Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, November 14, 2013

Mkuki ni kwa Nguruwe-28


Wakati nipo nje kwa dhamana, baada ya kushukiwa kuwa eti mimi ndiye niliyemuua Makabrasha kwa kutumia watu, kwa vile nilionekana kwenye ofisi ya marehemu huyo. Ili kuondoakana na kashifa hiyo, nikaona ni bora na mimi nifanye uchunguzi wangu wa kina, kubaini ni nini kinachoendelea ndani ya familia yangu, hadi kufikia hatua hiyo.

Niliona nianze na ndoa yangu mwenyewe, kwa kumchunguza mume wangu, kutokana na mabadiliko yake, ambayo mimi nahisi kuna kitu kimetokea na kumbadili mume wangu, kwani hakuwa hivyo kabla, japokuwa wazazi wangu waliniasa kuwa huyo ni kunguru hafugiki, ....sikukubaliana na hilo, eti kutokana na historia ya familia yake, ndio maana mambo yote hayo yanatokea.

Sikukata tamaa, mimi niliona nijaribu kila iwezekanavyo ili mume wangu arudi kwenye mstari, na ili nifanikiwe hilo, kwanza nilianza kwa kunyenyekea, kumuomba na kumsihi, lakini nilipoona hilo halifanikiwi, basi nikaona nitumie  ule uwezo wangu mungu alinionijalia nao, japokuwa sikupenda kufikia huko. Nilijaribu kuongea naye mara kwa mara, ili aniambie ukweli, lakini mazungumzo yetu hayakufika kokote, yeye aling’ang’ania kuwa anachofuata ni taratibu tulizokubaliana ambazo zipo kwenye mkataba , kila kitu anafuata mkataba, kila kitu anafuata mkataba...

‘Mume wangu nimeshakuambia mkataba huo unaoufuata wewe haukubaliki, ...na ukiendelea na tabia hiyo, mimi nitachukua hatua nyingine, ...’nikasema.

‘Hatua gani tena mke wangu,...mimi ni mume wako, na ninalofanya jesha ni kwa masilahi yetu sote, mimi na wewe na familia yetu, na watoto wetu,...sifanyi kwa kujinufaisha sisi, huoni siku hizi nimeacha kunywa kabisa....’akasema.

‘Umeacha kwasababu ya mipango yako ambayo unahisi imekamilika, ...’nikasema.

‘Mipango gani mke wangu...kwani mkataba wetu unasemaje, ..mbona hutaki kuukubali, kuna tatizo gani pale...’akarudio huko huko kwenye mkataba.

‘Kama unataka tuelewane, rejesha ule mkataba wa awali, hapo tutakaa meza moja kama mke na mume, lakini kama utaendelea na mkataba wenu huo wa kugushi, basi, nitakuacha uendelee na maisha yako na mimi nitaendelea na maisha yangu...’nikasema.

‘Hapana, siwezi kukubali hilo, mimi ni mume wako na mimi ndiye kiongozi wa familia, na natakiwa kuhakikisha familia yangu ipo pamoja, ...nataka watoto wetu watuone tuna upendo na mshikamano,..’akasema.

‘Wewe ndiye uliyesababisha haya yote, kashifa imeingia kwenye familia  , tumeanza kwenye ulevi, ndoa isiyo na masikilizano, ..kuzaa nje, imekwenda hasi kushutumiwa kuua, kugushi, ulaghai, hivi hayo ni maisha geni unayoyataka wewe, mimi sijakulia kwenye maisha ya namna hiyo, familia yangu ni safi....’nikasema

‘Ina maana unaninyanyapaa kuwa familia yangu ni chafu, ndio maana haya yote yanatokea?’ akauliza

‘Usiongelee kuhusu familia yako ongea kuhusu wewe mwenyewe,...kwasababu wewe una uwezo wa kujibadili na kuwa mtu mwema, mwaminifu, mkweli ....unaweza kabisa, lakini kama unataka kuishi kwa ujanja ujanja...hutafika mbali...’nikasema.

