyekiti akaniuliza na kabla sijamjibu akamgeukia huyo mtu na kusema;

‘Kikao hiki hakikuhusu, hiki ni kikao cha watu maalumu, sizani kama wewe ni mmoja wa waalikwa, kama unavyoona hawa ni wanafamilia, na watu maalumu...’akasema mwenyekiti.

‘Lakini mimi nimealikwa....’akajitetea huyo mtu.

‘Ni nani aliyekualika, majina yote ninayo hapa, sijaona jina lako,..., kwanza wewe unatafutwa na polisi, ukionakena hapa tutaambiwa kuwa tunakuficha, na tuna mipango na wewe, tafadhali, ondoka, usituharibie mipangilio yetu, sisi sio wavunja sheria...’akasema baba, na mimi nikaona niingilie kati nakusema;

‘Baba , oh mwenyekiti, mimi ndiye niliyemualika huyu mtu, nilimualika wakati nimeshakupa hayo majina ya wajumbe, kwani sikuwa na uhakika naye, kwa vile alikuwa haonekani, lakini ni mmoja wa watu muhimu kwenye hiki kikao, kuwepo kwake kunahitajika ili aweze kutoa ushahidi, kutokana na mambo tutakayoyaongelea leo hii hapa...’nikasema na mume wangu akadakia na kusema;

‘Unasema anakuja kutoa ushahidi, mdogo wangu, ana ushaidi gani hapa, kwani kuna kesi ya nani, sijaelewa mke wangu, anyway, vyovyote iwavyo, lakini kitu kinachomuhusu mdogo wangu nilitakiwa mimi nifahamu..’akasema akikunja uso, kuonyesha kukerekwa.

‘Utayafahamu baadaye, kikao hiki nimekiitisha mimi, kuna mambo mengi ambayo yatajitokeza, na yeye anayafahamu zaidi yako, kwa vile wewe ulikuwa unaumwa,....’nikasema

‘Sio kweli, mdogo wangu hawezi kufahamu jambo, mimi nisiwe nalifahamu, kuna kitu gani anakifahamu mimi nisikijue, kwanini unataka kumuingiza mdogo wangu kwenye matatizo.. huyu ni mdogo wangu, mimi ndiye mwenye dhamana naye, ...kama alivyosema mwenyekiti ni bora mdogo wangu uondoke, maana polisi hawana dogo wakikuona hapa watakimbilia kukufunga, kabla hatujaweka mambo sawa, nenda huko ulipokuwa tutakuja kuonana baadaye kwanza nakuhitaji sana......’akasema mume wangu.

‘Subiri kwanza, hiki kikao nimekiitisha mimi, na ajenda zote za kikao ninazo hapa kama katibu, na kwa bahati mbaya sikuwawagaia ajenda za kikao hiki, kwasababu maalumu, mimi sijwahi kumuingiza mdogo wako kwenye matatizo, ni wewe ndiye uliyemuingiza ndugu yako kwenye matatizo, kama tutakavyokuja kuona huko mbele, ...kwahiyo yeye ni mjumbe wa hiki kikao, na kuwepo kwake hapa ni kwa ajili ya kusema ukweli, ulitokana na wewe, yeye hawezi kuondoka mpaka huo ukweli uthibitishe...’nikasema

‘Aje kusema ukweli upi mke wangu, usitake kikao kituelewe vibaya, kuwa mimi sijui wajibu wangu, kila kitu hapa ni sahihi, na nathibitisha hilo, kwani siongei kinyume na mkataba wetu,wa kifamilia, ....’akasema na kuushika mkataba mkononi, utafikiri ndio mtetezi wake.
Mwenyekiti akaingilia kati na kusema;  ‘Hebu tusikilizane kwanza..’akasema na sisi tukatulia,

‘Kwanza , mimi kama mwenyekiti sijakubaliana na kuwepo kwa huyu mtu hapa, kwani anatafutwa na polisi, mnafahamu kuwepo kwake hapa ni kuvunja sheria,na mimi sio mvunjaji wa sheria, kama mwenyekiti ninaamuru huyu mtu atoke kwenye hiki kikao...’akasema mwenyekiti.

