Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, June 25, 2013

WEMA HAUZI-24


Aliitwa shahidi alIyejenga nyumba naye akaelezea jinsi gani alivyokutana na mlalamikaji, wakaingi naye mkataba wa kujenga hiyo nyumba na alisema kuwa aliwahi kumuuliza huyo mwanamama mlalamikaji jinsi gani alivyozipata hizo pesa, akasema kuwa pesa hiyo aliipata kutona na kushinda promosheni ya kampuni moja ya simu;

‘Je wewe kwa akili yako uliamini hayo maneno?’ akaulizwa.

‘Mimi kama fundi wa ujenzi, nitaamini kila kitu nitakachoambiwa na bosi wangu, siwezi kumpinga..kwasababu sio kazi yangu kupekenyua maisha ya watu, kazi yangu ni kujenga..’akasema.

‘Lakini nauliza kwa akili yako mwenyewe uliweza kuamini kuwa huyo mwanamama alishinda hizo pesa,..au kuna lolote ulisikia zaidi ya hilo?’ akauliza na swali hilo likapingwa kuwa shahidi analazimishwa kuongea hisia zake, na sio hali halisi.

‘Wakati unajenga ulisikia nini, kuhusiana na hizo pesa za ujenzi…’akauliza swali, na swali hilo likapingwa kuwa shahidi anaulizwa kusikia kwa watu wengine, …..

‘Lakini muheshimiwa hakimu, hapa ninachouliza ni hali halisi, kuwa kama huyo mama hakupata pesa hizo kwa ajili ya ushindi wa hiyo promosheni basi atakuwa kazipata kwa njia nyingine…ninachojaribu kutafuta hapa ni jinsi gani nyingine iliyofanya hizo pesa zikapatikana’akajitetea

‘Basi jenga msingi wa hoja yako….kwa kupitia shahidi sio kwa hisia kutoka kwa watu wengine, natumai unafahamu nini unachokifanya kama wakili’hakimu akasema.

‘Huyo mama alikuambia kuwa alipata pesa hizo kwa promosheni, lakini kuna njia nyingine angeliweza kuzipata hizo pesa sawa si sawa?’ akauliza.

‘Ndio inawezekana zipo njia nyingi, na sio kazi yangu kujua hilo…’akasema huyo shahidi

‘Wewe unaliwazia nini, kuwa huenda kama sio hiyo promosheni,inawezekana huyo mama alizipata hizo pesa kutoka kwa njia ipi nyingine?’ akauliza

‘Inawezekana, ndio kama binadamu niliwaza hilo kuwa huenda alizipata kutoka kwa mume wake, pia nilisikia watu wakisema kuwa huenda hizo pesa….’akakatizwa  kujibu hizo swali kuwa anahisi badala ya kusema ukweli kutoka kwake mwenyewe. Wakili yule akageuka kumwangalia hakimu, kama vile anazuiwa kupata hoja yake.

‘Je baada ya kukamilisha huo ujenzi uliwahi kukutana na mume wa mlalamikaji?’ akaulizwa shahidi.

‘Mara nyingi sana,….huyo mume wake nilimfahamu kabla na hata baada ya kutoka jela yeye na mkewe waliwahi  kuniita mara kwa mara kujenga baadhi ya sehemu, kwenye nyumba yao hiyo na duka…’akasema.

‘Je marahemu alisema nini kuhusu hiyo nyumba…?’ akaulizwa.

‘Mara nyingi alikuwa akimsifia mkewe kwa juhudu zake za kuweza kukamlisha hiyo nyumba, na pia niliwahi kumuuliza gharama za ujenzi wa nyumba kuwa ni za mkewe au na yeye alichangia’akasema.

‘Na alijibuje?’ akauliza.

‘Alisema hayo ni maswala yake ya ndani na mkewe, ila siku moja alisema aliwahi kuibiwa pesa zake, huenda ndizo hizi zilizojenga hiyo nyumba…wakati yeye akiwa jela’akasema.

