Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, August 12, 2013

WEMA HAUOZI-47



‘Ndugu muheshimiwa hakimu,..nawaruhusu watetezi kumhoji shahidi wetu huyu(mtaalamu), na kama hawana maswali basi, tutamuita shahidi mwingine kuja kuthibitisha kifo cha jemedari, kabla ya kumleta shadidi ambaye wenzetu wana hamu sana ya kumuona na kumhoji, …’akasema na hakimu akawageukia watetezi, na wakili mtetezi akasimama, na kumkabili huyo shahidi,….

Tuendeleze sehemu iliyopita kidogo….kwani sehemu hii ina mambo muhimu ambayo utakuja kuyaona baadaye.

‘Wewe unajiita mtaalamu au unaitwa mtaalamu?’ Wakili mtetezi akauliza swali huku akimwangalia huyo shahidi, na huyo shahidi, akainua macho yake kumtizama, macho ambayo yalikuwa kama ya mtu aliyeosa usingizi, akamwangalia wakili huyo kwa huku akipepesa macho.

‘Wao ndio wananiita mimi mtalaamu, siwezi kujiita mwenyewe mtalaamu…wewe vipi bwana’akasema kwa sauti ya ukakamavu.

‘Wanakuiita hivyo kwasababu una-utalalmu wa zaida kama ulivyodai, au sio, ya kuwa unaweza kumtizamia mtu, kwa kupiga ramli au sio?’ akauliza

‘Kama ulivyosikia maelezo yangu ya awali, ndivyo hivyo hivyo…kwani wewe unasemaje?’akasema na akawa kama anauliza kuonyesha kuwa anajiamini

‘Unapopiga ramli, unamwambia mtu yale ambayo yatatokea, au yaliyotokea hadi kufikwa na tatizo lililomleta kwako, na kutoa tiba yake au ushauri, au jinsi gani ifanyike, au sio?’ akauliza

‘Ndio hivyo hivyo….kumbe unajua bwana, unapoteza muda kuniuliza, au sio au sio…haisaidii, ….’akasema huku akitikisa kichwa kama kukubali

‘Kwahiyo yote yanayokuja kutokea baadaye kwa mteja wako, ni kutokana na ramli yako?’ akauliza

‘Unajua bwana mdogo, nikuambie kitu, ongea unachotaka kuongea kwanini unazunguka kwa maswali yasiyo na tija, eti….kwanini hasemi anachokitaka..’akasema shahidi huyo kwa ukali huku akimwangalia wakili mwanadada, ambaye alikuwa akiwaangalia wanavyojibizana.

‘Mimi ndiye ninayekuuliza maswali na ukiulizwa maswali unahitajika kuyajibu, ndio taratibu za hapa, hapa sio kwenye ofisi yako ya kupiga ramli, unasikia…?’akasema huyu wakili mtetezi huku akitabasamu.

‘Nimekuelewa, ila nataka uulize swali kwa kujiamini, sio kwa kuzunguka zunguka, maana najua ni kitu gani unataka kuniuliza, na mimi siogopi, ….kwasababu sio mimi, , nayafanya haya kutokana na mizumu, hamjui mateso gani ninayoyapata…nisingeliweza kumsaliti ndugu yangu kamwe, hata yeye atakuwa analifahamu hilo, kamwe, nisingeliweza kufanya haya ninayoyafanya hapa…’akawa anaongea kwa haraharaka kama vile anaogopa kukatishwa.

‘Swali langu ni kuwa wateja wako ukishawaambai kuwa mtu fulani ni mchawi, una uhakika gani kuwa huyo mtu ni mchawi kweli?’ akaulizwa.

‘Unapoenda kwa dakitari kwenye mahospitali yetu, ukaambiwa una malaria una uhakika gani kuwa kweli una malaria,?’ akauliza

‘Usiniulize swali jibu swali…’yule wakili akacheka kidogo, huku akitikisa kichwa kama kusikitika.

