Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, June 5, 2013

WEMA HAUOZI-17


Baada ya kuona kuwa kweli wanafamilia wale wamezamiria kuchukua haki yangu, nikaona njia bora ni kwenda mahakamani, lakini kabla ya hayo yote, ilibidi nikae na wazazi wangu tuone jinsi gani tutasaidiana kwa hilo. Wazazi wangu walipinga sana wazo hilo, wakidai kuwa tutajenga uadui mkubwa na hiyo familia, ….
‘Mwanangu acha kama ilivyo, mungu atakusaidia utapata nyingine na utajenga nyumba nyingine waacahe wachukue,…’akasema mama.

‘Hapana, hilo sio wazo jema, …tukiwaachia hawa watu watatuona sisi ni wajinga, ushauri mzuri, tukafungue kesi,….’akasema baba.

Kikao hicho kiliisha bila maafikiano, na mimi kesho yake, nikaenda kumuona baba wa kufikia ambaye alikuwa bado mgonjwa, nilimkuta akiwa na nafuu kidogo, kwani walimvunja mkono, na kumchoma kisu sehemu ya ubavuni, bahati nzuri kisu hicho hakikuingia ndani sana,.

‘Baba mimi pamoja na kuja kukuona, pia ningelipenda kukuarifu kuwa nimeamua kwenda mahakamani kutetea haki yangu…’nikamwambia.

‘Mimi nipo pamoja na wewe, na namuomba mungu siku hiyo ya kesi niweze kufika mahakani ili nitaoe ushahidi wangu…’akaniambia, na mimi nikashukuru kuwa angalau nina watu wapo nyuma yangu.

Na kweli nikaenda mahakama ya mwanzo kufungua kesi, na kesi ikapangwa tarehe ya kusikilizwa, na washitakiwa wakapelekewa barua ya kuitwa mahakamani. Na kipindi hicho huyu wanayemuita mwanasheria wa familia, hakuwepo, ikabidi wamtumie ujumbe wa haraka ili afike.

Na siku kabla ya kesi, akaja kunitembelea mchumba wa huyo wanayemuita mwanasheria wa familia, nilishangaa, kwani toka siku niliposema nitakwenda mahakamani kudai haki yangu, nilikuwa kama nimetengwa na hiyo familia ya mume wangu, na wanafamilia wote waliambiwa kuwa atakayeonekana yupo upande wangu basi yeye sio mwanandugu. Kwahiyo ndugu wote wa upande wa mume wangu walikuwa maadui zangu

‘Karibu ndani….’nikamkaribisha huyo mwanadada, nikiwa na mashaka na ujio huo, yeye hakuonekana kuwa na wasiwasi wowote, aliingia ndani ya kukaa kwenye kiti. Na baada ya kusalimiana tukaanza kuongea.

‘Ahsante kwa kunikaribisha, nimekuja mara moja tu, kama unavyojua, kuwa hakuna anayeruhusiwa kuja huku kwako,kwasababu wewe umeshaamua kujitenga na hiyo familia…..sikutakiwa kuja huku, na ujio huu hakuna anyefahamu kuwa nimekuja kwako….ndio mimi ni mwanafamilia hiyo japokuwa hatujafunga ndoa na huyo mchumba wangu, lakini wanachokifanya sio kizuri, kwani kila mmoja ana haki ya kudai na kutafuta haki yake….’akaanza kujieleza.

‘Sasa kwanini umefika hapa kwangu na kujiweka katika uhasama na familia yako, huoni kuwa unajitafutia mfarakano na jamaa zako….au wamekutuma?’ nikauliza

‘Nimekuja kwa ridhaa yangu mwenyewe, na wala sikutumwa….niliaga kuwa nakwenda sokoni, nikaona nikupitie mara moja,…kwanza kwa vile hili swala limenigusa sana kama mwanamke….nikuambie ukweli, nimekuwa nikijisikia vibaya sana, ….tangu siku ile nilipokuona umewekwa kwenye kile kichumba na ile hali, …moyo wangu hakuwa na amani, na nimekuwa sijisikii vyema, na ninaweza kukuambia kuwa hata ule moyo wa kuolewa huku kwenu, umepungua…’akasema .