‘Je kipindi anaongea hayo maneno huyo marehemu alikuwaje?’ akaulizwa na wakili mwanadada.

‘Alikuwa amelewa….’akasema shahidi.

‘Na akiwa hajalewa anasemaje ukimuuliza swali kama hilo, kuhusiana na gharama ya nyumba…?’ akauliza wakili mwanadada.

‘Anasema hayo ni maswala yao na mkewe, na anaishia kumsifia mkewe kuwa ana akili sana, na ana bahati kubwa sana…’akasema.

‘Kwanini alisema mkewe ana bahati kubwa sana…?’ akaulizwa.

‘Ni kwa vile aliweza kupata hizo pesa kwa bahati nasibu..’akasema.

‘Kwahiyo aliwahi kukuambia kuwa mkewe alishinda hiyo promosheni?’ akaulizwa

‘Ndio…’mwanadada akamgeukia wakili mtetezi  na kumwambia anaweza kuendelea  shahidi na wakili mtetezi akasema

‘Sina swali jingine..’

********
Akaitwa mjumbe naye akatoa ushahidi wake, na wakati haya yanaendelea mara mwanamama mlalamikajai akamnong’oneza wakili wake;

‘Nataka unisimamishe…’akasema mwanamama mlalamikaji.

‘Hapana huu sio muda muafaka wa wewe kusimama, utaharibu kila kitu,…wewe niachie mwenyewe.’akasema.

‘Nataka nisimame nikaonyeshe huo ushahidi wanaoutaka….nimechoka na uwongo wao’akasema mwanana mlalamikaji.

‘Ukaonyeshe ushahidi gani, wewe mwenyewe unajua fika kuwa hatujaweza kuupa ushahidi muhimu, lakini nina imani tutaupata tu  …ninachohitajia hapa ni kupoteza muda, ili kesi iahirishwe ili tuweze kuupata huo ushahidi, maana bado kuna watu wanaendelea kutafuta, ….kuna dalili kuwa kweli ile stakabadhi ya malipo, iliyoonekana kuwepo kwa jina la mtu mwingine ilikuja kuwekwa baadaye,……’akasema.

‘Mimi nina ushahidi wa kuweza kuimaliza hii kesi,naomba unisimamishe ….usiwe na shaka na mimi nisimamishe na utaona ni nini nitakachokifanya,….’akasema na wakili akatulia akiwaza jambo, na mara akakumbuka yule mtu aliyekuwa na mfuko wa Rambo, na sasa huo mfuko wa Rambo upo mikononi mwa huyu mwanamama.

‘Humo kwenye mfuko kuna nini…?’ akauliza na kabla hajajibiwa na huyo mwanamama , muheshimiwa hakimu akauliza

‘Mlalamikaji shahidi wako tafadhali, tufanye haraka kidogo ….’ Akaita hakimu huku akimwangalia wakili mwanadada

‘Muheshimiwa hakimu, sasa nitamsimamisha mlalamikaji…’akasema na hakimu akajikuta mwenyewe akishindwa kuficha hisia zake, akauliza;

‘Kwanini umsimamishe haraka hivyo, huna shahidi wengine, mbona bado kuna orodha ndefu ya mashahidi wako, na hawajapata muda wa kutoa ushahidi wao….huoni kuwa utahitimisha kesi kabla ya wakati wake….una uhakika na hilo wakili , maana tunahitaji haki itendeke…?’ akasema hakimu.

‘Muheshimiwa hakimu, …nina uhakika na hilo….nataka nimsimamishe mlalamikaji’akasema na hakimu akasema mlalamikaji apite mbele na ale kiapo na taratibu nyingine zikafuatwa…

‘Hata kule kwa upande wa utetezi, hawakuamini hilo, na wakaona ndio nafsi yako ya kuhitimisha kila kitui, wakili wao na mwanasheria wakawa wanateta kimiya kimiya…huku wakishindwa kuficha hisia zao kwani kwenye nyuso zao kulionekana tabasamu la ushindi.

