Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, August 2, 2013

WEMA HAUOZI-44



Kila mtu alikuwa na hamu ya kumuona huyo shahidi mpya alieingia, na wakati anaingia ni wachache sana walikuwa na hamu ya kumuona, kwani walisikia kuwa shahidi wa kwanza hatakuwepo, kwahiyo walijua ni shahidi mwingine ambaye sio vutio kwao. 

Alipoingia huyo shahidi mpya, na wale wachache waliomuna wakaguna na kuanza kunong'ona, wengine na wao wakashindwa kuhimili, waliinuka kwenye viti vyao, kuangalia upande ule anapotokea huyo shahidi, hata wakili upande  wa utetezi alijikuta akiangalia upande ule kwa mshangao na mshituko, na hata zile, tambo zote zilikwisha, akasogea na kumnong’oneza mteja wake, ambaye alikuwa naye kaduwaa…..

Kisa chetu kwenye sehemu hii inaanzia hapo….

‘Unahisi  huyu shahidi atasema kila kitu?’ akauliza wakili huyo wa utetezi akimuuliza mteja wake ambaye hakuwa na amani na wakati huo alikuwa akijifanya kukata kucha, kwa wembe aliokuwa kaomba ili aweze kukacha kucha zake, zilizokuwa ni ndefu…,.

‘Mimi niliwaambia huyu mtu hawezi kuuza kazi yake kwa tamaa ya pesa…’akasema huku akiwea ule wembe mbele yake.

‘Lakini usijali, hii ndio mitihani ya kazi zetu, mimi sitamtambua kwa wadhifa wake,kwangu mimi yoyote atakayesimama kwenye kile kizimba cha ushahidi ni sawa sawa na wengine wote…tutapambaan kisheria…’akasema huku akitikisa kichwa kwa kujiamini, …na mara sauti ya hakimu, ikasema.

‘Najua unafahamu taratibu zote za ushahidi, ….’akasema muheshimiwa hakimu, ambaye naye japokuwa alikuwa akitabasamu, lakini mshangao haukufichika usoni kwake.

‘Nafahamu muheshimiwa,…..’akasema huyo shahidi na kupita sehemu stahiki, akaapishwa, halafu akapanda kizimbani.

Wakili mwanadada akageuka kuwaangalia wenzake, ambao na wao walikuwa kwenye mshangao, hawakujua kabisa kuwa atakuwepo shahidi kama huyu kwa upande wao, na hata yule ambaye siku zote alikuwa akiendesha mashitaka alijikuta akimsogelea mwanadada, na kunyosha mkono wa kutoa pongezi, kwa mwanadada huyo lakini pia akasema;

‘Una uhakika atasema yote bila kuficha….?’ Akauliza

‘Wewe subiri,…’akasema mwanadada na kugeuka upande wa kambi ya utetezi, ambapo wote bado walikuwa wakikodoa macho kule mbele kumwangalia huyo shahidi, na mshitakiwa mkuu, alikuwa kaamua kuinama chini, sijui alikuwa akiomba, au akilia au mawazo yalimzidi na shinikizo la damu linampa shida.

‘Japokuwa ulishajitambulisha kwenye kiapo, lakini sasa kila mmoja anataka kukusikia vyema, kwahiyo hebu jitambulishe kwa uwazi zaidi, wewe ni nani na kazi yako ni ipi?’ akasema mwanadada.

‘Mimi ni hakimu wa mahakama ya mwanzo, lakini hapa sisimami kama hakimu, nasimama kama shahidi…’akasema huyo muheshimiwa baada ya kutaja jina lake.

‘Ni ajabu kabisa, eeh,.. hakimu leo kawa shahidi, …..’akasema mwanadada akiwaangalia upande wa utetezi, na wakati huo wakili mtetezi alikuwa akiandika andika na kujifanya hajali, aliposikia hivyo, akainua kichwa na kujifanya kutabasamu.

‘Ndugu muheshimiwa,….eeh, shahidi, maana humu ndani muheshimiwa ni mmoja, ….bwana hakimu pale mbele, …’akasema mwanadada na hakimu akatabasamu, na watu wakacheka.

‘Ndugu shahidi, nafahamu kwa uwazi unaifahamu kesi yetu hii, kwani kesi hii kwanza abisa ililetwa mbele yako kwenye mahakama ya mwanzo, na kwa mujibu wa sheria, ikaamuliwa ipelekwe ngazi za juu, je ni kwanini umeamua kuja kutoa ushahidi …?’ akauliza mwanadada.

Shahidi huyo alikohoa kidogo, kusuuza koo, na baadaye akasema;

‘Ngoja niende moja kwa moja kwenye hoja,..ni kweli kesi hii naifahamu huenda kuliko mtu yoyote, na ilipoletwa mbele yangu kwa mara ya kwanza, nilifahamu kuwa itakuwa ngumu sana, na hata pale nilipoamua kuwa iende hatua za juu bado nilikuwa sina amani, kwani nilitenda kinyume na walivyotaka hawo watu, …., lakini japokuwa kesi hiyo ilikwenda ngazi za juu, bado nilijua huenda , haki isingelitendeka….’akasema

‘Kwanini ulikuwa na wasiwasi huo?’ akaulizwa.