‘Ndio mila zetu, hatuwezi kuzikwepa,…na ukiolewa kwenye familia zetu mambo kama hayo yakitokea huwezi kuyakwepa,..sisi tunaliona ni jambo la kawaida maana tumelikuta lipo, na sio kuwa mimi ni kwanza kutendewa vile, ….ni kawaida za mila zetu. Lakini hata hivyo huwezi kukataa kuolewa eti kwa vile utafanyiwa mambo kama hayo, …pamoja na hayo, kuna mambo mengine mazuri..’nikasema.

‘Hapana, mimi ni wakili, na naheshimu sana mila na desturi zetu za Kiafrika, na naheshimu sana taratibu za kidini, lakini kuna haya ya kimila, ambayo hayana mshiko wa kidini, ni mambo ambayo wazee wetu waliyabuni, pengine kwasababu zao, huenda enzi hizo yalifaa, lakini kadri siku zinavyokwenda yanakutwa hayana maana tena,…’ akasema huku akiweka mguu mmoja juu ya mwingine.

‘Ukiangalia kiafya, na kiutu, hayana maana yoyote, nikutesana tu. Mambo mengina kama  hayo tunahitajika kuyaondoa au kuyarekebisha yawe katika mfumo unaokubalika, kwani kuna ubaya gani hata kama ni kuweka mahali tofauti, lakini kuwe na hadhi, namna ile utaishia kushikwa na maradhi, kama malaria…najua ni ngumu sana hasa kwa wazee wetu, lakini sisi wenyewe tunaweza kuyapigania na kuyasahihisha, kama tutakuwa na umoja..’akasema.

‘Wewe unasema hivyo kwa vile huajaolewa ndani ya hizi familia…ukiolewa mwenyewe utajikuta ukiyafuata yote, vinginevyo jamii, na familia ile uliyoolewa watakutenga, ..na kwa vile unampenda mume wako, inabidi ukubali yote, hata hivyo kwa jinsi nilivyokuwa nikijisikia, siweza kuhisi chochote, kuwa labda naumia,…hapa, akii yangu muda wote ilikuwa haipo....’nikamwambia huku akiniangalia kwa macho yaliyojaa mshangao.

‘Kama nilivyokuambia najua ni  vigumu sana kubadili haya na mengine yasiyofaa…..na huenda itachukua muda, lakini mabadiliko hayo yanatakiwa yaanza kuanzia kwetu, kwanza tukubali kuwa kuna mambo hayafai, na wanaoweza kuyaanzisha ni sisi wenyewe, tunaoumia, …tutaanza kidogo kidogo,….na lakini kama sisi tunaoumia tutanyamaza na kusema hiyo ndio kawaida, wao hawawezi kujua mateso tunayoyapata,..hebu nikuulize hivi mwnaume akifiwa na mke wake anafanyiwa kama mnavyofanyiwa wanawake?’ akaniuliza.

‘Hapana, wanaume hawafanyiwi hivyo..hayo ni mambo ya wanawake, na kama ulivyoona, hata wasimamizi ni wanawake wenyewe, wao ndio wanajua kipi kifanyike na kwa utaratibu gani….’nikasema.

‘Unaona, ….kwani mwanaume yeye hajisikii machungu kama aliyokuwa nayo mwanamke, anapofiwa na mkewe. Mimi hapo naona kuna kasoro,….wewe huoni hilo?’ akaniuliza.

‘Kama nilivyokuambia, haya yalikuwepo, na sisi tumeyakuta,. ..hata kama utaona hivyo, kuwa hakuna usawa, ….mimi kama mwanamke nitasema nini, ‘nikasema kwa unyonge.

‘Ni sawa huenda kwa namna fulani mwanamke anatakiwa kuwa na huzuni zaidi ya mwanaume kwa vile yeye atakuwa aliyepungukiwa na kitu kikubwa sana katika maisha yake,…na ukizingatia kuwa mtu huna kazi, wewe ulikuwa mama wa nyumbani, ..’akasema, na kutulia kidogo na baadaye akasema;

‘Huenda waliona kuwa, kwa kufanya hivyo, ndivyo itaonekana kweli kuwa mwanamke ana huzuni kubwa kuliko mwanaume…lakini hebu tuangalie kidni hivi kweli dini inaruhusu mambo hayo,..kweli dini inasema mwanamke ajengewe kilinga kama kile, anatengwa na aishi kwenye mazingira magumu kama hayo?’akauliza huku akiwa kakunja uso wa kusikitika.