‘Mke wangu mimi kama mume wako, naomba kauli hiyo, ya kuiniona mimi mchafu, tapeli mlaghai,..iishie, ..’akasema huku akinitolea macho, na mimi nikatabasamu na kusema;

‘Itaisha pale utakapoleta mkataba wetu wa awali, tuliokubalina kwa rizaa moja,....’nikasema.

‘Mkataba ni mmoja tu, hakuna mkataba mwingine, mkataba ni ule ule,...ila wewe unataka kunipanda kichwani, ili nisiwe na sauti kama mume..hili mimi siliafiki,...na nakuomba mke wangu, jaribu kuniangalia na mimi, unielewe na mimi...kwani nimefanya nini kibaya’akasema kwa sauti ya upole.

‘Wewe sio mkweli, ...’nikasema

‘Kwa vipi, mbona nimekuambia ukweli, kuhusu mkataba wetu, ...sijaukiuka, ..kuna jingine  mke wangu, hakuna, nimejaribu kuwa mume mwema, silewi tena, hilo huliungi mkono, unataka nianze kuelewa tena...’akasema.

‘Usibadili mada, mkataba wetu wa zamani upo wapi,..pili huyo mtoto uliyezaa nje ni nani, na umezaa nani, nijibu hayo maswali, na hayo ukiyaweka wazi, tutakubaliana, ...’nikasema.

‘Mkataba hauna shida, mkataba ndio huo, mimi sijui mkataba mwingine, mtoto niliyezaa nje, ilikuwa ni bahati mbaya, na ilitokea kutokana na wewe..’akasema

‘Kutokana na mimi, mimi ndiye niliyekutuma ukazini nje...’nikasema.

‘Matendo yako ndiyo yaliyonisukuma hadi nikafika huko, sikuwa na raha kama mume, wewe muda wote upo na kazi zako, sikuwa na raha kama mume, sikuwa na sauti kama mume, nilikuwa nipo nipo tu,....nikawa natafuta njia ya kijiliwaza,...nikaona pombe atakuwa mpenzi wangu, kumbe pombe ina mitihani yake...’akasema huku natamani kumzaba kibao, nilimuona kama mtoto mdogo vile.

‘Hivi wewe hujitambui hayo unayoyaongea, unaongea kama mtoto mdogo, ..ulewe kwasababu ya kujiliwaza, ....sikuelewi, ulienda kulewa kwasababu ya starehe zako, mimi muda wote nilikuwa hapa ndani, kwanini hukuniambia unachokitaka wewe...?’ nikamuuliza.

‘Hivi kulikuwa na raha gani, ....wewe hukutaka hata nikuguse, ..unakumbuka, au umesahau, ..tuyaache hayo, kwangu yamekwisha, nakuomba mke wangu tuishi kama mke na mume, tupendane kama zamani, tugange yajayo....’akasema.

‘Hujanijibu huyo mtoto uliyezaa nje, ni nani na ulizaa na nani?’ nikamuliza.

‘Hilo nitakuambia pale utakapokubaliana na mkataba wetu, maana kila kitu kipo wazi, na huyo anatambulikana kama mtoto wetu,...ana haki zote ndani ya familia hii....’akasema.

‘Una kichaa kweli...uzae ovyo mitaani, uniletee watoto, eti wana haki, ina maana gani ya ndoa...je na mimi nikizaa nje, nikaleta mtoto hapa utamtambua?’ nikamuuliza.

‘Kama io kwenye mkataba nitamtambua....’akasema.

‘Unanichefua,...nashindwa hata kukuelewa, sikiliza, mimi ninakupa wiki moja, nataka mkataba wa zamani uje, kama hautapatikana basi, ...tutaita mawakili wetu, tutaangalia haki ilipo, na ikibidi tutafikishana mbali,...nisingelipenda kuwashirikisha wazazi wangu kwa sasa...ila baada ya wiki moja hiyo kwisha, kama utaendelea na ujinga wako huo....hutaamini kuwa ni mimi...’nikasema.