‘Kwanza nianze kusema kuwa, kuna baadhi ya wahusika, ambao ndio shina, hawapo kwenye kesi hii, je ni kwanini, kwani nafahamu labda ni kutokana na wadhifa wao, lakini hata hivyo, walistahili angalau kutajwa kama washitakiwa,…, je huoni hapo kuwa huenda wanalindwa, na huko kulindwa, hakuwezi kuifanya haki isitendeke….’akasema na wakili wa utetezi akaweka pingamizi kuwa hakimu huyo anataka kuleta kesi isiyokuwepo kwenye kesi hiyo.

Hakimu akamwangalia hakimu mwenzake,akatabasamu na kusema ;

‘Endelea muheshimiwa,….usiwe na shaka haki itatendeka, nafahamu unafahamu hivyo…’hapo watu wakacheka.

‘Unaposema kuna wahusika ambao ni kama shina ambao hujawaona hapa, una maana gani muheshimiwa….?’ Akaulizwa

‘Nina maana kuwa hawo watu walikuwa mstari wa mbele, kuyakumbatia haya yote, na huenda kama wangelitimiza wajibu wao, huenda tatizo hili lingelikwisha mapema,….na kwasabau ya hilo, hawa watu wa chini, walijiona wana haki, na wasingelifaanywa lolote….’akasema shahidi

‘Ndugu muheshimiwa ….oh, samahani, ndugu shahidi,….’watu wakacheka.

‘Ndugu shahidi hebu tueleze sasa, je wahusika hao unaosema ndio mashina, walifanya nini, ambacho kiliwahi kuletwa kwako, na ukagundua kuwa ni wao…babadala ya hawa washitakiwa wengine?’ akauliza mwanadada, akijua kuwa kapeleka mbele zaidi, lakini alifanya hivyo, akijua kuwa muheshimiwa huyu anajua ni nini kinatakiwa kufanyika kabla hajajibu sehemu hiyo.

‘Kesi hii ilipoletwa mbele yangu, na kuitangaza, kuwa itasikilizwa kwa tarehe iliyotajwa, nilishangaa usiku nikijiwa na wageni,wageni hawo, walijitambulisha, kuwa ni wazee wa kijiji,….akiwemo mkuu wa kijiji hicho?’ akasema muheshimiwa hakimu.

‘Una maana huyo mkuu wa kijiji ndio huyo mshitakiwa mkuu?’ akaulizwa

‘Ndio yeye …yule pale, …’akasema hakimu wa mahakama ya mwanzo

‘Walikuja kwako kwa ajili gani?’ akaulizwa.

‘Kwanza hawakuliweka wazi jambo walilonijia, lakini baada ya kuwahoji, zaidi, wakasema wazi wazi, kuwa wanataka kesi hiyo ifutwe, na isisikilizwe tena…na nilipowaambia hilo haliwezekani, wakasema niwe makini kwa hilo, kwani mimi bado ni mgeni, na eneo hilo, lina taratibu ambazo nikizikiuka huenda , nikawa matatani…’akasema.

‘Ukawaambieje…?’ akaulizwa.

‘Nilijua ni vitisho ambavyo nilizoea kuvipata nikazarau, na kusema, mimi ninajua ni nini ninachokifanya hata hivyo, naomba wanipe muda wa kutuliza kichwa na kujua ni nini natakiwa nikifanye,…’nikawaambia kwa busara

‘Je wao walikupa sababu yoyote kuwa kwanini kesi hiyo isisikilizwe?’ akaulizwa.

‘Sababu  walionitajia ni kuwa kesi hiyo ni kifahamilia zaidi, imeingilia mambo ya mila na desturi na kama nitashinikiza na kukiuka hizo taratibu, ….nitakuwa nimeingilia mambo yaliyokuwepo tangu enzi na enzi, na kuleta mchanganyo…na yakuwa kama ni hayo mauaji yaliyotokea yalisababishwa na vijana wavuta bangi tu….’akasema.

‘Nikawaambia kuwa polisi walishafanya uchunguzi na wamegundua kuwa kuna mauaji ya kuwa hawakufa kama ilivyotajwa awali, na kwahiyo ni haki kesi hiyo sikilizwe…’akasema

‘Ina maana kesi hiyo ilikuwa ya mauji, …?’ akaulia mwanadada kama anashangaa.

‘Ndio ilikuwa ni mauaji…vijana wale waliuwawa,..ushaidi upo, lakini uliibiwa, …., na ililetwa baada ya uchunguzi, na kuletwa kwangu bado kulikuwa na utata, maana watu wa usalama walikuwa kwenye makundi mawili, wengine wakipinga kuwa sio sahihi na wengine wakisema ni sahihi…’akasema na kutulia.

‘Ukisema watu wa usalama una maana gani?’ akaulizwa

‘Kesi inapoletwa kwenye mahakama, hasa kesi ya muaji, ina maana polisi wameshafanya kazi yao, ya uchunguzi, hawo ndio watu wa usalama ninaowaongelea….’akatulia kidogo.