‘Hayo maswali ungeliwauliza wazee,na hayo ni ya kimila zaidi hayahusiani na dini, mimi sina jibu lake …. samahani sio kwamba nakufukuza,  …. …mimi kwasasa ninajiandaa kwaajili ya kesi yangu kesho, nisingelipenda kuumiza kichwa change kwa mambo mengine…’nikasema.

‘Mpendwa nalifahamu hilo, na ndio sababu ya kukupitia, ….lengo langu kubwa ni kwa ajili ya hiyo kesi, lakini niliona nianzie kwenye mambo hayo, maana kesi yako, pia ineonekana imegibikwa na taratibu nzima za mila za kuwazulumu wanawake haki zai, ….’akatulia kidogo huku akiangalia saa yake.

‘Na nimekuulizia upande wa dini unasemaje,…kwani mimi naogopa sana kuingilia maswala yanagusana na imani za dini,……mimi najua kabisa dini haijasema hivyo, …kuna taratibu nzuri tu za dini, lakini watu hawataki kuzisoma na kuzijua, wanachofuatilia kwa karibu ni hizi taratibu za kimila, ambazo nyingine zinapingwa vikali na imani za dini….’ Akashika kichwa kwa mkono mmoja, ukiwa kwenye shavu, na kuniangalia kwa huruma, kiasi kwamba sipenda ile hali, ya kunihurumia vile..baadaye akasema;

‘Mimi nijuavyo ni kuwa mwanamke kweli anatakiwa akae siku arubaini akiomboleza, hiyo ni kawaida,..lakini sio kwa kutengwa, na kufanyiwa hayo niliyoona ukifanyiwa….na hili sasa limekwenda mbali zaidi, unaona, sasa kwa vile wanawake wenyewe hatkusoma, hata hiyo dini yenyewe hatuijui, …tunafuata yale wanaume wetu wanayopenda, na sasa kama unavyoona wanakunyang’anya hata ile haki yako…’akasema.

‘Je na wewe unaamini kuwa hawa watu wameninyang’anya haki yangu, au na wewe upo upande wa familia kuwa hiyo sio haki yangu?’ nikamuuliza.

‘Mimi ni mwanasheria, na mwanasheia, anasimamia upande wa sheria, kutokana na ushahidi uliopo, huwezi ukadai haki kwa kuongea tu…kwasasa hivi siwezi nikajibu hilo swali, japokuwa ukiliangalia kwa undani, na ushahidi uliopatikana, inaonekana wazi kuwa huna haki….nazungumzia kisheria ilivyo, nikivaa kiatu cha hakimu….’akasema huku akisita.

‘Nilijua tu….wamekutuma ili uje ujue undani wangu, au sio?’  nikawa kama namuuliza na yeye akawa ananiangalia kwa macho ya huruma;

‘Kwahiyo naomba uondoke, maana hutanisaidia lolote….umekipata ulichokitaka, nenda kawaambie, wenzako, na mume wako anahitajia sana haya maelezo yangu, ili yamsaidie kuitetea familia yake’nikasema.

‘Nimekuja kukusaidia, kama upo tayari, sisemi kuwa nitakuwa wakili wako,…hapana, siwezi kufanya hivyo,…kutokana na hali ilivyo, ila naweza kukupa msaada wa kimawazo ili ikiwezekana uweze kutetea haki yako kisheria…’akasema.

‘Mawazo kama yapi, na wakati kila kitu nilikwisha kielezea pale mbele yenu kwenye kile kikao na nyie, mkasema maelezo yangu hayana mshiko kisheria, ni ya kutungwa …mimi ninauhakika na nililolisema, na kama kweli mahakama zipo kwa ajili ya kutetea haki, basi mimi nina imani kuwa nitaipata haki yangu…’nikasema.