‘Unaonaje ukiniachia mimi…..’akasema mwanasheria kwa sauti iliyosikika, akimuomba wakili wake, na wakili wake, akasema;

‘Lakini kweli mna uhakika hawana ushahidi mwingine, kama stakabadhi ya malipo, …nahisi kama kusimama kwake kunaweza kuwa wameshapata huo ushahidi…..’akasema

‘Waupate wapi huo ushahidi, mimi mwenyewe nilifika ofisini kwenye hiyo kampuni, nikaiona hiyo stakabadhi ya malipo, ilikuwa imeandikwa jina tifauti kabisa na la huyo mama…ni ujanja ujanja wanataka kuutumia, hawana lolote,….wewe ngoja nimchemshe kidogo huyo mwanamama, japokuwa namuonea sana huruma….’akasema

‘Sawa mkuu, uwanja ni wako…

Mlalamikaji akaanza kujielezea, ilivyokuwa, jinsi walivyokutana na marehemu, akaelezea jinsi walivyofika Dar na maisha ya Dar, halafu akaelezea jinsi marehemu alivyokamatwa, kama alivyowahi kuelezea awali….

‘Nikabakia mimi peke yangu na kuanza kuhangaika, na ilifikia sehemu nilikata tamaa kabisa ya maisha, na ndipo hapo nikapigiwa simu kuwa nimeshinda promosheni ya simu….’akasema mara wakili mtetezi akasimama na kumkabili, hapo mlalamikaji akamwangalia wakili huyo kwa uso wa huzuni na wasiwasi, akijua jinsi gani wakili anavyoweza kumuuliza maswali makali ya kumafanua yeye aonekane mwongo.

‘Je unaweza kutuambia ulipigiwa kwenye simu gani, unayo hiyo simu hapa kama ushahidi, na je namba yake ilikuwa namba gani, ili tuweze kuhakiki, maana watu wa simu wanaweza kuyarudia maongezi yenu na kuthibitisha hayo unayoyasema?’ akaulizwa.

‘Sikumbuki hiyo namba ya simu , kwani baadaye hiyo simu iliibiwa…’akasema na yule wakili akatabasamu na kusema;

‘Muheshimiwa hakimu, unaona, hata namba ya simu huikumbuki, kwa vile sio kweli, ingelikuwa ni kweli, ungelikumbuka vyema hiyo namba kwani ndiyo iliyokupatia pesa…nani anaweza kusahau kitu kilichompatia bahati kama hiyo..’akasema wakili huku akitamba kwa kutemba huku na kule.

‘Katika maisha yetu sio rahisi kukumbuka kila kitu, ni nani anaweza kufahamu kesho kutatokea nini, na ni nani angelijua kuwa mume wangu angelifariki,…..na ni nani angelijua haya yote yangelitokea, na ni nani angelijua kuwa vitu kama hivyo vya karatasi ya malipo vingehitajika….ni siku nyingi zimepita na hatukuweza kuona umuhimu wake tena…, kama ningelifahamu haya yote kuwa yangelitokea, ningelitunza kila kitu….lakini’akasema kwa uchungu na kabla hajaendelea wakili mtetezi akasema;

‘Kwa hali kama hiyo, ni nani atakuamini, je tumwamini marehemu au tukuamini wewe, fikiria mimi mwenyewe niliongea na marehemu uso kwa uso, kama ndugu yangu, akanifahamisha hivyo kuwa nyumba kajenga kwa pesa yake…, na akataka niandike maandishi ya kulinda mali yake, je kwa vile kafariki ndio nibadili kauli yake….?’akasema huyo mwanasheria ambaye aliamua kumsaidia wakili wake.