‘Kwanza kesi hiyo ilikasitishwa kuletwa mbele yangu, ikiaminika kuwai vijana hawo walikufa kwa kuvuta bangi, lakini ukumbuke kuwa vijana hawo ndio waliokua walinzi wa kijiji, ...na moja ya kazi yao ilikuwa kuwatafuta vijana wavuta bangi, leo unaambiwa kuwa wamekufa kwa sababu ya bangi zao…haiingii akilini…sasa alipokuja huyo mkuu idara ya upelelezi, nikamuomba afanye uchunguzi , na yeye akakubali, na ndipo, wakagundua mengi, ambayo ndiyo yaliyonifanya nije hapa kuyafichua, baada ya vielelezo vilivyokuwa vimeibiwa kupatikana….’akasema, na upande wa utetezi, ulitaka kutoa hoja, lakini ukasita.

‘Haya muheshimiwa uwanja ni wako unaweza kuendelea…’akasema mwanadada, akisogea nyuma, kuonyesha kuwa hapo anamuachia shahidi aendelee mwenyewe.

‘Kwanza kabisa niliamini waliyosema hawo wazee, unajue tena unapokuwa mgeni, na kutokana na kazi yetu ilivyo, nisingeliwakatalia moja kwa moja, nikawaambia wanipe muda, ili nione jinsi gani nitakavyofanya, maana wamekuja na ujumbe, na mimi siwezi kuwaahidi moja kwa moja kuwa nitafanya wapendavyo wao….’akatulia.

‘Kilichonishitua ni pale nilipokabidhiwa kitita cha pea na hati ya eneo la shamba, kuwa hivyo ni mali yangu…’akasema

‘Samahani kidogo muheshimiwa , nikurudishe nyuma, hawo vijana waliouwawa, uliweza kugundua walikufa kufa vipi?’ akaulizwa

‘Kwa sumu,…nitakuja kutoa ushahidi huo baadaye, na aina ya sumu waliyoitumia ambayo ni ya asili, sio rahisi kupima kwa vipimo vya haraka ukagundua…..’akasema na kutulia kidogo

‘Na endelea hapo uliposema ulipewa eneo , ni eneo lipo na lipo wapi….?’ akaulizwa.

‘Ni eneo kwenye kijiji hicho chenye migogoro, na sehemu kubwa iliyotoka kwa mke wa marehemu, huyu mwanamke, alinunua eneo, na hilo eneo hakutaka kuliweka katika madai yake, kwani alikuja kuambiwa baaadaye kuwa katapeliwa, kuwa alikuwa kanunua eneo langu, na alipoonyeshwa hati na kila kitu, akajiona hana chake…, hakutaka kujihusisha nalo tena...sijui kwanini hakupambana na watu waliomuuzia,….labda atakuja kuwakilisha madai yake kwenye kesi yake.’akasema hakimu huyo.

‘Kwakweli nilipokuja kugundua baadaye kuwa eneo hilo ni mali halali ya mjane,..na yeye mwenyewe katika madai yake hakuweza kuliweka, kama sehemu ya madai, iliniuma sana…lakini sikuweza kuonyesha hisia zangu kwa wakati huo, niliona jambo bora nikujifanya ni mmoja wao, na ipo siku nitayafuchua haya yote…na haki yake itarejea mikono mwake’akasema huyo shahidi.

‘Je ulipokea hizo pesa na hati ya nyumba waliyokupa?’ akauliza mwanadada.

‘Mwanzaoni nilikataa kata kata,, …, na walipokuja mara ya pili nikavipokea, nikiwa kwani nilikuwa nimejiandaa,…’akasema

‘Ulikuwa umejiandaa kwa vipi?’ akaulizwa.

‘Naomba ushahidi wa kanda ya DvD, uwakilishwe mbele ya mahakama hii, kuonyesha tukio zima lilivyokuwa, nahisi watakao-uona kwa haraka watafikiria kuwa mimi nilikubali kupokea hiyo rushwa, lakini je ningekubali vipi, na hapo hapo nijirekodi,…kama nilivyowaambia, nilifanya hivyo, nikiwa na maana ya kujifanya nipo nao, ili baadaye niweze kuwanasa…’akasema

‘Endelea muheshimiwa…tunakuelewa,’akasema mwanadada.

‘Ilibidi sasa nijihusishe kwenye uchunguzi binafsi kufuatalia, ni kwanini haya yote, ni kwanini ifikie hivyo, kwanza nikakutana na mkuu wa kituo cha polisi, nikaongea naye,…’akacheka

‘Msione kwanini nacheka, maana mkuu huyo alinisihi kuwa nichukue hizo pesa, na hiyo hati na kama nahitaji zaidi niseme, na yeye atahakikisha kuwa napata zaidi….’akasema na watu wakaguna na wengine kucheka.