‘Mahakama zipo kuhakikisha kuwa haki inapatikana, lakini mahakama haiwezi kwenda kinyume na ushahidi,….ushahidi ndio nguzo kubwa ya kuipeleka haki kwa mlengwa,….sasa hebu niambie una ushahidi gani zaidi ya yale maelezo yako…., kwa mfano,una viambatishi gani kuwa ulilipwa hizo pesa na hizo kampuni zilizokulipa hizo pesa, na je una shahidi yoyote, anayeweza kulithibitisha hilo, mfano ulishawahi kuwasiliana na hiyo kampuni iliyokulipa hizo pesa ikakubali kukusimamia kwa hilo?’ akaniuliza.

‘Ushahidi wote niliokuwa nao, siuoni tena, inavyoonekana wakati nipo kwenye msiba, waliingia watu humu ndani na kuchukua kila kitu ambacho kingenisaidia kwenye hiyo kesi..na hiyo kampuni nilijaribu kuwapigia simu, kuwaomba wanisaidie kwa hilo , lakini wamesema, kwenye kumbukumbu zao hakuna jina langu, na hii inanipa wasiwasi kuwa huenda, umefanyika mpango wa kuharibu ushahidi wote….’nikasema.

‘Hakuna aliyefanya hivyo, kama ni huyo mchumba wangu, nakuhakikishia kuwa hajafanya hivyo, maana wakati anafuatilia, nilikuwa naye, na kampuni hiyo walitafuta hizo kumbukumbu tukiwa na yeye, hakuna jina lako….na wafanyakazi waliokuwepo kipindi hicho, hawapo tena, …hapo inakuwa vigumu sana’akasema na kushika kidevu huku akionyesha kuwaza sana.

'Na namba ya simu uliyoshindia hiyo promosheni ndio hii inayotumia kwa sasa?’ akaniuliza.

‘Hapana hii ni simu nyingine na namba tofauti, na ile namba sikuwahi kuisajili, ila hii ya sasa nimeshaisajili,….. ile simu yangu ya mwanzo iliibiwa wakati nipo kwenye biashara zangu, na sikuirudishia tena ile kadi yake, maana nilikuwa na kadi za mitandao mingine, ….na hata namba yake nimeisahau kabisa…..unajua sikutilia maanani sana kuhusiana na hilo, maana sikufahamu kuwa haya yatakuja kutokea, ningelifahamu kuwa kuna jambo kama hili, ningelihifadhi kila kitu…’nikasema.

‘Sasa huko mahakamani utakwenda kusema nini…maana ushahidi na mshahidi ndio mambo muhimu , najua kabisa baada ya maelezo yako watakuuliza ushahidi na mashahidi, na vyote hivyo huna , unafikiria wao watakuamini vipi…naona kwenda kwako mahakamani umekurupuka bila kujipanga vyema,…lakini kwa vile umeshafikisha mahakamani basi tuone itakuwaje, lakini kwa sasa sizani kama utashinda hii kesi….’akasema.

‘Mimi ninachopigania ni haki yangu, na kama mahakama ipo kwa ajili ya kutetea haki za watu, mimi bado nina imani kuwa nitashinda, nitaelezea kila kitu, na wao kama kweli ni waadilifu nina imani kuwa wataniamini, …’nikasema na yule mwanadada akaniangalia kwa jicho lile lile linaloonyesha huruma.

‘Hivi niambie, sasa mimi ningelifanyeje, nikae kimiya kwa vile sina hayo yanayohitajika…hapana sitakaa kimiya, nitajitahidi kupigania hadi hatua ya mwisho, mungu atanisaidia maana ninachopigania ni haki yangu…’nikasema na huyo mwanadada akaniangalia kwa makini na baadaye akasema;

‘Nashindwa nikusaidie vipi, …maana huelewi sheria ilivyo, ….na sio kosa lako,…hili ni tatizo kubwa hasa kwa sisi wanawake, wengi hatujasoma, na hata wale waliosoma, hawatoi mchango mkubwa kuwasaidia wenzao angalau na wao wakasoma wakaijua haki yao,na hapo ndipo tunapojikuta tukinyanyasika kila siku… 'akasema huku akiwa kashikilia shavu, kuonyesha huzuni.

'Ohh, ningelisema niwe wakili wako ili niweze kukutetea, lakini hakuna wakili atakayekubali kesi isiyo na ushahidi, ….hii kesi yako ina utata, na ukisikiliza maelezo yako, yanakuwa kama ni ya kubuni au kuyatunga kwa jaili ya kupata mali…’akasema.