‘Hata mimi nakuunga mkono mwenyekiti...’akasema mume wangu.

‘Mwenyekiti, naomba huyu mtu awepo, na kama ni swala la uvunjifu wa sheria, hilo tutakuja kulimaza baadaye, kuwepo kwake, hapa kutasaidia kuyaweka mambo yote sawa, na huenda tukaisaidia hata hiyo polisi kwa hayo wanayoyatafuta..’nikasema na baba akaniangalia kwa makini, na akageuka kumwangalia huyo mtu,

‘Mimi bado sijaafiki kwasababu muda uliopita niliongea na mkuu wa upelelezi wa eneo lenu nikamkatalia kabisa kuwa huyu mtu sijawahi kumuona, na nikimuona moja kwa moja nitamfikisha kwao, au nitawaita waje wamchukue, na sasa hivi napiga simu waje wamchukue...’akasema

‘Usifanye hivyo baba, huyu ni mdogo wangu, na mimi ndiye nabeba dhamana naye, kama polisi wanamuhitaji kwanza waje kuonana na mimi,...mdogo wangu hana hatia, kama wanavyodai wao, wanamuhisi tu..mimi ndiye niliyesababisha aonekane hivyo...’akasema.

‘Wewe ndiye uliyemtia hatiani,..basi polisi wakija utawaambai hivyo, lakini kuwepo kwake hapa ni ukiukwaji wa sheria....’akasema baba.

‘Baba usijali tuendelee na kikao, ...’nikasema na baba akasema;

‘Sawa mimi naendelea na kikao, lakini msimamo wangu ni huo huo, huyu mtu atoke nje, ...na kwa vile nimemuona, nitawapigia polisi waje wamchukue..siwezi kwenda kinyume na sheria...’akasema

‘Kwanza mume wako kasema kuwa nyie katika familia yenu mna katiba, na Katina hiyo ndiyo inayowaongoza,..naona katika ajenda zako katibu, hilo swala la katiba umeliweka kuwa la kwanza, na mume wako keshalianza, naona tuanze na hicho kipengele, cha katiba, kwanza nataka kufahamu kwanini mliamua kuanzisha katiba, maana familia zipo, na sijawa kusikia mume na mke wakawa na katiba? Akauliza mwenyekiti, na mume wangu akasimama;

‘Nafahamu kuwa swali hilo limemlenga mke wangu,kwa vile ndiye mwenye hiki kikao, na diye alitakiwa aataje ajenda zake, na bahati mbaya , kikao kimeanza juu kwa juu, kutokana na hili lilitokea, ...ni kweli ndugu mwenyekiti, katika familia yangu, nikiwa na maana mimi na mke wangu na watoto, tuna aktiba yetu inayotuongoza....’akatulia kidogo akiishika ile katiba.

‘Kwanini tuliamau kuwa na katiba, ni kwasababu kwanza tulitaka familia yetu iongozwe kitaalamu zaidi, ...lakini sababu kubwa ya kimsingi ni kuwa tulijiona kuwa na mambo mengi, mimi nikiwa nashughulika kwenye kampuni yangu, na mke wangu kampuni yake,lakini vyote hivyo ni vyetu, japokuwa kitaalamu kutokana na hisa kila mmoja alikuwa na mamlaka na kampuni yake...’akatulia

‘Kwa vyovyote iwavyo, mnapoona, hata kama mke alikuwa na vitu vyake, kampuni yake, mali yake, lakini akishakuwa mke wa mtu, basi kila kitu chake kinakuwa kwenye mikono ya mume....na hili tumelibainisha kwenye katiba yetu....’akasema akitaka kufungua hiyo katiba.