‘Hilo ndio jibu langu, kwani ulikuwa unataka nikujibu vipi…’akasema huyo shahidi kama vile anauliza

‘Hilo ni jibu au ni swali ?’ akaambiwa na wakili ambaye alionyesha uso wa kushangaa.

‘Kwangu mimi ni jibu maana ukijibu swali langu utakuwa umeshajibu swali lako uliloniuliza…’akasema huyu shahidi akiwa kamkazia macho huyo wakili, na huyo wakili akamtizama na akageuka kuangalai watu huku akiuliza swali jingine.

‘Kuna matukuio mengi sasa hivi yanatokea, kuna maujai ya watu wenye matatizo ya ngozi wanaoitwa Alibino, wanauwawa kutokana na nyie mnaojiita wataalamu, na hata huyu….mama mkunga aliuwawa kutokana na … ramli zako za uwongo…..’kabla hajamaliza wakili mwanadada akaweka pingamizi kuwa wakili anaongea mambo yasiyohusika, anapnadikiza mambo ambayo shahidi hayajayasema.

‘Sawa …nitauliza kwa namna nyingine…’akasema wakili mtetezi baada ya hakimu kukubali pingamizi hilo.

‘Mteja nikiwa na maana mgonjwa au mtu mwenye matatizo yake anapokuja kwako, ukamwangalizia, au kama muitavyo, kumpigia ramli, na kumwambia mtu fulani ni mchawi wako,..na ukampa dawa, ambayo inakwenda kumdhuru huyu uliyemuita ni mchawi , huoni kuwa wewe ndiyo chanzo cha hayo…?’ akauliza na wakili mwanadada akaweka pingamizi, lakini ajabu hakimu akataka swali hilo lijibiwe.

‘Mimi sitaki kwenda mbali na kesi yetu hii, maana mimi sio mwanasheria lakini nina uzoefu na mambo haya, ….., nitakijibu kwa mujibu wa kesi yetu, maana hapa nilipo kama nilivyokuambia, nipo kwenye uangalizi wa hawa mizimu,mizimu ipo nami hapa inaniangalia kila ninalolifanya….sitakiwi kuongopa….mnasikia sana’akataka kuongea lakini wakili mtetezi, akasema inatosha hana swali jingine.

Wakili mwanadada akasema; ‘ Ndugu muheshimiwa hakimu, kwa vile wakili mtetezi kauliza hilo swali hebu naona ni vyema shahidi akalijibu, nilikuwa nataka shahidi huyu atuambie je ni kweli kuwa yeye alipiga ramli kuwa mama mkunga ni mchawi, na je ni kweli kuwa yeye ndiye aliyeamrisha kuwa mama huyo  auwawe kwa moto kutokana na ramli yake hiyo?’ akaulizwa wakili mwanadada.

Wakili mtetezi kusikia hivyo akaweka pingamizi kuwa yeye alisharizika na maelezo yake, hahitajii hilo swali kujibiwa tena, lakini hakimu akasema alisharuhusu hilo swali lijibiwe, na hapo shahidi akageuka kumwangalia kiongozi wa kijiji, na kusema;

‘Samahani sana ndugu yangu, nasema haya kwa vile sina jinsi,, na ingelikuwa ni uwezo wangu nisingelisema haya nitakayoyasema sasa hivi, na inabidi niyaongee haya kwa vile nihisi itakuwa ndio mara yangu ya mwisho kuonana mimi na wewe au kuniona tena katika ulimwengu huu….’akasema akionyesha huzuni, na huku akikunja uso kuashiria machungu, na sekunde cache zikapita bila ya yeye kusema kitu, halafu akasema;

‘Haya , haya waungana niachieni, nitasema yote…tafadahali niachieni,…..’akasema huku akijinyosha nyosha kama vile mtu anayehisi mauimvu mwilini.Hakimu alikuwa kaduwaa akimwangalia huyo mtu, huku akionyesha uso wa kushangaa, lakini hakusema kitu, akageuka kumwangalia wakili mwanadada, ambaye naye alikuwa kaduwaa vile vile, akimwangalia shahidi wake huyo.

