Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, June 21, 2013

WEMA HAUOZI-23


Ikafika siku ya kesi, na baada ya utangulizi wa maelezo ya kesi yenyewe, na hakimu kusema kuwa kinachohitajika ni kuskiliza ushahidi na mshahidi wa pande zote mbili, ikawa ni zamu ya mawakili kuingia ulingoni. Kwa upande wa wanaoshitaki alisimama mwanadada , na aliposimama watu wakashangilia, na hakimu ikabidi agonge rungu lake kwenye meza kuwa hiyo haitakiwi hapa ni mahakamani sio uwanja wa siasa.

Washitakiwa walishapata wakili wao mwingine, na yule mwanasheria wa familia, akawa kama msaidizi , kwani yeye alikuwa kwenye kundi la wanaoshitakiwa. Mwanasheria huyu alionekana mnyonge kidogo, japokuwa ile tambo yake ya kujiamini ilikuwa pale pale.Hakuacha kumtupia jicho mchumba wake mara kwa mara, japokuwa kwa uficho, na mara nyingine alikuwa akiniangalia mimi.

Wanasheria wakaanza kuita mashahidi wao mmoja baada ya mwingine, na baadhi ya mashahidi waliitwa kutoka kampuni ya simu iliyolipa pesa , ambayo imekuwa ni ushahidi mkubwa kwenye kesi hii, na shahidi huyu aliyetoka Dar, alisimamishwa na kuanza kuulizwa maswali;

‘Wewe ni mfanyakazi wa kampuni ya simu, ambayo moja ya promosheni zenu ni kutoa zawadi kwa wasindi mbali mbali,….sasa hebu tuambie taratibu zenu za kutoa hizo zawadi?’ akaulizwa swali na yule shahidi akaelezea jinsi gani mashindano hayo yanavyofanyika hadi mshindi kupatikana.

‘Mshindi akishapatikana, inafikia kipindi cha malipo, hebu tufaafnulie kidogo jinsi gani huyo mshindi anavyochukua pesa zake?’ akaulizwa.

‘Mara nyingi, mshindi analipwa kwenye hafla iliyoandaliwa, na pale anapewa hundi kivuli, na hata kama ni pesa kisualama hatuwezi kumkabidhi pale pale….labda ikiwa ni pesa za kiasi kidogo….hili tumelifanya kutokana na usalama wa mteja wetu huyo….lakini tukumbuke kuwa zoezi zima lote hilo ni sehemu ya kujitangaza kibiashara…’akasema.

‘Kwahiyo haiwezekani mtu akalipwa pesa bila kuwepo na hiyo hafla..?’ akaulizwa.

‘Mara nyingi promosheni kama hizo zinawakutanisha washindi wengi, na kwa vile washindi ni wengi , kukosekana kwa mtu mmoja hakuwezi kuvunja hiyo hafla, …kama kuna mtu mwenye sababu maalumu, anaweza akaleta muwakilishi wake na hafla ikaendelea kama kawaida bila ya huyo aliyeshinda kuwepo ….’akasema.

‘Na akiwepo huyo muwakilishi wake akakabidhiwa ushindi huo, labda iwe pesa, kwenye hundi au stakabadhi ya malipo, jina gani litaandikwa, je linabakia lile lile la mshindi au linaandikwa hilo la muwakishi wake?’ akaulizwa.

‘Jina la mshindi linabakia hilo hilo hata kama yeye mwenyewe hatakuwepo, hatuwezi kumwandika muwakilishi kwasababu sio yeye aliyeshinda…’akasema.

‘Katika uchunguzi uliofanyika hivi karibuni, iligundulika kuwa kuna mchezo mbaya ulikuwa unafanyika, kuwa mtu analipwa pesa, na jina lake huyo aliyelipwa halionekani, linakuja kuonekana la mtu mwingine …’swali hilo likapingwa na watetezi, na hakimu akakubali pingamizi hilo.

‘Je inawezekana kukatokea udanganyifu katika ulipaji wa malipo kama hayo?’ akaulizwa.

‘Udanganyifu kama upi? Akauliza shahidi.

‘Nakuuliza tena swali, wewe unachotakiwa ni kujibu, ndio au hapana, je katika kulipana hizo zawadi kunaweza, au kuliweza kutokea udanganyifu wowote?

‘Siwezi kukataa ,kwani yote hayo hifanywa na wanadamu,unaweza kutokea, lakini ni nadra sana’akasema

‘Unaweza kutaelezea kidogo kama utatokea udanganyifu, ni kama upi?’ akaulizwa, hilo swali lilipingwa lakini muulizaji wakili mwanadada akalitetea swali lake na hakimu akaliruhuhusu lijibiwe

‘Kunaweza kutokea mfanyakazi akaharibu utaratibu, kwa kuandika jina la mtu mwingine….hiyo imegundulika kipindi cha nyuma, na pia kuna udanganyifu wa kuandika kiasi kisicholingana na malipo lakini hilo limetokea mara moja tu, na ni nadra sana, ni kitu ambacho kama ni kutokea ni mara moja kwa bahati sana, maana wanaohusika ni watu waaminifu’akasema.

