Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, November 21, 2013

Mkuki ni kwa Nguruwe-33


‘Baada ya uchunguzi, ...kipindi kile tulipokuwa naye, alionyesha dalili, kuwa kapona, na mwenzangu akawa kaondoka, ..’Hii ilikuwa kauli wa dakitari aliyekuwa akimtibia mume wangu, na muda mwingi, wakati mume wangu alipokuwa kwenye matibabu ya mwisho nilikuwa jela...kumbe kuna mengi yalifanyika, na waliokuwepo hawakukumbuka kuniambia, mume wangu alionekana kuwa kapona..

Sasa haya yanayotokea sasa, yalinifanya niona kama mchezo wa kuigiza, ina maana kweli mume wangu kachanganyikiwa...

‘Docta mimi ninaweza kuwashitaki, ..hilo ni kosa kubwa sana, maana sasa hivi nimemuona mume wangu kama kachanganyikiwa, na mimi nilifikiria kuwa anajifanya..kwasababu nimekuwa nikimuuliza maswali., anajibu kama anaigiza, kuwa hajui, mara anasema kasahau, mara aliota,..katoka sasa hivi na gari, yupo kama ...’nikasema

‘Mfuatilieni haraka,...na mleteni hapa. ....’akasema docta, na mimi nikakata simu yake na kuingia kwenye gari langu, nikijaribu kumfuatilia, sikujua kabisa kaelekea wapi.....oh, ina maana mume wangu akchanganyikiwa kweli....

Endelea na kisa chetu....

***********

Ina maana mume wangu kachanganyikiwa, na kuchanganyikiwa huko ni kwa muda gani, je huko kuchanganyikiwa hakutakuwa na madhara yoyote kwake, na pengine kwangu, maana anaweza kufanya jambo la kuhatarisha maisha yake au yangu,au ya watoto....’nikawa nawaza huku nikiendesha gari  nikimfuatilia mume wangu,ambaye sijui atakuwa kaelekea wapi.

Nikiwa naendesha wazo likanijia kuwa nielekee njia ambayo mara nyingi hupita akielekea kazini kwake, sikuwa na uhakika, ila hisia zangu zilinituma hivyo, na nilipofika kwenye barabara inayoelekea maeneo anayoishi rafiki yangu, nikajikuta nikielekea huko, hisia zilinituma nifanye hivyo.

Nilipofika kwenye nyumba aliyokuwa akiishi rafiki yangu, niliona gari la mume wangu limesimama nje ya hiyo nyumba, haraka nikasimamisha gari langu na kutoka nje, nilisogea hadi kwenye lile gari lake, nikihisi bado yupo ndani ya hilo gari, lakini hakuwemo ndani ya hilo gari, nikageuka, kuangalia kwenye ile nyumba, nilimuona mume wangu akiwa kasimama pale mlangoni na mkono ukionekana kugonga ule mlango.

Kukaonekana mtu akifungua mlango, yule mtu alijitokeza sehemu ya juu, yaani kichwa na sehemu ya ndogo ya kiwiliwili, wakawa wanaongea na mume wangu, na yule mtu alionekana kama kushangaa, halafu akaongea jambo, kwa umbali ule sikuweza kufahamu wanaongea nini, lakini baadaye nilimuona mume wangu akigeuka, na kuanza kuja muelekeo wa gari lake.

Nilikuwa nimesimama pembeni ya gari lake, ina maana jinsi anavyokuja angeliniona lakini cha ajabu hakuniangalia wala hakuonyesha dalili ya kushituka, na inavyoonekana hakunitambua kabisa, akafika kwenye gari lake akaingia na kuliwasha, akasogeza nyumba kidogo, akageuza gari na kuelekea bara bara kuu.

Mimi kwa haraka nikakimbilia gari langu na kuliwasha, na hapo nikaanza kumfuatilia kwa nyuma, na wazo likanijia, kuwa nijaribu kumpigia rafiki yake niongee naye, huenda akanipa ushauri ;

‘Unasema mume wako anaonekana kuchanagnyikiwa kwa vipi?’ akaniuliza, nikamuelezea ilivyokuwa kwa kifupi , na yeye akasema;

‘Ndio madakitari wake, waliniambia niwe nikifuatilia nyendo na afya yake, kama kuna mabadiliko kama hayo, mwanzoni nilifatulia sana, na nikajaribu kuwa naye karibu, na sikuweza kuona dalili kama hizo, kwangu mimi nikaona huenda hali kama hiyo haitaweza kutokea, na ....sikuona hata umuhimu wa kukuambia hilo,...’akasema