‘Nikaona sasa kazi ipo, kama mwenzangu ambaye niliona kuwa tutashirikiana naye, anasema hivyo, je mimi nitafanya nini…elewa makosa kama hayo yakitoea, watu wazuri wa kuyafuatilia ni watu wa usalama , na ukimpata kiongozi wa juu ni vyema zaidi maana yeye atatoa amri kwa watu anaowaamini…sasa nimefika kwake, na kupewa hilo jibu kama hilo ningefanyaje….’akatulia.

‘Hapo nilichanganyikiwa, na ukumbuke kabla ya hapo nilishapata vitisho vingi, na hata familia yangu ikatishiwa usalama wake, ndio maana familia yangu haipo hapa, ….hayo yalitokea nyuma kwenye kesi nyingine, maana ilifikia htua nachaguliwa kesi za kusimamia, na nyingine naambiwa nizipotezee…’akasema na watu wakacheka…’na yeye akatabasamu.

‘Nilipokuwa mkaidi, …kama mnakumbuka vyema, binti yangu alipotea kijabu ajabu,…na ogopa mtu akikugusia familia yako, na binti nilikuwa nampenda sana…nilikuja  baadaye kuambiwa kuwa ili nimpate huyo binti yangu, nihakikisha nafuata hayo wanayotaka wao…maaliwatani wa kijiji, …’akatulia.

‘Kiubinadamu, unapogusiwa familia yako…hasa watoto wako, inashitua moyo, na hapo niliwaza kwanini nisiwe upande wao kwa muda, ili niikoe familia yangu kwanza , kwahiyo nikakubali, lakini hawakujua lengo langu ni-nini….’akatulia na wakili wa utetezi, akasema;

‘Usitudanganye muheshimiwa,…umewasaliti wenzako baada ya kuona mambo yanakuwa magumu…’akasema wakili mtetezi chini kwa chini, na watu wakasikia na kucheka, na hakimu akamwangalia huyo wakili, na huyo wakili akasema;

‘Samahani muheshimiwa imenitoka tu….sikuwa na nia ya kusema….’akasema huku akiinama kuomba msamaha, na atu wakacheka.

‘Tusifanye mzaha,…hapa tupo kwenye kesi ngumu, ambayo inahitaji umakini….tusipotimiza wajibu wetu, haki za watu zitapotea, na hata fitina zitatokea, nakuonya kwa mara ya mwisho …sitaki mzaha, na ikitokea tena, nitaanza kutoa adhabu, kutokana na vifungu vya sheria…’akasema hakimu.

‘Shahidi endelea…’akasema hakimu huku akiandika jambo kwenye makabrsha yake.

‘Basi kweli nilipoanza kufanya watakavyo wao, binti yangu akapatikana,…..sikuamini siku hiyo, mke wangu alilia sana, na ungemuona huyo binti alivyokuwa machozi yangekutoka, maana sisi tulishafikia hatua ya kuwa huyo binti keshafariki, na tulipomuuliza ulikuwa wapi, yeye anasema hajui, hajui kabisa, …na alikuwa kama kachanganyikiwa…akili haijui, imesimama, anakuwa kama zezeta fulani hivi…kachafuka, ana minywele mirefu….’akasema

‘Siku alipofika, kesho yake akaja mtu wanayemuita `mtaalamu’ yeye alisema kuwa ndiyo yeye aliyesaidia binti yangu kupatikana…akadai kuwa bint yangu alichukuliwa msukule, lakini hakufanywa kama wanavyochukuliwa watu wengine, alikuwa kahifadhiwa kwa muda…., na kwahiyo kuna dawa atampa na binti yangu huyo atarejea kwenye hali yake kama kawaida.

‘Mke wangu aifiki ahdi kumpigia magoti, kuwa afanye hivyo, amrejeshe inti yangu kuwa katika hali yake ya kawaida, na atamlipa pesa azitakazo, na huyo mtu akasema;

‘Mimi sitaki pesa yenu, ….timizeni matakwa ya hawa watu, kuwa msitende kinyume na maagizo yao, vinginevyo, binti yenu akipotea tena hamtamuona, maana atawekwa kwenye kundi la hawo msukule wa kawaida…mimi natimiza wajibu wangu tu, sihitaji hata senti moja kutoka kwenu…’akasema na kweli akampa dawa binti yangu na, kesho yake akaamuka akiwa yule binti yetu tuliyemzoea, akiwa na afya yake kama  ya kawaida, lakini hakuweza kukumbuka wapi alikuwa anaishi kwa miezi hiyo mitatu  aliyopotea….’akasema.

‘Sisi mahakimu hasa mahakimu wa mahakama ya mwanzo, tunafanya kazi hii kwenye mazingita hatarishi, tunakutana na majaribu mengi, na usipokuwa makini, unaweza ukasahau kazi yako na kufuata wayatakayo watu wenye ubinafsi , hasa wale wenye uwezo, au wale wanajiita maaliwatani wa eneo husika…kwasababu mahakam hizo ndizo zilizopo karibu na watu,…na nyingine ukifika zimechoka,…kama walivyo mahakimu wenyewe’akatulia na watu wakacheka..