Shahidi huyu akafuta jasho, halafu akaanza kuongea, huku akimwangalia mshitakiwa mkuu, na mshitakwia mkuu, alionekana kuwa mbali kimawazo, na hakuacha kumwangalia shahidi huyo, kama vile hataki jambo limpita, au alikuwa haamini hayo anayosema ndugu yake….

‘Kutokana na  hali ilivyokuwa, kuwa mali aliyoacha baba yetu, yaani mali ya aridhi kama alivyoigawa mafungu, kuwa shemu hii ni ya huyu na sehemu hii ni ya yule, na akatuambia tusiiguse sehemu ya pembeni, kwani ni mali ya m toto wake mwingine wa kike, yaani mama mkunga….’akatulia.

‘Kwa kipindi hicho sikuwa ninatambua kuwa ni huyo ni mama mkunga, nilikuja kufahamishwa baadaye na ndugu yangu huyo, kiongozi wa kijiji, lakini ndugu yangu huyo, pamoja na wanandugu wengine, hawakuwa tayari kufanya hivyo….’akatulia na kubetua mdom.

‘Unajua tena baba hakuwepo tena duniani, sisi ndio tulikuwa na mamlaka ya kufanya lolote, tukasahahu usia, ndivyo ndivyo tulivyo binadamu, au sio….., wengi wetu, tukaona hayo yalikuwa ya mzee, akiwemo ndugu yangu huyo,wakasema huyo ni mwanamke tu, hana stahili ya kurithi kitu , kwanza ana mume wake,kwahiyo hana mamlaka na mali hiyo tena…huko alipoolewa, atapata hicho anachokitaka, kwahiyo hastahili, kupewa chochote….’akatulia.

‘Wapo waliosema kuwa ni haki yake, lakini hawakuwa na nguvu sana kwasababu ni wachache…maamuzi yakapitishwa kuwa mama huyo asipate kitu,…na kweli eneo hilo likawekwa chini ya mamlaka ya familia, na ilivyopangwa, ni kuwa kama sipo kuuzwa, basi tugawane….ikapitishwa’akatulia kidogo.

‘Haaah, baadaye mama mkunga akatokea na kuanza kudai haki yake, kwani alishaambiwa kuwa kuna haki yake, na …..sisi kama wanafamilia, tukaziba masikio, na kujifanay kushangaa, lakini kama nilivyokuambai kati yetu kuna walioona kuwa ni haki yake, hawo, wakawa wanampa ndogondogo, …hapo sasa tutakaona ni tatizo, kwahiyo ikabidi itafute njia ya kuhakikisha mama huyo , hawezi kufanya lolote, na na hapo….mhhh, ile njia ya ukitaka kumuua mbwa kwanza umuite majina mabaya ikaanza kutumika, …’akasema na kutulia huku akitabasamu.

‘Kwahiyo mimi kama mtaalamu nikatakiwa kusema nimepiga ramli, na imeonekana mchawi wa watoto wachanga wanaokufa mara kwa mara hapo kijijini ameshafahamika….kuwa ni yeye, kuwa mama huyo ndiyee chazo cha yote hayo, anajifanya mkunga, huku anafanya mambo yake….’ Akakunja uso kuashiria huzuni.

‘Nikatakiwa kusema mama huyo ndiye mchawi ndiye anayewauwa watoto hawo kwa ajili ya mambo yake ya kichawi,….na ufahamu kuwa mimi ninaaminika kweli nitakachokisema huwa kinaaminika…kwani mambo yangu sio mchezo, na ni kweli nikikuangalizia nikasema kuna kitu…chunga sana, kweli kuan kitu, lakini kwa mama huyo nilitakiwa niongope…hapo niseme ukweli…’akacheka kidogo.