‘Lakini iliwahi kutokea?’ akaulizwa tena

‘Kama nilivyosema ni nadra sana…ndio ilitokea’akasema.

‘Na unaweza kukisia ni lini nadra kama hiyo iliwahi kutokea…’hilo swali likapingwa, lakini muulizaji akasema anauliza kwa vile tukio la ukiukwaji wa taratibu linahusiana na kesi iliyopo, na hakimu akaruhusu swali hili kujibiwa.

‘Ilitokea kipindi wakati kampuni yetu ilipokuwa na jina la zamani…na kipindi hicho tulikuwa na mchakato wa kubadili jina, kwahiyo mambo mengi yalikuwa kwenye njia panda…, lakini kwasasa hivi tumebadili jina na kuna udhibiti mkubwa wa taratibu zetu na haitaweza kutokea tena.

‘Katika hati za malipo, mnatumia vitabu kuandikia mtu kalipwa kiasi gani na hati hizo, zina namba juu yake, na zinakuwa na mfuatano, inawezekanaje namba hizi zipitane, yaani, kama ilianza moja, mbili , tatu halafu inaruka hadi mia sita…?’ akaulizwa.

‘Hizo ni moja ya taratibu ambazo zilikuwa zinakiukwa na kwasasa tuna mashine maalumu ambayo inahakikia kila malipo, na kuhakikisha namba hazirukwi tena…’akasema.

‘Hujajibu swali langu nirudie….inawezekanaje namba  ziruke…?’ akaulizwa, na wakili wa utetezi akazuia hilo swali, na hakimu akaomba muulizaji aulize vyema hilo swali

‘Je kwanini namba hizo zirukwe….na kuachana ule mfuatano,kama sio ukiukwaji wa taratibu au kuna jambo lilitakiwa kuharibiwa?’ akaulizwa.

‘Ni haraka haraka ya malipo, yaani muhusika badala ya kuchukua kitabu kilichokuwa kinaendelea anachukua kitabu chochote na kuandika hiyo stakabadhi ya malipo…’akasema.

‘Je haiwezi kuwa ni ukiukwaji wa taratibu, mtu huyu akiandika hati nyingine baada ya ile ya mwanzo, na kumwandika mtu mwingine?’ akaulizwa na hilo swali likapingwa, kuwa linamuelekeza shahidi kujibu, na hakimu akakubali pingamizi hilo.

‘Ipo sababu gani nyingine inayoweza kurukwa kwa hizi namba za malipo, hata zisifuatane?’ akaulizwa.

‘Kama nilivyosema kuwa awali kulikuwa na uzaifu na baadhi ya wafanyakazi wasio waaminifu wakawa wanatumia ujanja kupata pesa, ….na kubadili hati za malipo za awali na kuweka nyingine, aua kulitokea makosa, na badala ya muhusika kurekebisha inavyotakiwa, kachukua kitabu kingine na kaundika vocha nyingine……’akasema.

‘Kwahiyo mtu kama huyo akindika hati nyingine kuna taratibu zozote za kuhakiki baaadaye?’ akaulizwa.

‘Wahakiki wengine ni wakaguzi wa mahesabu, lakini hati haiwezi kuleta utata, maana wahasibu wa kuhakiki, wanachoangalia sana ni kiasi cha malipo, na kumbukumbu za benki….na ni mara chache kuhakiki ni nani alilipwa, maana ni makosa kama hayo hayatokei mara kwa mara….na tunaweza kusema hayawezi kutokea’akasema.

‘Lakini baada ya uchunguzi iligundulika kuwa makosa hayo yalitokea?’ akaulizwa

‘Ndio….’akasema, alipojibu hivyo, wakili wa utetezi akasimama tena na kuuliza;

‘Je unakumbukumbu za watu uliowahi kuwalipa kabla,…kwa mfani humu ndani kuna mtu yoyote unayeweza kusema uliwahi kumlipa?’ akauliza na wakili mwingine akapinga hilo swali, na muulizaji.

‘Katika kazi yako hiyo, natumai kuna wale waliowahi kulipwa pesa nyingi, na hawo sio rahisi kusahaulika, au sio? Akauliza.