‘Mke wangu, kwanini unakasirika,...kwanini yote hayo, mbona mimi nakupenda, na nafanya haya yote kwa mapenzi ya dhati...jaribu kunielewa na mimi....mbona hutaki angalau kuusoma huo mkataba ukaoana mambo yake, hakuna ubaya kabisa, ....mimi sitakubali kamwe ndoa yetu ivunjike, ....nakuhakikishia hilo....’akasema
Mimi sikutaka kuongea naye siku hiyo, nikaondoka kuendelea na shughuli zangu nyingine

***********

Kwa hali kama hiyo niligundua kuwa mume wangu anahusika na hayo yaliyotokea, lakini sikuwa na uhakika wa moja kwa moja kuwa alifanya hayo kwa dhamira yake au kulikuwa na shinikizo kutoka kwa marehemu.Na je nay eye anahusika na kifo cha rafiki yake. Hilo la kifo cha rafiki yake hata polisi walifika sehemu wakashindwa kumbaini muuaji ni nani, na kusema kuwa jamaa huyo aliuliwa na mmoja wa maadui zake, ambao walikuwa na kisasi naye, na uchunguzi bado unaendelea.

Siku zikawa zinakwenda, na mimi nikaendelea na msimamo wangu wa kutokuutambua mkataba huo waliotayarisha wao, sikutaka kulifuatilia kisheria zaidi, hata wakili wangu aliyetaka kulifuatilia kisheria, nilimwambia anipe muda kwanza nijaribu kivyangu, ikishindikana, itabidi tuingie kisheria.

Ikafika mahali mimi na mume wangu hatuongeai, sikutaka hata kuonana naye, mimi niliweka agizo langu kuwa nitakaa meza moja na yeye pale tu huo mkataba wa zamani utakapopatikana. Nikaanza kumwekea shinikizo, kwanza nikakata mawasiliano ya kuongea naye, na kutokushirikiana naye kwenye shughuli zozote alizozifanya kimkataba. Hata hundi za benki ambazo nilihitajia mimi kupitsha nikazizua, kwahiyo akawa hana uwezo wa kipesa zaidi ya kiasi kile alichoruhusiwa kukutoa kwenye kampuni yake, kwani kiasi kikzidi sana ilitakiwa sahihi yangu na yake, kutokana na kumbukumbu za kibenki.

Hali ilivyozid kuwa mbaya, akaona amtumie rafiki yake, ili aonge na mimi na ikibidi tukae tuyaonee kama mke na mume, lakini sikutaka maongezi yoyote na huyo rafiki yake, nikishinikiza kuwa mkataba wa awali uwepo kwanza.....halafu tutakaa na kuyamaliza.

‘Sasa kazi zitasimama, na kampuni zinaweza kuyumba...’akasema huyo rafiki wa mume wangu.

‘Kama analiona hilo ni wajibu wake, kuleta huo mkataba wa awali, na kama anajiona kuwa anauwezo wa kufanya anavyotaka basi aendelee, na siku nitakapo kamilisha uchunguzi wangu na kuwa na ushahidi kuwa yeye alishirikiana na marehemu kufanya hayo yaliyotokea, nitampeleka mahakamani....’nikasema.

‘Lakini mambo ya kampuni msiyaingize kwenye mambo yenu ya kifamilia’akashauri.

‘Sisi tulikuwa na utaratibu wetu zuri tu, yote hayo ya kikampuni , ya kifamilia, tulikuwa tumekubaliana, ili kulinda mali za familia, ...kama tusingelifanya hivyo, kampuni hizo zisinelikuwepo, angalia sasa anavyofanya yeye, ana mtoto nje, na kama ana mtoto nje, ina maana ana kimada nje, ni nini kitaendelea hapo, kama sio kuanza kugawa mali halali, zilizotokana na jasho letu kwa watu wasio jua kabisa zimetoka vipi...’nikasema.

‘Sitaki nikukumbushe ..lakini inabidi nikuambie, hayo umeyataka wewe mwenyewe...nilikuambia mwanzoni jaribu kuwa akribu na mume wako, jaribu kuangalia ana shida gani anataka nini, ujue kuwa binadamu wote sio sawa, kuna utofauti wa kuwaza, unavyowaza wewe, na kutathimini mambo sio sawa na ataakvyowaza mwingine...’akasema.