‘Kwahiyo nifanyeje sasa?’ nikamuuliza, sikutaka kumlaumu

‘Cha muhimu ni kumfuatilia, kuna mambo kayapanga kichwani mwake, kuyafanya, akiyamaliza atarudi nyumbani, lakini asije akawa kapanga kufanya jambo baya....’akasema

‘Una maana gani kusema hivyo?’ nikamuuliza

‘Hapo alipo yupo kama vile mtu aliyelala, na anakuwa kama anaota, ...sasa anaweza akapanga kufanya jambo kutokana na fikira zake zilizopita,anaweza akawa kajenga kisasi moyoni, na akataka kufanya lolote kwa mtu anayemuhisi ni mbaya wake, hiyo inaweza ikatokea, sio lazima itokee hivyo,.....’akasema

‘Mbona unanitisha..’nikasema

‘Unatakiwa uwe muangalifu kwa sasa, maana anaweza akafanyamatendo hata akiwa usingizini..’akasema

‘Kwa vipi , mbona sikulewi’nikasema

‘Hujawahi kusikia watu wanafanya matendo wakiwa usingizini , inaitwa `disambiguation, or somnambulism' mtu mwenye matatizo kama hayo anaweza akaamuka kabisa kitandani, akatoka hata nje, akaenda kufanya kazi kama mtu anayeota,..lakini anafanya kiukweli, ..’akasema

‘Mungu wangu...!’ nikasema

‘Wasi wasi wangu kwa jini mnavyoishi kwasasa, mnaweza mkawa mumekwaruzana, na ikawa imemkwaza, na akili za kwenye ndoto zikamtuma kufanya jambo baya kwako, kwahiyo, hakikisha mkilala, vitu kama visu, mapanga,...na...oh, na  ile bastola yako umesharudishiwa?’ akauliza

‘Ndio ninayo...’nikasema

‘Oh, sasa inabidi uiondoe hapo unapoweka, uiweke sehemu ambayo hataweza kuiona, vinginevyo kwa hali kama hiyo anaweza kufanya lolote baya, sio kwako tu, hata kwa mtu mwingine kwa jinsi akili yake itakavyomtuma....’akasema

‘Kwa namna hiyo unaweza kusema mume wangu keshaharibikiwa akili?’ nikauliza

‘Hapana..sio kihivyo sana kuwa kapungukiwa..., hiyo itakuja kuisha, au kurejea kwa kipindi fulanifulani, na walichoshauri wataalamu ni kuwa kama hali kama hiyo itatokea, ni vyema, akarudishwa na kuwa kwenye mikono yao....wamachunguze tena...kwani kuna hali ya mkwaruzano ulitokea baina yenu?’akasema na kuuliza

‘Hatujakwaruzana, ilikuwa mazungumzo ya kawaida, ...na hata hivyo, ni lazima ifike mahali tuyamalize haya, na ndivyo nilivyotaka, iwe, sikujua kuwa kuna tatizo kama hilo...’nikasema.

‘Pole sana, ....’akasema na kutulia.

‘Kwahiyo sasa nifanye nini, nimwambieje kuwa anatakiwa hospitalini?’ nikauliza

‘Kwasasa mfuatilie kwanza , uone anataka kufanya nini, na huenda huko anapokwenda kukaweza kukupa majibu ya mambo mengine, japokuwa nakushauri usichukulie kuwa ndio ukweli wenyewe, maana hapo anavutika na hisia za akili yake tu, ....kuna mambo keshayapanga kichwani mwake anayafuatilia, hakikisha unakuwa naye karibu..’akasema

‘Kwanini nisiwaambie polisi, wakamkamata,...?’ nikasema

‘Hapana, usije ukawaambia polisi, hatujui mume wako alikumbwa na nini huko nyuma, ....inaweza kuja kumletea matatizo baadaye, huenda aliwahi kufanya jambo, ambalo polisi wanalifuatilia, na kama ujuanvyo wenzetu hao, wakimuona au kumuhisi, hawatajali kuwa huyo mtu ana matatizo, watakamkata na kumweka, ndani, na hapo tutakuwa tumemaliza...’akasema.