‘Tulishauriana na mke wangu, kuwa ni bora wao waondoke, warudi huko kwetu, ili na mimi niweze kufanya kazi yangu, na lolote likitokea nijue nipo peke yangu…ilifikia hatua nilitaka kuacha kazi kabisa, japokuwa matukio kama haya sio mara yangu ya kwanza kukutana nayo, ..lakini hili lilinishitua sana, kuona binti yangu aanchukuliwa na anarejeshwa akiwa katika hiyo hali…..’akatikisa kichwa.

‘Basi nikawa nauma huku naupilizia, nikitafuta wapi niende ili tuweze kusaidiana kukomesha hii hali, na sehemu iliyotisha sana ni hicho kijiji,…na wengi wanakiita kijiji cha wanga…’akasema na watu wakacheka.

‘Ni kweli, sio kwamba natania, waulizeni watu, wanaokizunguak hicho kijiji,..na kila mara kulikuwa kukitokea mauaji na kupotea kwa watu kiajabu ajabu, na yakitokea mauaji, utakuta ni ya imani za kishirikiana…na ukiongea na polisi walifuatilie, watakuahidi kuwa watafanya hivyo, lakini huwezi kupata hitimisho lake, na wenyewe walifikia hatua ya kuogopa…mwisho wa siku kesi nyingi zilibakia kwenye majalada, na nikaonekana kama mimi sitimizi wajibu wangu….’akatulia.

‘Bahati nzuri, maombi yangu yakakubalika, kwani niliomba kutoka ngazi za juu, kuwa kuwe na kitengo maalumu cha upelelezi, kichunguze hayo yanayotokea, …na nashukuru kuwa kiongozi aliyeletwa hapo, alikuwa jasiri,…alijiamini, wanasema wenyewe aliga kwao…’watu wakacheka.

‘Na japokuwa na yeye alikuja kupata mitihani mingi, hadi…kufikia kuachana na mkewe….lakini hakurudi nyuma, nashukuru sana kupata mtu kama huyo….lakini hawa watu, na wao hawakurudi nyuma.

‘Kwa vipi shahidi, ndio iliyokufanya uhamishwe…..na je vitisho vyao vilifanikiwa, nakuharakisha shahidi wangu maana muda wako unakaribia kuisha..’akatulia.

‘Aendelee tu, usimharakishe….’akasema hakimu, na wakili upande wa utetezi akashika kichwa huku akiwa kainamia makabrasha yake, alikuwa kama vila hataki kuskia hayo yanayoongewa.

‘Sasa kama nilivyowakilisha huo ushahidi wa kanda za DvD, mtaona mengi yaliyokuwa yakitendeka, ila swali kubwa ukizinaglia hizo kanda, za DvD, utaona kuna mtu anatoa amri, lakini haonekani, je ni nani huyo, hapo ilikuwa kazi yangu ya ziada kumtafuta,..na sio rahisi kama mnavyofikiria nyie, hakuwa kazi rahisi kuja kumpata mtu huyo, na hata nilipompata, niligundua kuwa ni …..’akatulia na kutabasamu, na watu wakacheka.…’akatulia na hakumalizia sehemu hiyo hata wakili mwanadada hakupenda kumuuliza ni nani, kwani alijua hilo litakuja kujibiwa baadaye.

‘Alipokuja huyu mkuu wa kitengo cha upelelezi, nikakutana naye na nilimuelezea yote, na yeye akasema nimpe muda, kwani ndio amefika, na ili kuweza kufanya kazi yake vyema, ni vizuri, ukayasoma mazingira, na ndivyo alivyofanya, hakuwa na papara, …na siku nyingine nilipokutana naye, akasema…’hapo akatulia.

‘Kuwa adui mkubwa tunaishi naye….’akatulia na kutabasamu

‘Adui mkubwa ni mtu asiyeshikika kirahisi, na tusipoangalia tutaumia, kwani mwenzetu kashikilia mpini, kwahiyo tuwe makini kwa kila hatua,…nikamkubalia, na hakutaka kuniambia ni nani, alisema ipo siku ataniambia, lakini mpaka apate uthibitishi ulio wazi, ..maana huyo mtu huwezi ukapeleka shutuma zako zisizo na mguu wala kichwa, hizi shutuma zitakugeukia wewe mwenyewe…’akatulia.

‘Mimi nikamwambia nina ushahidi, nimeshaukusanya, kwahiyo kama anautaka basi nitampa ili tuufanyie kazi…’akasema bado hauhitaji huo ushahidi, yeye anataka kukushanya ushahidi wake mwenyewe kwa namna anayoijua yeye…mwanzoni nikajua ni wale wale…’akatulia na watu wakacheka

‘Na haikupita muda, ushahidi wangu wote ukapotea….’akatulia.

‘Hebu wewe fikiria ungelimshuku ni nani aliyeuiba huo ushahidi…sikuogopa nikamwendea huyu mkuu wa upelelezi nikamwelezea hisia zangu, kuwa ni yeye peke yake ndiye anayejua kuwa nina ushahidi kama huo, na sasa umepotea,…tukawa hatuelewani, kwani yeye alikataa kata kata kuwa hakuchukua yeye…’akatulia.