‘Basi, …., na ilikuwaje, maana nisingelisema tu, kilichofanyika ni kuwa alikuja mke wa Jemedari akiwa na matatizo yake kuhusiana na matatizo ya uzazi, huwa kila akijifungua, mtoto anafariki, basi tukaona ni hapo hapo, nikatakiwa kumwambia mchawi wake ni huyo mama….’ Akabetua mdomo kama anatabsamu.

‘Huyo mama kama walivyokuwa akina mama wengine, au watu wengi wanaoamini sana mambo hayo, wakakubali, …kwanini asikubali, wakati mimi naaminika kwa kazi hiyo, ….basi yeye akaenda kumuelezea mume wake, na habari zikaanza kutawanyika kwa haraka sana….unajua  uvumi wa uwongo husambaa kwa haraka sana, kama cheche za moto kwenye jangwa… mama mkunga akaonekaa kuwa kweli ni mchawi….’akasema na hayo maneno ya mwisho akayaongea kama ananong’ona.

‘Kwahiyo,kiukweli kutokana na huo utaalamu wako, mama mkunga ni mchawi au sio mchawi?’ wakili mwanadada akauliza kwa haraka.

‘Kwakweli kama nilivyosema awali, hayo yalipangwa iwe hivyo,…na nasikitika sana, kwani nilikiuka maadili ya akzi zangu, ……Inabidi nimuombe sana mama huyo msamaha kwa hayo yaliyotokea, kiukweli mama huyo yupo mbali kabisa na uchawi, …’aasema na kuangalia huku na kule kama vila anamtafuta huyo mama mahali alipo.

‘Mama wa watu hajui uchawi kabisa, sio mchawi jamani,…mama huyo ana kipaji cha kutibu watu na sio kuangamiza, ….ujue kuna tofauti ya mchawi na mganga wa kienyeji, tusichangaye haya mambo, ila mtu yoyote anaweza akawa mchawi, kama atakuwa anafanya mambo ya kuwaathiri wenzake….unalifahamu hilo, hata wewe hata muheshimiwa pale anaweza akawa mchawi,…kwa kijicho, kwa husuda, kwa wivu, akaona kwanini…..ile kwanini ni tabia za kichawi, sasa inategemea uvumilivu, kuna atakayeona kijicho, akameza ndani kwa ndani, lakini kuna yule atakayejenga fitina, ..na kuna yule atakayekwenda zaidi ya kutaka kuua….’akatulia kidogo.

‘Unajua, mchawi anatengeneza mambo yake kuumiza watu wengine ….ukiangaia ni kwasababu ya husuda na chuki zake binafsi,…. lakini mganga….’akatulia kidgogo.

‘Mganga ni kama hawo mnaowaita madakitari wa mahospitalini,…na ndio huyo mama mkunga, yeye hutengeneza dawa tu kutokana na kipaji,…..mama huyo hakuwa akitengeneza kutibia mtu aliyelogwa, kwasababu hayajui hayo mambo kulogwa, yeye alikuwa akitengeneza dawa, kutokana na ugonjwa  na uzoefu, au kipaji, alichokipata, hatumiii mizimu au ramli kama sisi wataalamu,….ukifika kwake kama unaumwa tumbo, atakuuliza tumbo linaumaje, yeye ukimfahamisha, anakupa dawa,anayoijua kuwa inatibu tumbo la namna hiyo, maana kuna matumbo ya namna nyingi……ndivyo alivyo, yeye sio mchawi kabisa, ….na zaidi ya hapo ana kipaji cha ukunga…’akatulia.

‘Je siku mama huyo alipochomewa nyumba yake moto ulikuwa ukifahamu?’ akaulizwa.

‘Kiukweli kabisa, sikujua ni lini watafanya hivyo, ila nilikuwa nafahamu kuwa kuna mpango kama huo, na shinikizo kubwa lilikuwa kutoka kwa vijana, kuwa kama kweli mama huyo ni mchawi…kama nilivyoagizwa niseme,…, basi dawa yake ni kumteketeza kwa moto….wao walipendekeza hivyo,lakini mizimu hataki hivyo, ndio maana napewa adhabu….’akasema

‘Na wewe uliunga mkono wazo hilo….?’ akaulizwa.