‘Nakufahamu sana, huenda hayo mliyapanga pamoja, ili kujionyesha kuwa nyie ni wanaume, mnaweza kufanya mpendavyo, au sio...mlewe , mtembee ovyo na wanawake , mzao ovyo, si ndio,...?’ nikamuuliza.

‘Sina maana hiyo..ila maisha ya ndoa,msipovumiliana, mkaweza kukaa pamoja, mkajaribu kuziangalia zile tofauti zenu za kifikira, mkazitafutia suluhu, siku mambo yakiharibika inaweza ikaleta shida sana kujirudi, kwasababu muda huo kila mmoja atakiona yupo sahihi...kama mngelikaa na kujuana, na kuangalia mwenzangu anataka nini, mgeliweza kulizuia hilo....’akasema.

‘Mwambie rafiki yako, kama anataka tukae tukubaliane, aulete mkataba wetu wa awali, kwasababu siwezi kukubali huo mkataba wa kugushi, wamekaa na mwenzake, marehemu, wakatunga mambo yao, mimi sikuwepo, na humo wameweka ammbo ambayo mume wangu atajifanyia apendavyo, bila hata kibali changu....huoni kuwa ni hatari, kutokana na hilo, nasikia kuna mkataba mwingine, ambao, yeye kama mume, kutokana na mkataba huu, ana hiari ya kuuza hisa kwa mtu mwingine...’nikasema.

‘Mhh, una uhakika na hilo?’ akaniuliza.

‘Ndio maana sitakubali huu mkataba wao, ..kamwe, kwani nikikubali tu, kampuni yake, hatakuwa na hiari nayo, kwani marehemu alishachukua zaidi ya nusu ya hisa, na kampunu yangu hii, marehemu ana hisa, ...ni nani alipitisha hilo, ....hebu niambie, mimi nikubali tu, ...ina maana gani kuhangaika, kutokulala, usiku na mchana tulihangaika, leo matunda yamepatikana, yachukuliwe na watu wengine kirahis rahisi tu....na kakubali mwenyewe ana mtoto nje, na huyo mtoto, mzazi wake, wana haki, na watachukua sehemu ya mali,...hivi nyie watu mnaniona mimi ni mjinga kiasi hicho...’nikasema.

‘mimi hayo siyajui, maana ulishanipiga marufuku kufuatilia mambo ya ndoa yako, nilishakuambia kama unanihitajia ni kusaidie,nipo tayari,...sasa nawashangaa, kesi yenu haijaisha, bado mpo kwenye migogoro ya kifamilia hamuoni kuwa mnaweza kukosa yote?’ akaniuliza.

‘Kama nilivyokuambia toka awali, wewe endelea na familia yako,mimi hili nitalimazia mwenyewe, yupo wakili wangu, nikishindwa nitamkabidhi, na hapo itakuwa ndio mwisho...’nikasema

‘Upo tayari kuvunja ndoa yako kwasababu ya hilo?’ akaniuliza

‘Wewe unaliona ni dogo eeh, ikifikia hapo, hutaamini, kwanza huo mkataba wa zamani ukipatikana tu,...kama tulivyoahidiana, hatua kwa hatua, tutatekeleza, na huyo mwanamke wake waliyezaa naye, mimi nitamuonyesha kuwa ni nani...huwa nikiahidi kitu sirudi nyuma,....’nikasema.

‘Ndio maana mume wako anaogopa kuulea mkataba wenu wa zamani...’akasema.

‘Huo ni uwoga,...yeye kama ni mwanaume, anatakiwa aingie uwanjani, apambane kiume, na asipofanya hivyo, akaegemea  mawazo ya wenzake, atakosa yote....hajui mimi ninawaza nini, hajui nina mipango gani kichwani, ..hajui...kwani nimetoka naye wapi,...hakumbuki hilo,...’nikasema.

‘Haya mimi sitaki tena kuingilia mambo yenu, nitakuja tu pale mtakaponihitajia, kama ulivyowaambia wazazi wako, wasiingilie, mambo yenu, sisi tunawaangalia lakini kama mkikwama, sisi tupo tayari kuwasaidia..’akasema na kuondoka.