‘Kwa hali kama hiyo utakwenda wapi, utamwambia nani, na nimeshatishiwa kuwa huyo ambaye hajulikani, ni mtu,anayejuana na wakubwa wote…’akatulia.

‘Siku moja nikiwa nimetulia, nikiwa sasa naendesha hii kesi ya mwanamama, alifika mtu mmoja, akiwa kava mawani meusi, akaniambia

‘Ndugu tunakupa onyo la mwisho,…kesi hii ya mwanamama, ipotezee, au hakikisha huyo mwanamama hashindi maana akishinda, hata eneo la shamba nililopewa, itabidi lichukuliwe….na pia nisijidangenya kuwa kwa vile nipo peke yangu bila familia …hakutafanyika kitu….akaniambia kuwa wenzangu hawo waliomtuma  wana ushahidi kuwa nilipokea rushwa…kwahiyo nisipofanya wapondavyo wao, watahakikisha nafukuzwa kazi na hiyo haitakuwa mwisho, wataniandama mimi na familia ayngu hadi nitatamani kujiua…’akatulia.

‘Nikagundua kuwa sasa kila kitu kimeharibika…na niligundua kuwa huenda ni kutokana na ule ushahidi ulioibiwa, na kama nilivyowaambia, kuwa ukiuangalai huo ushahidi kwa haraka utaona kama mimi nilikuwa napokea rushwa,….lakini ukitulia na kuangalai kwa makini, utaona kuwa kuna shinikizoa ndani yake…ikawa hivyo, na nikawa njia panda, nakujiuliza sasa nifanyeje…’

‘Hakikisha unafanya kila tunalokuambia ufanye, kuna kesi hii ya mauaji, ambayo ililetwa na watu wa usalama, unachotakiwa wewe ni kuipiga kalenda, na mengine tuachie sisi…’akasema na mimi nikamwambia

‘Acha nifikirie….’akatulia

‘Huyo mtu akaniuliza kwani mimi nina shida gani, na kwanini nafanya kazi, …eti kazi unafanya ili uate pesa, na hawo watu wapo tayari kunipa kila kitu, kama nahitaji eneo jingine, au kama nahitaji nyumba, au kama nahitaji gari…nisema na wao watanipa, lakini hakikisha kuwa kesi hii inafutika,…vinginevyo nitahama hapa na nitapelekwa sehemu ambayo sipendi kwenda na huko utakuwa ndio mwanzo wa kupoteza jira, na mwisho wake nitafukuzwa kazi na kubakia masikini …’akasema.

Hapo mimi sikuvumilia uajsiri ukanijia, na siku hiyo nilikuwa nimeandaa kifaa cha kurekodia kila kitakachotokea, kwahiyo niliongea kwa kujiamini, kuwa sasa nimewapata, nina ushahidi mwingine…’akasema huyo shahidi

Nikamwambia huyo mtu,….‘Mimi sifanyi kazi hii kwa ajili ya utajiri…kama ni utajiri wa namna hiyo ningelishaupata siku nyingi, lakini najua kuwa utajiri wa namna hiyo ni wa muda mfupi, …dhambi za namna hiyo hazina muamala, maana unakuwa rafiki wa shetani, na mimi sio shetani….’nikasema na huyo jamaa kacheka sana, na kuondoka.

'Ulikuja kumgundua huyo mtu ni nani?' akaulizwa

'Ndio nilikuja kumgundua,

‘Haikupita muda ndio nikapata huo uhamisho wa haraka haraka, na nilipata ujumbe kuwa huo ndio mwanzo wa kuhakikisha maisha yangu yanapotea…haitachukua muda nitafukuzwa kazi..’akasema.

‘Ndio umehamishwa na kazi umefukuzwa kama walivyodai wao…?’ akauliza mwanadada kitabasamu.

‘Kuna barua nimeletewa hivi karibuni, siwezi kuliongelea hili hapa kwasasa, …lakini hata hivyo nipo tayari kufukuzwa kazi, nikijua ninachofanya ni haki, na nitasimamia hiyo haki hadi hapo…na  kadri ya uwezo wangu, najua jinsi gani ilivyo ngumu , hasa familia yako inapoingiliwa, familia isiyo na hatia,na wala haijui ni nini kinaendelea, najua jinsi gani maisha yalivyo magumu, ukiacha kazi kwa hali tuliyo nayo, huna mbele wala nyuma,unaweza ukaishia kubaya, nimeliona hili kwa watu wengi….kwani hutaamini huko nilipohamishiwa kulikuwa na vitisho,juu ya vitisho, usiku mapaka yanahamia kwangu……’akatulia na akawa kama anaangalia juu na watu wakacheka.

‘Msicheke, …jamani kuna vioja huku duniani,….inataka moyo,..na kama huna imani thabiti, huwezi kabisa kuifanya hii kazi yetu, lakini mimi imefika sehemu nimesema basi,  liwalo na liwe, kama niliamua kufanya akzi hii, nahitajika kukubali matokea, ….na huwezi jua, ni bora ufe ukiwa mpinaji kulikuwa kufa ukiwa msaliti, wan chi yako…nilikwenda nyumbani mara moja, nikaaga,kiukweli,…’akasema na hapo watu wakacheka.