‘Ni kweli kwa wale ambao waliwahi kupokea pesa nyingi, sio rahisi kusahaulika maana kuna picha zao, kutangazwa sana….kwahiyo mimi kwa vile nipo kwenye hilo jopo la kuwatangaza, na kuhakikisha shughuli zinakwenda vyema,….ninawakumbuka sana…’akasema.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, lengo hapa ni kutaka kujua kweli mlalamikaji ndiye aliyekipwa hizo pesa, na huyu ni muhusika wa kulipa hizo pesa, nilikuwa nataka ajaribu kumuona ii kuhakikisha kweli pesa hizo alilipwa huyo mlalamikaji’akasema wakili na wakili mlalamikaji akasimama na kupinga hilo swali, akisema, hilo hitimisho,…..na hali halisi ilishaelezwa kuwa mlalamikaji hakuweza kuhudhuria hafla hiyo kwasababu zisizozuilika..

Hakimu alitulia kidogo, lakini baadaye akasema, mlalamikaji asimame na shahidi huyo amtambue, na shahidi alipoulizwa kuwa aliwahi kumuona huyo mwanamama, akatulia kidogo na baadaye akasema;

‘Kwakweli, ….siwezi kudanganya,….’akatulia.

‘Jibu swali uliwahi kumuona huyo mwanamama, kama mshindi wa promosheni yenu iliyofanyika kipindi hicho?’ akaulizwa.

‘Naomba niweke wazi, kuwa kipindi hicho, sikuwa akribu sana kama kipindi hiki, inawezekana siku hiyo sikuwepo, au….’akaanza kujieleza.

‘Jibu swali uliwahi kumuona?’ akaulizwa.

‘Sikumbuki…..’akasema na wakili mshitaki akasimama,

‘Wewe katika kazi yako hiyo ya kushughulikia promosheni , kuna kipindi ilitokea akawa anasguhulikia mtu mwingine?’ akaulizwa.

‘Inatokea, maana kama kampuni, kuna wafanyakazi wengi, katika kitengo chetu tupo wengi ambao wanasimamia kazi hiyo, inawezekana nilikuwa likizo..’akasema.

‘Nakumbuka kuwa ulisema mtu aliruhusiwa kuchukuliwa pesa zake na muwakilishi wake, je ni lazima huyo anayelipwa apitie kwako kwanza kabla ya hafla?’akaulizwa

‘Sisi tunawasiliana na mshindi, na kumuelekeza jinsi gani ya kupata pesa zake,…na kama ana dharura kama hiyo anajieleza ili tumfahamu muwakilishi wake…’akasema.

‘Sina swali jingine ..’akasema wakili mtetezi.

****

Baadaye aliitwa shahidi wa ukaguzi wa mahesabu na yeye akaulizwa maswali yake , yanayohusiana na kazi yake na pale alipouliwa kuhusu mpangilio wa namba za hati za malipo(payment vouchers), yeye akasema;

‘Hata sisi tunapoona namba zimeruka katika mpangilio huwa tunatilia mashaka, lakini kama kiasi kilicholipwa kimelipwa sawa sawa, na kuna uthibitisho wa malipo hayo , mara nyingi hatuingilii kwa ndani zaidi, kuangalia ni nani kalipwa, labda mtu huyu awe ni mteja, ambaye tutahitajia uthibitisho…’akasema.

‘Lakini kwa urukwaji wa mfuatano wa namba za hati ya malipo kwa kiasi kikubwa inaashiria kuwa kunawezakana kukawa na hujuma?’ akaulizwa.

‘Inawezekana,….au isiwezekane, kutegemeana na taratibu za kampuni hiyo, ….’akasema.

‘Je katika ukaguzi wenu huo mligundua kuwa kuna hujuma zilitokea?’ akauliza na wakili mtetezi akapinga hilo swali, akisema hilo halina msingi kwenye hiyo kesi, na kuna kesi nyingine inayoshughulia makosa hayo, kujibu kwake, kutaathiri kesi hiyo nyingine.

‘Sina swali jingine..’akasema

*****

Wakaitwa mashahidi wa upelelezi waliokuwa wakichunguza kama kuna hujuma ilifanyika na wao wakasema kuwa kulitokea hujuma mbali mbali ambazo zilikuja kubainisha kuwa kuna malipo yaliyokuwa yakifanyikja kinyume na taratibu…’hapa wakili mtetezi akaweka pingamizi, na mabishano ya kisheria yakatokea kwa muda, na mwisho wake, hakimu akainglia kati na kusema;

'Mapumziko ya nusu saa, na tukiwa kwenye mapumziko nawaomba mawakili tuonane , na watu wakaguna, maana walishaanza kufurahia mapambano ya mawakili hawa.

'Na pia nimeona kuna majina mengi ya mashahidi kwenye orodha ya mashahidi, hakikisheni wote wapo, na wamekamilika, sitaruhusu tena malumbano yasiyoendana na hii kesi,....hili ni onyo la mwisho...'akasema hakimu.
'Sawa muheshimiwa,...'wakasema mawakili

‘Hapa kwenye orodha ya mashahidi naona kuna watu wengi mumewataja, je wapo tayari kwa kutoa ushahidi huo ?’ akauliza.