‘Hapana, mimi nililipinga kwa nguvu zangu zote, maana nilikuwa nafahamu kuwa mama huyo sio mchawi, na uzushi huo kwake, ulitungwa, kutokana na matakwa ya familia, kuwa aonekane hivyo, na hata akidai madai yake, jamii, isimuamini,..na tulijua kwa aibu kama hiyo asingeliweza kuishi tena hapo kijijini, angelikimbia na sisi tufanye yetu kwa ulaini…lakini mama huyu hakutishika na uzushi huo…akatukwaza….unafikiri hapo shetani keshajaa kichwani mtafanyaje…mtu mmoja tu, atunyime raha….mhhhh.’akatulia.

‘Siku akichomewa moto, wewe ulikuwa wapi?’ akaulizwa.

‘Mimi niliitwa kijiji cha jirani, nilikuwa nafanya kazi zangu…siunajua tena, leo nipo hapa kesho naitwa kwingine,…., na nilipata taarifa hizo kuwa huyo mama keshachomewa nyumba yake moto, na inasadikiwa kuwa kaungua kabisa, hata kiwiliwili chake hakikupatikana, hapo nikaingiwa na wasiwasi,…haiwezekani mtu aungue kabisa, hata fuvu la kichwa lisipatikane,…inawezekana kutegemeana na moto ulivyo, lakini sio kwa moto kama huo, manyasi tu, na fito…na fito zenyewe basi fiti….hawakuwa na uwezo wa kujuenga nyumba imara sana, kwahiyo moto huo, usingelimaliza kiwili wili chote….’akasema

‘Ni nani aliyekufahamisha hivyo, kuwa huyo mama kachomewa nyumba yake moto, na kuteketea kabisa?

‘Wa kwanza kabisa ni ndugu yangu huyo mzee wa kijiji…..’akasema huku akiona aibu kumwangalia ndugu yake huyo,akawa anamnyoshea kidole huku akiwa katizama pembeni.

‘Je alikuwambia ni yeye kafanya hivyo ?’ akaulizwa

‘Alichoniambia ni kuwa ile kazi imefanyika, na nikaumuuliza kazi gani, akasema yule mama wanayemuita kuwa ni mwanga ameshateketezwa kwa moto, hayupo tena duniani , nikamuuliza una uhakika na hilo, je mwili wake ameuona…akasema hakuwa na haja ya kuuona, ila amethibitisha kwani alishuhudia moto ulivyokuwa na hakuona mtu aliyewahi kutoka nje…’akatulia na sauti ya kuguna ikasikika kutoka kwa mshitakiwa mkuu, kama vile anapinga,lakini wakili wake akamtuliza.

‘Wewe ulifanya nini baada ya kusikia hivyo?’ akaulizwa.

‘Kwakweli niliumia sana…..sijawahi kujisikia vibaya kiasi hicho, maana kupanga ni kitu kingine, na kutekeleza yale mliyoyapanga ni kitu kingine,..wakati tunapanga, ilikuwa ni kama maongezi tu, na sikuwa nayakini kuwa jambo baya kama hilo litatekelezwa, …sasa kusikia kuwa limetekelezwa, na mimi ndiye niliyetumiwa kama chambo, niliumia sana, na hapo hapo nikaanza kuandamwa na ndoto mbaya, mizimu ikaanza kunisakama….kuwa nimekiuka masharti ya taaluma yangu…’akasema.

‘Ulirejea nyumbani siku hiyo hiyo, baada ya kusikia hivyo?’ akaulizwa.