‘Mhh, usifungue hiyo katiba kwanza, ninachotaka kufahamu ni kwanini mliamua kuanzisha hiyo katiba, na kwa ufupi tumeelewa...swali langu la pili, je katiba hiyo imesajiliwa kisheria au ni katiba yenu tu kwa ajili ya mambo yenu ya ndani?’ akauliza

‘Sisi baba, ndug u mwenyekiti, kila kitu tumekipeleka kitaalamu, katiba yetu imesajiliwa, na aliyeiandika ni mwanasheria, kwahiyo katiba yetu ni kisheria, imetimiza matwakwa yote ya kisheria, ..hatuna matatizo na hilo....’akasema

‘Kwahiyo unataka kusema kila kitu chenu, taratibu zenu za kila siku mumeziainisha kwenye hiyo katiba, na likitokea tatizo, mnahukumiana kutokana na katiba yenu?’ akaulizwa

‘Ndio mwenyekiti, ndio maana nashangaa kikao hiki, kuitishwa na mke wangu, nilitakiwa mimi ndiye nikiitishe, lakini kuna dharura kama hizo, kama ikitokea dharura,basi mmojawapo anaweza kuitisha kikao, lakini ilitakiwa mimi niambiwe kila kitu, kwanini kikao kiwepo, hilo halikufanyika...nimeshitukiziwa tu, kuna kikao, cha nini na kwanini, sijaambiwa, huo ni ukiukwaji wa katiba...’akasema

‘Ndugu mwenyekiti naomba niliongee kidogo kuhusu hii katiba, samahani sana, kwani mimi ndio mwenye mamlaka, wa familia yangu, na kwahiyo nina mamlaka ya kuona kila kitu kinaenda sawa...’akasema na mwenyekiti akageuka kuniangalia, mimi nikamuashiria amuache mume wangu aendelee

 ‘Watu wanapofunga ndoa, wanakuwa na taratibu zao, kama mke na mume, na wanakuwa wameshajitoa kwenye mamlaka ya baba na mama zai, hawalindwi au kuchungwa tena na familia za baba na mama zao, kikeni au kiumeni, wao ni watu huru, na wanakuwa na utaratibu wao kama familia inayojitegemea, na  ndivyo tulivyofanya sisi, na kwa ajili ya kurahisisha mambo yetu tukaona tuwe na katiba, ni wachache sana wanakuwa na utaratibu kama huo, ....’akasema mume wangu.

‘Sisi tuna katiba inayokubalika kisheria, kwasababu imeandikwa na mwanasheri a wa familia, yetu, na sote tukaweka sahihi zetu, mimi na mke wangu, na wakili wetu..ikapitishwa na kusajiliwa kwa msajili wa mambo hayo, sio katiba ya mitaani , ni Katiba iliyokubalika kisheria, ukiangalia hapa ina kila sifa zote za kisheria, ...mimi kama kiongozi wa familia naitumia hii katiba na ninaweza kumshitaki yoyote atakyeingilia mambo yetu ya ndani....’akasema.

‘Kwahiyo itakuwa ni ajabu kama mtu atakuja na kuingilia familia yangu,wakati yeye ana familia yake,  .....’akasema na mwenyekiti akauliza

‘Hiyo Katiba yenu iliandikwa lini?’ akauliza

‘Muda mrefu sana, kipindi wakati tuna mtoto mmoja, imeshafanya  kazi zaidi ya miaka mitano, kwahiyo sio kitu kigeni ndani ya familia yangu...’akasema

‘Naomba niione hiyo katiba..’akasema mwenyekiti, na mume wangu akasimama huku akiwa kashika ile katiba na kwa madaha, akaelekea pale alipokaa mwenyekiti kumkabidhi hiyo katiba, na wakati huo shemeji yangu alikuwa bado kasimama, alikuwa hajafahamu kuwa akae au aondoke, na mimi nikamuonyeshea ishara kuwa akae kwenye kiti. Na mwenyekiti akamuona , na haraka akasimama na kusema;

‘Mimi sijakuruhusu ukae, mimi bado sijakukubalia na uwepo wako kwenye hiki kikao, kama mwenyekiti siwezi kukaa kwenye kikao kinachovunja sheria, nimeshasema huyu mtu anatafutwa na polisi, kuwepo kwake hapa ni uvunjifu wa sheria....’akasema mwenyekiti  na mimi nikasema;

‘Mwenyekiti nakuomba uniamini, huyu mtu ni mtu muhimu sana kwenye kikao hiki, nakuomba umruhusu awepo, na kama ni uvunjifu wa sheria mimi nitalijibu hilo, ...’nikasema.