‘Ok, nimekuelewa, ....’nikasema na kabla sijakata simu, akasema

‘Je unaweza kuyafanya hayo peke yako, au nije kukusaidia?’ akauliza

‘Ninaweza, usijali....’nikasema  na wakati huo niliona mume wangu akielekea barabara ya kuelekea uwanja wa ndege, na akilini mwangu nikahisi atakuwa anaelekea kule kwa marehemu, maana hata alipotoka nyumbani alisema anakwenda kwenye mazishi, sasa sijui mazishi ya nani, kwani Makabrasha alishazikwa zamani..

Nilimfuatilia kwa karibu, nikiogopa asije akafanya jambo la hatari, alikuwa akiendesha kama kawaida, na hakukuonekana kukosea kama kuyumbayumba hivi , au kwenda kinyume na utaratibu wa bara bara, na hapo sikumuelewa alivyosema kuwa mume wangu anaweza kuwa kama yupo usingizini.

Tukafika maeneo karibu na uwanja wa ndege, na kama nilivyohisi, nilimuona akigeuza gari kulia kwake, na kuingia eneo lililopo lile jengo, alipokuwa akifanyia kazi Makabrasha, alifika kwenye eneo la kuegesha magari, akasimamisha,

Na mimi nikafika na kugesha gari langu pembeni yake, nikatoka, na kumfuatilia, nilimuona akiongea na muhudumu mmoja, na baadaye akasogea pale alipokaa mlinzi wakawa wanaongea, ilionekana kama hawaelewani, na yule mlinzi akawa kama anafoka, na kumzuia mume wangu, kuna kitu mume wangu alikuwa anataka kukifanya , lakini mlinzi akawa anamzuia, na baadaye wakaongezeka walinzi wengine, na mlinzi mmoja akamshika mkono mume wangu na kumvuta pembeni, wakawa wanaongea halafu mume wangu akaonekana kutikisa kichwa..

Ilionekana kama kuna kutokuelewana, lakini baadaye niliona mume wangu akasalimu amri, akageuka na akawa anarudi kwenye gari lake, alifika kwenye gari lake, akakaa kwenye kiambaza cha hilo jengo,huku kainamisha kichwa chini, alikaa vile kwa muda, na mimi kwa haraka nikaenda kuongea na wale walinzi.

‘Yule ni mume wangu kuna nini kinaendelea?’ nikawauliza

‘Yule jamaa sijui kachanagnyikiwa, anakuja anamuulizia Marehemu Makabrasha, sisi tumemwambia huyo mtu hayupo tena duniani, keshafariki, lakini hatuelewi, yeye anadai wameahidiana kukutana ofisini kwake....’akasema

‘Oh, ...’nikasema hivyo tu, na huyo jamaa akahisi sijaelewa, akesema;

‘Tukamwambia huyo mtu hayupo duniani tena, lakini cha ajabu, huyo jamaa unayesema ni mume wako, yeye kakataa kata kata, akasema yeye ana uhakika Makabrasha yupo ofisini kwake, waliongea naye kwenye simu....’akasema

‘Hamna shida, ....muachenia atulie, nahisi bado hajaamini kuwa rafiki yake hayupo duniani.., alikuwa rafiki yake mkubwa...’nikasema

‘Unasema huyo jamaa ni mume wako,...mmh, huwezi amini alivyovalia kama bosi fulani, lakini mbona anaonekana  kama hazipo sawa, na anaendesha gari mwenyewe, ni hatari, uwe makini naye....’akasema huyo mlinzi na mimi nikageuka kumwangalia mume wangu, ambaye kwa muda huo alikuwa kasimama, na mara akaingia kwenye gari lake na kuanza kuondoka, na mimi kwa haraka nikachukua gari langu na kuanza kumfuatilia nyuma....

**********

Kutokana na hali hii, nikaona mtu anayeweza kunisaidia hili ni mdogo wake, ...hasa kipindi cha usiku, kama alivyoeleza rafiki yake kuwa anaweza kufanay lolote baya, basi usiku nitakuwa na wakati mgumu sana, kwahiyo nikampigia simu mdogo wake.

‘Shemeji kuna tatizo?’ akaniuliza

‘Nakuomba uje nyumbani, ...’nikasema

‘Kuna nini shemeji?’ akauliza kwa mashaka

‘Kuna kitu nataka unisaidie kuhusu kaka yako,....’nikasema, sikutaka kumwambia ni nini kinaendelea kwa wakati ule, lakini nilifahamu nikimwambia kuwa ni mambo ya kaka yake, atakuja haraka.