'Wapo tayari muheshimiwa....'akasema wakili mtetezi na wakili anayetetea mlalamikaji, akageuza kichwa kuangalia sehemu ya mashahidi, huku akiangalia makabrasha yake, kutafuta ni nani atakeyefuata, na akilini mwake alikuwa akiwaza jinsi gani ataweza kuifanya kesi hiyo iahirishwe tena, na kabla hajajibu, na mara akaona mtu akiinua mfuko wa Rambo, akiwa pembeni kabisa, ...alikuwa mzee, hakuweza kumfahamu vyema kwani alikuwa kazibwa na watu wengine.

'Ni nani huyu....'akasema huku akiangalia majina ya mashahidi na kuitiza sehemu ili ,huku anajiuliza ni nani huyo na kwanini kainua ule mfuko wa Rambo, na hapo akajikuta akipoteza sekunde kadhaa, bila kutoa jibu, na hakimu akakohoa kumshitua , akasema;

‘Watakuwepo muheshimiwa, wengine wapo njiani wanakuja…lakini bado nina wengine wataweza kutoa ushahidi wa kutosha’akasema

'Nina maongozi na nyie, kuhusiana na malumbano yenu ambayo hayaendani na taaluma zenu, habu niambieni kuna nini kinaendelea?' akauliza wakati wameshafika kwenye chumba ca maongezi.

'Muheshimiwa hakimu......mwenzangu anauliza maswali ambayo yataweza kuathiri kesi yetu inayofuata, kama ni maswala ya ukiukaji wa taratibu za malipo, kesi yake ipo mahakamani, na tuliongelea sasa hivi, linaweza likaathiri sana ushahidi wetu unaofuata..'akasema.

'Mimi haki yangu ni kumtetea mteja wangu, siwezi kujua kesi inayokuja inahusiana vipi na kesi yetu hii, na ni jukumu lao kujitetea , na sio kuzuia ushahidi wangu..'akasema wakili mwanadada.

'Hebu niambie ushidi gani ambao utasaidia kesi yako hii, kwani cha msingi ni wewe kutoa vielelezo vinavyoashiria kuwa mtu wako alilipwa hizo pesa, kama kulikuwa na ukiukwaji wa taratibu , hilo ni swali jingine,je ipo wapi, karatasi ya malipo ya mlalamikaji kuwa alilipwa, je ni nani alimlipa, ...huo ndio ushahidi'akasema wakili.

;Hiyo sio kazi yako, ya kuamua hayo, nimeaita hapa kuwaonya, kuwa kama hamna ushahidi wa kutosha, ni bora mkasema, na leo ndio mwisho wa kuskiliza kesi yenu hii, maana sio kesi ya jinai, au mauji ambayo inahitajia muda mrefu wa uchunguzi...'akasema hakimu na wakili mtetezi akawa anatabasamu, kuashiria kuwa ameshinda.

'Kama mlikuwa hamjajitosheleza mngelisema nikawapa muda, lakini mlisema kuwa mpo tayari kwa kila kitu....sasa nawapa muda wa mwisho, tukiingia ndani ya mahakama nataka taratibu za kimahakama, zifuatwe, nyie ni wanasheria, mnafahamu ni nini kinahitajika kuongelewa kwenye kesi husika, siarajii tena kuwafundisha,..natumai mumenielewa...'akasema hakimu.

'Sawa muheshimiwa hakimu....'wakasema na huku akili ya wakili mwanadada ikiwazia yule mtu aliyeinua mfuko wa rambo, ni nani.....'akaona awahi kutoka ili afike akaonane na yeye...na alipotoka, na kuangalia ile sehemu aliyokuwa amekaa, hakuona mtu...akageuka kwenda kumuona mteja wake, na alimkuta akiwa kashika ule mfuko wa rambo...

'Kakupa nani huu mfuko?' akauliza na ,mteja wake, akasema.

'Sijui,.....

NB: Inabidi sehemu hii niishie hapa, …tutaendelea zaidi mungu akipenda


WAZO LA LEO: Ukipigania haki yako usichoke, simamia kwenye ukweli na haki, kwani kwa kufanya hivyo, upo pamoja na mwenyezimungu.

Ni mimi: emu-three

4 comments :

Unknown said...

Dah naimani mungu ni mwema hapa ndio patamu sasa, hongera Sana dada MN inafundisha na kuburudisha.kazi njema.

Unknown said...

Dah naimani mungu ni mwema hapa ndio patamu sasa, hongera Sana dada MN inafundisha na kuburudisha.kazi njema.

Unknown said...

Dah basi Tu mungu abariki.

emuthree said...

Ndugu yangu Nancy, tupo pamoja mpendwa nashukuru kwa kunipa faraja, Tupo pamoja, na wengine wote,