************

Siku moja wakati nipo nyumbani nimepumzika, nikaambiwa kuna mgeni anataka kuongea na mimi, nilikuwa sitaki kuongea na mtu, lakini nikaona ni vyema kumsikiliza huyo mgeni, kibusara, nikauliza;

‘Ni mgeni gani huyo?’ nikauliza.

‘Ni mtoto wa marehemu Makabrasha..’akasema msaidizi wanguu wa ndani.

‘Huyu mtu, nilishampiga marufu....’nikaanza kufoka, lakini akili yangu ikanituma niongee naye tu, nilikuwa nimekataa kata kata kuongea naye, nikiwa kwenye shinikizo lile lile la kupata mkataba wa zamani, lakini siku hiyo sijui kilinijia kitu gani, nikasema wamkaribishe bustanini, sikutaka kuongea naye ndani.

Walimkaribisha bustanini, nikaenda na nilipofika tu, nikamsalimia kama ada, sikutaak kumuonyesha jinsi gani nilivyochukia, maana moyoni niliona kuwa wao, kutokana na bba yao, watakuwa wamepanga jambo la kuifisidi familia yangu. Nilipokaa nikasema;

‘Haya niambie una shida gani na mimi?’ nikamuuliza huku nikimwangalia moja kwa moja usoni, maana tulikaa tukawa tunaangaliana na kati kati yetu kulikuwa na meza. Nilitaka nimuone usoni, kwani mtu unaweza kumpima ukweli wake, au ujasiri wake, kwa kumwangalia usoni.

‘Samahani sana kwa usumbufu wangu, wa kutaka kuongea na wewe...maana nimejaribu mara nyingi bila mafanikio, na leo nilipanga, kama ikishindikana basi nitaondoka,...siku zangu za likizo zimeisha, natakiwa kurudi kazini...Ulaya...’akasema.

‘Sawa pole sana, ehe, unasemaje..?’ nikauliza.

‘Mimi sina nia mbaya kama unavyofikiria wewe,..huenda ungelisikiliza toka awali tungelishamalizana, na kila mtu akashika hamsini zake. Hapa nilipo nakwama kuondoka maana mambo bado hayajakaa sawa, na mimi nimeachiwa majukumu mengi na marehemu baba....’akasema.

‘Hayo majukumu uliyoachiwa, yananihusu nini mimi?’ nikauliza na yeye bila kujali swali langu akaendelea kuongea.

‘Mimi nilipofika hapa Dar kutoka nje kutokana na kifo cha baba...nilitarajia mengi, maana mimi namfahamu 
sana baba. Kwani nilitaka kujua ukweli wa kifo cha baba, na nilipewa taarifa yote kutokana na uchunguzi wa polisi. Na nilihisi nyie mnaweza mkahusika, ...na kiukweli kama mngelikuwa mnahusika, ningesimama kidete kuhakikisha haki inapatikana,..lakini kutokana na taarifa ya uchunguzi wa polisi, ikaonekana hauhusiki, na kwa kujirizisha, nikafanya uchunguzi wangu binafsi, na kuhakiki taarifa niliyopewa, nikagundua kuwa mambo ni yale yale....’akasema.

‘Mimi ninamfahamu sana marehemu baba yangu, nafahamu sana mbinu zake za kupata mali, ..ndio yeye alikuwa ni wakili, lakini kazi hiyo, aliitumia kama kivuli, nilikuwa nafahamu kuwa kuna mambo alikuwa akiyafanya ambayo sio sahihi, na hilo nilikuwa napingana nalo sana.....’akasema.

‘Kifo chake hakikunishitua sana, maana ukiishi kwa kazi kama hiyo aliyokuwa akiifanya yeye, ujue kifo kipo pembeni yako, mimi naishi nje, na nimeona watu wa aina hiyo wanavyouwawa...blackmail,ni kazi ya hatari sana, sio mchezo, kumghilibu mtu, na kupata kile alichokihangaikia kwa jasho lake kwa shida, wewe uje ukichukue kilaini, ..na unapoanza kwa tabia hiyo, hukomi, utataka leo, kesho na kesho kutwa, inafikia huyo mtu anaona ni bora akuue tu,..nilimkanya sana baba yangu, lakini hakunielewa...’akaendelea kusema.