‘Sawa nakuja shemji, lakini haumwi sana?’ akauliza

‘Haumwi, ni jambo dogo tu nitakuambia ukifika’nikasema

Niliona mume wangu anaelekea ofisini kwangu, alifika eneo la ofisini kwangu akasimamisha gari, akapiga honi, na mlinzi akatoka, na nikasikia akimuuliza;

‘Mke wangu yupo ofisini kwake?’ akauliza

Mlinzi alimwambia hapana, na wakati huo nilikuwa nimeshasimamisha gari langu, mbali kidogo, na pale aliposimamisha gari lake, yule mlinzi hakuliona gari langu, nikatoka kwa haraka na kusogea, nikasimama seehmu ambayo hawo wawili walikuwa hawawezi kuniona, nikawasikia  wanachoongea, haraka nikachukua simu yangu na kutuma ujumbe kwa yule mlinzi.

‘Mwambia mimi nipo nyumbani namsubiri...’nikatuma kwa yule mlinzi, ambaye kwa vile gari la mume wangu limemzuia, hakuweza kuliona gari langu, akasikia sauti ya ujumbe kwenye simu yake, akawa anausoma, halafu akamwambia mume wangu.

‘Mke wako yupo nyumbani anasema anakusubiri...’akamwambia

‘Hapana mimi nina uhakika yupo ofisini kwake, nina uhakika huo, ..nataka kwenda kuonana naye...’akasema

‘Ofisi kwasasa imefungwa, huoni kabisa kuwa huu sio muda wa kazi, hakuna mtu ndani...’yule mlinzi akasema

‘Mh, oh, ina maana muda wa kazi umekwisha,..oh, samahani, ....’akasema na kulirudisha  gari lake nyuma na kuligeuza, nikajua kwasasa atakuwa akielekea nyumbani.

Nilimfuatilia hadi tukafika nyumbani , na niliona gari la mdogo wake limeshafika, na yeye wala hakuangalia pembeni, akatoka kwenye gari lake na kwa haraka akakimbilia ndani, na mimi nikatoka kwenye gari langu na kuingia ndani.

Nilipofika ndani nilimuona mdogo wake, akiwa kakaa kwenye sofa, lakini mume wangu hakuwepo, nikamuuliza

‘Umemuona kaka yako akiingia?’ nikamuuliza

‘Ndio kaingia, lakini hakunisemesha, alionekana kama hanioni, kanipita kwa haraka akakimbilia chumbani kwenu kwani kuna nini?’ akaniuliza

‘Nitakuambia, ila nataka ulale hapa leo, kesho inabidi tumpeleke kaka yako hospitalini,  kaka yako anaonekana kuchanganyikiwa kidogo....’nikasema.

‘Ina maana hiyo hali imejitokeza?’ akauliza

‘Ina maana ulikuwa unafahamu kuwa hali kama hiyo itajitokeza?’ nikamuuliza

‘Ndio kipindi akiwa kule hospitali kwenye uchunguzi walisema hivyo, lakini jinsi alivyokuwa alipotoka huko, tuliona kuwa haitaweza kutokea tatizo kama hilo, hata docta, rafiki yake, alisema huenda hiyo hali haitajitokeza tena, baada ya yeye kumfuatilia kwa muda.....’akasema

‘Sasa ndio hivyo imejitokeza, na kwa hali kama hiyo, kunahitajika mtu wa kuwa naye karibu wakati wote, naogopa usiku nisije nikashindwa, nikapitiwa na usingizi, ....kama kuna lolote la kufuatilia huko kazini kwako nenda , au wapigie simu, ...kuwa kuna dharura, hutarudi huko...’nikasema

‘Hakuna shinda nimeshaaga tayari,...’akasema na mara mume wangu akatoka  na kuniangalia alionekana kama kunishangaa, halafu akasema;

‘Mke wangu, sijui kuna nini kinaendelea kwenye kichwa changu...’akasema

‘Kwani unajisikiaje?’ nikamuuliza

‘Hivi lini tulikuwa tunaongea kuhusu mtoto, ukaniuliza kuwa nina mtoto nje, mtoto wa kiume?’ akaniuliza

‘Mchana, tuliongea mchana, kwani vipi?’ nikamuuliza

‘Nimekwenda kumfuatilia huyo mtoto, hayupo,... hayupo , hata mama yake hayupo.....nahisi watakuwa wameamua kutukimbia na mtoto, huenda wameamua kunisaliti, una uhakika, kuwa nina mtoto ....tuna mtoto wa kiume, una uhakika?’ akawa ananiuliza

‘Hamna kitu kama hicho mume wangu, nilikuwa nakutania tu ...’nikasema

‘Sio utani huo, nikweli nina mtoto...ni lazima tumchukue mtoto wetu, mama yake hawezi kunikatalia, anasema mtoto ni wa kwake, sio wa kwangu na sina haki naye,...sikubali, nilimwambia Makabrasha alifuatilie hilo , na alisema kila kitu kipo sawa sawa.....kwahiyo usijali mke wangu, mtoto yule ni wa kwetu, kwahiyo tuna watoto hawa....’akasema akionyesha vidole vitatu.