‘Kuna makosa yalifanyika, nahisi kuna mbinu zilifanyika, huenda wewe huzijui, na kama unafahamu, basi umeshiriki katika kuhadaa…’akasema mwanamama, na yule wakili hakujali hayo maelezo akasema;

‘Hebu niambie, kama ungelikuwa wewe ndio mimi, upo sehemu yangu ungelifanya nini…kumbuka yule ni ndugu yangu, kaniomba nifanye hivyo, je ni kuamini wewe kuliko ndugu yangu, sasa angalia huyo sasa ni marehmu, wewe huoni kuwa tukiamini maneno yako na kumpinga  marehemu kwa vila hayupo duniani, tutakuwa tunakiuka kauli ya marehemu, na tutakuwa hatumtendei haki,….wewe huoni hiyo?’ Akawa kama anauliza.

‘Hatutatenda vibaya kwasababu sio kweli,….hayo mumezua baadaya ya mrehemu kufariki…’akasema mwanamama mlalamikaji, akionyesha hisia za uchungu.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, lengo la kutetea haki hiyo, haki ya kumuliki, sio kwamba tunafanya hivyo kwa vile ni mali,…kwa vie nyumba yenye thamani kubwa,… kwani tunaweza tukajenga wenyewe nyumba kama hiyo, …mimi nina kazi, Napata mshahara, ninaweza nikajitahidi nikajenga nyumba kama hiyo, kwanini nipoteze muda kupigania vitu kama hivyo…nafanya hivi kwa vile najitahidi kutetea kile alichoniagiza marehemu, natetea haki ya marehemu, sio kwamba mtu akifa basi haki yake ipotee, haiwezekani kabisa…’akasema huku akimwangalia hakimu na baadaye watu waliohudhuria,halafu akamgeukiwa mlalamikaji,…akamwangalia kwa muda, na baadaye akawageukiwa watu waliohudhuria, akasema;,

‘Mwenzetu anapofariki, anakuwa hana mtetezi tena, kwahiyo inategemea nyie wanandugu mliobakia, kama alitaka jambo fulani lifanyike, ina maana kuondoka kwake, kutategemea nyi e wanandugu mliobakia dunia, muweza kumsaidia kutetea haki yake, na kama alitoa kauli yake, ni haki yenu nyie mliobakia dunia kuitekeleza, ….na ndicho sisi tunachokifanya, hatuna zaidi, hatuna haja na hiyo mali,…..’akatulia.

‘Ni kweli kuwa aliacha mjane, ni kweli kuwa aliacha mtoto, lakini vyote hivyo kipindi ananielekeza kutayarisha hiyo hati, nilimuuliza, na akasema mjane na mtoto wake wote ananiachia mimi, vyote hivyo vitakuwa kwenye mikono yangu, nihakikishe kuwa familia yake haiteseki…je kwa hali kama hiyo mimi mlitaka nifanye nini….niake kimiya nimsikilize huyu mwanamama, kwa kutaka nini kwake….’akamgeukiwa mwanamama mlalamikaji.

‘Kwahiyo, ndugu mlalamikaji, sifanyi haya kwa matamanio yangu, eti kukudhulumu jasho lako, hapana nafanya haya kutokana na kauli na maandishi ya marehemu, ..kamwe sitadhulumu jasho la mtu, kama kweli ulijenga kwa pesa yako, …basi ni haki yako…na mimi ningelipata ushahidi wa kuthibitisha hilo, …..nisingelipoteza muda wangu hapa’akatulia na kumwangalia wakili mwanadada aliyetaka kusema jambo, lakini wakili yule hakusema kitu.

‘Sasa hebu tuambie una ushahidi gani, wa kuthibitisha hayo yote, maana katika kulipwa kitu kama hicho ni lazima kungelikuwa na kumbukumbu ya malipo, na nina uhakika kuwa huna kumbukumbu hiyo na kama unayo….sijui,…au huenda uligushi, …kama unayo kwa sasa, basi onyesha kwenye mahakama hii ili tuthibitishe hilo…’akasema huku akishika kidevu kama kuzarau.