‘Mimi nilikuwa sielewani  na baba tangu niwe na fahamu naye, japokuwa sikuwa ninaishi naye, maisha yangu, nililelewa na babu na bibi, maana mama alikuwa akiishi huko ,....na hata nilipokuwa nasoma hapa mjini ambapo nilikuja kukaa naye, hatukuwa tunaelewana, damu zetu haikufanana,....mimi nia na lengo langu ni kusoma, na kutokumtegemea baba, na kweli juhudi zangu na dua zangu zikakubaliwa, nikafaulu mitihani, na nikapata nafasi ya kwenda kusoma nje ..kwenda kwangu nje, hakukuwa na mkono wake, nilihangaika kivyangu, nikafanikiwa, na huko nikasoma kwa shida sana, na aliposikia nasoma kwa shida, akanitumia pesa...nilizikataa kabisa...nikamrudishia, hutaamini.

Hapo nikamuuliza;

‘Kwanini ulifanya hivyo?’ nikamuuliza nikimwangalia machoni, huyu mtu huwezi kumhisia vyovyote, hajionyeshi tabia yake usoni,..ni watu wachache wenye tabia hii.

‘Kwasababu nilijua pesa zake ni chafu na mimi sitaki pesa chafu, ndio maisha yangu nilivyoamua yawe hivyo, wewe hujiulizi kwanini baba alikuwa hakai na mama, ..mama alifahamu tabia ya baba, akaona ajitenge naye, na mimi nimerithi tabia ya mama...nataka niishi kwa jasho langu, sio kama alivyokuwa akiishi baba...’akasema.

‘Kifo cha baba, kikatufanya tukutane kama familia, nashukuru sana kuwa wanafamilia wote walikuwa wakimfahamu baba, hakuna aliyetaka kuingilia mambo yake, kila mmoja aliona kuwa akigusa huko huenda damu za watu, walioumia zitamuandama. Mimi nikapewa jukumu la kusafisha jina la baba, maana keshakufa, na maisha yanahitajika kuendelea, ..je tutaendelea kukumbatia hiyo hali, hapana, ni lazina jambo lifanyika..’akatulia.

‘Kazi yangu kubwa, ilikuwa kufuatilia kwa kile aliyeumia kutokana na baba...wapo wanaojulikana, na tulitanagaza kama kuna mtu kwa namna moja au nyingine alipata athari, kutokana na utendaji wa baba akitokeze,..watu waliona kama ni utani,..mimi nikafanya kazi ya zaida kuwafuta, na kujaribu kutafuta suluhu...na ili hayo yafanikiwe, tulimtafuta mwanasheria ambaye alisaidia kisheria....’akasema.

‘Tatizo likaja, kuna huo mkataba ...ambao hatukuwa na uelewi sana nao, unaonyesha ni wa karibuni, ndio tukaanza kuufuatilia, na hapo nikakutana na mume wako....namfahamu sana mume wako , maana mimi namtambua kama baba mdogo, kwa jinsi familia yao na yetu zilivyokuwa karibu, na baba yangu na mume wako walikuwa marafiki sana japokuwa baba yangu alikuwa mkubwa  kwa mume wako.

‘Huu  mkataba kama tungelikuwa ni watu wa tamaa, basi tungeliutumia, kiukweli kama tungeliamua kuutumia, tungeliweza na kuhakikisha kuwa tunarithi hayo aliyoyaacha baba, ikiwemo kumiliki kampuni zako,....’akasema

‘Huo mkataba upo wapi?’ nikamuuliza

‘Huo mkataba ninao, ....’akasema

‘Nataka kuuona,...’nikamwambia.