‘Niliposikia hivyo, nilimuaga mwenyeji wangu,…kuwa nimesikia jambo la kuhuzunisha, na mimi ni mwanandugu, kwahiyo inabidi nirejee nyumbani haraka iwezekanavyo,…nikarejea usiku ule ule…na nilifika eneo hilo na kukuta bado moto unawake, nikazunguka, nikitumia hisia zangu za kitaalamu, lakini hisia hizo zilikuwa zimeshaondolewa mwilini, nilikuwa mtupu kabisa….’akasema

‘Kilichobakia akilini mwangu ilikuwa ni uzoefu tu,…nikajua kuwa mimi sio mtaalamu tena, ..sina changu tena, mizimu imeshanitoa kwenye kundi lao, iliyobakia ni adhabu yao…nikalia sana,…nikajuta sana, na wakati nazunguka eneo hilo, ndipo nikasikia mtu akigugumia kwa maumivu, hapo akili ikaniashiria jambo, ….nikakumbuka hisia nilizokuwa nazo nilipopewa hiyo taarifa, kuwa kama hawakuona mwili,au mabaki yoyote basi yamkini, mama huyo atakuwa hajafa….’akatulia.

‘Nilifuatilia ile sauti imetoka wapi,..na karibu kabisa na eneo hilo la nyumba, kuna mfereji wa maji, …mfereji huo walikuwa wakiutumia kunyweshea bustani na kulishia mabata, kwa msimu kama huo, ulikuwa na maji mchafu tu, katikati ya maji hayo, niliona kitu kimelala,…’akatulia.

‘Niliposogelea  nikagundua ni mtu, nikainama kumwangalia…mamamama….’akawa kama anaanglia pembeni kama vile mtu kaona kitu cha kustaajibika, na kuogopa kukiangalia moja moja kwa moja,…

‘Alikuwa ni mtu, kaungua,eneo lote la mgongoni, …..unajua mtu akiungua anakuwaje, ….cha ajabu hapo hapo, nguvu za utalaamu zikanirejea, mizimu ikanirejeshea nguvu hizo, ili niweze kumtibia huyo mama kama ilivyokuwa,….nikaanza kuelekezwa jinsi gani ya kufanya,…nikambeba huyo mtu, hadi maporini….na kwa muda huo sikuwa namtambau kuwa ni huyo mama…kwani nguo, zimeshangua, yupo na mabaki mbai ya nguo…sikuwa na jinsi,…’akatulia

‘Huko nikaelekezwa aina fulani ya majani, ambayo ukiyatangwa, yakawa laini, ukampaka mtu aliyeungua, hufanya kazi mara moja, huyakausha yale majeraha kwa haraka, na baada ya masaa sita, yanaanza yale majani yaliyogandana kwenye majeraha hubanduka na kuondoka na ngozi iliyosinyaa, kinachobakia ni makovu tu….’akatulia.

‘Nilifanya hivyo, na adhabu niliyopewa nikuyatafuna, hayo majani kwa mdogo wangu, hadi yatoshe mwili mzima, nilitafuna hadi kinywa kikawa kinauma, lakini sikuweza kupumzika, hadi mwili wote, sehemu zilizoungua, zikawa zimeweza kuenea ile dawa, na baada ya hapo nikaelekezwa dawa ya kumpa, ambayo aliinywa , na nikaelekezwa nimjengee kibanda, na humo niwe ninamsaidia mpaka apone….’akatulia kidogo.

‘Nilikaa na mgonjwa huyo kwa siku tatu, na alipozindukana, …nikaambiwa niondoke haraka, ili asinione, na nikafanya hivyo, na hapo nikachukuliwa na mizimu, sikujitambua nilijikuta ndani ya mapango ya watu wa kale, huko nikaweka kwenye ulinzi na adhabu yangu ikaanza kutekelezwa….’akatulia

‘Kwahiyo hukujua ni nini kilitokea huku nyuma baadaye?’ akaulizwa

‘Kwakweli hapo nilipokuwa nilikuwa nje ya dunia hii mnayoifahamu nyie, na hata kama watu waneglifika hapo wasingeliweza kuniona….nilitoka pale nilipoambiwa natakwia kuja kutoa ushahidi…’akatulia.