‘Ndugu mlalamikaji kama kweli unayo, sisi kwa moyo mmoja tutabatilisha hayo yote na kukukabidhi mali yako, maana kweli hiyo itakuwa ni mali yako, …ulijenga kwa jasho lako…kama kweli unayo, na ukathibisha hivyo, basi nyumba na duka havikustahili kuwepo kwenye mali za urithi za marehemu, pili unasema hata namba ya simu huna, hivi ni kweli kwa hali ya kawaida upate pesa nyingi kama hizo usikumbuke kabisa hiyo namba yako ya bahati….nina mashaka makubwa na malalamiko yako hayo…’akasema akimwangalia mlalamikaji kwa macho ya huruma.

‘Na je inawezekanaje ushinde, kwa pesa nyingi kiasi hicho, hata watu wa kampuni hiyo wasikukumbuke….kwa hali yoyote sisi tunaolalamikiwa tunakuwa na mashaka na malalamiko yak o hayo na tunaona unatumia mwanya huo kudai mali ya marehemu, kwa vile hayupo duniani, na wengi tunaona kuwa mtu akifa hana lake…..hapana , mtu akifa kama alikuwa na haki yake bado itaendelea kulindwa kisheria kama alivyotaka iwe, na sis ndicho tunachokifanya, tafadhali heshimuni kauli za marehemu, msipende mali za dezo …..’akatulia na kuangalia watu ambao walikuwa wametulia kimiya wakimsikiliza.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, sisi tunaolalamikiwa tunasema tena, je walalamikaji wana ushahdi gani, kama vile hati ya malipo, japo moja tu, ili tuwe na ushawishi wa madai yao hayo, aionyeshe hii mahakama yako tukufu,..kuachilia mbali ushahidi wa maneno, wa kuongea, ….’akasema akimwangalia wakili mwanadada.

‘Kuongea kila mtu anaweza kujenga hoja na kuwashawishi watu,….na huenda akaweza kufanya hivyo, hata kama anayoongea sio kweli, lakini sio hapa. Hapa ni shemu ya kutafuta haki, haki kwa ushahidi wa vitendo, wa vitu, …kwahiyo sisi kisheria, bado tunahitaji ushahidi halisi. Je unayo huo ushahidi kuweza kuishawishi mahakama kuwa kweli wewe ndiye uliyelipwa hizo pesa na wala sio udanganyifu…’akasema huyu wakili akiwa kamkazia macho huyo mwanamama, na yule mwanamama akasema.

‘Je na wewe unao ushahidi kuwa ndugu yako ndiye aliyejenga hiyo nyumba kwa pesa zake, na pesa hizo alizipatia wapi, wakati alikuwa amefungwa jela….?’ Akauliza huyo mwanamama na watu wakawa kama wanaguna, maneno ya huyo wakili mtetezi yalionekana kuwagusa watu, na kila mtu alihisi kuwa huyo mwanamama huenda alikuwa akidanganya ili apate mali ya marehemu kiujanja.

‘Hilo tulishaliongea awali, kuwa marehemu pamoja na shughuli zake nyingi, alikuwa akijishughulisha na biashara ya kutafuta madini, na hilo linafanywa na wakazi wengi wa hapa, kama unavyoona,  kuwa eneo letu limezungukwa na aridhi yenye madini, na yeye katika kuhangaika akajaliwa kupata hizo pesa….sio ajabu wengi wamefanikiwa hivyo hivyo. Tatizo la huyu marehemu alipopata hizp pesa alikuwa na wenzake, ….na wenzako walipogundua hilo, wakataka kumdhulumu, na ndipo akaamua kukimbilia Dar…’akasema.

‘Una uhakika na hayo maneno yako,…na je unawezaje kuithibitishia hii mahakama kuwa kweli unayozungumza yana ukweli, yapo wapi maandishi kuwa pesa hiyo aliipata kwa kuuza madini, upo wapi ushahidi wa kulipwa hizo pesa, maana tujuavyo ni kuwa wengi wakiuza madini wanauza kwenye makampuni makubwa ambayo hutoa stakabadhi za malipo….je upo wapi ushahidi wako?’ akaliza mlalamikaji.