‘Bado anao mwanasheria wetu, ....’akasema

‘Anao kwa ajili gani?’ nikamuuliza

‘Kuna mambo bado hayajakaa sawa, na hili linatokana na mume wako, kama mume wako angelikubaliana na sisi, basi tungelishamalizana,...’akasema

‘Mambo gani hayo mume wangu hajakubaliana na nyie?’ nikamuuliza

‘Kuna vipengele vingi vipo humo, vikionyesha kuwa mume wako ndiye anamiliki kampuni yake na yako kwa asilimia fulani za hisa, lakini katika mkatana aliouacha baba , kuna kipengele walishindwa kukubaliana, ...’akasema

‘Kipengele gani hicho?’ nikauliza

‘Baba alitaka kumiliki zaidi ya aslimia hamsini ya hiza za kampuni  ya jina la mume wako, na alitaka jina hilo libadilishwe....na hapo kukatokea sintofahamu, nahisi hata kifo cha baba kilitokea siku walipokuwa wakibishana kuhusu hilo...’akasema

‘Wewe umejuaje hayo, na wakati hukuwepo....?’ nikamuuliza

‘Baba alikuwa na kawaida ya kuhifadhi kumbukumbu za matukio yote, ..tulichokuja kuona ni ajabu ni kuwa mle ndani kwenye hicho chumba kulikuwa na kifaa cha kunasa matukio, lakini sehemu hiyo ya kifo cha baba haikuwepo, ina maana huyo muuaji, alirudi na kufuta sehemu hiyo.

Mimi ni mtaalamu sana wa komputa, nikafanya mambo yangu,  nikagundua sehemu ndogo inayoonyesha jinsi gani kifo cha baba kilivyokuwa, ndio nikagundua kuwa aliuwawa na watu wake waliokuwa hawaelewani naye...’akasema

‘Ni watu gani hao?’ nikauliza

‘Imeshindikana kuwagundua ni akina nani, huyo muuaji hakuonekana sura, ...na alitokeza kiogo tu, huku kiasi cha kuweza kulenga shabaha..na hakuweza kuonekana sura, alikuwa kaziba kabisa uso wake, na kuacha macho tu,hata polisi hawanafahamu sehemu hiyo, mimi nafahamu ilivyokuwa kutokana na kumbukumbu hizo,, na kwa vile niligundua kuwa huyo muuaji hataweza kugundulikana, nikaona haina haja ya kuwapa polisi hiyo taarifa...’akasema

‘Kwanini?’ nikauliza.

‘Kwasababu sehemu kubwa inamuonyesha mume wako, na polisi wangeliona sehemu hiyo mume wako angelikuwa kwenye hatia,...’akasema

‘Mimi sikuelewi hapo mume wangu alikuwa anaumwa, inaonyeshaje kuwa  alihusika?’ nikauliza

‘Siku huyo mume wako alikwenda kumuona baba, marehemu baba, ndivyo inavyoonyesha, na walikuwa akibishana kuhusu huo mkataba na kiasi cha hisa baba anachokihitajia....’akasema.

‘Hebu samahani kidogo, kwanini baba yako alihiaji kiasi kikubwa cha hisa?’ nikamuuliza.

‘Kutokana na hayo mazungumzo, wazo, na mambo mengi kuhusu kampuni ya mume wako yalitokana na marehemu baba, alivyokuwa akielezea ni kuwa kumbe japokuwa baba hakuwa moja kwa moja kwenye hiyo kampuni, lakini yeye alichangia mambo mengi,...kuna mambo yalikuwepo humo, yalifanywa ba marehemu baba....’akasema.

‘Hapo sizani kama ninaweza kuelewa, anyway, endelea....’nikasema.

‘Siku ile mume wako, alifika kwa baba, ...haya ninayokuambia hata mume wako hajui kuwa ninayafahamu,...sijamwambia, ila alifika wakaanza kuongea, na siku hiyo walipanga kuhitimisha makubaliano yao,...na ikafika sehemu mume wako akakubali na kuweka saini, walipomaliza,  na wakati wanapena mikono ya kuagana, mara mlango ulifunguliwa na mtu aliyekuwa kajifunika sehemu zote za  usoni, usingeliweza kuiona sura yake, akampiga baba risasi, kifuani kwenye moyo, na kufa hapo hapo..’akatulia kidogo.