‘Mimi nakubaliana na mwenyekiti, ndugu yangu atoke nje, kwanini  mke wangu unamkaidi mwenyekiti, mimi kaka yake nipo , nitawakilisha mawazo yake, kwanini ung’an’ganie awepo apa, au unataka polisi waje wamkamate...’akasema na kuongeza kusema;

‘Mke wangu umekuwa ukimuandama sana mdogo wangu, sijui kwanini,kama kuna lolote dhidi yangu niambie mimi, na sio kumtumia mdogo wangu kinyemela,mimi sipendi, kama kaka yake ninaamuru atoke kwenye hiki kikao, mimi nitawakilisha mawazo yake kama kuna umuhimu huo, ni kwa usalama wake kwa sasa, mengine aniachie mimi ...’akasema mume wangu.

‘Hata mimi sioni umuhimu wake hapa, maana anatafutwa na polisi akionekana hapa itaonekana kuwa tunamficha sisi, au nimuite mkuu wa upelelezi aje amchukue,...’baba akasema huku akinua simu yake kumpigia huyo mkuu wa upelelezi

‘Baba tafadhali utaharibu kila kitu, nilishakuomba kuwa unipe nafasi nifanye nionavyo mimi , kama utamuita huyo mkuu wa polisi utaharibu kila kitu, naomba tafadhali endelea na kikao chako, muda utafika , utaona ni kwanini nimeamua awepo hapa kwenye kikao hiki...’nikasema,
Shemeji yangu alipoona malumbano dhidi yake yanapamba moto, akaona aingilie mwenyewe, akasema;

 ‘Tafadhali mzee na wajumbe wote wa kikao hiki,mimi naomba mnipe muda, niongee kilichonileta hapa, na baadaye kama unaona nimevunja sheria, basi utampigia huyo mkuu wenu, ...huyo mpelelezi, simu aje kunichukua, mimi siogopi kukamatwa kwa hivi sasa, ..kwa vile nimeshathibitisha kile nilichokuwa nikikichunguza, kumgundua muuaji wa Makabrasha,...

Mimi kuja kwangu hapa,ni kusema ukweli, na hasa ni kumtetea kaka yangu, kwani kuna mipango ilipangwa dhidi yake, yeye hafahamu, kuwa kuna watu walioshirikiana kumuua Makabrasha, na kwa vile wanataka wasikamatwe, wameona kosa hilo wambambikie kaka, bila ya yeye kufahamu, ...’akasema na kaka yake akabakia kuduwaa,

‘Mimi nina ushaidi kuwa kaka hajamuua Makabrasha, na wala hajui ni kitu gani kilitokea siku ile, yeye kwanza alikuwa mgonjwa, na pili, aliyemuua, alikuja bila ya yeye kufahamu akafanya hayo mauaji na kukimbia, kaka, hamjui na hajui kwanini ilitokea hivyo..’akasema na kaka mtu akataka kumzuia mdogo wake asiendelee kuongea.

‘Kaka nakuomba utulie , nataka kuongea haya kwa masilahi yako, na masilhi ya wote waliohusika, kwasababu nimeona huk o tunapokwenda ni kubaya, na hayo yaliyopangwa dhidi yako, yatakutia matatani, wewe hujui tu...’akasema na kaka yake akamsogelea na kumshika mkono na kusema;

‘Mdogo wangu hayo sio ya kuongea hapa, tutakuja kuyaongea tukiwa wawili, wewe toka nje ya kikao,...’akasema huku akimshika mdogo wake mkono, ili watoke naye nje...mwenyekiti alipooa hivyo akasema;

‘Naomba mtulie mimi ndiye mwenyekiti wa kikao, nimeshamfahamisha mkuu wa upelelezi, amesema tuendelee na kikao, lakini kikao kikisha, huyu mtu tunatakiwa tumkabidhi kwake, kwahiyo kuanzia sasa upo mikononi mwa polisi mimi siwezi kuvunja sheria kwa ajili ya kumfurahisha mtu yoyote, hata akiwa mwanangu, hili nitalifanya,mimi nafuata sheria na taratibu zilikubalika ....’akasema

‘Kwahiyo mimi sina haja ya kusema ukweli ambao nilitarajia kuusema?’ akauliza shemeji yangu.