‘Ndugu hakimu, mlalamikaji anauliza swali ambalo halihusiani na kesi yetu hii,lakini kama atashikilia kauli yake hiyo, sisi tunaweza kuipata hiyo staakbadhi, lakini sio kwa leo, maana haikuwa na umuhimu kwa kesi hii hapa …na sisi tumemuuliza yeye kisheria kwa vile yeye ndiye anayedai kuwa pesa hiyo aliipata kwa kulipwa na kampuni ya simu, na sio sisi kudai kuwa pesa hiyo tumelipwa kutokana na kuuza madini…kama anahitajia kesi nyingine, madai mengine kuhusiana na hilo, tunaweza kuja kuthibitisha hayo….’akasema.

‘Sasa nyie mnataka nitoe ushahidi gani kuhakikisha kuwa kweli nililipwa hizo pesa, wakati hali halisi nilishaielezea..?’ akauliza na hapo wakasikika sauti kutoka kwa mmoja wa watu waliohudhuria kwenye hiyo mahakama akisema;

‘Waonyeshe huo ushahidi…..’na watu wakageuka kuangalia sauti ilipotokea lakini hakukugundulika kwa haraka ni nani alitamka maneno haya ,….labda kwa wale waliokuwepo karibu na mzungumzaji,… hata hakimu ambaye alitaka kusema neno akatulia na akawageukia wazee wa mahakmaa na kuanza kuteta nao jambo na wakili mtetezi akasema, bila kujali kuwa hakimu anaongea na wazee wa mahakama akasema;

‘Tunahitaji ushaidi wa kumbukumbu za malipo, ambazo zitathibitisha kuwa kweli ulilipwa hizo pesa….vinginevyo kwa vile mnataak kulipaka jina la marehemu, tutafikiria kuchukua hatua nyingine…’akasema huyo mwanasheria akimsaidia wakili wake.

Yule mwanamama,  akageuka kuangalia kule walipokaa watu, ilionekana alikuwa akimtafuta mtu kwenye kundi hilo, na watu wote wakageuka kufuata macho yake, lakini hakuna cha tofauti kilichoonekena, na watu waliokuwepo pale wengi wao walikuwa wametulia kimiya wakifuatilia hayo malumbano,…

Baadaye huyo mwanamama akamgukia wakili wake ambaye alionekana naye akiangalia kule walipokaa watu, ambapo mwanzoni alimuona yule mtu aliyekuwa na huo mfuko wa Rambo, na alipoona mteja wake, anaangalia huko,  akasema

‘Endelea kuongea, usijali watu na usijali maelezo yake, nia yake ni kukuchanganya ukate tamaa, usikate tamaa ukitetea haki yako…uwanja ni wako,….’akasema akiagalia saa yake kwani kwa mtizamo wake muda wa hiyo kesi umekwisha kwahiyo hapo itakuwa nafasi yake ya kuomba kuiahirisha hiyo kesi hadi siku nyingine,ambapo angeliweza kupata ushahidi wa kutosha kutetea hoja yao...kauli ya mwanamama mlalamikaji ikamshitua wakili wake, yule mwanamama alisema;

‘Nataka kuutoa huo ushahidi wanaoutaka,..tumalizane na hii kesi’akasema.

‘Ushahidi gani….?’ Akauliza mwanadada akiwa anamuangalia mwanamama mlalamikaji kwa kushangaa, maana siku zote wanahangaika kuutafuta huo ushahidi na hawakuweza kuupata, na hawakuwa na ushahidi wowote wa maana, …Na alipoona yule mwanamama akiuchezesha ule mfuko,  akauangalia ule mfuko wa Rambo, ambao bado yule mwanamama alikuwa kaushikilia mkononi.

‘Ninataka kuutoa huo ushahidi wanaoutaka wao,nimeshaupata ….je ukipatikana kesi yetu itakwisha na hakutakuwa na malumbano tena, maana mimi sitaki hizo kauli zao za kusema mimi nataka kumzulumu marehemu….’akasema huku akiinua ule mfuko wa Rambo, aliokuwa ameushika mkonononi na yule wakili akamsogelea na kuuchukua ule mfuko, akaingiza mkono ndani  na kutoa kilichoko ndani yake, ulikuwepo  mkoba mdogo wa akina mama, akautoa,, halafu akamwangalia huyo mwanamama.