‘Hapana mume wangu sisi tuna watoto wawili,....’nikasema

‘Usinibishie mimi, ...., mimi ndio najua, mimi ndio mume wako,...tuna watoto wanne, ...na ...’mara akamuona mdogo wake, akatabasamu na kumsogelea, kama vile anataka kumkumbatia, lakini mdogo wake akanyosha mkono wakashikana kusalimiana.

‘Jembe, umekuja, sasa mambo safi, utanisaidia kazi moja..kuna kazi moja usiku, sio sasa, hiyo ni siri yetu,..unasikia, sitaki mke wangu afahamu,...unasikia jembe....’akasema na hayo maneno kuwa hataki mimi nifahamu akawa kama anamnong’oneza, .

Mdogo wake akawa anamwangalia kaka yake kwa mashaka.Nilimuonyeshea ishara akubali tu, na mdogo wake, akamsogelea kaka yake na wakawa kama wanakumbatiana, nilimuona mdogo wake akijizuia kutoa machozi.

Niligeuka na kuangalia pembeni, maana kwa hali kama ile hata mimi hali ilinishinda, karibu nitoe machozi, sikuamini, mimi nilishafahamu kuwa mume wangu keshapona, na tunatakiwa kuganag mengine, sasa ahli hiyo imerudi,..na haijulikani kuwa ni ya muda tu au ndio keshaanza kuchanganyikiwa kabisa...lakini anavyoongea inaonyesha kuna mengi kayatenda, ina maana kuna mengi kayaafanya, ina maana kweli ana mtoto nje...ina maana...haiwezekani

‘Sasa mke wangu nataka kutoka na mdogo wangu, tutaonana baadaye...’akasema na kunishitua kwenye lindi la mawazo, nikamwangalia, yeye akamshiak mdogo wake mkono

‘Lakini mume wangu unatakiwa kupumzika...’nikasema

‘Hatutakawia, nipo na jembe, huyu ndiye mimi, ukimuona huyu umeniona mimi, hata nikifa leo, usije ukamtupa mdogo wangu,....usije ukamnyanyasa mdogo wangu, nitafufuka na kuja kumtetea, nampenda sana mdogo wangu.....hili ndilo jembe langu...’akasema na kumshika mdogo wake mkono, wakatoka naye.

Nilibakia mle ndani nikiwa sijui nifanye nini, na mara simu ikaita, ilikuwa ni namba ya nje, na nilifahamu atakuwa ni rafiki yangu.

‘Habari za huko?’ nikauliza

‘Nzuri tu, bosi, tumemaliza mitihani mmoja kesho tunafanya mwingine, na huenda nikaja huko siku za karibuni...’akasema

‘Itakuwa vizuri sana, maana kuna mambo nataka tuyamalize...’nikasema

‘Yale yale..au?’ akauliza

‘Ndio,..yale yale, na hapa tunapozungumza mume wangu anaonekana hayupo sawa’nikasema

‘Mhh, hiyo hali imeshajitokeza ehe..?’ akawa kama anauliza

‘Ina maana unafahamu?’ nikamuuliza

‘Wewe hukuwa makini na mume wako, ooh, kumbe kipindi hicho ulikuwa jela, ..ok, samaahni nimesahau, nimekumbuka, nilipofika hapo , kwa dharura, nilimtembelea mume wako hospitalini, na docta alisema mume wako kapona, lakini kuna mambo yanaweza kujitokeza, kama vile kupoteza kumbukumbu, na kitabia anaweza akabadilika badilika, asiwe kama alivyokuwa mwanzoni, na pia anaweza kufanya mambo kama yupo kwenye ndoto...’akasema

‘Kwanini docta alikuambia hivyo, wakati hayo nilitakiwa kuambiwa mimi ?’ nikauliza

‘Wewe siulikuwa  haupo, ..ulikuwa Segerea, na mimi yule docta ananitambua sana kuwa ni ndugu yako wa karibu, ...’akasema

‘Ni ndugu yangu wa karibu,ehe, ...kweli wewe ni ndugu yangu wa karibu, kama ungelikuwa ni ndugu yangu wa karibu ungelinifanyia hayo uliyonifanyia’nikasema

‘Yapi tena bosi, mbona kila siku unakuja na hoja mpya, ...?’ akauliza.