‘Ukitaka kuusema sawa, sasa hivi upo huru kusema, maana wenyewe wameshatambua kuwa upo hapa, na ukweli gani ulio nao ambao ni tofauti na ukweli ninaoufahamu mimi, hayo unayotaka kuyasema , na jinsi ulivyoelezea hapo, ni mbinu tu ya kuficha ukweli, ni kumtetea kaka yako kiujanja unjana, na mimi sikubaliani na hilo....maana ushahidi wote ninao hapa...’akasema baba.

 ‘Baba labda tufuate utaratibu wa kikao chetu, wewe endelea na kikao, ukifika muda wake wa kuongea ataongea, na ukweli utajionyesha, labda tuanze na ajenda zetu kama zilivyojiapanga, kama tulivyoanza awali, tulikuwa tukiongelea kuhusu katiba,,...’nikasema.

‘Utaratibu kama huu siutaki, ..lakini sawa tuanze kikao...’akasema mwenyekiti kwa hasira.

‘Ninataak niliweke hili wazi, siku nyingine mkiniita kwenye vikao vyenu, kwanza mumechelewa kufika, mimi kama mwenyekiti natoa onyo, sipendi tabia hiyo itokee tena, mkiniita kwenye kikao chenu mjipange vyema, pili sitaki mambo kama haya ya watu kujitokeza katikati ya kikao bila mipangilio, na tatu kikao kama hiki mkinichagua mimi kama mwenyekiti, sitaki mtu kujiona yeye yupo juu yangu, mimi ndiye mwenye mamlaka ya kikao hiki, mambo ya familia mnayaweka pembeni...’akasema.

Pili kuna mambo nataka kuyaweka wazi, ndio nimesikia kuwa mna katiba mna utaratibu wenu wa kimaisha, mimi sikatai, na nimefurahi kama mlifikia hatua hiyo,lakini ninataka niwarejeshe nyuma kidogo, niwakumbushe kwa muhutasari....

‘Kikao hiki kimeitishwa na binti yangu, na baadhi yetu tumealikwa kuna mambo anataka kutuambia ambayo sisi kama wanafamilia, tumekuwa tukiona kuwa yanakwenda kinyume cha maadili, ambayo sio tu yanaharibu sifa za kifamiia, lakini pia yanaharibu biashara na maendeleo yetu. ..’akasema.

‘Kwa kawaida mimi nimekuwa kiongozi wa familia kuu, ...ni kiongozi wetu hadi hapo nikapokufa, japokuwa nikiona sina muda, ninaliachia hilo jukumu kwenu, ...ndio ninakubali kuwa kuna familia ndogo ndogo, za watoto, maana kila mmoja ana familia yake, ya mke na mume, na watoto, wao, lakini kuna familia kuu, na tangu awali, kila aliyekuja kuoa kwangu, nimekuwa nikimwambia hilo, na akakubaliana nami..’akasema na kumwangalia mume wangu.

‘Nilishasema kwenye familia yetu hatutaki mambo ay kashifa, ikiwemo kuvunja sheria, na kuvunja sheria ni swala pana zaidi, ni pamoja na uwongo, kusalitiana, na kugushi, na mambo kama hayo, ..mambo ambayo yanatuharibia jina letu,achilia mbali kuua, ambalo ni kosa la jinai ....hilo niliwakanya tangu mapema, na nilisema hata kama ni mtoto wangu kafanya hayo, sitasita kumfikisha kunakostahili..

‘Mnafahamu madharaya yote hayo, binti yangu alifungwa, na nilipoona kafungwa, sikukimbilia kumtoa, nilifanya utafiti kwanza kuhakikisha kuwa kweli hana hatia, na kama ingeligundulikana kuwa ana kosa, ana hatia, kafanya makosa, mimi nisingelihangaika, ..lakini nilipofuatilia, niliona kuwa hana kosa,hana hatia, yote ni visingizio juu yake kwa masilahi ya watu wachache ...