‘Kama huamini basi, wewe ondoka, nahisi wamekutuma ili kunichimba,..haya umesikia kila kitu nenda kawaambie, ….lakini mimi najua mungu atanisaidia tu…’nikasema kwa hasira.

‘Nimeshakuamba kuwa mimi sijatumwa na mtu….Nimekuja kwa ridhaa yangu mwenyewe, na sijakata tamaa kukusaidia, nitajitahidi kukusaidia kadri niwezavyo, maana lengo na mdhumuni yangu nikutumia elimu niliyoipata kwa ajili ya kwasaidia wanawake, …..na sijakuwa mzoefu sana wa kazi hii, lakini lengo na nia yangu ni kufanya hivyo, na kila mara ninapotembelea vijijini nakutana na mambo mengi ambayo, yananipa uchungu sana, na kunifanya nijione msalati kama nitakaa kimiya…..’akasema huku akisimama kuondoka.

‘Nataka nianzie mahali…nimeshafanya kesi chache lakini kesi hizo zilikuwa za kiofisi, sijajiweka sawa kuwa wakili wa kujitegemea, sijawahi kufanya kesi yakutetea akina mama,….nyingi ni za wafanyakzi kudai haki zao, au mwajiri kutetea haki yake,…sasa naona muda umefika kugeukia upande huo, nataka nianze kufanya hivyo…., ngoja nifike nyumba, nitulize kichwa, ninaweza kuja kukutembelea hata kama ni usiku, kama nitakuwa na wazo linaloweza kukusaidia….kwaheri, ….. lakini kwa kesho nina uhakika hutaweza kushinda hiyo kesi, …huna ushahidi, utamshawishi vipi hakimu….lakini usikate tamaa, vyovyote itakavyokuwa ujue nipo pamoja na wewe…’akasema.

‘Wewe nenda kwa watu wako, waambie kuwa mimi nitaipigania haki yangu,…hata kama nikishindwa hiyo kesi ya kesho nitakata rufaa hadi mahakamu ya juu, na ikishindikana huko, …nita…nita….’nikashindwa kutamka neno nililokusudia kulisema, na huyu mwanadada akawa ananiangalia kwa macho ya huruma, na alipoona nasita kusema hilo neno, akasema.

‘Usijali, tupo pamoja,….nimekuelewa mpendwa,….’akasema na kuondoka.

NB: Je wewe ungemsaidiaje huyu mwanamke?


WAZO LA LEO: Imekuwa ni kawaida kufanya mambo mengi bila kuwa na kumbukumbu, ikiwemo kuuza na kununua badhaa , au kukopeshana bila kuwa na maandishi yoyote au ushahidi wa watu, hili ni kosa kubwa sana, na huwezi kujua ni nini kitatokea baadaye. 

Tujenge tabia ya kudai stakabadhi kila tunaponunua, na kwa wafanyabishara tujenge tabia ya kuweka kumbukumbu za kimahesabu katika biashara zetu…na pia tukumbuke kuandikishana pale tunapokopeshana au kupeana pesa, kwa ajili ya kumbukumbu za baadaye, kwani bashara bila daftari, hupotea bila habari

Ni mimi: emu-three

4 comments :

MTU KWAO said...

kweli nimesoma nikapata mawazo mengi ila ninataka nifuatilie mpaka nione mwisho je ulienda mahakamani na yule mwolewa pamoja alikusaidiaje hapo baadae ,tupo pamoja

Anonymous said...

Tunga vitabu kaka unalaza damu wenzako wanatumia jasho lako hata bila ahsante

Justin Kasyome said...

Aisee!Kama uko juu ila fanya biashara ya vitabu kaka..ni mimi www,swahiliabroad.blogspot.com

emuthree said...

Nawashukuruni sana wapendwa na mumenipa faraja, kuonyesha kuwa kumbe ninachoandika kinafaa hasa katika jamii yetu hii. Ni kweli kama ningelifanikiwa kutunga vitabu ingelikuwa ni vyema, sana, ....gharama , muda na vitendea kazi imekuwa ni kikwazo kwangu, kuna kipindi niliwaza kuwa huenda nikapata mdhamini, lkn kumbe nayo hiyo ni kazii ya aina yake. Hata hivyo sijakata tamaa, tupo pamoja