‘Sasa nimerudi na nipo tayari kupambana na lolote lile….’akasema akijiamini …’Na kwa vile ushahidi uliokuwa umepotea umepatikana, sioni kwanini nisije kutimiza azima yangu…na kuna ushahidi mpya nilikusanya, na wapo watu wameshajitokea kusaidia hili, wanajua, na walihusika, wataongea kila kitu,…nina imani haki itatendeka,  …’akasema huku akitikisa kichwa

‘Sasa niingie kwenye sehemu ya pili, naruhusiwa kuendelea muheshimiwa….?’ akauliza

‘Endelea muheshimiwa….’akasema hakimu huku akiatabasamu na watu wakacheka.

‘Sasa basi ngoja turejee kwenye ushahidi wa hii kesi, ili niweze kuelezea yote, na nitamuhitajia mwenzangu upande wa usalama, mkuu wa upelelezi , aje anisaidie kuthibitisha haya, maana bila yeye nitaonekana muongo…na pia nitauhijia ushahidi huo wa kanda za DvD, uonyeshwe wazi ili muona ni nini kilikuwepo, …’akasema na kumgeukiwa wakili mwanadada.

‘Usijali muheshimiwa, …wewe ongea sehemu yako, na ikifikia muda huo wa ushahidi tutafanya hivyo, kwa idhini ya muheshimiwa hakimu, na mashahidi wengine watakuja kwa wakati muafaka, …tunakwenda kwa ratiba na …idhini ya muheshimiwa, usijali tupo pamoja’akasema mwanadada.

‘Naanza kwa kuelezea tukio la kuchomwa nyumba ya mama mkunga, ni tukio la kusikitisha sana na tukio ambalo sijawahi kukutana nalo katika maisha yangu..na siku nilipoletewa hiyo kesi, sikuamini…maana ni unyama wa hali ya yajuu…mtajionea wenyewe muda ukifika wa kuona huo ushahidi.

‘Lakini cha ajabu, nilikuja kugundua kuwa huyo muhanga, wa kuchomwa moto, sio mtu baki, kumbe wana udugu kabisa na …kiongozi wa kijiji….huko nilipopelekwa nilikutana na familia , sehemu ambapo huyo mama mkunga alilelewa, …kuna kisa cha aina yake kilitokea kwenye huo ukoo…hapa sina muda wa kukismulia,….nilichoshangaa ni kuwa huenda huyu mzee, wetu alifahamu hilo, au hakuwa analifahamu,…

‘Nilipofika hapa jana, niliuliza kama huyo mzee anafahamu kuwa huyo mama mkunga ni ndugu yake, nasikia alikuwa hajui kuwa huyo alikuwa dada yake, lakini kutokana na mifarakano ya akina mama , ndugu yake huyo aliondoka na kwenda kulelewa huko nilipopelekwa, na mungu akanikutanisha na walezi wa huyo mama…na bahati huyo mama akaja kuolewa huku, sehemu yake alipozaliwa, bila kujulikana, bila hata ya yeye kujua,…kwani yeye alirudi hapa akiwa mkubwa,…na hakuna aliyekuwa akijua kuwa  huyo mama na mzee wetu huyo wana udugu, taarifa hiyo waliletewa hivi karibuni….’Alipofika hapo, akasikia mtu akipiga yowe….’

Kila mtua akageuka kule yowe lilipotokea, ilikuwa ni upande wa kambi ya utetezi na wakati huo ilionekana, ni kama lile tatizo la mwanzo limetokea tena, lakini kwa sasa ilikuwa ni zaidi ya hayo, kwani mshitakiwa mkuu alikuwa kalala sakafuni, na alioneka mlinzi akijaribu kufanya kazi yake…..ya kuwasogeza watu wa kambi hiyo wakae mbali na mshitakiwa mkuu, ili aone ni nini kimtokea…

‘Kuna nini….?’ Akauliza hakimu

‘Limetokea tatizo kama lile la mwanzo, huyu mtu kashikwa na mshituko, na inaonyesha  hali yake ni mbaya zaidi,….’akasema huyu mlinzi na hakimu akaamrisha watu wa huduma ya kwanza wafike haraka, kuhakikisha wanadhibiti hali ya mshitakiwa huyo....kama inawezekana kesi iendelee

Ilipita dakika kumi, na mseamji wa wahudumu wa huduma ya kwanza akasema huyo mtu anahitajika kuwahishwa hospitali haraka iwezekanavyo, kwani inawezekana ni shinikizo la damu,ambalo limekuja ….na hali yake ni tete zaidi ya mwanzo.

****

‘Ilikuwaje…..?’ akauliza mmoja wa watu wa kambi ya utetezi ambaye hakuona jinsi ilivyokuwa, akimuuliza mtu wa karibu wa mshitakiwa huyo.