'Hayo ni madhara ya kutukuaminiana, hakuna uaminifu kati yenu, kila mmoja ana lengo lake binafsi na kufikia hata  kuvunja sheria, hayo ni madhara, ya kutokuwa waadilifu, ...hilo nilishawakanya toka mwanzoni, silitaki katika familia yangu, iwe iwavyo, kama umeungana na mimi sitakubali, na kuungana na mimi ni kama umeoa kwangu, una hisa na kampuni zangu nk...’akasema baba.

‘Kwenye familia yetu maovu yamegawanywa kwenye vipengele, kuna maovu ya bahati mbaya, yanajulikana na unaweza kusema hilo ni kwa ajili ya kuhangaika, inatokea kama biandamu ukateleza, lakini kuna maovu ambayo kabisa unayaona kuwa huyu kakusudia, ...

‘Sasa basi sisi kama familia kuu, tumaliona hilo, kuwa kuna mambo yametendeka kinyume na sheria, na ni kwa makusudi kabisa, sio kwa bahati mbaya, sisi tulitaka tuchukua maamuzi yetu wenyewe, lakini tukaona ni vyema wahusika wenyewe waseme, waeleze ilivyokuwa, na nyie kama kikao mtaona je hiyo inastahili adhabu gani,..japokuwa adhabu sisi tunaifahamu, na adhabu ya familia yetu haina msamaha,..maana ukisamehe makosa kama hayo, ya makusidi, yenye nia mbaya ya kuliharibu jina la familia hii, wengine wataiga, wataona wakifanya hayo watasamehewa, hilo halipo, kwasababu sio bahati mbaya....’akatulia.

‘Sasa basi nakukaribishwa mwenyeji, au mtu ambaye umetuita kwenye hiki kikao uelezee, ni kwanini sisi kama wanafamilia kuu tusichukue maamuzi, tuliyoona ni sahihi, kwa masilahi ya familia na vizazi vijavyo, kwani  nyie wenyewe mumeshindwa kutimiza wajibu wenu ndani ya familia zenu, sitaki kusema yapi ni yapi mumeyakiuka, lakini kwa ujumla wake, mumetia doa familia yetu, haijawahi kutokea hivyo kabla, je ni kwanini, na kuna nini...’akasema na kuniangalia mimi, kabla sijasema kitu, mume wangu akasimama;

‘Mimi kama mume wa familia inayoshutumiwa kwa kukiuka hayo aliyosema baba, nataka kuelezea ni kwanini hayo yalitokea, naomba niongee mimi kwanza kabla hajaanza kuongea mke wangu japokuwa ni yeye aliyeitisha hiki kikao,....’akasema na baba, akataka kumkatiza lakini mimi nikasema;

‘Baba, muache aongee tu, akimaliza nitaongea...’nikasema

‘Kikao ni lazima kiwe na mpangilio, sio kwamba mimi sifahamu hilo, kuwa wewe ni mume wako familia, lakini kikao hiki sio wewe uliyekiitisha, tumeitwa na mke wako, ...na kama nilitaka wewe uongee, ningelikupa hiyo nafasi, sipendi kabisa huo utaratibu, heshima ni muhimu sana, lakini kwa vile mke wako kakuruhusu haya ongea kama ulivyotaka wewe, maana kila hatua mnazidi kunionyesha jinsi gani mlivyo....’akasema baba na mume wangu bila kujali akasema;

‘Nakubali kuwa kuna udhaifu ulitokea, na hilo linaweza kutokea kwa yoyote yule, hasa mnapokuwa katika harakati za kutafuta maisha, kuna changamoto za hapa na pale,..huenda katika kuyafanikisha hayo tulijaribu njia ambayo sio stahiki, ...ni katika kujaribu, ndio tukajikuta tumeteleza,..naomba tusamehewe kwa hilo...’akasema.