‘Kabla hujaondoka, tukuulize swali kuhusu sumu ambayo ilitumiwa kuwaua hawo vijana waliohusika kumchomea huyo mama na pia sumu hiyo ikatumika  kumuua Jemedari , je ni wewe uliyeitengeneza?’ akaulizwa.

‘Hapana,… ila niliwahi kumuelekeza ndugu yangu huyo jinsi ya kutengeneza sumu ambayo inaweza ikamuua mtu, na hata ukitumia vipimo vya hospitalini huwezi kugundua kuwa mtu huyo kauwawa kwa sumu, …sumu hiyo ikashafika kwenye ubongo, mtu huyo anakuwa kama kapagawa, kwasababu huathiri, mawasiliano ya ubongo, na kinachofuata hapo ni mtu huyo kuvuja damu sehemu zote za mwili, na hachukui muda anafariki…’akasema.

Wakili mwanadada akasogea kwenye sehemu walipoweka vielelezo vya ushahidi akatoa chupa mbili zenye vinywaji ndani akamuonyesha huyo shahidi.

‘Unaweza ukagundua vinywaji hivi ni kitu gani?’ akaulizwa na huyo mtalaamu akachukua chupa mojawapo, na kuifungua akanusa, akatikisa kichwa kuashiria sio yenyewe, halafu akachukua chupa nyingine akaitikisa, halafu akafungua na kunusa, ….lipuliza kwa pua kuashiria muwasho ndani ya pua na kuanza kupiga chafya, mfulululizo…na alipotulia akasema;

‘Ndio yenyewe, hii ni sumu, akiichanganywa kwenye kinywaji, kijiko kimoja tu, inatosha…ukikinywa hicho kinywaji..inaanza kufanya kazi taratibu,na kufanya kama nilivyoelezea awali…ni hatari kabisa, na mtengenezaji hakuweza kutumia vipimo sawasawa, alizidisha ndio maana imenipa taabu lakini mimi siwezi kuzurika maana nipo na mizimu inanilinda, ianasubiri muda wangu ufike…nawashauri sumu hii muiharibu haraka isje ikafika kwa watu wabaya, ni mbaya sana..’akasema na kuifunga, na wakili mwanadada,a akaichukua na kuiinua juu, na kusema;

‘Muheshimiwa hakimu, nawakilisha kielelezo hiki kama ushahidi wa sumu iliyowauwa vijana na ….Jemedari, na hapo aligeuka na kumwendea msaidizi wake akamnongoneza jambo, halafu akageuka, kwenye kambi ya utetezi, na kwa muda huo, mmoja katika kambi ya utetezi, alisimama, na kutoka nje, alikuwa sio mwingine, bali ni mwanasheria wa familia, na wakili mwanadada hakujali hilo, akaendelea kuonmgea, akasema;

‘Na sasa ni zamu ya shahidi wetu mwingine…..’ na aliyetoa mguno wa nguvu, alikuwa ni kiongozi wa kijiji, na wakili wake akamtizama kwa mshangao, na akataka kumuuliza jambo, lakini akasita, kwani shahidi huyo alishafika mbele…

NB: Ni nani huyo tena, kwanini mshitakwia mkuu akatoa mguno,…je ni mama mkunga tena, au kuna mtu mwingine..naona niishie hapa kwa leo.


WAZO LA LEO:Binadamu ni kiumbe wa ajabu sana,…huwezi amini, kuwa pamoja na kujua kuwa mali, na vilivyopo dunia ni vya kupita tu, kuwa ipo siku utaviacha, lakini kila mmoja yupo mbioni kulimbikiza, na haitoshi , bado mtu anaona ni vyema kumdhulumu mwingine, ili yeye apate zaidi, au kwanini yule kapata na sio mimi….hata kama anacho, anapata kila siku, lakini kwanini zinakuwa nyingi….husuda, wivu, chuki, ubinafsi vimetawala nafasi ya mwanadamu, ndio maana amani, na upendo vinatowekea duniani. Tumuombe mungu atuepushe na tabia hizi mbaya.

Ni mimi: emu-three

No comments :