‘Unayafahamu sana.....’nikasema.

‘Bosi nakuomba bosi, usichukulie hayo mambo kwa hasira, nikirudi tutaongea, nina imani hakitaharibika kitu..’akasema

‘Kama ni kweli, ninavosikia, kama ni kweli, wewe umezaa na mume wangu...sizani kama tutakaa kwenye meza moja tuongee, hilo sahau, na nilishakuambia, kama kuna mtu anataka ubaya na mimi ...basi atembee na mume wangu, sitajali kama ni nani, hata kama ni ndugu yangu wa tumbo moja, nitafanya yale yale niliyowahi kukuambia...’nikasema.

‘Lakini...’akaanza kujitetea.

‘Sasa hivi mume wangu anaumwa, na hali aliyo nayo siwezi kufanya lolote, lakini akipona tu,...kama ni kweli, basi, ...mkataba utafanya kazi yake, na mengine yatafuta baadaye....’nikasema.

‘Mkataba upi bosi ...maana kama nilivyoona, kwenye mkataba hakuna tatizo, ...mume wako ana uhuru wa kufanya lolote, huoni kwamba ukitumia huo mkataba utakuwa umejimaliza mwenyewe..’akasema

‘Ndivyo unavyojidanganya ehe, ndivyo mlivyopanga, au sio?’ nikauliza

‘Mimi sijapanga lolote, mimi niliitwa kuja huko kwa dharura, na nilipofika hapo, nikajikuta naingizwa kwenye mambo ambayo hata siyajui,....walipanga wao wenyewe, ..kama ningelifahamu hivyo nisingelikuja huko, hadi nimalize mitihani,...unaona ilivyotokea,nimefika tu wakamshikilia mtoto wangu , nikalazimishwa kufanya mambo ambayo sikuwa na hiari nayo, na ndio nikauona huo mkataba, sijui lolote jingine, ....’akasema

‘Msijidanganye kwa hilo,yaani yote niliyowatendea fadhila zangu zote ndio malipo yake ni hayo...msijiona nyie ni wajanja sana, ....’nikasema

‘Jamani dada, ...bosi, usinifikirie hivyo kabisa, sipo kabisa kwenye hayo mambo yao, ndio maana wakatumia mbinu hizo walizotumia, ...hebu niambia mimi ningelifanya nini kwa hali kama hiyo,...Bosi, nakuhakikishia nikirudi tutayamaliza...’akasema

‘Ndivyo unavyofikiria kwa vile utakuwa  mke mwenza, au mshirika, au nani ?’ nikamuuliza

‘Mimi sielewi una maana gani kusema hivyo’akasema

‘Unaelewa sana....’nikasema.

‘Basi subiri nirudi, naona hapa kwenye simu  hatutaelewana, ila nakuhakikishia kuwa sijui lolote kwenye mambo yao, na mimi siwezi kufanya jambo baya dhidi yako, na ukiona nimefanya jambo, ujue ni kutokana na ushauri wako,....’akasema

‘Niliwahi kukushauri uje ufanya ufusuka na mume wangu?’ nikamuuliza

‘Bosi,...naona hatutalewana,...kwasasa, naomba uniache ili nimalize masomo kwanza, hayo na mengine mengi tutayamaliza, hakuna tatizo kabisa....mimi sijawahi kufanya jambo kinyume na matakwa yako, hilo nakuthibitishia, ...mengi nimeyafanya kutokana na kinywa chako mwenyewe.....nitakuja kukuthibitishia hilo..’akasema na kukata simu.

NB: Kisa kinarudi kuleee...na kuashiria kuwa mambo yanawekwa hadharani


WAZO LA LEO: Tuwe makini na kauli zetu , ulimi unaweza ukasababisha mema na mabaya,ukiutumie vyema ulimi wako unaweza ukapata faida kubwa, lakini ulimi huo huo, unaweza ukawa ni silaha yenye sumu,ukapandikiza chuki nafitina,  urafki ukageuka kuwa uadui, Tuweni makini sana, na ulimi.
Ni mimi: emu-three

No comments :