‘Lakini, pamoja na hayo, mimi nimeshaitoa katiba yetu, ambayo inalinda haki za familia yangu , na nimewekaw azi kuwa hiyo katiba inatambulika kisheria, sio katiba ya kutunga, na kuishia mitaani, mimi sijafanya kitu kinyume na katiba, na kama nilifanya, basi ujue nilifanya kwa nia njema, na kama nilitelekeza, kama mume, nina haki zangu, kisheria...na nilifanya mengine kwa minajili ya msilahi ya familia...’akatulia

‘Katiba niliyokupa ni halali, na nisingelipenda watu waingilie familia yangu, nina mamlaka yangu kama kiongozi wa familia. Ni sawa nilipoona kwako mzee, ulitoa masharti yako, ni sawa, kama mzazi nilitakiwa kufanya hivyo,lakini ukumbuke kuwa sisi sio watoto tena, sisi tuna mamlaka yetu, ..tuna utaratibu wetu, kama mtaona tumekwenda kombo, ni swala la kutushauri, na sio kutuingilia kiasi cha kutoa hata adhabu,...katiba yetu ipo wazi, inatulinda, inanilinda mimi kama mume wa familia, naomba hilo liwekwe bayana...’akasema.

‘Umemaliza...?’ akauliza mwenyekiti

‘Ndio mwenyekiti, nilitaka kuweka hilo wazi, maana nimeona ukitoa vitisho kwenye utangulizi wako..’akasema

‘Sio vitisho, hayo niliyoongea ni kweli na yatafanyika , kama ulikubali kuona kwangu, ujue una wajibu wa kuunza heshima yangu, sio kwamba nakuingilia, ...na sina haja ya kukuingilia, ila kama umevuka mpakana sitasita kukuwajibisha,...’akasema mwenyekiti.

‘Katiba ya familia yangu inanilinda...’akasema mume wangu, na mwenyekiti akaichukau ile katiba na kuinua juu na kuuliza

‘Hii ndio Katiba inayosema inakulinda?’ akauliza mwenyekiti

‘Ndio ...’akasema mume wangu.

‘Katika katiba yenu halali, mlikubaliana kuwa kila kilichonadikwa kitasimamiwa, kitatekelezwa, na sheria itafuata mkondo wake, kama mmoja akikosea, kutokana na mlivyokubalia atawajibishwa kisheria, hata kama ni kuvunjika kwa ndoa..., au sio?’ akauliza mwenyekiti

‘Ndio tumekuliana, na kila mmoja analifahamu hilo, ndio maana tukaisajili hiyo katiba, na mimi nipo tayari kuwajibka kwayo, hiyo hapo isome,utaona kila kitu kipo wazi, hakuna nilichokosea hapo, lakini unaposema kuvunjika kwa ndoa una maana gani maana ukisome vyema utaona kuwa mimi ndiye mwenye usemi wa mwisho kuhusu ndoa, siwezi kukubali ndoa yangu ivunjike...’akasema

‘Nauliza tena,  upo tayari kuwajibika kutokana na katiba yenu halali,ambayo inatambulikana na msajili wa katiba, ?’ akauliza mwenyekiti

‘Ndio nimeshakuambia hilo, yote yapo wazi kwenye hiyo katiba, sioni kwanini uniulize swali hilo, wakati katiba unayo hapo, na mimi nimekubali na sahihi yangu ipo na ya mke wangu ipo?’ akauliza mume wangu.

‘Una uhakika kuwa hii ndio katiba halali mliyokubaliana wewe na mke wako,...?’ akauliza mwenyekiti na nilimuona mdogo wake akiinamisha kichwa chini, na kujishika na mikono yake miwili, kuonyesha kukata tamaa....

NB: Mambo yamenza, ushaidi wa kwanza wa uaminifu kwenye ndoa, ....ni uaminifu...

WAZO LA LEO: Heshima ndiyo inayolinda utu wa mwanadamu, bila heshima, kutakuwa hakuna utaratibu wa kimaisha, heshima ni pamoja na kutii amri, taratibu na sheria,zilikubalika na jamii husika, zenye maadili mema,  na hili huanzia nyumbani, kwenye familia zetu, mkubwa kwa mdogo kila mmoja anatakiwa kutambua nafasi yake. Mke na mume , kila mmoja anatambua nafasi yake, kwe wema na hekima tukilifahamu hili, amani na upendo utakuwepo tu.


Ni mimi: emu-three

No comments :