‘Huu ndio ushahidi wenyewe?’ akauliza,

‘Fungua hiyo pochi, …’sauti ikasikika tena kutoka kwa waliohudhuria kwenye hiyo mahakama, na yule wakili akafungua ule mkoba na kukutana na karatasi zilizokunjwa , na akazifungua, na kuanza kuzisoma kwa haraka, akasema;

Payment voucher….mmh, to, amount,….exactly….’akainua macho na kumwangalia huyo mwanamama mlalamikaji huku uso ukionyesha kushangaa,h alafu akageuka kumwangalia hakimu ambaye kwa muda huo alikuwa akiteta na wazee wa mahakama, na ilionyesha wazi hakimu alitaka kumaliza kesi, huenda kutoa muda wa kuisikilza tena baadaye au kusubirisha hukumu.

Akageuka kuwaangaia watu walioshiriki kwenye mahakama hiyo, halafu akapitisha macho na kuangalia sehemu ile ambayo mwanzoni alimuona mtu akiinua huo mfuko wa Rambo, na akamuona mtu, ambaye kwa muda huo alikuwa kainama chini, akiwa na kofia pana, akiwa kama anasoma kitu, hakuweza kubahatisha kuwa ni mtu gani, akaona ageuke kumuuliza mteja wake,

‘Umeupatia wapi huu ushahidi, ..na nakumbuka nilimuona mtu akiwa na huo mfuko ni nani huyo mtu?’ akauiliza huku akiwa na hamasa ya kumtambua huyo aliyempa huo ushahidi.

‘Je kwasasa  ni lazima kumfahamu huyo mtu, maana kinachohitaka hapa ni huo ushahidi, na umepatikana, hata hivyo aliyenipa huo ushahidi hakutaka ajulikane kwasasa, ila amesema mtaongea naye  baadaye, kwani anataka uwe wakili wake kusimamia kesi yake ya malalamiko…’akasema.

‘Kesi gani tena hiyo ya malalamiko?’ akauliza na mara wakashituliwa na sauti ya hakimu ikasema;

‘Je mlalamikaji una ushahidi wowote wa kuthibitisha hayo yote, …kuwa ulishinda na kulipwa hizo pesa, au tumalize hii kesi maana muda umekwisha..’akasema hakimu akimwangalia wakili wa mlalamikaji?’

‘Ndugu hakimu, kabla sijatoa huo ushahidi, namakumbusha mtetezi kwa kauli yake kuwa ukipatikana huo ushahidi, basi anatabatilisha umiliki wao kwenye hizo mali walizozimiliki isivyo halali…je wapo tayari kwa hilo?’ akauliza. Hakimu akageuka kumwangalia wakili mtetezi, ambaye alipoona karuhusiwa kujibu hilo swali akasema;

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, sisi tuna imani kuwa hawa watu hawana ushahidi wowote, wanachotaka kwa sasa ni kupoteza muda, ili kesi hii ichukue muda mrefu, sisi kauli zetu zilisikika na kuwekwa kwenye kumbukumbu hatuna haja ya kuzirejea,…’akasema huyo wakili mtetezi.

Wakili mwanadada akasema; ‘Namuomba nimsimamishe mtu wa kampuni ya simu waliolipa hizo pesa  …’akasema.

‘Wa nini…?’ akauliza hakimu akinangalia saa yake.

‘Ili athibitishe huo ushahidi wetu..’akasema wakili mwanadada, na hakimu akamuangalia wakili wa utetezi kama  anapingamizi lolote, lakini wakili wa utetezi alikuwa akiteta na mwenzake, na pasipo na kujali akasema;

‘Hatuna pingamizi muheshimiwa hakimu, tuna uhakika kuwa hawana ushahidi …’akasema na yule shahidi wa kampuni ya simu akafika pale mbele , na wakati huo mlalamikaji alikuwa keshaondoka kwenye kiti cha mashahidi.