‘Na wakati anataka kumpiga mume wako, ikasikika sauti ya mtu akiita kwa nje, kwahiyo huyo mtu akashindwa kumpiga risasi mume wako,, akageuka kukimbia, lakini akaiacha hiyo bastola pale ilipokuwa...kama inavyoonekana kwenye huo mkanda...’akasema

‘Ukiangalia hiyo sehemu utaona vyema jinsi gani mume wako alivyochanganyikiwa, kuonyesha kuwa hakuwa anafahamu ...maana ungelisema ni mtu wake, aliyempanga kuja kufanya hivyo, alishituka, na kuweka mikono usoni, kama vile mtu anavyoogopa kupigwa ...akainama na huyo muuaji alipoondoka, akikimbia , mume wako akafunua mikono, na alipoona baba keshafariki, akawa anahangaika, akishindwa afanye nini...baadaye, sijui alijiwa na wazo gani, akafungua mlango, na kutoka, ...huwezi kuona kitu nje ya chumba...na sehemu hiyo iliondolewa.

‘Kwahiyo sura ya huyo muuaji haikuonekana, na huyo mtu alitaka kumuua pia mume wangu?’ nikauliza

‘Ndivyo ilivyokuwa inaonyesha, kwani baadaye mume wako alionekana akiuliza;

‘Wewe nani....’akatoka na hakuonekana kurudi tena...

‘Sasa kwanini usiwaonyeshe polisi, maana ingewasaidia kujua zaidi?’ nikamuuliza.

‘Tunafuata maagizo ya baba, licha ya kuwa sikuwa na mahusiano mema na yeye, lakini nakumbuka jinsi alivyokuwa akiniambia kuwa mume wako nimuheshimu kama baba yangu mdogo, kwani amewahi kumsaidia sana..hata mimi alinisaidia sana nikiwa mdogo..na alimsaidia sana mama, kipindi mama alikuwa anaumwa sana, hana pesa, yeye alijitolea kuuza mbuzi wake, aliyekuwa naye, mmoja, kwa ajili ya kumtibia mama,...mimi nilimwahidi baba kuwa mume wako atakuwa baba yangu mdogo, na sitaweza kumvunjia heshima.

‘Sijakuelewa hapo, hata kama ni mhalfu, utamtetea tu, na huenda akahusika na kifo cha baba yako?’ nikamuuliza.

‘Mume wako hahusiki na kifo cha baba yangu, hilo nina uhakika nalo...usuhuba wao ni wahali ya juu, kifo cha baba kimemuumiza sana mume wako, ..wewe hujui tu, yeye ndiye aliyekuwa kichwa chake, kila uliloliona mume wako akilitenda, mara nyingi, alikuwa akifuata ushauri wa baba...’akasema.

‘Hata kuzaa nje ya ndoa?’ nikamuuliza

‘Hiyo ni sehemu ambayo nitakusimulia kama utakubaliana na maombi yangu...’akasema

‘Maombi gani?’ nikamuuliza

‘Umsikilize mume wako..mkubaliane naye..mkisha kubaliana naye , mkawa kitu kimoja,basi sisi tutajitoa kabisa kwenye huo mkataba ulioandaliwa kuwa baba alikuwa na hisa, ...maana nyie bila kukubaliana bado tutakuwa hatujafanya lolote, na sisi hatutaki kujihusisha na mambo yake, hatutaki kupata mali isiyo halali,...lakini tunahitajika kumsaidia mume wako, kwani ...wema wake kwetu ni mkubwa sana...’akasema.
Mimi nikatabasamu na kumwangalia huyo jamaa kabla sijamjibu, nikasema;

‘Naweza kuonana na mama yako.....?’

NB: Inatosha kwa leo


WAZO LA LEO: Urafiki ni mzuri, unajenga mahusiano mema, lakini tujaribu kuangalia aina ya marafiki wetu,kuna marafiki wengine wana tabia mbaya, kazi zao sio nzuri, ni za dhuluma, marafiki hao hawafai , na ikiwezekana tengana nao kabisa, kwani ukiungana nao, hata kama hutafanya wanachokifanya wao, lakini ubaya wao unaweza kukuleta matatizo kwani ukikaa na muuza uturi, utanukia uturi....

Ni mimi: emu-three

No comments :