‘Shahidi alipokuwa akielezea habari za huyo mama mkunga, mzee wetu huyu, alionekana hana amani, alikuwa mwingi wa mawazo, tofauti na siku nyingine, …alikuwa kama hakuwepo mahakamani, na nilimweleza wakili wake, kama vipi tuombe kesi iahirishwe, lakini mzee mwenyewe alisema lazima isikilizwe kwani anataka kumuona huyo mama mkunga, …cha ajabu pale huyo shahidi alipooanza kuelezea habari za huyo mama mkunga, ghafla akaanza kubadilika, na akawa anatingishwa, ..na kabla sijamuwahi, akadondoka sakafuni, na huku akisema;

‘Nisamehe ndugu sikujua …sikuwa nakufahamu, sikujua, sikujua, oh nisamehe ndugu yangu, halafu akapiga yowe…..ndio kauli yake niliyoiskia ya mwisho, kabla hajanyamaza na kupoteza fahamu.

‘Ina maana kweli ni ndugu yake?’ akaulizwa

‘Ni kweli, lakini hawakuwa wakifahamiana, hadi alipokuja mzee mmoja ambapo mama huyo alilelewa, na amabaye anafahamu historia ya wazazi wa hao, yeye ndiye aliyemlea huyo mama, na ilikuwa hakupenda hilo lijulikane, lakini kutokana nah ii kesi, akaona ni bora aeleze ukweli,

‘Je mshitakiwa alikubaliana na hilo …?’ akaulizwa.

‘Alisema ni kweli, anajua kuwa kuna ndugu yake, alichukuliwa akiwa mdogo, lakini walifuatilia kwa muda mrefu, na kauli za mwisho, waliambiwa alifariki dunia, kwahiyo hawakuwaweza kufuatilia tena,…ila kuna alama zao, na alitaka hiyo alama ikithibiti, basi atajua ni ndugu yake….’akasema msemaji wa mzee huyo.

‘Kwahiyo hadi hapo bado, ukweli hakuwa umetambulikana, ….?’ Akauliza.

‘Ulikuwa bado…maana hakuna anayeruhusiwa kumuona huyo mama, na je ni kweli ni huyo mama, kama mlivyoona, kafunikwa utafikiri ni kitu gani sijui….lakini leo tulijipanga kushinikiza hadi huyo mama tumuone, ili tuthibitishe, ….’akasema.

‘Lakini mzee huyu ni ngangari, sikujua kuwa leo anaweza kufika hapa, maana ule mshituko wa mwanzo ulimchukua vibaya,….hadi jana, tulijua kuwa hataweza kufika mahakamani, lakini asubuhi, anasema yupo tayari, na hata dakitari alithibitisha hilo..’akasema mtu mwingine wa karibu wa huyo mzee.

‘Mhh, tuombe mzee wetu aweze kusimama tena, maana mzigo wote katupiwa yeye, wakati inavyoonyesha kuna watu wengine, wahusika, wapo nje,….hawajakamatwa,…wasiwasi wangu ni kuwa dakitari alishauri, kama inawezekana kesi hii iahirishwe kwa wiki mbili hivi, lakini mshitakiwa alikataa, akasema atajikongoja,, na dakitari alionya kuwa kama  hali hiyo ikitokea mara tatu, basi, tunaweza kuongea mengine, ….’akasema huyo msemaji.

Sauti ikasikika ikisema kesi imeahirishwa, hadi hapo itakapotangazwa tena, na amri ikatolewa kukamatwa kwa washitakiwa wengine ambao hawakuwepo kwenye orodha ya washitakiwa.

NB: Je ilikuwaje,….Je udugu wa huyo mama mkunga na huyo mzee,ulikuwaje, kuna nini kimejificha hapa.je huyo mshitakiwa ambaye hakamatiki ni nani,….kuna nini zaidi hapo….tuwepo kwenye karibu na hitimisho cha kisa hiki.


WAZO LA LEO: Dua ya mwenye kudhulumuwa haina kizuizi, huenda moja kwa moja kwa mwenyezimungu, tuogope dhuluma, kwa kutenda wema, ili  dhuluma hiyo iweze kufutika, na kama umemtendea mwenzako dhuluma, kwanza tubu na ikiwezekana nenda kamuombe msamaha, kabla hujachelewa, kabla mlango wa toba haujafungwa, ….tusijidanganye kwa kufanya ujanja ujanja, kwa vile tuna uwezo, … 

Ni mimi: emu-three

2 comments :

Yasinta Ngonyani said...

Nasubiri kujya kinachoendelea kesi inaonekana ni ngumu kweli....inasisimua na kugopesha

Anonymous said...

First off I would like to say awesome blog! I had a quick question that I'd like to ask if you don't mind.
I was interested to find out how you center yourself and clear your thoughts
prior to writing. I've had trouble clearing my thoughts in getting my thoughts out there. I do enjoy writing however it just seems like the first 10 to 15 minutes are usually wasted simply just trying to figure out how to begin. Any recommendations or tips? Cheers!

Take a look at my web page: Laubsauger Test (smtp.Greatgiftcircle.com)