‘Hizi hapa ni stakabadhi za malipo, naomba uchukue muda kuzichunguza na utuambie ni kitu gani…na je ni za uhakika, hazijagushiwa kama anavyodai wakili mtetezi..?’ yule shahidi akazichukua zile nyaraka na kuanza kuzifungua na kuziangalia vyema , halafu akasema;

‘Hii ni payment voucher, ni nakala ya mlipwaji, huwa tukilipa pesa kuna kuwa na nakala mbili, moja tunabakia nayo kwenye kumbukumbu zetu na nyingine anaondoka nayo mlipwaji..’akasema.

‘Je ni ya ukweli nakala hiyo, umeichunguza vyema, kuwa kweli inatoka kwenye kampuni yenu na haikugushiwa kama walivyodai watetezi…?’ akaulizwa.

‘Ni ya ukweli inatoka kwenye kampuni yetu, haina shaka…’akasema.

‘Je unaweza kutaja jina mlipwaji kwenye nakala hiyo, na ililipwa kwa ajili gani…’ akaambiwa huyo shahidi na yule shahidi akaanza kusoma jina la mlipwaji na kiasi cha pesa na maelezo ya kwanini pesa hiyo ililipwa….

‘Muheshimiwa hakimu tunawakilisha ushahidi walioutaka walalamikiwaji, na kutokana na kauli yao, sisi hatuna zaidi…’akasema wakili mwanadada, na kumfanya wakili mtetezi na msaidizi wake wabakie wameduwaa…na mara kwa nyuma ikatokea sauti ya ukali ikisema;

‘Haiwezekani, hatukubali kamwe….mimi kama kaka mkubwa wa familia sitakubaliana na hilo….’ Watu wote wakageuka kuangalia hiyo sauti imetoka wapi………

NB: Haya...KUMEKUCHA, ushahidi ndio huo...sijui ndio wenyewe au..., na kama ndio huo, je wanafamilia walalamikiwa watakubaliana nao, je watachukua hatua gani,  tusikose sehemu ijayo ya kisa hiki, wema hauozi. Kwakweli natamani nipate moderm, haraka iwezekanavyo..

WAZO LA LEO: Siku hizi watu hawaogopi kusema uwongo, kuzulia wenzao ubaya, na zaidi ya hayo, watu hawaogopi kudhulumu mali za marehemu. Wapo ambao walioaminiwa na marehemu alipo kuwa hai, wakapewa dhamana hzio, ili kuzitunza au kuwakabidhi wanaostahiki, baadaye mlengwa alipofariki,wanageuka kuwa mawakala wa kuzihujumu hizo mali,na kuwaacha mayatima na wajane wakihangaika


Jamani, kumbekeni kula mali ya mayatima na wajane ni dhambi kubwa sana, na kumbukeni kuwa, na nyie hamtakaa milele kwenye hii dunia, mtaondoka, na jinsi mlivyowatendea wenzenu na nyie watoto wenu watatendewa hivyo hivyo….kumbukua dhambi ya dhuluma haidumu.

Ni mimi: emu-three

6 comments :

Unknown said...

dhuluma mbaya na m'mungu apendi na haki ya mtu aipotei bure.

Unknown said...

haki ya mtu haipotei bure

Yasinta Ngonyani said...

dhuluma mbaya kwa kweli.....ila watu inapofika kwenye jambo hili husahau kabisa...tupo pamoja...

Unknown said...

Ni kweli kabisa mnayosema dhulma haifai na haki itaonekana. Ubarikiwe M3

Unknown said...

Ni kweli kabisa mnayosema dhulma haifai na haki itaonekana. Ubarikiwe M3

Unknown said...

Kweli kbs hali ya mtu haiendi hivi hv dhulma mbaya jamani hii Ni fundisho kwa wote. Ubarikiwe m3 kwa kutupa darasa na kutuburudisha.